Hotuba

- Dec 18, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI WA CCM KWENYE UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA TISA WA TAIFA W...
Soma zaidiHotuba
Ndugu Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Makamu Mwenyekiti wa CCM - Zanzibar;
Ndugu Philip Mangula, Makamu Mwenyekiti
wa CCM- Tanzania Bara;
Ndugu Wenyeviti na Makamu Wenyeviti
Wa CCM wa Taifa Wastaafu mliopo;
Ndugu Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM;
Ndugu Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Ndugu Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu mliopo;
Ndugu Wake za Viongozi Wastaafu mkiongozwa
na Mama Maria Nyerere na Fatuma Karume;
Ndugu Wajumbe wa Kamati Kuu;
Ndugu Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa;
Ndugu Viongozi Wastaafu mliopo;
Ndugu Wawakilishi wa Vyama Rafiki
na Shindani vya CCM mliopo;
Ndugu Viongozi na Wazee Wastaafu wa CCM mliopo;
Ndugu Wageni Wetu Wote Waalikwa: Viongozi wa
Serikali na Dini mliopo;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Ndugu Wana-CCM Wenzangu; Mabibi na Mabwana:
CCM OYEE! MAPINDUZI, DAIMA!
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, kwa kutujulia uhai na kutuwezesha kukutana hapa Dodoma leo. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwakaribisha ndugu wajumbe pamoja na wageni wote waalikwa katika Mkutano huu Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) unaofanyika hapa Dodoma; Makao Makuu ya Chama chetu pamoja na Serikali. Karibuni sana.
Natambua kuwa baadhi yenu mmelazimika kusafiri umbali mrefu kuja kuhudhuria Mkutano huu. Hivyo basi, napenda nitumie fursa hii kuwapa pole ya safari. Bila shaka, mmesafiri umbali mrefu kuja kuhudhuria Mkutano kwa kuwa mnafahamu umuhimu wake, lakini pia hii ni ishara ya mapenzi ya kweli mliyonayo kwa Chama hiki. Na ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza wajumbe wote wa Mkutano huu kwa kuchaguliwa kwenu. Hongereni sana.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu na Wana-CCM Wenzangu;
Mkutano huu unafanyika zikiwa zimepita takriban wiki 3 tangu nchi yetu ifanye Uchaguzi Mdogo wa Madiwani katika kata 43. Na kama mtakavyokumbuka, katika uchaguzi huo, Chama chetu kilishinda viti vya udiwani 42. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kutoa pongezi nyingi kwa wanachama, wapenzi na mashabiki wa CCM kwa ushindi mkubwa tuliopata.
Kwa tathmini yangu binafsi, ushindi huu tuliopata umetokana na mambo makubwa manne. Kwanza kabisa, ni matokeo ya uungwaji mkono mkubwa na kukubalika kwa Chama chetu miongoni mwa Watanzania. Pili, unatokana na uimara na ukomavu wa Chama chenyewe. Sio siri kuwa Chama hiki ni kikongwe. Mwaka huu kimetimiza miaka 40 tangu kianzishwe. Hakuna Chama kikongwe kama hiki hapa nchini. Kimeongoza Dola tangu kimeanzishwa mwaka 1977 na tangu kurejeshwa kwa Mfumo wa Vyama vingi nchini 1992. Kina mashina, matawi, pamoja na wanachama, wapenzi na washabiki nchi nzima. Na katika kudhihirisha kuwa Chama hiki ni kikubwa na kikongwe, ni katika kudhihirisha hili, ninyi wenyewe mnajionea hapa viongozi wakuu wastaafu wa Chama na Serikali wapo hapa. Tunaye hapa Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Mzee Karume, Mzee Malecela, Mzee Msekwa, Mzee Msuya, Mzee Dkt. Salim na Mzee Pinda. Hii inadhihirisha kuwa Chama hiki ni kikongwe na kina hazina kubwa.
Sababu ya tatu, iliyotufanya tushinde Uchaguzi huu ni kwamba tunatekeleza kwa vitendo mambo tuliyoahidi wakati wa Kampeni kupitia Ilani yetu ya Uchaguzi ya Mwaka 2015 – 2020. Na nne, tumeshinda kwa vile hivi sasa wana-CCM tuna umoja. Na tunashirikiana. Hivyo basi, napenda kurudia tena kuwapongeza wana-CCM kote nchini kwa ushindi tuliopata.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema kuwa huu ni Mkutano Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama chetu. Mkutano Mkuu wa CCM wa Taifa ndiyo kikao kikubwa zaidi kuliko vyote vya Chama; na kina madaraka ya mwisho kwa mujibu wa Katiba. Kwa kuzingatia hilo, na kwa kuwa Chama chetu ni Chama Tawala, ni dhahiri kuwa Mkutano huu ni muhimu sana. Maamuzi yatakayofanywa na Mkutano huu yatakuwa na athari (impact) sio tu kwenye Chama chetu bali Taifa letu kwa ujumla.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu na Wana-CCM Wenzangu;
Kama mnavyofahamu, Mkutano huu una ajenda kubwa tatu. Kwanza, utapokea na kujadili Taarifa ya Kazi za Chama itakayotolewa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na kutoa maelekezo ya mipango ya utekelezaji wa Siasa ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Aidha, Mkutano huu utapokea na kujadili Taarifa za Serikali zote mbili (yaani Muungano na Zanzibar) kuhusu utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi pamoja na uongozi wa Serikali na Nchi kwa ujumla. Vilevile, Mkutano huu utafanya uchaguzi wa Mwenyekiti wa CCM Taifa; Makamu wake wawili, mmoja wa Zanzibar na mwingine Tanzania Bara; pamoja na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa.
Na kwa mujibu wa ratiba iliyopo, Taarifa ya Kazi za Chama itawasilishwa na Katibu Mkuu wa Chama, Ndugu Abdulrahaman Kinana. Aidha, Taarifa za Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi na Uendeshaji wa Serikali zitawasilishwa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idd kwa upande wa Serikali ya Zanzibar. Kwa sababu hiyo, hotuba yangu haitagusia sana masuala hayo. Nitajikita zaidi katika suala la uchaguzi wa Chama chetu na nitaeleza baadhi ya mambo ambayo natamani sana kuona Chama hiki kikifanya katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama mnavyofahamu, tangu mwezi Aprili mwaka huu Chama chetu pamoja na Jumuiya zake zote tatu (Umoja wa Wazazi, Umoja wa Wanawake na Umoja wa Vijana) kimekuwa kwenye zoezi muhimu la uchaguzi. Tulianza uchaguzi kwenye ngazi ya mashina, kisha tukaelekea kwenye ngazi ya tawi, kata, wilaya na mkoa; na kwenye Jumuiya, uchaguzi tayari umekamilika hadi katika ngazi ya Taifa. Nimefarijika sana kuona kuwa katika zoezi hili la uchaguzi wagombea wengi walijitokeza, tena wengi sana. Hii inathibitisha ukukomavu wa demokrasia ndani ya Chama chetu.
Baada ya kukamilisha uchaguzi wa Chama kuanzia ngazi ya shina hadi mkoa; na kwa upande wa Jumuiya hadi ngazi ya Taifa; sasa tunakwenda kuhitimisha zoezi la uchaguzi wa Chama katika ngazi ya Taifa. Kama nilivyotangulia kusema, Mkutano huu utamchagua Mwenyekiti wa CCM Taifa; Makamu Wenyeviti wawili, pamoja na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa. Na nawaomba ndugu wajumbe mchague kwa umakini. Usimchague mtu kwa sababu ya urafiki, udini, ukabila, ukanda, au kwa kutegemea kupata maslahi fulani fulani binafsi. Zaidi ya hapo, kamwe! Narudia tena, kamwe, msimchague mtoa rushwa. Ahadi Namba 3 ya mwana- CCM inasema, nanukuu, “rushwa ni adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa”, mwisho wa kunukuu.
Ndugu zangu wana-CCM, Chama chetu kimedhamiria kwa dhati kabisa kupambana na rushwa. Hivi majuzi mmesikia wenyewe tulitengua matokeo ya kura za maoni ya kupata mgombea wa Ubunge kule Singida baada ya kupatikana kwa tuhuma za rushwa. Na niwahakikishie kuwa, hata kwenye uchaguzi huu, endapo itathibitika kuna wagombea wameshinda kwa kutoa rushwa, hatutasita kutengua. Rushwa ni kansa. Rushwa ni adui wa haki. Ninyi wenyewe ni mashahidi kuwa kuna wakati ilikuwa vigumu kwa mtu kwenye Chama chetu kupata uongozi bila kutumia rushwa. Lakini, nimeshukuru sana Mwenyekiti Mstaafu Mzee Kikwete, kama isingekuwa uimara wake mimi nisingepata nafasi hivyo. Ahsante sana Mzee Kikwete. Hivyo basi, nawasihi sana wana-CCM wenzangu, msimchague mtoa rushwa. Badala yake, chagueni watu waadilifu, wachapakazi, wasio endekeza makundi na wenye mapenzi ya dhati kwa Chama chetu.
Ndugu Wana-CCM wenzangu;
Nafahamu kuwa jukumu langu leo ni kufungua Mkutano wetu. Lakini kabla sijafanya hivyo, ninayo masuala mawili ambayo ningependa kueleza. Suala la kwanza, linahusu zoezi la uchaguzi tulilolifanya ndani ya Chama chetu mwaka huu. Kwenye uchaguzi wowote ule kuna kushinda au kushindwa. Hivyo basi, wakati tunaelekea kuhitimisha zoezi la uchaguzi kwenye Chama chetu, ninalo ombi moja kwenu. Uchaguzi huu tulioufanya kwenye Chama chetu kuanzia mwezi Aprili 2017 hadi mwezi huu wa Desemba 2017 usiwe chanzo cha mifarakano au kuvurugika kwa umoja na mshikamano ulioanza kujengeka ndani ya Chama chetu. Bali utuimarishe na kutufanya kuwa wamoja zaidi.
Tuwapongeze wale walioshinda; na napenda kutumia fursa hii kuwapongeza wale wote waliochaguliwa kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye Chama pamoja na Jumuiya zake. Hongereni sana. Ushindi mlio upata ni uthibitisho wa imani kubwa waliyonayo wana-CCM juu yenu.
Kwa wale ambao kura hazikutosha, msikate tamaa au kuwa wanyonge. Kama nilivyosema, kwenye uchaguzi wowote kuna kushinda na kushindwa. Safari hii kura hazikutosha; lakini huenda kwenye uchaguzi ujao, nanyi mkaibuka washindi. Hivyo, jambo la msingi kwenu hivi sasa ni kuchapakazi kwa bidii na kuwaunga mkono viongozi waliochaguliwa. Na niwaombe sana ndugu wajumbe na wana-CCM kwa ujumla, sasa tuyavunje makundi yote tuliyoanzisha wakati wa Uchaguzi. Uchaguzi umekwisha. Wakati wa kampeni umekwisha. Sasa, tunatakiwa tuchape kazi ili kukiimarisha zaidi Chama chetu. Napenda kutumia fursa hii kueleza kuwa, kamwe; narudia tena, kamwe, Chama hakitamvumilia mtu yeyote mwenye kuendeleza makundi. Awe ni kiongozi aliyechaguliwa, awe mgombea aliyeshindwa ama mwanachama wa kawaida.
Ndugu Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Suala la pili ambalo ningependa kueleza linahusu maono niliyonayo ya namna ambayo natamani Chama chetu kifanye kazi katika kipindi cha miaka mitano ijayo. Na hili, nitalieleza kwa kirefu kidogo. Hivyo, nawaomba ndugu wajumbe mnivumilie kiasi.
Ndugu wajumbe na wana-CCM wenzangu, Mkutano wetu huu Mkuu wa Tisa wa Taifa unafanyika katika mazingira ya kipekee sana. Ni ya kipekee kwa sababu, kwanza, unafanyika katika kipindi ambacho Chama chetu kimetimiza miaka 40. Pili, unafanyika wakati nchi yetu imetimiza miaka 25 tangu kurejeshwa kwa Mfumo wa Vyama vingi. Na tatu, ambalo nadhani ni kubwa na muhimu zaidi ni kwamba, Mkutano huu unafanyika katika mwaka ambao Chama kimeanza kutekeleza Awamu ya Nne ya Mradi wa kuimarisha na kujenga uhai wa Chama.
Kama mnavyofahamu, ukiachilia mbali suala la ukongwe na kukomaa kidemokrasia, kama ambavyo nimeeleza awali; sifa nyingine muhimu na kubwa zaidi ya CCM, ni utaratibu wake wa kujitathmini na kujikosoa mara kwa mara, na kisha kufanya mageuzi yanayokwenda sambamba na wakati na hali halisi. Ni kutokana na ukweli huo, tangu imeanzishwa mwaka 1977, CCM imetekeleza awamu tatu za miradi ya kujenga na kuimarisha Chama. Mradi wa kwanza ulitekelezwa kati ya mwaka 1985 hadi 1987, ambapo Mwenyekiti wa wakati huo, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alizunguka nchi nzima kwa lengo la kukiimarisha Chama, hususan katika ngazi za chini.
Na wakati akihitimisha Awamu hiyo ya Kwanza, Baba wa Taifa alitangaza kuzindua Awamu ya Pili ya Mradi wa kuimarisha Chama, ambao pamoja na masuala mengine, ulihimiza Chama katika ngazi zote na kujenga itikadi; kuwa na mpango kazi unaotekelezwa; na kuimarisha mfumo wa nidhamu na demokrasia ndani ya Chama. Awamu ya Tatu ya Mradi wa kujenga na kuimarisha Chama ilianza kufuatia hotuba aliyotoa mtangulizi wangu, Mwenyekiti Mstaafu, Mzee Kikwete, wakati wa kupokea Uenyekiti wa Chama hapa hapa Dodoma tarehe 25 Juni, 2006. Msisitizo katika Awamu hii ilikuwa kujenga uongozi imara kwa kuhakikisha kuwa nafasi zote za uongozi ndani ya Chama zinakamilika; na viongozi wanakuwa mfano wa kuigwa kwa kuonesha njia.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Wakati Chama kikiendelea kutekeleza Awamu ya Tatu ya uimarishaji Chama, kutokana na mabadiliko na changamoto mbalimbali, haja ya kukifanyia Chama chetu mageuzi makubwa ya kimfumo, muundo na utendaji ilijitokeza. Hivyo basi, kufuatia majadiliano ya kina na ya muda mrefu yaliyofanyika; na hususan baada ya Chama kutazama itikadi yake, mwenendo wake, matendo yake, dhamira yake, malengo yake pamoja na kuangalia nidhamu ya viongozi wake. Na baada ya Chama kusikiliza sauti ya wanachama na wananchi kwa ujumla. Kama mnavyofahamu, Chama hiki ni cha wananchi wote. Hatimaye, mwezi Machi mwaka huu (2017), Chama chetu kilikubali kufanya mageuzi kupitia Mkutano Mkuu.
Mageuzi yaliyofanyika yamejikita katika mawanda makubwa matatu: mfumo, muundo na utendaji. Msingi mkuu wa mageuzi haya ni kukirejesha Chama kwa wanachama ili kukifanya kuwa kimbilio la wananchi. Na malengo mahususi ya mageuzi tuliyofanya ni kuongeza tija na ufanisi katika utendaji wa Chama, uwajibikaji miongoni mwa viongozi; pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji wa Chama.
Mambo muhimu yaliyozingatiwa katika mageuzi haya ni kupunguza idadi ya vikao na wajumbe wa vikao ili kuondoa urasimu, kuongeza tija ya vikao husika na halikadhalika kupunguza gharama. Kwa kuwakumbusha tu, tumepunguza idadi ya wajumbe wa Mkutano huu Mkuu kutoka 2,422 hadi 1,706. Tumepunguza wajumbe wa Halmashauri Kuu kutoka 388 hadi 163; na Kamati Kuu kutoka 34 hadi 26. Tumefanya hivyo, ili viongozi watumie muda mwingi kushughulikia matatizo ya wanachama na wananchi kwa ujumla, badala ya kutumia muda mwingi kukaa ofisini na kushiriki kwenye vikao.
Tunaamini kuwa, endapo Chama kitaweza kushughulikia vizuri matatizo ya wananchi, kitaweza kuwavuta watu wengi zaidi kujiunga nacho. Katika mageuzi tuliyofanya pia, tumefuta utaratibu wa mtu mmoja kuwa na vyeo zaidi ya kimoja. Tumefuta vyeo ambavyo havikuwepo Kikatiba (kamanda, mlezi, n.k). Mageuzi tuliyoyafanya pia yamehimiza uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa viongozi na wanachama, pamoja na kusisitiza Chama chetu kujitegemea kiuchumi. Ili kuhakikisha kuwa mageuzi tuliyofanya yanapata msingi wa kisheria, tumelazimika kuifanyia marekebisho Katiba ya Chama pamoja na Jumuiya zake.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Sio siri kuwa mageuzi tuliyoyafanya mwaka huu ni makubwa sana. Na ni lazima tuyasimamie. Na watu wa kwanza ambao watawajibika kuyasimamia ni viongozi ambao wamechaguliwa kushika nafasi mbalimbali hivi karibuni. Napenda kutumia fursa hii kuwasisitiza viongozi wote wa Chama waliochaguliwa kwenda kusimamia mageuzi tuliyoyafanya. Na niseme tu kuwa binafsi nitafurahi sana endapo viongozi waliochaguliwa wataweza kusimamia masuala makubwa manne, ambayo Mkutano huu ukiridhia unaweza kuyafanya kuwa ndiyo malengo makuu ya Mradi wa Awamu ya Nne ya kujenga na kuimarisha Chama.
Suala la kwanza kabisa, ni kukiimarisha Chama chetu kwa kuongeza idadi ya wanachama. Kama mnavyofahamu, lengo kuu la Chama chochote cha siasa ni kushinda uchaguzi na kushika Dola. Na katika nchi ya kidemokrasia kama yetu, mtaji pekee wa kufanikisha hili ni kwa Chama kuhakikisha kinakuwa na idadi kubwa ya wanachama, wapenzi na washabiki. Hivyo basi, viongozi mliochaguliwa, jukumu lenu la kwanza, ni kuhakikisha kuwa mnaongeza idadi ya wanachama, wapenzi na washabiki wa Chama chetu katika maeneo yenu. Tunataka ikifika wakati wa uchaguzi, washindani wetu, wasiambulie chochote.
Jambo la pili, ambalo naomba viongozi waliochaguliwa kulisimamia ipasavyo, ni katika kuhakikisha kuwa Chama chetu kinajitegemea kiuchumi. Chama chetu ni kikubwa na kikongwe. Hivyo, ni aibu kwa Chama hiki kuwa tegemezi. Kwa sababu hiyo, natoa wito kwa viongozi wote waliochaguliwa kuhakikisha Chama chetu kinajitegemea kiuchumi. Hivyo, tuwahimize wanachama waliopo kwenye maeneo yenu kulipa ada zao za mwaka. Na njia nzuri ya kuwashawishi wanachama kulipa ada ni kuhakikisha kunakuwa na uwazi katika ukusanyaji na matumizi wa mapato. Watu wanataka waone fedha zao wanazotoa zimeenda na kufanya nini. Sambamba na kuweka uwazi kwenye mapato na matumizi, jengeni utamaduni wa kuwatembelea wanachama. Msikae ofisini kuwasubiri wanachama walete michango. Na niwaombe wana-CCM wenzangu tujitahidi kulipa ada zetu za mwaka. Zama za kusubiria matajiri watulipie ada zetu wakati wa kampeni, zimepitwa na wakati. Ni lazima sisi wenyewe tujitoe. Chama kitajengwa na wenye chama, siyo matajiri wachache.
Njia nyingine ya kuhakikisha Chama kinajitegemea kiuchumi ni kusimamia vizuri rasilimali za Chama. Kama ambavyo nimesema mara kadhaa, Chama hiki kina rasilimali nyingi: viwanja vya michezo, majengo, mashamba, n.k.; lakini kwa bahati mbaya, kwa muda mrefu, rasilimali hizi hazijakinufaisha Chama chetu. Hii imetufanya, tutegemee zaidi ruzuku na michango ya wahisani. Mathalan, mapato ya Chama kwa mwaka wa fedha 2014/2015 ilikuwa takriban shilingi bilioni 29.35. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 21.95 ni ruzuku na michango ya hiari. Mwaka 2015/2016, mwaka wa uchaguzi, mapato yalikuwa shilingi bilioni 73.19, ambapo ruzuku na michango ya hiari ni shilingi bilioni 56.82; na katika mwaka 2016/2017, mapato yalikuwa shilingi bilioni 40.01, ambapo ruzuku na michango ya hiari ni shilingi bilioni 27.56. Hii inadhihirisha kuwa uwezo wetu wa kujitegemea ni mdogo. Ni lazima turekebisha hali hii, na kwa bahati nzuri tumeanza kuchukua hatua, ikiwemo kufanya uhakiki wa mali zetu zote, halikadhalika tupo mbioni kuanzisha mfumo wa kielektroniki utakaokiwezesha Chama kutambua na kusimamia rasilimali na mali zake zote, mapato na kusimamia uendeshaji kwa ujumla. Hivyo basi, niwaombe viongozi wapya mkaendeleze jitihada zilizoanzishwa.
Sambamba na hilo, viongozi wapya hamna budi kubuni miradi mipya. Na katika hili, niseme tu kwamba, itakuwa aibu kwa Chama chetu, ambacho Serikali yake inahubiri ujenzi wa uchumi wa viwanda, tutashindwa hadi ikifika mwaka 2020 kuanzisha angalau kiwanda kimoja.
Tatu, nawasihi sana viongozi wapya, kila mtu mahali pake alipo, ahakikishe kuwa Chama chetu kinakuwa kiungo kati ya Serikali na wananchi. Chama, hususan Chama tawala kama chetu, kinao wajibu wa msingi wa kuwaeleza na kuwafafanulia wananchi umuhimu wa utekelezaji mipango na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali. Zaidi ya hapo, kinao wajibu wa kuchukua maoni, mapendekezo na kero mbalimbali za wananchi na kuziwasilisha Serikalini. Niwe mkweli, hivi sasa, Chama chetu hakitekelezi vizuri jukumu hili. Tumekuwa hodari sana wa kufanya kampeni na kuhakikisha Chama kinashinda uchaguzi. Lakini, baada ya hapo, huwa tunajiweka pembeni, ama kwa kuvaa sura ya Userikali au kwa kuwaogopa watendaji wa Serikali. Nilisema kwenye Mkutano Mkuu uliopita, viongozi wa Chama hawapaswi kuwaogopa watendaji wa Serikali, hususan katika kutetea maslahi ya wananchi wanyonge.
Katika kusisitiza umuhimu wa Chama chetu kuwa kiungo kati ya Serikali na wananchi, napenda ninukuu maneno yafuatayo, ambayo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyatamka tarehe 7 Juni, 1968 alipohutubia Mkutano Mkuu wa Chama cha Uganda People’s Congress, na nitanukuu kwa lugha yetu adhimu ya Kiswahili:“Kazi ya Chama kilicho imara ni kuwa daraja linalowaunganisha wananchi na Serikali yao. Ni wajibu wa Chama kuwasaidia wananchi kuelewa Serikali yao inafanya nini na kwanini; na kuwashawishi wananchi kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali yao, ikiwemo kuondoa umaskini wao....Zaidi ya hapo, Chama kina jukumu au wajibu wa kuwasemea wananchi (The Party must speak for the people)”, mwisho wa kunukuu.
Hivyo basi, nawasihi sana viongozi wapya, nendeni makatekeleze jukumu hili ipasavyo. Pongezeni pale inapobidi kupongeza, na kosoeni inapobidi. Na ili muweze kutekeleza jukumu hili vizuri, hakikisheni kuwa mnakuwa karibu na wananchi, lakini pia mnaifahamu vizuri mipango ya Serikali na mikakati ya kutekeleza mipango hiyo, ikiwemo bajeti zinazotengwa. Nitashangaa na kwa kweli nitasikitika, kama nitaona wananchi wanadai kufahamishwa mapato na matumizi ya Serikali ya Kijiji, huku Mwenyekiti wa CCM wa Shina au Tawi yupo; nitashangaa wananchi walalamike kuhusu ubadhirifu katika ujenzi wa kituo cha afya au shule wakati Mwenyekiti wa CCM na Kamati ya Siasa ya Kata wapo; na vilevile nitashangaa wananchi kushindwa kuelewa umuhimu wa kununua ndege, kujenga reli ya standard gauge na mradi wa umeme wa Stiglier’s Gorge wakati kuna Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Mkoa na Wajumbe wa Halmashauri Kuu na Mbunge wa CCM. Nitashangaa sana. Na niwaombe viongozi wa Serikali kutoa ushirikiano na ufafanuzi kwa viongozi wa Chama. Lakini ningependa pia kusema kuwa wana-CCM mkitaka kukosoa jambo linalofanywa na Serikali, mkumbuke kuwa ninyi ni Chama Tawala. Mnazo njia nyingi za kufikisha mapungufu mnayoyaona kwenye Serikali. Kuna usemi ambao Umoja wa Wazazi hupenda kuutumia, usemao “Uchungu wa Mwana, Aujuaye Mzazi”. CCM Oyeee! Mapinduzi, Daima mbele!
Jambo la nne, na la mwisho lakini sio kwa umuhimu, ambalo ningependa viongozi wapya mlipe mkazo unaostahili, ni uadilifu. Na uadilifu unapaswa kuanza na ninyi. Kiongozi anapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwa wanachama na wananchi kwa ujumla. Haifai, na kwa kweli, kamwe Chama hakitamvumilia kiongozi au mwanachama wa CCM mwenye kutuhumiwa au kujihusisha na vitendo vya rushwa, utapeli, wizi, ubadhirifu, ujambazi, ulevi uliopindukia, kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya, n.k. Upo usemi wa enzi usemao “Mke wa Mfalme hapaswi hata kuhisiwa kuwa anachepuka”. Hivyo basi, kama kuna viongozi wa namna hiyo wamechaguliwa, ni vyema wakajirekebisha.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema, taarifa ya Utekelezaji wa Ilani na uendeshaji wa Serikali zitawasilishwa na Waziri Mkuu na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Hata hivyo, napenda nitumie fursa hii kueleza mambo machache kuhusiana na masuala hayo. Kwanza kabisa, kama mnavyofahamu, jukumu kubwa la Serikali zetu mbili ni kuhakikisha amani, umoja na Muungano wa nchi yetu unadumishwa. Hii pia ni moja ya ahadi zilizopo kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi. Bila shaka, mtakubaliana nami kuwa Serikali zetu mbili zimeweza kutekeleza jukumu na ahadi hii kikamilifu. Nchi yetu ipo salama na ina utulivu. Muungano wetu upo imara. Na watanzania tumeendelea kuwa wamoja. Watu wachache waliojaribu kutishia amani, Muungano na umoja wetu tumewadhibiti kikamilifu.
Suala la pili ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu utekelezaji wa ahadi kubwa ya uchaguzi ya kujenga nchi ya uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025. Ahadi hii nayo tunaitekeleza vizuri. Uchumi wetu unaendelea kuimarika, ambapo nchi yetu ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika ambao uchumi wake unakua kwa kasi. Aidha, mfumuko wa bei unaendelea kushuka, ambapo mwaka huu mwezi Novemba ulishuka kumefikia asilimia 4.4. Vilevile, akiba ya fedha za kigeni imefikia Dola za Marekani milioni 5,820.4 mwezi Septemba 2017. Kiasi hiki kinaiwezesha nchi yetu kulipia gharama ya kununua bidhaa kwa miezi mitano. Hii ina maana kwamba leo hii Watanzania tunaweza kukaa bila kufanya kazi yoyote kwa miezi mitano na tukaendelea kupata huduma kama kawaida. Lakini hii haimanisha kwamba watu waache kufanya kazi. Ni lazima tuendelee kufanya kazi. Kama maandiko matakatifu yanavyosema, asiye fanyakazi na asile. Nanyi mnafahamu kuwa mtu asiye kula maana yake atakufa.
Kuhusu ujenzi wa Viwanda, kwa kipindi cha miaka 2 iliyopita takriban Viwanda vipya 3,306 vimejengwa, na hizi ni takwimu za mwezi Juni 2017. Lakini jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba viwanda vingine vinajengwa na hata vile vya zamani vimeanza kufufuliwa. Mathalan, Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii (NSSF, ZSSF, PSPF, GEPF, Bima ya Taifa ya Afya, LAPF na WCF) hivi sasa inatekeleza miradi takriban 15 ya viwanda, ambavyo nimeambiwa kuwa vitazalisha takriban ajira 350,000. Baadhi ya miradi ni ulimaji wa mashamba ya Miwa na ujenzi wa Viwanda vya Sukari vya Mkulazi na Mbigiri mkoani Morogoro, ambako pia kutakuwa na uzalishaji wa umeme utakaoingizwa kwenye Gridi ya Taifa; Ufufuaji wa Vinu vya Kusindika Nafaka na Ukamuaji Mafuta vya Shirika la Usagishaji la Taifa (National Milling Corporation – NMC) vilivyopo hapa Dodoma, Iringa na Mwanza; Ufufuaji wa Kiwanda cha Bidhaa za Ngozi pale Karanga, Moshi Mjini; Kiwanda cha Katani na Agave Syrup itokanayo na mabaki ya mkonge Mkoani Tanga; Kiwanda cha Madawa TPI Arusha; Kiwanda cha Kutengeneza Matofali ya Kuchoma na Vigae hapa Dodoma; Kiwanda cha Kusindika Tangawizi Kilimanjaro; Kiwanda cha Nyama cha Nguru Ranch Morogoro; Kiwanda cha Mvinyo wa Zabibu hapa Dodoma; Kiwanda cha bidhaa za hospitali (pamba na maji tiba) Simiyu, n.k. Naipongeza Mifuko hii kwa kuitikia wito wa Serikali wa kujenga viwanda. Na hii ndio sababu nahimiza Chama chetu nacho kushiriki katika utekelezaji wa ahadi hii.
Ndugu Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Wageni wetu Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Nimezungumza mengi. Hivyo basi, napenda nihitimishe hotuba yangu kwa kuwashukuru wajumbe wa Mkutano huu kwa kuhudhuria kwa wingi. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru, Makamu wangu wawili, Mheshimiwa Dkt. Shein na Mzee Mangula kwa ushirikiano mkubwa walionipa tangu nilipochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama chetu mwezi Julai mwaka jana. Nimejifunza na naendelea kujifunza mambo mengi kupitia kwao. Lakini, kwa namna ya pekee, namshukuru Mzee Kinana pamoja na Sekretarieti ya Chama kwa ujumla kwa kunisadia katika kutenda kazi za Chama na kufanya mageuzi mbalimbali. Nakushukuru sana Mzee Kinana. Na ni matarajio yangu kuwa Mzee huyu ataendelea kunisaidia katika kazi.
Napenda pia kutumia fursa hii, kuwashukuru wageni wetu waalikwa, Wawakilishi pamoja na Mabalozi mnaowakilisha Vyama Rafiki vya CCM kutoka nchi mbalimbali. Tunawashukuru sana kwa kushiriki nasi katika Mkutano huu. Napenda pia kuwashukuru wawakilishi wa vyama shindani mliohudhuria Mkutano huu. Mmeonesha ukomavu mkubwa wa kisiasa. Licha ya tofauti zetu za kiitikadi, lengo letu sisi sote ni kuijenga nchi yetu. Hii ndio sababu nimefarijika sana kwa kuja kuhudhuria Mkutano huu. Ahsanteni sana. Maendeleo hayana Chama japo naamini kuwa maendeleo ya kweli yataletwa na CCM.
Nitumie fursa hii pia kuwashukuru viongozi wetu wastaafu, wakiwemo Wenyeviti na Makamu Wenyeviti Wastaafu, Makatibu Wakuu Wastaafu, pamoja na na wazee wetu wengine, wakiwemo mama zetu wapendwa, Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume kwa kuja kushiriki nasi kwenye Mkutano huu. Tunawashukuruni sana.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru viongozi na wanachama wapya ambao wamejiunga na Chama chetu hivi karibuni. Na napenda kuwaarifu kuwa wapo wengi wanaotamani sana kujiunga na Chama chetu.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa Mkutano Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi umefunguliwa rasmi hapa Dodoma. Nawatakia wajumbe wenzangu Mkutano mwema na maamuzi ya busara.
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!
Mapinduzi, Daima!
Mungu Wabariki Wajumbe wa Mkutano huu!
Mungu Ibariki CCM!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Dec 14, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA CHAMA CHA WALIMU TANZANIA (...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Mwalimu Leah Ulaya, Kaimu Rais
wa Chama Cha Walimu Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Seleman Jafo, Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais – TAMISEMI;
Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu
na Mafunzo ya Ufundi;
Mheshimiwa George Mkuchika, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais – UTUMISHI;
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu;
Waheshimiwa Mwalimu Janet Magufuli,
Mke wa Rais, na Mwalimu Mary Majaliwa, Mke wa Waziri Mkuu;
Mheshimiwa Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Mheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama
vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);
Ndugu Katibu Mtendaji wa Tume ya Utumishi wa Walimu;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi
mliohudhuria kutoka Ndani na Nje ya Tanzania;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa
wa Chama Cha Walimu Tanzania;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote napenda niwashukuru sana walimu kwa kunikaribisha. Kwangu mimi, leo ni siku ya pekee sana. Na nakiri kwamba nimefurahi sana. Nimefurahi, kwanza, kwa kupata fursa hii adhimu ya kuzungumza nanyi walimu wenzangu. Kama mnavyofahamu, mimi ni mwalimu. Mke wangu naye ni mwalimu. Nazijua shida na raha za ualimu. Hivyo basi, kuwepo mahali hapa, ni faraja kubwa kwangu. Lakini, jambo la pili lililonifurahisha ni kwamba, sasa nimetambua kuwa Chama Cha Walimu kimedhamiria kufanya kazi na Serikali. Ahsanteni sana walimu wenzangu. Na napenda kutumia fursa hii kuwahikikishia kuwa Serikali itashirikiana na ninyi kwa karibu.
Kabla sijaendelea zaidi, napenda nami niungane nanyi katika kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu na jamaa wa Marehemu Alhaji Yahya Msulwa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CWT, ambaye aliaga dunia tarehe 17 Novemba, 2017, wakati akiwa kwenye maandalizi ya Mkutano huu. Sambamba na hilo, kama mnavyofahamu, leo nchi yetu imeiaga rasmi miili ya askari wetu mashujaa 14 waliouawa hivi karibuni nchini DRC wakiwa katika ulinzi wa amani. Hivyo basi, naomba tuzidi kuwaombea mashujaa wetu roho zao zipumzike mahali pema pepoi. Aidha, tuwaombee mashujaa wengie waliojeruhiwa kwenye tukio hilo ili wapone kwa haraka. Amina.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Walimu Wenzangu;
Leo ni mara yangu ya kwanza kukutana rasmi na walimu tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano ya Nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru walimu kote nchini kwa kura nyingi mlizonipa zilizoniwezesha kuibuka mshindi kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita. Ahsanteni sana walimu wenzangu. Nawaahidi kufanya kazi kwa bidii kwa manufaa ya Watanzania wote.
Napenda pia kutumia fursa hii, kutoa shukrani zangu nyingi kwa uongozi wa CWT kwa uamuzi wenu wa kuhamishia Mkutano huu hapa Dodoma. Kama mnavyofahamu, Mkutano huu awali ulipangwa kufanyika Arusha. Lakini baadaye, mliamua kuuhamishia hapa Dodoma. Nawashukuru sana. Hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya nchi yetu. Hapa pia ni Makao Makuu ya Ofisi za Bunge. Aidha, hapa ni mahali ambako, chuo kikubwa zaidi katika eneo zima la Afrika Mashariki na Kati, Chuo Kikuu cha Dodoma, kipo. Hivyo basi, nina imani kuwa Wajumbe wa Mkutano wamefurahi kuja kufanya mkutano wao hapa Dodoma.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sekta ya elimu ni nyeti na muhimu katika jamii na pia kwa maendeleo ya Taifa lolote. Sisi Waswahili tuna msemo usemao “Elimu ni Ufunguo wa Maisha”. Marafiki zetu Wachina nao wana msemo usemao, naomba niunukuu kwa Lugha yetu adhimu ya Kiswahili, “Ukitaka kuwekeza kwa mwaka mmoja, panda mpunga; Ukitaka kuwekeza kwa miaka kumi, panda miti; lakini ukitaka kuwekeza katika maisha, wekeza kwenye elimu”. Hii yote ni katika kudhihirisha kuwa elimu ni muhimu kwa mtu mmoja mmoja, katika jamii na kwa maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Na bila shaka, kwa kutambua umuhimu huo, Serikali za Awamu zote za nchi yetu, ya kwanza hadi ya sasa, imeweka mkazo mkubwa katika kukuza na kuboresha sekta hii. Juzi kwenye Maadhimisho ya Sherehe za Uhuru nimeeleza kuwa wakati tunapata Uhuru, mwaka 1961, baada ya utawala wa Kikoloni uliodumu kwa takriban miaka 76, nchi yetu ilikuwa na shule za msingi 3,100. Lakini katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru wetu, tumeweza kujenga shule za msingi mpya 14,279 na hivyo kutufanya tuwe na jumla ya shule za msingi 17,379. Katika kipindi hicho Shule za sekondari zilikuwa 41, lakini hivi sasa zipo 4,817. Tulikuwa na Chuo Kikuu kimoja, lakini leo hii tuna vyuo vikuu 48.
Mtakubaliana nami kuwa haya ni mafanikio makubwa sana. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi zangu nyingi kwa viongozi wa awamu zote za nchi yetu kwa kufanikisha kupatikana kwa mafanikio haya. Pamoja na pongezi hizo nilizozielekeza kwa viongozi watangulizi wangu, upo usemi usemao “unaweza kuwa na shule, chuo au chuo kikuu bila ya kuwepo kwa majengo, vitabu, madawati, maabara, chaki na kalamu; lakini kamwe huwezi kuwa na shule au chuo bila ya walimu”. Kwa maana hiyo, pongezi nyingi zaidi inafaa ziwaendee ninyi walimu. Hivyo basi, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi nyingi sana kwenu walimu kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya ya kuwaelimisha Watanzania. Kwa hakika, walimu mnafanya kazi kubwa sana. Hongereni na ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CWT;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema hapo awali, Serikali za Awamu zilizotangulia zimefanya juhudi kubwa za kukuza na kuendeleza sekta ya elimu nchini. Kwa lengo la kuendeleza mafanikio hayo, na sisi Serikali ya Awamu ya Tano tunachukua hatua mbalimbali za kupanua wigo na kuboresha sekta ya elimu. Kama mnavyofahamu, hivi sasa tunatekeleza elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo awali tulikuwa tukitenga shilingi bilioni 18.77 kwa mwezi kugharamia, lakini kuanzia mwezi Julai 2016 tuliongeza fedha hizo hadi kufikia shilingi bilioni 23.868. Hii maana yake ni kwamba, tangu utaratibu huu uanze mwezi Desemba 2015 hadi Novemba 2017, Serikali imetumia kiasi cha takribani shilingi bilioni 535.
Ninyi walimu ni mashahidi wazuri. Uamuzi wa Serikali wa kuanzisha elimu bila malipo, umeleta mafanikio makubwa sana, hususan katika kuongeza idadi ya wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza. Lakini, kutokana na ongezeko hilo la wanafunzi, zilijitokeza changamoto, ikiwemo upungufu wa madawati, vyumba vya madarasa, pamoja na vifaa na vitendea kazi vingine. Kutokana na matatizo hayo, Serikali ilianza kuchukua hatua ili kushughulikia.
Tulishirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo wananchi, na kuweza kupunguza kwa takriban asilimia 95 tatizo la madawati kwenye shule zetu za msingi na sekondari nchini kote. Aidha, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, Serikali imejenga na kukarabati miundombinu katika shule za msingi na sekondari 365, zikiwemo shule za sekondari kongwe 88; kwenye halmashauri 129. Miundombinu hiyo ni nyumba za walimu 12, vyumba vya madarasa 1,435, mabweni 261, majengo ya utawala 11, mabwalo 6, matundu ya vyoo 2,832, maktaba 4, na visima vya maji safi 4. Aidha, katika bajeti ya Mwaka huu wa Fedha 2017/2018, Serikali, kupitia bajeti ya Halmashauri, imetenga shilingi bilioni 126.65 kwa ajili ya kujenga na kukarabati miundombinu ya shule za msingi na sekondari, itakayojumuisha nyumba za walimu 2,364; madarasa 6,636; vyoo 9,355; madawati 118,921; mabweni 157; hosteli 176 na maabara zipatazo 1,817. Waheshimiwa Mawaziri wahusika hakikisheni haya yanatekelezwa.
Sambamba na hayo, tumeanza kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha elimu yenyewe. Ninyi walimu ni mashahidi, mwaka huu wa 2017 tumegawa vifaa vya maabara kwenye shule za sekondari 1,696 pamoja na vifaa vya wanafunzi wenye mahitaji maalum katika shule za msingi 213 na shule za sekondari 22.
Ukiachilia mbali Elimu ya Msingi na Sekondari, Serikali pia inaboresha Elimu ya Juu, hususan kwa kutoa mikopo kwa wanafunzi. Idadi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu wanaopewa mikopo imeongezeka kutoka 98,300 mwaka 2015 hadi kufikia takriban 124,000 hivi sasa. Hii imewezekana baada ya Serikali kuongeza bajeti ya mikopo kutoka shilingi bilion 373 hadi kufikia shilingi bilion 483. Wanafunzi walimu wanaonufaika na mikopo ya elimu ya juu ni 22,867, ambapo mwaka huu Serikali itatumia shilingi billion 79.63 kuwagharamia. Na ninyi wenyewe ni mashahidi kuwa hivi sasa mikopo inatolewa kwa wakati; na hata rufaa za mikopo hivi sasa zinashughulikiwa mapema. Wito wangu kwa walimu wanaopata mikopo; wakimaliza, wakubali kufanya kazi kwenye vituo wanavyopangiwa.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Mbali na kupanua wigo na kuboresha sekta ya elimu, tunafanya jitihada za kuboresha maslahi na kushughulikia kero mbalimbali za walimu. Hivi punde mmemsikia Kaimu Katibu Mkuu wa CWT akiipongeza Serikali kwa jitihada inazofanya kuboresha maslahi ya walimu na kushughulikia kero mbalimbali zinazowakabili. Mathalan, ameipongeza Serikali kwa kutoa Waraka wa Muundo Mpya wa Watumishi wa Walimu; Upandishwaji madaraja ya Walimu; uanzishaji wa Tume ya Utumishi wa Walimu, n.k.
Lakini, licha ya hatua hizo, Serikali pia imefanya mambo mengine mengi ya kuboresha maslahi na kushughulikia kero za walimu. Mathalan, awali nilieleza kuwa Serikali iliongeza kiwango cha ruzuku inayopelekwa kwenye shule kutoka shilingi bilioni 18.77 hadi shilingi bilioni 23.868 kwa mwezi. Kiasi kilichoongezeka ni mahususi kwa ajili ya kutoa posho za madaraka kwa Wakuu wa Shule na Waratibu wa Elimu Kata. Tangu utaratibu huu uanze tayari tumetoa shilingi bilioni 86.56. Niwaombe watu wanaopewa, posho hizo ziwaongezee motisha ya kufanya kazi kwa maslahi ya Taifa. Aidha, naziagiza mamlaka za uteuzi kutoa vyeo kwa watu wenye sifa na wenye kustahili.
Sambamba na hilo la kutoa posho, tangu tumeingia madarakani, tumetoa kiasi cha shilingi bilioni 56.92 kulipia madeni ya walimu, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 14.23 tumelipa madeni ya mshahara na shilingi bilioni 42.69 ni madeni yasiyo ya mshahara. Kadri tutakavyokamilisha uhakiki wa madeni, tutalipa madeni yote halali.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
NduguWajumbe wa Mkutano;
Licha ya jitihada mbalimbali zilizofanywa na Serikali katika kuimarisha sekta ya elimu na kuboresha maslahi ya walimu nchini, ni dhahiri kuwa sekta ya elimu na ninyi walimu wenyewe bado mnakabiliwa na matatizo kadhaa. Mathalan, tuna upungufu wa madarasa, vyoo, nyumba za walimu, madawati na maabara.
Sambamba na matatizo hayo, hivi punde, Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, katika Risala yake, ameeleza matatizo na kero mbalimbali zenye kuwakabili walimu. Ametaja suala la upandishaji vyeo kwa wakati; suala la walimu waliopandishwa madaraja mwaka jana na kisha kusitishwa; malipo ya walimu wastaafu; suala la posho ya kufundishia (teaching allowance); upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi; n.k. Amezungumzia pia hofu mliyonayo walimu kuhusu uwezekano wa kupungua kwa mafao ya kustaafu kufuatia uamuzi wa kuiunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii ili ibaki miwili.
Kama nilivyotangulia kusema hapo awali, mimi ni mwalimu. Hivyo basi, hata kabla sijawa Rais, nilikuwa nikizifahamu shida na matatizo mbalimbali yanayowakabili walimu wa Tanzania. Na kama nilivyosema, Mke wangu, naye ni mwalimu; na amekuwa kila mara akinikumbusha kuhusu masuala ya walimu. Lakini, mbali na yeye, kwa bahati nzuri viongozi wengi niliowateua kushika nyadhifa mbalimbali ni walimu. Waziri Mkuu ni mwalimu. Mke wake ni mwalimu Hapa pia tunao Mawaziri Mhagama na Prof. Ndalichako, ambao wote ni walimu. Na wote hawa wamekuwa wakiwatetea sana. Lakini zaidi ya hapo, Makamu wa Rais, Mama Samia, naye ni mtetezi mkubwa sana wa walimu. Kwa hiyo, viongozi wote wamekuwa wakiwatetea sana ninyi walimu.
Na niseme tu kuwa, kutokana na kazi kubwa ambayo ninyi walimu mnayoifanya, ni haki yenu kutetewa na kwa kweli Serikali inao wajibu wa kuhakikisha inashughulikia shida na kero zenu. Mimi binafsi natamani sana; tena sana, kuona shida mbalimbali za walimu zinaisha kabisa. Hata haya, matatizo mliyonieleza leo ningetamani sana nitoe majibu yake yote hapa hapa ili yaweze kushughulikiwa mara moja. Lakini, hilo ni jambo lisilowezekana. Kama mnavyofahamu, uwezo wa Serikali bado mdogo na majukumu iliyonayo ni mengi. Mbali na kushughulikia sekta ya elimu, tunawajibika kushughulikia masuala ya afya, maji, umeme, barabara, ulinzi, n.k., ambayo yote haya ni muhimu kwa nchi, lakini pia ni muhimu hata kwenu ninyi walimu. Walimu mnahitaji huduma bora za afya, mnahitaji maji, umeme, barabara, ulinzi na usalama, n.k.
Kwa sababu hiyo, Serikali inawajibika kuhakikisha kuwa kidogo kinachopatikana, tunakigawa kwenye sekta zote muhimu. Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alipata kusema, nanukuu, “Ndama hunyonya kiwango cha maziwa ambacho mama yake anacho”. Hivyo, nawasihi sana walimu wenzangu, kwa kile kidogo tunachokileta kwenu mkipokee na kuiona dhamira nzuri ya Serikali ya kushughulikia shida na kero zenu mbalimbali. Napenda tu niwahakikishie kuwa Serikali inatambua kero zenu zote na kadri uwezo wa Serikali kifedha utakavyokuwa ukiongezeka, tutaendelea sio tu kuboresha maslahi yenu bali sekta ya elimu kwa ujumla.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano huu;
Pamoja na maelezo hayo, napenda kutolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizotolewa na Kaimu Katibu Mkuu katika Risala yake. Moja ya hoja aliyoizungumza ni uhaba wa walimu wa sayansi nchini. Ni kweli kuwa tatizo hili lipo na limeongezeka baada ya Serikali kuanza kutoa elimu bila malipo, ambapo idadi ya wanafunzi kwenye shule zetu imeongezeka. Serikali inachukua hatua mbalimbali kushughulikia tatizo hili. Mwaka huu pekee tumeajiri walimu wa masomo ya sayansi na hisabati wapatao 3,462. Aidha, walimu wengine wapatao 15,135, wakiwemo wa sayansi, wanatarajiwa kuajiriwa wakati wowote baada ya vyeti vyao kuhakikiwa na kuthibitishwa uhalali wake.
Vilevile, tunaendelea kupanua wigo wa kuzalisha walimu. Mathalan, kati ya wanafunzi 22,867 wanaosomea ualimu niliowataja awali na ambao Serikali inawapa mikopo ya vyuo vikuu, wanafunzi 13,510 ni wa masomo ya sayansi na hesabu. Zaidi ya hapo, Serikali ipo katika ukarabati wa vyuo vyake takriban 20 na ujenzi wa vyuo 3. Ujenzi na ukarabati huu utakapokamilika, utaongeza idadi ya udahili wa wanafunzi wa ualimu kutoka 20,535 hadi kufikia wanafunzi takriban 30,000. Hatua hizi, bila shaka, zitapunguza tatizo la uhaba wa walimu.
Hata hivyo, nafahamu kuwa wakati mwingine, tatizo la uhaba wa walimu linatokana na mgawanyo usio linganifu. Shule nyingi za mijini zina walimu wengi kuliko mahitaji yake. Hivyo niziombe Mamlaka husika kuliangalia suala hili kwa umakini. Lakini huu usiwe mwanya wa kuwahamisha walimu bila kufuata utaratibu. Agizo langu kuhusu kutomhamisha mwalimu mpaka atakapolipwa stahiki zake liko pale pale. Lakini pia nitoe wito kwenu walimu; mkipangiwa kazi mahali, mkubali kwenda.
Suala jingine ambalo Kaimu Katibu Mkuu amelizungumzia ni hofu mliyonayo kuhusu uwezekano wa kupungua kwa malipo ya mkupuo baada ya kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii. Hakuna kitakachopungua. Lengo la Serikali kuiunganisha mifuko ya jamii na kubakisha miwili ni kuongeza ufanisi na tija katika mifuko hiyo. Kama mnavyofahamu, kutokana na mifuko kuwa mingi, ililazimu kila mfuko kutumia fedha nyingi kutafuta wanachama. Jambo hili liliongeza gharama za uendeshaji kwenye mifuko hiyo na hivyo kusababisha mifuko hiyo kutoa mafao madogo ya kustaafu kwa wanachama wake. Sasa tumeamua kuwa na mifuko miwili tu; mmoja kwa ajili ya watumishi wa umma na mwingine sekta binafsi. Hii itasaidia sio tu kuondoa ushindani usio na tija, bali pia unatarajia kuiwezesha mifuko hii kutoa mafao mazuri zaidi kwa wanachama wake wanaostaafu. Hivyo basi, napenda kuwatoa hofu walimu wenzangu kwamba mafao hayatapungua. Lakini sambamba na hilo, sheria ya kuunganisha mifuko bado haijatungwa. Mswada umesomwa mara moja Bungeni. Na sasa maoni ya wadau mbalimbali yanaendelea kupokelewa. Hivyo, na ninyi CWT mnayo nafasi ya kuendelea kutoa maoni yenu ili kuboresha mswada huo.
Kuhusu suala la posho ya kufundishia (teaching allowance), mtakumbuka kuwa kwa mujibu wa Waraka wa Watumishi wa Serikali Na.1 wa mwaka 1996 kuhusu Mfumo, Miundo na Ngazi Mpya za Mishahara kwa Watumishi wa Serikali kuanzia tarehe 1 Julai, 1996 posho zote zilijumuishwa katika mishahara. Lengo lilikuwa kuboresha mishahara na mafao ya uzeeni ya Watumishi. Kufuatia utekelezaji wa Waraka huo, nyongeza halisi ya mshahara wa kima cha chini baada ya kujumuishwa posho katika mishahara ilikuwa ni asilimia 55.2; na nyongeza halisi ya kima cha juu baada ya kujumuishwa posho katika mshahara ilifikia asilimia 36.9. Hii ndio sababu posho ya kufundishia waliyokuwa wakipewa walimu, iliondolewa. Pamoja na maelezo hayo, natambua umuhimu wa posho hii. Hivyo, napenda kurudia tena kadri mama ndama atakapoongeza maziwa, tutaangalia uwezekano wa kurejesha posho hii ili kuwapa motisha walimu wetu. Hivyo, nawaomba Watanzania tuchape kazi kwa bidii ili kuongeza uwezo wetu kiuchumi.
Kuhusiana na suala la mafunzo kwa walimu, Serikali inafahamu umuhimu wa kuwapatia mafunzo endelevu ya mara kwa mara walimu wetu. Na kwa kweli tumekuwa tukifanya hivyo. Jumla ya walimu 5,920 wa masomo ya sayansi, hisabati na kiingereza wamepata mafunzo hivi karibuni. Na tutaendelea kutoa mafunzo hayo.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano huu;
Suala jingine ambalo ningependa nilizungumzie ni kuhusu madeni mbalimbali ya walimu. Serikali inatambua uwepo wa madeni hayo. Na tumekuwa tukiyalipa. Kama nilivyosema awali, tangu tumeingia madarakani tayari tumelipa madeni ya walimu yenye thamani ya shilingi bilioni 56.92. Lakini, madeni bado yapo. Hivi punde Kaimu Katibu Mkuu wenu ameeleza kuwa hivi sasa walimu wanaidai Serikali kiasi cha shilingi bilioni 25.6. Napenda, kwanza kabisa, kuwapongeza viongozi wa CWT kwa kuwa wakweli. Nakumbuka kuwa kuna wakati aliwahi kujitokeza mmoja wa viongozi wa CWT na kusema kuwa walimu wanaidai Serikali takriban shilingi trilioni 1.5. Hivyo, nawapongeza sana viongozi wa sasa wa CWT kwa kuwa wakweli. Na kwa kuwa mmeonesha uungwana na mmekuwa wakweli, napenda kuwahakikishia kuwa mara tu tutakapomaliza kuhakiki deni hili, tutawalipa mara moja.
Lakini pia ningependa kutumia fursa hii kueleza kuwa, Serikali imekuwa ikichelewa kulipa madeni yenu pamoja na ya watumishi wengine wa umma, kutokana na kuwepo kwa matatizo kadhaa, ikiwemo tatizo la watumishi hewa na wenye vyeti feki. Hii ndio sababu mwaka jana tuliamua kusitisha zoezi la upandishaji vyeo na madaraja kwa watumishi; na tukaanzisha zoezi la uhakiki kwa watumishi wote wa Serikali. Zoezi la uhakiki mpaka sasa limetuwezesha kubaini watumishi hewa wapatao 19,706, ambao walikuwa wakiigharimu Serikali kiasi cha shilingi bilioni 19.848 kwa mwezi, sawa na shilingi bilioni 238.17 kwa mwaka. Aidha, tumeweza kubaini watumishi wenye vyeti feki wapatao 12,000, wakiwemo walimu 3,655. Baada ya kukamilisha zoezi hili, Serikali mwezi Novemba 2017, imewapandishaji vyeo watumishi 59,967, wakiwemo walimu na ambao marekebisho ya mishahara yao itaanza kutolewa kuanzia mwezi huu. Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 159.33 kwenye bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya marekebisho hayo ya mishahara.
Na kuhusu zoezi la uhakiki wa madeni, lenyewe bado linaendelea. Na kimsingi, zoezi hili ni endelevu. Hata hivyo, nawahakikishia kuwa kadri tutakavyokuwa tunakamilisha uhakiki wa madeni tunayodaiwa, tutayalipa. Wito wangu kwenu walimu wenzangu, endapo unafahamu kuwa katika madeni uliyowasilisha Serikalini kuna udanganyifu, ni vyema ujaze upya. Na niwaombe viongozi wa CWT kupitia tena madeni yote ya walimu ili kujiridhisha; na mkijiridhisha pelekeni madeni hayo kwa viongozi wa Wilaya na Mikoa, nao wakijiridhisha na kuweka saini zao; baada ya hapo madeni hayo yawasilishwe kwa Waziri Mkuu. Nawaahidi kuwa, Serikali ikijiridhisha kuwa madeni hayo ni sahihi, tutayalipa mara moja. Lakini nitoe onyo kwamba, endapo itatokea mtu ameidhinisha madeni yenye udanganyifu, naye tutawachukulia hatua.
Kuhusiana na hoja zenu nyingine mlizoziwasilisha, ikiwemo upandishaji wa vyeo kwa wakati; Serikali kutoa mikopo ya ujenzi wa nyumba isiyo na riba; uhaba wa vifaa vya kufundishia; kushirikishwa katika mabadiliko yoyote ya mitaala; masomo ya TEHAMA; Serikali imepokea hoja zenu zote na tutashirikiana nanyi katika kuzitafutia ufumbuzi. Nafahamu baadhi ni masuala ya kiutendaji tu na hayahitaji gharama yoyote; hivyo, naziagiza mamlaka husika kushughulikia kwa haraka. Na kwa yale yenye kuhitaji fedha, tutaendelea kuyashughulikia taratibu, kadri uwezo wa Serikali kifedha utakavyokuwa ukiimarika.
Waheshimiwa Viongozi;
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Jukumu langu leo ni kufungua tu Mkutano wenu. Lakini kabla sijatekeleza suala hili, ninalo suala moja la mwisho ambalo ningependa kulizungumza. Nafahamu kuwa, kwenye Mkutano huu, pamoja na mambo mengine, mtafanya uchaguzi wa Rais wa CWT kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Rais wenu Mstaafu, Mwalimu Gratian Mukoba. Napenda kutumia fursa hii kuwasihi sana walimu wenzangu, kuchagua kwa umakini mkubwa. Chagueni mtu atakayeshughulikia masuala yenu. Na kamwe msichague mtu mwenye nia ya kuitumia CWT kutekeleza maslahi yake binafsi.
Sio siri kuwa kuna wakati mliwachagua watu ili wawaongoze na kuwatumikia, lakini hawakufaya hivyo. Badala yake, walitumia Chama hiki kutekeleza maslahi yao binafsi. Na walitumia Chama chenu kujinufaisha. Niwaulize walimu wenzangu, hivi mnafahamu fedha za michango mnazokatwa kila mwezi zinatumikaje? Au mmeshawahi kujiuliza kuhusu utendaji kazi wa Benki yenu na ni namna gani inawanufaisha? Sina hakika kama mnafahamu. Lakini niwaambie, kwa taarifa nilizonazo, Benki yenu haifanyi vizuri, na ni miongoni mwa Benki ambazo wakati wowote inaweza kufungwa. Nakumbuka wakati fulani nilialikwa kwenda kuizindua lakini sikwenda, baada ya kujiridhisha kuwa Benki hiyo haifanyi vizuri na haipo kwa maslahi ya walimu. Ni watu wachache tu ndio wananufaika nayo. Hivyo basi, nawasihi tena walimu wenzangu, katika uchaguzi huu, msichague watu wenye nia ya kujinufaisha kupitia CWT.
Lakini zaidi ya hapo, msiwachague watoa rushwa. Rushwa ni ugonjwa. Ni kansa. Ukimchagua mtoa rushwa hutoweza kamwe kumuuliza michango yenu ya kila mwezi inatumikaje; na utashindwa kumuuliza manufaa yaliyopatikana kwenye Benki yenu. Hivyo basi, narudia tena kuwasihi walimu wenzangu katika uchaguzi huu chagueni vizuri. Chagueni watu watakaowatetea na kuwasemea matatizo yenu. Na kamwe msimchague mtu ambaye lengo lake ni kuigombanisha CWT na Serikali. Mapambano mara nyingi hayajengi. Na niwashauri walimu wenzangu, wakati mwingine, mkitaka kufanikisha jambo, tumieni ule usemi usemao, “If you want to win an enemy, join him and work with him…” Siwapigii kampeni; lakini kwa dhati kabisa nawapongeza viongozi wa sasa wa CWT kwa kuonesha nia ya kweli ya kuwatetea na kushughulia shida za walimu. Wameonesha kuwa wapo tofauti na wapo tayari kufanya kazi na Serikali. Huo ndio unapaswa kuwa muelekeo wa CWT hivi sasa. Mimi naamini kuwa kama Serikali na CWT tukiwa kitu kimoja tutaweza kushughulikia matatizo mengi yanayowakabili walimu tena kwa haraka.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuushukuru tena uongozi wa CWT kwa kunikaribisha kufungua Mkutano huu. Aidha, kwa namna ya pekee, naushukuru uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kukubali kuwa wenyeji wa Mkutano huu. Tunawashukuru sana na tunawashukuru pia walimu wanafunzi wa Chuo hiki kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kwenye ufunguzi wa Mkutano wa CWT.
Halikadhalika, nawashukuru viongozi wa vyama vya wafanyakazi kwa kuhudhuria kwenye Mkutano huu. Na vilevile, nawashukuru wageni wote waalikwa kutoka ndani na nje kwa kuamua kutenga muda wenu kuja kushiriki kwenye Mkutano huu. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, wajumbe wa Mkutano huu, na nawaomba mfikishe salamu kwa walimu wote nchini kuwa Serikali ipo pamoja nao.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa nimeufungua Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa CWT. Nawatakia Mkutano mwema.
Mungu Ibariki CWT!
Mungu Wabariki Walimu Wote!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Dec 13, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA TAWI JIPYA LA BENKI YA CRDB DODOMA, TAREHE 13 DESEMB...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa John Malecela, Waziri Mkuu
Mstaafu wa Tanzania;
Ndugu Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
Ndugu Ally Hussein Laay, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi
wa Benki ya CRDB;
Dkt. Charles Kimei, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo hapa;
Waheshimiwa Wazee wa Mkoa wa Dodoma;
Wageni Waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu kwa kutupa afya njema na kutuwezesha kukutana hapa leo. Napenda pia, kwa namna ya pekee kabisa, kuushukuru uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Benki ya CRDB kwa kuniliaka kushiriki kwenye tukio hili la kuzindua Tawi la Benki yenu hapa Dodoma.
Napenda kukiri kuwa nimefurahi sana kushiriki kwenye hafla hii. Nimefurahi kwa sababu kwanza mimi ni mteja wa Benki ya CRDB kwa muda mrefu; tangu nikiwa Mwanafunzi wa Chuo Kikuu. Zaidi ya hapo, hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya nchi yetu. Ni hivi karibuni tu tumefanya maamuzi makubwa ya kuhakikisha Serikali yote inahamia Dodoma ifikapo mwaka 2020. Kama mnavyofahamu, Waziri Mkuu pamoja na Viongozi na Watendaji wa Wizara tayari wamehamia. Aidha, Makamu wa Rais naye anatarajiwa kuhamia mwezi huu; na mimi nitahamia mwakani.
Ni dhahiri kuwa, kutokana na uamuzi huu wa kuhamia Dodoma, idadi ya watu katika Mji huu hapa itaongezeka sana. Na huduma za taasisi kama za benki zitahitajika zaidi. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuushukuru na kuupongeza uongozi wa Benki hii kwa uamuzi wenu wa kufungua Tawi hili hapa Dodoma. Kwa kufungua Tawi hili, mmeunga mkono uamuzi wa Serikali wa kuhamia Dodoma. Ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sekta ya benki ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi. Ni muhimu kwanza kabisa katika ukuzaji uchumi. Sekta ya benki inatoa mchango mkubwa katika pato la taifa. Mathalan, mwaka 2014, sekta hii ilichangia asilimia 3.4 ya pato la taifa; mwaka 2015 na mwaka jana 2016 ilichangia asilimia 3.6. Aidha, benki zinachangia ukuaji uchumi kupitia ulipaji wa kodi kwa Serikali. Hivi punde mmetoka kumsikia Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt. Kimei, akisema kuwa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita Benki yake imelipa kodi zaidi ya shilingi bilioni 800 na hivyo kuiwezesha kushinda tuzo ya kuwa mlipaji kodi bora mara kadhaa. Hongereni sana CRDB.
Lakini mbali na kukuza uchumi, sekta ya benki ni muhimu katika kupiga vita umaskini. Benki zinashiriki katika kupiga vita umaskini, kupitia kwanza mikopo inayoitoa kwa wananchi, hususan wafanyabiashara na wajasiliamali wadogo kama vile machinga na mama lishe. Pili, zinachangia kupiga vita umaskini kwa namna inavyoshiriki katika kukuza sekta nyingine. Kama mnavyofahamu, sekta ya benki ni muhimu sekta nyingine zote. Iwe viwanda, kilimo, uvuvi, ufugaji, ujenzi, biashara, usafirishaji; na hata sekta za huduma kama afya, elimu, maji, n.k. Kwa mfano, benki ikitoa mkopo wa mtaji wa kujenga kiwanda; kupitia mkopo huo, wananchi watapata ajira wakati wa ujenzi na baada ya kiwanda kukamilika. Fikiria pia benki ikitoa mkopo kwa ajili ya ujenzi wa barabara; wakati wa ujenzi wa barabara hiyo wananchi wanapata ajira, lakini pia ikikamilika itapunguza gharama na usafiri kwa wananchi, na hivyo kusaidia kupunguza umaskini.
Sambamba na hayo, sekta ya benki ni umuhimu kwa vile inatoa ajira za moja kwa moja. Mathalan, nimeambiwa kuwa Benki hii imetoa ajira kwa Watanzania wapatao 3,200. Lakini pia sekta ya benki ni muhimu kwa vile inawasaidia wananchi kutunza amana (fedha) kwa usalama, na wakati wowote wakihitaji, wanapewa. Tena kwa siku hizi, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, hata ukihitaji fedha zako usiku wa manane unazipata kwa njia ya ATMs au Simu kiganjani.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kwa kuzingatia hayo yote, ni dhahiri kuwa sekta ya benki ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa lolote. Na kwa sababu hiyo, inatia moyo kuona kuwa kwa takriban miongo mitatu iliyopita, sekta ya benki imezidi kuimarika hapa nchini. Mathalan, mwaka 1990, nchi yetu ilikuwa na benki 3 tu, lakini kwa sasa nchi yetu ina zaidi ya benki 58. Na jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba miongoni mwa benki zinazofanya vizuri ni Benki hii ya CRDB, ambayo kwa takriban asilimia 86 zinamilikiwa na Watanzania (asilimia 40 watu binafsi, asilimia 21 Serikali na mifuko ya pensheni ina asilimia 15).
Hivi punde, Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Kimei, ameeleza mafanikio ambayo Benki hii imepata tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996. Baadhi ya mafanikio aliyoyataja ni kuongezeka kwa rasilimali zake kutoka thamani ya shilingi bilioni 54 hadi kufikia shilingi trilioni 5.5; kupanua wigo wa benki kutoka matawi 19 hadi 260, ukiachilia mbali ATMs 600 ilizonazo, Mawakala 3,000, SACCOS shirikishi 455 na matawi ya kutembea 21. Benki pia imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi trilioni 3.5; ambapo shilingi trilioni 1 zimekwenda kwenye sekta mbili za kilimo na viwanda. Aidha, kama nilivyosema awali, benki imelipa kodi ya shilingi bilioni 800 na kutoa ajira 3,200 kwa Watanzania. Vilevile, mwaka huu, baada ya kuwabana sana hatimaye wametoa gawio la shilingi bilioni 19 kwa Serikali. Na natumaini wataendelea kutupa gawio letu kila mwaka. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kwa dhati kabisa, kutoa pongezi nyingi sana kwa Benki hii chini ya Dkt. Kimei kwa kazi kubwa inazofanya kwa ajili ya kukuza uchumi lakini pia kupiga vita umaskini katika nchi yetu.
Mtakumbuka kuwa Benki hii kihistoria ilikuwa ikimilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali, wakati huo ikijulikana kama Tanzania Rural Development Bank (TRDB). Mwaka 1996 ilibinafsishwa ili kuongeza ufanisi wake. Kwa mfano mzuri uliooneshwa na Benki hii, ni dhahiri kuwa kama mashirika na taasisi zote zilizobinafsishwa zingefanya kazi kama Benki hii, nchi yetu ingekuwa imepiga hatua kubwa za kimaendeleo. Lakini mashirika na viwanda vingi vilivyobinafsishwa, hivi sasa havifanyi kazi.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kufungua benki hii. Hata hivyo, kabla sijatekeleza jukumu hilo, ninayo masuala machache ya kueleza. Suala la kwanza kabisa, ni malalamiko kuhusu kupungua kwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi. Serikali inalitambua suala hili, na kupitia Benki Kuu, imechukua hatua mbalimbali kulishughulikia. Mathalan, Mwezi Aprili, mwaka huu tuliamua kupunguza kiwango cha kisheria cha sehemu ya amana inayotakiwa kuwekwa benki kuu na benki za Biashara kutoka asilimia 10 hadi asilimia 8. Sambamba na hilo, tumeshusha riba ya Benki Kuu (discount rate) mara mbili kutoka asilimia 16 hadi 12 mwezi Machi 2017, na mwezi Agosti tukaishusha tena hadi asilimia 9. Pamoja na hayo, tumetoa mikopo maalum kwa benki za biashara na halikadhalika Benki Kuu inanunua fedha za kigeni kwenye soko la jumla la benki ili kuongeza ukwasi wa shilingi kwenye uchumi. Hatua nyingine tulizochukua ni kuendelea mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuongeza chachu katika shughuli za uchumi.
Kutokana na hatua hizi, hali ya ukwasi imeanza kuimarika na kusaidia kupunguza riba katika soko la fedha baina ya benki (IBCM rate) kutoka asilimia 13.69 mwezi Desemba 2016 hadi asilimia 3.29 mwezi Novemba 2017. Aidha, riba katika soko la dhamana za Serikali zimepungua kutoka wastani wa asilimia 15.12 mwezi Desemba 2016 hadi asilimia 8.76 mwezi Novemba 2017. Kwa matokeo haya, tuna matumaini makubwa kuwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi utazidi kuimarika katika siku za hivi karibuni.
Suala jingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu benki kushiriki kwenye shughuli za maendeleo. Kama nilivyosema hapo awali, sekta ya benki ni muhimu kwenye sekta zote, ikiwemo viwanda na kilimo. Hivyo basi, napenda kutoa wito kwa benki zote nchini kuangalia wa kutenga fedha nyingi za mikopo kwenye sekta hizi mbili. Kama mnavyofahamu, nchi yetu kwa sasa imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda; na miongoni mwa viwanda tunavyolenga kuvijenga ni vile vinavyotumia zaidi malighafi za hapa nchini, hususan mazao ya kilimo. Hivyo basi, naziomba benki kuunga mkono dhamira hiyo ya Serikali. Nimefurahi kusikia kuwa ninyi CRDB mmekuwa mkitenga asilimia 15 kwa ajili ya sekta ya viwanda, na mwakani mmepanga kuongeza hadi kufikia asilimia 20, sawa na shilingi bilioni 700. Hongereni sana. Na naziomba benki nyingine ziige mfano wenu.
Napenda pia kuzungumzia kidogo suala la benki kupanua wigo wa mtandao wenu. Ni kweli kuwa idadi ya benki imeongezeka hapa nchini. Lakini kwa bahati mbaya, benki nyingi zipo Dar es Salaam na kwenye baadhi ya miji mikuu ya mikoa na wilaya. Mathalan kwa taarifa za mwaka 2015 asilimia 36.3 ya matawi yote ya Benki yalikuwa Dar es Salaam asalimia 7.1 Arusha, asilimia 6.5 Mwanza, asilimia 5.4 Mbeya na asilimia 4.6 Moshi. Ni benki chache tu ndizo zina matawi kwenye vijijini. Hivyo, natoa wito kwenu kusambaza huduma zenu hadi vijijini, ambako Watanzania wengi wanaishi. Na ninaposema kusambaza huduma hadi vijijini simaanishi kwamba lazima mjenge majengo, ninachomaanisha ni kwenu ninyi kubuni njia mbalimbali za kufikisha huduma za kibenki kwa wananchi waliopo vijijini, ikiwemo kuanzisha matawi mengi zaidi ya kutembea, kuingia ubia na mawakala (Bank Agents), kuanzisha huduma za kifedha za kwa njia za mtandao (Sim Banking, Internet Baking n.k.) kama ambavyo ninyi CRDB na baadhi ya Benki nyingi mmeanza kufanya.
Nina imani mkiweza kufikisha huduma zenu hadi vijijini, sio tu mtawasaidia wananchi kupata huduma za kibenki bali pia itawaongezea benki nchini ukwasi wa kutosha. Kwa mujibu wa taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania ya mwaka 2015, ukwasi wa benki zote nchini mwaka 2014 ulikuwa una thamani ya shilingi trilioni 22.5. Kiasi hiki bado ni kidogo sana ukilinganisha na mahitaji makubwa ya fedha (mikopo) yaliyopo hapa nchini. Mathalan, Mpango wetu wa Taifa wa Maendeleo wa miaka mitano, ambao tumeanza kuutekeleza katika mwaka wa fedha 2016/2017 unahitaji kiasi cha shilingi trilioni 107. Hivyo, nawahimiza benki kusambaza huduma zenu kwenye maeneo ya vijijini ili muweze kuongeza ukwasi katika benki zenu. Aidha, nawakaribisha wawekezaji wengine kuja kuwekeza kwenye sekta hii ya benki hapa nchini.
Jambo jingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu tatizo la riba za mikopo kuendelea kuwa juu. Riba za mikopo hapa nchini bado zipo juu. Natambua kuwa tatizo hili linasababishwa na mambo mengi, ikiwemo kutokuwepo kwa taarifa za kutosha za wakopaji, wasiwasi wa benki kutolipwa na wakopaji na hivyo kuongeza gharama za ufuatiliaji, n.k. Pamoja na matatizo hayo, Serikali imechukua hatua mbalimbali, ambazo binafsi nilidhani zingeweza kushusha kiwango cha riba nchini ili kuwawezesha wananchi, hususan wa kipato cha chini kuchukua mikopo. Mojawapo ya hatua hizo ni kuanzisha Mfumo wa Kuhifadhi Taarifa za Wakopaji ( yaani Credit Reference Bureau) ambao unaziwezesha benki zote kuwatambua wakopaji na kuweza kuchukua tahadhari stahiki. Aidha, tunaendelea kutoa vitambulisho vya taifa ambavyo kwa sasa vina taarifa nyingi. Hivyo, basi naziomba benki kuanza kupunguza viwango vya riba. Aidha, naihimiza Benki Kuu kukamilisha zoezi la kutangaza Sera ya Riba (Policy Rate), ambayo itazifanya taasisi za kifedha kuwa na riba zinazowiana na sera hiyo. Vilevile, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza wananchi kuwa na utamaduni wa kurejesha mikopo. Dawa ya deni ni kulipa. Na niiombe Mahakama ya Biashara kuharakisha kesi zinazohusiana na madeni ya mikopo.
Mbali na hayo, napenda kutoa wito kwa Wizara ya Fedha na Benki ya Kuu kudhibiti matumizi ya ya fedha za kigeni (Dola) nchini. Na jambo hili, liende sawia na kuongeza usimamizi kwa Maduka ya Kubadilisha Fedha (Bureau De Change). Ni lazima tuondokane na utaratibu wa matumizi holela ya fedha za kigeni nchini; lakini pia Maduka ya Kubadilisha Fedha yasitumike kuwa sehemu za kutakatisha fedha zisizo halali kutoka nje. Aidha, natoa wito kwa Benki Kuu kuongeza usimamizi katika uanzishaji na uendeshaji wa shughuli za Kibenki hapa nchini. Kabla Benki haijaanzishwa wamiliki wake wafuatiliwe kwa makini; na halikadhalika, benki inayoshindwa kujiendesha ifutwe hata kama ni ya Serikali.
Sambamba na hayo, mtakumbuka kuwa mwezi Juni mwaka huu, nikiwa pale Kijitonyama kuzindua Kituo cha Data na Mfumo wa Ukusanyaji Mapato kwa njia ya Kielektroniki, niliagiza kuwa benki zijiunge na Mfumo huo wa kukusanya mapato kwa njia ya kielektroniki. Na nakumbuka Kamishna wa TRA aliahidi kuwa hadi mwezi Desemba makampuni yote ya benki na simu yatakuwa yamejiunga. Hivi sasa tupo katikati ya mwezi Desemba, lakini kwa taarifa nilizonazo ni benki chache tu ndizo tayari zimejiunga na mfumo huo. Benki nyingi pamoja na baadhi ya Makampuni ya Simu bado hazijajiunga na mfumo huo. Napenda kurudia tena agizo langu kwa benki na kampuni zote za simu kuhakikisha zinajiunga na mfumo huo kabla ya mwaka huu kwisha. Kwa kampuni ya simu au benki itakayoshindwa kutekeleza agizo hili, taratibu husika zifanyike, ikiwezekana makampuni au benki hizo zifungiwe kufanya kazi nchini.
Jambo la mwisho ambalo ningependa kulisema ni kutoa wito kwa Watanzania wote kutumia huduma za kibenki hususan kwa kufungua akaunti za benki. Mbali na usalama, benki inasaidia mtu kupanga matumizi yake vizuri. Unakuwa huwezi kutumia fedha ovyo. Lakini, nawasihi na nanyi wamiliki wa Benki kuimarisha mifumo yenu ya usalama ili kukabiliana na vitendo vya wizi kwa njia za mtandao. Aidha, wachukulieni hatua watumishi wenu ambao sio waaminifu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuushukuru tena uongozi wa CRDB kwa kunikaribisha na kwa zawadi ya hundi ya kiasi cha shilingi milioni 100 mliyonikabidhi. Hundi hii mmenikabidhi hadharani. Hivyo basi, na mimi naikabidhi kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ili fedha hizo zikatumike kwa ya kujenga Wodi katika Hospitali ya Mkoa. Siku moja nitakuja kuikagua hiyo wodi.
Mwisho kabisa lakini sio kwa umuhimu napenda kuwapongeza LAPF kwa kujenga jengo hili hapa Dodoma. Jengo ni zuri sana.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kufungua Tawi la Sita la Benki ya CRDB hapa Dodoma.
Mungu Ibariki CRDB!
Mungu zibariki Benki zote nchini!
Mungu wabariki wana-Dodoma!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 09, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE SHEREHE ZA MIAKA 56 YA UHURU WA TANZANIA BARA, DODOMA, TA...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Marais Wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa na Mzee Kikwete;
Waheshimiwa Viongozi Wakuu Wastaafu wa Serikali zetu mbili mliopo, Mzee Bilal, Mzee Malecela, Mzee Kificho;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi Wakuu mliopo, mkiongozwa na Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Wabunge;
Waheshimiwa Mabalozi na Viongozi wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni waalikwa wote;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Kabla ya kuanza hotuba yangu, naomba sote tusimame kwa dakika moja kuwaombea mashujaa wetu, askari 14, waliouawa wakiwa katika jukumu la kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) juzi. Tunamwomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mashujaa wetu mahali pema peponi na kuwaponya askari waliojeruhiwa. Amina.
Baada ya utangulizi huo, napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha kuiona siku hii adhimu kwenye historia ya nchi yetu. Siku kama ya leo ya Jumamosi, tarehe 9 Desemba mwaka 1961, Jamhuri ya Tanganyika, hivi sasa Tanzania Bara, ilipata Uhuru wake. Uhuru huu ulihitimisha utawala wa kikoloni uliodumu nchini kwa takriban miaka 76; ikijumuisha miaka 33 ya Utawala wa Ujerumani na miaka mingine 43 ya Utawala wa Uingereza.
Kama mnavyofahamu, harakati za kutafuta Uhuru wa nchi yetu ziliongozwa na Chama cha Tanganyika African National Union (TANU), ambacho mwaka 1977 kiliungana na Chama cha Afro Shiraz (ASP), ambacho kiliongoza mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964, na kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama Tawala. Hii ndiyo historia yenyewe. Haiwezi kubadilika. Uhuru wa nchi yetu uliletwa na Vyama Mama vya CCM, yaani TANU na ASP. Hivyo basi, leo tunaposheherekea Miaka 56 ya Uhuru wa Tanganyika (Tanzania Bara), hatuna budi kuwashukuru na kuwapongeza Wazee wetu 17, ambao mwezi Julai 1954, wakiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, walianzisha Chama cha TANU. Tunawakumbuka pia wananchi wote, ambao kabla na wakati wa Chama cha TANU, walishiriki katika harakati za kutafuta uhuru wa nchi yetu. Nafahamu wengi wao tayari wametangulia mbele za haki; hivyo, kwa niaba ya Watanzania wote, namwomba Mwenyezi Mungu azipumzishe roho zao mahali pema peponi. Amina!
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Ni ukweli usiopingika kuwa, katika kipindi cha Miaka 56 ya Uhuru wa nchi yetu, tumepata mafanikio makubwa. Ndio! tumepata mafanikio makubwa, tena sana tu. Nafahamu wapo watu ambao wakisikia kauli hiyo huwa wanaumia; lakini huo ndio ukweli. Nchi yetu imepiga hatua kubwa za maendeleo tangu kupata Uhuru. Naomba nitoe mifano michache. Wakati tunapata Uhuru, baada ya utawala wa takriban miaka 76 ya Kikoloni, nchi yetu ilikuwa na mtandao wa barabara wenye urefu kilometa 33,600. Kati ya barabara hizo ni kilometa 1,360 tu ndio zilikuwa na lami. Kwa sasa tuna mtandao barabara wenye kilomita 122,500, ambapo kilometa 80,000 zipo chini ya TAMISEMI na zinahudumiwa na TARURA; kilometa 36,000 zipo chini ya TANROADS, na kilometa 6,500 zipo chini ya Hifadhi za Wanyama za Taifa (TANAPA). Aidha kati ya Mtandao huo wa barabara, kilometa 12,679.55, ni za lami. Sambamba na hayo, kuna jumla ya kilometa 2,480 zinazoendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na barabara nyingine zenye urefu wa kilometa 7,087 zipo kwenye hatua mbalimbali za maandalizi kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Vilevile, tumejenga madaraja makubwa 17, na mengine 14 yapo kwenye hatua mbalimbali.
Ukiachilia mbali ujenzi wa barabara, wakati tunapata Uhuru, nchi yetu ilikuwa na vituo vya kutolea huduma za afya 1,095 (hospitali 98, vituo vya afya 22 na zahanati 975), leo hii tuna vituo 7,293 (hospitali 178, vituo vya afya 795 na zahanati 6,285). Wakati tunapata Uhuru tulikuwa na Shule za Msingi 3,100 hivi sasa zipo 17,379; shule za sekondari zilikuwa 41 hivi sasa zipo 4,817; na tulikuwa na Chuo Kikuu kimoja tu, lakini leo vipo 48. Madaktari waliosajiliwa walikuwa 403, ambapo kati yao Watanganyika walikuwa 12 tu, leo tuna madaktari 9,343. Mwaka 1961, Wahandisi wazalendo walikuwa wawili (2) tu; lakini hadi kufikia mwezi Juni 2017 nchi yetu imefikisha wahandisi 19,164. Makandarasi nao walikuwa wawili tu (2), lakini hivi sasa wakandarasi waliosajaliwa wamefikia 9,350. Halikadhalika, wakati tunapata Uhuru, wastani wa umri wa mtu kuishi ulikuwa miaka 37, leo hii wastani ni miaka 61. Mifano ipo mingi. Siwezi kuitaja yote leo.
Itoshe tu kusema kuwa katika kipindi cha miaka 56 ya uhuru wetu, tumepiga hatua kubwa za kimaendeleo kwenye nyanja mbalimbali, ikiwemo huduma za jamii, ulinzi, umeme, kilimo, utalii, biashara, mifugo, uvuvi, demokrasia, diplomasia, utamaduni, n.k. Zaidi ya hapo, na pegine kubwa zaidi ni kwamba, katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru, tumeweza kulinda na kudumisha amani, umoja na Muungano wetu.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kuwashukuru na kuwapongeza kwa dhati kabisa Viongozi wa Awamu zote za Serikali zetu mbili, ya Muungano na ya Zanzibar, kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru wa nchi yetu. Na nimefarijika sana kuona kuwa viongozi wastaafu wa nchi yetu, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Mzee Bilal, Mzee Malecela tunao hapa. Na niwaambie ndugu zangu Watanzania kuwa mambo kama haya ya kuwaona viongozi wastaafu wakishiriki kwenye tukio kama hili kwa pamoja ni nadra sana Duniani. Sio kwenye nchi zote jambo kama hili linawezekana. Kwenye nchi nyingine haiwezekani. Hivyo basi, nawasihi Watanzania wenzangu tuzidi kudumisha amani na umoja wetu. Na mimi namuomba Mwenyezi Mungu siku moja niweze kuhudhuria tukio kama hili nikiwa nimeungana na viongozi wengine wastaafu.
Lakini mbali na kuwapongeza viongozi wastaafu kwa mafanikio yaliyopatikana, napenda kuwapongeza Watanzania wote: wakulima, wafanyakazi, wavuvi, wafugaji, wafanyabiashara, wasanii, n.k.; kwa michango yenu ya hali na mali iliyowezesha kupatikana mafanikio niliyoyataja na mengine ambayo sikuyataja. Bila ya ninyi kujitoa, mafanikio haya kamwe yasingepatikana. Navipongeza pia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama (JWTZ, Polisi, Usalama wa Taifa, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto, n.k.), kwa kushiriki kikamilifu na kufanikisha kupatikana kwa mafanikio haya. Napenda kuwahakikishia vyombo vyote vya ulinzi kuwa Serikali yenu ipo pamoja nanyi na tutaendelea kushughulikia changamoto mbalimbali zinawakabili.
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Sherehe za Uhuru wa Tanzania Bara mwaka huu zinafanyika hapa Dodoma. Hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya Nchi yetu. Na zitaendelea kufanyika hapa. Napenda niwahakikishie ndugu Watanzania kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza mambo yote mazuri yaliyopatikana, na kutekeleza mambo mengine mapya kwa lengo la kuhakikisha kuwa Watanzania wote wanafaidi matunda ya uhuru.
Ombi langu kwa Watanzania endeleeni kuziamini Serikali zetu mbili, za Muungano na ya Zanzibar. Mimi na mwenzangu Dkt. Shein, tunaahidi kuwa tutasimamia na kutekeleza mambo yote tuliyowaahidi, ikiwemo ahadi zilizomo kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi. Na kutekeleza hayo, hatutambagua mtu kwa misingi ya dini, kabila, itikadi ya kisiasa, jinsia au rangi. Daima tutakuwa watumishi wenu.
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Leo wakati tunaadhimisha Sherehe za Miaka 56 ya Uhuru wa Tanzania Bara, napenda kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa Ibara ya 45 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa mamlaka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa msamaha kwa wafungwa wa makosa mbalimbali. Kwa faida ya hadhira hii, napenda kuinukuu Ibara hiyo, kama ifutavyo:
45 (1) bila kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Ibara hii, Rais anaweza kutenda lolote kati ya mambo yafuatayo:-
(a) kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia mbele ya mahakama kwa kosa lolote, na aweza kutoa msamaha huo ama bila ya masharti au kwa masharti, kwa mujibu wa sheria;
(b) kumwachilia kabisa au kwa muda maalum mtu yeyote aliyehukumiwa kuadhibiwa kwa ajili ya kosa lolote ili mtu huyo asitimize kabisa adhabu hiyo au asitimize adhabu hiyo wakati wa muda huo maalum;
(c) kuibadilisha adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa kosa lolote iwe adhabu tahafifu;
(d) kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa ajili ya kosa lolote au kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu ya kutoza, au kuhozi (au kuchukua) kitu cha mtu mwenye hatia ambacho vinginevyo kingechukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka utaratibu utakaofuatwa na Rais katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa Ibara hii.
(3) Masharti ya Ibara hii yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Zanzibar na kwa adahabu zilizotolewa Tanzania Zanzibar kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge inayotumika Zanzibar, halikadhalika, masharti hayo yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Bara kwa mujibu wa sheria.
Sambamba na Ibara hii inayompa Rais mamlaka ya kutoa msamaha, nimesoma pia Presidential Affair Act ya mwaka 1962 cap 9 of Tanzania.
Ndugu Watanzania wenzangu;
Hivi sasa nchi yetu ina wafungwa wapatao 39,000, ambapo wanaume ni takriban 37,000 na wanawake ni 2,000. Kati ya wafungwa waliopo magerezani, wafungwa 522 wamehukumiwa adhabu ya kifo, ambapo wanaume ni 503 na wanawake ni 19. Idadi ya wafungwa waliofungwa kifungo cha maisha ni 666, ambapo wanaume ni 655 na wanawake 11.
Hivyo basi, kwa mujibu wa mamlaka niliyopewa na Katiba kupitia Ibara ya 45, nimeamua kutoa msamaha kwa wafungwa 8,157. Kati ya wafungwa hao niliowapa msamaha, wafungwa 1,828 watatoka leo na waliosalia 6,329 watapunguziwa vifungo vyao vya kukaa gerezani na kutoka kulingana na vifungo vyao. Vilevile, kwa kutumia Ibara hiyo ya 45, nimetoa msamaha kwa wafungwa 61 waliokuwa wamehukumiwa kunyongwa. Halikadhalika, nimeamua kutoa msamaha kwa wafungwa kutoka Familia ya Nguza (Nguza Vicking na Johnson Nguza). Wengi niliowapa msamaha, hususan waliohukumiwa kunyongwa na kufungwa vifungo virefu, wametumikia vifungo vyao kwa muda mrefu na wameonesha tabia njema na kujutia makosa yao.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nimeeleza mambo mengi; mengi sana. Hivyo, napenda niishie hapa. Lakini kabla sijahitimisha, napenda nitoe shukrani zangu nyingi kwa Kamati ya Maandalizi kwa kufanikisha Sherehe hii. Sherehe zimefana sana. Hongereni sana wana-Kamati. Tunavishukuru pia vyombo vya ulinzi na usalama, vikundi vya burudani, chipukizi na waandishi wa habari kwa kufanikisha sherehe hii.
Kwa namna ya pekee, napenda kuwashukuru wageni wetu waalikwa waliokuja hapa kushiriki nasi katika shughuli hii muhimu na ya kihistoria kwa taifa letu.Tunawashukuru Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali za Kimataifa. Napenda niwahakikishie kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Mataifa yenu pamoja na Taasisi mnazoziwakilisha.
Napenda pia kuwashukuru wana-Dodoma wote, mkiingozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, Mheshimiwa Mahenge, kwa ukarimu mkubwa mliotuonesha na kwa kujitokeza kwa wingi kwenye Sherehe hizi. Nimejionea mwenyewe kuwa watu wengi wapo nje. Hii ina maana kuwa mnahitaji uwanja mpya. Na kwa bahati nzuri, rafiki zetu wa Morocco wamekubali kutujengea Uwanja Mpya hapa Dodoma, ambapo Jiwe la Msingi tunatarajia kuliweka mwezi Machi au Aprili 2018. Sambamba na hilo, napenda kuwahakikishia wana-Dodoma kuwa dhamira ya Serikali kuhamia Dodoma ipo pale pale. Hakuna kurudi nyuma. Makamu wa Rais atahamia kabla ya mwisho wa Mwaka huu, na mimi nitahamia mwakani. Tutaendelea kuboresha miundombinu pamoja na upatikanaji wa huduma za jamii hapa Dodoma, hususan kwa kuwa hivi sasa mji huu ndio kioo cha nchi yetu. Ahadi yetu ya kujenga barabara ya mzunguko, uwanja wa michezo, njia ya reli kutoka kitongoji cha Chalinze hadi hapa mjini pamoja na kuboresha huduma za maji na afya zipo pale pale. Nawaomba muendelee kutuamini. Na kamwe hatutawaangusha.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kurudia tena kuwashukuru viongozi wastaafu kwa kuja kujumuika nasi kwenye sherehe hizi. Aidha, navishukuru vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na nzuri wanazofanya kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa kisiwa cha amani. Wito wangu kwa Watanzania tuendelee kuenzi na kudumisha tunu za Amani, Muungano pamoja na Umoja na Mshikamano, ambazo tumeachiwa na waasisi wetu, Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere na Mzee Abeid Karume.
Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Wabariki Watanzania!
“Ahsanteni Sana kwa kunisikiliza”

- Nov 25, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA HOSPITALI YA TAALUMA NA TIBA YA CHUO KIKUU CHA...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais
Mstaafu pamoja na Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda,
Waziri Mkuu Mstaafu;
Mheshimiwa Anna Makinda, Spika Mstaafu wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu,
Sayansi na Teknolojia;
Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto;
Mheshimiwa Seleman Said Jafo, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais - TAMISEMI
Mheshimiwa Song Geum Yong, Balozi wa Jamhuri
ya Korea ya Kusini;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Prof. Apolinary Kamuhabwa, Makamu Mkuu wa Chuo cha Afya
na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi
za Kimataifa mliopo;
Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, Maprofesa pamoja na
Wana-Jumuiya wote wa Chuo Kikuu cha Afya na
Sayansi Shirikishi Muhimbili;
Viongozi wengine wa Serikali, Vyama vya Siasa
pamoja na Viongozi wa Dini mliopo;
Ndugu Wananchi wa Mloganzila na maeneo jirani;
Wageni waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa uzima na kutuwezesha kukutana hapa leo. Aidha, namshukuru Mkuu wa Chuo, Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Mzee Ali Hassan Mwinyi, pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako, kwa kunialika kwenye tukio hili la ufunguzi wa Hospitali hii ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili, hapa Mloganzila. Hili ni tukio muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu; hivyo basi, ninawashukuru sana kwa kunialika.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru Wana-Jumuiya wa Hospitali hii pamoja na wananchi wa hapa Mloganzila na maeneo jirani, kwanza, kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kushuhudia tukio hili. Lakini pili, kwa mapokezi yenu mazuri.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Afya njema ni msingi mkubwa wa maendeleo katika Taifa. Nchi ambayo wananchi wake hawana afya njema kamwe haiwezi kupata maendeleo. Hii ni kwa sababu mwananchi asiye na afya njema hawezi kushiriki kwenye shughuli za ujenzi wa Taifa, kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, biashara, lakini pia kufanya kazi ofisini, viwandani, migodini, n.k.; na kama atashiriki, basi mchango wake utakuwa mdogo sana.
Hii, bila shaka, ndio sababu Awamu zote za Uongozi wa nchi yetu, kuanzia Awamu ya Kwanza hadi sasa, zimekuwa zikiweka mkazo mkubwa katika kuboresha huduma za afya hapa nchini. Na mimi leo nafurahi kuja hapa Mloganzila kufungua Hospitali hii ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili. Kama ambavyo mmesikia, Hospitali hii, ambayo ilianza kujengwa mwezi Machi 2014 na kukamilika mwezi Agosti 2016, ni kubwa na pia ya kisasa. Ina uwezo wa kulaza wagonjwa 571 na kuhudumia wagonjwa wengine wa nje. Ujenzi wake pamoja na vifaa umegharimu takriban Dola za Marekani milioni 94.5, sawa na Shilingi za Tanzania bilioni 206.7. Kati ya fedha hizo, Serikali yetu ilitoa Dola za Marekani milioni 18 sawa na takriban shilingi bilioni 39.4; na kiasi kingine, Dola za Marekani 76.5, sawa na takriban shilingi bilioni 167.3 ni mkopo wa masharti nafuu kutoka kwa marafiki zetu wa Korea Kusini.
Napenda kutumia fursa hii, kuishukuru sana Serikali ya Korea Kusini kwa kutupatia mkopo wa masharti nafuu uliotuwezesha kujenga hospitali hii. Korea Kusini ni marafiki zetu. Wametekeleza miradi mbalimbali nchini. Aidha, hivi karibu, Serikali ya Korea inatarajia kufadhili ujenzi wa Daraja la kupita Juu ya Bahari kutoka Aga Khan hadi ufukwe wa Coco Beach umbali wa takriban kilometa 7.1. Kama hiyo haitoshi, kampuni kutoka Korea Kusini itaanza ujenzi wa meli kwa ajili ya kutoa huduma kwenye Ziwa Victoria. Hivyo, tunawashukuru sana marafiki kwa kukuza ushirikiano. Na nimefurahi Balozi wa Korea Kusini, Mheshimiwa Song Yong yupo hapa. Tafadhali, naomba sana utufikishie shukrani zetu nyingi kwa Serikali pamoja na wananchi wa Korea Kusini. Lakini niseme tu kwamba katika kukuza na kuimarisha zaidi uhusiano wetu na Korea Kusini na sisi tumefungua Ubalozi nchini humo hivi karibuni.
Sambamba na kuishukuru Serikali ya Korea kwa ufadhili wao, napenda, kwa namna ya pekee kabisa, kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Awamu wa Nne kwa kuridhia kuanza kwa ujenzi wa Hospitali hii wakati wa uongozi wake. Mimi nataka niwaeleze ukweli, bila Rais mstaafu Kikwete, Hospitali hii isingejengwa. Yeye ndio aliyeasisi wazo la kujengwa kwa Hospitali hii. Sisi wengine tulikuwa tunatekeleza maelekezo yake. Nakumbuka nikiwa Waziri wa Ardhi alinipa maelekezo ya kufuatilia upatikanaji wa eneo hili. Aidha, nikiwa Waziri wa Ujenzi aliniagiza kujenga barabara ya kuja hadi hapa. Nafurahi niliweza kutekeleza maelekezo yake. Eneo hili lenye ukubwa wa ekari 3,800 lilipatikana na barabara ilijengwa na kukamilika. Lakini, nasema kwa dhati kabisa kuwa, sifa zote kuhusiana na ujenzi wa Hospitali hii ziende kwa Mheshimiwa Kikwete. Napenda pia kuwashukuru na kuwapongeza Mkandarasi, Kampuni ya Kolon Global Corporation ya Korea Kusini, pamoja na Wasimamizi wa mradi kwa kukamilisha ujenzi wa Hospitali hii.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama ambavyo Mheshimiwa Ndalichako ameeleza, Hospitali imejengwa kwa madhumuni makubwa matatu. Kwanza, kufundishia wataalam wa masuala ya afya kwa ngazi ya stashahada, shahada, pamoja na shahada za uzamili na uzamivu. Pili, kutoa huduma za afya za kibingwa kwa magonjwa mbalimbali. Na tatu, kufanya tafiti kuhusu namna ya kuboresha tiba na huduma za kinga. Hospitali tayari imekamilika, hivyo, hatua inayofuata sasa ni kuanza ujenzi wa miundombinu ya kufundishia, hususan kumbi za mihadhara (lecture halls), maktaba, maabara, hosteli na cafeteria.
Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali imedhamiria kwa dhati kuhakikisha miundombinu hiyo inajengwa ili kuifanya Hospitali hii itekeleze majukumu yake ipasavyo. Nimeambiwa kuwa ujenzi wa miundombinu hiyo utagharimu shilingi bilioni 13.32. Na kama alivyosema Mheshimiwa Waziri Ndalichako tayari Mkandarasi, Wakala wa Majengo ya Serikali (TBA), amelipwa malipo ya awali kiasi cha shilingi bilioni 3.9. Hivyo, natoa wito TBA kuanza mara moja ujenzi wa mradi miundombinu inayohitajika ili kukiwezesha Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili kudahili wanafunzi wengi zaidi, kutoka 3,000 wa sasa hadi kufikia 15,000; na hivyo kupunguza tatizo la uhaba wa watumishi wa afya katika hospitali zetu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kukamilishwa na kufunguliwa rasmi kwa Hospitali hii ya Mloganzila ni sehemu tu ya jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano za kuboresha huduma za afya hapa nchini. Tangu tumeingia madarakani miaka miwili iliyopita, tumejenga na kuboresha miundombinu mbalimbali kwa ajili ya kutoa huduma za afya. Tumejenga vituo vipya vya kutoa huduma za afya vipatavyo 268 na hivyo kufanya nchi yetu kuwa na vituo vya kutoa huduma za afya vipatavyo 7,284. Vituo vingine vya kutoa huduma za afya vinaendelea kujengwa sehemu mbalimbali nchini, ikiwemo ujenzi wa Hospitali za Mikoa mipya ya Njombe, Geita, Katavi na Simiyu. Sambamba na ujenzi wa vituo hivyo vipya, hivi sasa tunaviboresha vituo vya afya 170 kwa gharama ya shilingi bilioni 161.9 ili kuviwezesha kutoa huduma ya uzazi wa dharura. Lengo la uboreshaji huu ni kupunguza vifo vya mama na mtoto kutoka wastani wa vifo 556 katika kila vizazi hai 100,000 vya sasa hadi kufikia angalau vifo 292 mwaka 2020. Tumekamilisha pia ujenzi wa nyumba 220 kwa ajili ya watumishi wa afya.
Mbali na ujenzi wa miundombinu, tumeendelea na uimarishaji wa huduma za kibingwa kwenye Hospitali zetu za Rufaa za Muhimbili, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Taasisi ya Mifupa (MOI), Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (na napenda nimhakikishie Mheshimiwa Waziri wa Afya kuwa tutampatia fedha kwa ajili ya kununua Scan aliyoomba) pamoja na hospitali za rufaa za Bugando, Mbeya na KCMC. Uboreshaji huu ni pamoja kuanzisha huduma za kupandikiza vifaa vya kuongeza usikivu (cochlea implant). Tumeziongezea pia vifaa, vifaa tiba na vitendanishi. Mathalan, kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili tumeongeza vitanda vya ICU kutoka 21 hadi kufikia 75, na vitanda kwa ajili ya wagonjwa wa kusafisha figo vimeongezeka kutoka 27 hadi 42. Tumeongeza pia vyumba vya upasuaji kutoka 13 hadi kufikia 20. Kwa upande wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road tumeiongezea vifaa na vitanda vya wagonjwa kutoka 40 hadi 100; wakati Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete hivi sasa ina uwezo wa kufanya upasuaji wa wagonjwa watatu kwa siku kutoka mmoja hapo awali.
Sambamba na hatua hizo, Serikali imeongeza bajeti ya dawa na vifaa tiba, kutoka shilingi bilioni 31 kwenye Mwaka wa Fedha 2015/2016 hadi kufikia shilingi bilioni 251 mwaka 2016/2017; na Mwaka huu wa Fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 269 kwa ajili hiyo. Matokeo yake upatikanaji wa dawa muhimu katika Bohari Kuu ya Dawa na vituo vya Serikali vya kutoa huduma za afya umeongezeka. Jambo la kutia moyo zaidi ni kwamba bei ya dawa na vifaa nayo imeanza kupungua, hususan kufuatia uamuzi wa Serikali wa kuanza kununua moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji badala ya kupitia kwa madalali. Mathalan, bei ya dawa ya chanjo ya homa ya ini (hepatitis B Vaccine) imepungua kutoka shilingi 22,000 hadi shilingi 5,300; dawa ya kupambana na maambukizi ya bacteria (Amoxicillin/clavulanic Acid Potassium 625 mg) yenye vidonge 15 bei yake imepungua kutoka shilingi 9,800 hadi shilingi 4,000. Aidha, bei ya shuka za hospitalini imepungua kutoka shilingi 22,200 hadi shilingi 11,100. Hii ni mifano michache tu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Licha ya hatua tunazozichukua, na ambazo zinatia moyo, natambua kuwa bado sekta yetu ya afya inakabiliwa na matatizo kadhaa. Moja ya matatizo hayo, ni uhaba wa watumishi wa afya. Na tatizo hili kimsingi lina sura kubwa mbili. Sura ya kwanza, ni uhaba wa watumishi wenyewe. Nchi yetu bado ina mahitaji makubwa ya watumishi wa afya. Tulionao ni 89,842 kati ya 184,901 wanaohitajika. Hivyo, tuna upungufu wa watumishi wa afya takriban 95,059. Serikali inalifahamu hili ndio maana tayari tumetoa vibali vya ajira zipatazo 3,410 (madaktari 258 na wataalam wa kada mbalimbali za afya 3,152) ili kupunguza pengo la watumishi wa afya lililopo, na hasa baada ya kuondolewa watumishi wenye vyeti vya kughushi. Aidha, tumevifanyia ukarabati na upanuzi vyuo vyetu vya uuguzi na ukunga vya Nzega, Mirembe, Mtwara na Tanga pamoja vyuo vya maafisa tabibu Musoma na Mpanda. Matokeo yake udahili wa wanafunzi wa afya imeongezeka hadi kufikia 13,632 na hivyo kuvuka lengo lililowekwa la kudahili wanafunzi 10,000 ifikapo mwaka 2017. Aidha, hivi sasa Serikali inatoa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 54.26 kwa wanafunzi wanaosomea masuala ya afya wapatao 10,189. Lakini sio kwamba tunataka kuongeza idadi tu. Hapana. Tunahimiza pia ubora wa wataalam wanaozalishwa kwenye vyuo vyetu. Hii ndio sababu Serikali iliamua kuvisimamisha baadhi ya vyuo kudahili wanafunzi kwa mwaka huu baada ya kujiridhisha kuwa havina uwezo.
Sura ya pili ya tatizo la uhaba wa watumishi wa afya hapa nchini, linatokana na mgawanyo usio mzuri wa watumishi wenyewe. Mathalan, nimeambiwa kuwa takriban asilimia 60 ya madaktari wote nchini, wapo hapa Dar es Salaam. Na ni asilimia 40 tu ndio wapo Mikoani. Nafahamu kuwa tatizo hili linasababishwa na mambo mengi, ikiwa ni pamoja na hospitali nyingi kubwa kuwepo hapa Dar es Salaam lakini kuwepo na mazingira mazuri ya kufanyia kazi. Hata hivyo, natambua pia kuwa suala la Wizara ya Afya kusimamia Hospitali za Kibingwa na Maalum pekee, na hospitali nyingine kuanzia ngazi ya mkoa kuwa chini ya TAMISEMI nalo linachangia kuwepo kwa mgawanyo usiowiana wa madaktari kati ya hapa Dar es Salaam na Mikoani; na halikadhalika kati ya Hospitali za Kibingwa na zisiso za Kibingwa.
Napenda nitoe mifano michache. Hospitali ya Taifa ya Muhimbili yenye takriban vitanda 1,600, ina jumla ya madaktari bingwa, madaktari wanafunzi na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Muhimbili wapatao 532. Hii maana yake ni kwamba kila daktari anahudumia vitanda vitatu. Lakini katika Mkoa wa Tabora daktari 1 alikuwa akihudumia wagonjwa 208,329, kwa mujibu wa Sensa ya Mwaka 2012. Mfano mwingine ni wa hapa hapa Dar es Salaam. Hospitali ya Manispaa ya Temeke yenye kuhudumia wastani wa wajawazito wanaojifungua 100 kwa siku ina madaktari bingwa wa akinamama wawili. Lakini Hospitali ya Taifa ya Muhimbili yenye kuhudumia wastani wa akinamama wanaojifungua kati ya 40 hadi 50 kwa siku, ina madaktari bingwa 40; ukiachilia mbali madaktari wanafunzi waliopo. Hii inadhihirisha kuwa hakuna mgawanyo mzuri wa madaktari wachache tulionao. Ni kweli, tunahitaji kuwa na madaktari bingwa wengi katika hospitali zetu. Lakini, haina maana kuwa na madaktari wengi kwenye Hospitali za Kibingwa wakati hospitali nyingine za kawaida, zenye kuhudumia watu wengi, hazina madaktari. Tukiruhusu hali hii kuendelea, wananchi wengi wataendelea kukosa huduma za afya; na hata wakipewa rufaa kwenda hospitali za rufaa au kibingwa wanakuwa tayari wamechelewa na watashindwa kutibika.
Hivyo, niziombe Mamlaka husika kulitafakari suala hili kwa kina, ikiwezekana, kuangalia uwezekano wa Hospitali za Mikoa nazo ziwe chini ya Wizara ya Afya. TAMISEMI ibaki kusimamia hospitali za Wilaya, vituo vya afya na zahanati. Nina imani kuwa hii itasaidia kuboresha huduma katika Hospitali za Rufaa za Mikoa na hivyo kuipunguzia mzigo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Lakini, sambamba na hilo, niwaombe madaktari nao kuwa wazalendo pindi wakipangiwa kwenda kufanya kazi Mikoani na Wilayani. Serikali imeanza kuboresha maslahi ya watumishi wa afya wanaofanya kazi kwenye Hospitali za Mikoa na Wilaya, ambapo, mathalan, katika Hospitali za Rufaa za Mikoa, daktari bingwa alikuwa akilipwa shilingi 2,000 kwa ajili ya kumuona mgonjwa ambaye ni mwanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima, lakini sasa analipwa shilingi 15,000. Daktari wa kawaida alikuwa akilipwa shilingi 2,000 lakini sasa analipwa shilingi 7,000. Katika Hospitali za Wilaya, daktari alikuwa akilipwa shilingi 1,000 lakini sasa analipwa shilingi 7,000. Tumefanya hivyo ili kuwavutia madaktari kwenda kufanya kazi katika Hospitali za Mikoa na Wilaya nchini.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ukiachilia mbali suala la uhaba wa watumishi wa afya, nchi yetu bado ina upungufu wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, hususan zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, nyumba za watumishi, n.k. Kama nilivyoeleza hapo awali, Serikali inaendelea na jitihada za kujenga miundombinu hiyo. Lakini nawakaribisha watu binafsi, makampuni na mashirika ya dini kuendelea kuunga mkono jitihada hizo.
Tatizo la tatu ambalo mimi naliona lenye kuikabili sekta yetu ya afya ni kukosekana kwa viwanda vya kuzalisha madawa hapa nchini. Dawa nyingi tunaagiza kutoka nje kwa gharama za juu. Kama tungekuwa na viwanda vingi vya kuzalisha dawa hapa nchini, nina uhakika bei ya dawa ingekuwa chini zaidi na hospitali zetu zingekuwa na dawa za kutosha. Hivyo basi, napenda kurudia wito wangu kwa wafanyabiashara, makampuni na mashirika mbalimbali kuwekeza kwenye viwanda vya madawa na vifaa tiba hapa nchini. Soko lipo, tena ni kubwa. Mmesikia kuwa tumeongeza bajeti ya dawa, lakini pia washirika wetu mbalimbali wameendelea kutufadhili kwa kutupatia fedha za kununulia dawa. Mathalan, Global Fund wametupatia takriban Dola za Marekani milioni 300 kwa ajili hiyo. Lakini sambamba na hayo, mnafahamu kuwa sisi ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ambazo zina takriban nchi 18. Kama hiyo haitoshi, hivi karibuni taasisi yetu ya Bohari Kuu ya Madawa imekabidhiwa jukumu la kununua dawa kwa niaba ya nchi zote za SADC. Hivyo, soko lipo. Kilichobaki ni kwa wafanyabiashara na wataalam wetu kujipanga vizuri katika kutumia fursa hiyo ya kuwa na soko kubwa la dawa. Nimefurahi kusikia kuwa Hospitali hii ya Mloganzila imetenga eneo mahususi kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya dawa. Na nina imani mtakuwa mmetenga pia eneo maalum kwa ajili ya kulima mimea mbalimbali kwa ajili ya kufanya utafiti wa madawa, ambayo yalikuwa ndio mawazo ya Mzee Kikwete. Napenda pia kutumia fursa hii kuushauri Mfuko wa Bima ya Afya kujielekeza katika mwelekeo huo wa ujenzi wa viwanda vya madawa.
Tatizo jingine ambalo naliona ni wananchi wetu wengi kushindwa kujiunga na Mifuko ya Bima ya Afya. Kama mnavyofahamu, gharama za afya huwa ni kubwa na ugonjwa mara nyingi hutokea bila kutarajia. Hali hii inafanya wananchi wengi kushindwa kumudu gharama za matibabu, licha ya kwamba Serikali imejitahidi sana kupunguza gharama za matibabu. Mifuko ya Bima ya Afya (NHIF na CHF) ina nafasi kubwa ya kuwasaidia wananchi kupunguza gharama za matibabu. Lakini kwa bahati mbaya, idadi ya wananchi waliojiunga na mifuko hii ni ndogo. Hivyo basi, nitumie fursa hii kuwaomba wananchi kote nchini kujiunga na Mifuko ya Bima ya Afya ili iwasaidie pindi wanapokumbwa na magonjwa au kuuguliwa na ndugu au jamaa. Gharama za kujiunga na mifuko ya bima ya afya sio kubwa, ni ndogo.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimeeleza masuala mengi. Lakini kabla sijahitimisha hotuba yangu, ninayo masuala mengine madogo ya kueleza. Jambo la kwanza, ni kuhusu utunzaji wa miundombinu hii. Kama mlivyosikia, ujenzi wa miundombinu na ununuzi wa vifaa kwa ajili ya Hospitali hii hapa Mloganzila umegharimu fedha nyingi. Hivyo basi, nawasihi sana wafanyakazi na watumishi wa hapa muitunze. Na niziombe mamlaka husika za hospitali zote nchini kuhakikisha vifaa kwenye Hospitali za Serikali vinatunzwa. Kitunze kidumu.
Jambo la pili linaihusu Hospitali hii. Hospitali hii inakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo uhaba wa watumishi. Wanaohitajika ni takriban 950, lakini waliopo ni wachache kutokana na vibali vichache vya ajira na uhaba wa watumishi wenyewe wa afya. Hata hivyo, kwa taarifa nilizonazo ni kuwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, ukijumuisha Taasisi ya Moi pamoja na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, ina takriban vitanda 1,940. Aidha, madaktari na watumishi kwa pamoja idadi yao inafikia 3,812. Wodi ya Mwaisela peke yake ina vitanda 244 na kuhudumia wagonjwa wa nje wapatao 400. Wodi hii pia imekuwa ikihudumiwa na madaktari bingwa wapatao 75, wakisaidiwa na madaktari wanafunzi takriban 20 na wauguzi wapatao 69. Lakini, kama nilivyosema, Hospitali hii ya Mloganzila ina vitanda 571, ambavyo havina wagonjwa na inakabiliwa na changamoto ya watumishi.
Nimekuwa nikijiuliza kama Hospitali ya Taifa ya Muhimbili yenye kukabiliwa na ufinyu wa nafasi za kulaza wagonjwa ina watumishi wengi kama nilivyoeleza, kwanini basi tusiwahamishe baadhi ya madaktari na wagonjwa kutoka Muhimbili kuja hapa, na hivyo kuweza kupiga ndege wawili kwa jiwe moja. Kwanza, kupunguza uhaba wa watumishi katika Hospitali hii ya Mloganzila. Na pili kupunguza mrundikano wa wagojwa kwenye Hospitali yetu ya Taifa ya Muhimbili. Vilevile, Hospitali hii itaweza kuhudumia watu wengi zaidi kuliko sasa na wanafunzi pia wataweza kujifunza vizuri zaidi. Halikadhalika, tutaipunguzia Serikali gharama kwa vile watumishi watakaohamishiwa hapa kutoka Muhimbili tayari ni waajiriwa wa Serikali; na kwa kuwa Hospitali hii ipo hapa Dar es Salaam hata gharama za uhamisho hazitakuwepo. Hivyo basi, nitoe wito kwa wahusika wote, hususan Wizara ya Elimu na Chuo cha Muhimbili, Wizara ya Afya na Hospitali ya Muhimbili, Taasisi za Moi na ya Moyo ya Jakaya Kikwete pamoja na wahusika wengine, kukutana na kulitafakari suala hili vizuri ili uwekezaji huu ulete manufaa yaliyokusudiwa.
Suala jingine lenye kufanana na hili nililotoka kulizungumzia ni kuhusu ushirikiano miongoni mwa taasisi zenye kusimamia Hospitali hii. Kama nilivyoeleza hapo awali, Hospitali hii ina jukumu la kufundisha wataalam wa afya na pia kutoa huduma za afya, hususan za kibingwa kwa wananchi. Inafahamika kuwa jukumu la kusimamia sekta ya afya lipo Wizara ya Afya na Wizara ya Elimu inashughulikia sekta ya elimu. Kwa maana hiyo, ili Hospitali hii iweze kutekeleza majukumu yake yote mawili ipasavyo ni lazima Wizara hizi mbili pamoja na watendaji wake zifanye kazi kwa karibu na kwa ushirikiano. Nimefurahi kusikia kuwa Waheshimiwa Mawaziri wa Afya na Elimu wanashirikiana; japo sina hakika kama hali iko hivyo hadi kwa watendaji wao. Endapo hapatakuwa na ushirikiano, upo uwezekano wa Hospitali hii kushindwa kutekeleza majukumu yake, ikajikita kwenye jukumu moja, mathalan la kufundisha wataalam na kuacha jukumu la kutoa huduma za afya kutokana na ama utashi wa viongozi wa Hospitali wenyewe au kwa kukosa bajeti ya kutoa huduma ya afya kutoka Wizara ya Afya. Hivyo basi, natoa changamoto kwa wahusika wote kuhakikisha washirikiana ili Hospitali hii itekeleze majukumu yake yote mawili ipasavyo; jukumu la kufundisha wataalam na jukumu la kutoa huduma za afya kwa wananchi. Wizara ya Elimu itoe bajeti ya kufundishia kwa Hospitali hii Wizara ya Afya itenge bajeti itakayoiwezesha Hospitali hii kutoa huduma za afya kwa wananchi, kwa sababu wao ndio wenye jukumu la kusimamia sekta ya afya. Huu ndio wito wangu kwa mamlaka zenye kusimamia Hospitali hii.
Suala la tatu linahusu ulipaji wa fidia kwa wananchi waliokuwa wakiishi katika eneo hili. Historia ya eneo hili ipo wazi. Kabla ya kumilikishwa kwenye Hospitali hii, eneo hili, tangu mwaka 1946 lilikuwa chini ya milki ya Serikali, kupitia kwanza Tanganyika Packers na baadaye Kampuni ya Biashara ya Mifugo Tanzania (KABIMITA) chini ya Wizara ya Maji na Maendeleo ya Mifugo. Eneo hili lilitumika kwa ajili ya kufuga, kutunza na kunenepesha mifugo (holding ground) kabla ya kuuzwa au kuchinjwa. Wakati huo hapakuwa na wananchi waliokuwa wakiishi. Baada ya KABIMITA kuacha kulitumia, wananchi walianza kuishi na kuliendeleza, na hatimaye likasajiliwa vijiji vya ujamaa vya Kwembe (1980) na Mloganzila (1993); lakini umilki ardhi ulibaki kuwa Serikalini ndio maana tulipotaka kujenga Hospitali hii, hatukupata taabu kulichukua. Hata hivyo, kwa busara na huruma ya Serikali iliamua kuwa wananchi waliokuwa wakiishi hapa walipwe fidia ya mandelezo waliyoyafanya. Kiasi cha takriban shilingi bilioni 8.07 kililipwa kwa watu 1,919 waliofanyiwa tathmini kati ya mwaka 2008 – 2010. Aidha, mwaka 2011 Serikali iliwalipa fidia wananchi wengine 619 kiasi cha shilingi bilioni 1.61. Hivyo basi, nitumie fursa hii kusema kuwa Serikali haitalipa tena fidia kwenye eneo hili. Na wala wasipite watu kuwadanganya kuwa kuna fidia nyingine. Kama nilivyosema, fidia tayari ilishalipwa. Lakini nafahamu kuwa wapo wakazi wawili waligomea malipo yao, lakini hundi zao zipo; wakati wowote wakiwa tayari wanaweza kuzifuata kwenye Wizara husika. Fidia iliyotolewa ni kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi yetu.
Mheshimiwa Rais Mstaafu Mzee Mwinyi;
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kuwashukuru tena viongozi wa Hospitali hii pamoja na Wizara husika kwa kunikaribisha kwenye shughuli hii. Nawashukuru pia Mheshimiwa Makamu wa Rais Mstaafu, Dkt. Bilal pamoja na Waziri Mkuu Mstaafu Mzee Mizengo Pinda, ambao kwa kushirikiana na Rais Mstaafu Mzee Kikwete walifanikisha ujenzi wa Hospitali. Aidha, namshukuru pia Mheshimiwa Mama Anna Makinda, Spika Mstaafu ambaye Bunge aliloliongoza ndilo lilipitisha bajeti ya kujenga Hospitali hii. Na narudia tena kuishukuru Serikali ya Korea Kusini ambao walitupatia mkopo wa ujenzi wa Hospitali hii ya kisasa; pamoja na wengine wote waliofanikisha. Napenda kuwahakikishia viongozi wa Hospitali hii pamoja na wananchi kwa ujumla kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kufanya kila jitihada kuhakikisha hospitali hii ya kisasa inakuwa bora sio tu hapa nchini bali Barani Afrika.
La mwisho kabisa, hususan kwa wananchi wa maeneo haya, hivi karibuni Serikali imeanza maandalizi kwa ajili ya ujenzi wa barabara kutoka Ubungo hadi Kibaha. Ili kutekeleza mradi huo, nyumba zilizokuwa zimejengwa kwenye hifadhi ya barabara zimebomolewa kwa mujibu wa sheria. Ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 16 utaanza wakati wowote kuanzia sasa.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta hapa Mloganzila la kuifungua rasmi Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili.
Mungu Ibariki Hospitali Hii!
Mungu Wabariki Wana-Mloganzila!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Oct 18, 2017
HOTUBA YAMHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE MAADHIMISHO YA KUMBUKUMBU YA BABA WA TAIFA, MWALIMU JULIUS N...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YAMHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE MAADHIMISHO YA KUMBUKUMBU YA BABA WA TAIFA, MWALIMU JULIUS NYERERE PAMOJA NA SHEREHE ZA KILELE CHA MBIO ZA MWENGE NA WIKI YA VIJANA KITAIFA MKOANI MJINI MAGHARIBI, TAREHE 14 OKTOBA, 2017
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
Mheshimiwa Moudline Cyrus Castico, Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Vijana, Wazee, Wanawake na Watoto wa Zanzibar;
Mheshimiwa Jenista Muhagama, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu- Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu;
Ndugu Mwakilishi wa Familia ya Baba wa Taifa, Mheshimiwa Makongoro Nyerere;
Mama Yetu Mpendwa, Mama Fatuma Karume;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi pamoja na Wakuu wa Mikoa wote mliopo;
Mheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa mkiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mjini Magharibi;
Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Ndugu Makatibu Wakuu na Manaibu Makatibu Wakuu mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Dini mliopo;
Ndugu Waandishi wa Habari;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu, ambaye ametuwezesha kukutana katika siku hii muhimu. Kama mnavyofahamu, Siku hii imebeba mambo makubwa mawili, au naweza kusema matatu. Kwanza, tunakumbuka kifo cha Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambaye tarehe kama ya leo, miaka 18 iliyopita, alitutoka hapa duniani. Na Pili, kulingana na maelekezo ya Waraka wa Baraza la Mawaziri Na. 11 wa Mwaka 2002, Siku ya leo pia ni kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka huu na Wiki ya Vijana Kitaifa.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri husika kwa kunialika kwenye shughuli hii muhimu. Kama mnavyofahamu, hii ni mara yangu ya kwanza kushiriki kwenye shughuli hii tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano. Mwaka jana, sherehe hizi zilipofanyika kule Simiyu, nilimwomba Mheshimiwa Rais Dkt. Ali Mohamed Shein Rais wa Serikali ya Zanzibar aniwakilishe, ambapo alifanya kazi hiyo vizuri sana huko Bariadi. Hivyo, kwa hakika kabisa, nimefurahi sana kushiriki kwenye shughuli hii.
Nitumie pia fursa hii kuwashukuru wananchi wa Mkoa wa Mjini Magharibi na Zanzibar kwa ujumla kwa mapokezi yenu mazuri. Aidha, nawashukuru kwa kujitokeza kwenu kwa wingi katika shughuli hii. Kama msemo wa Kiswahili usemavyo ”shughuli ni watu”. Hivyo, nasema, ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema, moja ya mambo yaliyotukutanisha hapa leo ni kukumbuka kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambacho kilitokea London, Uingereza, siku kama ya leo mwaka 1999. Tangu wakati huo, kila mwaka, ifikapo tarehe 14 Oktoba, tunafanya maadhimisho haya. Tutafanya hivyo pia mwakani na naamini tutafanya hivyo kwa miaka mingi ijayo kama si katika kipindi chote cha uhai wa Taifa letu.
Lakini, Watanzania wenzangu, tujiulize, hivi ni kwanini hasa tunamkumbuka Mwalimu Nyerere? Je, ni kwa sababu tu Siku hii imetamkwa kwenye sheria? Au tuna sababu za msingi za kumkumbuka? Tusipojiuliza maswali hayo, tutaendelea kuiadhimisha Siku hii kwa mazoea na hatimaye itapoteza umuhimu wake. Lakini niseme tu kuwa, nijuavyo mimi ni kwamba, Siku hii iliamriwa kuwa Siku ya Kitaifa ili kuwapa Watanzania fursa ya kujikumbusha mchango mkubwa na usiosahaulika uliotolewa na Mwalimu Nyerere katika nchi yetu. Na katika kujikumbusha huko, tujifunze na kutumia mafunzo tunayoyapata katika kusukuma mbele maendeleo ya nchi yetu.
Mabibi na Mabwana;
Nafahamu kuwa Watanzania wengi wanamfahamu au wamewahi kusikia habari za Mwalimu Nyerere. Baadhi walishiriki naye katika shughuli mbalimbali. Wengine walimuona wakati akiwa Rais. Wapo pia waliomfahamu kupitia vitabu au simulizi mbalimbali. Hata hivyo, kwa kuzingatia umuhimu wa siku hii, na kwa kuwa hii ni mara ya kwanza kushiriki kwenye maadhimisho haya tangu niwe Rais, nimeona ni jambo jema kumzungumzia kidogo Mwalimu Nyerere. Hii ni kwa sababu, sisi wenyewe, lakini hasa vijana na watoto wetu, wanahitaji kumfahamu vizuri mtu huyu tunayemkumbuka leo na pia kufahamu kwa nini tunafanya hivyo.
Ndugu Watanzania, Mabibi na Mabwana;
Historia ya uongozi wa Mwalimu Nyerere ni ndefu sana. Lakini niseme tu kuwa tunamkumbuka kwa sababu, kwanza, alikuwa kiongozi mzalendo. Mwalimu Nyerere alianza uongozi wa kisiasa mwaka 1953 alipochaguliwa kuwa Rais wa Tanganyika African Association (TAA). TAA ndio iliyozaa Chama cha Tanganyika African National Union (TANU), ambacho ndicho kilichoongoza harakati za kupigania uhuru wa nchi yetu.
Katika kipindi hicho cha mwanzoni kabisa cha uongozi wake kisiasa, Mwalimu Nyerere alionesha uzalendo wa hali ya juu na kuthamini kwake utu na usawa wa binadamu. Wakati anachaguliwa kuwa Rais wa TAA na baadaye TANU, alikuwa anafundisha St.Francis College, hivi sasa inajulikana kama Shule ya Sekondari Pugu. Umbali wa kutoka Pugu hadi kwenye Ofisi za TAA/TANU kwenda na kurudi ilikuwa kama kilometa 46. Na enzi hizo hapakuwa na usafiri wa daladala kama ilivyo sasa. TAA/TANU haikuwa na usafiri na hata fedha za kumlipa mshahara. Lakini kwa uzalendo wake, Mwalimu Nyerere alitumia fedha zake kujigharamia usafiri na wakati mwingine kulazimika kutembea kwa miguu. Alifanya hivyo kwa kujitolea. Tujiulize leo, ni viongozi wangapi wa Serikali na hata kwenye vyama wameweza kujitolea kiasi hicho?
Lakini kama hiyo haitoshi, mwaka 1955, alipotakiwa na Mwalimu Mkuu wa St.Francis College kuchagua ama kuendelea na kazi au kuacha kujihusisha na shughuli za kisiasa, Mwalimu Nyerere aliamua kuacha kazi na kubaki kuwa kiongozi wa TANU; kazi ambayo alikuwa halipwi mshahara wowote. Aliamua hivyo ili aendelee kuongoza harakati za kudai uhuru. Sijui kama tunafahamu maisha aliyoishi Mwalimu Nyerere na familia yake baada ya kuacha kazi; lakini, nina uhakika, yalikuwa magumu sana.
Kitu pekee kilichomsukuma kufanya uamuzi huo ni uzalendo wake. Isingekuwa hivyo, angetafuta kazi nyingine nzuri ya mshahara mzuri, kwa maana alikuwa msomi mzuri; na wasomi wa kiwango chake, wakati huo walikuwa wakihitajika sana. Je, tujiulize ni wangapi hivi leo wanaweza kufanya uamuzi wa kizalendo kama huo uliofanywa na Baba wa Taifa? Leo hii kuna Watanzania wangapi ambao kwa sababu tu wanalipwa vizuri kwenye makampuni ya wageni wanakofanya kazi, wanaisaliti nchi kwa vitendo vya wizi? Je, kuna viongozi wangapi waliopewa dhamana na wananchi lakini kwa sababu ya ubinafsi na kukosa uzalendo, wamekubali kusaini mikataba isiyo na tija kwa nchi? Je, tuna viongozi wangapi ambao wametanguliza maslahi yao binafsi mbele kuliko maslahi ya Tanzania? Majibu mnayo.
Ndugu Watanzania, Mabibi na Mabwana;
Sifa ya pili ya Mwalimu Nyerere alikuwa kiongozi asiye mbinafsi na mwenye kuthamini utu na usawa wa binadamu. Hili linadhihirishwa kwa jinsi yeye na familia yake walivyoishi. Waliishi maisha ya kawaida sana kama Watanzania wengine. Hakujilimbikizia mali wala hakuishi maisha ya anasa na kifahari. Kuna mtu niliwahi kumsikia akisema”kama Mwalimu Nyerere angekuwa mbinafsi au mpenda utajiri angeweza kuchukua fukwe yote ya Msasani ili iwe yake”. Na kweli angeweza, maana kuna mifano mingi tu ya viongozi wengi wa zama zake, na hata wa sasa, wanafanya hivyo. Lakini hakufanya hivyo. Yeye, Mama Maria, watoto na ndugu zake wengi waliishi na wanaendelea kuishi maisha ya kawaida kabisa, sawa na Watanzania wengi, licha ya kuwa Rais kwa takriban miaka 23.
Mfano mwingine unaodhihirisha kuwa Mwalimu Nyerere hakuwa mbinafsi bali mwenye kuthamini utu na usawa wa binadamu, ni jambo alilolifanya mwanzoni tu mwa uongozi wake akiwa Rais wa Tanzania. Baada ya nchi yetu kupata uhuru, baadhi ya wasomi waliokabidhiwa madaraka walianza kutoa shinikizo kwa Serikali kutaka kuongezewa mishahara na marupurupu. Mwalimu Nyerere hakukubaliana kabisa na madai hayo na hakusita kuikemea tabia hiyo ya ubinafsi kwa ukali na uwazi kabisa.
Hakuishia hapo. Ili kuonesha mfano, yeye mwenyewe, aliamua kupunguza mshahara wake ili kuwakumbusha wasomi hao kuwa haiwezekani kwa watu wachache kuongezana mishahara wakati wananchi wengi masikini hawapati huduma muhimu za afya, elimu na maji kutokana na ukosefu wa fedha. Tujiulize, je, sisi tuko tayari kuacha mishahara hewa? Je, mishahara tunayoipata tunaifanyia kazi? Je,nasi tupo tayari kujipunguzia, au kuacha kushinikiza kuongezwa kwa mishahara na marupurupu yetu ili kuiwezesha Serikali kuboresha huduma za jamii kwa manufaa ya Watanzania wote? Nasema hayo sio kwa sababu sitaki mishahara iongezwe. La hasha. Ninachotaka kusema ni kwamba kabla ya kudai nyongeza ya mishahara ni lazima kwanza kufahamu uwezo wa Serikali; lakini pia tutambue kuwa kuna Watanzania wenzetu wengi tu wanaohitaji kuboreshewa huduma.
Nafahamu kuwa huku Zanzibar mishahara ya watumishi wa kima cha chini imeongezwa kutoka Shilingi laki moja na nusu hadi shilingi laki tatu. Na kwa upande wa kule Bara, baada ya kukamilisha zoezi la uchambuzi wa watumishi hewa na wenye vyeti vya kughushi, Serikali imewapandisha vyeo watumishi 59,967 na kurekebisha mishahara yao, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 159.33 kimetengwa kwenye bajeti ya mwaka huu. Mishahara mipya ya watumishi hao inatarajiwa kuanza kulipwa mwezi huu. Endapo tusingefanya uchambuzi, Serikali ingepoteza takriban shilingi bilioni 89 kwa mwaka kwa kuwalipa watumishi hewa na wenye vyeti feki.
Ndugu Watanzania, Mabibi na Mabwana;
Sifa nyingine ya Mwalimu Nyerere alikuwa mpenda amani, umoja na mshikamano. Wakati wa harakati za kudai uhuru, aliwahimiza Watanganyika kutotumia nguvu, licha ya kuwepo kwa vitendo vya uchokozi na hila chafu zilizofanywa na wakoloni. Hii ndio moja ya sababu, zilifanya nchi yetu kupata uhuru kwa njia ya amani. Aidha, licha ya kuwa Tanganyika ilikuwa na takriban makabila 121 na dini mbalimbali, alifanikiwa kuwaunganisha wananchi wote katika harakati za kudai uhuru wa nchi yao.
Mwalimu Nyerere pia alikuwa muumini mzuri wa Muungano. Tanganyika ilipokaribia kupata uhuru, alikuwa tayari kuchelewesha uhuru huo kuzisubiri nchi nyingine za Afrika Mashariki (Kenya, Uganda na Zanzibar) ili uhuru huo upatikane kwa pamoja na kuwezesha kuundwa kwa taifa moja la Shirikisho la Afrika Mashariki. Lakini hata pale ilipodhihirika kuwa suala hilo haliwezekani, mwaka 1964, Baba wa Taifa pamoja na shujaa mwingine wa nchi yetu, Hayati Mzee Abeid Aman Karume, waliasisi Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuunganisha Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Na mwaka 1977, viongozi hao waliasisi Muungano wa vyama vya TANU na Afro Shiraz Party, na kuunda CCM, Chama Tawala, ambacho kimebaki kuwa miongoni mwa vyama vikongwe duniani. Hii inadhihirisha kuwa Mwalimu Nyerere alikuwa mpenda muungano. Tujiulize je, vitendo vyetu leo vinalenga kudumisha amani ya nchi yetu au kuivunja? Je, sisi hatuna udini au ukabila? Je, maneno na vitendo vyetu vinadumisha au vinahatarisha Muungano wetu? Haya ni maswali muhimu kujiuliza Watanzania wote tunapoadhimisha siku hii ya Mwalimu Nyerere.
Wheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kiongozi yoyote ana sifa kubwa moja; kuwa na maono (vision). Mwalimu Nyerere alikuwa ni kiongozi mwenye maono, tena makubwa na ya mbali sana. Alijua kuwa anataka kujenga Taifa huru na linalojitegemea. Taifa la watu wenye kujali na kuheshimu utu wa kila mmoja. Hayo ndio maono yake. Lakini, kama mnavyofahamu, maono peke yake bila mikakati, ni ndoto. Mwalimu Nyerere alibuni na kusimamia utekelezaji wa mikakati ya kutekeleza maono yake. Ndani ya miaka michache tu baada ya nchi yetu kupata uhuru, Mwalimu Nyerere alibaini kuwa huwezi kujenga Taifa huru na linalojitegemea kama njia kuu za uzalishaji zitamilikiwa au kusimamiwa na wageni au watu binafsi peke yake. Ni lazima Serikali ishiriki kikamilifu. Na huo ndio ukweli wenyewe. Nchi zote zilizofanikiwa kiuchumi duniani, Serikali zao zilishiriki moja kwa moja katika shughuli za kiuchumi. Hivyo basi, aliona upo umuhimu wa kujenga misingi itakayoiwezesha Serikali kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za uzalishaji; na hapo ndipo Azimio la Arusha likazaliwa mwaka 1967.
Mbali kuweka miiko ya kuwabana viongozi kutumia nafasi zao kujilimbikizia mali, Azimio la Arusha liliipa nguvu Serikali ya kuzuia viwanda, mashirika na makampuni ya kibepari kutorosha rasilimali zetu kwenda nje ya nchi. Lakini pia, kupitia Azimio la Arusha, Serikali ilijenga viwanda pamoja na kuanzisha mashirika na makampuni mengine mapya. Tukawa na viwanda vingi tu, vikiwemo vya nguo, viatu, matairi, vifaa vya kilimo, chuma, n.k.; na hivyo tukapunguza utegemezi wa kuagiza bidhaa hizo kutoka nje. Shirika letu la ndege lilikuwa na uwezo wa kutoa huduma ndani na nje ya nchi. Nakumbuka tulikuwa na ndege 9; mbili aina ya Boeing, Fokker 3 na Twin Otters 4. Aidha, Serikali ikaanzisha Shirika la Nyumba (NHC), ambalo lilikuwa na nyumba zipatazo 6,000 kwa ajili ya wananchi wa kipato cha chini. Na huku Zanzibar, Hayati Mzee Karume, akajenga majengo ya ghorofa sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na pale Michenzani.
Sambamba na hayo, Serikali iliweka mkazo kwenye elimu, ambapo ilitolewa bure bila ubaguzi, kuanzia shule ya msingi hadi chuo kikuu. Mwalimu Nyerere aliamini kuwa ukitaka kumkomboa mtu mnyonge ni lazima umpe elimu. Vilevile, alihimiza watu kufanya kazi kwa bidii kwa kutumia kaulimbiu za “uhuru na kazi”, “siasa ni kilimo”, n.k. Hii ni baadhi tu ya mikakati iliyotumiwa na Mwalimu Nyerere katika kujenga Tanzania aliyotaka. Lakini pia, kwa kutambua hali halisi ya nchi yetu wakati huo, Baba wa Taifa, aliwahi kutamka, nanukuu “madini yetu tuliyonayo ni vema tukayaacha mpaka Watanzania watakapokuwa na ufahamu wa kutosha wataamua kuyachimba”, mwisho wa kunukuu.
Pamoja na misingi hiyo mizuri iliyowekwa na Baba wa Taifa, kupitia Azimio la Arusha, miaka michache tu baada ya Mwalimu Nyerere kung’atuka Azimio la Arusha lilikatupwa. Sasa sijui ilitokea kwa makusudi au bahati mbaya. Mimi sijui, ila ukweli ni kwamba, tulilitupa. Na baada ya kulitupa tukaanza kuuza mashirika na viwanda vyetu, hata vile vilivyojiendesha kwa faida, kwa matarajio kwamba tutakaowauzia wangeviendesha kwa ufanisi zaidi. Lakini haikuwa hivyo. Viwanda na mashirika mengi tuliyoyabinafsisha, sasa yamekufa. Leo viko wapi viwanda vya nguo, ngozi, nyama, matairi n.k? Kwa takwimu nilizonazo, jumla ya viwanda 197 vilivyoanzishwa na Mwalimu Nyerere hivi sasa havipo; vimekufa. Na hapa ndipo mara nyingi mimi huwa najiuliza, ni nani hasa aliyeturoga sisi Watanzania? Kwa nini tuliamua kuuza viwanda vyetu? Ilikuwaje tukaruhusu Shirika letu la Ndege libaki na ndege moja kutoka 9 zilizokuwepo? Kwanini Shirika letu la Nyumba lishindwe kujenga nyumba za wananchi wa kipato cha chini? Hivi wananchi wana namna hiyo hivi sasa hawapo? Au hawahitaji tena makazi mazuri na ya gharama nafuu? Lakini swali kubwa ninalojiuliza kila wakati ni kwanini tuliliacha Azimio la Arusha wakati maudhui na misingi yake, binafsi, mpaka leo, naiona kuwa ni mizuri. Ndio, ni mizuri. Tunachoweza kujadiliana ni kuhusu mikakati ya utekelezaji wake kwa nyakati za sasa, lakini maudhui na misingi yake bado ni mizuri.
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jitihada za Baba wa Taifa kutetea wanyonge, kupigania umoja, amani, haki na usawa, hazikuishia tu hapa nchini. Zilivuka hadi nje ya mipaka ya nchi yetu. Tanzania, chini ya uongozi wa Mwalimu, ilikuwa mstari wa mbele kwenye harakati za ukombozi wa Bara la Afrika. Ilikuwa Makao Makuu ya Kamati ya Ukombozi ya OAU; na pia ilitoa hifadhi na mafunzo kwa vyama vya ukombozi vya Afrika Kusini, Angola, Msumbiji, Namibia na Zimbabwe, hadi nchi hizo zilipopata uhuru. Kama hiyo haitoshi, jana niliongea na Rais Yoweri Museveni wa Uganda ambaye aliniambia kuwa bila Mwalimu Nyerere huenda yeye asingekuwa Rais wa Uganda hivi sasa.
Mbali na kutoa mchango kwenye harakati za ukombozi, Baba wa Taifa alikuwa miongoni mwa waanzilishi wa OAU, sasa Umoja wa Afrika, na pia Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Tanzania pia chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere, ilikuwa mtetezi wa haki za wanyonge duniani kote. Mathalan, tulikuwa mstari wa mbele kutetea haki ya Jamhuri ya Watu wa China kupata uanachama kwenye Umoja wa Mataifa. Zaidi ya hapo, Mwalimu Nyerere alishiriki kwenye usuluhishi wa migogoro Barani Afrika. Na katika kudhihirisha hilo, wakati anafariki alikuwa Msuluhishi wa mgogoro wa Burundi.
Huyo ndiye Mwalimu Julius Kambarage Nyerere: Mpigania Uhuru; Mwanafrika halisi (Pan-Africanist); Mpenda Amani, Haki, Umoja na Usawa; Rais wa TAA na TANU; Waziri Mkuu wa kwanza wa Tanganyika; Rais wa Jamhuri ya Tanganyika; Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mwenyekiti wa kwanza wa CCM; Baba wa Taifa letu, ambaye leo tunakumbuka kifo chake na kusheherekea maisha yake. Kwa ujumla, naweza kusema kuwa Mwalimu Nyerere alikuwa miongoni mwa viongozi bora kuwahi kutokea sio tu hapa nchini, bali pia Barani Afrika na duniani kwa ujumla. Vijana na watoto wetu hawana budi kumfahamu mtu huyu wa aina yake katika historia ya nchi. Tuwafundishe watoto wetu fikra za Mwalimu Nyerere. Tuwasimulie kazi na mambo aliyoyasimamia. Na Watanzania wote kwa ujumla, hatuna budi kuenzi mambo mazuri aliyotuachia Baba wa Taifa letu. Nyerere oyeeee!!!!!
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Hayo niliyoeleza na maswali niliyouliza lengo lake sio kumtuhumu mtu yeyote. Nimeeleza na kuuliza maswali hayo kwa lengo la kumpa kila Mtanzania, fursa ya kutafakari ili kubaini wapi tulijikwaa au kukosea; na hatimaye tutafute njia ya kujisahihisha. Ni wazi kuwa, Baba wa Taifa, kama binadamu, alikuwa na mapungufu yake. Hata hivyo, mimi naamini kuwa endapo kila Mtanzania ataamua kwa dhati ya moyo wake kuenzi mambo mazuri ya Mwalimu Nyerere, nchi yetu itapata maendeleo makubwa tena kwa haraka.
Na katika hili, napenda nitumie fursa hii kuwathibitishia, kwa niaba ya mwenzangu Mheshimiwa Rais Shein, kuwa Serikali zetu mbili zimejipanga kuhakikisha zinaendelea kusimamia masuala na misingi mizuri iliyoachwa na waasisi wetu, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume, pamoja na viongozi waliofuata wa nchi yetu. Ni dhahiri kuwa kuvaa viatu vyao sio jambo rahisi. Lakini, nina imani kuwa, kwa ushirikiano wenu, tutaweza kuyasimamia na kuyatekeleza haya. Mathalan, moja ya ndoto za Baba wa Taifa ilikuwa kuhamishia Makao Makuu ya nchi yetu, Dodoma. Uamuzi wa kuhamia Dodoma ulifanyika tangu mwaka 1973, lakini utekelezaji wake ulikuwa ukilegalega kwa sababu mbalimbali. Sisi tumeamua kuhamia Dodoma. Na tayari tumeshaanza kuhamia huko. Mawaziri, Makatibu Wakuu na baadhi ya watendaji kutoka Wizara zote tayari wameshamia. Waziri Mkuu naye amehamia. Makamu wa Rais atahamia mwaka huu; na mimi nitahamia mwakani. Hii inadhihirisha kuwa tumedhamiria kwa dhati kumuenzi Baba wa Taifa kwa vitendo na siyo maneno.
Sambamba na hilo, Serikali zetu mbili zitaendelea kuimarisha Umoja, Mshikamano na Muungano wetu. Tutadumisha pia amani yetu. Yeyote atakayejaribu kuhujumu Muungano wetu au kuvuruga amani yetu, tutapambana naye kwa nguvu zetu zote; na kwa vyovyote vile, atambue kuwa kamwe hatoshinda.
Zaidi ya hapo, tutaendeleza harakati za kujiletea maendeleo ya kiuchumi. Tutaimarisha na kuboresha miundombinu muhimu ya kiuchumi, hususan ya usafiri na nishati. Na katika hili, tumeamua kwa dhati kabisa kufufua Shirika letu la Ndege, ambalo kama nilivyoeleza awali, wakati wa Baba wa Taifa lilikuwa likifanya vizuri sana. Tayari tumenunua ndege mpya sita; mbili tayari zimewasili na zinatoa huduma. Na zile nyingine, napenda niwahakikishie kuwa nazo zitakuja. Aidha, tumeamua kutekeleza mradi mkubwa wa umeme wa Stiglier’s Gorge, ambao nao ulibuniwa tangu enzi za Baba wa Taifa. Sisi tumeamua kuutekeleza. Mradi huu utakapokamilika utazalisha takriban Megawati 2,100. Tumeshatangaza zabuni; na nimearifiwa kuwa makampuni 79 yamejitokeza kuomba zabuni ya kujenga mradi huo.
Tutaendelea kupanua wigo na kuboresha huduma za jamii, hususan afya, elimu na maji. Kwa bahati nzuri, Serikali zetu mbili kila mwaka zimekuwa zikiongeza bajeti kwenye sekta hizo. Aidha, tutaimarisha usimamizi wa rasilimali zetu. Kama mnavyofahamu, nchi yetu ina rasilimali nyingi: madini, mafuta, gesi, misitu, maeneo ya hifadhi na wanyamapori, pamoja na rasilimali za kwenye bahari, maziwa na mito. Lakini ninyi ni mashahidi, rasilimali hizi bado hazijatunufaisha. Ni watu wachache tu humu nchini na wengine kutoka nje, ndio wenye kunufaika nazo.
Napenda kuwaahidi kuwa katika kipindi changu cha uongozi, kamwe sitaruhusu hali hiyo kundelea. Nitashirikiana na mwenzangu Rais Shein pamoja na ninyi wananchi katika kuhakikisha rasilimali zetu zinatunufaisha. Tayari tumeshaanza kuchukua hatua mbalimbali. Kule Bara, kwa mfano, mwezi Julai mwaka huu, tulishapitisha sheria ya kulinda rasilimali zetu, hususan madini. Aidha, tumedhibiti biashara ya madini; na matokeo yake tumeanza kuyaona. Mathalan, kufuatia agizo langu nililolitoa mwezi Machi, 2017 kuhusu kuimarisha usimamizi wa rasilimali zetu, hususan madini, uzalishaji umeongezeka tofauti na tulivyokuwa tukiambiwa awali. Nitatoa mifano michache. Kabla ya agizo langu, almasi iliyozalishwa mwezi Januari 2017, ilikuwa carats 18,808.1; Februari 2017 carats 11,260.8; na mwezi Machi 2017 carats 15,743. Na niaka ya nyuma nayo, hali ilikuwa ni hivyo. Lakini baada ya agizo, uzalishaji umeongezeka. Mwezi Juni 2017 tulizalisha carats 28,889.7; mwezi Julai 2017 carats 27,578.75; Agosti 2017 carats 32,753; na Septemba 2017 carats 27,578.75. Na sio almasi pekee ndio uzalishaji umeongezeka. Uzalishaji wa Tanzanite piaumeongezeka.
Huu ni mwanzo tu. Tutachukua hatua hizi tulizozianza kwenye rasilimali zetu zote, ikiwemo gesi, utalii, misitu na baharini; ambako pia tumekuwa tukiibiwa sana. Na kuhusu rasilimali za maji, tayari tumeshaunda Chombo cha kusimamia uvuvi kwenye Bahari Kuu (Deep Sea Fishing Authority), ambacho kwa bahati nzuri Makao Makuu yake yapo huku Zanzibar.
Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Nafahamu kuwa kutokana na hatua tunazozichukua, wamejitokeza baadhi ya watu wanaowapotosha wananchi kwa kuwaambia kuwa hali ya uchumi wetu inadorora. Huo ni uzushi. Ukweli ni kwamba uchumi wetu unazidi kuimarika. Mwaka huu unatarajiwa kukua kwa asilimia 7.1, na hivyo kuifanya nchi yetu kushika nafasi ya tatu Barani Afrika. Sambamba na hilo, mfumuko wa bei unazidi kupungua. Mwezi Julai, mfumuko wa bei ulikuwa asilimia 5.2, lakini mwezi Agosti ulishuka hadi kufikia asilimia 5.0. Na matokeo yanaonekana. Bei za bidhaa nyingi zimeshuka. Mathalan, mfuko mmoja wa saruji hivi sasa unauzwa kwa wastani wa shilingi 10,500 kutoka wastani wa shilingi 15,000; mafuta ya kupikia yameshuka kutoka wastani wa shilingi 3,095 kwa lita hadi shilingi 2,863; mafuta ya taa yameshuka kutoka wastani wa shilingi 2,862 kwa lita hadi shilingi 1,925. Mifano ipo mingi.
Kama hiyo haitoshi, ujenzi wa viwanda unaendelea vizuri. Nafahamu kuna watu wanaobeza kuhusu ujenzi wa viwanda; lakini kweli ni kwamba vinajengwa. Mathalan, mwaka 2015 vilikuwepo viwanda 49,243, lakini hadi kufikia mwanzoni mwa mwaka huu, vimeongezeka hadi kufikia viwanda 52,549. Hii inamaanisha kwamba tangu tumeingia madarakani vimejengwa viwanda vipya 3,306. Halikadhalika, uwekezaji unazidi kuongezeka. Kwa mujibu wa Ripoti ya Uwekezaji Duniani (World Investment Report) ya mwaka 2017 iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalosimamia Biashara na Maendeleo (UNACTAD), mwaka 2016 nchi yetu ilisajili miradi yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.35, na hivyo kuongoza katika eneo letu la Afrika Mashariki. Aidha, kwa mujibu wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), hadi kufikia mwezi Septemba mwaka huu, tulikuwa tumesajili miradi 271 yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.496 itakayotoa ajira zipatazo 22,000. Hii inadhihirisha kuwa uchumi wa nchi yetu unakwenda vizuri.
Licha ya ukweli huo, natambua kuwa, kutokana na hatua tunazozichukua za kuwabana mafisadi na wabadhirifu wa mali za umma, wapo wananchi wa kawaida kabisa, ambao sio wezi wala mafisadi, wanaothirika. Chukua mfano, umemkamata mwizi wa fedha za umma. Mwizi huyo kama alikuwa anatumia fedha alizoziiba kujenga nyumba zake, ni lazima ujenzi wa nyumba hizo utasimama. Ujenzi ukisimama, atakayeathirika sio huyo mwizi pekee, bali wajenzi waliokuwa wakijenga nyumba, mama lishe waliokuwa wakiwapikia wajenzi, bodaboda waliokuwa wakiwabeba wajenzi, wauza maji, soda n.k. Hili nalifahamu. Lakini kama kweli tunataka kupambana na wizi na ubadhirifu pamoja na kuleta maendeleo kwa nchi yetu, athari hizi hatuwezi kuzikwepa. Mabadiliko ya aina yoyote ile, lazima yana athari kama hizi. Lakini jambo la kututia moyo ni kwamba, athari hizi mara nyingi huwa ni za kipindi kifupi. Baada ya muda, zinakwisha. Kuna usemi usemao “Mabadiliko ni magumu mwanzoni, yanakuwa machungu yanapofikia katikati, lakini mwishoni matokeo yake ni mazuri na matamu”.
Hivyo, nawaomba wananchi mtuvumilie katika kipindi hiki cha mpito. Baada ya muda mfupi, mambo yatakuwa mazuri. Lakini hata kama hayatakuwa mazuri hivi karibuni, watoto na wajukuu wetu watanufaika. Na huo ndio uzalendo. Uzalendo maana yake ni kuwa tayari kujitolea kwa faida ya wengi au vizazi vijavyo. Waasisi na wazee wetu walifanya hivyo. Walijitolea kupigania uhuru wa nchi yetu, lakini tunaofaidi matunda ya uhuru ni sisi. Hivyo, na sisi hatuna budi kujitoa ili vizazi vyetu vijavyo vinufaike. Mimi pamoja na mwenzangu, Rais Shein, tumeamua kujitoa kuleta maendeleo ya nchi yetu. Hivyo, nawaomba wananchi mtuunge mkono. Je, mko tayari kutuunga mkono? Ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Wageni Waalikwa;
Kama nilivyosema awali, Siku ya leo pia tunaadhimisha Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka huu wa 2017. Mwenge wa Uhuru ni moja ya tunu za nchi yetu, na uliasisiwa na Baba wa Taifa. Hata kabla ya nchi yetu kupata uhuru, Baba wa Taifa alitamka maneno yafuatayo katika Bunge la Kikoloni tarehe 22 Oktoba Mwaka 1959, nanukuu,”Sisi Watanganyika tunataka kuwasha Mwenge na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete matumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo pale ambapo pana chuki, heshima ambapo pamejaa dharau”, mwisho wa kunukuu. Tamko hili, mbali na kuamsha zaidi hamasa na kuchochea harakati za nchi yetu kudai uhuru; lilibeba falsafa nzito inayotoa taswira ya Taifa ambalo Baba wa Taifa alitaka kulijenga: Taifa lenye amani, linalojitegemea na lenye kuheshimu misingi ya utu, haki na usawa wa binadamu.
Azma ya kuwasha Mwenge ilitimia kwenye mkesha wa Uhuru, tarehe 9 Desemba, 1961, ambapo marehemu Kapteni Alexander Nyirenda, na wenzake, waliupandisha Mwenge wa Uhuru katika kilele cha Mlima Kilimanjaro. Na tangu mwaka 1964, kila mwaka, Mwenge wa Uhuru umekuwa ukikimbizwa nchi nzima, kuzunguka Mikoa yote ya Tanzania Bara na huku Zanzibar, Halmashauri zote za Wilaya, Vijiji pamoja na Mitaa mbalimbali ili kuendelea kukumbushana misingi ambayo juu yake nchi yetu imejengwa na inaendelea kujengwa; na pia nafasi ya nchi yetu mbele ya mataifa na watu wa mataifa wengine.
Katika kukumbushana huku, mbio za Mwenge huambatana na shughuli za ujenzi na uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo shabaha yake ni kukuza utu na ustawi wa watanzania. Kila Mwaka, Mwenge huzindua miradi mbalimbali. Mathalan, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Mwenge wa Uhuru umezindua jumla ya miradi 6,838 yenye thamani ya takriban shilingi trilioni 2.51; wastani wa miradi 1,367.6 kwa mwaka, ambayo thamani yake kwa wastani ni shilingi milioni 500. Mwaka huu pekee (2017), miradi iliyozinduliwa ni 1,512 yenye thamani ya shilingi trilioni 1.1. Miradi ambayo imekuwa ikizinduliwa na Mwenge inahusu sekta za afya, elimu, kilimo, maji, mawasiliano, mazingira, ujenzi, uwezeshaji, uvuvi na viwanda.
Sambamba na hilo, kila mwaka, mbio za Mwenge wa Uhuru zimekuwa na kaulimbiu yake, ambapo mwaka huu inasema“Shiriki Kukuza Uchumi wa Viwanda kwa Maendeleo ya Nchi Yetu”. Nawapongeza waliobuni kaulimbiu hiyo ambayo inakwenda sambamba na Dira ya Maendeleo ya Taifa letu na pia dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga Tanzania ya viwanda ifikapo mwaka 2025. Nimefarijika zaidi kusikia kuwa katika Mbio za Mwenge mwaka huu, jumla ya viwanda 148 vimeziduliwa. Viwanda hivyo vimejengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 468.46 na vinatarajiwa kuzalisha ajira 13,370. Pamoja na ajira hizo, nina uhakika kuwa viwanda hivyo vitaingizia nchi fedha za kigeni na kuipatia Serikali yetu mapato kupitia kodi; na hatimaye kusaidia kupunguza umaskini nchini. Hii ndiyo sababu tumekuwa tukihimiza ujenzi wa viwanda. Na hizi ni baadhi ya faida za Mwenge.
Watanzania Wenzangu;
Licha ya dhana na falsafa nzuri pamoja na faida za Mwenge nilizozitaja, wapo watu wanaoupinga na kutaka ufutwe. Mimi nawashangaa sana wanaosema ufutwe! Sijui ni watu wametokea sayari gani? Wakati mwingine huwa najiuliza hivi hawa nao kweli ni sehemu ya historia ya nchi hii? Najiuliza hivyo kwa sababu, kama kweli wewe ni Mtanzania na unaifahamu kidogo historia ya nchi hii pamoja na ya Baba wa Taifa na Mzee Karume, huwezi kuthubutu kutamka kuwa eti Mwenge ufutwe. Huwezi! Mwenge wa Uhuru ni tunu tuliyoachiwa na waasisi wa Taifa hili. Na kamwe mimi siwezi kukubali Mwenge ufutwe. Niwaombe Watanzania wenzangu tuwapuuze, tuwazomee na kuwasuta wote wanaosema Mwenge ufutwe. Tunazo sababu nyingi za kukataa Mwenge wetu kufutwa, lakini kwa ajili ya muda, nitataja kama tatu hivi.
Kwanza, Mwenge wa Uhuru hautafutwa kwa sababu unachochea maendeleo. Kama mlivyosikia, wakati wa Mbio za Mwenge za Uhuru Mwaka huu, miradi mbalimbali ya maendeleo imezinduliwa. Natambua kuwa mojawapo ya hoja zinazotolewa na wenye kuupinga Mwenge wetu ni suala la gharama. Lakini mimi nafahamu kuwa katika mbio za Mwenge mwaka huu, Serikali ilitenga shilingi milioni 463 kugharamia. Sasa ukilinganisha kiasi hicho na miradi 1,512 iliyozinduliwa yenye thamani inayokaribia shilingi trilioni 1.1, ni dhahiri kuwa hoja ya gharama haina mashiko? Lakini nafahamu kuwa wapo watakaosema kuwa miradi hiyo ingeweza kuzinduliwa hata bila ya Mwenge. Huenda hilo ni kweli. Lakini tujiulize, je kama Mwenge usingekuwepo, viongozi wa vijiji, kata, tarafa, wilaya na hata mikoa kweli wangekuwa wanahagaika kila mwaka kubuni miradi, kama ilivyo sasa? Nadhani majibu mnayo.
Lakini ukiachilia mbali hilo, Mwenge wa Uhuru pia unatumika kufichua maovu. Hivi punde nimepokea taarifa ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu, ambayo pamoja na masuala mengine, imefichua ubadhirifu kwenye utekelezaji wa baadhi ya miradi. Hii ndio kazi nyingine ya Mwenge wa Uhuru. Na napenda kutumia fursa kumhakikishia Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu na Watanzania kwa ujumla kuwa Serikali itafuatilia miradi hiyo na kuwachukulia hatua stahiki watakaohusika na ubadhirifu huo.
Pili, Mwenge wa Uhuru unawaunganisha Watanzania na kuimarisha Muungano wetu. Kama nilivyogusia hapo awali, Mwenge wa Uhuru uzunguka nchi nzima, Tanzania Bara na Visiwani. Wanaokimbiza Mwenge wanatoka pande zote mbili za Muungano. Kwa kufanya hivyo, Mwenge unatuunganisha Watanzania na kuimarisha Muungano wetu. Na kila unapopita mahali, unatoa matumaini mapya (kupitia miradi) na kusambaza upendo miongoni mwa Watanzania.
Tatu, na muhimu zaidi, ni kwamba Mwenge wa Uhuru ni alama ya uhuru na utaifa wetu. Kama mnavyofahamu, kila nchi hapa duniani ina alama zake za Taifa. Na sisi ni hivyo hivyo. Moja ya alama yetu ni Mwenge wa Uhuru. Nyingine ni Wimbo ya Taifa, Bendera ya Taifa, n.k. Hivyo kuufuta Mwenge wa Uhuru ni sawa na kufuta historia na alama inayotambulisha utaifa wetu.
Zaidi ya hapo ningependa kuwataarifu Watanzania wenzangu kuwa Mwenge au alama zinazofanana na Mwenge hazipo tu hapa nchini. Zipo nchi na taasisi za kimataifa zenye alama kama hii ya Mwenge wetu wa Uhuru. Baadhi ya nchi hizo ni majirani zetu wa Kenya, Msumbiji na Rwanda. Aidha, ninyi nyote hapa ni mashahidi, nchi yetu mara kadhaa imekuwa ikipokea Kifimbo cha Malkia wa Uingereza, Mwenge wa Olimpiki, Kombe la Dunia, n.k; lakini sijawahi, hata siku moja, kusikia watu wakipinga vifimbo hivyo kuja nchini au kutaka vifutwe. Sana sana tu, baadhi ya wanaoupinga Mwenge wetu, ndio hao hao wamekuwa mstari wa mbele kwenda kuvipokea vifimbo hivyo. Binafsi, siwapingi wao kwenda kupokea vifimbo hivyo. Acha waende, hakuna ubaya. Ubaya ni pale wanapoupinga Mwenge wetu, huku wakiona fahari kupokea vifimbo hivyo.
Hivyo basi, kwa niaba ya mwenzangu Mheshimiwa Rais Dkt. Shein, napenda kurudia tena kuwaambia watu hao kuwa, katika kipindi chetu cha uongozi, Mwenge wa Uhuru utaendelea kuwepo. Na niwaombe Watanzania wote wenye mapenzi mema na nchi yetu, mtuunge mkono.
Ndugu Viongozi,
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Jambo la tatu ambalo limetukutanisha hapa leo ni kuadhimisha kilele cha Siku ya Vijana Kitaifa. Kama mnavyofahamu, duniani kote, vijana ndio uhai wa Taifa. Hii ni kwa sababu wapo wengi; wana nguvu na uthubutu. Hivyo basi, katika Siku hii ya kilele cha Sherehe ya Wiki ya Vijana Kitaifa, napenda kuwahimiza vijana kote nchini kushiriki kikamilifu katika shughuli za ujenzi wa Taifa letu. Mtambue ya kuwa Taifa hili ni lenu. Na maendeleo yake yanawategemea ninyi.
Lakini ili kijana aweze kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za ujenzi wa Taifa na kutoa mchango wenye tija kwa nchi, hana budi, kujiendeleza kielimu kila wakati na kujiepusha na vitendo vitakavyopunguza uwezo wake, ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya na ngono zembe. Na huo ndio wito wangu mwingine kwenu vijana wa Tanzania leo mnapoadhimisha kilele cha Wiki ya Vijana Kitaifa.
Waheshimiwa Mawaziri;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimesema mengi. Lakini kabla sijahitimisha hotuba yangu, napenda kuwashukuru tena Mawaziri husika kwa kunialika kwenye tukio hili. Aidha, nawashukuru tena wananchi wa Mjini Magharibi na Zanzibar kwa ujumla kwa mapokezi yenu mazuri na pia kwa kujitokeza kwa wingi kwenye tukio hili. Lakini shukrani za pekee ziende kwenye makundi yafuatayo:
Kwanza, kwa waandaji wa tukio hili. Shughuli imefana sana. Hongereni sana. Pili, natoa shukrani kwa viongozi wa dini wote ambao wametuombea dua na kuliombea Taifa letu. Tatu, natoa shukrani na pongezi nyingi sana kwa wakimbiza Mwenge wetu wa Uhuru mwaka huu wakiongozwa na Amour Hamad Amour. Mmefanya kazi kubwa sana. Hatuna cha kuwalipa.
Napenda pia kutoa shukrani zangu nyingi kwa vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuhakikisha usalama unakuwepo hapa uwanjani na sehemu zote ambazo Mwenge ulipita. Nawashukuru pia Vijana wa Halaiki kwa kutuburudisha. Mmetia fora. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, navishukuru vyombo vya habari vyote vilivyoripoti tukio hili. Tunawashukuru sana.
Mwisho kabisa, kama mnavyofahamu, mimi pamoja na kuwa Rais, ni Mwenyekiti wa CCM. Natambua kuwa hapa kuna wana-CCM wengi. Na hivi sasa Chama chetu kipo kwenye zoezi muhimu la uchaguzi. Hivyo basi, napenda niwatakie wana-CCM wote uchaguzi mwema. Wito wangu kwenu, chagueni viongozi bora, wenye uwezo wa kuongoza, wasio makundi na wala kujihusisha na vitendo vya rushwa; ili Chama chetu kibaki kuwa imara. Mara zote tukumbuke wosia wa Baba wa Taifa wakati aking’atuka mwaka 1985, kuwa “Bila CCM imara, nchi itayumba”. Kidumu Chama cha Mapinduzi.
Napenda kuhitimisha kwa moja ya kauli za Baba wa Taifa, aliyoitoa kwenye Sherehe za Miaka 40 ya Uhuru wa Ghana zilizofayika tarehe 6 Machi, 1997 mjini Accra, nanukuu “Kizazi changu kiliongoza jitihada za kuleta uhuru wa kisiasa wa Bara letu. Kizazi cha sasa cha Waafrika hakina budi kuchukua kijiti pale tulipoishia, na kwa nguvu mpya, kusukuma mbele maendeleo ya Bara letu”, mwisho wa kunukuu. Hivyo basi, leo tunapokumbuka maisha ya Baba wa Taifa pamoja na falsafa ya Mwenge wa Uhuru, sisi Watanzania wa kizazi cha sasa, hatuna budi kukumbushana kuchukua kijiti kilichoachwa na waasisi wetu ili kulipeleka Taifa letu mbele zaidi, hasa kiuchumi.
Mungu Ibariki Familia ya Baba wa Taifa!
Mungu Ibariki Familia ya Mzee Karume pamoja na Waasisi wote!
Mungu Ubariki Mwenge wa Uhuru!
Mungu Wabariki Vijana wote wa Tanzania!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Oct 03, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA 33 WA JUMUIYA YA TAWALA ZA M...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Gulamhafeez Mukadamu, Mwenyekiti wa ALAT
na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga,
Mheshimiwa Stephen Peter Mhapa, Makamu Mwenyekiti wa ALAT
na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa,
Mheshimiwa Seleman Jafo, Naibu Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais-TAMISEMI;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Waheshimiwa Wabunge mliopo hapa;
Wastahiki Mameya wa Majiji na Manispaa pamoja na
Waheshimiwa Wenyeviti wa Halmashauri za Miji na Wilaya;
Waheshimiwa Madiwani wa Dar es Salaam, mkiongozwa
na Mstaiki Meya Isaya Mwita;
Mstahiki Meya wa Zanzibar pamoja na Viongozi mbalimbali
kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;
Mhandisi Mussa Iyombe, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – TAMISEMI;
Prof. Faustin Kamuzora, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais;
Bwana Abdallah Ngodu, Kaimu Katibu Mkuu wa ALAT;
Wakurugenzi wa Majiji, Manispaa, Miji na Halmashauri za Wilaya;
Wawakilishi wa Jumuiya za Serikali za Mitaa kutoka
Nchi za Afrika Mashariki mliopo;
Wawakilishi wa Wadhamini kutoka Makampuni
na Mashirika ya Serikali na Yasiyo ya Kiserikali,
Wawakilishi wa Vikundi vya Wajasiriamali;
Ndugu Waandishi wa Habari;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu, ambaye ametupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa. Aidha, nakushukuru sana Mwenyekiti wa Jumuiya ya Tawala za Serikali za Mitaa Tanzania (Association of Local Government Authorities of Tanzania – ALAT), Mheshimiwa Mukadamu, kwa kunialika kufungua Mkutano huu Mkuu wa 33 wa ALAT. Nasema Ahsante sana.
Natambua baadhi yenu hapa mmesafiri umbali mrefu kuja kuhudhuria Mkutano huu, ambao awali ulipangwa kufanyika Jijini Mbeya, lakini siku za mwishoni ukalazimika kuhamishiwa hapa Dar es Salaam. Hivyo basi, kwanza, napenda kuwapa pole kwa uchovu wa safari. Lakini pili, kama mnavyofamu, mimi pamoja na kuwa na majukumu ya Urais, nina dhamana kwenye Wizara ya TAMISEMI; hivyo basi, napenda niwakaribishe wajumbe wote hapa Dar es Salaam na katika Mkutano huu wa 33 wa ALAT. Karibuni sana ndugu wajumbe.
Napenda pia hapa mwanzoni kabisa nimshukuru Mwenyekiti wa ALAT Taifa kwa salamu za pongezi alizozitoa kwangu, hususan kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa nchi yetu. Namshukuru pia kwa pongezi zake kuhusu utendaji kazi wa Serikali ya Awamu ya Tano. Nasema ahsante sana. Mmezidi kutupa moyo wa kuendelea kufanya kazi kwa bidii. Lakini nami ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza, wewe Mheshimiwa Mwenyekiti na Makamu wako, Wastahiki Mameya wa Majiji na Manispaa pamoja na Wenyeviti wa Halmashauri zote nchini kwa kuchaguliwa kwenu. Napenda niwaahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itashirikiana nanyi kwa karibu katika kuhakikisha tunaleta maendeleo kwa wananchi na nchi yetu kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ndugu Wajumbe, Mabibi na Mabwana;
Kwangu mimi, Mkutano huu ni muhimu sana. Ni muhimu kwa sababu, kama mnavyofahamu, ALAT ni chombo kinachounganisha pamoja mamlaka na wadau mbalimbali wanaohusika na masuala ya Serikali za Mitaa hapa nchini. Na sote hapa tunatambua kuwa Serikali za Mitaa ni mamlaka ambazo zipo karibu zaidi na wananchi. Kwa sababu hiyo, binafsi naona kuwa hii ni fursa nzuri kwangu kuzungumza kwa kina na Watanzania wenzangu; na hasa kwa kuzingatia kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kuhudhuria Mkutano huu wa ALAT, tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa nchi yetu. Hivyo basi, nina imani Mheshimiwa Mwenyekiti pamoja na ndugu wajumbe mtaniruhusu, kabla ya kuzungumzia masuala yaliyotuleta hapa, kueleza hatua mbalimbali ambazo tumechukua tangu tumeingia madarakani pamoja na mipango na mikakati tuliyonayo ya kuleta maendeleo kwa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe;
Tangu tumeingia madarakani, takriban miezi 23 iliyopita, tumefanya mambo mengi ya kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Mtakumbuka, tulianza kwanza kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kudhibiti ubadhirifu wa mali za umma. Tulibana mianya ya ukwepaji kodi na hivyo kutuwezesha kuongeza ukusanyaji wa mapato kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 kwa mwezi hadi kufikia shilingi trilioni 1.3. Sambamba na kuongeza ukusanyaji mapato, tuliamua kudhibiti ubadhirifu wa mali za umma. Tumezuia safari za nje, warsha na semina zisizo na tija. Hivi majuzi tu mmesikia kuwa ujumbe wetu kwenye Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ulikuwa na watu watatu tu na walituwakilisha vyema.
Kutokana na kuongeza mapato na kubana matumizi, hivi sasa tunawalipa mishahara ya watumishi wetu kwa wakati. Aidha, tumeweza kulipa madai mbalimbali ya watumishi, ikiwa ni pamoja na michango yao kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii. Zaidi ya hayo, tumeweza kuongeza bajeti yetu ya maendeleo kutoka wastani wa asilimia 26 hadi kufikia wastani wa asilimia 40 hivi sasa.
Hii ndiyo imetuwezesha kupanua wigo na kuboresha huduma mbalimbali za jamii, hususan elimu, afya na maji. Kama mnavyofahamu, kwenye elimu, baada ya kuingia madarakani, tulianza kutoa elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo mwanzoni tulikuwa tukitenga kila mwezi shilingi bilioni 18.77. Mwezi Julai 2016, kiasi hicho kiliongezwa hadi kufikia shilingi bilioni 23.868, na hivyo kufanya hadi mwezi Agosti mwaka huu, kuwa tumetumia kiasi cha shilingi bilioni 465.6 kugharamia elimu bila malipo. Matokeo yake, bila shaka, nyote hapa mnafahamu. Idadi ya wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza imeongezeka maradufu; darasa la kwanza kwa takriban asilimia 90 na kidato cha kwanza takriban asilimia 25. Tumeongeza pia idadi ya wanafunzi wa elimu ya juu wanaopata mikopo kutoka 98,300, wakati tunaingia madarakani, hadi kufikia takriban 125,000. Hii imewezekana baada ya kuongeza bajeti ya mikopo kutoka shilingi bilioni 365 hadi kufikia shilingi bilioni 483.
Kwenye afya, nako tumeimarisha na kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo. Tumeongeza bajeti ya kununua madawa kutoka shilingi bilioni 31 wakati tunaingia madarakani hadi kufikia shilingi bilioni 269, mwaka huu wa fedha. Hii imeongeza sana upatikanaji wa madawa kwenye hospitali zetu, na hasa baada ya Serikali kuanza utaratibu wa kununua dawa moja kwa moja kutoka kwenye viwanda zinakozalishwa. Aidha, Serikali imegawa katika kila halmashauri vifaa tiba, ikiwemo vitanda ya kawaida, vitanda vya kujifungulia, magodoro na mashuka, ambavyo thamani yake kwa ujumla ni shilingi bilioni 3.58. Halikadhalika, katika kuboresha Huduma za Afya ya Mama na Mtoto, Serikali ilipata fedha jumla ya shilinigi bilioni 161.9 kutoka Benki ya Dunia pamoja na wadau wengine wanaosaidia sekta ya afya kwenye Mfuko wa Pamoja (Busket Fund). Fedha hizo zimepangwa kutumika kuboresha vituo vya afya 170 ili kuviwezesha kutoa huduma za uzazi za dharura kwa lengo la kuokoa maisha ya mama na mtoto; na zinatumwa moja kwa moja katika vituo vya afya husika katika mwaka huu wa fedha.
Kuhusu sekta ya maji, miradi mingi ya maji hivi sasa inatekelezwa sehemu mbalimbali nchini. Karibu kwenye mikoa yote kuna miradi mikubwa ya maji inatekelezwa. Mathalan, mwezi Machi 2017, nilikuwa Mkoa wa Lindi ambapo nilitoa maelekezo ya kukamilishwa kwa haraka mradi wa maji wa Ng’apa wenye thamani ya shilingi bilioni 32, ambao nimeambiwa unaendelea kukamilika. Mwezi Juni mwaka huu, nilizindua Mradi wa Maji wa Ruvu Juu pale Mlandizi kwa ajili ya kuhudumia Jiji hili la Dar es Salaam na sehemu za Mkoa wa Pwani. Aidha, mwezi Julai, nilizindua mradi mkubwa wa maji pale Sengerema wenye thamani ya shilingi bilioni 22.4. Mwezi Julai pia niliweka Mawe ya Msingi kwenye mradi wa maji wa Kigoma wenye thamani ya shilingi bilioni 42 na Mradi Mkubwa wa Maji kutoka Ziwa Victoria kwenda miji ya Nzega, Tabora na Igunga wenye thamani ya shilingi ya shilingi bilioni 550. Juzi mmeshuhudia Mheshimiwa Waziri Mkuu akizindua mradi wa maji kule Longido wenye thamani ya shilingi bilioni 16; lakini nafahamu pia mradi wa maji wa Musoma umekamilika na unasubiri kuzinduliwa. Halikadhalika, nafahamu kuwa kuna mradi mkubwa wa maji unatekelezwa katika jiji la Arusha wenye thamani ya shilingi bilioni 476, na wakati wowote tutaanza utekelezaji wa mradi mwingine mkubwa wenye thamani ya shilingi bilioni 250 kwa ajili ya miji ya Bariadi, Legangabilili, Maswa, Meatu na Busega. Kama hiyo haitoshi, mwezi Julai mwaka huu, Serikali ya India ilitupatia mkopo wa masharti nafuu wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 500, sawa na takriban shilingi trilioni 1.2, kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji kwenye miji 17, ikiwemo Zanzibar. Kwa ujumla, miradi mingi inatekelezwa sehemu mbalimbali nchini. Hivyo basi, nina imani kuwa baada ya muda mfupi, tutakuwa tumepunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la maji nchini. Nitoe wito kwenu viongozi wa Serikali za Mitaa kuendelea kuwahamasisha wananchi kutunza mazingira pamoja na vyanzo vya maji. Bila kufanya hivyo, itafika wakati tutakuwa na miundombinu mizuri isiyotoa maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe;
Mbali na kuboresha huduma za jamii, tumeweza kuimarisha miundombinu ya kiuchumi, hususan usafiri na nishati. Tumeanza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza na Kigoma na kisha nchi za Burundi na Rwanda, kwa fedha zetu wenyewe. Ujenzi wa kipande cha kilometa 300 kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro tayari umeanza, ambapo kiasi cha shilingi trilioni 2.74 kitatumika. Na hivi majuzi (ijumaa), tumesaini mkataba wa kuanza ujenzi wa kipande cha kilometa 412 kutoka Morogoro hadi Dodoma (Makutopora) kwa thamani ya shilingi trilioni 4.328; na hivyo gharama za ujenzi kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma kufikia shilingi trilioni 7.062.
Tunafanya upanuzi wa Bandari zetu za Mtwara na Dar es Salaam. Mwezi Machi mwaka huu, niliweka Jiwe la Msingi la Upanuzi wa Bandari ya Mtwara kwa thamani ya shilingi bilioni 130. Aidha, mwezi Julai mwaka huu, niliweka Jiwe la Msingi la Upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, ambao thamani yake ni shilingi bilioni 926.2. Kama hiyo haitoshi, wakati nikiwa Tanga katika sherehe za kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga, nilimwagiza Waziri wa Ujenzi kuanza taratibu za kutafuta mkandarasi wa kupanua Bandari ya Tanga kwa thamani ya shilingi bilioni 16. Vilevile, tumetengeneza meli mbili za Mv. Iringa na Mv. Ruvuma, ambazo zinatoa huduma katika Ziwa Nyasa. Aidha, tupo katika hatua za mwisho za kupata wakandarasi kwa ajili ya ukarabati wa meli mbili za Mv. Victoria na Butiama pamoja na ununuzi wa meli mpya kwa ajili ya Ziwa Victoria.
Sambamba na hayo, tunakamilisha upanuzi wa Viwanja Vikubwa vya Ndege vya Mwalimu Julius Nyerere kwa gharama ya shilingi bilioni 560 na Kilimajaro kwa thamani ya shilingi bilioni 91. Aidha, tunaendelea na ukarabati wa viwanja takriban 11 vya ndege sehemu mbalimbali nchini, ikiwemo Mwanza (shilingi bilioni 90); Mtwara (shilingi bilioni 46); Shinyanga (shilingi bilioni 49.2); Sumbawanga (shilingi bilioni 55.9); Musoma (shilingi bilioni 21), Songea (shilingi bilioni 21) na Iringa (shilingi bilioni 39). Tumenunua ndege mpya sita, mbili tayari zimewasili na kuanza kazi, kwa ajili ya kutoa huduma ya usafiri na kukuza sekta ya utalii. Kama mnavyofahamu, ukuaji na ustawi wa sekta ya utalii kwa kiasi kikubwa unategemea uwepo na ubora wa usafiri wa anga katika nchi. Vilevile, ujenzi wa barabara unaendelea vizuri. Tangu tumeingia madarakani tumeshajenga takriban kilometa 1,500 za lami kwa thamani ya shilingi trilioni 1.8. Na nyingi bado tunaendelea kuzijenga. Nikianza kuzitaja tunaweza kumaliza kesho. Lakini kwa kuwa leo tupo hapa Dar es Salaam, niseme tu kuwa, moja ya barabara tunayotarajia kuanza kujenga hivi karibuni ni barabara ya njia sita kutoka Dar es Salaam hadi Chalinze. Aidha, tunaendelea na ujenzi wa barabara za juu pale TAZARA (shilingi bilioni 94.031) na Ubungo (shilingi bilioni 177.424); na muda si mrefu tutaanza ujenzi wa Awamu ya II, III na III za miundombinu ya magari ya mwendokasi kwa thamani ya shilingi bilioni 891. Tunajenga miundombinu hii ili kupunguza tatizo la msongamano wa magari katika Jiji hili.
Kuhusu umeme, nako tunaendelea vizuri. Lakini tunafahamu kuwa mahitaji ya umeme nchini bado ni makubwa. Hivyo, tunaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuzalisha umeme, ikiwemo Kinyerezi I na II, ambayo kwa pamoja inatarajiwa kuzalisha Megawati 565, kwa kutumia gesi yetu asilia. Miradi hii kwa ujumla ina thamani ya shilingi trilioni 1.2. Aidha, maandalizi kwa ajili ya miradi ya Kinyerezi III na IV, ambayo itazalisha takriban Megawati 600, inaendelea vizuri. Tumeanza pia maandalizi ya ujenzi wa mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa maji pale Stiglier’s Gorge, ambao utazalisha Megawati 2,100. Tunataka, hadi kufikia mwaka 2020, nchi yetu iwe na angalau Megawati 5,000 kutoka Megawati 1,460 za sasa. Sambamba na hilo, tunaendelea na jitihada za kupeleleka umeme vijijini. Mpaka sasa, tumeshapeleka umeme kwenye vijiji zaidi ya 4,000. Aidha, mwaka huu tumeanza Awamu ya Tatu ya Mpango wa Umeme vijijini. Lengo letu ni kufikisha miundombinu ya umeme kwenye vijiji vipatavyo 7,873 ifikapo mwaka 2020/21. Katika bajeti ya mwaka huu, tumetenga shilingi bilioni 469.09 kuanza kutekeleza mradi huo. Tunataka dhana ya viwanda inasambae hadi vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe;
Mbali na kuongeza ukusanyaji mapato na kudhibiti matumizi, tumeimarisha nidhamu na kurejesha heshima kwenye utumishi wa umma. Tumewachukulia hatua za kinidhamu baadhi ya watumishi wazembe na wala rushwa. Zaidi ya hapo, tumewaondoa takriban watumishi hewa wapatao 20,000, ambao walikuwa wakiigharimu Serikali takriban shilingi bilioni 19.848 kwa mwezi; na kwa mwaka shilingi bilioni 238.176. Vilevile, tumewaondoa watumishi wenye vyeti feki wapatao 12,000, ambao kwa mwaka waligharimu Serikali shilingi bilioni 142.9. Tumefanya hivyo ili kurudisha nidhamu na kuenzi elimu na ueledi katika utumishi wa umma. Mtakubaliana nami kuwa, uwepo wa watumishi hewa na wenye vyeti feki ulikuwa ukizorotesha na kupunguza ufanisi katika utoaji huduma kwenye taasisi za umma. Aidha, uwepo wa watumishi wenye vyeti feki ulikuwa unapunguza heshima na hadhi ya elimu na ujuzi, na hivyo, kushusha ari na morali miongoni mwa watumishi wenye sifa.
Sambamba na hilo, tumejitahidi kuondoa kero mbalimbali, ambazo zilikuwa zikiwasumbua wananachi. Mathalan, tumeondoa kero za utitiri wa kodi kwa wakulima, wafugaji na wavuvi. Tumefuta tozo 80 kwa wakulima, tozo 7 kwa wafugaji na tozo 5 kwa wavuvi. Tumepiga marufuku kutoza kodi mazao yanayosafirishwa kutoka Halmashauri moja kwenda nyingine, ambayo uzito wake hauzidi tani moja. Na kwa kuwa tozo hizi nyingi tulizozifuta zilikuwa zikisimamiwa na ninyi watu wa Serikali za Mitaa, niwaombe kupitia vikao vyenu, mkafanye taratibu za kuzifuta kama bado hamfanya hivyo. Lakini, kama hiyo haitoshi, kwa wakulima pia, kufuatia uamuzi wa Serikali wa kuanzisha utaratibu wa kununua mbolea kwa pamoja (Bulk Procurement System – BPS), tumeweza kupunguza bei ya mbolea ya kupandia na kukuzia kuanzia mwezi uliopita (Septemba). Mathalan, Mkoani Lindi, bei ya mfuko mmoja wa mbolea ya kupandia imeshuka kutoka shilingi 100,000 hadi kufikia shilingi 51,000. Mikoa mingine bei zimepungua kutegemeana na gharama za usafirishaji. Na huu ni mwanzo tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe;
Baada ya kuchukua hatua za kuimarisha ukusanyaji wa mapato na kudhibiti matumizi; kuboresha huduma za jamii; kuimarisha miundombinu ya uchumi; kurejesha heshima ya utumishi wa umma na kushughulikia baadhi ya kero zinazowakabili wananchi wetu; ambazo kimsingi, bado tunaendelea nazo, sasa tumeanzisha vita ya uchumi. Kama mnavyofahamu, nchi yetu ni tajiri. Tuna rasilimali za kila aina. Tunayo madini misitu, rasilimali za misitu na majini, n.k. Aidha, nchi yetu inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya utalii duniani baada ya Brazil. Lakini pamoja na kuwa na rasilimali nyingi kiasi hicho, bado hazijatunufaisha. Wanaonufaika ni watu wengine.
Kutokana na hali hiyo, tumeamua kuchukua hatua za makusudi kulinda rasimali zetu. Mlisikia kuwa tuliunda Tume za kuchunguza biashara ya madini na vito vya thamani. Matokea yake, kila mmoja wetu hapa amesikia. Lakini kwa kifupi, tulikuwa tunaibiwa sana. Kwa sababu hiyo, mwezi Julai 2017 tulipitisha Sheria za kulinda rasilimali zetu, hususan madini. Aidha, kwa lengo hilo hilo la kulinda rasilimali zetu, hivi majuzi nikiwa Mererani niliagiza kuanza mara moja kwa ujenzi wa uzio kuzunguka eneo lenye rasilimali nyingi ya madini ya Tanzanite, ili kudhibiti vitendo vya wizi. Nafurahi ujenzi huo tayari umeanza. Lakini niseme tu kuwa huu ni mwanzo tu. Hatutaishia kwenye madini pekee. Tutaenda pia kwenye rasilimali zetu nyingine, ikiwemo za utalii, misitu na za majini. Tunataka kuona, rasilimali za nchi yetu, zinatunufaisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe;
Katika kuchukua hatua hizi, ni dhahiri kuwa wapo watu walioathirika na kuumia. Na natambua kuwa wapo watu wanalalamika. Lakini kwangu mimi, hili ni jambo la kawaida, kama kweli tunahitaji maendeleo. Maendeleo hayaji kirahisi. Maendeleo sio lelemama. Maendeleo ni mapambano. Hivyo basi, niwaombe Watanzania wenzangu tujidhatiti katika harakati za kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Waingereza wana usemi wao usemao “No Pain, No Gain” au “No sweet without sweat”. Lakini ningependa kusema tu kuwa watu wengi wanaolalamika hivi sasa ni wale waliokuwa wakinufaika na mfumo ulikuwepo zamani. Huwezi kutegemea mmiliki wa benki iliyokuwa ikinufaika kwa kufanya biashara na Serikali afurahie hatua tunazozichukua; Haiwezekani mtu aliyekuwa akilipwa mishahara na posho za watumishi hewa afurahie hatua tunazochukua; Huwezi kutegemea mtu aliyekuwa akikwepa kodi afurahie hatua tunazozichukua; Huwezi kutegemea mtu aliyezoea kusafiri nje kila wiki afurahie hatua tunazozichukua; huwezi kutegemea mtu aliyepata ajira kwa kutumia cheti feki alichokinunua Kariakoo afurahie hatua tunazozichukua. Lakini pia huwezi kutegemea mtu aliyekuwa akinufaika na fedha za pembejeo hewa (ambapo katika Halmashauri 140 zilizofanyiwa uchunguzi, imebainika kuwa zilitolewa pembejeo hewa zenye thamani ya shilingi bilioni 57.963) na kaya masikini hewa (56,000) kupitia TASAF, afurahie hatua tunazozichukua. Ni dhahiri kuwa watu waliokuwa wakinufaika, watalalamika.
Hivyo basi, binafsi sishitushwi sana na malalamiko yanayotolewa na baadhi ya watu. Natambua, ukitumbua mtu jipu ni lazima atalalamika. Sana sana tu, kelele zinazopigwa hivi sasa zinatuongezea nguvu zaidi ya kuendelea na jitihada tulizozianza, ambazo kwa hakika kabisa, naweza kusema sio tu zinaungwa mkono na wananchi walio wengi bali pia zimeanza kuleta matokeo chanya ya kiuchumi kwa nchi yetu. Kama mnavyofahamu, nchi yetu ni miongoni mwa nchi zinaongoza kwa ukuaji uchumi Barani Afrika hivi sasa, ambapo mwaka huu uchumi wetu unatarajiwa kukua kwa asilimia 7.1. Hii inafanya nchi yetu kushika nafasi ya tatu. Sambamba na hilo, tumeweza kudhibiti mfumko wa bei. Mathalan, mwezi Julai, mfumko wa bei ulikuwa asilimia 5.2, lakini mwezi Agosti ulishuka hadi kufikia asilimia 5.0. Hii ni dalili njema. Lakini zaidi ya hapo, kinyume na baadhi ya watu wanavyosema, nchi yetu imeendelea kung’ara katika kuwavutia wawekezaji wengi. Hivi majuzi mmemsikia Mkurugenzi Mkuu wa Kituo Cha Uwekezaji (Tanzania Investment Centre – TIC) akieleza kuwa mwaka uliopita nchi yetu iliongoza kwa kuvutia wawekezaji wengi kwenye Ukanda wetu wa Afrika Mashariki. Tathmini hii inaenda sambamba na Ripoti ya African Economic Outlook Toleo la 16 iliyotolewa kwa pamoja na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), ambayo inataja nchi yetu kuwa miongoni mwa nchi kumi bora Barani Afrika kwa kuvutia wawekezaji mwaka 2016. Na hiki ni kielezo kuwa hatua tunazochukua ni nzuri na mwelekeo wetu ni mzuri. Na huenda hii ndio sababu viongozi wengi wa nje wanatembelea nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Ndugu Wajumbe, Mabibi na Mabwana;
Niliona nianze na hayo ili kuwapa taswira halisi ya hali ilivyo hapa nchini. Na kwa kuwa ninyi mko karibu zaidi na wananchi na mnashirikiana nao kwenye mambo mengi, nina uhakika kuwa mtaenda kuwafafanuliwa kuhusu hatua hizi tunazozichukua. Baada ya kusema hayo, sasa naomba nizungumzie masuala yanayohusu Mkutano huu wa leo.
Kwanza kabisa, napenda kuipongeza ALAT pamoja na mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kwa kazi kubwa mnazofanya katika kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Mafanikio mengi ya Serikali niliyoyataja hapo awali, yamepatikana kutokana na jitihada mnazozifanya ninyi lakini pia ushirikiano mnaotupa sisi wa Serikali Kuu. Kwa kutumia vyanzo vyenu vya mapato, mmeweza kutekeleza miradi mingi ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa shule, hospitali, vituo vya afya, zahanati, miradi ya maji pamoja na barabara. Aidha, mara nyingi, ninyi ndio mmekuwa wasimamizi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali Kuu kwenye maeneo yenu. Kwa sababu hiyo, sina budi, kuwapongeza.
Lakini pamoja na pongezi hizo, hampaswi kuridhika na mafanikio yaliyopatikana. Kama mnavyofahamu, nchi yetu bado ina safari ndefu ya kufikia kule tunakotamani. Mathalan, nimeeleza hapo awali kuwa Serikali hivi sasa inatekeleza elimu bila malipo, lakini ukiachilia mbali tatizo la uhaba wa madawati ambalo tumelipunguza kwa kiwango kikubwa, bado tuna upungufu wa madarasa, maabara, vyoo, nyumba za walimu, n.k. Hivyo basi, Mamlaka za Serikali za Mitaa, hazina budi, kubuni mikakati ya kushughulikia matatizo hayo. Aidha, kwa kuwa mko karibu na wananchi, mnao wajibu wa kuwahimiza wananchi kupeleke watoto wao mashuleni ili wanufaike na fursa iliyotolewa na Serikali ya kutoa elimu bila malipo.
Kwenye afya pia, bado kuna upungufu mkubwa ya miundombinu, ikiwemo hospitali, vituo vya afya, zahanati, nyumba za watumishi, n.k. Huko nako hamna budi kubuni mikakati ya kushughulikia matatizo hayo. Aidha, kwa kuwa hivi sasa Serikali imeongeza upatikanaji wa madawa kwenye hospitali zetu, niwaombe waheshimiwa Madiwani na Wakurugenzi mwendelee kuhamasisha wananchi kujiunga na mifuko ya bima za afya ili kupata matibabu bila vikwazo. Vilevile, hakikisheni mnasimamia vyema fedha na matumizi ya dawa, ikiwemo kuanzisha mifuko ya dawa (Drug Revolving Fund) kwa kila Halmashari, ili kuhakikisha upatikanaji endelevu wa fedha za dawa.
Sambamba na hayo, ili kuhakikisha mnakuwa na uwezo wa kutosha wa kuboresha huduma za jamii nilizozitaja na kutekeleza miradi ya maendeleo, hamna budi kuimarisha ukusanyaji wa mapato. Nafahamu hii ni changamoto kubwa inayozikabili mamlaka za Serikali za Mitaa. Na kimsingi, nionavyo mimi, tatizo sio kwamba hakuna vyanzo vya mapato. Hapana. Hali hii inatokana na sababu kubwa mbili. Kwanza, fedha nyingi zinazokusanywa hupotelea kwenye mifuko ya “wajanja” wachache. Pili, watendaji wengi wanakosa ubunifu katika kubuni vyanzo endelevu vya mapato. Ndio maana kila siku utaona wanaongeza tozo kwenye mazao ya wakulima, wavuvi au wafugaji. Hivyo basi, nitoe wito kwenu kuhakikisha mnatengeneza mifumo madhubuti ya ukusanyaji mapato, hususan ukusanyaji mapato kwa njia ya kielektroniki. Na katika hili, ningependa kuwasisitiza kutumia Wakala wa Serikali Mtandao katika kutengeneza mifumo yenu ya ukusanyaji kodi. Aidha, nawahimizeni kubuni vyanzo endelevu vya mapato.
Halikadhalika, kuhakikisheni mnasimamia vizuri fedha mnazokusanya na zile zinazotolewa na Serikali Kuu kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. Natambua hivi sasa suala la hati chafu limepungua kwenye halmashauri nyingi. Lakini hii haimanishi kuwa ubadhirifu na wizi umekwisha kwenye Halmashauri zetu. Ubadhirifu bado upo. Imethibitika kuwa mara nyingi taarifa za vitabuni hazifanani na hali halisi ya utekelezaji wa miradi na kazi (value for money). Kwa maneno mengine, kazi inayofanyika hailingani na thamani halisi ya fedha inayotumika. Hivyo basi, nawaomba ndugu wajumbe mlipe suala hili la usimamizi wa fedha za Serikali kipaumbele kinachostahili. Miradi inayotekelezwa ni lazima iendane na thamani ya fedha zinazotolewa. Na katika hili, msisite kuwachukuliwa hatua za kinidhamu au kuwatumbua wale wote wakatakaojihusisha na ubadhirifu wa fedha zinazotolewa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi. Lakini niwaombe na ninyi kuacha mtindo wa kutoa zabuni kwenye makampuni yenu au ya washirika wenu, ambayo hayana uwezo wa kutekeleza miradi husika.
Masuala mengine ambayo ningetamani sana kuona mnayapa kipaumbele kwenye maeneo yenu ni kudhibiti migogoro na makundi kwenye halmashauri zetu. Haipendezi kuona, kwenye Halmashauri, kuna kundi la Meya na Naibu Meya; ama kundi la Mwenyekiti na Mkurugenzi. Hali hii inazorotesha utendaji na kupunguza kasi ya kuwapelekea maendeleo wananchi. Nawasihi pia muendelee kushughulikia kero mbalimbali zinazowakabili wananchi, hasa wananchi wa kipato cha chini, ikiwemo, kama nilivyosema awali, utitiri wa kodi kwa wakulima, wafugaji na wavuvi; na halikadhalika ukosefu wa maeneo ya biashara kwa wafanyabiashara wadogo. Vilevile, nawasihi muendelee kuwahimiza wananchi kuhusu umuhimu wa kudumisha amani na umoja wetu, kulipa kodi na kuchapa kazi kwa bidii. Nina imani, sote tukifanya haya, nchi yetu itapata maendeleo, tena kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika risala yako umeeleza kuhusu mipango yenu mbalimbali na kuwasilisha baadhi ya maombi. Kwa ujumla, niseme tu kuwa nimeyapokea maombi yenu yote. Lakini nakiri kuwa nimefarijika sana kusikia azma yenu ya kuhamishia Makao Makuu yenu kutoka hapa Dar es Salaam kwenda Dodoma, Makao Makuu ya nchi yetu. Nawapongezi sana kwa kuunga mkono dhamira ya Serikali ya kuhamia Dodoma. Na napenda kutumia fursa hii kuwahakikishia kuwa, kama nilivyoahidi kwenye hotuba yangu ya kupokea wadhifa wa kuwa Mwenyekiti wa CCM mwezi Julai mwaka jana, hadi kufikia mwaka 2020, Serikali yote itakuwa imehamia Dodoma. Kama mnavyofahamu, tayari Waziri Mkuu, Mawaziri, Makatibu Wakuu na baadhi ya watendaji wa Wizara wameshahamia Dodoma. Makamu wa Rais anatarajia kuhamia mwaka huu. Na mimi natarajia kuhamia mwakani. Hivyo basi, narudia tena, kuwashukuru kwa uamuzi wenu wa busara wa kuhamia Dodoma. Na kuhusu jengo mnalotaka kujenga Dodoma kwa ajili ya ofisi na kitega uchumi, wakati ukifika, Serikali kulingana na uwezo wake wa kifedha, itaangalia uwezekano wa kuwaunga mkono.
Kwenye Risala yako pia umeeleza suala la ucheleweshaji wa fedha za maendeleo kutoka Serikali Kuu, suala la uhaba wa watumishi wa Serikali za Mitaa na pia posho za Waheshimiwa Madiwani. Serikali inatambua masuala hayo yote. Tutaendelea kuhimiza HAZINA kutoa fedha za maendeleo kwa haraka. Kama mnavyofahamu, tangu tumeingia madarakani, tumejitahidi sana kuhakikisha fedha zinatolewa kwa wakati. Mathalan, katika Bajeti ya mwaka 2014/2015 fedha za maendeleo zilizotengwa kwenda kwenye halmashauri (Serikali za Mitaa) ni shilingi bilioni 339.8 lakini zilizotoka zilikuwa shilingi bilioni 250.2 sawa na asilimia 62; mwaka 2015/16 zilitengwa shilingi bilioni 296.3, zikatolewa shilingi bilioni 168.8 sawa na asilimia 57; mwaka 2016/17 zilitengwa shilingi bilioni 256.7, zilizotolewa ni shilingi 251.5 sawa na asilimia 98. Na katika mwaka huu wa fedha, tumetenga shilingi bilioni 308.6, na napenda niwahakikishie fedha zote zitatolewa. Sambamba na hilo, mwaka huu, tumeanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), ambayo imetengewa shilingi bilioni 246, ukiachilia mbali fedha zilizoahidiwa na wafadhili mbalimbali, ikiwemo Benki ya Dunia. Hivyo basi, sina shaka, tatizo la fedha za maendeleo litazidi kupungua.
Kuhusu tatizo la uhaba wa watumishi baada ya kuwaondoa watumishi wenye vyeti feki, Serikali mwaka huu imepanga kuajiri watumishi wapya wapatao 52,000, wakiwemo watumishi wa afya, walimu na watumishi wa kada nyingine. Hivyo basi, nina imani kuwa hii itapunguza uhaba wa watumishi kwenye Serikali za Mitaa. Ombi langu tu msiajiri watumishi wasio na sifa. Lakini niwe mkweli ombi lenu la kuongeza posho kwa madiwani, kidogo litaiwia Serikali vigumu kulitekeleza kwa wakati huu. Kama nilivyosema hapo awali, kwa sasa, Serikali imeelekeza nguvu zake katika kuboresha huduma za jamii na kujenga miundombinu ya kiuchumi. Hivyo basi, niwaombe Waheshimiwa Madiwani mtuelewe katika hili. Aidha, nawaombeni mzidi kuwahamisha Watanzania kuchapa kazi kwa bidii na kulipa kodi ili kuongeza uwezo wetu wa kifedha. Uwezo wetu ukiimarika, Serikali kamwe haitasita kuboresha maslahi sio tu yenu ninyi Waheshimiwa Madiwani bali pia watumishi wote wa umma.
Umeeleza pia kuhusu ombi la kutaka kuridhiwa kwa Mkataba wa Umoja wa Afrika kuhusu Ugatuaji Madaraka (The African Union Charter on Principles and Values on Decentralization, Local Governance and Local Development) pamoja na ombi la kutaka nchi yetu kuwa Makao Makuu ya Jumuiya ya Tawala za Serikali ya Mitaa kwa Kanda ya Afrika. Maombi haya nayo tumeyapokea. Nitaziagiza taasisi husika kupitia Mkataba huo na endapo haukinzani na Katiba na Sheria zetu, uweze kuridhiwa na Bunge letu. Na kuhusu ombi la nchi yetu kuwa Makao Makuu, natambua faida za kuwa mwenyeji wa Taasisi hiyo. Hata hivyo, kabla ya kukubali kuipokea taasisi hiyo, ni vyema tathmini ikafanyika kuhusu mahitaji ya fedha yanayotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Siwezi kuhitimisha hotuba yangu bila kugusia kaulimbiu ya Mkutano huu, ambayo inasema “Ardhi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ni chachu ya Maendeleo, Halmashauri zitenge ardhi kwa ajili ya Uwekezaji wa Viwanda Vidogo na Vikubwa”. Kama mnavyofahamu, kipaumbele kikubwa cha Serikali ya Awamu ya Tano ni ujenzi wa Viwanda. Na ili kujenga viwanda, unahitaji ardhi. Hivyo, kaulimbiu hii ni nzuri na imekuja kwa wakati muafaka. Kwenye ziara zangu maeneo mengi nchini, nimekuwa nikihimiza wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya na Mikoa kutenga maeneo na kuweka miundombinu rafiki ili kuwavutia wawekezaji kujenga viwanda. Hivyo basi, kwa mara nyingine napenda kurudia tena wito huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI;
Ndugu Wajumbe, Mabibi na Mabwana;
Nimezungumza mengi. Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kukushukuru tena Mwenyekiti wa ALAT kwa kunialika kufungua Mkutano huu. Napenda kuwahakikishia tena kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ipo pamoja nanyi. Nitafuatilia Mkutano huu, na yote mtakayokubaliana, nawaahidi kuwa Serikali itayazingatia na kuyatekeleza. Wito wangu kwenu, mjadiliane kwa amani na uwazi.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka kuwa Mkutano wa 33 wa Jumuiya ya Tawala za Serikali za Mitaa (ALAT) umefunguliwa rasmi.
Mungu Ibariki ALAT!
Mungu Zibariki Mamlaka zote za Serikali za Mitaa Nchini!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Aug 23, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA KUWEKA JIWE LA MSINGI LA MRADI WA KUBORESHA BANDARI Y...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Waziri mliopo;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Dkt. Noman Sigala King, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu;
Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mwenyekiti wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Bajeti;
Mheshimiwa Sarah Cooke, Balozi wa Uingereza nchini;
Mheshimiwa Mama Bella Bird, Mwakilishi wa Benki ya Dunia;
Mwakilishi wa Trade Mark East Africa;
Waheshimiwa Wabunge mliopo na Mstahiki Meya wa Dar es Salaam;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo hapa;
Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi ya Mamlaka ya Bandari Tanzania;
Ndugu Mkurugenzi Mkuu na Wafanyakazi wa Mamlaka
ya Bandari Tanzania;
Waheshimiwa Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nianze kwa kuungana na wote walionitangulia kuzungumza katika kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kushuhudia tukio hili. Aidha, napenda nitoe shukrani zangu nyingi kwa Mheshimiwa Waziri, Prof. Mbarawa, pamoja na uongozi mzima wa Mamlaka ya Bandari Tanzania kwa kunipa heshima ya kuwa Mgeni Rasmi katika hafla hii ya kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Kuboresha Bandari ya Dar es Salaam. Ahsanteni sana.
Mbele yangu hapa nawaona wageni. Namwona Mheshimiwa Balozi Cooke wa Uingereza; Mama Bird, Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini; pamoja na wawakilishi wa Shirika la Maendeleo la Uingereza (DFID) na Trade Mark East Africa, ambao kwa pamoja wametoa mchango wao katika kufadhili mradi huu. Tunawashukuru sana kwa ujio wenu lakini pia kwa kutuunga mkono katika kuutekeleza mradi huu muhimu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tukio hili la uwekaji Jiwe la Msingi la mradi wa kuboresha Bandari ya Dar es Salaam ni muhimu sana kwa maendeleo na ustawi wa nchi yetu. Ni muhimu kwa sababu Bandari ya Dar es Salaam ni lango kuu la biashara na pia ni kitovu cha uchumi sio tu kwa nchi yetu bali pia kwa baadhi ya nchi jirani. Takwimu zinaonesha kuwa asilimia 90 ya shehena za mizigo inayoingia na kutoka hapa nchini inapita kwenye Bandari hii. Aidha, nchi takriban 6 hupitisha mizigo yao katika Bandari hii. Nchi hizo ni Burundi, DRC, Malawi, Rwanda, Uganda na Zambia. Lakini kama hiyo haitoshi, hivi majuzi tu tumeanza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge). Ufanisi na manufaa ya reli hiyo yatategemea sana utendaji kazi mzuri wa Bandari hii.
Kwa kuzingatia mambo hayo yote, ni dhahiri kuwa uboreshaji huu ni umuhimu kwa nchi yetu pamoja na nchi nyingine jirani zinazotumia Bandari hii. Uboreshaji huu utaongeza shehena ya mizigo inayopita katika Bandari hii na hivyo kuipatia Serikali yetu mapato mengi kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na pia kuboresha huduma za jamii. Hivyo basi, napenda nitoe pongezi nyingi kwa Wizara pamoja na Mamlaka ya Bandari Tanzania kwa kuanza kutekeleza mradi huu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama mlivyosikia hivi punde, mradi huu utatekelezwa kwa awamu mbili. Awamu ya kwanza, ambayo leo tunaweka jiwe la msingi, itahusisha uboreshaji wa Gati Na. 1-7 na Gati la kuhudumia magari (Roll-on-Roll off Berth –RORO). Awamu ya pili ya mradi huu, itahusisha kuongeza kina na kupanua lango la kuingilia Bandarini, mzunguko wa kugeuzia meli (Turning Basin), pamoja na kujenga kujenga Gati mpya Na. 12-15.
Gharama za utekelezaji wa mradi huu kwa awamu zote mbili ni Dola za Marekani milioni 421, sawa na takriban Shilingi za Tanzania bilioni 926.2. Kati ya fedha hizo, Serikali ya Tanzania itatoa Dola za Marekani 63.4; Benki ya Dunia itatoa Dola za Marekani milioni 345.2; na Serikali ya Uingereza kupitia Shirika lake la Maendeleo (DFID) itatoa Dola za Marekani milioni 12.4. Hivyo basi, napenda kurudia tena kuwashukuru washirika wetu hawa ambao wamekubali kutuunga mkono katika kutekeleza mradi huu muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama mlivyosikia, awamu ya kwanza ya mradi huu, awali, ilipangwa kutekelezwa kwa miezi 36. Lakini baada ya mashauriano yaliyofanyika, Mkandarasi, Kampuni ya China Harbour Construction kutoka China, amekubali kukamilisha mradi huu kwa kipindi cha miezi 28. Hili ni jambo jema sana. Sidhani kama kulikwa na sababu za msingi za kufanya mradi huu uchukue muda mwingi kiasi hicho kuutekeleza. Kampuni iliyopewa kandarasi ya kuutekeleza ni kubwa; lakini fedha pia zipo. Hivyo, nimefurahi kusikia muda wa kutekeleza mradi huu umepunguzwa.
Kukamilika mapema kwa mradi huu kutaiwezesha Bandari ya Dar es Salaam kupokea meli nyingi na kubwa; na hivyo kupunguza ucheleweshaji. Hii pia itasaidia Bandari yetu kushindana na Bandari nyingine katika Ukanda wetu. Kama mnavyofahamu, katika siku za hivi karibuni, zimekuwepo taarifa zakupungua mizigo katika Bandari hii. Moja ya sababu zinazochangia hali hiyo ni kwamba kina cha Bandari yetu ni kidogo. Hii inafanya meli kubwa zishindwe kuja au zilazimike kutumia muda mrefu kusubiri. Bila shaka, nyote hapa mnafahamu, katika dunia ya sasa ya ushidani, hakuna mfanyabiashara aliye tayari kupotezewa muda. Hivyo, mradi huu utakapokamilika, utaondoa tatizo la ucheweleshaji katika Bandari yetu. Kama utatokea, basi labda usababishwe na watendaji wetu, ambao ningependa tu kusema kuwa Serikali kamwe haitawavumilia.
Lakini mbali na kuondoa tatizo la ucheleweshaji, mradi huu utakuza biashara na shughuli nyingine za kiuchumi kati yetu na nchi nyingine. Kama nilivyosema awali, Bandari hii inatumiwa na mataifa jirani takriban saba. Na mnafahamu pia kuwa nchi yetu ni mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ambazo kwa pamoja zina watu wapatao milioni 600. Hivyo, mradi huu utakapokamilika, utakuza biashara kati yetu sio tu na mataifa yanayotumia Bandari yetu bali pia na nchi zote wanachama wa EAC na SADC. Hii ni kwa sababu, Bandari ni kichocheo muhimu cha kukuza biashara miongoni mwa mataifa. Takriban asilimia 90 ya shehena ya mizigo duniani husafirishwa kwa usafiri wa majini, ambapo Bandari ni kiungo muhimu.
Ndugu Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kuweka Jiwe la Msingi la Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Upanuzi na Uboreshaji wa Bandari ya Dar es Salaam. Hivyo basi, sitapenda kuwachosha kwa hotuba ndefu sana. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, napenda nizungumze masuala manne ya mwisho.
Kwanza kabisa, napenda kuwahakikishia kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kabisa kuboresha na kuimarisha miundombinu ya usafiri hapa nchini. Mbali na kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, tunaboresha na kupanua Bandari zetu za Mtwara na Tanga na halikadhalika kwenye Maziwa Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa. Tunaendelea pia na ujenzi na ukarabati wa viwanja vya ndege na barabara. Tunafanya hivyo kwa vile tunatambua kuwa huduma na miundombinu imara ya usafiri na usafirishaji ni muhimu sio tu katika kukuza biashara bali pia katika ukuaji wa sekta nyingine za uchumi, ikiwemo kilimo, viwanda, utalii, ufugaji, uvuvi, n.k.
Suala la pili ni kwa ndugu zangu wa Mamlaka ya Bandari na Bodi yake. Nawapongeza kwa hatua mnazochukua katika kuboresha na kuongeza ufanisi wa Bandari yetu. Lakini hamna budi kuzidisha juhudi hasa katika usimamizi wa Bandari Kavu Binafsi (ICDs). Bandari hizi kavu zilianzishwa kwa makusudi ya kusaidia pale mizigo inapozidi hapa Bandarini. Lakini kwa taarifa nilizonazo ni kwamba, siku hizi hata kabla ya mizigo kujaa hapa Bandarini, inapelekwa kwenye Bandari hizo Kavu, ambako kuna dalili za ukwepaji kodi. Nimeambiwa pia kwamba mara nyingi mizigo inayopelekwa huko husemekana kuwa inasafirishwa kwenda nje lakini mingi hushushwa hapa hapa nchini. Nitoe wito kwa Mamlaka ya Bandari, Mamlaka ya Mapato pamoja na vyombo vingine husika kushughulikia suala hili la Bandari Kavu na pia ukwepaji wa kodi unaofanyika kupitia Bandari kavu hizo.
Suala la tatu, napenda kuihimiza Mamlaka ya Bandari kuimarisha ulinzi na usalama wa hapa Bandarini, hususan kuhusu mizigo inayoteremshwa. Nimearifiwa kuwa hivi majuzi vimeshushwa vichwa vya treni vipatavyo 15 lakini mpaka sasa havijulikani mmiliki wake. Shirika la Reli limevikana. Sasa mimi najiuliza inawezekanaje vichwa vya treni viletwe na kushushwa hapa bila kufahamika mmiliki wake. Na kama hilo limewezekana, je haitawezekana pia kwa watu wenye nia mbaya na nchi yetu kuleta vitu vyenye kuhatarisha usalama wetu? Hivyo basi, niwaombe Mamlaka ya Bandari kuimarisha usalama wa Bandari yetu. Na kuhusu tukio hili la vichwa vya treni, niviombe vyombo vya dola kulichunguza ili kuweza kumbaini mmiliki wake.
Suala la nne na la mwisho ni kuhusu wana-siasa wenzangu, ambao wamekuwa wakiibuka kuzungumzia mambo wasiofahamu undani wake. Mathalan, hivi karibuni kuna wanasiasa wamejitokeza kujaribu kuwatetea watu wanaoshikiliwa kwa makosa ya kuhatarisha amani na usalama wa taifa letu. Nawasihi wanasiasa wa namna hiyo kuacha kutafuta sifa na umaarufu usio na tija. Ninyi ndugu zangu hapa nyote ni mashahidi kuwa katika muda mfupi uliopita, nchi yetu imewapoteza askari pamoja na wananchi wasio na hatia zaidi ya 30. Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba wanasiasa hao hawakuwahi kulaani na kukemea mauaji hayo; lakini badala yake wanaibuka kuwatetea watu ambao inaaminika kuwa wanahusika na vitendo hivyo vya mauaji. Hii inatia mashaka kuwa huenda hata wanasiasa hao pia wanahusika, hasa kwa kuzingatia kuwa ukiondoa askari, walengwa wa mauji hayo ni watu kutoka chama kimoja tu. Nitoe wito kwa wanasiasa wenzangu tuchunge ndimi na kauli zetu. Amani ya nchi yetu ni muhimu sana. Tusiichezee. Maendeleo haya tunayoyaona na kuyatamani leo kamwe hayawezi kupatikana kama amani itapotea. Hivyo, tuiache Serikali itekeleze majukumu yake. Kinyume na hapo, hatutawavumilia wanasiasa wa namna hiyo. Nilichaguliwa kuwa Rais wa Tanzania, na hivyo nawajibika kulinda amani na usalama wa nchi yetu kwa nguvu zangu zote. Naviomba vya ulinzi na usalama visiwaogope au kuwaonea aibu wanasiasa wa namna hiyo. Lakini zaidi, nawaomba Watanzania wote, bila kujali tofauti zetu za dini, kabila au vyama, kuilinda amani yetu na pia kuweka mbele maslahi ya taifa letu.
Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote, lakini hasa Wabunge wa Kamati za Miundombinu na Bajeti kwa kuiunga mkono Serikali. Upauzi na uboreshaji wa Bandari hii umezungumzwa kwa muda mrefu, hata hivyo, utekelezaji wake ulikuwa ukikwama kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo ukosefu wa fedha. Lakini baada ya Kamati hizi mbili kuupitisha mradi huu pamoja na bajeti yake, sasa tunautekeleza. Nazipongeza sana Kamati hizi mbili kwa uamuzi wenu huo wa kijasiri.
Naomba pia mniruhusu kuwashukuru tena washirika wetu katika mradi huu kwa kutuunga mkono. Aidha, nawashukuru Mabalozi wote mliojitokeza kuhudhuria shughuli. Hii inadhihirisha kuwa mnatambua umuhimu wa mradi huu. Tunawashukuru sana na napenda niwaahidi kuwa tutaendelea kushirikiana nanyi kwa karibu.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru tena viongozi wa Wizara pamoja na Mamlaka ya Bandari kwa kunialika kwenye tukio hili. Aidha, nawapongezeni kwa kazi nzuri mnayoifanya. Endeleeni kujituma. Ongezeni mapambano dhidi ya rushwa. Vitendo vya rushwa na wizi viwe mwiko katika Bandari. Zaidi ya hapo zingatieni muda. Msiwacheleweshe wateja wenu. Mkiyafanya hayo, nina imani kuwa Bandari hii itatoa huduma bora na kuchangia maendeleo ya nchi yetu; na hata maslahi ya wafanyakazi wake pia yataboreshwa.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza shughuli iliyonileta ya kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Kuboresha Bandari ya Dar es Salaam.
Mungu Ibariki Bandari ya Dar es Salaam!
Mungu Zibariki Bandari Zetu Zote!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Aug 23, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE SHEREHE ZA UZINDUZI WA MFUMO WA KUKUSANYA MAPATO KWA NJIA YA...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania pamoja na Serikali ya Zanzibar mliopo;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Watendaji wa Makampuni mbalimbali mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, napenda niungane na walionitangulia kuzungumza katika kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa hivi leo. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa Mawaziri, Prof. Mbarawa na Dkt. Mpango, kwa kunialika ili nami nishiriki katika tukio hili muhimu kwa nchi yetu. Ahsante sana.
Vilevile, napenda nitumie fursa hii niwashukuru wageni wote waalikwa na wananchi kwa ujumla kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kwenye tukio hili. Hakuna shaka, uwepo wenu mahali hapa leo ni uthibitisho tosha kwamba mnatambua umuhimu wa tukio hili kwa ustawi na maendeleo ya nchi yetu.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Napenda nikiri kuwa leo nina furaha sana. Furaha yangu inatokana na ukweli kwamba muda mfupi tu uliopita, nimetoka kutembelea Kituo cha Kutunza Taarifa au Kumbukumbu (Data Centre) hapa Kijitonyama. Nimejionea miundombinu ya Kituo hicho na kupata maelezo ya namna kinavyofanya kazi. Kwa hakika nimeridhika na kile nilichokiona na kukisia kutoka kwa wataalam. Nimeshuhudia miundombinu na mitambo ya kisasa na nimefarijika zaidi kusikia kuwa Kituo hiki kina ubora wa kimataifa na ni cha pili kwa ukubwa kwa nchi za Bara la Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara. Cha kwanza kilichopo nchini Afrika Kusini. Haya ni mafanikio makubwa kwa nchi yetu.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza sana wote walioshiriki katika kubuni na kufanikisha ujenzi wa kituo hiki, ambacho ni muhimu kwa ustawi na maendeleo ya nchi yetu. Kama mnavyofahamu, Serikali yetu iliamua kujenga Kituo hiki kwa makusudi makubwa mawili. Kusudi la kwanza ni kuhakikisha usalama wa taarifa za taasisi za Serikali na Makampuni binafsi yanayoendesha shughuli zake hapa nchini. Taasisi za Serikali na Makampuni binafsi yatakayotunza taarifa zao katika Kituo hiki yatakuwa na uhakika wa usalama wa taarifa zao, endapo ajali au uhalifu ukitokea kwenye taasisi au makampuni yao.
Kusudi la pili ambalo limeifanya Serikali ijenge kituo hiki ni dhamira yake ya kutaka kuimarisha na kukuza sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano nchini. Kama mnavyofahamu, sekta hii inakua kwa kasi na ni kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi sio tu hapa nchini bali duniani kote. Nchi zote ambazo zimepiga hatua kubwa na kupata mafanikio makubwa katika sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano zimejenga vituo vya kutunza taarifa (Data Centre) kama hiki. Hivyo basi, uwepo wa Kituo cha Kutunza Taarifa hapa nchini sio tu unatufanya twende sambamba na nchi zilizoendelea kwenye sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano bali pia itasaidia kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa nchi yetu. Hii ni kwa sababu, sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano ni mhimili muhimu wa maendeleo kwenye sekta zote, ikiwemo viwanda, utalii, ujenzi, elimu, afya, kilimo, uvuvi, ufugaji, n.k.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Katika maelezo niliyopata leo nimeambiwa kuwa Kituo cha Kutunza Kumbukumbu kilianza kazi tangu mwezi Oktoba 2016. Hata hivyo, mwitikio wa taasisi za Serikali na Makampuni binafsi kujiunga sio mkubwa sana. Ni taasisi na makampuni machache tu ndiyo tayari yamejiunga. Sio zaidi ya taasisi na makampuni kumi (10). Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuhimiza taasisi za Serikali na makampuni binafsi kujiunga na Kituo kilichojengwa na Serikali. Kama nilivyosema hapo awali, Kituo chetu ni kikubwa sana. Kina uwezo wa kutunza kumbukumbu sio tu za taasisi na makampuni yote ya hapa nchini bali pia taasisi na makampuni ya nje ya nchi. Ubora wake ni wa daraja la juu kabisa (Tier Three). Hivyo, nazikaribisha taasisi na makampuni ya ndani na nje ya nchi kutunza kumbukumbu/taarifa zao kwenye kituo hiki.
Ninazo taarifa kuwa, licha ya Serikali kuingia gharama kubwa ya kujenga Kituo kikubwa cha Kutunza Taarifa, zipo taasisi za Serikali ambazo zinaendelea na taratibu za kujenga vituo vyao wenyewe. Sasa naziagiza taasisi zote za Serikali zenye nia ya kujenga vituo vyao vya kutunza kumbukumbu kuachana na mipango hiyo. Tunzeni taarifa zenu kwenye Kituo hiki ambacho kimejengwa na Serikali. Nasema hivyo kwa sababu nina uhakika, hata kama mkijenga, vituo hivyo havitakuwa na ubora kama wa kituo hiki.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jambo la pili lililonifanya leo nifurahi ni kwamba, mbali na kushuhudia Kituo hiki cha Kutunza Kumbukumbu, muda mfupi ujao nitazindua Mfumo wa Ukusanyaji Mapato ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) na Ushuru wa Bidhaa (Excise Duty) kwa njia ya kielektroniki, yaani Electronic Revenue Collection System (e-RCS). Mfumo huu nao ni muhimu kwa ustawi na maendeleo ya nchi yetu. Kama mnavyofahamu, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, shughuli nyingi za kiuchumi na kifedha kwa sasa zinafanyika kwa njia ya kielektroniki. Mathalan, makampuni ya simu, mabenki, televisheni pamoja na taasisi za serikali na makampuni binafsi yamekuwa yakifanya miamala mingi ya kifedha kwa njia ya kielektroniki.
Licha ya maendeleo hayo, ni bahati mbaya kuwa kwa muda mrefu, nchi yetu imekuwa haina mfumo mahsusi wa kutambua miamala inayofanyika na kukokotoa kodi. Mara nyingi, tumekuwa tukikusanya kodi kwa kukadiria au wakati mwingine imetubidi tupokee kile tunachoambiwa au kuletewa na makampuni husika. Kwa maneno mengine, tulitegemea zaidi uaminifu wa walipa kodi na wakadiria kodi wetu. Lakini sasa tumepata mwarobaini. Mfumo huu utawezesha kuona miamala yote kadri inavyofanyika. Hii itawezesha Serikali kukusanya kodi inayostahili tena kwa wakati. Mualama ukifanyika tu, muda huo Serikali inapata kodi yake. Zaidi ya hapo, Mfumo huu utapunguza kama sio kuondoa kabisa malalamiko ya wafanyabiashara wetu kuhusu kubambikiwa kodi kubwa na wakadiriaji.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kamishna Mkuu wa TRA, ameeleza hivi punde kuwa Mfumo huu umepangwa kutekelezwa kwa awamu tatu. Awamu ya kwanza inahusisha ujenzi wa mfumo na kuunganisha Makampuni nane (8) ya Mawasiliano ya simu yaliyopo nchini ambayo ni Vodacom, Tigo, Zantel, TTCL, Halotel, Smart, Smile na Airtel. Awamu ya pili itahusu kuunganisha mfumo huu na mifumo ya taasisi za kifedha na Kibenki. Na awamu ya tatu itahusisha uunganishaji wa mfumo wa e-RCS na mifumo yote ya taasisi na makampuni yanayotoa huduma za malipo kwa njia ya kielektroniki.
Ametueleza pia kuwa katika awamu ya kwanza ya utekelezaji, Makampuni matatu (3) ya Halotel, TTCL na Smart tayari yameunganishwa kwenye mfumo; na kampuni ya Smile ipo katika hatua za mwisho kuunganishwa. Nayapongeza makampuni hayo. Aidha, nayahimiza makampuni mengine ya simu kujiunga kwenye mfumo huo ili kuiwezesha Serikali kukusanya kodi yake kama inavyostahili. Nimefurahi leo katika shughuli hii tunao watendaji wakuu wa makampuni karibu yote ya simu, mabenki pamoja na taasisi nyingine. Ni imani yangu kuwa wameusikia na wataufanyia kazi wito wangu wa kujiunga na mfumo huu wa ukusanyaji mapato kwa njia ya kielektroniki.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyosema hapo awali, Serikali imeamua kutengeneza Mfumo huu kwa ajili ya kuongeza ukusanyaji mapato ili kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo hapa nchini. Baadhi yenu mtakumbuka kuwa, takriban miezi miwili iliyopita, nchi yetu ilipata bahati ya kutembelewa na Waziri Mkuu wa Ethiopia. Katika mazungumzo yetu, alinieleza kuwa nchini mwake kuna Kampuni moja tu la simu, Ethio Telecom, ambalo linamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100. Mwaka jana Shirika hilo lilipata mapato ya takriban Dola za Marekani bilioni 1.5, na mwaka huu linatarajiwa kukusanya takriban Dola bilioni 2. Makusanyo hayo makubwa ndio yamechangia kuiwezesha Serikali ya Ethiopia kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa reli.
Sisi pia, hapo zamani, tulikuwa na shirika moja tu la simu la TTCL. Nimeambiwa kuwa mwaka 1992, Shirika hilo lilitoa gawio lake kwa Serikali kiasi cha takriban shilingi bilioni moja. Baadaye, kutokana na dhamira nzuri ya Serikali ya kutaka kuliongezea ufanisi Shirika hili, iliamuliwa libinafsishwe. Jambo la kusikitisha ni kwamba, baada ya kubinafsishwa, shirika hilo likaanza kujiendesha kwa hasara na halikuwahi kutoa gawio kwa Serikali hadi ikailazimu mwaka jana tulichukue tena. Kwa sasa nchi yetu ina mashirika mengi ya simu, lakini kiasi cha kodi tunachopata, bado ni kidogo. Ni kutokana na ukweli huo, tumeamua kutengeneza mfumo huu wa ukusanyaji mapato kwa njia ya kieletroniki.
Hivyo basi, napenda kurudia tena wito wangu kwa makampuni ya simu nchini kujiunga na mfumo huu. Sambamba na hilo, nayakumbusha na kuyahimiza tena Makampuni ya Simu kujisajili kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam, ambako nako nimearifiwa kuwa kuna kusuasua katika kujisajili. Fanyeni hivyo kwa hiari. Lakini mkiendelea kukaidi, hatutasita kuchukua hatua kali. Na katika hili naviagiza vyombo vyote husika, hususan TCRA, kuchukua hatua kali dhidi ya kampuni ya simu itakayoshindwa kujiunga na mfumo huu wa kodi wa kieletroniki na pia kujisajili kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam; ikiwezekana kampuni hiyo ifungiwe kabisa kuendesha shughuli zake hapa nchini. Nakuomba Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mawaziri husika kusimamia suala hili.
Nasisitiza jambo hili sio kwa sababu tunayachukia makampuni ya simu, bali kwa sababu tunataka shughuli za makampuni haya ziwanufaishe pia Watanzania na nchi yetu kwa ujumla. Wengi wenu hapa mnafahamu kuwa nchi yetu imekuwa ikipoteza mapato mengi ya kodi. Sio tu kwenye makampuni haya ya simu bali pia kwenye shughuli za uchimbaji madini pamoja na shughuli nyingine. Mathalan, hivi sasa tumekuwa tukihangaishana na wamachinga katika kulipa kodi. Lakini naamini kama tungeamua kuwarasimisha wamachinga kwa kuwatengenezea vitambulisho ambavyo watavilipia kwa kiasi kidogo cha fedha, Serikali ingepata mapato mengi. Hata kwenye kodi ya majengo ni hivyo hivyo. Kama kodi ingekuwa ndogo, watu wengi wangeimudu na kuilipa kwa hiari na hivyo kuipatia Serikali mapato makubwa.
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimeeleza mengi niliyotaka kueleza. Hivyo, napenda niishie hapa. Lakini kabla sijahitimisha hotuba yangu, napenda nitumie fursa hii kutoa pongezi zangu nyingi kwa taasisi zote zilizoshiriki katika kubuni na kutengeza Kituo chetu cha Kutunzia Kumbukumbu pamoja na Mfumo wa Ukusanyaji Kodi na Mapato kwa Njia ya Kieletroniki. Nimefarijika sana kusikia kuwa Mfumo huu Ukusanyaji wa Mapato umetengenezwa na sisi Watanzania wenyewe tena kwa gharama nafuu sana. Hili na jambo zuri na huu ni uthibitisho mwingine kuwa sisi Watanzania, tukiamua, tunaweza.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kufanya uzinduzi rasmi wa Mfumo wa Ukusanyaji Kodi na Mapato kwa njia ya kielektroniki.
Mungu Ibariki Tanzania!
Mugu Wabariki Watanzania!
“Ahsanteni Sana kwa Kunisikiliza”

- Aug 23, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA MAONESHO YA 41 YA BIASHARA YA KIMATAIFA YA DAR ES SA...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Charles Mwijage (Mb),
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji;
Mheshimiwa Amina Salum Ali, Waziri wa Viwanda,
Biashara na Masoko wa Serikali ya Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa
Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza
la Wawakilishi;
Mheshimiwa Isaya Mwita, Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam;
Mheshimiwa Mhandisi Christopher Chiza,
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TANTRADE,
Ndugu Edwin Rutageruka, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE;
Viongozi wa Ngazi Mbalimbali wa Serikali, Vyama vya Siasa
Pamoja na Dini mliopo;
Waheshimiwa Washiriki wa Maonesho;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha kufika siku hii ya leo. Aidha, napenda nitoe shukran zangu nyingi kwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mheshimiwa Mwijage, pamoja na uongozi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) kwa kunialika kuwa Mgeni Rasmi wa Maonesho haya ya 41 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar Es Salaam. Kama mnavyofahamu, hii ni mara yangu ya kwanza kuwa Mgeni Rasmi wa Maonesho haya. Mwaka jana nilikuja hapa kumsindikiza aliyekuwa Mgeni Rasmi, Mheshimiwa Rais Kagame. Hivyo basi, nawashukuru sana kwa kunipa heshima hii kubwa mwaka huu.
Kabla sijaendelea zaidi, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza waandaaji kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuboresha Maonesho haya. Tumeelezwa hivi punde kuwa idadi ya washiriki wa Maonesho haya kila mwaka inaongezeka. Mwaka huu, idadi ya makampuni ya Kitanzania yanayoshiriki ni 2,520, wakati makampuni ya nje ni 515 kutoka mataifa 30. Zaidi ya hapo, tumearifiwa kuwa Shirikisho la Maonesho ya Biashara ya Kimataifa (The Global Association of the Exhibition Industry - UFI) limeyataja Maonesho haya kuwa ni makubwa na bora zaidi katika ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati. Huu ni uthibitisho tosha kuwa maonesho haya ni makubwa. Hivyo basi, napenda kwa dhati kabisa, kuwapongeza waandaaji, Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara, kwa jitihada kubwa mnazozifanya.
Mheshimiwa Waziri;
Ndugu Washiriki, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Hakuna shaka yoyote kuwa Maonesho ya Biashara ni nyenzo muhimu ya kutangaza biashara. Ni kweli kuwa katika dunia ya sasa zipo njia nyingi za kutangaza biashara, ikiwemo vyombo vya habari, mitandao ya kijamii, mabango, n.k. Hata hivyo, jambo lililo dhahiri ni kwamba maonesho ya biashara yamebaki kuwa njia kuu inayoaminika duniani kote katika kutangaza biashara. Hii ni kwa sababu Maonesho ya Biashara yana faida nyingi. Kwa ajili ya ufinyu wa muda, nitataja faida chache za Maonesho ya Biashara.
Kwanza kabisa, tofauti na njia nyingine za kutangaza biashara, Maonesho ya Biashara yanampa fursa mzalishaji wa bidhaa au mtoa huduma kukutana ana kwa ana na mteja wake. Hii humwezesha mzalishaji kupata mrejesho kuhusu namna bidhaa yake (hasa bidhaa mpya) inavyokubalika kwenye soko, mapungufu ya bidhaa hiyo na nini kinahitajika kuboreshwa. Mathalan, katika maonesho haya nina uhakika kuwa yapo makampuni yamekuja kutangaza bidhaa zao mpya. Na kupitia mrejesho watakaoupata kutoka kwa wateja wao, makampuni hayo yatafanya uamuzi wa ama kuendelea na uzalishaji wa bidhaa husika, au kuiboresha ama kuachana nayo.
Pili, Maonesho ya Biashara hutoa fursa ya kuyakutanisha makampuni mengi yanayojihusisha na uzalishaji bidhaa au utoaji huduma zinazofanana. Makampuni hayo yanaweza kuwa yanatoka mataifa tofauti au kwenye nchi moja. Hii huyawezesha makampuni hayo kujifunza kutoka makampuni mengine kwa kubadilishana uzoefu, utaalamu na ujuzi wa kutengeneza bidhaa husika kulingana na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Sababu ya tatu, ambayo kimsingi inaendana kwa karibu na sababu mbili za mwanzo, ni kwamba Maonesho ya Biashara yanarahisha kuanzisha uhusiano wa kibiashara kati ya makampuni au kati ya kampuni na wateja wake. Mathalan, katika Maonesho haya nina imani kubwa kuwa makubaliano mbalimbali ya kibiashara au mauziano ya bidhaa yatafikiwa kati ya makampuni au makampuni na wateja wao. Kama isingekuwa Maonesho haya, huenda ingechukua muda mrefu na gharama kubwa kuweza kufikia makubaliano hayo.
Kutokana na sababu hizi na nyingine nyingi ambazo sikuzitaja, napenda kurudia tena kutoa pongezi kwa waandaaji wa maonesho haya. Lakini zaidi, napenda kuyashukuru na kuyapongeza makampuni ya ndani na ya nje ambayo yamejitokeza kushiriki kwenye Maonesho yetu ya 41 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam.
Wageni Waalikwa, Ndugu Washiriki, Mabibi na Mabwana;
Maonesho haya, mbali na kutumika kutangaza bidhaa, yanafungua milango kwa washiriki, hususan kutoka nje, kuweza kufahamu fursa nyingine za kiuchumi zilizo hapa nchini. Na katika hili, ningependa kusema kuwa nchi yetu ina fursa nyingi za kiuchumi. Hivyo basi, nawakaribisha washiriki wa ndani na pia kutoka nje kutumia Maonesho haya kutafuta fursa nyingine za kiuchumi, ikiwemo kuwekeza kwenye sekta ya viwanda ili kwenda sambamba na kaulimbiu ya Maonesho haya inayosema “Kukuza Biashara kwa Maendeleo ya Viwanda”.
Kama mnavyofahamu, hivi sasa tumejipanga kuhakikisha nchi yetu inakuwa ya uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025. Ili kufikia azma hiyo, tumeanza kuchukua hatua za kuondoa vikwazo na kero mbalimbali zilizokuwa zikiwakwamisha wawekezaji kuwekeza kwenye sekta hii ya viwanda hapa nchini. Tumeondoa baadhi ya kodi. Na hivi sasa tumeweka mkazo katika kushughulikia tatizo la uhaba wa umeme. Hakuna shaka, ukosefu wa umeme wa uhakika ndio kikwazo kikubwa kinachokwamisha ustawi wa viwanda hapa nchini. Hivi sasa tunazalisha umeme usiozidi Megawati 1,500. Hiki ni kiwango kidogo sana kwa nchi yenye nia ya kujenga uchumi wa viwanda.
Hivyo basi, tumeamua kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme. Tunapanua mradi wa umeme wa Kinyerezi I ili uweze kuzalisha Megawati 325 kutoka Megawati 150 za sasa. Aidha, tunatekeleza mradi wa Kinyerezi II, ambao utazalisha Megawati 240. Aidha, tumeanza maandalizi ya kutekeleza miradi ya Kinyerezi III na IV, ambayo kwa pamoja inatarajiwa kuzalisha Megawati 600. Miradi hii yote ya Kinyerezi itazalisha umeme kwa kutumia gesi asilia.
Sambamba na miradi hiyo, tumeanza maandalizi ya kutekeleza mradi mkubwa wa umeme wa maji wa Stiglier’s Gorge, ambao umekuwa katika maandishi tangu enzi za Baba wa Taifa. Mradi huu utazalisha takriban Megawati 2,100. Nafahamu baadhi ya watu wameanza kuupinga mradi huu kwa kisingizio cha kuharibu mazingira na makazi ya viumbe hai kwenye Hifadhi ya Selou. Napenda niwahakikishie mradi huu tutautekeleza. Sababu zinazotolewa na wanaopinga mradi huu hazina nguvu. Mradi huu tumepanga utatekelezwa katika eneo lisilozidi asilimia 3 ya eneo zima la Hifadhi ya Selou. Hivyo, hoja kwamba utaharibu mazingiza na makazi ya viumbe hazina mashiko. Badala yake, mbali na kuzalisha umeme, mradi huu utawanufaisha viumbe hai kwenye eneo hilo na pia kukuza sekta za uvuvi na kilimo. Hivyo basi, napenda kurudia kusema kuwa mradi huu tutautekeleza. Na nina imani washirika wetu wa maendeleo watatuunga mkono.
Wageni Waalikwa, Ndugu Washiriki, Mabibi na Mabwana;
Katika hotuba yake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania, Mheshimiwa Mhandisi Chiza, ameeleza kuwa Mamlaka ina mpango wa kufanya maboresho makubwa katika viwanja hivi. Amesema kuwa mmejipanga kubomoa mabanda yaliyopo ili kujenga mapya pamoja na kujenga hoteli na kumbi za mikutano za kisasa.
Jambo hili ni jema. Lakini mimi nina mawazo tofauti kidogo. Kwa mtazamo wangu, mimi naona badala ya ninyi kutumia fedha kujenga majengo haya, mngeweza kuingia makubaliano ya aina fulani na makampuni au taasisi zinazoonesha bidhaa hapa kujenga na kuboresha majengo yao. Na ninyi fedha zenu mzitumie kwenye shughuli nyingine, angalau kujenga kiwanda cha mfano ili kuitikia wito wa Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga Tanzania ya Viwanda. Naamini, kiwanda kitakuwa na faida nyingi kuliko majengo mliyopanga kuyajenga kwenye viwanja hivi. Hii ni kwa sababu, kupitia kiwanda hicho, watanzania wengi zaidi watapata ajira za kudumu lakini pia Serikali itapata kodi hasa katika kipindi hiki ambacho Watanzania wengi wameanza kuhamasika kulipa kodi. Hayo ndio mawazo yangu, hivyo, kama mtaona yanafaa, mnaweza kuyatafakari.
Waheshimiwa Mawaziri;
Ndugu Washiriki, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kufungua Maonesho ya 41 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam. Kwa sababu hiyo, sitapenda kuwachosha kwa hotuba ndefu. Lakini kabla sijahitimisha, napenda kurudia tena kuwashukuru waandaaji kwa kunikaribisha. Aidha, nawapongeza kwa kuendelea kuyaboresha Maonesho haya. Lakini nitoe kwenu, kama mtaona inafaa, muangalie uwezekano wa kuyaongezea muda kidogo Maonesho haya. Nasema hivyo kwa sababu, mara nyingi, Maonesho haya yamekuwa yakifungwa wakati ambapo yanaanza kuchangamka na wananchi wanaanza kuhamasika kuhudhuria. Hivyo, kama itawapendeza, mnaweza kuongeza hata siku tano hivi.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza washiriki wote. Binafsi ningetamani sana kutembelea mabanda yote lakini kwa sababu ya muda, itaniwia vigumu. Itoshe tu kusema kuwa nawashukuru na kuwapongeza sana kwa kushiriki kwenu kwenye Maonesho haya. Kwa washiriki wa Tanzania, nawasihi sana myatumie vizuri Maonesho haya katika kujifunza na kuboresha bidhaa na huduma mnazozalisha. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Mabalozi mnaowakilisha nchi mbalimbali hapa nchini kwa kuja kushiriki nasi katika shughuli hii ya Ufunguzi wa Maonesho ya 41 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam. Tunaahidi tutaendelea kushirikiana nanyi katika masuala mbalimbali.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutamka kuwa Maonyesho ya 41 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yamefunguliwa rasmi.
Mungu Yabariki Maonesho Yetu ya Saba Saba!
Mungu Wabariki Washiriki wa Maonesho Haya!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Aug 23, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA YA KUKABIDHI UENYEKITI WA JUMUIYA YA AFRIKA KWENYE MKUTANO WA 18 WA WAKUU...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda;
Mheshimiwa William Ruto, Makamu Rais wa Jamhuri ya Kenya;
Mheshimiwa Joseph Butore, Makamu wa Pili
wa Rais wa Jamhuri ya Burundi;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Waheshimiwa Wawakilishi wa Marais wa Rwanda na Sudan Kusini;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo hapa;
Mheshimiwa Spika wa Bunge la Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Jaji Rais wa Mahakama ya Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Balozi Liberat Mfumukeko, Katibu Mkuu wa Jumuiya;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu Wastaafu wa Jumuiya;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Wageni Wote Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Naomba mniruhusu nianze kwa kuwakaribisha washiriki wote katika Mkutano huu 18 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Lakini kwa namna ya pekee kabisa, napenda niwakaribishe Wakuu wa Nchi wenzangu pamoja na viongozi mbalimbali mnaoziwakilisha nchi zenu kwenye Mkutano huu hapa Tanzania, hususan katika Jiji letu la Dar es Salaam. Nikiwa Rais, nafahamu mnayo majukumu mengi, hata hivyo, mmeweza kutenga muda wa kuja kuhudhuria Mkutano huu muhimu. Hii ni ishara ya dhamira kubwa tuliyonayo sisi viongozi wa Jumuiya katika kutekeleza ajenda yetu ya utangamano.
Napenda pia kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu nyingi kwa Baraza la Mawaziri pamoja na Sekretarieti yetu ya Jumuiya, chini ya uongozi wa Balozi Liberat Mfumukeko kwa maandalizi mazuri ya Mkutano huu. Mmeturahisishia sana kazi yetu sisi viongozi. Na nina imani, kutokana na maandalizi mazuri yaliyofanyika, Mkutano huu utakuwa wa mafanikio makubwa.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Viongozi wetu, wakati wa kuanzisha Jumuiya hii, na ninafurahi Mheshimiwa Rais Museveni tupo naye hapa, walikuwa na dhamira moja kubwa. Dhamira ya kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi pamoja na utangamano wa nchi za ukanda huu. Aidha, walikuwa na dhamira ya kujenga Jumuiya imara ambayo itazifanya nchi za ukanda wetu zishiriki kikamilifu kwenye masuala ya kimataifa. Walifahamu kuwa, kutokana na udogo na uchanga wa mataifa yao, ingewawia vigumu kushindana na mataifa mengine makubwa, ambayo yameendelea.
Inatia faraja kuona kuwa, tangu kufufuliwa kwa Jumuiya yetu mwaka 2000, mafanikio mengi makubwa ambayo yanakwenda sambamba na dhamira ya waanzilishi wa Jumuiya hii, yamepatikana. Umoja na mshikamano miongoni mwa wana-Afrika Mashariki unazidi kukua. Utangamano wetu unaimarika kila kukicha na unazinufaisha nchi zetu na watu wake. Tumefanikiwa kuanzisha Umoja wa Forodha (Customs Union); hivi sasa tupo kwenye utekelezaji wa Mkataba wa Soko la Pamoja (Common Market Protocol); na hatua za kuanzisha Ushirikiano katika Masuala ya Kifedha (Monetary Union) umeanza. Jumuiya yetu nayo inazidi kuimarika na imebaki kuwa mfano wa kuigwa Barani Afrika na duniani kwa ujumla. Haya ni mafanikio makubwa na napenda niwapongeze wote walioshiriki katika kuyapata.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado tuna safari ndefu ya kufikia kule ambako waanzilishi wetu walitamani Jumuiya yetu ifike. Jitihada kubwa bado zinahitajika katika kuboresha na kuimarisha Jumuiya na Utangamano wetu. Ni dhahiri kuwa kazi ya kuimarisha Jumuiya yetu sio rahisi, lakini hatuna budi sote kushirikiana katika kuifanya. Na katika hilo, nafurahi kuuarifu Mkutano huu kuwa, katika kipindi ambacho Tanzania ilipewa jukumu la kuongoza Jumuiya yetu, jitihada kubwa zimefanyika za kuboresha na kuimarisha Jumuiya yetu. Natambua muda mfupi ujao, Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri atawasilisha Ripoti ambayo imeeleza kwa kirefu mambo yaliyofanyika, lakini naomba nitaje machache:
Kwanza, ni kuhusu utekelezaji wa ajenga ya utangamano: Kama mnavyofahamu, utekelezaji wa Eneo Moja la Ushuru wa Forodha (Single Customs Union Territory) unaendelea vizuri. Jitihada za kushughulikia vikwazo vya biashara visivyo vya kodi (Non Tariff Barriers), zimeendelea vizuri. Katika kipindi chetu cha uongozi, tuliweza pia kusimamia utekelezaji wa baadhi ya masuala yanayohusu Soko la Pamoja (Common Market), ambapo baadhi ya sekta zimeanza kutekeleza, wakiwepo wanasheria na wahandisi. Kuhusu Ushirikiano wa Kifedha, tumeweza kufanikisha uandaaji wa miswada miwili ambayo ipo tayari kupelekwa kwenye Bunge letu la Afrika Mashariki kwa ajili ya kujadiliwa. Mswada wa kwanza unahusu uanzishaji wa Taasisi ya Fedha ya Jumuiya (East African Monetary Institute Bill), ambayo itakuwa taasisi ya mpito kuelekea kuanzishwa kwa Benki Kuu ya Afrika Mashariki; na mswada wa pili unahusu Tume ya Jumuiya ya Ufuatiliaji na Usimamizi (the East African Surveillance, Compliance and Enforcement Commission Bill).
Pili, Maendeleo ya Miundombinu: Kama mnavyofahamu, ujenzi wa miundombinu, hususan ya usafiri, ni nguzo muhimu katika ustawi wa ushirikiano baina ya mataifa. Hivyo basi, nafurahi kuarifu kuwa, katika kipindi chetu cha Uenyekiti, miradi kadhaa ya miundombinu ya usafiri imeweza kufikia hatua nzuri ya utekelezaji. Mradi wa ujenzi wa Barabara ya Arusha – Holili/Taveta – Voi tayari umeanza. Upembuzi wa mradi wa Barabara ya Malindi – Lunga Lunga/Tanga – Bagamoyo umekamilika na kwa sasa unasubiri fedha ili uanze kutekelezwa. Aidha, miradi ya Barabara za Lusahuga – Rusumo – Kigali na ile ya Nyakanazi – Kasulu – Rumoge – Bujumbura ipo kwenye hatua mbalimbali za usanifu. Utekelezaji wa miundombinu hiyo ya usafiri, umeenda sambamba na ujenzi wa vituo vya pamoja vya mpakani (One-Stop Border Posts). Vituo vya Mpakani 9 kati ya 15 tayari vimeanza kazi, kikiwemo Kituo cha Rusumo kwenye Mpaka wa Tanzania na Rwanda, ambacho mimi na mwezangu Rais Kagame tulikizindua mwezi Aprili mwaka jana.
Tatu, Masuala ya Amani na Usalama: Katika kipindi chetu pia, tumefanya jitihada za kutafuta ufumbuzi wa migogoro iliyopo kwenye Ukanda wetu, hususan nchini Burundi na pia Sudan Kusini, ambako Jumuiya ya IGAD inashughulikia kwa karibu. Jitihada zilizofanyika, kwa kiasi fulani, zimesaidia kupunguza uhasama miongoni mwa pande zinazopingana. Napenda kutumia fursa hii kupongeza jitihada kubwa zinazofanywa na Msuluhishi wa Mgogoro wa Burundi, Mheshimiwa Rais Museveni wa Uganda pamoja na Mpatanishi wa Mgogoro huo, Rais Mstaafu wa Tanzania, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa. Wamefanya kazi kubwa sana. Lakini niziombe pande husika kwenye migogoro niliyoitaja kuweka nyuma maslahi yao binafsi na kutanguliza mbele maslahi ya mataifa yao ili kuwezesha migogoro hiyo kumalizika kwa haraka. Wafahamu kuwa, kurejea kwa amani ya kudumu katika nchi hizo, kwa kiasi kikubwa kunawategemea wao.
Nne, Masuala ya Utawala Bora na Demokrasia: Hakuna shaka, ukanda wetu umepiga hatua kubwa katika eneo hili. Utawala Bora na masuala ya demokrasia yameimarika katika Mataifa Wanachama yote. Mathalan, mwaka huu pekee, mataifa mawili ya Kenya na Rwanda yanatarajiwa kufanya Uchaguzi Mkuu. Na napenda nitumie fursa hii, nizitakie heri nchi hizi mbili wanachama katika kutekeleza hatua hiyo muhimu. Chaguzi zifanyike kwa utulivu na amani ili tuioneshe tena dunia kuwa demokrasia imeimarika na kuota mizizi katika ukanda wetu.
Tano, Kuimarisha na kukuza mahusiano na Washirika wetu wa Maendeleo. Katika kipindi chetu cha Uenyekiti, Jumuiya yetu imesaini makubaliano ya kifedha na Serikali ya Marekani, kupitia Shirika lake la misaada la USAID; Serikali ya Ujeruma kupitia shirika lake la KfW; Umoja wa Ulaya; Benki ya Dunia pamoja na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Makubaliano hayo yana thamani ya takriban Dola za Marekani milioni 300.
Sita, Kubana Matumizi ya Jumuiya. Kwenye hotuba yangu ya kupokea Uenyekiti wa Jumuiya yetu mwezi Machi mwaka jana niliahidi kusimamia matumizi ya fedha ya Jumuiya yetu. Leo nafurahi kuripoti kuwa, katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, tumeweza kupunguza matumizi ya Jumuiya, hususan Sekretarieti, kutoka Dola za Marekani milioni 12.6 hadi kufikia Dola za Marekani milioni 9.1. Nampongeza Katibu Mkuu Dkt. Mfumukeko kwa kusimamia jambo hili vizuri. Nina matumaini makubwa kuwa Mwenyekiti Mpya naye ataendeleza suala hili la usimamizi mzuri wa rasilimali ili fedha nyingi zitumike kwenye shughuli za maendeleo.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Haya niliyoyataja ni baadhi tu ya mafanikio. Yapo mengine mengi ambayo yamepatikana. Hivyo, napenda nitumie fursa hii kuwashukuru Viongozi wenzangu kwa heshima kubwa waliyoipa Tanzania kuongoza Jumuiya yetu kwa kipindi cha takriba miaka miwili na ushee. Kama mnavyofahamu, awali tulipewa jukumu hili mwezi Februari 2015, lakini mwezi Machi 2016 tuliongezewa tena mwaka mmoja kuendelea kuongoza Jumuiya hii. Kwa maana hiyo, tumeongoza kwa miaka miwili na zaidi. Hii ilikuwa ni heshima kubwa sana kwa nchi yetu. Lakini napenda niwashukuru Waheshimiwa Viongozi kwa imani kubwa mliyoionesha kwangu mimi binafsi. Kama mtakumbuka, mwaka jana wakati nakabidhiwa jukumu la kuwa Mwenyekiti, nilikuwa na kama miezi minne tu tangu niingie madarakani. Lakini licha ya uchanga wangu, mliniamini. Nawashukuru sana.
Napenda pia nitumie fursa hii kuwashukuru kwa ushirikiano na msaada mkubwa mliutoa kwangu mimi binafsi na kwa nchi yangu katika kipindi chote tulichokuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hii. Hivi punde, nimetoka kueleza baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika kipindi chetu cha Uenyekiti. Mafanikio hayo yasingepatikana kama msingetupa ushirikiano wa kutosha. Hivyo, nawashukuru sana kwa ushirikiano wenu mkubwa mliotupa.
Waheshimiwa Wakuu wa Nchi;
Waheshimiwa Viongozi mnaowakilisha nchi zetu;
Waheshimiwa Mawaziri;
Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Jumuiya;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu kubwa leo lilikuwa kuwakaribisha na kukabidhi majukumu ya Uenyekiti wa Jumuiya kwa Mzee wetu, Mheshimiwa Rais Yoweri Museveni wa Uganda. Tayari nimewakaribisha. Sasa nimebakiza jukumu moja la kukabidhi madaraka. Lakini kabla ya kutekeleza jukumu hilo la pili, naomba mniruhusu nitoe shukrani zangu nyingi kwa Katibu Mkuu wa Jumuiya Balozi Mfumukeko, Naibu wake Dkt. Enos Bukuku, wafanyakazi wote wa Jumuiya pamoja na washirika wetu mbalimbali wa maendeleo kwa ushirikiano mkubwa walionipa katika kipindi chote cha Uenyekiti. Niwaombe tu ushirikiano huo muuendeleze pia kwa Mwenyekiti mpya.
Natambua Naibu Katibu Mkuu Dkt. Bukuku anamaliza muda wa kutumikia Jumuiya yetu hivi karibuni. Hivyo basi, napenda nitumie fursa hii kumshukuru kwa mchango aliotoa katika Jumuiya yetu; na namtakia kila la heri mahali popote atakapokuwa baada ya kumaliza majukumu haya. Niruhusuni pia nitangulize pongezi zangu kwa Naibu Katibu Mkuu Mteule na Jaji Mteule wa Mahakama ya Jumuiya kutoka Sudan Kusini. Nina imani Mkutano huu utawapitisha, hivyo, napenda niwatakie kila la heri wakati watakapoanza kutekeleza majukumu yao mapya.
Mabibi na Mabwana, kwa hakika, ilikuwa ni heshima kubwa kwangu mimi binafsi na kwa nchi yangu kushika wadhifa wa Uenyekiti wa Jumuiya hii, lakini sasa wakati umewadia wa kukabidhi madaraka hayo kwa Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda. Kama mnavyofahamu, Mheshimiwa Rais Museveni ni mzoefu katika masuala ya Jumuiya yetu. Yeye ni miongoni mwa watu walioshiriki kikamilifu katika kuifufua Jumuiya yetu. Hivyo basi, nina matumaini makubwa kuwa, kutokana na uzoefu wake mkubwa, Jumuiya yetu itazidi kuimarika wakati wa uongozi. Na hata yale masuala ambayo hatukuweza kuyamaliza wakati wa uongozi wetu, hususan suala la migogoro ya Burundi na Sudan Kusini pamoja na Mkataba wa Ubia wa Kiuchumi kati ya Jumuiya yetu na Umoja wa Ulaya, yatapata ufumbuzi. Napenda nihitimishe kwa kuahidi kuwa Tanzania itatoa ushirikiano wa kutosha kwa Mwenyekiti mpya ili hatimaye tuweze kufikia malengo ya kuanzishwa kwa Jumuiya hii.
Mungu Ibariki Jumuiya Yetu!
Mungu Ibariki Afrika!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Aug 23, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UWEKAJI JIWE LA MSINGI LA MRADI WA BOMBA LA MAFUTA KUTOKA HOI...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Uganda;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tannzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Kirunda Kivejinja,
Naibu Waziri Mkuu wa Uganda;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge la Tanzania;
Mheshimiwa Abdulrahaman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM;
Waheshimiwa Spika Mstaafu na Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania,
Mama Anna Makinda na Mzee Othman Chande;
Waheshimiwa Mawaziri kutoka Tanzania na Uganda;
Mheshimiwa Martin Shigela, Mkuu wa Mkoa wa Tanga;
Wawakilishi wa Makampuni ya Wawekezaji wa Mradi huu;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu na Manaibu mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi
wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa mliopo;
Viongozi wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Viongozi Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni Waalikwa, Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kushuhudia tukio hili muhimu katika historia ya uhusiano wa Tanzania na Uganda. Aidha, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda nimkaribishe Mheshimiwa Rais Yoweri Kaguta Museveni pamoja na ujumbe wake hapa Chongoleani. Namshukuru sana kwa kukubali kushiriki nasi katika hafla hii ya kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Bomba wa Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi hapa Tanga.
Hii ni mara yangu ya kwanza kuja Tanga tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu. Hivyo basi, kabla sijazungumzia tukio lililotuleta hapa, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wana-Tanga kwa kunichagua. Binafsi, sina cha kuwalipa zaidi ya kuwaahidi kuwa mimi pamoja na wenzangu Serikalini tutawatumikia kwa bidii na kamwe hatutawaangusha.
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Mkoa wa Tanga una historia ndefu na umetoa mchango mkubwa kwa nchi yetu. Enzi za kupigania uhuru, mwaka 1958, Baba wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kabla hajaenda Tabora kwenye Mkutano Mkuu wa TANU, ambao uligubikwa na mgawanyiko, alikuja Tanga. Akiwa Tanga, alikutana na wazee na kupanga nao mikakati ya kudhibiti mgawanyiko uliokuwepo, ambao ulitokana na uamuzi wa Serikali ya Kikoloni kuanzisha utaratibu wa kura tatu. Baada ya kupanga mikakati, Wazee wa Tanga walimsomea dua ndipo akaelekea Tabora kwenye Mkutano, ambao ulihitimishwa kwa kupitisha Azimio la Tabora, maarufu kama “Uamuzi wa Busara”. Azimio hili lilisaidia sana kuharakisha kupatikana kwa uhuru wa nchi yetu.
Lakini mbali na kutoa mchango huo mkubwa kwa nchi yetu, Mheshimiwa Rais Museveni ameeleza hivi punde kuwa silaha zake za kwanza wakati akielekea Uganda kuanzisha mapambano, alizipitishia huku Tanga pale Horohoro. Huu ni uthibitisho kuwa Mkoa huu sio tu umetoa mchango kwa nchi yetu bali pia kwa nchi nyingine. Na mimi naamini hata jina la Tanganyika huenda lilitokea huku Tanga.
Ni kutokana na sababu hizo zote, nimefurahi sana leo kuwepo hapa kushuhudia uwekaji wa Jiwe la Msingi la Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga. Kama ambavyo mmesikia, Mradi huu ni mkubwa na wa kihistoria kwa mataifa yetu mawili. Bomba litakalojengwa litakuwa na urefu wa kilometa kilometa 1445, na litakuwa bomba refu zaidi duniani linalotumia teknolojia ya kupasha joto (longest heated pipeline in the world). Tumesikia pia kuwa mradi huu utagharimu Dola za Marekani bilioni 3.5, sawa na takriban Shilingi za Tanzania trilioni 8. Hiki ni kiasi kikubwa sana cha fedha. Hivyo basi, natoa pongezi nyingi sana kwenu wana-Tanga, Watanzania wenzangu, ndugu zetu wa Uganda pamoja na wana-Jumuiya Afrika Mashariki wote kwa kuanza kutekeleza mradi huu mkubwa.
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Leo tupo hapa kuweka Jiwe la Msingi la Mradi huu. Lakini niwe mkweli, hatua hii haikufikiwa kirahisi. Tulikumbana na changamoto nyingi. Walijitokeza watu wengi tu waliojaribu kuzuia Bomba hili kujengwa upande wa Tanzania. Na hata majadiliano hayakuwa mepesi. Kuna nyakati ilitulazimu mimi na mwenzangu Mheshimiwa Rais Museveni kuingilia kati. Na napenda kutumia fursa hii kusema hapa hadharani kuwa Mheshimiwa Rais Museveni ni rafiki wa kweli wa Watanzania. Licha ya baadhi ya watu kumshawishi Bomba hili lisijengwe Tanzania, tulishirikiana naye kwa karibu katika kuwahimiza watendaji wetu kuendelea na majadiliano hadi hatimaye tukaweza kufikia makubaliano ya kujenga Bomba hili upande wa Tanzania.
Hivyo basi, namshukuru sana Mheshimiwa Rais Museveni, Serikali pamoja na wananchi wa Uganda kwa kukubali Bomba hili kujengwa Tanzania. Aidha, nawashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri, watendaji na wataalam wa Serikali zote mbili ambao walishiriki na kufanikisha majadiliano yetu. Napenda kuwahakikishia ndugu zetu wa Uganda pamoja na wawekezaji kuwa hamjafanya makosa kuichagua Tanzania. Mbali na amani na usalama tulionao pamoja na mazingira mazuri kwa ajili ya kusafirisha mafuta, sisi tuna uzoefu katika kutekeleza, kusimamia na kuendesha miradi kama hii. Tunayo mabomba makubwa ya kusafirisha mafuta na gesi. Mwaka 1968 tulishirikiana na wenzetu wa Zambia kujenga na kukamilisha ujenzi wake Bomba la Mafuta lenye urefu wa kilometa 1,710 kutoka Dar es Salaam hadi Ndola. Na hivi karibuni tumejenga mabomba mengine ya kusafirisha gesi asilia kutoka Songo Songo na Mnazi Bay, kusini mwa nchi yetu, kwenda Dar es Salaam. Huu ni uthibitisho tosha kuwa tuna uzoefu wa kutosha kwenye miradi kama hii.
Ndugu Watanzania wenzangu,
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Katika kuhakikisha kuwa mradi huu unakuja Tanzania, ilitulazimu kujitolea baadhi ya mambo, ikiwemo kusamehe baadhi ya kodi na tozo, kama ambavyo Mheshimiwa Rais Museveni amezitaja kwenye hotuba yake. Tulifanya hivyo kwa kutambua kuwa Mradi huu utakuwa na manufaa makubwa kwa nchi zetu mbili. Bomba litakapokamilika litakuwa linasafirisha takriban lita 200,000 za mafuta ghafi kwa siku, ambapo nchi yetu italipwa Dola za Marekani 12.5 kwa kila pipa. Mbali na hilo, mradi huu utatoa ajira nyingi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja, wakati na baada ya ujenzi kukamilika. Baadhi ya ajira ni hizi ambazo tunazishuhudia hivi leo, ambapo watu wanauza bidhaa zao mbalimbali: chakula; maji, juisi n.k. Lakini wakulima nao watanufaika; na hata wafanyabiashara na wenye viwanda nao watanufaika. Mathalan, Mheshimiwa Rais Museveni ameeleza kuwa ujenzi wa Bomba hili utahitaji saruji nyingi. Hivyo, viwanda vya saruji vitanufaika. Na kwa bahati nzuri, maandalizi ya kujenga kiwanda cha saruji hapa Tanga, ambacho kitakuwa kikubwa zaidi katika Ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati, yanaendelea vizuri.
Sambamba na faida hizo, mradi huu unatarajiwa kuweka misingi ya ushirikiano kwenye sekta ya mafuta na gesi kati ya mataifa yetu. Mathalan, kwa kuwa mafuta kutoka Uganda yatasafirishwa kupitia hapa Tanga, ni dhahiri kuwa sisi nasi tutaweza kuyanunua na hivyo kupunguza gharama za kuagiza bidhaa hiyo kutoka mataifa ya mbali. Aidha, kwa vile mafuta kutoka Uganda yatakuwa ghafi, ni fursa kwa wafanyabiashara wetu na wawekezaji kujenga viwanda vya kuyasafisha. Na kama mlivyomsikia Rais Museveni, hydrocarbons zinazalisha bidhaa nyingi. Mbali na mafuta ya petrol, dizeli, mafuta ya ndege na taa; zinatumika pia kutengeneza plastiki.
Kama hiyo haitoshi, bila shaka, baadhi yenu hapa mnafahamu kuwa katika nchi yetu, hususan kwenye maeneo ya Ziwa Tanganyika na Eyasi, zimeonekana dalili za hydrocarbons ambazo zinaashiria uwepo wa mafuta. Kwa kuwa ugunduzi wa mafuta nchini Uganda kwa kiasi kikubwa ulifanywa na wataalam wa nchi hiyo, tumewaomba ndugu zetu wa Uganda nao wamekubali, kushirikiana nasi katika kuendeleza utafiti wa mafuta katika maeneo hayo. Na mafuta yakipatikana, tutayasafirisha kupitia Bomba hili. Zaidi ya hapo, mmemsikia Mheshimiwa Rais Museveni akisema kuwa angependa kuona tunajenga bomba jingine kutoka Tanzania kwenda Uganda kwa ajili ya kusafirisha gesi yetu. Ni dhahiri kuwa mambo haya yote yakifanyika, ushirikiano wetu utaimarika lakini pia tutaufungua kiuchumi Ushoroba wa Kaskazini (Northern Corridor), ambao unahusisha nchi za Burundi, DRC, Rwanda na Sudan Kusini. Hivyo basi, niwaombe wana-Tanga na Watanzania wenzangu kwa ujumla, kujipanga vizuri katika kutumia fursa zitakazoletwa na mradi huu.
Nafahamu kuwa ili kutekeleza mradi huu, baadhi ya wananchi wameanza kulipwa fidia zao. Napenda kuhakikishia kuwa watu wote wenye kustahili, watalipwa fidia zao kwa mujibu wa sheria za nchi yetu. Bahati nzuri, kama mlivyosikia, kati ya kilometa 1445 za Bomba hili, kilometa 1,100 zitakuwa upande wa Tanzania; na litapita katika mikoa minane. Napenda niwahakikishie kuwa watu wote wenye kustahili, kulipwa fidia kwenye Mikoa yote 8, watalipwa fidia zao. Hakuna hata mtu mmoja atakayedhulumiwa. Lakini nitoe ushauri kwa watu ambao, baada ya kusikia Bomba hili linajengwa, wameanza kuendeleza maeneo ambayo wamepata fununu kuwa Bomba litapita. Waachane kabisa na mpango huo. Wamechelewa. Tulikwishachukua picha za satellite. Tunayafahamu maeneo yote ambayo tunatarajia Bomba hilo litapita. Hivyo, ukianza kujenga sasa, ujue “umeula wa chuya”.
Mheshimiwa Rais Museveni;
Ndugu Watanzania wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Tumekutana hapa kwa ajili ya kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Bomba la Mafuta. Lakini kama nilivyokwishatangulia kusema, hii ni mara yangu ya kwanza kuja Tanga tangu nimekuwa Rais. Kwa sababu hiyo, naomba mniruhusu, japo kwa kifupi, nieleze utekelezaji wa ahadi pamoja na mipango ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa nchi yetu. Na kwa kuwa nipo Tanga, nitaeleza yale tu yanayowahusu wana-Tanga.
Kama mtakavyokumbuka, ahadi yetu kubwa wakati wa kampeni ilikuwa ujenzi wa viwanda. Ninyi wana-Tanga mnafahamu kuwa kuna wakati Mkoa wenu ulikuwa na viwanda vingi. Lakini hapo katikati mkaviua. Lakini nimefurahi kusikia kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wenu kuwa hivi sasa viwanda vingi vinajengwa hapa Tanga. Na kesho amenialika kuzindua na kuweka mawe ya msingi kwenye baadhi ya viwanda hivyo. Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati ya kujenga uchumi wa viwanda, na kwa hapa Tanga tumejipanga kurejesha hadhi ya Tanga, kwa kujenga viwanda vipya na kuvifufua vya zamani vilivyotelekezwa.
Suala la pili ni kuhusu ardhi. Nafahamu kuwa moja ya matatizo makubwa yanayowasumbua wana-Tanga hivi sasa ni ukosefu wa ardhi kwa ajili ya kuendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi, ikiwemo kilimo. Maeneo mengi ya ardhi yanamilikiwa na watu wachache ambao wameshindwa kuyaendeleza. Nilitoa maelekezo kwa Wizara ya Ardhi pamoja na uongozi wa Mkoa kupitia mashamba 72 makubwa yaliyopo katika Mkoa huu. Kufuatia uchambuzi uliofanyika, tayari tumeyachukua mashamba makubwa matano kule Muheza yenye ukubwa wa takriban hekta 14,000, na tumeagiza sehemu ya ardhi hiyo igawiwe kwa wananchi bure na itakayobaki itumike kwa ajili ya shughuli nyingine za maendeleo, ikiwemo kutenga maeneo ya viwanda. Aidha, tumewaandikia barua (notice) wamiliki wa mashamba mengine 12 tukitaka watueleze kwanini tusiwafutie umiliki wao kwa kushindwa kuyaendeleza. Napenda kuwaahidi kuwa zoezi hili ni endelevu. Tutaendelea kuwanyang’anya watu walihodhi ardhi bila ya kuiendeleza na kuwagawia kwa wananchi. Lakini na ninyi wananchi mkipewa, hakikisheni mnaiendeleza. Kinyume chake, nanyi tutawanyang’anya na kuwapa wengine.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwaarifu wana-Tanga kuwa hivi karibuni tunatarajia kuanza ujenzi wa barabara ya lami kutoka hapa Tanga hadi Bagamoyo yenye urefu wa takriban kilometa 175. Barabara hii, ambayo itapugunza umbali wa kutoka Tanga kwenda Dar es Salaam pamoja na kuiunganisha nchi yetu na majirani zetu wa Kenya, ni moja ya miradi iliyopo chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na itajengwa kwa ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika.
Sambamba na hayo, hivi punde Mkuu wa Mkoa wenu amewasilisha ombi kuhusu kupauliwa na kuongezwa kina Bandari ya Tanga. Niseme tu kwamba nimelipokea ombi hilo. Ni jambo lililo wazi kuwa kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanyika hapa Tanga hivi sasa, ni lazima tuipanue Bandari hii ili iweze kuhudumia meli kubwa. Hii itasaidia kupunguza msongamano katika Bandari ya Dar es Salaam. Mizigo inayokuja Tanga na maeneo ya jirani, ikiwemo mafuta, itashushwa hapa na hivyo kuwapunguzia wananchi gharama. Hivyo basi, napenda kuwahakikishia kuwa Bandari yenu itapanuliwa. Na kwa bahati nzuri, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mheshimiwa Prof. Mbarawa, yupo hapa. Bila shaka, amesikia na ataliweka suala hili katika mipango ya Wizara yake.
Mheshimiwa Rais Museveni;
Ndugu Watanzania wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Siwezi kuhitimisha hotuba yangu bila ya kuwashukuru na kuwapongeza wawekezaji wa mradi huu, kampuni za Total, Tullow na CNOOC, kwa kukubali kuwekeza katika mradi huu mkubwa. Napenda kuwahakikishia kuwa Tanzania itatoa ushirikiano wote unaohitajika katika kutekeleza mradi huu, kulingana na masharti ya Mkataba.
Lakini niwaombe jambo moja. Na ninyi mjitahidi kukamilisha mradi huu mapema. Mwaka 2020 ni mbali sana. Mimi sioni kwanini mradi huu uchukue muda mrefu kiasi hicho kutekelezwa. Makampuni yaliyopewa dhamana ya kujenga Bomba ni makubwa na yana uzoefu wa kutosha. Fedha mmesema mnazo. Na wafanyakazi pia wapo. Hivyo, nawasihi sana mjitahidi kukamilisha mradi huu mapema. Watanzania na bila shaka wananachi wa Uganda pamoja na wana-Afrika Mashariki kwa ujumla wanausubiri kwa hamu mradi huu.
Mheshimiwa Rais Museveni;
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mababi na Mabwana:
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kumshukuru tena Mheshimiwa Rais Museveni kwa kuja kushiriki kwenye tukio hili. Namuahidi kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi yake. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuahidi kuwa kwenye sherehe za kuweka Jiwe la Msingi kama hili kule Hoima, nami nitashiriki.
Nawashukuru tena wana-Tanga kwa kujitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hili. Aidha, nawashukuru kwa kunichagua kuwa Rais wenu. Nawaahidi kuwa Serikali ninayoingoza itawatumikia bila kuwabagua kwa misingi ya dini, kabila au vyama. Utekelezaji wa mradi huu ni kielelezo kuwa Serikali ninayoingoza haina ubaguzi. Bomba hili lingeweza kujenngwa mahali popote nchini, lakini tumeamua kulileta hapa Tanga, ambako Mbunge wake hatokani na Chama tawala. Tumefanya hivyo kwa vile maendeleo hayana chama.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, navishukuru na kuvipongeza vikundi vya burudani vilivyotuburudisha kwa nyimbo zao nzuri, hususan zinazotukumbusha sisi Watanzania kuimarisha uzalendo. Navishukuru pia vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa nchi yetu. Aidha, napenda kuwashukuru na kuwapongeza wana-habari kutoka vyombo vyote kwa kuuhabarisha umma kuhusu tukio hili kubwa na muhimu kwa nchi zetu mbili.
Baada ya kusema hayo, mimi pamoja na Mheshimiwa Rais Museveni tupo tayari kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga.
Mungu Ubariki Uhusiano kati ya Tanzania na Uganda!
Mungu Ibariki Jumuiya ya Afrika Mashariki!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- May 11, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT, JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA DHIFA YA KITAIFA ALIYOIANDAA KWA HESHIMA YA MHESHIMIWA JACOB...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini
na Mama Sizakele Zuma;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge la Tanzania;
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania;
Waheshimiwa Marais Wastaafu mliopo;
Mheshimiwa Makamu wa Rais Mstaafu na Mawaziri Wakuu Wastaafu;
Waheshimiwa Mawaziri wa Afrika Kusini na Tanzania mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali,
Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wakuu wa Vyombo Vya Ulinzi na Usalama;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda kwa mara nyingine tena nikushukuru kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais Zuma kwa kukubali mwaliko wetu wa kuja kututembelea. Natambua vizuri kwamba hii si mara yako ya kwanza kutembelea nchi yetu. Umeshatembelea mara kadhaa. Lakini napenda nikuthibitishie kuwa mimi pamoja na Watanzania wenzangu tumefarijika sana kwa ujio wako. Tunayo matumaini makubwa kuwa ziara yako hii, kama nyingine zilizotangulia, itakuza zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya mataifa yetu mawili.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kwa ajili ya Chakula tulichokiandaa kwa heshima ya wageni wetu, Mheshimiwa Rais Zuma na Mkewe Mama Sizakele Zuma pamoja na ujumbe wao. Na kama mnavyofahamu, katika tamaduni nyingi za Kiafrika, wakati wa chakula, sio wa kuzungumza. Lakini kwa leo naomba mnivumilie niseme japo mambo machache.
Kwanza kabisa, napenda niseme kuwa Tanzania na Afrika Kusini ni nchi marafiki na pia ni ndugu. Urafiki na udugu wetu una historia ndefu. Baadhi yenu mtakuwa mkikumbuka kuhusu vita vya mfecane na historia ya Kabila la Wangoni lililopo Kusini mwa Tanzania, ambalo asili yake ni Afrika Kusini. Lakini ukiachilia mbali historia hiyo ya Wangoni, wengi mnafahamu kuwa wakati wa utawala dhalimu na wa kibaguzi nchini Afrika Kusini, Tanzania ilishirikiana kwa karibu na wananchi wa Afrika Kusini, hususan kupitia Chama chao cha ANC.
Kufuatia makubaliano yaliyofikiwa mwaka 1962 kati ya viongozi wetu wawili, yaani Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania na Hayati Mzee Nelson Mandela, Tanzania ilitoa msaada kwa wapigania uhuru wa Afrika Kusini, ikiwemo kuwapatia mafunzo wapiganaji wake katika makambi yaliyopo Kongwa, Dakawa, Mazimbu, Mgawawo na kule Iringa.Kutokana na uhusiano huo wa kihistoria, haishangazi leo hii kuona kuwa Mataifa yetu mawili yana Nyimbo za Taifa zinazofanana; Bendera zetu zinashabihiana; lakini pia vyama vyetu tawala, yaani CCM na ANC vinashirikiana kwa karibu sana.
Na bila shaka, hii ndiyo sababu pia kuwa, tangu kurejea kwa utawala wa wengi nchini Afrika Kusini mwaka 1994, ushirikiano wetu kiuchumi nao umeimarika. Taifa la Afrika Kusini ni miongoni mwa nchi 10, ambazo ni washirika wakuu wa Tanzania katika biashara na uwekezaji. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, biashara kati yetu ilifikia thamani ya shilingi za Tanzania trilioni 2.4 mwaka 2016, wakati uwekezaji wa Afrika Kusini hapa nchini hivi sasa una thamani ya Dola za Marekani milioni 803.15 na umetoa takriban ajira 20,916. Hii ni kudhihirisha kuwa uhusiano wetu ni mzuri; na unakua kila kukicha.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Katika Ziara hii ya Mheshimiwa Zuma hapa nchini, tumeweza kufanya Mkutano wa Kwanza wa Tume ya Marais ya Ushirikiano (Bi-National Commission - BNC). Katika Mkutano huo, tumejadiliana kwa kirefu kuhusu namna ya kuimarisha ushirikiano katika nyanja mbalimbali, ikiwemo biashara na uwekezaji; maendeleo ya viwanda, miundombinu; kilimo; afya; elimu; sayansi na teknolojia; ulinzi na usalama; nishati na madini; pamoja masuala ya maliasili na utalii. Na tumehimizana katika kusimamia utekelezaji wa makubaliano tuliyofikia. Aidha, tumekubaliana kuharakisha utekelezaji wa Mikataba yote iliyosainiwa na nchi zetu siku za nyuma, ambayo kwa sasa imefikia 16, ukiwemo mmoja tuliousaini leo.
Lakini mbali na kufanya Mkutano wa Tume yetu ya Ushirikiano, katika ziara hii, Mheshimiwa Rais Zuma ameambatana na wafanyabiashara wapatao 80. Kwa siku nzima ya leo, wafanyabiashara hao wamekutana na wenzao wa Tanzania. Na nimeambiwa kuwa Mkutano ulikuwa ni mzuri sana. Wamepashana habari kuhusu fursa za biashara na uwekezaji zilizopo katika nchi zetu; na pia wamebadilishana uzoefu na kupeana mbinu za kufanya biashara. Hivyo basi, nina uhakika, muda mfupi ujao, tutaona matunda yake. Namshukuru tena Mheshimiwa Rais Zuma kwa kufanya ziara, ambayo imekuza zaidi ushirikiano kati yetu.
Mheshimiwa Rais Zuma na Mama Sizakele Zuma;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Niliahidi kuzungumza kwa kifupi. Lakini siwezi kuhitimisha hotuba yangu bila ya kumpongeza Mheshimiwa Rais Zuma, Serikali na Wananchi wote wa Afrika Kusini kwa kuadhimisha Miaka 23 ya kumalizika kwa utawala wa kibaguzi hapo tarehe 27 Aprili, 2017. Hakuna shaka, katika kipindi hicho Afrika Kusini imepiga hatua kubwa, hususan katika kujenga haki, usawa na demokrasia. Afrika Kusini pia imetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Kanda yetu ya SADC, Bara letu la Afrika na Duniani kwa ujumla. Napenda kuahidi kuwa Tanzania chini ya uongozi wangu itaendelea kushirikiana na Afrika Kusini ili kudumisha na kukuza zaidi uhusiano na ushirikiano wa kidugu na kihistoria kati yetu.
Baada ya kusema hayo, mabibi na mabwana, kwa heshima na taadhima, sasa naomba sote tusimame na kisha tunyanyue glasi zetu juu:
- Kwa ajili ya afya njema ya Rais Jacob Zuma na Mama Zuma;
- Kwa Ustawi wa Uhusiano wa Tanzania na Afrika Kusini; na
- Kwa Maendeleo ya nchi zetu mbili na watu wake.
“Ahsanteni kwa kunisikiliza”.

- May 11, 2017
REMARKS BY H.E. DR. JOHN POMBE MAGUFULI, PRESIDENT OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA DURING THE TANZANIA – SOUTH AFRICA BUSINESS FORUM, DAR ES SALAAM, 11TH...
Soma zaidiHotuba
Your Excellency Jacob Zuma, President of the Republic of South Africa;
Honourable Ministers here present;
Distinguished Members of the Business Community
from Tanzania and South Africa;
Invited Guests, Ladies and Gentlemen;
I am very pleased for this opportunity to meet with the members of the Business Community not only from my own country but also from a brotherly and friendly country, South Africa. I understand you have been here since morning and much has already been said. However, allow me to take this opportunity to warmly welcome to Tanzania our guests from South Africa. As you are all very well aware, Tanzania and South Africa are very good friends and strong allies. Our friendship has been maintained for years and that our two countries have been enjoying excellent cooperation at bilateral, regional and international levels. It is for this reason that I would like to very sincerely welcome our South African friends to Tanzania. Please, feel at home. This is indeed your home.
It is unfortunate that you will be here just for a short stay, but it is my sincere hope that you will find time to visit our country again so that you get a chance to experience and enjoy, in particular, Tanzania’s touristic attractions, such as Mount Kilimanjaro, Serengeti National Park, Ngorongoro Crater, as well as the beautiful shores of the spice Island of Zanzibar.
Distinguished Members of the Business Community;
I have noted, with great encouragement, that trade and investment are on the increase since 2011. However, as we strive to further consolidate the relations between our two countries, we also need to enhance further our cooperation in trade and investments. To that end, and this being a Business Forum, I am sure serious business has been discussed since morning. And by now, each side has sufficient or necessary information about the investment and business opportunities available in each other’s country. That notwithstanding, I would like to add my voice on the investment and business opportunities available in Tanzania.
To begin with, Tanzania has got a conducive business environment. We are a peaceful and politically stable nation. We have enjoyed uninterrupted peace, political stability and national concord since independence. We are a vibrant democracy and committed to advancing good governance and the rule of law. I should also mention that the basic infrastructure services such as power, road, rail, air and water transport are available at a satisfactory level.
Furthermore, our country has put in place stable and predictable economic policies and investment regimes that are friendly to investors. They are comparable to any other environment that an investor would enjoy in almost all the hot spots of investment flows in the developing world. There are favourable fiscal incentives to investors with regard to corporate tax, customs duty, VAT, capital investments, work and resident permits. The investment law provides for protection of investments and we are committed to fighting corruption, terrorism and other vices. Additionally, we are a member of the International Centre for Settlement of Investment Dispute and the Multilateral Investment Guarantee Agency (MIGA) of the World Bank. So, it is safe to invest in Tanzania, as we are also ready to improve the business environment.
Apart from that, we have a huge market. As you know, we are located in a very strategic area, bordered with 8 countries, including six landlocked countries, namely Burundi, DRC, Malawi, Rwanda, Uganda and Zambia. These countries, by and large, use Tanzania territory to conduct their international trade. As a Member of the East African Community (EAC) and the Southern African Development Cooperation (SADC), investors are assured of the huge market of about 400 million people. Besides, we have trade quota and tariff free trade arrangements with China, India, Japan, USA and the EU.
Your Excellency, President Zuma;
Distinguished Members of the Business Community;
In addition to good business environment, we have plenty of business and investment opportunities in our country. We have 44 million hectors of arable land of which less than 10 million hectors are currently under use. The climate is favourable for agriculture, water for irrigation is also plenty, and the land is fertile. Almost all crops can grow in Tanzania.
Fishery is yet another sub-sector that presents business and investment opportunity for the private sector. Our country now needs at least 400,000 tonnes of fish per annum. Yet, we are now producing only 30,000 tonnes. In this respect, in order to promote fisheries business in Tanzania, the government has reduced import taxes on most of the fishery equipment, including those used in fish farming. In line with this we invite investors to invest in this sector whereby, opportunities range from Deep Sea Fishing, Fish Processing & Canning, Aqua/Mari culture and Establishment of lending facilities.
We also invite investors to come to invest in one of the fast growing sectors in the country, that is, Tourism. This industry accounts for about 24.0 % of exports and 17.2% of GDP. We are the only country in the world that has allocated more than 25 percent of its total area for wildlife and other resources’ conservation. There are 16 National Parks, 28 Game Reserves, 44 Game Controlled areas, 1 Conservation Area and 2 Marine Parks. Opportunities exist for investing in areas such as tour-operators business, and tourism infrastructure development particularly construction of first class hotels in towns, game parks as well as along the 1,424 Kilometres coast line of mainland Tanzania and the beautiful shores of the spice Island of Zanzibar.
Our construction sector is also growing very fast. The list of projects in the pipeline is very long. We have huge infrastructure projects which require investments, especially in the fields of transport, energy and water. These projects include a 1,200 kilometre Standard Gauge Railway line from Dar es Salaam to Mwanza, as well as Kiwira and Mchuchuma coal to power projects. We, therefore, welcome South African investors to come to invest in these projects.
Your Excellency, President Zuma;
Distinguished Members of the Business Community;
Tanzania is committed to becoming a semi-industrialized nation by 2025. To this end, we have decided to put greater accent on building a strong industrial base, including setting up Export Processing Zones (EPZs) and Special Economic Zones (SEZs) as ponds of industrial growth and services to promote export trade. I, therefore, invite you to come to make full use of these ponds for our mutual benefit.
In this respect, one of the areas that present great opportunities is manufacturing. Tanzania offers abundant natural resources which provide for plenty of raw materials for the manufacturing industries such as cotton for garment and textile industries, sisal for canvassing, etc.
For those of you who have a capability for minerals processing, investment opportunities exist in the mining sector where we have precious gemstones and minerals including gold, diamond, nickel and tanzanite, just to mention a few. These locally available raw materials will assure investors with raw materials for extractive industries on low cost but with high value investments.
Our service sector is also growing very fast. There are enormous opportunities in the services sector particularly ICT, which is among the fastest-growing sub-sectors in Tanzania. In the last 10 years, the ICT market has grown in terms of subscribers, variety of services and the expansion of the coverage area. Potential areas for investment include provision of mobile services especially in rural areas, provision and operation of value added network/data services, as well as repair and maintenance of telecommunications facilities. We also welcome potential investors to establish financial institutions such as Industrial and Agricultural banks.
Your Excellency, President Zuma;
Dear Members of Business Community;
Distinguished Invited Guests, Ladies and Gentlemen;
I could go on and on mentioning opportunities for investments that are available in Tanzania. But, it is not my intention to labour you with a long speech. Let me end here. But, before I conclude, I wish to take this opportunity to once again thank His Excellency President Zuma for coming with all of you to meet with your counterparts, the businessmen and women of Tanzania.
I wish also to commend all the Organizers of this Business Forum. It has been a success by all standards. Finally, I wish to once again welcome South African business people to come to invest in Tanzania. I encourage you to come to make full use of these opportunities. Tanzania is a safe place for investment and also to do business.
“I thank you for your kind attention”

- May 01, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KILELE CHA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI MOSHI, KILIMANJAR...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika
wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Ndugu Tumaini Nyamhokya, Rais wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania;
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,
Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Bolozi John Kijazi, Katibu Kiongozi;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Mecky Sadick, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro;
Mheshimiwa Mary Kawar, Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani,
Ofisi za Afrika Mashariki;
Waheshimiwa Majaji mliopo;
Mheshimiwa Almas Maige, Mwenyekiti
Chama cha Waajiri Tanzania;
Waheshimiwa Wabunge mkiongozwa na Mbunge wa Moshi Mjini;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Mheshimiwa Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi;
Ndugu Reginald Mengi, Mwenyekiti wa Sekta Binafsi Tanzania;
Ndugu Dkt. Yahya Msigwa, Katibu Mkuu wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA);
Ndugu Dkt. Aggrey Mlimuka, Mkurugenzi Mtendaji
wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE);
Viongozi wa Serikali, Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;
Wanahabari, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa tukiwa salama. Aidha, napenda na mimi nikiri kuwa sijawahi kuona kwenye sherehe za Mei Mosi umati mkubwa kama huu. Hii inanipa shida hata mimi ya namna ya kujibu hoja nilizoelezwa na Katibu Mkuu wa TUCTA. Lakini kwa ujumla, niseme tu kwamba leo Moshi mmevunja rekodi na kwa kweli mmenipa nguvu kubwa sana ya kuwatumikia. Na namwomba Mwenyezi Mungu anisaidie ili nisiwaangushe katika kuwatumikia.
Napenda pia kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa Uongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), wakiongozwa na Rais wa Shirikisho, Ndugu Tumaini Nyamhokya kwa kunialika kuwa Mgeni Rasmi katika Siku hii muhimu kwa Wafanyakazi Duniani. Aidha, nawapongeza Viongozi Wapya wa TUCTA kwa kuchaguliwa kwenu kuongoza Shirikisho hili. Hakuna shaka, ushindi mlioupata ni kielelezo cha imani kubwa waliyonayo Wafanyakazi wa Tanzania juu yenu. Nawatakia utekelezaji mwema wa majukumu yenu mpya. Na kwa namna ambavyo mmeanza nina ukakika kabisa mtayamudu vyema.
Binafsi,nimeshakutana nanyi mara moja pale Ikulu, Dar es Salaam, ambapo tulifanya mazungumzo. Kwa kile ambacho nilikiona katika mazungumzo yetu, ni dhahiri kuwa mmedhamiria kwa dhati kuwasaidia wafanyakazi na nchi yetu kwa ujumla. Napenda kurudia ahadi niliyotoa siku ile kwamba,mimi pamoja na wenzangu Serikalini, tutawapa ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza majukumu yenu.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru wana-Kilimanjaro kwa kukubali kuwa wenyeji wa maadhimisho haya. Tunawashukuru pia kwa mapokezi makubwa na kwa ukarimu mliotuonesha tangu tumewasili. Lakini kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kufika katika Mkoa wa Kilimanjaro tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda niwashukuru wana-Kilimanjaro kwa maombezi na kura zenu zilizoniwezesha kuchaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Nchi yetu. Ahsanteni sana.
Uchaguzi sasa umekwisha, jukumu kubwa ambalo lipo mbele yetu kwa sasa ni kujenga Taifa letu. Mimi ni Rais wa Watanzania wote. Nitafanya kazi kwa maslahi ya Watanzania wote. Na napenda niwaahidi wana-Kilimanjaro kuwa yale yote tuliyoahidi wakati wa kampeni tutayatekeleza. Na kwa kweli, tayari mambo mengi tumeshaanza kutekeleza, ambayo sina shaka mengi mnayafahamu.
Tumeongeza wastani wa ukusanyaji wa mapato kwa mwezi kutoka shilingi bilioni 850 hadi kufikia shilingi trilioni 1.3, na tumeweza kubana matumizi yasiyo ya msingi. Hii imetuwezesha kuongeza bajeti ya maendeleo kutoka wastani wa asilimia 26 za awali hadi kufikia asilimia 40. Tunajenga na kuimarisha miundombinu ya usafiri, umeme na maji. Tumenunua ndege sita mpya, ambazo nina uhakika zitakuza utalii, hususan katika Mkoa huu wa Kilimanjaro. Watalii sasa watakuja hapa moja kwa moja bila kupitia nchi jirani.
Tunatoa elimu bila malipo kutoka shule ya msingi hadi sekondari, kama tulivyoahidi, ambapo Serikali inatenga kiasi cha shilingi bilioni 18.77 kila mwezi kugharamia.Tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo ya elimu ya juu kutoka 98,300, wakati tunaingia madarakani, hadi kufikia 124,198, hivi sasa.Tumeongeza bajeti ya kununua madawa kutoka shilingi bilioni 31 hadi kufikia shilingi bilioni 250.
Leo sio siku ya kueleza mafanikio ambayo tayari tumepata. Leo ni Siku ya Wafanyakazi. Hivyo basi, itoshe tu kusema kuwa tangu tumeigia madarakani, Serikali imefanya mambo mengi yenye manufaa kwa taifa letu na watu wake, wakiwemo wafanyakazi.
Ndugu Wafanyakazi, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Hakuna shaka,leo ni siku muhimu. Kama mnavyofahamu, Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani, maarufu kama Mei Mosi; ni siku muhimu sio tu hapa nchini bali duniani kote. Ni siku ambayo wafanyakazi duniani kote wanapata fursa ya kukumbushana kuhusu umuhimu wa kujenga umoja na mshikamano katika kutetea maslahi yao. Ni siku ambayo wafanyakazi wanapata fursa ya kutafakari masuala yanayowahusu, hususan kwa kuanisha changamoto zinazowakabili na kupendekeza mikakati ya kuzishughulikia. Lakini, mbali na hayo, Mei Mosi, ni siku ambayo hutumika Duniani kote kutambua na kuenzi mchango unaotolewa na wafanyakazi katika shughuli za maendeleo.
Kama mnavyofahamu, wafanyakazi ndio injini ya maendeleo ulimwenguni kote. Hakuna jambo la maendeleo limewahi kufanyika hapa duniani ambalo wafanyakazi hawajashiriki. Katika kila jambo, wanahusika. Kuanzia kwenye shughuli za kilimo, uvuvi, ufugaji, utalii, ujenzi wa miundombinu ya kiuchumi, ulinzi wa amani na usalama, utoaji wa huduma za jamii, maendeleo ya sayansi na teknolojia, n.k. Kote wafanyakazi wanahusika.
Ni kwa sababu hiyo, napenda kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali, kutumia fursa hii kuwapongeza sana Wafanyakazi wote, hususan Wafanyakazi wa Tanzania, kwa kuadhimisha siku hii; na kwa mchango wenu mkubwa katika maendeleo ya taifa letu. Serikali inatambua mchango wenu mkubwa na tunawasihi sana muendelee kujituma na kuchapakazi kwa bidii. Maendeleo ya taifa letu, kwa kiasi kikubwa, yanawategemea ninyi. Serikali itaendelea kushughulikia changamoto zinazowakabili ili muweze kufanya kazi katika mazingira mazuri.
Ndugu Viongozi wa TUCTA na Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Muda mfupi uliopita tumesikia Risala ambayo imesomwa kwa ufasaha mkubwa na Katibu Mkuu wa TUCTA, Dkt. Msigwa. Ni Risala ambayo inajieleza yenyewe. Na bahati nzuri, viongozi wote muhimu ambao wanapaswa kushughulikia hoja zilizotolewa na TUCTA wapo hapa. Kuanzia Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Spika wa Bunge, Naibu Spika, Mawaziri na Katibu Mkuu Kiongozi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wabunge; wote wapo hapa. Hivyo, nina imani wamesikia mambo yaliyoelezwa na watayashughulikia.
Na napenda niwahakikishie ndugu wafanyakazi wenzangu kuwa Serikali imesikia na itazifanyia kazi hoja zenu zote. Sisi kwa upande wetu tumedhamiria kwa dhati kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano na Wafanyakazi. Tutaimarisha uhusiano na ushirikiano wetu na Vyama vya Wafanyakazi pamoja Chama cha Waajiri. Tutaujenga na kuimarisha kikamilifu utatu huu. Ombi langu kwenu wafanyakazi endeleeni kuiunga mkono Serikali, hususan kwa kuchapa kazi kwa bidii.
Ndugu Viongozi wa TUCTA na Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Kama nilivyosema, Risala ya Katibu Mkuu wa TUCTA imeeleza hoja nyingi. Lakini niseme tu kwamba hoja na madai mengi yaliyowasilisha sio mageni. Ni masuala ya muda mrefu. Na baadhi Serikali ilishaanza kushughulikiwa na tumefikia hatua nzuri. Mathalan, katika Risala yenu, mmeomba kuboreshwa kwa mfumo wa Hifadhi ya Jamii, hususan kuanzishwa kwa Fao la Kukosa Ajira, kama mbadala wa Fao la Kujitoa ambalo limefutwa kwa Sheria Na. 5 ya mwaka 2012. Napenda kuwaarifu kuwa Serikali inaendelea na taratibu za kuanzisha Fao la Kujitoa/Bima ya Ajira ili kuwawezesha wafanyakazi ambao ni wanachama wa Mifuko ya Pensheni kulipwa sehemu ya michango yao kwa mujibu wa sheria pindi wanapopoteza ajira kabla ya kufikisha umri wa kustaafu. Utaratibu wa kuanzisha Fao/Bima hiyo unaendelea vizuri. Wadau, wakiwemo waajiri na vyama vya wafanyakazi, wameshatoa maoni yao. Na nimearifiwa kuwa, hivi karibuni, Muswada wa Sheria wa kuanzisha Fao hilo utapelekwa Bungeni. Na Bunge likipitisha, siku hiyo hiyo nitasaini.
Kuhusu Mifuko ya Hifadhi ya Jamii pia, mmezungumzia suala la kuharakisha kuundwa kwa mifuko miwili ili kupunguza utitiri wa mifuko hiyo na hatimaye kupunguza gharama za uendeshaji. Kama mnavyofahamu, suala hili lilikwishakubaliwa na Serikali na tumefikia hatua nzuri. Wadau muhimu, mkiwemo ninyi vyama vya wafanyakazi pamoja na waajiri, tayari mmetoa maoni na mapendekezo kuhusu namna ya kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii. Kwa sasa Waraka wa Baraza la Mawaziri unaandaliwa ili hatimaye itungwe sheria itakayowezesha kuunganisha mifuko ya hifadhi ili ibaki miwili. Zoezi hili likikamilika, tutakuwa tumepata mwarobaini wa tatizo la tofauti ya fomula ya ukokotoaji wa mafao, ambalo nalo ni moja ya malalamiko ya wafanyakazi nchini.
Risala yenu pia imeeleza kuhusu suala la ucheleweshaji wa malipo ya mafao. Hili nalo Serikali inalishughulikia tena kwa nguvu sana. Kama mnavyofahamu, suala hili la ucheleweshaji, kwa kiwango kikubwa, lilikuwa linasababishwa na waajiri kushindwa au kuchelewa kuwasilisha michango ya wafanyakazi wao. Na mmoja wa waajiri hao ni Serikali. Mathalan, wakati tunaingia madarakani, Serikali ilikuwa inadaiwa takriban shilingi trilioni 1.5 kwenye mifuko ya hifadhi ya jamii. Tangu wakati huo, tumeshalipa shilingi trilioni 1.23. Na zilizobaki tutazilipa hivi karibuni.
Kufuatia Serikali kulipa deni hilo, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii sasa inawalipa wastaafu mafao yao kwa wakati. Na hii sasa itaipa nguvu Serikali ya kufuatilia na kuwahimiza waajiri wengine, hususan wa sekta binafsi, kuwasilisha michango ya wafanyakazi wao kwa wakati.
Ndugu Viongozi wa TUCTA na Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Suala jingine ambalo mmelieleza vizuri kwenye Risala yenu ni kuhusu Usalama Kazini, Afya na Gonjwa la Ukimwi. Haya ni masuala ambayo hayana mjadala. Hivyo, naahidi tutayasimamia na kuyatekeleza.
Kwenye Risala pia limegusiwa suala la Uhuru wa Wafanyakazi Kujiunga na Vyama vyao. Suala hili nilishalizungumzia mwaka jana. Lakini napenda kurudia tena leo. Vyama vya wafanyakazi mahali pa kazi si suala la hiari. Lipo kwa mujibu wa sheria. Hivyo basi, hakuna sekta, kampuni wala mwekezaji aliye juu ya sheria hii. Kila taasisi na mwajiri ni lazima watekeleze takwa hili la kisheria. Wito wangu kwa wafanyakazi kote nchini ni kwamba msigeuzi vyama hivyo kuwa vyanzo vya migogoro au migomo sehemu za kazi.
Sambamba na hilo, napenda kuhimiza Wizara na taasisi mbalimbali kuhakikisha zinaunda Mabaraza ya Wafanyakazi kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Namba 6 ya Mwaka 2004. Nimeambiwa, mpaka sasa, yameundwa mabaraza ya wafanyakazi 487. Bado 28, yakiwemo 14 katika halmashauri na 14 mengine katika taasisi nyingine za umma.Nazihimiza taasisi ambazo hazijaunda mabaraza kufanya hivyo mara moja na kuhakikisha yanafanya kazi.
Kuhusu suala la Mikataba ya Ajira kwa Wafanyakazi. Hili nalo sio suala la hiari. Kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya Mwaka 2004, waajiri wote wanapaswa kutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi wao. Kinyume chake ni kosa kisheria. Hivyo basi, namwagiza Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kusimamia ipasavyo suala hili, hususan kwa kuimarisha ukaguzi na usimamizi . Aidha, Vyama vya Wafanyakazi navyo vinapaswa kutoa ushirikiano kwa Serikali kwa kuwafichua waajiri wasiotoa mikataba ya ajira ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
Kuhusiana na suala la Utekelezaji wa Mikataba ya Kimataifa, napenda kwanza kulishukuru Shirika la Kazi Dunia (ILO) kwa misaada mbalimbali inayotoa kwa nchi yetu, hususan yenye lengo la kukuza ajira, kupanua wigo wa hifadhi ya jamii na kuimarisha utekelezaji wa viwango vya kazi kimataifa. Napenda kuahidi kuwa Serikali itaendelea kusaini, kuridhia na kutekeleza mikataba ya kimataifa kuhusu masuala ya kazi na ajira yenye maslahi kwa wafanyakazi na Taifa kwa ujumla.
Na katika hili, napenda kuarifu kuwa katika Mkutano wa Bunge unaoendelea, Serikali imewasilisha Azimio la kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi za Ubaharia wa Mwaka 2006 (Marine Labour Convention) na Mkataba wa Kimataifa wa Vitambulisho Na. 185 wa Mwaka 2003 (Seafarer’s Identity Documents Convention). Kuridhiwa kwa Mikataba hii kutaongeza fursa za ajira kwa mabahari wa Tanzania na nchi yetu itanufaika na fursa za mafunzo na ajira.
Mheshimiwa Rais wa TUCTA;
Ndugu Viongozi wa TUCTA;
Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Mbali na hatua za kushughulikia baadhi ya hoja ambazo zimetajwa kwenye Risala ya Katibu Mkuu wa TUCTA, Serikali pia inaendelea kuchukua hatua nyingine zenye lengo la kuboresha mazingira ya kazi na maslahi ya wafanyakazi nchini. Baadhi ya hatua hizo ni kama ifuatavyo:
Kwanza kabisa, tumeendelea kuhimiza ujenzi wa Viwanda. Kama mnavyofahamu, kukua kwa sekta ya viwanda nchini kutaleta matokeo chanya kwa Watanzania wote, wakiwemo wafanyakazi. Hii ni kwa sababu viwanda vitaongeza mapato kwa Serikali na kuiwezesha kuboresha maslahi ya watumishi nchini. Lakini sio hivyo tu. Viwanda pia vitaongeza idadi ya wanachama kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Idadi ya wanachama ikiongezeka, Mifuko itaboresha mafao ya wanachama pindi wanapostaafu.
Nafurahi wito wa kujenga viwanda umepokewa vizuri. Viwanda vingi hivi sasa vinajengwa katika maeneo mbalimbali nchini. Hata Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya NSSF, PPF, PSPF na GEPF nayo imejitokeza kuwekeza kwenye sekta ya viwanda. Miradi ya viwanda yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 156 inatarajiwa kutekelezwa na mifuko hiyo. Viwanda hivyo ni vya Sukari (Mkulazi –Morogoro), Viatu (Moshi) na Viwatilifu vya kuulia vimelea vya malaria (Kibaha), ambavyo vitaajiri Wafanyakazi wapatao 310,000. Tunaendelea kuwahimiza wafanyabiashara wengine kuwekeza kwenye sekta ya viwanda, ikiwemo katika Mkoa huu wa Kilimanjaro, ambao Mheshimiwa Mkuu wenu wa Mkoa ameeleza kuwa zamani ulikuwa na viwanda vingi, lakini hivi sasa vimekufa.
Mbali na kujenga viwanda, Serikali inachukua hatua nyingine mbalimbali zenye lengo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi nchini. Hatua hizo ni pamoja na kuwaondoa watumishi hewa. Mpaka sasa tumeshawabaini watumishi hewa wapatao 19,706 ambao, kama wangekuwa hawajaondolewa, wangeigharimu Serikali kiasi cha shilingi bilioni 19.848 kwa mwezi, sawa na shilingi bilioni 238.17 kwa mwaka. Fedha hizi zingeweza kutumika kuboresha maslahi na mazingira ya kazi ya watumishi waliopo kazini au kufanya shughuli nyingine ambazo zingewanufaisha wafanyakazi. Ni kwa sababu hii, Serikali ililazimika kusitisha kwa muda zoezi la kuajiri na kupandisha vyeo watumishi. Kwa sasa, zoezi hili limefikia hatua nzuri, takriban asilimia 98.
Sambamba na kuhakiki watumishi hewa, tulianzisha zoezi la uhakiki wa vyeti vya watumishi. Nchi yetu inaruhusu kila mtu kuajiriwa kulingana na elimu yake. Lakini wapo ambao wamekuwa wakitafuta vyeti vya kughushi ili kupata nafasi ambazo hawastahili. Wiki iliyopita nimepokea Taarifa kuhusu Ukaguzi wa Vyeti vya Wafanyakazi. Katika Ukaguzi huo, tumebaini kwamba, kati ya watumishi 400,035 wa Serikali za Mitaa, mashirika ya umma na taasisi za Serikali ambao wamehakikiwa, watumishi 9,932 wana vyeti vya kughushi; wakati watumishi 1,538 wana vyeti vyenye utata, kwa maana kwamba vyeti vyao vinatumiwa na zaidi ya mtu mmoja. Aidha, watumishi 11,596 waliwasilisha vyeti vya taaluma bila ya vyeti vya elimu. Watumishi wote wenye vyeti vya kughushi tumewapa hadi tarehe 15 Mei, 2017 kuwa wamejiondoa kazini. Kinyume na hapo, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Ndugu Viongozi wa TUCTA na Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Uwepo wa vyeti vya kughushi umesababisha matatizo mengi hapa nchini. Umepunguza tija katika utendaji wa kazi, umewakosesa watu wenye sifa ajira, vyeo na stahili mbambali, n.k. Na jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba, wengi wenye vyeti feki ni watoto wa viongozi na watu wenye uwezo. Mtoto wa maskini hawezi kupata fedha ya kununua cheti feki. Anajihangaikia mwenyewe.
Baada ya kufikia hatua nzuri katika mazoezi haya ya uhakiki, Serikali sasa imepanga kuanza kuajiri tena. Kwenye Mwaka ujao wa fedha, tunatarajia kuajiri watumishi wapya wapatao 52,000 wa kada mbalimbali na pia tutaanza kuwapandisha tena madaraja watumishi. Aidha, katika mwaka ujao wa fedha, Serikali itatoa nyongeza ya kawaida ya mshahara kwa watumishi (annual increment). Lakini niseme tu kwamba uamuzi huu wa kuanza tena kuajiri, kupandisha madaraja na kutoa nyongeza ya mshahara, haumaanishi kuwa tumefikia mwisho. Bado tutaendelea na uhakiki wa watumishi hewa na vyeti. Zaidi ya hapo, tutaanza ukaguzi wa watumishi ambao wamebadilisha umri wao wa kustaafu.
Ndugu Viongozi wa TUCTA na Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Suala jingine ambalo tunalishughulikia ni ulipaji wa madeni ya watumishi. Mathalani, tangu tumeingia madarakani mwezi Novemba 2015, tumelipa madeni ya walimu ya kimshahara yenye thamani ya shilingi bilioni 14.23 na pia tumelipa madeni ya watumishi yasiyo ya kimshahara yenye thamani shilingi bilioni 42.4. Tutaendelea kulipa madeni mengine kadri tutakavyokuwa tumejiridhisha kuwa hakuna udanganyifu. Hivyo, nawasihi sana wafanyakazi, mtuvumilie.
Kama mnavyofahamu, kumekuwa na tabia ya kutengeneza madeni ya uongo (madeni hewa). Mathalan, kuna baadhi ya viongozi wanashirikiana na watumishi kutengeneza uhamisho na kisha kugawana fedha hizo za uhamisho. Wakati mwingine uhamisho umekuwa ukitolewa kwa sababu ya ugomvi binafsi kati ya kiongozi na mtumishi. Kwa sababu hiyo, naagiza, kuanzia sasa, ni marufuku kumwamisha mtumishi kabla ya kumlipa fedha zake za uhamisho.
Mbali na kulipa madeni ya watumishi, tumeweza kulipa madeni kwa ajili ya kutekeleza miradi mbali ya miundombinu ya barabara, umeme, maji na reli kiasi cha shilingi trilioni 3.68. Kati ya fedha hizo shilingi trilioni 1.1697 lilikuwa ni deni la wakandarasi wa barabara. Sambamba na hilo, tumetoa kiasi cha shilingi bilioni 80 kwa ajili ya kuwalipa wazabuni na watoa huduma mbalimbali, wakiwemo wanaotoa huduma katika shule na magereza yetu.
Kama mnavyofahamu, madeni haya ya wakandarasi na wazabuni ilikuwa ni mzigo mkubwa kwa Serikali. Hivyo, baada ya kufanikiwa kupunguza mzigo huu, Serikali itaweza kuelekeza fedha kwenye shughuli nyingine, ikiwemo kuboresha mazingira na maslahi ya wafanyakazi. Lakini niseme tu kwamba, ingawa tumepunguza madeni, Serikali bado inadaiwa. Hivyo, hatutaweza kuelekeza fedha zote katika kuboresha maslahi ya wafanyakazi. Tutaendelea kulipa madeni na kuwekeza fedha tunazozipata kwenye shughuli nyingine za maendeleo, ambazo pia zitawanufaisha wafanyakazi. Mathalan, hivi sasa tunajenga reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa na tumenunua ndege sita. Mambo haya yote yatawanufaisha wafanyakazi na Watanzania kwa ujumla.
Ndugu Viongozi wa TUCTAna Ndugu Wafanyakazi wenzangu,
Siwezi kuhitimisha hotuba bila ya kugusia masuala mengine machache ambayo baadhi yamegusiwa kwenye Risala ya Katibu Mkuu wa TUCTA. Kwanza kabisa ni kuhusu kaulimbiu ya Mei Mosi mwaka huu, ambayo inasema “Uchumi wa Viwanda Uzingatie Kulinda Haki, Maslahi na Heshima ya Wafanyakazi”. Hii ni kauli mbiu nzuri na imenipa moyo kuwa wafanyakazi mnatambua azma ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda. Nawahakikishia kwamba ujenzi wa viwanda utazingatia haki, maslahi na heshima ya kazi nchini. Lakini niwe muwazi tu kuwa, hatutamvumilia mfanyakazi mzembe na atakayetaka kutukwamisha katika kufikia azma yetu ya kujenga uchumi wa viwanda. Nimefarijika kusikia kwenye Risala yenu kuwa nanyi matuunga mkono. Risala yenu imeeleza kuwa TUCTA, nanukuu “…haitatetea wafanyakazi wavivu, wazembe, wabadhirifu, wala rushwa, wenye majungu, walevi wa kupindukia na wasiofuata sheria za kazi na za nchi…”, mwisho wa kunukuu. Nawashukuru sana kwa kutuunga mkono.
Nimefurahi pia katika Risala ya TUCTA mmehimiza suala la amani nchini. Hili ni suala muhimu sana. Amani ndio msingi mkuu wa maendeleo. Bila ya amani, hakuna maendeleo. Nashukuru kwa kuunga mkono juhudi za Serikali za kupambana na biashara ya madawa ya kulevya. Ahsanteni sana.
Mmezungumzia pia kuhusu suala la Ugumu wa Maisha na Mfumko wa Bei ya Bidhaa Muhimu. Serikali imepokea suala hilo na tutalifanyia kazi. Lakini niseme tu kwamba Serikali imejitahidi sana kudhibiti mfumko wa bei nchini. Mathalan, mwezi Januari mwaka 2016, mfumko wa bei ulikuwa asilimia 7. Lakini kuanzia mwezi Machi tuliweza kuushusha hadi kufikia asilimia 4 na kiwango hicho kilidumu hadi mwezi Novemba 2016, ambapo mfumko wa bei ulianza kupanda tena na sasa umefikia asilimia 6.4, kutokana na kuchelewa kwa mvua kwenye baadhi ya maeneo ya Nchi yetu. Lakini sasa mvua zinanyesha katika maeneo mengi ya nchi yetu na hivyo nina uhakika mfumko wa bei utashuka.
Jambo jingine ambalo ningependa kuzungumzia ni suala la Makato ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Napenda niarifu kuwa kuwa tangu utaratibu wa kutoa mikopo ya elimu ya juu uanze mwaka 1994/95, Serikali imeshatoa jumla ya shilingi trilioni 2.9. Mikopo ambayo imeiva hivi sasa ina thamani ya shilingi trilioni 1.4 na ambayo inapaswa kuwa imerejeshwa ni shilingi bilioni 427. Lakini mpaka sasa, ni shilingi bilioni 181.4 tu ndizo zimerejeshwa. Hii maana yake ni kwamba kuna wanufaika wengi wa mikopo ambao hawataki kuirejesha. Ni kwa sababu hiyo, Serikali ilifikia uamuzi wa kuongeza makato kutoka asilimia 8 hadi asilimia 15 ili kuwezesha mikopo hiyo kurejeshwa haraka na kuwanufaisha wengine. Uamuzi huu unawalenga watu wote walionufaika na mikopo ya elimu ya juu. Hivyo, niwaombe TUCTA na Vyama vya Wafanyakazi kuwahimiza wanachama wenu kurejesha mikopo hiyo.
Ndugu Rais wa TUCTA;
Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimeeleza mengi. Naomba niishie hapa. Lakini kabla sijahitimisha, napenda niwashukuru tena kwa kunialika kwenye shughuli hii. Nawaahidi wafanyakazi wote nchi kuwa Serikali itaendelea kuboresha mazingira yenu ya kufanyia pamoja na maslahi yenu, kadri uwezo wa kufanya hivyo utakavyokuwa ukiongezeka.
Leo nimewaahidi kuwa tutaajiri watumishi wapya, tutaanza tena kupandisha vyeo na tutatoa nyongeza ya kawaida ya mshahara kwa watumishi katika mwaka ujao. Nimeagiza pia kuanzia sasa ni marufuku kwa mtumishi kuhamishwa kabla ya kulipwa fedha zake. Haya yote, tutayasimamia na kuyatekeleza ipasavyo.
Mungu Tubariki Wafanyakazi wa Tanzania!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Apr 26, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA SHEREHE ZA MIAKA 53 YA MUUNGANO UWANJA WA JAMHURI, DO...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan,
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa,
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Job Ndugai,
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
MheshimiwaProf. Ibrahim Juma, Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mzee Mwinyi na Mzee Kikwete, Marais Wastaafu wa Awamu ya Pili na Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Gharib Bilal,
Makamu wa Rais Mstaafu wa Tanzania;
Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu wa Tanzania mliopo;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi Wakuu Wastaafu, mkiongozwa na Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Mheshimiwa Jordan Rugimbana, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wabunge;
Waheshimiwa Mabalozi na Viongozi wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni waalikwa wote;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kuiona siku hii ya leo. Tunamshukuru pia kwa kuendelea kulilea taifa letu na kulifikisha salama hapa tulipo.
Aidha, napenda nitumie fursa hii kutuma salamu nyingi za pongezi kwa Watanzania wote kwa kuadhimisha Miaka hii 53 ya Muungano wetu na kuzaliwa taifa letu. Hakuna shaka, hii ni siku muhimu na ya kihistoria kwa taifa letu. Hivyo, kila Mtanzania, mahali popote alipo, hana budi kuifurahia na kujivunia.Hii ndio sherehe ya Birthday ya nchi yetu.
Ndugu wananchi, Mabibi na Mabwana:
Kama mnavyofahamu, siku kama ya leo Mwaka 1964 taifa jipya, la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilizaliwa. Taifa hili jipya lilizaliwa baada ya aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume, na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Tanganyika, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kutia saini Hati ya Muungano kuunganisha nchi hizi mbili na kuunda taifa moja.
Yapo mambo mengi yaliyowezesha kwa Muungano wetu. Jambo la kwanza ni niudugu wa kihistoria uliokuwepo baina ya wananchi wa mataifa yetu mawili. Kabla hata ya kuja kwa wakoloni, wananchi wa mataifa haya mawili walikuwa wakishirikiana kwenye masuala ya kiuchumi, kisiasa na kijamii. Kutokana naushirikiano huo, baadhi ya Watanganyika walilowea Zanzibar na walikuwepo Wazanzibari waliolowea Tanganyika. Hapana shaka, hii ndio sababu leo tunao akina Jaji Makungu. Uhusiano huu wa kidugu ndio ulirahisha mataifa yetu kuungana mara tu baada ya kupata uhuru wao.
Sababu ya pili iliyosababisha kuanzishwa kwa Muungano wetu ni uhusiano na ushirikiano mzuri uliokuwepo kati ya vyama vyetu vya ukombozi, kwanza kabisa wakati wa Tanganyika African Association (TAA) na African Association na baadaye TANU na ASP. Viongozi na wanachama wa vyama hivi viwili walikuwa na ushirikiano wa karibu. Walikuwa wanatembeleana, kubadilishana mawazo na kusaidiana kwa hali na mali. Hivyo, kutokana na uhusiano na ushirikiano mzuri uliokuwepo kati ya vyama hivi viwili, haikuwa jambo gumu kuunganisha mataifa haya mawili baada ya uhuru.
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Leo tunaposheherekea Sikukuu ya Muungano, sisi Watanzania ni lazima tutafakari mustakabali wa Taifa letu. Kama mnavyofahamu, wengi wa Watanzania wa sasa wamezaliwa baada ya Muungano. Tutumie basi sherehe hizi katika kutafakari mahali tulikotoka, mahali tulipo na kule tunakoelekea. Ni kwa namna hiyo tu tutaweza kuulinda na kuudumisha Muungano wetu.
Katika kipindi cha Miaka 53 ya Muungano wetu, nchi yetu imefanikiwa kupata mafanikio makubwasana. Nitataja makubwa matatu.Mosi, kwa kuunganisha Mataifa yetu mawili tumeweza kuunda Taifa moja lenye nguvu. Hii imetuwezesha kulinda uhuru amani na umoja wetu. Nchi yetu imebaki kuwa na amani na mipaka yetu ipo salama. Na tunajiamulia mambo yetu sisi wenyewe.
Pili, Muungano wetu umetuwezesha kupata mafanikio makubwa katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Serikali zetu mbili, yaani Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar, zimefanya jitihada kubwa za kukuza uchumi na kukabiliana na matatizo ya umaskini na ukosefu wa ajira. Tumejenga miundombinu ya usafiri wa anga, majini, reli na nchi kavu. Miradi ya umeme pia imejengwa.Aidha, tumeimarisha na kuboresha upatikanaji wa huduma za jamii. Idadi ya shule na hospitali zimeongezeka. Upatikanaji wa huduma za maji nazo zimeimarika. Demokrasia imepanuka. Kwa ujumla, naweza kusema kuwa Tanzania ya sasa sio ile ya mwaka 1964.
Tatu, nchi yetu inaheshimika kimataifa na inatoa mchango mkubwa katika ngazi ya Kanda, Bara na duniani kwa ujumla. Tumeshiriki katika harakati za ukombozi wa Bara letu na tunaendelea kushiriki kwenye shughuli za kutafuta amani sehemu mbalimbali duniani. Haya ni baadhi tu ya mafanikio. Yapo mengine mengi.
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Wahenga husema “usione vyaelea, vimeundwa”. Mafanikio niliyoyataja hayakujileta. Wapo watu ambao wamefanya kazi mchana na usiku kuhakikisha yanapatikana. Kama mnavyofahamu, kulinda Muungano kama wetu sio jambo rahisi. Yapo mataifa mengi yaliyojaribu lakini yameshindwa. Lakini wengi wetu hapa pia tunafahamu kuwa hata kulinda muungano wa ndoa kati ya watu wawili sio jambo rahisi. Hivyo basi, hatuna budi kuwapongeza wote waliowezesha nchi yetu kufikisha Miaka hii 53 ya Muungano.
Nafahamu wapo watu wengi waliotoa mchango wao, lakini kwa leo nitawataja wachache. Kwanza kabisa, napenda kwa niaba yenu, niwashukuru na kuwapongeza sana viongozi wetu wakuu waasisi, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Rais wa Kwanza wa Tanganyika na Sheikh Abeid Amani Karume, Rais wa Kwanza wa Zanzibar kwa kuwezesha Muungano huu. Kama nilivyosema, hawa ndio waasisi wa Muungano huu. Hawa ndio walisaini Hati za Muungano. Tunawashukuru sana Waasisi wetu hawa wawili; Bahati nzuri leo hapa tunao wajane wa waasisi hao, Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume ambao wamekuja kuungana nasi katika kusheherekea siku hii muhimu kwa taifa letu.
Sambamba nao, nawapongeza viongozi wetu waliowafuatia, wa awamu zote za Serikali zetu mbili, kwa uongozi wao bora uliowezesha Muungano wetu kudumu, kustawi na kuzidi kuimarika mpaka sasa. Nimefarijika sana kuwaona Marais Wastaafu Mzee Mwinyi na Mzee Kikwete; Mawaziri Wakuu Wastaafu, na viongozi wengine wastaafu tuko nao hapa. Wote kwa pamoja, tunawashukuru sana. Napenda kutumia fursa hii kuahidi kuwa mimi pamoja na mwezangu, Mheshimiwa Rais Dkt. Shein, tutafuata nyayo za viongozi waliotutangulia katika kuulinda na kuudumisha Muungano wetu.
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Licha ya mafanikio ya Muungano tuliyoyapata,ni dhahiri kuwa bado zipo changamoto. Lakini kwa bahati nzuri tunayo Kamati ya Pamoja inayoshughulikia masuala ya Muungano, ambayo Mwenyekiti wake ni Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Hassan Suluhu. Wajumbe wengine ni pamoja na Waziri Mkuu, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Serikali zote mbili. Kamati hii inafanya kazi nzuri sana, hata hivyo, hatupaswi kuiachia Kamati ifanye mambo yote. Ni lazima kila Mtanzania mahali popote alipo ahakikishe anafanya jitihada za kuuimarisha na kuulinda Muungano wetu.
Ni kwa sababu hii nimefurahishwa sana na kaulimbiu ya Sherehe za Muungano mwaka huu ambayo inasema “Miaka 53 ya Muungano: Tuulinde na Kuuimarisha, Tupige Vita Madawa ya Kulevya na Kufanya Kazi kwa Bidii”. Kaulimbiu hii ni muafaka na imekuja kwa wakati. Kila Mtanzania anao wajibu wa kulinda Muungano wetu. Na njia bora ya kuulinda na kuuimarisha Muugano wetu ni kuchapa kazi kwa bidii.
Waheshimiwa Viongozi na Wageni Waalikwa;
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Kabla sijahitimisha hotuba yangu hii fupi, ninayo masuala mawili ningependa kugusia. Mosi, hii nimara ya kwanza katika historia ya Muungano wetu, Maadhimisho ya Muungano yanafanyika hapa Dodoma, Makao Makuu ya nchi yetu. Hii ni ishara tosha kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Chama Cha Mapinduziimedhamiria kwa dhati kabisa kuhamishia Makao Makuu ya Serikali hapa Dodoma. Na niwahakikishie wana-Dodoma na Watanzania kwa ujumla kuwa, kama tulivyoahidi, ifikapo mwaka 2020, Serikali yote itakuwa imehamia Dodoma.
Bahati nzuri, hatua za kuhamia Dodoma tayari zimeanza. Viongozi Wakuu wa Wizara zote, yaani Mawaziri, Naibu Mawaziri; Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na baadhi ya Wakurugenzi na watumishi wameshahamia hapa Dodoma. Zaidi ya watumishi 3,000 nao wameshahamia. Awamu ya Pili na Tatu ya kuhamia Dodoma imepangwa kutekelezwa mwaka ujao wa fedha, ambapo Serikali imetenga takriban shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kujenga ofisi na nyumba za viongozi wa Serikali. Natumaini Bunge litapitisha Bajeti hiyo. Sambamba na hilo, tunaendelea na jitihada za kujenga miundombinu ya usafiri ya kuja na kutoka hapa Dodoma. Tumeshapanua uwanja wa ndege (na tutaendelea kuupanua) na hivi majuzi nimeweka Jiwe la Msingi la kuanza ujenzi wa Reli ya Kati ya kisasa ambayo itapita hapa Dodoma. Tunaendelea na ujenzi wa barabara mbalimbali na tuna mipango kabambe ya kuboresha upatikanaji wa umeme na maji pamoja na huduma za afya na elimu. Maandalizi ya ujenzi wa Uwanja wa Michezo wa Kisasa kwa ufadhili wa Serikali ya Morocco yanaendelea vizuri.
Tunachukua hatua hizi zote kuufanya mji huu wa Dodoma ukidhi mahitaji ya kuwa Makao Makuu ya Serikali. Hivyo basi, niwaombe wakazi wa Dodoma pamoja na Mikoa jirani ya Singida, Arusha, Iringa na Morogoro kujipanga vizuri kutumia fursa zitakazotokana na uamuzi wa kuhamishia Makao Makuu hapa Dodoma.
Jambo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ni kuhusu umuhimu wa kudumisha amani yetu. Tumeweza kufikisha miaka 53 ya Muungano kwa sababu ya kuwepo kwa amani. Na tumeweza kupata mafanikio yote niliyoyataja kwa sababu ya uwepo wa amani hapa nchini. Bila ya amani, mambo yote haya yasingewezekana. Hivyo basi, kila Mtanzania ni lazima ashiriki katika kulinda na kudumisha amani yetu.
Waheshimiwa Viongozi na Wageni Waalikwa;
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kutoa shukrani kwa Kamati ya Maandalizi kwa kufanikisha Maadhimisho haya. Maadhimisho yamefana. Uwanja umefurika na bado nje kuna watu wengi . Hongereni sana wana-Kamati.
Napenda pia kuwashukuru wageni wetu waalikwa waliokuja hapa kushiriki nasi katika shughuli hii muhimu na kihistoria kwa taifa letu.Tunawashukuru Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali za Kimataifa.
Tunavishukuru vyombo vya ulinzi na usalama, vikundi vya burudani, chipukizi na waandishi wa habari kwa kufanikisha sherehe hii. Napenda pia kutoa shukrani nyingi kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma, chini wa kiongozi wenu Mheshimiwa Rugimbana, kwa kutukaribisha vizuri kwenye Mkoa wenu. Mmedhihirisha kuwa hapa kweli ni Makao Makuu ya Nchi yetu.
Ndugu Watanzania wenzangu, Muungano wetu ndio umoja wetu; ndio nguvu yetu na silaha yetu. Hivyo basi, hatuna budi kuulinda na kuudumisha. Kwa sababu hiyo, napenda kurudia tena kuwa mimi na mwenzangu, Mheshimiwa Rais Shein, tutaulinda kwa nguvu zetu zote. Yeyote atakayejaribu kuuvunja Muungano wetu, atatangulia kuvunjika yeye kwanza.
Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Wabariki Watanzania!
“Ahsanteni Sana kwa kunisikiliza

- Apr 20, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA SHEREHE YA UWEKAJI WA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA INTE...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Jim Yong Kim, Rais wa Benki ya Dunia;
Mheshimiwa Profesa Makame M. Mbarawa (Mb),
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Balozi Mhandisi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam;
Mheshimiwa Prof. Norman Adamson Sigalla, Mwenyekiti
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu;
Waheshimiwa Wabunge na Madiwani wote mliopo;
Mheshimiwa Mama Bella Bird, Mwakilishi Mkazi wa Benki
ya Dunia Tanzania, Burundi, Malawi na Somalia;
Watendaji Wakuu wa TANROADS;
Viongozi wa Serikali, Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutukutanisha hapa tukiwa wazima. Aidha, napenda kutoa shukrani nyingi sana kwa Mheshimiwa Dkt. Jim Yong Kim, Rais wa Benki ya Dunia kwa kuja kutembelea. Kama inavyofahamika, Benki ya Dunia ni taasisi muhimu duniani; hivyo, kutembelewa na kiongozi wake ni jambo la heshima kubwa kwa nchi yetu. Tunamshukuru sana Dkt. Kim na tumefurahi kujumuika naye katika hafla hii ya kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Barabara za Juu (interchange) hapa Ubungo. Ujio wake hapa nchini ni ishara tosha kuwa anaipenda nchi yetu; na kwamba yeye ni rafiki wa kweli wa Watanzania.
Sisi Waswahili tuna usemi wetu usemao: “Mwenyeji njoo, mgeni apone”. Napenda kutumia fursa hii kuwaarifu Watanzania wenzangu kuwa ziara ya Mheshimiwa Dkt. Kim hapa nchini imekuwa ya mafanikio makubwa kwa nchi yetu. Imeleta neema kwa nchi yetu. Wakati wa mazugumzo yetu leo asubuhi nimemweleza mipango yetu mbalimbali na yeye amekubali kushirikiana nasi katika kuitekeleza. Tunamshukuru sana.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ni jambo lililodhahiri kuwa moja ya kero kubwa kwenye Jiji letu la Dar es Salaam, lenye wakazi wapatao milioni tano, ni suala la msongamano wa magari barabarani. Kwa kutambua hilo, mtakumbuka wakati wa kampeni, Chama changu kiliahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza jitihada zilizoanzishwa na Serikali zilizotangulia katika kushughulikia kero hiyo. Nafurahi utekelezaji wa ahadi hiyo, unaendelea vizuri. Tayari mambo mengi yamefanyika. Mara tu baada ya kuingia madarakani tulijenga barabara ya kilometa 4.3 kutoka Morocco hadi Mwenge, kwa kutumia fedha zilizopangwa kugharamia Sherehe za Uhuru. Aidha, mwaka jana mwezi Aprili tuliweka Jiwe la Msingi la Barabara ya Juu (flyover) pale TAZARA na pia kuzindua Daraja la Nyerere (maarufu kama Daraja la Kigamboni). Aidha, barabara ya Dar es Salaam, Bagamoyo hadi Msata nayo imekamilika na hivyo imepunguza msongamano katika barabara ya Dar es Salaam-Chalinze. Hakuna shaka, uamuzi wetu wa kuhamia Dodoma nao umesaidia kupunguza foleni hapa Dar es Salaam.
Kama hiyo haitoshi, tarehe 25 Januari mwaka huu, tulifanya uzinduzi wa Mradi wa Usafiri wa Mwendokasi Awamu ya Kwanza. Mradi huo umehusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 20.9 kutoka Kivukoni kwenda Kimara, Morocco na Gerezani. Tayari tumeanza kuona manufaa ya mradi huo. Hivi sasa watu wanatumia wastani wa dakika 45 kutoka Kivukoni hadi Kimara, wakati awali, walikuwa wakitumia masaa mawili hadi matatu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Licha ya mafanikio yaliyopatikana katika Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Mwendokasi, mtakubaliana nami kuwa mradi huo unakabiliwa na tatizo kubwa hapa Ubungo. Kama mnavyofahamu, hapa Ubungo ndio lango kuu la usafiri wa barabara kwa nchi yetu. Magari mengi ya kwenda na kutoka mikoani pamoja na nchi jirani hupita hapa na hivyo kusababisha msongamano mkubwa wa magari katika eneo hili. Hata magari ya mwendokasi nayo yakifika hapa yanakwama.
Ni kutokana na kero hiyo, mtakumbuka kuwa siku ya uzinduzi wa usafiri wa mwendokasi, tukiwa pamoja na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia Kanda ya Afrika, Dkt. Mukhtar Diop, nilihimiza ukamilishaji wa majadiliano kuhusu ujenzi wa barabara za juu (interchange) hapa Ubungo. Nafurahi, baada ya kama miezi miwili tu kupita, leo tupo hapa kusaini Mkataba wa Mkopo na kuweka Jiwe la Msingi la mradi huo. Nimefarijika sana na nawashukuru wote waliowezesha mradi huu kuanza kutekelezwa.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Mradi huu wa interchange hapa Ubungo ni mkubwa na wa aina yake katika nchi yetu. Utahusisha ujenzi wa barabara za juu za ghorofa tatu; na utakapokamilika, unatarajiwa kuondoa kabisa kero ya msongamano wa magari katika eneo hili. Magari kutoka njia zote nne yatapita hapa bila kusimama na hivyo kurahisisha sio tu huduma ya usafiri wa mwendokasi bali kwa watumiaji wote wa barabara katika eneo hili. Sambamba na hilo, mradi huu utaboresha mandhari ya Jiji letu la Dar es Salaam, ambalo ni miongoni mwa Majiji yanayokua kwa kasi Barani Afrika.
Kwa sababu hiyo, napenda nitumie fursa hii, kwa niaba ya Watanzania wote, kuishukuru sana Benki ya Dunia kwa kutupatia mkopo wa kutekeleza mradi huu. Aidha, namshukuru tena Dkt. Kim pamoja na Mwakilishi wa Benki ya Dunia hapa nchini Mama Bird, kwa kubali kushiriki kwenye hafla hii. Kama alivyosema Mheshimiwa waziri, mradi huu utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 188.71. Kati ya fedha hizo, Benki ya Dunia itatoa takriban shilingi bilioni 186.725 kwa ajili ya usanifu, usimamizi na ujenzi wa mradi. Serikali imetoa shilingi bilioni 1.985 kwa ajili ya fidia kwa wananchi wanaostahili kulipwa kwa mujibu wa sheria.
Lakini niseme tu kwamba huu sio mradi wa kwanza kufadhiliwa na Benki ya Dunia hapa nchini. Wamefadhili miradi mingi. Hivi sasa Benki ya Dunia inafadhili jumla miradi 28 hapa nchini yenye thamani ya takriban Dola za Marekani bilioni 4.2. Baadhi ya miradi hiyo ni mradi wa maboresho ya usafiri wa reli; mradi wa maboresho ya mahakama; mradi wa kupeleka umeme vijijini; mradi wa maboresho ya Vyuo Vikuu vya Sokoine na Nelson Mandela; mradi wa TASAF; na pia mradi wa maboresho wa elimu ya msingi.
Mbali na miradi hiyo, muda mfupi tu ujao tutasaini mikataba ya kupata mkopo kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kutekeleza miradi mingine mipya mitatu. Miradi hiyo ni :
(i) Mradi wa Ujenzi wa Miundombinu ya Usafiri katika Jiji la Dar es Salaam (Dar es Salaam Urban Transport Project). Mradi huu, ambao thamani yake ni Dola za Marekani milioni 425, utahusisha ujenzi wa Interchange hii hapa Ubungo pamoja na miundombinu ya usafiri wa mwendokasi kwa Awamu ya Tatu na Nne;
(ii) Mradi wa Usambazaji Maji safi pamoja na Utunzaji Mazingira na ukusanyaji wa maji taka wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 225. Tunataka kumaliza kabisa suala la maji hapa Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla; na
(iii) Mradi wa Kuboresha huduma katika miji ya Arusha, Dodoma, Kigoma, Mbeya, Mwanza na Mtwara wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 130.
Hii inafanya jumla ya mkopo tutakaopata leo kuwa na thamani ya Dola za Marekani milioni 780, sawa na takriban shilingi trilioni 1.74. Lakini kuna miradi mingine ambayo ipo njiani kuanza kutekelezwa yenye thamani ya takriban Dola za Marekani bilioni 1.284 ambayo ni sawa na shilingi trilioni 2.79. Miradi hiyo ni pamoja na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam (USD milioni 345); mkopo kwa TANESCO (USD milioni 200); upanuzi wa mradi wa gesi (USD milioni 100); kilimo (USD milioni 100); elimu (USD milioni 224); na afya (USD milioni 200) na mkopo kwa Zanzibar (USD milioni 35). Mikopo hii inadhihirisha sio tu kuwa Benki ya Dunia ni washirika wetu wakubwa wa maendeleo, bali pia nchi yetu inakopesheka. Ndiyo, tunakopesheka. Tungekuwa hatukopesheki, Benki ya Dunia isingetupatia kiasi hiki kikubwa cha fedha. Napenda nimhakikishie Rais wa Benki ya Dunia kuwa tutalipa deni letu, hasa kwa kuzingatia kuwa masharti yao ni nafuu.
Wageni Waalikwa,
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kupunguza kama sio kumaliza kabisa kero ya foleni za magari hapa Dar es Salaam. Mbali na ujenzi miundombinu ya usafiri wa mwendokasi, tumepanga kutekeleza miradi mingine ya miundombinu ya usafiri. Baadhi ya miradi hiyo ni ujenzi wa Daraja la kupita juu ya bahari kutoka Aga Khan hadi Coco Beach lenye urefu wa kilometa 7 kwa mkopo kutoka Korea Kusini; ujenzi wa barabara za njia sita za kutoka Ubungo hadi Chalinze; na ujenzi wa barabara za juu kwenye maeneo ya Mwenge, Morocco, Magomeni na Tabata. Aidha, tupo kwenye maandalizi ya ujenzi wa babaraba za lami za mzunguko (Dar es Salaam Outer Ring Road) zenye urefu wa kilometa 34. Na katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/17, Serikali imetenga fedha za ndani Shilingi billioni 38 kwa ajili ya kuboresha barabara za Jiji hili.
Sambamba na ujenzi wa miundombinu ya barabara, tunao mpango kabambe wa kuboresha huduma za usafiri wa reli katika Jiji la Dar es Salaam. Aidha, ujenzi wa Reli ya Kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) nao unatarajiwa kupunguza tatizo la msongamano wa magari hapa Dar es Salaam. Hii ni kwa sababu mradi huo utahusisha pia ujenzi wa Kituo Kikubwa cha kupokea Mizigo pale Ruvu. Kituo hicho kikikamilika, magari ya mizigo hayataruhusiwa tena kuja Dar es Salaam kufuata mizigo Bandarini. Hivyo basi, tuna matumaini makubwa kuwa, kutokana na ujenzi wa miundombinu unaoendelea, muda mfupi ujao, suala la msongamano barabarani litakuwa historia hapa Dar es Salaam.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana ;
Kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba nieleze masuala matatu ya mwisho. Jambo la kwanza ni kuhusu usimamizi wa mradi. Napenda kutoa wito kwa Wasimamizi wa Mradi huu kuhakikisha wanamsimamia ipasavyo Mkandarasi ili mradi huu ukamilike kwa viwango vinavyohitajika na ikiwezekana kabla ya wakati uliopangwa. Fedha zipo. Hivyo, hakuna sababu mradi huu kuchukua muda mrefu kutekelezwa. Watanzania wanausubiri kwa hamu mradi huu. Sambamba na hilo, nawasihi watu watakaopata kazi kwenye mradi huu kuwa waaminifu na wazalendo. Msiibe vifaa wala kuanzisha migomo isiyokuwa na sababu.
Jambo la pili, mradi huu unajengwa kwa gharama kubwa. Fedha zitakazotumika ni za mkopo na hivyo Serikali italazimika kuzilipa. Hivyo basi, niwaombe Watanzania wenzangu tuendelee kulipa kodi. Kodi ndiyo itakayowezesha Serikali kupata fedha sio tu kwa ajili ya kurejesha mkopo wa mradi huu, bali pia kutekeleza miradi mingine mbalimbali ya maendeleo.
Suala la tatu na la mwisho ambalo napenda kuwaeleza Watanzania wenzangu ni kwamba, tujitahidi kuelekeza nguvu zetu kwenye masuala ya msingi yenye maslahi kwa nchi yetu. Nchi yetu inahitaji kuondokana na umasikini. Inahitaji kuwa na viwanda. Na sote hapa tunahitaji maendeleo. Haya ndiyo mambo yanapaswa yatuchukulie muda wetu mwingi kuyajadili. Tusipoteze muda kujadili mambo yasiyo na msingi, ambayo hayatupi majibu ya changamoto zinazotukabili.
Nafahamu mnao uhuru wa kujadili mnachopenda lakini huo ndio ushauri wangu kwenu. Nchi yetu inahitaji maendeleo. Tunapaswa sote tushirikiane katika kuijenga nchi yetu. Hii ndio sababu nimefurahi sana leo hapa tunao viongozi wa vyama mbalimbali. Hivi ndivyo inavyotakiwa. Maendeleo hayana Chama. Sote tukishirikiana nchi yetu itapiga hatua kimaendeleo na kuwa mfano wa kuigwa Barani Afrika.
Mheshimiwa Dkt. Kim;
Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Napenda kuhitimisha kwa kumshukuru tena Rais wa Benki ya Dunia kwa kuja kuungana nasi katika hafla hii na pia kwa misaada mbalimbali ambayo Benki ya Dunia imekuwa ikitoa kwa nchi yetu. Napenda nimhakikishie kuwa fedha zote wanazozitoa zitatumika kwa malengo yaliyokusudiwa. Hakuna fedha itakayopotea.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu napenda kuishukuru Wizara ya Ujenzi pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu mbalimbali iliyowezesha kuanza utekelezaji wa mradi huu. Ahsanteni sana.
Baada ya kusema hayo, sasa niko tayari kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Barabara za Juu (interchange) hapa Ubungo.
Mungu Wabariki Wana-Dar es Salaam!
Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu bariki mahusiano kati ya Tanzania na Benki ya Dunia!
“Asanteni Sana kwa Kunisikiliza”.

- Apr 12, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UWEKAJI JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA RELI YA KATI KWA K...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa,
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Waheshimiwa Mawaziri na Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Yesamin Eralp, Balozi wa Uturuki nchini;
Mheshimiwa Mama Bella Bird, Mwakilishi wa Benki ya Dunia
nchini Tanzania, Burundi, Malawi na Somalia;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Mstahiki Meya na Waheshimiwa Madiwani mliopo;
Ndugu Viongozi wa Serikali, Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya njema na kutuwezesha kukutana hapa kushuhudia uwekaji Jiwe la Msingi la Mradi wa Reli ya Kati kwa Kiwango cha Kimataifa (Standard Gauge). Aidha, namshukuru Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Prof. Mbarawa pamoja na uongozi mzima wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kunialika ili nishiriki nanyi katika shughuli hii muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru kwa dhati kabisa wana-Pugu. Hii ni mara yangu ya kwanza kuzungumza nanyi tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa nchi yetu. Hivyo basi, nawashukuru kwa kura zenu nyingi mlizonipigia. Nawaahidi kufanya kazi kwa bidii kwa manufaa ya Watanzania wote.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 yapo mambo tuliahidi. Yalikuwa mengi lakini moja wapo ilikuwa ni kuimarisha miundombinu ya usafiri. Ahadi ni deni. Nafurahi leo tupo hapa kushuhudia uwekaji Jiwe la Msingi la Mradi huu wa reli. Hakuna shaka, tukio hili ni la kihistoria kwa nchi yetu.
Kama mnavyofahamu, nchi yetu kwa sasa inazo njia mbili kuu za usafiri wa reli. Reli ya Kati, ambayo sehemu yake kubwa, ilijengwa enzi za ukoloni wa Ujerumani na Uingereza kati ya mwaka 1899 hadi 1929. Na Reli ya TAZARA iliyojengwa kwa ufadhili wa Serikali ya China mwanzoni mwa miaka ya 1970, ambayo inatuunganisha na ndugu zetu wa Zambia. Hivyo basi, reli hii mpya tunayotaka kuijenga itakuwa ya tatu. Hili ni jambo la kihistoria kwa nchi yetu na hasa kwa kuzingatia kuwa mipango na mikakati yote ya kuijenga reli hii tumeibuni sisi wenyewe. Na hata utekelezaji wake, tumejipanga kuusimamia wenyewe, ingawa tunawakaribisha washirika mbalimbali kuja kushirikiana nasi.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ujenzi wa reli hii una umuhimu wa pekee na manufaa mengi kwa nchi yetu. Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ametaja baadhi ya manufaa yatakayoletwa na reli hii. Lakini naomba mniruhusu nirudie kutaja kwa uchache baadhi ya manufaa:
(i) Kwanza kabisa, reli hii itarahisisha usafiri wa mizigo na abiria hapa nchini na kwenda nchi jirani za Burundi, Rwanda, DRC, Uganda na Sudan Kusini. Kama mnavyofahamu, reli hii inajengwa kuanzia hapa Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Mwanza na Kigoma na baadaye inatarajiwa kuelekea nchi za Burundi na Rwanda. Na kwa kuwa Kigoma na Mwanza ni karibu na nchi za DRC, Uganda na Sudan Kusini, itarahisisha usafiri kwenda nchi hizo pia.
(ii) Pili, reli hii itakuza biashara kati ya nchi yetu na nchi hizo nilizozitaja. Moja ya kikwazo kikubwa cha biashara miongoni mwa nchi za Afrika ni ukosefu au ubovu wa miundombinu ya usafiri. Ukosefu/ubovu wa miundombinu ya usafiri unakadiriwa kuongeza gharama za biashara kwa asilimia 40 Barani Afrika. Hii ndio sababu mchango wa Bara la Afrika kwenye biashara duniani (Africa’s share in the global trade) ni chini ya asilimia 5. Na hii ndiyo sababu pia biashara miongoni mwa nchi za Afrika (intra-African trade) ni chini ya asilimia 15, wakati kwenye Mabara mengine ni kati ya asimilia 40 na 60. Hivyo, kwa kujenga reli hii, biashara kati ya nchi yetu na mataifa mengine itaongezeka maradufu.
(iii) Tatu, ujenzi wa reli hii utakuza sekta nyingine za uchumi nchini. Kama mnavyofahamu, ustawi wa sekta za viwanda, kilimo, ufugaji, uvuvi, madini na utalii hutegemea sana kuwepo kwa usafiri wa uhakika. Mathalan, reli hii itakapokamilika itawezesha malighafi kama vile pamba, samaki, ngozi, nyama, maziwa, madini, mbao, asali, n.k, kusafirishwa kutoka maeneo yanakozalishwa kwenda kwenye maeneo ya viwanda. Na bidhaa zitakazozalishwa viwandani zitafika kwenye masoko kwa wakati. Reli hii pia itakuza utalii. Kama mtakumbuka, miezi kama miwili au mitatu iliyopita, mlishuhudia watalii kutoka Afrika Kusini wakija hapa Dar es Salaam kwa kutumia reli ya TAZARA. Hivyo, reli hii ikikamilika, mtalii ataweza kutoka nchini Afrika Kusini hadi Mikoa ya Kigoma na Mwanza.
(iv) Nne, ujenzi wa reli hii utasaidia kutunza barabara zetu. Kama mnavyofahamu, nchi yetu imepiga hatua kubwa katika kujenga barabara. Zaidi ya kilometa 17,000 zimejengwa na binafsi nafurahi nilishiriki katika ujenzi wa barabara hizo. Lakini barabara zetu nyingi zinaharibika ndani ya muda mfupi kutokana na kutumika kusafirishia mizigo mizito. Tafiti nyingi zimethibitisha kuwa usafiri wa reli ndio sahihi katika kusafirisha mizigo mikubwa. Una gharama nafuu na unawezesha kusafirisha mzigo mkubwa umbali mrefu kwa kipindi kifupi. Mathalan, treni zitakazotumia reli hii zitaweza kusafirisha mzigo wa tani 10,000 kwa mara moja sawa na malori ya semi-trella 500 yenye uwezo wa kubeba tani 20 kila moja. Hivyo basi, hii itasaidia sana kutunza barabara zetu.
(v) Tano,ujenzi wa reli hii utaongeza upatikanaji wa ajira nchini. Kama alivyosema Mheshimiwa Waziri, inakadiriwa kuwa, wakati wa ujenzi wa reli hii, takriban watu laki sita watapata ajira, wakiwemo 30,000 ambao watapata ajira za moja kwa moja. Aidha, reli hii itakapokamilika, inatarajiwa kutoa ajira takriban milioni moja kupitia viwanda na kukua kwa sekta nyingine za kiuchumi, ikiwemo kilimo, ufugaji, uvuvi, uchimbaji madini, utalii, nk.
Hizi ni baadhi tu ya faida zitakazopatikana kutokana na ujenzi wa reli hii. Zipo nyingine nyingi. Hivyo basi, niwasihi Watanzania wenzangu kujipanga ili kuweza kunufaika na mradi huu.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ujenzi wa reli hii yenye urefu kilometa 1,219 umegawanywa kwenye vipande vitano. Kipande cha kwanza ni hiki ambacho nitaweka Jiwe la Msingi hivi punde. Kipande hiki kinahusisha ujenzi wa njia kuu ya reli kutoka hapa Dar es Salaam hadi Morogoro yenye urefu wa kilometa 205 pamoja na kilometa 95 kwa ajili ya njia za kupishana na maeneo kupangia mabehewa; na hivyo kufanya jumla yake kuwa kilometa 300. Aidha, awamu hii itahusisha ujenzi wa stesheni 6 na Yadi kubwa ya kupanga mabehewa pale Ruvu mkabala na Bandari Kavu ya Mamlaka ya Bandari na hivyo itapunguza msongamano wa magari hapa
Reli hii itakuwa ya kisasa kabisa na yenye uwezo mkubwa. Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Mkurugenzi Mkuu wa RAHCO wameeleza kuwa injini za treni katika reli hii zitatumia umeme na dizeli. Mwendokasi wake utakuwa kilometa 160 kwa saa kwa treni za abiria na kilometa 120 kwa saa kwa treni za mizigo. Reli hii itakuwa na uwezo wa kuhimili uzani wa tani 35 kwa ekseli. Ujenzi wa kipande hiki cha kwanza unatarajiwa kuchukua miezi 30, sawa na miaka miwili na nusu.
Gharama za ujenzi za kipande hiki cha kutoka Dar es Salaam ni Dola za Marekani milioni 1.22 sawa na shilingi trilioni 2.8. Katika bajeti ya mwaka huu wa fedha (2016/2017), Serikali imetenga shilingi trilioni 1 kuanza kugharamia. Nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kupitisha bajeti ya kuanza ujenzi wa reli hii. Na haya ndio majibu kwa baadhi ya watu wanaodai kuwa Serikali imeshindwa kutekeleza bajeti ya maendeleo katika mwaka huu wa fedha kwa kukosa fedha. Hii sio kweli. Fedha tunazo. Lakini ni vyema ikaeleweka kuwa wakati mwingine Serikali inashindwa kutoa fedha ya kutekeleza miradi ya maendeleo kwa vile maandalizi yanakuwa bado kukamilika. Mathalan, fedha za mradi huu zilikuwepo tangu mwezi Julai mwaka jana. Lakini Mkandarasi, kampuni ya Yapi Merkezi ya Uturuki na Mota-Engil ya Ureno, tumewekeana naye saini mwezi Februari 2017. Sasa Serikali ingewezaje kutoa fedha wakati Mkandarasi alikuwa bado kupatikana? Sasa Mkandarasi amepatikana na tayari tumeshamlipa kiasi cha shilingi bilioni 300.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Baada ya kumpata Mkandarasi na kuanza ujenzi wa kipande hiki cha Dar es Salaam, sasa Serikali inaelekeza nguvu katika vipande vilivyobaki vya Marogoro - Makutopora (km. 336), Makutopora – Tabora (km. 294), Tabora – Isaka (km. 133) na Isaka – Mwanza (km. 248). Zabuni za usanifu na kujenga tayari zimetangazwa na zinatarajiwa kufunguliwa mwanzoni mwa mwezi ujao.
Ninayo furaha kuarifu kuwa wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki hapa nchini mwezi Januari 2017, aliahidi kutusaidia kupata fedha kwa ajili ya kujenga kipande cha kutoka Morogoro hadi Dodoma. Na mpaka sasa wawakilishi wa Mabenki takriban matano kutoka Uturuki wameshakuja nchini kwa ajili ya kufanya mazugumzo ili watupatie mkopo nafuu wa kujenga kipande hicho. Lakini pia alipokuja Rais wa Benki ya Dunia hapa nchini mwezi uliopita (Machi 2017) alionesha nia ya kutusaidia kupata fedha za kutekeleza mradi huu pamoja na kutupatia mkopo wenye thamani ya shilingi bilioni 300 kukarabati reli ya zamani. Nimefurahi hapa leo tunaye Mwakalishi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini, Mama Bird, ambaye naamini ataendelea kuwakumbusha viongozi wake ili kutupatia mkopo huo.
Kama mnavyofahamu, reli ya kati tunayoitumia sasa bado ni muhimu. Tutaendelea kuitumia kusafirisha mizigo na abiria. Aidha, vifaa vya ujenzi wa reli hii mpya vitasafirishwa kupitia reli yetu hii ya sasa. Na hata ujenzi wa reli mpya utakapokamilika, reli ya zamani itaendelea kuitumia. Hii ni kwa sababu, reli mpya ya standard gauge tunayoijenga itakuwa na stesheni 28 tu kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza. Reli ya kati inayotumika sasa ina stesheni 67. Hivyo, itaendelea kuhitajika kutoa huduma kwenye maeneo ambayo reli mpya haitakuwa na stesheni.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ni dhahiri kuwa hatua hizi tulizoanza kuzichukua ni nzuri na kila Mtanzania hana budi kujivunia. Hata hivyo, nafahamu kuwa wapo baadhi ya wenzetu ambao wanabeza hatua hizi. Kubeza kwao kusitukatishe tamaa. Tukumbuke tu kuwa safari ya maendeleo. Safari ya maendeleo inafanana sana na usafiri wa lori. Madereva wa malori wanafahamu kuwa ukibeba abiria ni kawaida kumwona kila mmojawapo anaangalia upande wake, lakini watakuwepo pia wenye kuongea, kuimba na kukaa kimya. Dereva mzuri huwa hajishughulishi sana kuwaangalia au kuwasikiliza abiria hao. Yeye atajitahidi sana kuangalia mbele lori linakoelekea ili awafikisha abiria wake salama. Hivyo basi, napenda niwahakikishie Watanzania wenzangu kuwa mimi ni dereva mzuri. Ninafahamu ninakoelekea na nitawawafikisha salama. Na dalili zimeanza kujionesha.
Jana Benki ya Dunia imetoa Ripoti yake ambayo imetaja nchi yetu kuwa miongoni mwa nchi tano zinazofanya vizuri kiuchumi Barani Afrika. Hii ni ishara tosha kuwa tunaelekea sehemu nzuri. Lakini hata ninyi wana-Dar es Salaam ni mashahidi kuwa tunaendelea. Mwezi uliopita tumeweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Barabara za Juu (interchange) pale Ubungo. Tunajenga nyingine pale TAZARA. Aidha, baada ya kukamilisha ujenzi wa Awamu ya Kwanza wa Barabara za Mwendokasi, tumefanikiwa kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa Awamu ya Pili hadi ya Nne, ambapo Awamu ya Tatu itahusisha barabara ya kutoka maeneo ya huku, hapo Gongo la Mboto, kupita Barabara za Nyerere, Uhuru, Bibi Titi, Mitaa ya Azikiwe na Maktaba zenye jumla ya urefu wa kilometa 23.6. Mipango ya kuanza ujenzi wa Daraja la kupita juu ya bahari kutoka Aga Khan hadi Coco Beach, ujenzi wa barabara za njia sita za kutoka Ubungo hadi Chalinze inaendelea vizuri. Aidha, katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga shilingi bilioni 38 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za lami za mzunguko (Dar es Salaam Outer Ring Road) zenye urefu wa kilometa 34.
Lakini sio hivyo tu. Kwenye usafiri wa anga, tumenunua ndege mpya sita, mbili zimeshawasili na kuanza kufanya kazi. Ndege nyingine zinatarajiwa kuwa zimewasili mapema mwakani, ikiwemo ndege kubwa moja aina Boeing 787 Dreamliner yenye uwezo wa kubeba watu 262. Tunaendelea pia na ukarabati wa viwanja vya ndege sehemu mbalimbali nchini, ikiwemo Dodoma, Iringa, Mwanza, Mtwara, Kigoma, Songea, n.k. Haya ndiyo mambo Chama Cha Mapinduzi kiliwaahidi Watanzania wakati wa kampeni. Tutaendelea kuyasimamia na kamwe hatutamruhusu mtu yeyote kutuyumbisha na kututoa katika agenda zetu za maendeleo.
Mheshimiwa Wazi wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kabla sijahitimisha hotuba yangu, ninayo masuala mawili ya mwisho ambayo ningependa kueleza. Jambo la kwanza ni kuhusu usimamizi wa mradi. Nawasihi sana Wasimamizi wa Mradi huu kuusimamia ipasavyo mradi huu ili ukamilike kwa wakati na viwango vinavyohitaji. Aidha, natoa wito kwa Mkandarasi kuonesha umahiri wake, ikiwezekana mradi huu umalizike kabla ya muda uliopangwa. Fedha zipo, hivyo, hakuna sababu ya mradi huu kuchelewa kukamilika kwa mradi huu. Watanzania wanausubiri kwa hamu kubwa. Sambamba na kuwahimiza Wasimamizi na Mkandarasi, nawasihi sana Watanzania wenzangu watakaopata fursa za kufanya kazi kwenye mradi huu kuwa wazalendo na waaminifu. Tusiibe vifaa wala kuanzisha migomo isiyo na msingi.
Jambo la pili, napenda kutoa shukrani zangu nyingi kwa Kamati za Bunge zinazosimamia masuala ya Bajeti na Miundombinu kwa kazi nzuri zinazofanya. Tunawashukuru kwa kupitisha bajeti ya kuanza ujenzi wa reli hii. Natumaini katika mwaka huu pia mtapitisha bajeti kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa mradi huu. Watanzania wanahitaji maendeleo. Maendeleo hayana chama.
Baada ya kusema hayo, sasa niko tayari kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Reli Mpya ya Kisasa (Standard Gauge) kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro.
Mungu Wabariki Wana-Dar es Salaam!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Asanteni Sana kwa Kunisikiliza”.

- Mar 12, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT.JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI WA CHAMA CHA MAPINDUZI WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Makamu Mwenyekiti wa CCM - Zanzibar;
Mzee Philip Mangula, Makamu Mwenyekiti wa CCM- Tanzania Bara;
Ndugu Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM;
Ndugu Viongozi Wastaafu wa CCM;
Wajumbe wa Kamati Kuu;
Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa;
Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM;
Wageni Waalikwa, Viongozi wa Vyama Rafiki;
Ndugu Wana-CCM Wenzangu;
Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutukutanisha hapa tukiwa wazima. Aidha, nawashukuru ninyi wajumbe wa Mkutano Mkuu kwa kuja kwa wingi kuhudhuria Mkutano huu. Hii inathibitisha kuwa mtambua wajibu wenu na kuthamini umuhimu wa Mkutano huu. Nafahamu kuwa baadhi yenu mmesafiri umbali mrefu kuja hapa Dodoma kuhudhuria Mkutano huu; hivyo nawapa pole ya safari.
Napenda pia kutumia fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kuwashukuru Wajumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya iliyowezesha tukutane hapa leo. Lakini kwa namna ya pekee kabisa, nawashukuru watendaji wa Chama chetu wakiongozwa na jembe letu, Komredi Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa Chama, kwa maandalizi ya Mkutano huu. Maandalizi ni mazuri sana. Hongereni na ahsanteni sana.
Ndugu Wana-CCM Wenzangu;
Kama mnavyofahamu, tarehe 5 mwezi Februari mwaka huu, Chama chetu kilitimiza miaka 40 tangu kilipozaliwa. Miaka 40 sio muda mfupi. Ni kipindi kirefu. Na katika kipindi chote hicho, Chama chetu kimeshika hatamu ya uongozi wa Taifa letu. Kimeweza kusimamia vizuri amani, umoja na mshikamano wa Taifa letu. Na pia kimewaongoza Watanzania katika harakati za kujiletea maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa. Hayo, bila shaka, ni mafanikio makubwa. Hivyo basi, sisi wana-CCM tunapaswa kujipongeza. Tuzidi kumwomba Mungu na kufanya kazi kwa bidii ili Chama chetu kiendelee kudumu na kubaki madarakani milele daima. Amina.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwapongeza wana-CCM wote kwa ushindi mkubwa tuliopata kwenye chaguzi ndogo za Ubunge na Udiwani zilizofanyika hivi karibuni. Ushindi huu tulioupata unadhihirisha sio tu uimara na ubora wa Chama chetu, bali pia imani kubwa waliyonayo Watanzania kwetu. Ninawashukuru Watanzania wote wa vyama mbalimbali kwa kuendelea kuonesha imani kwa CCM, Chama kikongwe na chenye kuheshimika duniani kote.
Niwaombeviongozi waliochaguliwawakafanye kazi kwa bidii na kushirikiana na Serikali katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu. Na katika hili, napenda niwapongeze na kuwashukuru kwa dhati kabisa, Wabunge na Madiwani wote wa CCM kwa namna ambavyo wanaiunga mkono Serikali katika masuala mbalimbali Bungeni na pia kwenyeHalmashauri zetu. Endeleeni na moyo huo ambao unadhihirisha mapenzi makubwa mliyonayo kwa Chama.
Waheshimiwa Makamu Wenyeviti wa CCM Taifa;
Ndugu Katibu Mkuu;
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Leo ni sikumuhimu na ya kihistoria kwa Chama chetu. Tumekutana hapa kwa kazi maalum. Kazi ya kufanya marekebisho madogo kwenye Katiba ya Chama chetu, lakini makubwa kwa ajili ya uhai na ustawi wa Chama. Hata hivyo, kabla sijazungumzia suala hilo kubwa ambalo limetuleta hapa leo, napenda nitumie muda mfupi kueleza utekelezaji wa majukumu ya Serikali, hususan Ilani yetu ya Uchaguzi.
Kama mnavyofahamu, sasa yapata mwaka mmoja na ushee tangu Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Chama chetu kuingia madarakani. Hivyo, ni dhahiri kuwa wana-CCM na Watanzania kwa ujumla wanayo haki ya kufahamu mambo ambayo yametekelezwa na Serikali yao. Kwa ujumla, katika kipindi cha mwaka mmoja tuliokaa madarakani, tumetekeleza mambo mengi. Lakini kwa sababu ya ufinyu wa muda, nitaeleza machache.
Suala la kwanza, tumeendelea kudumisha na kuimarisha amani nchini.Vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vimeendelea kulinda usalama na kudhibiti mipaka ya nchi yetu. Vitendo vyenye kutishia usalama, ikiwemo ujambazi wa kutumia silaha tumevidhibiti kwa kiasi kikubwa. Tumezidisha mapambano dhidi ya biashara haramu ya madawa ya kulevya, ambayo nayo ilikuwa inahatarisha usalama wa nchi yetu. Kwa ujumla, nchi ni tulivu na mipaka yetu yote ipo salama. Navipongeza sana vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa zinavyofanya za kuhakikisha nchi yetu inabaki kuwa na amani.
Halikadhalika, tumeendelea na jitihada za kudumisha na kuimarisha umoja na mshikamano wetu. Watanzania wamebaki wamoja licha ya tofauti zetu za dini, kabila, itikadi na rangi. Muungano wetu nao unazidi kuimarika. Diplomasia yetu nje ya nchinayo imezidi kukua. Viongozi mbalimbali wa nchi za nje wametembelea nchi yetu. Mimi pamoja na Makamu wa Rais, Rais wa Zanzibar, Waziri Mkuu, Makamu wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar tumetembelea nchi mbalimbali. Halikadhalika, ndani ya mwaka mmoja uliopita tumeweza kufungua Balozi mpya sita kwenye nchi za Uturuki, Israeli, Sudan, Algeria, Qatar na Korea Kusini.Kupatikana kwa mradi mkubwa wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga ni ishara nyingine ya kuimarika na kukua kwa Diplomasia yetu.
Kuhusu hali ya uchumi tunaendelea vizuri. Mwaka jana uchumi wetu ulitarajiwa kukua kwa asilimia 7.2 kutoka asilimia 7.0 mwaka uliotangualia. Hii imefanya nchi yetu kushika nafasi ya pili kwa ukuaji uchumi Barani Afrika baada ya Cote d’Ivoire. Tumeongeza ukusanyaji wa mapato kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 hadi kufikia shilingi trilioni 1.2 kwa mwezi. Lakini bado hatujaridhika. Tunataka angalau tuwe tunakusanya shilingi trilioni 1.8. In Sha Allah, naamini tutafika huko, hasa kwa vile tumeazimia kuziba mianya yote ya ukwepaji kodi.
Tumeimarisha nidhamu ya watumishi wa umma kwa kuwatumbua baadhi yao. Aidha, tumedhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma kwa kuwaondoa watumishi hewa wapatao 19,708 na pia wanafunzi hewawapatao 65,000. Tumepunguza safari za nje zisizo na tija na kuzidisha mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa rasilimali za umma. Tayari tumeanzisha Kitengo Maalum cha Mahakama kwa ajili ya kushughulikia makosa makubwa ya rushwa na uhujumu uchumi kama tulivyoahidi wakati wa Kampeni. Kitengo hicho cha Mahakama kilianza kazi mwezi Novemba mwaka jana. Napenda nitumie fursa hii kuwapongeza Wabunge wa CCM kwa kutunga sheria ya kuanzisha Kitengo hiki cha Mahakama. Kama mnavyofahamu, wakati wa mjadala wa kuanzisha Mahakama hii pale Bungeni, wale wenzetu walitoka nje na kususia mjadala. Lakini kwa uimara wa Wabunge wa CCM, mswada ulipitishwa. Nawapongeza sana Wabunge wa CCM. Mmedhihirisha kuwa mnachukia rushwa na ufisadi.
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Kutokana na ongezeko la ukusanyaji mapato na kufanikiwa kudhibiti matumizi, Serikali imeweza kuwa na fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, hususan ujenzi wa miundombinu ya usafiri na umeme. Mathalani, kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha, ambapo takriban asilimia 40 tumeielekeza kwenye miradi ya maendeleo, tumetenga takriban shilingitrilioni 5.47 sawa na asilimia 25.4 ya bajeti yote kwa ajili ya miundombinu ya usafiri. Fedha hizo, ndizo zimetuwezesha kutangaza zabuni ya ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge), ambapo Mkandarasi amepatikana kwa gharama ya shilingi trilioni moja. Ujenzi wa reli hiyo utaanza wakati wowote kuanzia sasa. Tumenunua ndege sita mpya, ambapo mbili zimewasili na tayari zimeanza kutoa huduma. Ndege nyingine moja itakuja mwezi Mei mwaka huu, nyingine tatu zitakuja mwakani, ikiwemo moja kubwa yenye uwezo wa kubeba abiria 250. Ununuzi wa ndege hizi utasaidia sana kukuza sekta yetu ya utalii, ambapo kwa sasa bado tunapokea watalii wachache; chini ya milioni moja na nusu. Tunataka wafikie milioni mbili au tatu.
Tunaendelea naukarabati viwanja vyetu vya ndege, upanuzi wa bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara.Wiki iliyopita nimeshiriki uwekaji wa Jiwe la Msingi la upanuzi wa Bandari ya Mtwara kwa gharama ya shilingi bilioni 137. Aidha, tunaendelea na ukarabati wa meli zetu na mipango ya kununua meli mpya kwa ajili ya kutumika kwenye Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika unaendelea vizuri. Kwa upande wa ujenzi wa barabara na madaraja nao unaendelea vizuri. Barabara kadhaa zimekamilika na nyingine zinaendelea kujengwa. Tatizo la usimamishaji kazi limekwisha kwa sababu Makandarasi wanalipwa fedha zao. Tunataka kuhakikisha nchi yetu yote inafunguka kwa barabara.
Tuliahidi wakati wa Kampeni kushughulikia tatizo la msongamano wa magari kwenye jiji la Dar es salaam. Tayari tumeanza ujenzi wa barabara ya juu pale TAZARA kwa gharama ya shilingi bilioni 100na mwezi huu natarajia kuweka Jiwe la Msingi kwa ajili ya interchange ya Ubungo kwa gharama ya shilingi bilioni 188.715. Napenda pia kuwafahamisha kuwa tumefanikiwa kupata fedha za ujenzi wa miundombinu ya usafiri wa mwendokasi kwa awamu ya pili hadi ya nne. Barabara zitakazohusika ni za Kilwa na Chang’ombe; Nyerere na Uhuru; pamoja na Babarara ya Bagamoyo hadi Tegeta na Sam Nujoma. Ujenzi wa Barabara hizo unatarajiwa kuanza mwaka ujao wa fedha kwa gharama za shilingi bilioni 820. Katika Jiji la Mwanza, tunaendelea na Ujenzi wa Daraja la Furahisha pamoja na upanuzi wa barabara ya kwenda Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Tunayo pia mipango kabambe ya ujenzi wa barabara hapa Dodoma. Tunataka kuufanya mji wa Dodoma kuwa wa kisasa ili uendane na hadhi ya kuwa Makao Makuu ya Chama na Serikali.
Kwenye sekta ya nishati, tumetenga shilingi trilioni 1.3kwenye bajeti ili kuongeza uzalishaji wa umeme. Bila shaka mtakubaliana nami kuwa Watanzania kwa sasa wameanza kusahau msamiati wa “mgawo wa umeme”. Hivi sasa tunatekeleza miradi mikubwa miwili ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia. Mradi wa kwanza ni Kinyerezi I, ambao tunapanua uwezo wake ili uweze kuzalisha Megawati 335 kutoka Megawati 150 za sasa. Mradi mwingine ni waKinyerezi II wenye uwezo wa kuzalisha Megawati 240. Sambamba na miradi hiyo, Serikali ipo kwenye maandalizi ya ujenzi wa mradi wa Kinyerezi III utakaokuwa na uwezo wa kuzalisha Megawati 600, na Kinyerezi IV wenye uwezo wa kuzalisha Megawati 330.
Tunaendelea pia na utekelezaji wa miradi mingine ya kufua umeme kwa kutumia maji, jua, makaa ya mawe, upepo n.k. Tunataka ikifika mwaka 2020nchi yetu izalishe angalauMegawati 5000kutoka kama Megawati1500 za sasa. Aidha, tumeanza utekelezaji wa awamu ya tatu ya programu ya kusambaza umeme vijijini kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA), ambapo mwaka huu zimetengwa shilingi bilioni 534.4 kuanza utekelezaji wa mradi huo. Tunataka Watanzania wengi zaidi wapate huduma hii muhimu ya umeme.
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Sambamba na hatua hizo za kuboresha miundombinu, tunaendelea na jitihada za kupanua na kuboresha upatikanaji wa huduma za jamii, hususan elimu, afya na maji. Kwenye elimu, kama mtakavyokumbuka, mara tu baada ya kuingia madarakani, Serikali ilipitisha uamuzi wa kuanza kutoa elimu ya msingi na sekondari bila malipo, ambapo kila mwezi tunatenga shilingi bilioni 18.77. Tangu kuanza kutekeleza uamuzi huu wanafunzi waliodahiliwa darasa la kwanza na kidato cha kwanza wameongezeka maradufu. Kama mtakavyokumbuka, ongezeko la wanafunzi lilikuza tatizo sugu na la muda mrefu lililokuwa likiikabili nchi yetu; tatizola upungufu wa madawati katika shule zetu za msingi na sekondari. Lakini kufuatia jitihada zilizofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine, tulifanikiwa kulimaliza tatizo hilo ndani ya muda mfupi. Hivi sasa kwenye baadhi ya shule zetu kuna madawati mengi kuliko vyumba vya madarasa. Jitihada za kujenga vyumba vya madarasa, na miundombinu mingine kama vile ofisi za walimu, maabara, vyoo na nyumba za walimu zinaendelea. Tunataka watoto wetu wasome katika mazingira mazuri na kupata elimu bora.
Kwa upande wa vyuo vikuu, tuliongeza bajeti kwa ajili ya ufadhili kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka shilingi bilioni 340 iliyokuwa imepitishwa na Bunge kwenye bajeti ya Mwaka wa Fedha 2015/2016hadi kufikia shilingi bilioni 473. Hatua hii iliongeza idadi ya wanachuo waliopata ufadhili wa Serikali kutoka 98,300 hadi kufikia 124,358. Katika mwaka huu wa fedha, tumeongeza bajeti ya ufadhili wa wanachuo kutoka shilingi bilioni 473 hadi kufikia shilingi bilioni 483.
Kuhusu afya, tumeendelea na jitihada za kuongeza upatikanaji wa huduma za tiba, ikiwemo madawa na vifaa. Tunaendelea pia na ujenzi wa zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya pamoja na hospitali za rufaa za mikoa, hususan kwenye maeneo ambayo huduma hizo hazipo. Kwenye bajeti ya mwaka huu, ambapo sekta ya afya imetengewa shilingi trilioni 1.99, tumeongeza bajeti ya ununuzi wa madawa kutoka billion 31 mwaka jana hadi billioni 250. Katika kuhakikisha dawa hizo zinawafikia walengwa, tumeagiza Hospitali zote za Serikali kuanzisha Maduka ya Madawa kwenye maeneo yao.
Kwenye sekta ya Maji, tunaendelea na utekelezaji wa miradi ya kusambazaji maji kwenye maeneo mbalimbali, ikiwemo Jiji la Dar es Salaam, Musoma, Sumbawanga, Kigoma, Lindi, Sengerema na Chalinze. Miradi mingine mikubwa tunayoitekeleza ni ujenzi wa Bwawa la Kidunda Dar es Salaam ambalo litagharimu shilingi bilioni 430 na mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda Mkoa wa Simiyu ambao utagharimu shilingi bilioni690. Halikadhalika, katika Mkoa wa Tabora, tunatarajia kuanza utekelezaji wa miradi mikubwa miwili; mradi wa kwanza ni wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria utakaogharimu shilingi bilioni 592 na mwingine wa kutoa maji Mto Malagalasi wenye thamani ya shilingi bilioni 720. Kama tulivyoahidi wakati wa kampeni, tunataka ifikapo mwaka 2020, asilimia 85 ya watu wa vijijini na asilimia 90 - 95 ya wananchi wanaoishi mijini wawe wanapata maji safi. Hii ndiyo sababu katika bajeti ya mwaka huu wa fedha, Wizara ya Maji imetengewa fedha nyingi, takribani shilingi trilioni 1.02.
Waheshimiwa Makamu Wenyeviti wa CCM Taifa;
Ndugu Katibu Mkuu;
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Licha ya hatua tulizozichukua na mafanikio makubwa tuliyoyapata katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, ni dhahiri kuwa yapo masuala ambayo bado yanayohitaji muda kuendelea kuyashughulikia na kuyatatua. Baadhi ya masuala hayo ni matatizo ya umaskini na ukosefu wa ajira, uboreshaji wa huduma za jamii; vita dhidi ya rushwa na ubadhirifu wa mali za umma; uwajibikaji usioridhisha miongoni mwa watendaji wa serikali; migogoro kati ya wakulima na wafugaji, maslahi madogo kwa watumishi n.k.Lakini niseme tu kati ya masuala hayo yote, tatizo la umaskini na ukosefu wa ajira ni kubwa zaidi na linahitaji mbinu endelevu katika kukabiliana nalo.
Suala hili la umaskini na ukosefu wa ajira halipo tu hapa nchini kwetu bali katika nchi zote zinazoendelea. Hata hivyo, napenda niwahakikishie kuwa Serikali imejipanga vizuri kulishughulikia. Tunafahamu njia rahisi ya kukabiliana na tatizo hili ni kujenga viwanda. Tayari tumeanza kuchukua hatua za kujenga uchumi wa viwanda, ambapo mwezi Julai mwaka jana Serikali ilipitisha Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/2017 – 2020/2021)wenye dhima kuu ya kujenga uchumi wa viwanda. Tunataka ifikapo mwaka 2020 sekta ya viwanda iwe inachangia asilimia 40 ya ajira zote.
Nafarijika kuona kuwa dalili za Tanzania ya viwanda zimeanza kuonekana. Kwa mujibu wa takwimu tulizonazo, kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita, jumla yaviwanda 2169 vimesajiliwa, vikiwemo vya mbolea, saruji, chuma na usindikaji wa mazao. Wiki iliyopita wakati nikiwa safarini kuelekea Mikoa ya Lindi na Mtwara, niliweka jiwe la Msingi la Kiwanda kikubwa cha vigae pale Mkuranga, lakini nikiwa njiani niliweza kuona zaidi ya viwanda kumi, vikiwa vinajengwa na vingine vimeanza uzalishaji. Kwa Mkoa wa Pwani pekee kuna viwanda vikubwa 83 na vingine vidogo vidogo vidogo zaidi ya 200. Miongoni mwa viwanda vinavyotarajiwa kuanza uzalishaji hivi karibuni ni cha kutengeneza matrekta. Nina imani kuwa kwa kasi hii, baada ya muda si mrefu tutakuwa na viwanda vingi. Tukiwa na viwanda vingi tutapunguza tatizo la ajira nchini. Na ajira zikipatikana tutaweza pia kukabiliana na tatizo la umaskini.
Halikadhalika, kukua kwa sekta ya viwanda, kutasaidia kuimarisha sekta nyingine za uchumi, hususan kilimo, uvuvi na mifugo, madini, misitu na biashara ambazo nazo zinaajiri wananchi walio wengi. Sekta hizi zikikua zitasaidia sio tu katika kupambana na umaskini na tatizo la ajira bali pia kukuza uchumi wetu. Hivyo basi, Serikali inaendelea na jitihada za kuzikuza sekta hizi, hasa kwa kuhakikisha upatikanaji wa zana bora na za kisasa, pembejeo na ruzuku. Tutaendeleakutenga maeneo ya malisho na ya wachimbaji wadogo wa madini; kutafutamasoko ya mazao pamoja na kuondoa baadhi za kero zinazokwamisha ukuaji na ustawi wa sekta hizo. Mwaka uliopita, tulifanikiwa kupata soko la zao la dengu nchini India na mihogo nchini China. Aidha, tulianza kushughulikia tatizo la utitiri wa kodi kwa baadhi ya mazao, hususan kwa zao la korosho. Matokeo yakesote tumesikia, sihitaji kueleza. Tutaendelea kuchukua hatua kama hizo kwenye mazao mengine. Niwaombe tu wakulima kote nchini kuendelea kulima kwa bidii mazao mbalimbali.
Nina uhakika kabisa kuwa, kutokana na mipango na mikakati mizuri iliyopo Serikalini, tutaweza kushughulikia masuala na kero nyingine ambazo bado zinawasumbua wananchi. Wito wangu kwa wana-CCM wenzangu, kwanza tujitahidi kutangaza mafanikio yaliyopatikana. Tuzidi pia kuisimamia Serikali kutekeleza yale yote tuliyowaahidi wananchi. Aidha, tushirikiane katika kuhamasisha sekta yetu binafsi kushiriki kwenye shughuli za maendeleo nchini, hususan ujenzi wa viwanda. Binafsi nafurahi sana kuonakuwa sekta binafsi imeitikia vizuri wito wa Serikali wa kujenga viwanda. Lakini tuzidi kuwahamasisha. Tunawahitaji wafanyabiashara kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na shughuli nyingine za maendeleo.
Sambamba na hilo, napenda kuwahimiza Watanzania wote kufanya kazi kwa bidii. Kazi ni utu. Kazi ni msingi wa maendeleo. Lakini pia kazi ni uhai. Bila kufanya kazi tutakufa ama kwa njaa au kukosa huduma muhimu. Nawaomba pia kuwahimiza Watanzania wenzangu tuendelee kulipa kodi. Nafurahi tangu tumeingia madarakani, mwamko wa wananchi kulipa kodi umeongezeka. Naomba tuendelee na moyo huo. Kodi mnazozilipa ndizo zinaiwezesha Serikali, kutekeleza miradi ya maendeleo na kuboresha huduma za jamii. Nawahakikishia kuwa hakuna senti hata moja itakayotumika vibaya. Fedha zote zitatumika kwa ajili ya manufaa ya Watanzania wote. Hakuna mtu atakayejinufaisha nazo binafsi.
Waheshimiwa Makamu Wenyeviti wa CCM Taifa;
Ndugu Katibu Mkuu;
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Naomba sasa nizungumzie suala muhimu ambalo limetuleta hapa. Kama mnavyofahamu, Chama chetu kimekuwa na utamaduni wa kujitathmini kila wakati na kufanya mageuzi. Mageuzi hayo ndio yamekuwa chachu yenye kukifanya Chama chetu kiendelee kudumu, kizidi kuimarika na kwenda na wakati.Kutokana na utamaduni huo huo ambao umejengeka ndani ya Chama chetu, Halmashauri Kuu yetu ya Taifa ilikutana mwezi Desemba mwaka jana na kupokea Taarifa ya Tathmini ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Baada ya kupitia taarifa hiyo ambayo ilibainisha changamoto na mapendekezo ya kushughulikia, Halmashauri Kuu ilipitisha maazimio yenye lengo la kukiwezesha Chama chetu kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ili kuendana na mazingira ya sasa ya ushindani.
Baadhi ya maazimio yalianza kutekelezwa mara moja lakini mengine yalihitaji kufanyika kwanza kwa marekebisho ya Katiba yetu ndipo yaweze kutekelezwa. Hii ndiyo sababu kubwa ya kuitisha Mkutano Mkuu huu Maalum. Tumeuitisha ili kuwapa fursa ninyi wajumbe kupitia marekebisho ya Katiba yanayopendekezwa, muyatafakari na ikiwezekana muyapitishe.Natambua kuwa Katibu Mkuu wetu, Mzee Kinana, baadaye leo atawasilisha waraka utakaofafanua kwa kirefu kiini, shabaha na maeneo tunayotaka kuyafanyia marekebisho. Kwa sababu hiyo, mimi nitajikita zaidi kueleza malengo na madhumuni ya mabadiliko tunayotaka kuyafanya. Yapo mengi, lakini nitataja machache makubwa.
Kwanza kabisa,marekebisho ya Katiba yanayopendekezwa na Halmashauri Kuu yanalenga kuboreshamfumo na muundo wa Chama chetu na Jumuiya zake. Kama mnavyofahamu, mfumo na muundo wa Chama tulionao, licha ya kuwa umetupatia mafanikio kwa miaka 40 iliyopita, una mapungufu. Mathalani, kuna mwingiliano mkubwa wa kimajukumu baina ya taasisi za Chama na Jumuiya zake. Mwingiliano huo ndiyo umechangia Chama chetu kuwa na watendaji wengi wanaotekeleza majukumu yanayofana na hivyo kuleta migongano. Sambamba na hilo, hivi sasa ndani ya Chama chetu kumeibuka vyeo ambavyo vinanguvu katika maamuzi lakini havipo kikatiba, kama vile Makamanda wa Vijana au Washauri wa Jumuiya. Na wapo baadhi ya watu wametumia vyeo hivyo kwa maslahi yao binafsi. Hivyo basi, marekebisho ya Katiba yanayopendekezwa yanalenga kuondoa mapungufu niliyoyataja kwa kuboresha mfumo na muundo wa Chama. Tunataka Chama chetu kiwe na muundo mdogo kitaasisi, wenye kuonesha mgawanyo wa majukumu na uwajibikaji (yaani pawe distribution of duties and clear chain of command), kuanzia ngazi ya juu ya Chama hadi chini. Na pia uoneshe uhusiano kati ya Chama na Jumuiya zake.Vyeo vyote ambavyo havipo kikatiba, tunataka kuviondoa.
Pili, Halmashauri Kuu inaleta kwenu mapendekezo ya marekebisho ya Katiba yenye lengo la kuongeza ufanisi na kuboresha utendaji kazi wa Chama. Naamini mtakubaliana nami kuwa utendaji kazi wa Chama chetu umekuwa ukishuka sana, hasa uchaguzi ukimalizika. Hali hii inatokana na Chama kujiweka pembeni katika kusimamia Serikali na kuwahamasisha wananchi kushiriki shughuli za maendeleo. Baadhi ya viongozi na watendaji wa Chama wanabaki kuwa watazamaji na walalamikaji badala ya kuwa mfano wa utendaji bora kwa wananchi. Mathalan, hivi sasa mvua zinanyesha karibu nchi nzima lakini nina uhakika ni viongozi wachache wa Chama wanawahamasisha wananchi kulima. Hivyo basi, tunataka tuboreshe utendaji kazi wa Chama, ikiwemo kwa kukifanya Chama kuwa na watumishi wachache lakini wenye moyo na weledi wa kukitumikia vizuri. Aidha, tunataka kupunguza idadi ya vikao vya Chama na wajumbe wa vikao hivyo kwa lengo lakuongeza ufanisi na kutoa fursa kwa watendaji kutumia muda mwingi kutekeleza shughuli za Chama.
Tatu, mabadiliko tunayotaka kuyafanya yanalenga kukipeleka Chama kwa wananchi. Waasisi wetu, walianzisha Chama hiki kwa ajili ya kuwatetea wananchi wanyonge, hususan wakulima, wafanyakazi, wafugaji, wavuvi n.k. Hivyo, tunataka tukirudishe Chama kwa wananchi badala ya kubaki kwa viongozi na matajiri wachache. Tunalenga kuimarisha utendaji kazi wa Chama kwenye ngazi ya matawi na mashina. Kama mnavyofahamu, kwenye matawi na mashina ndiko kwenye wanachama na wananchi wengi. Hivyo, tukiimarisha ngazi hizo itakuwa rahisi kwetu kufahamu matatizo yanayowakabili wanachama na wananchi na hivyo kuweza kutafuta majawabu yaharaka. Hii ndiyo sababu nyingine pia tunalenga kupunguza idadi ya vikao vya Chama na wajumbe wake. Tunataka viongozi na watendaji wetu watumie muda mwingi kushughulikia matatizo ya wananchi badala ya kufanya vikao ambavyo vinatumia fedha nyingi huku tija yake ikiwa ni ndogo. Vikao hivyo ndivyo wakati mwingine vimekuwa vikitumika kutengeneza majungu ndani ya Chama na hata kupanga mikakati ya kuwazuia baadhi ya watu wenye sifa kugombea nafasi za uongozi kwenye Chama.
Nne, mabadiliko tunayotaka kuyafanya yana nia ya kukifanya Chama kijitegemee kiuchumi. Nyote mnafahamu kuwa Chama chetu kina rasilimali nyingi. Lakini mnajua pia jinsi gani rasilimali hizo hazikinufaishi sana Chama chetu. Licha ya utajiri wa rasilimali tulionao, tumeendelea kuwa ombaomba. Hivyo basi, mabadiliko tunayotarajia kuyafanya ni pamoja na kujenga uwezo wetu wa kitaasisi wa kuweza kutambua, kutunza na kutumia vizuri rasilimali za Chama. Yeyote atakayetaka kujinufaisha na rasilimali za Chama, hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.
Haya niliyoyaeleza ni baadhi tu ya malengo na madhumuni ya mabadiliko tunayokusudia kuyafanya. Yapo mengine mengi. Napenda kusisitiza kuwa, mabadiliko ndani ya Chama chetu si kitu kigeni. CCM imekuwa ikifanya mabadiliko mara kwa mara kulingana na mazingira na mahitaji. Mabadiliko haya tunayoyapendekeza ni ya 16 tangu Chama chetu kizaliwe mwaka 1977. Mabadiliko haya, kama mengine yaliyopita, yanalenga kukiimarisha Chama chetu kimfumo, kimuundo, kiungozi, kiutendaji na kirasilimali. Tunataka kukipa Chama chetu uwezo wa kustahimili mazingira ya sasa na yajayo kwa lengo la kukifanya kiendelee kubaki madarakani kwa miaka mingi ijayo. Mabadiliko haya ni kwa maslahi ya wananchama wetu wa sasa na wajao. Hivyo, niwaombe wajumbe wa Mkutano Mkuu myaunge mkono na kuyapitisha. Nafahamu wapo wanachama wenzetu watakaoguswa na mabadiliko haya kwa namna moja au nyingine, lakini kutokana na mapenzi ya dhati kwa Chama na kuweka maslahi ya Chama mbele, naamini wataunga mkono. Na sisi hatutawaacha.
Waheshimiwa Makamu Wenyeviti wa CCM Taifa;
Ndugu Katibu Mkuu;
Ndugu Wajumbe na Wanachama wenzangu;
Kabla sijahitimisha hotuba yangu ninayo masuala mawili ya mwisho ambayo ningependa kuyaeleza. Jambo la kwanza, mtakumbuka katika Mkutano Mkuu uliopita nilieleza dhamira yangu ya kuhakikisha Serikali inahamia Dodoma kabla ya mwaka 2020. Napenda kuwahakikishia kuwa tumedhamiria kwa dhati kabisa kuhamia Dodoma. Nasema hivi, tutahamia Dodoma. Na utekelezaji wa dhamira hiyo tayari umeanza. Katika awamu ya kwanza ya utekelezaji, Waziri Mkuu pamoja naViongozi Wakuu wa Wizara zote, yaani Mawaziri, Naibu Mawaziri; Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na baadhi ya Wakurugenzi na watumishi wameshahamia Dodoma. Aidha, vikao vya Makatibu Wakuu na Baraza la Mawaziri kuanzia mwezi Machi, vyote vitafanyika hapa Dodoma. Kwa maneno mengine, maamuzi makuu ya Serikali yameanza kufanyika Dodoma. Mimi nami najipangapanga kuhamia Dodoma. Mabalozi na Wawakilishi wa nchi na taasisi mbalimbali za kimataifa nao wameonesha nia ya kuanza kuhamia Dodoma. Hivyo, nina uhakika kuwa lengo letu la kuhakikisha Serikali yote imehamia Dodoma ifikapo mwaka 2020 litatimia.
Jambo la pili ni suala la uchaguzi ndani ya Chama chetu. Kama mnavyofahamu, mwezi ujao tutaanza uchaguzi wa viongozi wa ngazi mbalimbali wa Chama chetu. Uchaguzi huo ni muhimu sana kwa uhai na ustawi wa Chama. Hii ni kwa sababu viongozi tutakaowachagua ndio watakaotuongoza kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 2019 na Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. Tukichagua viongozi wazuri tutakirahisishia Chama chetu kupata ushindi kwenye chaguzi hizo, lakini tukichagua wasiofaa tutapata shida. Hivyo basi, natoa wito kwa wanachama wenzangu kuchagua viongozi waadilifu, wachapakazi, wenye mapenzi ya dhati kwa Chama chetu na wanaokubalika na wananchi.
Tusichague watu kwa fedha zao au umaarufu wao. Natambua chaguzi ndani ya Chama chetu zimekuwa zikigubikwa na matatizo ya rushwa na udanganyifu. Nilishasema na napenda kurudia tena leo, chini ya uongozi wangu, rushwa haitakuwa na nafasi katika kuchagua viongozi wa chama. Nasisitiza kuwa msisumbuke kuhonga. Najua na ninaelewa namna ya kushughulika na wote watakaojihusisha na vitendo hivyo. Kama Serikalini hatuvumilii na tunawatumbua, hatutashindwa kuchukua hatua kama hizo ndani ya Chama. Nawasihi Sekretarieti kujipanga vizuri kusimamia uchaguzi huu. Hatutaki uchaguzi huu uvurugike kwa kuingiza mapandikizi, mamluki au kwa namna yoyote ile. Atakayebainika kuvuruga uchaguzi wetu, hatua kali za kinadhamu na maadili zitachukuliwa dhidi yake.
Waheshimiwa Makamu Wenyeviti wa CCM Taifa;
Ndugu Katibu Mkuu;
Ndugu wajumbe na Wanachama wenzangu;
Napenda kuhitimisha kwa kuwashukuru tena wajumbe kwa kuhudhuria mkutano huu. Nawasihi tufanye uamuzi wa busara wa kupitisha mapendekezo yatakayoletwa kwenu. Narudia tena, mapendekezo hayo ni muhimu kwa ajili ya uhai, ustawi na mustakabali mzima wa Chama chetu.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru Wenyeviti na viongozi wetu mbalimbali wastaafu waliokuja kujumuika nasi hapa. Nafurahi kumwona Mzee Mwinyi, Mzee Kikwete, Makamu wa Rais Mstaafu Mzee Bilal; Rais Mstaafu wa Zanzibar Mzee Karume; Mawaziri Wakuu Wastaafu, Mzee Warioba, Mzee Macelela, Mzee Dkt. Salim na Mzee Pinda; pamoja na Spika Wastaafu, Mama Makinda na Mzee Kificho. Tunawashukuru sana. Uwepo wenu mahali hapa leo unadhihirisha upendo na mapenzi ya dhati mliyonayo kwa Chama hiki. Napenda kuwahakikishia kuwa sisi vijana ambao mmetuachia dhamana tunawapenda, tunawahitaji na tutaendeleakutumia busara na uzoefu wenu. Maana kama msemo wa kiswahili usemavyo, “uzee ni dawa”.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa Mkutano Mkuu Maalum wa CCM umefunguliwa rasmi.
Mungu Ibariki Tanzania!
Kidumu Chama cha Mapinduzi!
“Asanteni sana kwa Kunisikiliza”

- Feb 10, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA ALIYOINDAA KWA AJILI YA MABALOZI NA VIONGOZI WA TAASI...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje
na Ushirikiano wa Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Meja Jenerali Mstaafu Edzai Chimonyo,
Balozi wa Zimbabwe na Kiongozi wa Mabalozi nchini;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda niwashukuru sana, Waheshimiwa Mabalozi, kwa kukubali mwaliko wangu wa kuhudhuria hafla hii. Nawakaribisheni nyote hapa Ikulu na naomba mjisikie kuwa mko nyumbani. Aidha, napenda nitumie fursa hii hapa mwanzoni kabisa, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania niwatakie Waheshimiwa Mabalozi pamoja na familia zenu Heri ya Mwaka Mpya 2017. Naomba pia mnifikishie salamu zangu za Heri ya Mwaka Mpya 2017 kwa Viongozi, Wananchi pamoja na watumishi wa Taasisi mnazoziwakilisha.
Waheshimiwa Mabalozi;
Kama ilivyo ada, hafla hii hutoa fursa kwetu sote kutafakari masuala ya mwaka uliopita na kupanga mikakati ya mwaka mpya. Napenda kutumia fursa hii, kueleza kuwa kwa nchi yetu, mwaka uliopita ulikuwa wenye matukio mengi. Licha ya kuwa ulikuwa mwaka wa kwanza tangu Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani, tulipata mafanikio makubwa katika ngazi ya kitaifa na kimataifa.
Tuliweza kudumisha amani, umoja na mshikamano wetu. Nchi yetu iliendelea kuwa ya amani na kimbilio la watu wengi. Watanzania tulibaki kuwa wamoja na Muungano wetu ulizidi kuimarika. Tuliongeza jitihada za kuimarisha demokrasia na utawala bora. Tumezidisha vita dhidi ya wala rushwa, ujangili na biashara haramu ya madawa ya kulevya.
Kiuchumi pia mwaka 2016 ulikuwa ni mzuri kwa nchi yetu. Tulikuwa miongoni mwa nchi ambazo uchumi wake ulikua kwa kasi Barani Afrika. Taasisi mbalimbali za kimataifa zinazoshughulikia masuala ya uchumu, ziliitaja nchi yetu kushika nafasi ya pili kwa ukuaji uchumi baada ya Cote d’Ivoire. Uchumi wetu ulitarajiwa kukua kwa asilimia 7.2 mwaka jana kutoka asilimia 7.0 mwaka uliotanguliwa. Mfumko wa bei nao ulishuka kutoka asilimia 6.5 mwezi Januari hadi kufikia asilimia 4.5 mwezi Septemba 2016, ingawa uliongezeka kidogo kufikia asilimia 4.8 mwezi Novemba 2016. Tuliongeza ukusanyaji wa mapato kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 hadi kufikia shilingi trilioni 1.2 kwa mwezi.
Waheshimiwa Mabalozi, Mabibi na Mabwana;
Mwaka jana nchi yetu ilipitisha Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/17 – 2020/21). Dhima kuu ya Mpango huu ni kujenga misingi imara ya sekta ya viwanda ili kuifanya nchi yetu kuwa ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025, kama ambavyo Dira yetu ya Maendeleo inavyoelekeza. Utekelezaji wa Mpango huu utatumia takriban shilingi trilioni 107. Kati ya fedha hizo, Serikali inatarajiwa kutoa shilingi trilioni 59 sawa na takriban shilingi trilioni 11.8 kwa mwaka. Utekelezaji wa Mpango huo, umeanza mwezi Julai mwaka jana ambapo Serikali ilipitisha bajeti ya shilingi trilioni 29.5. Kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu, tumeelekeza asilimia 40 ya bajeti yote kwenye shughuli za Maendeleo.
Kama mnavyofahamu, ili kujenga uchumi wa viwanda unahitaji miundombinu imara ya usafiri na nishati ya umeme. Hivyo, tumezielekeza fedha nyingi kwenye sekta hizo. Tumetenga shilingi trilioni 5.47 kwenye sekta ya ujenzi na shilingi trilioni 1.2 kwenye nishati. Hii imetuwezesha kuendelea au kuanza utekelezaji wa miradi mikubwa ya usafiri ikiwemo reli, barabara, anga, maji pamoja na miradi ya umeme. Tuliweza pia kununua ndege mpya sita lengo likiwa ni kuimarisha usafiri wa anga na hatimaye kukuza sekta ya utalii nchini.
Maeneo mengine ambayo tumeyapa kipaumbele ni uboreshaji wa huduma za jamii, hususan elimu na afya. Tumetenga shilingi trilioni 4.77 kwa ajili ya elimu na maendeleo ya sayansi na shilingi trilioni 1.99 kwenye sekta ya afya. Matokeo yake ni kwamba udahili kwa darasa la kwanza, kidato cha kwanza na wanufaika wa mikopo ya elimu ya juu umeongezeka maradufu. Tumeboresha pia huduma za afya, hususan upatikanaji wa vifaa tiba na madawa.
Waheshimiwa Mabalozi;
Kwenye masuala ya diplomasia nako tulipata mafanikio makubwa mwaka jana. Nchi yetu ilitembelewa na viongozi wa mataifa kadhaa. Mimi pia niliweza kutembelea baadhi ya nchi. Ziara hizi zilikuza zaidi uhusiano wetu. Tuliweza kusaini mikataba kadhaa ya ushirikiano kwenye maeneo mbalimbali. Aidha, mwaka jana tuliweza kufungua Balozi kwenye mataifa kadhaa ambayo hatukuwa na uwakilishi.
Sambamba na kuimarisha uhusiano na mataifa ya nje, tumeendelea kutoa mchango wetu kupitia taasisi mbalimbali za kimataifa ambazo sisi ni wanachama. Mwaka 2016 tulipata heshima ya kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Chombo kinachosimamia Siasa, Ulinzi na Usalama cha Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Troika Organ on Politics, Defense and Security). Kupitia taasisi hizo, tumeweza kutoa michango mbambali, hususan kwenye usuluhishi wa migogoro nchi za Burundi, DRC, Lesotho na Sudan Kusini. Aidha, vikosi vyetu vimeendelea kulinda amani nchini Sudan na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Kwa ujumla mwaka uliopita ulikuwa wenye mafanikio makubwa kwa nchi yetu. Hata hivyo, napenda kusema kuwa tumepata mafanikio haya yote kutokana na ushirikiano mkubwa mliotupa. Hivyo basi, napenda nitumie fursa hii kuwashukuru Mabalozi wote mnaowakilisha nchi na taasisi za kimataifa hapa nchini kwa ushirikiano wenu mkubwa.
Mheshimiwa Kiongozi wa Mabalozi;
Waheshimiwa Mabalozi,
Mabibi na Mabwana;
Pamoja na mafanikio hayo niliyoyataja, mwaka jana pia ulikuwa na changamoto. Tena nyingi tu. Lakini kubwa ni kutokea kwa athari za mabadiliko ya tabianchi. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuzipongeza nchi zote, ambazo tayari zimeridhia Mkataba wa Paris kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi. Sisi Tanzania tayari tumeanza mchakato wa kuridhia Mkataba huo, ambao tuliusaini mwezi Aprili mwaka jana. Nina matumaini makubwa kuwa endapo nchi zote zitasaini, kuridhia na kutekeleza Mkataba huo, tutaweza kukabiliana na tatizo hili la mabadiliko ya tabianchi.
Waheshimiwa Mabalozi,
Katika mwaka huu tulioanza, Serikali na wananchi wa Tanzania wamejipanga kuendelea na utekelezaji wa mipango na mikakati mbalimbali ya maendeleo, hususan Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Tunataka ifakapo mwaka 2020 uchumi wetu ukue kwa asilimia 10, sekta ya viwanda itoe ajira kwa asilimia 40 ya Watanzania, pato la kila Mtanzania liongezeke na hatimaye ikifika mwaka 2025 tuwe nchi ya kipato cha kati. Hivyo basi, tunawakaribisha wawekezaji kutoka nje kuja kuwekeza kwenye sekta ya viwanda hapa nchini. Nchi yetu ina fursa nyingi za ustawi wa viwanda, ikiwa ni pamoja na malighafi za kutosha, nguvu kazi na soko kubwa. Tunawakaribisha pia wawekezaji kuja kushirikiana nasi katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya uchumi. Mwaka huu tunaanza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa kutoka Dar es Salaam kwenda mikoa ya Mwanza na Kigoma na ambayo itafika nchi za Burundi na Rwanda. Hii ni fursa nzuri ya uwekezaji, hivyo, tunawaomba Waheshimiwa Mabalozi mtangaze fursa zilizopo hapa Tanzania kwa wananchi wenu.
Sambamba na kutekeleza mipango hiyo ya maendeleo, tumejipanga katika mwaka huu, kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano na mataifa pamoja na taasisi mnazowakilisha. Na pia mataifa ambayo hayana uwakilishi hapa nchini. Aidha, tutaendelea kuwa mwanachama mwadilifu na mwaminifu wa taasisi zote ambazo sisi ni wanachama, ikiwemo EAC, SADC, Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Madola, Nchi zisizofungamana na Upande wowote, Umoja wa Mataifa, n.k. Tutaendelea kutekeleza mipango mbalimbali ambayo imepitishwa katika ngazi ya kikanda na kimataifa, ikiwemo Agenda 2063 ya Umoja wa Afrika pamoja na Agenda 2030 kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa.
Mheshimiwa Kiongozi wa Mabalozi;
Waheshimiwa Mabalozi,
Mabibi na Mabwana;
Ningependa nikomee hapa. Lakini kabla sijahitimisha, ninalo jambo moja la mwisho ambalo sina budi nilieleze. Mwaka 1973, Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitangaza uamuzi wa kuhamishia Makao Makuu ya nchi yetu kutoka hapa Dar es Salaam kwenda Dodoma. Hata hivyo, kwa sababu mbalimbali, uamuzi huo haukuweza kutekelezwa kikamilifu. Mwaka jana mwezi Julai, wakati nikipokea Uenyekiti wa Chama changu, Chama Cha Mapinduzi (CCM), niliahidi kuwa ndani ya kipindi cha miaka mitano ya uongozi wangu, nitahakikisha Serikali itahamia Dodoma. Napenda niwaarifu Waheshimiwa Mabalozi kuwa Serikali itahamia Dodoma katika kipindi hicho. Tayari baadhi ya taasisi zimeanza kuhamia Dodoma. Hivyo, nina uhakika ahadi hiyo itatimia. Kwa sababu hiyo, niwaombe Waheshimiwa Mabalozi nanyi muanze kufikiria kuhamia Dodoma. Serikali imejipanga kuanza kutoa viwanja kwa ajili yenu hivyo anzeni kuleta maombi yenu. Nafurahi kuwa baadhi ya Balozi tayari zimeanza kuleta maombi yao.
Napenda kuhitimisha kwa kuwashukuru tena kwa kukubali mwaliko wangu. Nawashukuru pia kwa jitihada mbalimbali mazozifanya za kuimarisha ushirikiano kati yetu. Nawahidi kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwenu ili muweze kutekeleza majukumu yenu ipasavyo.
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”