Hotuba

- May 07, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE CHUO KIKUU CHA KILIMO CHA SOKOINE, MOROGORO, TAREHE 7 MEI,...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE CHUO KIKUU CHA KILIMO CHA SOKOINE, MOROGORO, TAREHE 7 MEI, 2018
Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako;
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi;
Mheshimiwa Steven Kebwe,
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro;
Prof. Raphael Chibunda, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA);
Prof. Lughano Kusiluka, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Mzumbe;
Rasi na Manaibu Rasi wa Chuo Kikuu cha SUA;
Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Dini mliopo;
Ndugu Wanajumuiya wa Chuo Kikuu Kilimo
Cha Sokoine (SUA)
Wageni Waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika hapa Chuo Kikuu cha Kilimo; Chuo ambacho kimepewa Jina la mmoja wa viongozi mahiri, shupavu na mtetezi wa wanyonge, aliyewahi kutokea katika nchi yetu, Hayati Edward Moringe Sokoine. Ingawa ametangulia mbele za haki, nina imani, kupitia jina la Chuo hiki, Watanzania wengi, kizazi kwa kizazi, wataendelea kumkumbuka na kumuenzi Kiongozi wetu huyo.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru wana-SUA kwa mapokezi yenu mazuri. Nafahamu kuwa kama sio wote basi wengi weu hapa mlinipigia kura. Hivyo basi, kwa kuwa hii ni mara yangu kufika hapa tangu nimechaguliwa, napenda nitumie fursa hii kuwashukuru kwa dhati kabisa kwa kunichagua kuwa Rais wenu. Nasema “ahsanteni sana wana-SUA”. Niwaahidi tu kwamba sitowaangusha. Nitakuwa pamoja nanyina wakati wote.
Ndugu Wanajumuiya wa SUA;
Mabibi na Mabwana;
Tangu ijumaa iliyopita nimekuwa kwenye ziara ya Mkoa huu wa Morogoro. Nimepata fursa ya kukutana na kuzungumza na wananchi na halikadhalika kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo. Nimeweka Jiwe la Msingi la Barabara ya Kidatu – Ifakara yenye urefu wa kilometa 66.9 inayojengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 104.5. Nimeshiriki Uzinduzi wa Daraja la Kilombero lenye urefu wa mita 384, ambalo ni la nne kwa ukubwa nchini na ambalo wameamua kulipa jina la Magufuli.
Jana niliingia hapa Morogoro mjini, ambapo mchana nilizindua Stendi ya Kisasa ya Mabasi pale Msamvu. Leo asubuhi nilitakiwa niondoke kurudi Dar es Salaam. Sikuwa nimepangiwa kuja hapa SUA. Lakini, nikasema hapana; siwezi kumaliza ziara yangu bila kufika hapa SUA; Chuo Kikuu cha pekee cha Kilimo hapa nchini. Hii ndio maana mnaniona nipo hapa muda huu.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Nimekuja hapa kwa sababu kubwa tatu. Kwanza kuwasalimu wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu hiki. Sababu ya pili iliyonileta hapa ni kutambua mchango mkubwa unaotolewa na Chuo hiki katika maendeleo ya nchi yetu. Hakuna shaka yoyote kuwa Chuo hiki, tangu kianzishwe tarehe 1 Julai, 1984 kimetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi yetu, kupitia kozi mbalimbali kinazofundisha na tafiti kilizofanya katika fani mbalimbali (sayansi ya kilimo, misitu, tiba ya mifugo, ufugaji wa samaki, maendeleo vijijini, utalii, ualimu, n.k.). Na mojawapo ya tafiti kubwa zilizowahi kufanywa na Chuo hiki, ambazo zinatambulika kimataifa, ni ule wa kuwafundisha panya kubaini mabomu na kuweza kugundua vimelea vya ugonjwa wa Kifua Kikuu.
Nitumie fursa hii, kukipongeza sana Chuo hiki kwa utafiti huo mkubwa ambao umeiletea sifa kubwa nchi yetu. Kwa hakika, mmetekeleza kwa vitendo dhamira ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, ya kuanzisha Chuo hiki. Nawapongezeni pia kwa ubunifu wenu wa kuongeza idadi ya kozi na fani mnazozifundisha. Nafahamu kuwa wakati Chuo hiki kinaanzishwa mwaka 1984, kilikuwa na vitivo vitatu tu; yaani kitivo cha kilimo, kitivo cha misitu na kitivo cha tiba ya mifuko. Sasa mmeongeza kozi nyingine, ikiwa ni pamoja na utalii, maendeleo vijijini, ualimu, n.k. Hongereni sana.
Ndugu Wanajumuiya wa SUA;
Sababu ya tatu iliyonisukuma kuja hapa leo ni kuwapa moyo na kuamsha ari na hamasa mpya kwenu ya kuendelea kujituma zaidi. Na katika hili, naomba nitaje maeneo machache, ambayo nitatamani sana Chuo hiki kiyape kipaumbele cha kutosha.
Eneo la kwanza ni kuendelea kufanya utafiti wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. Ndugu zangu wana-SUA, mimi niliwahi kuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Ninafahamu, kama tukiweka mkazo na kuisimamia vizuri sekta hizi za kilimo, mifugo na uvuvi, nchi yetu itapata maendeleo ya haraka. Hii ni kwa sababu takriban asilimia 70 ya Watanzania wanaendesha maisha yao kupitia shughuli za kilimo, mifugo na uvuvi. Aidha, nchi yetu inashika nafasi ya pili kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo Barani Afrika. Zaidi ya hapo, tunayo maeneo mengi yenye kufaa kufanya shughuli za uvuvi. Hivyo basi, ni wazi kuwa endapo tutaziwekea mkazo sekta hizi; tutapiga hatua kubwa kimaendeleo.
Sambamba na hilo, hivi sasa nchi yetu imejipanga kujenga uchumi wa viwanda kwa lengo la kuharakisha maendeleo na kukabiliana na tatizo la ajira. Viwanda tunavyovilenga kuvijenga ni vile vyenye kutumia malighafi zinazopatikana kwa wingi hapa nchini, hususan mazao ya kilimo, mifuko na uvuvi. Hii yote inafanya sekta hii ya kilimo, mifugo na uvuvi kuwa na umuhimu wa pekee kwa nchi yetu. Hii ndio sababu nakisisitiza sana Chuo hiki cha pekee cha Kilimo nchini kuendelea kufanya tafiti zaidi ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi na hatimaye kuiwezesha nchi yetu kufanya mageuzi ya kiuchumi.
Nimefurahi wakati nikija hapa nimeona shamba lenu zuri la mfano. Nimeona mipapai midogo kabisa ikiwa tayari imezaa matunda. Hayo ni mafanikio makubwa. Na ni matumaini yangu kuwa utaalamu kama ule utasambazwa kwenye maeneo mengi ya nchi yetu. Tunataka wakulima wetu wajifunze mbinu za kisasa za kilimo ili waongeze uzalishaji. Na mahali pekee pa kujifunza mbinu hizo ni kwenye Chuo chenu hiki. Hakuna mahali pengine. Hii ndio sababu Serikali inakithamini sana Chuo hiki. Na nitumie fursa hii kuwahakikishia kuwa tutaendelea kuwathamini na kushirikiana kwa karibu na ninyi. Baadhi yenu mtakuwa mkifahamu kuwa, mimi, tangu nikiwa Waziri mpaka sasa nimekuwa Rais, nimekuwa nikiwaamini sana wasomi wa Chuo hiki na nimewateua kushika nyadhifa mbalimbali. Naahidi nitaendelea kuwatumia wasomi wa Chuo hiki. Na katika kudhihirisha dhamira ya Serikali ya kutaka kuona Chuo hiki kinachangia maendeleo ya kilimo nchini, leo niwaahidi kuwapatia fedha za kununua matrekta 10 mapya kwa ajili ya kufanya mafunzo ya vitendo.
Ndugu Wana-SUA;
Ukiachilia mbali utafiti wa mazao, eneo jingine ambalo nitafurahi kama mtalipa kipaumbele ni sekta ya utalii. Kama mnavyofahamu, nchi yetu ina vivutio vingi vya utalii. Na hivi sasa tumeanza kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuikuza sekta hii ili iweze kutunufaisha zaidi kuliko ilivyo sasa. Tumejipanga kuanza kutangaza vivutio vyetu vyote, vikiwemo vya Ukanda wa Kusini, ambavyo ni karibu kabisa na hapa Morogoro. Sambamba na hayo, tunaimarisha miundombinu na huduma za usafiri, hususan usafiri wa ndege. Tunajenga viwanja vya ndege lakini pia tumenunua ndege mpya saba, tatu tayari zimeshawasili. Tumefanya hivyo kwa vile tunatambua kuwa ustawi wa sekta ya utalii kwa kiwango kikubwa inategemea usafiri wa anga. Takriban asilimia 70 ya watalii husafiri kwa kutumia ndege.
Kutokana na hatua tunazozichukua, ni wazi kuwa idadi ya watalii itaongezeka. Hii maana yake ni kwamba, nchi yetu itahitaji wataalam na watoa huduma wenye katika sekta ya utalii. Ni kwa sababu hiyo, narudia tena kukipongeza Chuo hiki kwa kuanzisha kozi ya utalii. Ombi langu kwenu endeleeni kuboresha elimu mnayoitoa na pia shirikianeni na mamlaka husika za utalii nchini katika kuibua na kutangaza vivutio vipya vya utalii. Vipo vivutio vingi ambavyo bado hatujavitangaza.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wanajumuiya wa SUA;
Mabibi na Mabwana;
Moja ya vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuimarisha na kuboresha elimu nchini. Tangu tumeingia madarani tumechukua hatua mbalimbali kuendeleza jitihada zilizoanzishwa na Awamu zilizotangulia katika kuimarisha na kuiboresha sekta ya elimu nchini. Kama mjuavyo, elimu yetu imetoka mbali na kupitia kwenye changamoto nyingi. Hivyo basi, kwa upande wetu, tuliamua tuanze kwa kutoa elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo kila mwezi tunatenga shilingi bilioni 23.868 kuigharamia. Tangu utaratibu huu uanze mwezi Desemba 2015 hadi mwezi Machi 2018, Serikali imetumia takriban shilingi bilioni 650.
Uamuzi huu wa kutoa elimu bila malipo umeongeza idadi ya wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza maradufu. Mathalan, kwa upande wa shule ya msingi, idadi ya wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza imeongezeka kutoka wastani wa watoto milioni 1 hadi kufikia milioni 2. Kwa upande wa sekondari idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa kidato cha kwanza imeongezeka kwa wastani wa takriban asilimia 30. Hii maana yake ni kwamba watoto wengi, hususan kutoka familia masikini, walikuwa wakishindwa kupata elimu kwa kukosa ada au karo.
Kwa upande wa Elimu ya Juu, ninyi hapa mnafahamu vizuri, kuwa tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaonufaika na mikopo kutoka 98,300 mwaka 2015 hadi kufikia takriban 124,000 hivi sasa. Hii imewezekana baada ya Serikali kuongeza bajeti ya mikopo kutoka shilingi bilioni 365. Mwaka wa Fedha 2015/2016 hadi kufikia shilingi bilioni 427 Mwaka 2017/2018. Na siku hizi fedha za mikopo zinatoka kwa wakati. Hata hivyo, ni ukweli kuwa, kutokana na rasilimali fedha kuwa ndogo na mahitaji kuwa makubwa, imefanya isiwe rahisi kutoa mikopo kwa wanafunzi wote. Hii ndio sababu tumeamua kuweka baadhi ya vigezo, ikiwemo uwezo wa familia ya mwanafunzi, masomo anayosomea, n.k. Kwa bahati nzuri, kama mlivyosikia, wanafunzi wa Chuo hiki cha Sokoine ni wanufaika wakubwa wa mikopo inayotolewa. Kati ya wanafunzi wapatao 8,000 wa Chuo hiki, zaidi ya wanafunzi wanafunzi 6,000 wamepata mikopo. Tumeamua kuwapatia mikopo wanafunzi wengi wa Chuo hiki kwa sababu hivi sasa nchi yetu inahitaji wataalamu wengi wa kilimo. Kupanga ni kuchagua.
Ndugu Wana-SUA, Mabibi na Mabwana;
Mbali na kuongeza wigo wa elimu kwa kuongeza idadi ya wanafunzi wa elimu msingi na vyuo vikuu, tunaboresha miundombinu mbalimbali ya taasisi zetu za kutolea elimu. Hivi sasa tupo kwenye utekelezaji wa mradi kabambe wa kukarabati shule za sekondari kongwe 88, zikiwemo Kilakala na Mzumbe zilizopo katika Manispaa hii ya Morogoro. Serikali pia imejenga na kukarabati miundombinu ya shule za msingi na sekondari za wananchi zipatazo 542, ambapo mpaka sasa tumetumia kiasi cha shilingi bilioni 88.402. Aidha, tumefanikiwa kumaliza kwa kiasi kikubwa tatizo la uhaba wa madawati kwenye shule nyingi za msingi na sekondari.
Kwa upande wa elimu ya juu, miradi mbalimbali ya miundombinu inaendelea. Mathalan, hapa SUA, kwenye bajeti ya mwaka huu, tumetoa shilingi bilioni 2 kwa ajili ya kujenga maabara kubwa (Multi-purpose Laboratory), ambayo ujenzi wake unatarajiwa kuanza mwezi Juni 2018. Tumetoa pia shilingi milioni 700 kwa ajili ya kujenga Mgahawa (Cafeteria) itakayochukua wanafunzi 400 kwa mpigo, ambayo nimeambiwa kuwa ujenzi wake unatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2018. Vilevile, hapa SUA, kwenye bajeti ya Mwaka ujao wa Fedha (2018/2019) tumetenga shilingi bilioni 8 kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. Na napenda nitumie fursa hii kumwagiza Waziri wa Elimu fedha zilizotengwa kwa ajili ya kujengea Hosteli katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, shilingi bilioni 2, nazo zihamishiwe hapa SUA ili zisaidie kupunguza kwenye Chuo hiki. Nitoe wito kwa uongozi wa Chuo, kuhakikisha wanatumia vizuri fedha zinazoletwa na Serikali kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Chuo chenu.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wanajumuiya wa SUA;
Mabibi na Mabwana;
Hivi punde nimetoka kusikiliza hoja mbalimbali kutoka kwa wana-Jumuiya wa Chuo hiki. Niseme tu kwa ujumla kuwa hoja zenu nimezipokea. Na kama mtakavyoona, baadhi tayari nimezijibu katika maelezo yangu, hususan kuhusu masuala mikopo na makazi ya wanafunzi. Hoja nyingine nadhani zipo ndani ya uwezo wenu wenyewe kuzitatua. Mathalan, masuala kama michango kuwa mingi kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza, suala la kubebana, n.k. Haya mnaweza kuyatatua ninyi wenyewe. Hivyo basi, nitatumia fursa hii kujibu au kutolea ufafanuzi baadhi ya hoja chache mlizowasilisha.
Kwanza, ni kuhusu suala la kuimarisha uhusiano na nchi ya Israeli, hususan katika masuala ya kilimo. Hili nakubaliana nalo na binafsi sina pingamizi kwa wataalam wetu kutembelea Israeli kwenda kujifunza. Na sio Israeli pekee, pamoja na nchi nyingine. Hatuwezi kuendelea endapo tutabaki tukijifungia tu sisi wenyewe hapa nchini. Hatuna budi tutoke nje ili kupata uzoefu kutoka kwa wenzetu. Na kwa bahati nzuri, nchi yetu ina marafiki wengi ambao wamekuwa wakitupatia fursa nyingi za masomo: Austaralia, China, Cuba, India, Urusi, Marekani, n.k. Lakini kwa bahati mbaya, fursa hizo hatujazitumia vizuri.Hivyo basi, nitoe wito kwa mamlaka husika kuhakikisha nchi yetu inanufaika na fursa hizo za elimu.
Suala la pili ambalo napenda kulizungumzia ni kuhusu madeni ya watumishi. Suala hili nimelieleza kwenye Sherehe za Mei Mosi hivi karibuni. Serikali ina dhamira ya dhati kabisa ya kulipa madeni yote inayodaiwa na watumishi wake. Tangu tumeingia madarakani, tayari tumelipa madai ya watumishi yenye thamani ya takriban shilingi bilioni 220.4. Tuendelea kulipa madeni yaliyosalia kwa kadri tutakavyokamilisha uhakiki. Kama mjuavyo, baadhi ya watumishi hawakuwa wakweli. Walitengeneza madeni mengi ya uongo. Hii ndio sababu inatulazimu tujiridhishe vizuri kabla ya kulipa madeni tunayodaiwa. Hivyo basi, nitoe wito kwa Mheshimiwa Waziri wa Elimu kuwasiliana na vyuo vyako vyote ili kupata madeni halali ya watumishi ili tuweze kuyalipa kwa haraka.
Tatu, ni kuhusu makazi na ofisi za watumishi. Suala hili nalo Serikali inalitambua. Hata hivyo, kutokana na uwezo mdogo wa kifedha na majukumu mengi tuliyonayo hivi sasa, imekuwa sio rahisi kuwapatia watumishi wetu wote makazi. Kama mnavyofahamu, Serikali ina watumishi wapatao laki 5. Hata hivyo, kupitia taasisi na mashirika yetu mbalimbali, tumekuwa tukiendelea kujenga nyumba za gharama nafuu maeneo mbalimbali nchini ili kuwawezesha watumishi kupanga au kununua. Hivyo basi, niwaombe watumishi kuchangamkia fursa hiyo. Aidha, nitumie fursa hii kuziomba taasisi za fedha, hususan benki, kujitahidi kutoa mikopo ya riba nafuu kwa watumishi ili kuwawezesha kununua na kujenga nyumba. Kuhusu tatizo la ofisi, niviombe vyuo vyote nchini kutumia vizuri fedha za malipo ya ada zinazobaki kwenye vyuo kutekeleza miradi ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa ofisi.
Hoja ya mwisho ambayo napenda kuijibu ni kuhusu suala la watumishi wa darasa la saba. Suala hili ni la kisheria na ni hivi majuzi tu Serikali imelitolewa ufafanuzi Bungeni. Lakini, kwa kifupi tu napenda kusema kuwa, Mwaka 2004, Serikali ilitoa Waraka ambao uliweka katazo la kuajiri watu wenye elimu chini ya kidato cha nne kwenye taasisi zake. Uamuzi huu ulifikiwa baada ya kujiridhisha kuwa nchi yetu ilikuwa na wahitimu wengi wa kidato cha nne na kuendelea. Hata hivyo, Waraka huo haukuwahusu watumishi wenye elimu ya darasa la saba ambao tayari walikuwa wameajiriwa. Wao waliendelea na kazi zao kama kawaida kwa vile Sheria hiyo mpya iliwakuta wakiwa tayari kazini. Pamoja na kutolewa kwa Waraka huo, wapo watu, ambao kwa njia za ujanja ujanja, ikiwemo kwa kutumia vyeti vya kughushi, waliajiriwa. Kufuatia zoezi tulilolifanya la uhakiki, tuliwabaini watumishi wa namna hiyo wapatao 14,000 na hivyo ikabidi tuwaondoe kazini. Huu ndio ufafanuzi ambao naweza kuutoa kuhusu suala hili; na kama nilivyosema, hili ni suala la Sheria hivyo sina mamlaka ya kuliingilia.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wanajumuiya wa SUA;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyosema, nimekuja hapa kuwasalimu lakini pia kuwapa moyo ili muendelee kujituma zaidi. Napenda kurudia tena kuwapongeza kwa kazi nzuri na kubwa mnayoifanya lakini pia nawashukuru kwa mapokezi yenu mazuri. Wito wangu kwenu wana-SUA, hususan wanafunzi, someni kwa bidii. Hili ndilo jukumu lililowaleta hapa. Serikali inawapa mikopo kutoka kwenye kodi tunazokusanya kwa wananchi maskini ili muweze kusoma vizuri na hatimaye muweze kulikombea Taifa letu kiuchumi.
Hivyo basi, narudia sana kuwasihi wanafunzi wa Chuo hiki kuitumia vizuri fursa hii adimu mliyopata. Nitawashangaa sana na kwa kweli sitasita kuchukua hatua kali endapo, badala ya kusoma, ninyi mtatumia muda wenu hapa kufanya mambo mengine ambayo hayaendani kabisa na masuala ya elimu: kushiriki kwenye migomo au kuendesha shughuli za kisiasa. Mkifanya hivyo, nitachukua hatua kali. Na hili siwatishi bali nawaeleza ukweli.
Baada ya kusema hayo, narudia tena kusema kuwa, nakipenda sana Chuo hiki, na Serikali itaendelea kukiimarisha ili kiweze kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake.
Mungu Kibariki Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
.jpg)
- May 03, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA BARABARA YA IYOVI - IRINGA –MAFINGA PAMOJA NA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA BARABARA YA IYOVI - IRINGA –MAFINGA PAMOJA NA KIWANDA CHA KUTENGENEZA CHAKULA CHA KUKU (SILVERLANDS TANZANIA LTD)
IHEMI, IRINGA, TAREHE 3MEI, 2018
Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa,
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Mheshimiwa Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda,
Biashara na Uwekezaji;
Bibi Camilla Christensen, Naibu Balozi wa Denmark;
Mheshimiwa Amina Masenza, Mkuu wa Mkoa
wa Iringa na Wakuu wa Mikoa wote mliopo;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Suleiman Kakoso, Mwenyekiti wa Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu;
Waheshimiwa Wabunge na Madiwani wote mliopo;
Viongozi wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Mtendaji Mkuu na Wafanyakazi wa TANROADS;
Viongozi wengine wa Serikali, Vyama vya Siasa
na Dini mliopo;
Waheshimiwa Wageni Wote Waalikwa;
Ndugu Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na kutuwezesha kukutana mahali hapa. Nawashukuru pia Waheshimiwa Mawaziri Prof. Mbarawa na Charles Mwijage, Uongozi wa Mkoa wa Iringa pamoja na Uongozi wa Kiwanda cha Silverlands Tanzania Ltd kwa kunialika kuja kuzindua barabara ya Iyovi – Iringa – Mafinga pamoja na Kiwanda cha Kutengeneza Chakula cha Kuku cha Silverlands Tanzania Ltd. Ahsanteni sana kwa kunialika.
Kwa namna ya pekee, napenda niwashukuru wananchi wa hapa Ihemipamoja na wakazi wote wa Wilaya hii ya Iringa Vijijini kwa mapokezi yenu mazuri. Hii ni mara yangu ya kwanza kuja hapa Ihemi tangu niwe Rais wa nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru sana wana-Ihemi kwa kunipa kura nyingi za “ndiyo” zilizoniwezesha kuchaguliwa. Ahsanteni sana. Nawaahidi nitaendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuwatumikia na kuiletea maendeleo nchi yetu.
Ndugu Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Kama mtakavyokumbuka, moja ya ahadi kubwa tulizotoa wakati wa kampeni ilikuwa kujenga uchumi wa viwanda. Nakumbuka pia tulitaja na kuelezea sifa za viwanda tulivyolenga kuvijenga. Kwanza, vyenye kuajiri watu wengi ili kupunguza tatizo la ajira nchini. Pili, vyenye kutumia malighafi zinazopatikana kwa wingi hapa nchini ili mazao yetu na rasilimali nyingine tulizonazo zipate masoko. Tatu, ambayo bidhaa zake zinatumika kwa wingi hapa nchini na pia kuweza kuuzwa nje ya nchi. Lengo hapa ni kupunguza utegemezi wa kununua bidhaa kutoka nje, lakini pia kuipatia nchi yetu fedha za kigeni. Na nne, vyenye kutumia teknolojia ya kati ili iwe rahisi kwa wananchi wetu kujifunza.
Kiwanda cha Silverlands Tanzania Ltd kinazo sifa zote hizo nne nilizozitaja. Kinaajiri watu wengi. Tumesikia hivi punde kuwa Kiwanda kimetoa ajira zipatazo 938. Hii ni idadi kubwa. Kiwanda pia kinatumia malighafi nyingi za hapa nchini. Wamesema wenyewe hapa, asilimia 80 ya malighafi za Kiwanda chao zinapatikana hapa hapa nchini. Mahindi na Soya. Hii inamaanisha kuwa wakulima wa mazao hayo, hususan wa Wilaya hii ya Iringa Vijijini, hivi sasa wana uhakika wa soko la mazao yao. Aidha, bidhaa zinazozalishwa na Kiwanda (yaani chakula cha kuku) zinatumika kwa wingi hapa nchini. Kama mnavyofahamu, siku hizi Watanzania wengi wanafuga kuku. Lakini kama mlivyosikia, chakula cha kuku wanachozalisha, wanakiuza pia nje ya nchi. Wanauza Ethiopia, Kenya, Nigeria na Uganda. Hii maana yake ni kwamba Kiwanda cha Silverlands kinaingiza nchi yetu fedha za kigeni.
Napenda nitumie fursa kuwapongeza wamilikiwa Kiwanda cha Silverlandskwa kuamua kuwekeza kiasi cha Dola za Marekani milioni 71 hapanchini. Mmetoa ajira kwa Watanzania, mmewapa wakulima soko la mazao yao, mnaipatia Serikali yetu mapato kupitia kodi, na pia kuingiza fedha za kigeni nchini. Ninawashukuru na kuwapongeza sana. Aidha, nawapongeza kwa kuanzisha Kituo cha Mafunzo, ambapo mpaka sasa mmesema mmetoa mafunzo ya watu wapatao 895. Tunawashukuru na kuwapongeza sana. Na ninawahakikishia kuwa Serikali ipo pamoja nanyi. Ninafahamu kuwa yapo matatizo madogo kati ya Kiwanda na wananchi wa hapa, lakini nimefurahi Uongozi wa Kiwanda umeahidi kuyashughulikia. Hilo ni jambo zuri; na ni imani yangu kuwa Kiwanda hiki pia sasa kitaanza kulipa kodi kwa Serikali.
Napenda pia kuipongeza Wizara ya Viwanda kwa kuendelea kuwahamasisha wawekezaji wa hapa nchini na nje ya nchi kuwekeza kwenye sekta ya viwanda nchini. Vilevile, naupongeza uongozi wa Mkoa wa Iringa kwa kuweka mazingira mazuri yaliyowezesha Kiwanda cha Silverlands Tanzania Ltd kujengwa. Nimeambiwa Mkoa wa Iringa hivi sasa una jumla ya viwanda 2,663. Hongereni sana wana-Iringa. Endeleeni kuwavutia wawekezaji kwenye Mkoa wenu ili kusaidia kuondoa tatizo la ukosefu wa ajira, hususan kwa vijana.
Ndugu Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Ili sekta yetu ya viwanda izidi kukua, kustawi na kushamiri, tunahitaji kufanya mambo mawili muhimu. Kwanza, kuimarisha upatikanaji wa nishati ya umeme. Umeme ni injini ya viwanda. Mitambo mingi ya viwandani inahitaji umeme ili iweze kufanya kazi. Pili, miundombinu ya usafiri. Ili malighafi ziweze kufika viwandani zinahitaji kusafirishwa. Na vilevile, ili bidhaa za viwandani ziweze kufika kwenye masoko, zinahitaji huduma ya usafiri. Mathalan, ili mahindi na soya yaweze kufika kwenye Kiwanda cha Silverlands inabidi yasafirishwe. Na vivyo hivyo, ili chakula cha kuku cha Kiwanda cha Silverlands kiweze kufika kwenye masoko, huduma ya usafiri inahitajika. Hii inadhihirisha kuwa miundombinu ya usafiri ni muhimu katika kujenga viwanda.
Ni kwa kutambua hilo, Serikali imeweka mkazo mkubwa katika kujenga miundombinu ya usafiri. Tunajenga reli. Tunapanua Bandari. Tunajenga viwanja vya ndege. Na halikadhalika, tunajenga barabara. Wiki iliyopita nilizindua Barabara ya Dodoma – Babati yenye urefu wa kilometa 251. Juzi tena (Jumapili) nimezindua Barabara ya Fufu – Migori – Iringa yenye urefu wa kilometa 189. Na leo nimefurahi kuja hapa Ihemikuzindua barabara hii ya Iyovi – Iringa – Mafinga yenye urefu wa kilometa 218.6. Nimefurahi sana.
Barabara hii ya Iyovi – Iringa – Mafinga ni muhimu sana, sio tu katika kujenga viwanda, bali pia katika kukuza uchumi wa nchi yetu. Kama mlivyosikia, Barabara hii ni sehemu ya Barabara Kuu ya TANZAM (Tanzania na Zambia) inayoanzia Dar es Salaam na kupita Mikoa ya Pwani, Morogoro, Iringa, Njombe, Mbeya na kuishia Tunduma, Mkoani Songwe, kwenye mpaka wa nchi yetu na Zambia, yenye urefu wa kilometa 918. Barabara hii pia inaungana na Barabara Kuu ya Kaskazini (The Great North) inayoanzia Cairo hadi Cape Town, ambayo inapita kwenye nchi 8. Kwa kuzingatia hilo, ni wazi kuwa, kukamilika kwa barabara hii kutafungua fursa nyingi za kiuchumi kwenye maeneo inakopita. Kuanzia biashara, kilimo, ufugaji, shughuli za misitu, n.k. Na kwa kuwa Barabara hii inapita kwenye maeneo ya vivutio vingi vya utalii, ikiwemo Hifadhi za Taifa za Ruaha, Mikumi, Selous, Milima ya Udzungwa, n.k., ni imani yangu kuwa watalii wengi watakuja. Kwa sababu hiyo, nawasihi sana wananchi wanaoishi kandokando ya barabara hii, kuchangamkia fursa. Itumieni barabara hii kuinua vipato vyenu na kuboresha hali yenu ya maisha. Hayo ndio malengo makuu ya Serikali kukopa fedha ili kujenga barabara hii.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana:
Kama mlivyosikia, ujenzi wa Barabara hii ya Iyovi – Iringa – Mafinga umegharimu shilingi bilioni 283.715. Fedha hizo ni mkopo kutoka kwa marafiki zetu wa Denmark. Mbali na kutufadhili mradi huu, Denmark tulishirikiana nao katika ukarabati wa barabara ya Ubungo – Mlandizi yenye urefu wa kilometa 65.7; Chalinze – Melela yenye urefu wa kilometa 129 pamoja na Chalinze – Segera – Tanga yenye urefu wa kilometa 245. Vilevile, Denmark wamefadhili ukarabati wa barabara za kiwango cha changarawe zenye urefu wa kilometa 900 hapa nchini.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Wananchi wa Tanzania, kutoa shukran zangu nyingi kwa Serikali na Wananchi wa Denmark kwa kutufadhili kutekeleza mradi huu pamoja na miradi mingine ya maendeleo. Tunawashukuru sana, tena sana. Nimefurahi kuona Naibu Balozi wa Denmark, Bibi Camilla yupo hapa. Tunaomba utufikishie shukrani zetu kwenye Serikali na Wananchi wa Denmark. Endeleeni kutuunga mkono. Misaada mtakayotupatia, tutaitumia vizuri. Hakuna senti itakayopotea.
Lakini kupitia kwako, Naibu Balozi, Bi. Camilla, naomba nichomekee jambo moja. Barabara hii mliyotufadhili imejengwa vizuri sana. Na napenda nitumie fursa hii kumpongeza sana Mkandarasi aliyeijenga. Hata hivyo, Barabara hii tatizo lake inapita katikati ya Mji wa Iringa na hivyo imeanza kusababisha msongamano wa magari. Zaidi ya hapo, kama unavyofahamu, kupitisha barabara kubwa kama hii katikati ya mji ni hatari. Hivyo basi, nitumie fursa hii, kuiomba Serikali ya Denmark kuona uwezekano wa kufadhili ujenzi wa Barabara ya Mzunguko ya takriban kilometa 12 ili magari makubwa yasilazimike kupita mjini. Ni imani yangu kuwa Serikali ya Denmark itakubali ombi letu, hata kama itakuwa mkopo.
Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Nimekuja hapa kwa ajili ya kuzindua Kiwanda cha Silverlands Tanzania Ltd na Barabara ya Iyovi - Iringa –Mafinga yenye urefu wa kilometa 218.6. Nimetumia fursa hii pia kuwasalimu na kuwashukuru kwa kunipigia kura. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba niseme maneno machache ya mwisho.
Kwanza, napenda kutumia fursa hii kuendelea kuwahamasisha Watanzania na pia watu kutoka nje kuja kuwekeza nchini. Nchi yetu ina fursa nyingi za kuwekeza kwenye sekta ya viwanda. Tuna sheria nzuri za kuwalinda wawekezaji. Na halikadhalika, tunalo soko kubwa la kuuzia bidhaa. Kama mjuavyo, sisi ni wanachama wa EAC na SADC, ambapo kwa pamoja, Jumuiya hizi zina idadi ya watu wapatao milioni 500. Hili ni soko kubwa la bidhaa.
Pili, wahimiza wananchi na watumiaji wa barabara nitakayoizindua hivi punde, kuhakikisha mnaitunza. Ujenzi wa miundombinu ya barabara kama hii unagharimu fedha nyingi. Hivyo, ni lazima tuzitunze. Aidha, barabara hii haipaswi kuwa chanzo cha ajali. Hivyo, nawasihi madereva kuwa waangalifu pindi wanapoendesha vyombo vya moto barabarani.
Tatu na mwisho, lakini sio mwisho kwa umuhimu, ni kwenu wana-Ihemi na wana-Iringa kwa ujumla. Fursa nyingi sasa zinakuja kwenye Mkoa wenu. Tumeanza kutekeleza mpango kabambe wa kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo katika Ukanda huu wa Kusini. Tunajenga Kiwanja cha Ndege cha Nduli. Barabara ndio kama hivi zinajengwa. Sambamba na hilo, hapa Iringa ni karibu kabisa na Dodoma, ambako Serikali imeamua kuhamishia Makao yake Makuu. Waswahili wanasema, “ukikaa karibu na uaridi lazima utanukia”. Hivyo, nawasihi mjiandae kutumia fursa ambazo Serikali inawaletea.
Lakini nina maombi mawili kwenu. Nawasihi muendelee kuiunga mkono Serikali, hususan kwa kudumisha amani na umoja wetu, kuchapa kazi kwa bidii na bila kusahau kulipa kodi. Ulipaji wa kodi ni muhimu sana. Aidha, nawasihi mjitahidi kujikinga na ugonjwa wa ukimwi. Hali ya ugonjwa huu katika Mkoa wenu sio ya kuridhisha sana.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana, napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa kunialika kwenye shughuli hii. Nawapongeza Wamiliki wa Kiwanda cha Silverlands kwa kuamua kuwekeza hapa nchini. Aidha, naipongeza Wizara ya Ujenzi, TANROADS, wakiongozwa na Mhandisi Mfugalea, pamoja na Mkandarasi kwa kujenga Kiwanda hiki. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, naushukuru uongozi wa Mkoa wa Iringa pamoja na wana-Iringa kwa ujumla kwa mapokezi yenu mazuri mliyonipa tangu nimewasili kwenye Mkoa wenu.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kuzindua barabara ya Iyovi - Iringa – Mafinga yenye urefu wa kilometa 218.6 iliyojengwa kwa gharama za shilingi bilioni 283.715 kwa ufadhili wa Serikali ya Denmark.
Mungu Ibariki Iringa!
Mungu Ubariki Uhusiano kati ya Tanzania na Denmark!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- May 01, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE SHEREHE ZA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI IRINGA, TAREHE...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWENYE SHEREHE ZA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI
IRINGA, TAREHE 1 MEI, 2018
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
Ndugu Tumaini Nyamhokya, Rais wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi,
Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu;
Waheshimiwa Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Balozi Mhandisi John Kijazi,
Katibu Mkuu Kiongozi;
Mheshimiwa Amina Masenza, Mkuu wa Mkoa wa Iringa pamoja na Wakuu wa Mikoa mingine
mliopo;
Mheshimiwa Aisha Nyerere, Jaji Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi ya Mahakama Kuu;
Ndugu Wellington Chibebe, Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Ofisi ya Nchi za Afrika Mashariki;
Ndugu Jayne Nyimbo, Mwenyekiti wa Chama
cha Waajiri Tanzania (ATE);
Waheshimiwa Wabunge na Madiwani mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Ndugu Makatibu Wakuu mliopo;
Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya mliopo;
Dkt. Yahya Msigwa, Katibu Mkuu wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA);
Viongozi Wengine wa Vyama vya Wafanyakazi mliopo;
Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Viongozi wa Vyama vya Siasa na Viongozi wa
Dini mliopo;
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;
Wageni Waalikwa wote;
Ndugu Wana-Iringa, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa napenda nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kukutana hapa. Namshukuru pia Mheshimiwa Waziri Mhagama pamoja na Viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA), wakiongozwa na Rais wake, Bwana Nyamhokya, kwa kunialika tena kushiriki kwenye maadhimisho haya ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, au Mei Mosi, ambayo mwaka huu kitaifa yanafanyika hapa Iringa. Nawashukuru sana kwa kunialika.
Napenda pia kutumia fursa hii kuungana na wazungumzaji walionitangulia katika kutoa pole nyingi za misiba ya viongozi wa vyama vya wafanyakazi iliyotokea tangu tulipoadhimisha sherehe hizi mwaka jana. Vilevile, nawakumbuka wafanyakazi wote waliotutoka katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita. Tuzidi kuwaombea marehemu wote ili Mwenyezi Mungu azipumzishe roho za marehemu mahali pema peponi. Amina.
Ndugu Wafanyakazi na Ndugu Wananchi;
Hii ni mara yangu ya kwanza kuja Iringa tangu nichaguliwe kuwa Rais wa Awamu ya Tano wa nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wana-Iringa kutoka dini zote, makabila yote na vyama vyote kwa kunichagua kuwa Rais wenu. Nawashukuru sana wana-Iringa. Sina cha kuwalipa. Ninachowaahidi tu ni kwamba, nitashirikiana na viongozi wenzangu wa Serikali pamoja na wengine mliowachagua, wakiwemo Waheshimiwa Wabunge na Madiwani, katika kuhakikisha kuwa yale yote tuliyowaahidi tunayatekeleza. Na bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, baadhi ya mambo tuliyoahidi tumeyatekeleza kwa mafanikio makubwa na mengine tunaendelea kuyatekeleza.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;
Leo ni Mei Mosi. Ni Siku ya Wafanyakazi. Naamini wengi wetu hapa tunafahamu kwa nini kila mwaka dunia inaadhimisha Siku hii. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza wafanyakazi wote nchini kwa kuadhimisha Siku hii muhimu. Aidha, nawapongezeni kwa mchango wenu mkubwa mnaoutoa katika kuiletea maendeleo nchi yetu. Hongereni sana wafanyakazi wa Tanzania.
Kwa hakika, mnafanya kazi kubwa. Mnastahili pongezi nyingi kwa mchango wenu mkubwa katika kuliletea maendeleo Taifa letu. Nitumie fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kuwahakikishia wafanyakazi wote nchini kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inatambua mchango wenu na kuuthamini sana. Tunawapenda sana wafanyakazi. Tupo pamoja nanyi. Tutaendelea kushughulikia kero zenu zinazowakabili na kuboresha mazingira yenu ya kazi.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,
Hivi punde tumetoka kusikia Risala nzuri ya TUCTA iliyosomwa na Katibu wake Mkuu, Bwana Msigwa. Kupitia Risala hiyo, TUCTA imeipongeza Serikali kwa kuchukua hatua mbalimbali za kuiletea maendeleo nchi yetu na halikadhalika kutatua baadhi ya kero za wafanyakazi nchini. Zaidi ya hapo, TUCTA imeeleza kuwa haitakuwa tayari kuwatetea wafanyakazi “mabazazi”, yaani wazembe, wavivu, watovu wa nidhamu, wajeuri, wala rushwa, mafisadi, wenye majungu, wafitini, walevi na wote wenye kufanana na sifa hizo. Nawashukuru sana TUCTA.
Ndugu zangu, nidhamu na uwajibikaji kwa mfanyakazi ni jambo la msingi sana. Kwenye hotuba yake ya Mei Mosi mwaka 1974, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema, naomba nimnukuu “Mkulima asiyefanya juhudi katika shamba lake wakati wa kilimo anapunguza mapato ya nchi. Lakini angalau yeye anapata adhabu yake: hatopokea malipo yoyote, mazao yakikosekana au kuharibika kwa sababu ya uvivu wake. Kwa mfanyakazi ipo tofauti. Yeye hapati adhabu anayoipata mkulima. Yeye anaweza kuharibu kazi lakini mwisho wa mwezi anaendelea kupata mshahara wake kamili kama kawaida”, mwisho wa kunukuu.
Hii maana yake ni kwamba nidhamu katika kazi kwa mtumishi ni kitu cha muhimu na cha lazima. Mtumishi au mfanyakazi akiwa mzembe na mvivu, anakosa kutoa mchango katika maendeleo ya Taifa, lakini zaidi ya hapo, anakuwa mnyonyaji kupitia mshahara anaopokea. Hivyo basi, narudia tena kuwashukuru na kuwapongeza viongozi wa TUCTA kwa kuiunga mkono Serikali katika kusimamia nidhamu na uwajibikaji kwenye watumishi wa umma.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,
Sambamba na pongezi walizotoa kwa Serikali na ahadi ya kutotetea ubazazi kwa wafanyakazi, Risala ya TUCTA imewasilisha hoja mbalimbali kwa Serikali. Baadhi ya hoja hizo zinahusu kero za wafanyakazi ambazo wameomba Serikali izishughulikie. Hoja nyingine ni mapendekezo yao kwa Serikali yenye lengo la kuiletea nchi yetu maendeleo zaidi. Kwa ujumla, niseme tu kwamba, hoja zenu zote ni sahihi. Serikali inazikubali na tunazipokea kwa ajili ya kuzifanyia kazi, ikiwa ni pamoja na zile zenye kuhusu Mikataba ya Kimataifa, Fomu za Polisi Na 3 (PF3), ushirikishwaji Wafanyakazi, uboreshaji elimu, masuala ya Walemavu, n.k. Kwa bahati nzuri, watendaji wakuu wa Serikali karibu wote wapo hapa. Naamini wamezisikia, watazichukua na kwenda kuzifanyia kazi. Hata hivyo, pamoja na kwamba tunazichukua hoja zenu zote, naomba mniruhusu na mimi nieleze baadhi ya mambo ambayo Serikali imefanya.
Ndugu Wafanyakazi;
Tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani imefanya mambo mengi yenye manufaa na faida kwa Wafanyakazi. Baadhi ya mambo hayo ni kama ifuatavyo;
(i) Tumefanikiwa kudhibiti mfumko wa bei za bidhaa muhimu nchini. Mathalan, wakati tunaingia madarakani, mwezi Novemba 2015, mfumko wa bei ulikuwa ni wastani wa asilimia 6.6. Tumefanikiwa kuishusha, na hivi sasa, kwa mujibu wa takwimu za mwezi Machi 2018, mfumko wa bei umefikia asilimia 3.9. Hii imekuwa njia nzuri ya kumsaidia mfanyakazi. Kama mnavyofahamu, unaweza kupandisha mshahara, lakini endapo bei za bidhaa zitapanda kiholela, uongezaji wa mishahara unakuwa hauna maana yoyote ile. Kwa sababu hiyo, Serikali itaendelea kufanya jitihada za kudhibiti mfumko wa bei za bidhaa muhimu zisipande kiholela ili kuwapa unafuu wafanyakazi na wananchi kwa ujumla, lakini pia tutahakikisha kuwa bidhaa zote muhimu, kama vile vyakula, mafuta na dawa zinapatikana maeneo yote na tena kwa urahisi zaidi.
(ii) Tunatoa elimu bure, ambapo kila mwezi tunatoa shilingi bilioni 23.8, sawa na shilingi bilioni 285.6 kwa Mwaka. Katika miaka miwili na nusu zimetolewa takriban shilingi bilioni 714. Elimu bila malipo imewanufaisha hadi wafanyakazi kwa vile watoto wenu nao sasa hawalipishwi ada na michango.
(iii) Tumelipa Madeni ya Mifuko ya Hifadhi za Jamii. Serikali ilikuwa ikidaiwa michango ya wafanyakazi, ambapo tangu mwaka 2013 ilikuwa haijalipwa au kulipwa kidogo. Madai yalifikia shilingi Trilioni 1.6. Lakini mpaka sasa tumelipa shilingi trilioni 1.4.
(iv) Tumelipa madeni ya Wazabuni na Wakandarasi kiasi cha shilingi trilioni 2. Kufuatiwa kulipwa kwa madeni hayo, wazabuni wameendelea kutoa huduma kwenye taasisi zetu. Aidha, wakandarasi wameendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo iliyokuwa imekwama; na kukamilika kwa miradi hiyo kumeleta na kutazidi kuleta manufaa kwa wafanyakazi.
(v) Madeni ya Ndani na Nje tunalipa kila mwezi takribani shilingi bilioni 900. Kwa miaka miwili na nusu tumelipa shilingi trilioni 2.7
(vi) Mishahara kila mwezi zinalipwa shilingi bilioni 564.501 baada ya kutoa Watumishi hewa. Awali tulikua tukilipa shilingi bilioni 777. Hii maana yake kwa mwaka tunalipa shilingi trilioni 6.77 na kwa miaka miwili na nusu tumelipa shilingi trilioni 16.935. Na bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, siku hizi mishahara inalipwa kwa wakati.
(vii) Tunatekeleza miradi mbalimbali ya miundombinu na kuboresha huduma za jamii, ambapo kukamilika kwake kutaleta manufaa kwa nchi yetu, ikiwa ni pamoja na kwenu wafanyakazi. Miradi hiyo ni ujenzi wa SGR kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma unaotarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi trilioni 7.06 na hadi sasa tumelipa shilingi trilioni 1.1. Miradi mingine mikubwa ni mradi wa kuzalisha umeme wa Stiglier’s Gorge; ununuzi wa ndege; ujenzi wa barabara na madaraja; miradi ya umeme; viwanja vya ndege; ujenzi wa meli; ujenzi wa miundombinu ya afya na elimu; mikopo elimu ya juu, ambapo mwaka huu wa fedha tunatumia shilingi bilioni 483; ujenzi wa Bandari kubwa Dar es salaam, Mtwara na Tanga (shilingi trilioni 1.1); miradi ya maji (takriban shilingi bilioni 600); ukarabati wa Reli ya Kati na Reli kutoka Tanga na Arusha; ujenzi wa Rada Dar es salaam, Mwanza, Songwe na Kilimanjaro; kusambaza vifaa vya maabara kwenye shule 1,696, n.k. Aidha, kuna miradi mingine mingi inayoendelea ikiwa ni pamoja na mradi wa Bomba la Mafuta; miradi ya kilimo, uvuvi na ufugaji. Miradi na shughuli zote hizi zinaigharimu Serikali fedha nyingi .
Sambamba na hayo, tangu tumeingia madarakani mwaka 2015, tumepata mafanikio makubwa katika kubadilisha taswira ya Utumishi wa Umma. Tulianza na zoezi la kuhakiki Watumishi wa Umma ili kuhakikisha kwamba Watumishi wa Umma wanakuwa wale wenye sifa stahiki. Tumefanikiwa kuondoa Watumishi hewa 19,708 na watumishi wenye vyeti feki 14,152. Haya ni mafanikio makubwa ambayo yametuwezesha kuokoa mabilioni ya shilingi, lakini pia tumeweza kubaki na watumishi wenye sifa ya kufanya kazi. Mazoezi haya mawili yamekamilika mwezi Oktoba mwaka 2017.
Kukamilisha kwa mazoezi hayo ya uhakiki, yametufanya tuanze kuajiri watumishi wapya. Mpaka sasa tumeajiri watumishi wapya 18,101 (walimu 6,495, watumishi wa afya 3752, watumishi wa Mambo ya Ndani 6164, Mahakama watumishi 200, Mafundi Sanifu wa Maabara 386, na watumishi wengine) na tunatarajia kuajiri watumishi wengine 22,150 kabla ya kumalizika kwa mwaka huu wa fedha. Aidha, tumeweza pia kuwapandisha madaraja (promotion) watumishi 88,016 mpaka hivi sasa. Tunategemea kukamilisha promosheni nyingine 25,504 kabla ya kumalizika kwa Mwaka huu wa Fedha. Hivyo, jumla, tutakuwa tumetoa promosheni 113,520 kabla ya mwezi Julai, mwaka huu 2018. Napenda kuwahakikishia kwamba Serikali itaendelea kuajiri watumishi wapya na kuwapandisha madaraja kadri bajeti inavyoruhusu.
Ndugu Wafanyakazi;
Kama mnavyojua, tofauti na ilivyokuwa zamani, siku hizi Serikali siyo mwajiri mkubwa. Sekta Binafsi ndiyo mwajiri mkubwa. Na katika hili, napenda kuipongeza sekta binafsi ya hapa nchini kwa kuendelea kutoa fursa nyingi za ajira kwa Watanzania. Wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani, Sekta Binafsi ilikuwa na watumishi 2,334,969. Katika miaka miwili na nusu iliyopita, ajira hizo zilizoongezeka hadi kufikia 582,073, ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 24.9. Hili ni ongezeko kubwa la ajira.
Aidha, tukijumlisha na ajira za sekta isiyo rasmi, ajira zilizoongezeka zimefikia 1,826,743. Ongezeko hili ni kutokana na miradi mingi inayoendelea kutekelezwa, hususan kwenye miundombinu ya barabara, madaraja, reli, viwanja vya ndege na rada, bandari, miradi ya umeme, ujenzi wa shule na vyuo, miradi ya afya, miradi ya maji, viwanda, miradi ya gesi, pamoja na miradi katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, madini na utalii, n.k. Haya ni mafanikio ya kujivunia ya Serikali ya Awamu ya Tano.
Tunaendelea kuboresha mazingira ya sekta binafsi ili izidi kustawi nchini na kutoa ajira nyingi kwa Watanzania. Kama mnavyojua, dhamira yetu ya Tanzania ya viwanda inaendelea kushika kasi. Viwanda vingi vimeanzishwa nchini na vinaendelea kuanzishwa. Kwa mujibu wa matokeo ya sensa ya viwanda iliyotolewa mwezi Juni 2017, viwanda vipya 3,306 vimejengwa, vikiwemo viwanda vya kati na vikubwa; na vingine vingi vinaendelea kujengwa. Katika Mkoa wa Pwani pekee, zaidi ya viwanda vikubwa 80 vinaendelea kujengwa hivi sasa. Hivi vyote maana yake ni ajira mpya kwa Watanzania.
Ndugu Wafanyakazi;
Kukamilika kwa mazoezi ya uhakiki pia kumeiwezesha Serikali kuanza kulipa malimbikizo ya madeni ya watumishi. Mpaka hivi sasa, tumeshalipa malimbikizo ya madeni ya mishahara ya watumishi 52,851 yenye thamani ya shilingi bilioni 68.323. Aidha, tumelipa madeni yasiyo ya mishahara yeye thamani ya shilingi bilioni 152.304. Hii imefanya jumla ya madeni yote ya watumishi tuliyolipa kufikia shilingi bilioni 220.627, ambapo mengi yalikuwa hayajalipwa tangu mwaka 2007.
Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma wanaendelea kuhakiki na kulipa madeni yaliyosalia kila mwezi. Napenda kuwahakikishia Watumishi wa Umma wote kwamba, yeyote mwenye madai halali atalipwa haki yake. Lakini mwenye madai ya uongo, hatolipwa kamwe.
Ndugu Wafanyakazi;
Kama nilivyosema, Serikali imefanya mambo mengi. Tumetoa ajira, tumelipa madeni yote niliyotaja; tunatoa elimu bure; tunatekeleza miradi mikubwa ya Reli, Bandari, Barabara, Maji, Umeme, Afya. Masuala haya yote yanategemea fedha kutoka mfuko mmoja tu. Sio rahisi kufanya mambo hayo yote, na pia kuweza kupandisha mishahara. Msema kweli ni mpenzi wa Mungu. Ni lazima tuchague. Na mimi kwa mtazamano wangu, nilidhani tuanze kwanza kutekeleza miradi hii mikubwa ya maendeleo ambayo itakapomalizika itatupatia fedha nyingi za kuweza kuongeza mishahara na kufanya mambo mengine ya maendeleo.
Kwa mfano, mimi naamini, tukijenga reli na ikianza kufanya kazi ya kubeba mizigo kwenda nchi za Burundi, Rwanda na pia kuhudumia nchi za DRC na Uganda, itatupatia fedha nyingi za kuweza kupandisha mishahara. Vivyo hivyo, tuktekeleza miradi ya barabara na umeme, tutapata fedha nyingi za kuweza kuongeza mishahara. Tukiongeza bajeti ya afya, wananchi watakuwa na afya njema na hivyo kuweza kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwangu mimi naona mambo hayo ni ya msingi zaidi kwa sasa kuliko kupeleka fedha mahali kwingine.
Nchi yetu imeazimia kujenga uchumi wa viwanda, lakini umeme tulionao ni takriban Megawati 1,500. Hivyo, kwangu mimi naona kutekeleza Mradi wa Umeme wa Stiglier’s Gorge utakaogharimu takriban shilingi trilioni 3 kuzalisha Megawati 2,100 ni muhimu zaidi kwa sasa kuliko kupeleka fedha hizo mahali kwingine. Kwangu mimi naona ni busara kutoa fedha za kujenga barabara za kuunganisha Mkoa wa Iringa na mikoa mingine pamoja na kujenga Uwanja wa Ndege wa Nduli ili utuletee watalii wengi, hususan katika kipindi hiki ambacho tumeamua kuifanya Iringa kuwa kitovu cha utalii kwenye Ukanda huu wa Kusini, kuliko fedha hizo kuzipeleka mahali kwingine. Kwangu mimi naona ni jambo jema kutoa fedha takriban shilingi bilioni 23.8 kwa mwezi kugharamia elimu bure ili watoto wengi wa maskini wapate elimu, kuliko kutumia fedha hizo kulipana mishahara. Kwangu mimi pia naona ni vizuri kutoa shilingi bilioni 483 kuwakopesha watoto wa maskini ili waweze kwenda kwenye Vyuo Vikuu, kuliko kutumia fedha hizo kujiongezea mishahara. Kupanga ni kuchagua.
Lakini, mbali na miradi hiyo ya maendeleo, nawaomba wafanyakazi mkumbuke kuwa, kwenye nchi yetu wapo pia wakulima, wafugaji na wavuvi, ambao nao wanahitaji maisha yaliyo bora. Hivyo, wakati tunajifikiria sisi, na wao pia tuwafikirie.
Pamoja na ukweli huo, matumaini bado yapo. Napenda nitumie fursa hii kuwahakikishia Wafanyakazi kuwa, baada ya kukamilisha mazoezi ya kuhakiki na kuanza kuajiri watumishi wapya, jambo kubwa ambalo sasa ni kipaumbele changu kwa watumishi wa umma ni kuboresha mishahara na maslahi mengine ya wafanyakazi. Nafarijika sana kwamba sasa tumeanza kukaa kwenye mstari, nidhamu imerejea, uadilifu unazidi kujengeka, mnafanya kazi kwa uzalendo na weledi, isipokuwa wachache ambao tutazidi kuwachukulia hatua stahiki. Tunaendelea kukamilisha ulipaji wa madeni ya watumishi. Lakini mwaka huu pia tutaendelea kutoa nyongeza ya mwaka ya mishahara (Annual increment). Naomba mniamini.
Ni bahati mbaya tu Katibu Mkuu wa TUCTA amenichomekea kuwa kwenye Sherehe za Mei Mosi mwaka jana niliahidi kupandisha mishahara. Hiyo sio kweli. Mwaka jana sikuahidi kupandisha mishahara. Na hotuba yangu ipo. Hata hivyo, leo ndio naweza kuahidi. Kama miradi hii itaenda vizuri, kama wafanyakazi mtaendelea kujituma na kuchapaka kazi kama mnavyofanya sasa, na kama Vyama vya Wafanyakazi vitaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Serikali kama sasa, nawaahidi, na naomba mninukuu vizuri kuwa, kabla sijamaliza muhula wangu wa uongozi nitapandisha mshahara. Na nitakapopandisha, itakuwa kiwango kikubwa. Sio shilingi elfu 10. Narudia tena. Naomba wafanyakazi mniamini. Mimi ni mfanyakazi mwenzenu. Nilikuwa Mwalimu. Ninafahamu shida za wafanyakazi na kwa kweli ninawapenda sana wafanyakazi wenzangu. Kama ingekuwa inawezekana hata leo ningepandisha. Hata hivyo hali kwa sasa hairuhusu. Hivyo, narudia tena kuwasihi muwe wavumilivu na kuendelea kuchapa kazi kwa bidii ili tuweze kukuza uchumi wetu na hatimaye tutengeneze maisha bora ya baadaye. Mimi naamini kuwa miradi ya maendeleo tunayoitekeleza itakapokamilika, haitachukua muda mrefu kupandisha mishahara. Hata hivyo, kwa sasa, tutaendelea kuweka mkazo mkubwa katika kudhibiti mfumko wa bei.
Ndugu Wafanyakazi;
Mwaka jana katika risala yenu mliomba zoezi la kuunganisha mifuko likamilike mapema. Napenda kuwafahamisha kwamba zoezi hilo limekamilika baada ya Bunge kupitisha Sheria tarehe 31/01/2018 na mimi kuisaini tarehe 08/02/2018. Kilichobaki sasa ni kuanza kutumika kwa Sheria hiyo ambapo kutakuwa na mifuko miwili. Mfumko mmoja wa Watumishi wa Umma na mwingine kwa ajili ya Sekta Binafsi. Sheria iliyotungwa mbali na kuanzisha Mfuko wa Hifadhi ya Watumishi wa Umma (PSSSF) imefanya marekebisho katika Sheria ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (The National Social Security Fund Act) Sura ya 50 ili kuifanya NSSF kuhudumia Watumishi wa Sekta Binafsi wakiwemo Wakulima, Wafugaji, Wavuvi, Wajasiriamali wadogo (machinga na mama lishe).
Uunganishaji wa mifuko hii, unategemewa kurahisisha ulipaji wa mafao, kupunguza gharama za uendeshaji wa mifuko na hivyo kuboresha mafao ya wanachama. Katika kipindi hiki pia, kama nilivyoeleza hapo awali, tumeweza kulipa deni la shilingi trilioni 1.4 ya malimbikizo ya michango ya wanachama kwenye mifuko ya pensheni. Malipo haya yamewezesha wastaafu kuendelea kulipwa mafao yao kama wanavyostahili. Napenda kutumia fursa hii kuziagiza Mamlaka husika kukamilisha kwa haraka taratibu husika ili Mifuko hii ianze kazi mara moja; maana naanza kuona dalili za kuwepo kwa kigugumizi na kusuasua katika kukamilisha taratibu za kuanzisha Mifuko hiyo.
Ndugu Wafanyakazi,
Risala yenu pia imegusia suala la makato ya kodi ya mshahara (Pay As You Earn – PAYE); viwango vya mishahara, hususan ya kima cha chini; na vikao vya Bodi za Kima cha Chini cha Mishahara, Bodi za Mishahara pamoja na Chombo cha Ushauri (Labour Economic and Social Council – LESCO). Kuhusu suala hili, napenda kwanza niseme kuwa masuala haya ya maslahi kimsingi yanategemea pia uwezo wa kifedha wa Serikali. Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kusema ‘A calf can only suck the amount of milk her mother cow produces (yaani, ndama hunyonya kulingana na kiwango cha maziwa aliyonayo mama yake)”.
Lakini, pamoja na ukweli huo, Serikali kwa kile kidogo ilichonacho, imekuwa ikijitahidi sana kuboresha maslahi ya watumishi wake. Mathalan, kuhusu suala la PAYE, mwaka juzi tulipunguza kwa asilimia 2 kodi ya mshahara kutoka asilimia 11 hadi asilimia 9. Hii ilitufanya tufanikiwe kufikia malengo tuliyokubaliana (kati ya Serikali na Vyama vya Wafanyakazi) ya kuwa na kiwango cha tarakimu moja (single digit), miaka miwili kabla ya muda uliotakiwa.
Ndugu Wafanyakazi;
Kuhusu suala la ucheleweshaji wa kesi za Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi, kama mlivyosikia hivi karibuni nimeteua Majaji 12 wa Mahakama Kuu. Hivyo basi, ni imani yangu kuwa uteuzi huo utapunguza tatizo lililokuwepo la uhaba wa majaji na hivyo kusaidia kupunguza kero ya ucheleweshaji wa kesi kwenye Mahakama Kuu Kitengo cha kazi.
Kuhusu suala la Watumishi wenye Vyeti vya Darasa la Saba, napenda tu niwakumbushe kuwa uamuzi wa Serikali kuendesha zoezi la ukaguzi wa vyeti ulilenga kulinda hadhi ya elimu nchini lakini pia kuamsha ari ya utendaji kazi kwa watumishi wenye sifa. Ni bahati mbaya tu katika kutekeleza zoezi hilo, yalitokea mapungufu. Lakini bahati nzuri, Serikali iliona mapungufu hayo, na kama mlivyosikia Waziri mwenye dhamana tayari ametoa msimamo wa Serikali Bungeni hivi majuzi. Kilichobaki sasa ni utekelezaji. Lakini, endapo bado mfanyakazi ataona ameonewa, namshauri afuate taratibu. Kama ambavyo nimekuwa nikisema, Serikali hii inawapenda wafanyakazi. Hatutaki kumwonea mfanyakazi yoyote. Hatutaki kuona mfanyakazi akinyanyasika. Na katika hili, napenda kurudia, kwa mara ya mwisho, agizo langu kuhusu kutomwamisha mtumishi kabla ya kumlipa fedha zake. Sitarudia tena kusema hili. Atakiuka agizo hili, hatutasita kumshughulikia. Na naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kulisimamia hilo.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,
Kama nilivyosema, mbali na hoja hizo zilizohusu kero za wafanyakazi, Risala ya TUCTA pia imetoa mapendekezo na ushauri mbalimbali kwa Serikali kwa lengo la kuiletea nchi yetu maendeleo. Pendekezo lenu la kwanza linahusu umuhimu wa kutangaza vivutio vya utalii. Risala imeeleza kuwa Tanzania inashika nafasi ya pili kwa vivutio vya utalii duniani baada ya Brazil. Licha ya ukweli huo, idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu ni ndogo. Mmetaja sababu mojawapo yenye kusababisha hali hii kuwa ni kushindwa kwetu kutangaza vivutio vyetu. Hilo ni kweli kabisa. Lakini naomba niongeze sababu nyingine. Hatupati watalii wengi kwa vile, kwa muda mrefu, sekta ya usafiri wa anga nchini ilikuwa hoi bin taabani. Na kama mnavyofahamu, asilimia 70 ya watalii hutumia usafiri wa anga.
Kwa kutambua hilo, tumeanza kuchukua hatua za kutangaza vivutio vyetu mbalimbali na kuimarisha usafiri wa anga. Ninyi wana-Iringa mnafahamu vizuri. Mwezi Februari 2018, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, alizindua mpango kabambe wa kutangaza vivutio vya Ukanda huu wa Kusini ujulikanao kwa jina la Resilient Natural Resorce for Tourism and Growth (REGROW), ambapo takriban Dola za Marekani milioni 150, ambazo ni sawa na takriban shilingi bilioni 330 zitatumika. Kama mnavyofahamu, Ukanda huu wa Kusini, kama ulivyo Ukanda wa Kaskazini, una vivutio vingi, ikiwemo Hifadhi ya Ruaha yenye kusifika kuwa na tembo wengi, Hifadhi ya Kitulo, au maarufu kama Bustani ya Mungu, ambayo ina maua ndwele ambayo hayapatikani mahali popote duniani, Maporomoko ya Kalambo ambayo ni ya pili Barani Afrika, maeneo ya kihistoria ya Kalenga na Isimila, n.k.
Sambamba na mkakati huo wa kutangaza vivutio, kama nilivyosema awali, tunaimarisha pia usafiri wa anga. Hivi sasa, tunajenga viwanja takriban 11 vya ndege kikiwemo kiwanja cha hapa Iringa, ambacho ujenzi wake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 90. Tumenunua pia ndege mpya 7, tatu tayari zimewasili na zimeanza kufanya kazi, na nyingi nne zinatarajiwa kuwasili baadaye mwaka huu, zikiwemo ndege kubwa mbili aina ya Boieng Dreamliner zenye uwezo wa kubeba watu 264. Tuna matumaini makubwa kuwa kutokana na hatua hizi, watalii wengi watatembelea nchi yetu na mchango wa sekta ya utalii, ambayo hivi sasa inaongoza kwa kuipatia fedha nyingi za kigeni nchi yetu, itazidi kuimarika.
Ndugu Wafanyakazi;
Kwenye Risala yenu pia mmegusia umuhimu wa kuwaelimisha wananchi kuhusu viwanda pamoja na kuwekeza kwenye miundombinu wezeshi. Serikali imekuwa ikijitahidi sana kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa viwanda na aina ya viwanda tunavyovitaka.
Kwa kifupi napenda kusema kuwa viwanda vina faida nyingi, ajira, mapato; n.k. Na kuhusu aina ya viwanda tunavyovilenga ni vile vyenye kuajiri watu wengi; vyenye kutumia malighafi zinazopatikana kwa wingi nchini; vyenye kutumia teknolojia ya kati; na ambavyo bidhaa zake zinahitajika kwa wingi hapa nchini lakini pia zinaweza kuuzwa nje ya nchi. Aina hizi za viwanda ni kama vile vya nguo, bidhaa za ngozi pamoja, usindikaji mazao ya kilimo, n.k. Kwa bahati nzuri, wana- Iringa ni wakulima wazuri wa mazao mbalimbali, hivyo wanayo nafasi kubwa katika kujenga Uchumi wa Viwanda nchini.
Ndugu Wafanyakazi;
Risala yenu pia imetoa ushauri kwa Serikali kuimarisha sekta ya elimu, hususan kuliangalia kwa makini suala la tofauti kubwa kati ya wavulana na wasichana kwenye taasisi za elimu; na halikadhali kusimamia suala la ubora wa elimu inayotolewa. Niseme tu kwamba suala la elimu ni ajenda muhimu ya Serikali ya Awamu ya Tano. Tangu tumeingia madarakani tumechukua hatua mbalimbali za kuboresha na kuimarisha sekta hii nyeti na muhimu kwa maendeleo ya nchi. Hatua hizo tayari nimezieleza hapo awali. Elimu bure, nyongeza kubwa ya bajeti ya mikopo ya wanafunzi wa vyuo vikuu kutoka shilingi bilioni 365 mwaka 2015/2016 hadi kufikia shillingi bilioni 427 Mwaka huu wa Fedha, ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya elimu (shuleni, vyuoni na kwenye vyuo vikuu). Haya yote yamewezekana kufuatia uamuzi wa Serikali kuongeza bajeti ya elimu. Mwaka 2016/2017 tulitenga shilingi trilioni 1.36 na Mwaka huu wa Fedha shilingi trilioni 1.4. Hivyo basi, niwaombe wazazi kote nchini, kuwahimiza watoto wao, wa kike na wa kiume, kutumia fursa hiyo iliyotolewa na Serikali.
Kwa upande wa kuboresha elimu yenyewe, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali. Mathalan, kwenye shule za sekondari tumesambaza vifaa vya maabara kwenye shule takriban 1,696. Tumewaajiri mafundi sanifu wa maabara wapatao 386. Aidha, katika Mwaka huu wa Fedha, mpaka sasa, tumewaajiri walimu takribani 6,500 wa shule za msingi na sekondari, wakiwemo walimu 3,728 wa masomo ya sayansi na hisabati. Kwa upande wa elimu ya juu, bila shaka, mlisikia hatua tuilizochukua za kufungia baadhi ya vyuo kudahili wanafunzi au kutodahili wanafunzi kwenye baadhi ya fani, baada ya kujiridhisha kuwa havina sifa. Tulifanya hivyo ili kuhakikisha tunalinda ubora wa elimu inayotolewa hapa nchini.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,
Nimezungumza mengi sana. Na leo ni Siku ya Wafanyakazi. Hata hivyo, kama nilivyosema mwanzoni, leo ni mara yangu ya kwanza kufika Iringa tangu niingie madarakani. Kwa sababu hiyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba kwa haraka haraka mniruhusu niseme mambo machache yenye kuhusu Mkoa huu wa Iringa. Tayari nimeeleza kuhusu Uwanja wa Ndege wa Nduli, tumepanga kupeleka umeme kwenye vijiji vyote 179 vya Mkoa huu ambavyo havina umeme kupitia REA Awamu ya Tatu.
Sambamba na hayo, tunaendelea kuboresha huduma za afya. Hivi sasa tunafanya ukarabati wa Hospitali ya Mkoa, na napenda kuwaahidi hata mgogoro wa kiwanja wa Hospitali hiyo, nao tutaushughulikia. Tumekamilisha upanuzi wa Hospitali ya Wilaya ya Iringa Manispaa, na hivi sasa tupo kwenye upanuzi wa Hospitali ya Wilaya ya Halmashauri ya Mafinga. Na kesho naenda kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Wilaya Kilolo. Tunafanya ukarabati na upanuzi wa vituo vya Idodi (Iringa Vijijini); Kidabaga (Kilolo); Ihongole (Mafinga) na Malangali (Mufindi). Haya yote yamewazekana kutokana na Serikali kuongeza bajeti za Wizara ya Afya. Mwaka wa Fedha 2016/2017 tulitenga shilingi trilioni 1.8 na Mwaka huu wa Fedha (2017/2018) shilingi trilioni 2.2.
Kuhusu maji, nafahamu kuwa kuna Wilaya tatu za Mkoa huu zenye kukabiliwa na shida kubwa ya uhaba wa maji, ambazo ni Kilolo, Ilula na Mafinga. Lakini nafahamu pia kuwa hivi sasa kuna takriban miradi 14 yenye thamani ya shilingi bilioni 18.24 inayotekelezwa kwenye Mkoa huu. Aidha, wadau wa maendeleo wanatekeleza miradi mingine 10 kwa thamani ya shilingi bilioni 3.512. Kwenye barabara, TANROADS ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 17.948 kwa ajili ya kuhudumia barabara zake; na TARURA imetengewa shilingi bilioni 9.657 kwa ajili ya kuhudumia barabara zake. Vilevile, tupo mbioni kuanza ujenzi wa barabara ya lami kutoka Iringa mjini hadi Msembe katika Wilaya hii ya Iringa Vijijini yenye urefu wa kilometa 104, ambayo Mheshimiwa Waziri Mahiga ameilezea vizuri.
Mabibi na Mabwana; nafahamu ninyi wana-Iringa ni wakulima wazuri wa mazao mbalimbali. Mwezi Julai mwaka jana Serikali ilifuta tozo 87 za kilimo ili kuwapunguzia wakulima kero ya utitiri wa kodi. Aidha, tulipiga marufuku utozaji kodi wa mazao yanayosafirishwa kutoka Halmashauri moja kwenda nyingine, ambayo hayazidi tani moja. Ni matumaini yangu kuwa kwenye halmashauri hii hamlipishwi ushuru. Kwa marafiki zangu, Wamachinga na Mama Nitilie, Serikali imeanza kuwarasimisha wajasiliamali wadogo kwa kuwapatia vitambulisho maalum, ambavyo mtavilipia kwa kiasi kidogo. Lengo la kuanzisha vitambulisho hivyo ni kuwawezesha kufanya shughuli zenu bila kubughuziwa lakini pia kuchangia maendelea ya nchi yetu.
Ndugu Wafanyakazi wenzangu;
Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuwashukuru kwa kunialika. Napenda niwahakikishie wafanyakazi kote nchini kuwa Serikali yenu inawathamini sana. Nawaahidi tutaendelea kuboresha mazingira yenu ya kufanyia pamoja na maslahi yenu, kadri uwezo wa kufanya hivyo utakavyokuwa ukiongezeka. Napenda niwapongeze Chama Cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara, Taasisi za Fedha, Huduma na Ushauri (TUICO) kwa maandalizi mazuri ya shughuli hii. Nawapongeza pia waandamanaji kwa namna mlivyopendeza. Kwa hakika, shughuli zimefana sana.
Napenda pia kuwashukuru wageni wote waalikwa, wakiwemo Mabalozi, kwa kushiriki kwenye Siku hii muhimu. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru wana-Iringa, mkiongozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, Mheshimiwa Amina Masenza, Wakuu wa Wilaya pamoja na wana-CCM kwa mapokezi yenu mazuri. Napenda niwahakikishie kuwa yale yote tuliyoahidi, tutayatekeleza. Niwaombe tu tuendelee kudumisha amani na umoja wetu.
Mwisho kabisa, ni kuhusu suala la UKIMWI. Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti uliotajwa na ofisi yetu ya Taifa ya Takwimu inaonesha kuwa Mkoa wa Iringa umeshika nafasi ya pili baada ya Njombe. Hapa maambukizi ni asilimia 11.2 wakati Njombe ni asilimia 11.6. Hii inatisha. Hivyo, nawaomba wana – Iringa kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huu hatari. UKIMWI bado ni tishio.
Mungu Wabariki Wafanyakazi wa Tanzania!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Apr 26, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA SHEREHE ZA MIAKA 54 YA MUUNGANO, DODOMA, 26 APRILI, 20...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA SHEREHE ZA MIAKA 54 YA MUUNGANO, DODOMA, 26 APRILI, 2018
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan,
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Akinwumi Ayodeji Adesina,
Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa,
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Job Ndugai,
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
MheshimiwaMartin Ngoga, Spika wa Bunge
la Afrika Mashariki;
MheshimiwaProf. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mzee Mkapa, Rais Mstaafu wa Awamu
ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Viongozi Wastaafu wote mliopo;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi Wakuu,
mkiongozwa na Mama Fatuma Karume;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Viongozi wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wazee wa Mkoa wa Dodoma, Wageni Waalikwa wote;
Ndugu Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Tarehe kama ya leo Mwaka 1964, Mataifa mawili ya Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar yaliungana na kuunda Taifa jipya, ambalo kwa sasa linajulika kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Taifa hili jipya lilizaliwa baada ya aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Tanganyika, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kutia saini Hati ya Muungano kuunganisha nchi hizi mbili mwezi Aprili, 1964 na baadaye Hati hiyo kuridhiwa na Mabunge ya nchi zote mbili.
Mambo mengi yamewezesha kuwepo kwa Muungano huu. Kwanza, ni maono ya mbali ya waasisi wa Muungano, Mwalimu Nyerere na Mzee Karume, hususan kuhusu utengamano wa Bara la Afrika. Pili, ukaribu wa Kijiografia uliopo kati ya Tanganyika na Zanzibar. Tatu, ni mahusiano ya kidugu na urafiki baina ya wananchi wa Zanzibar na Tanganyika, ambayo yalichagizwa na lugha moja ya Kiswahili na mwingiliano wa masuala ya utamaduni. Na nne, uhusiano wa karibu na kirafiki uliokuwepo kati ya vyama vilivyopigania uhuru wa nchi zetu mbili, yaani Tanganyika African National Union (TANU) na Afro Shiraz Party (ASP).
Ndugu wananchi, Mabibi na Mabwana;
Napenda nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwanza kabisa kwa kutuwezesha kuiona siku ya leo; lakini pili kwa kuendelea kuulinda Muungano na Taifa letu kwa ujumla. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza Watanzania wote; wa dini zote, makabila yote, vyama vyote, rangi zote, waliopo hapa nchini na nje ya nchi, kwa kuadhimisha Sherehe hizi za Miaka 54 ya Muungano wetu na kuzaliwa Taifa letu. Happy Birthday Tanzania! Happy Birthday Watanzania wenzangu! Happy Birthday Muungano wetu!
Naomba pia mniruhusu niwashukuru wageni wetu mbalimbali, Waheshimiwa Mabalozi pamoja na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa, ambao wamekuja kuungana nasi kwenye Sherehe hizi, ikiwa ni pamoja na Spika wa Bunge la Afrika Mashariki pamoja na Wabunge wote wa Afrika Mashariki. Lakini, kwa namna ya pekee kabisa, napenda nimshukuru na kumkaribisha Mgeni wetu, Mheshimiwa Dkt. Akinwumi Adesina, Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, pamoja na ujumbe wake wote. Mheshimiwa Dkt. Adesina karibu sana nchini kwetu. Mimi pamoja na Wanazania wenzangu tumepokea kwa furaha kubwa ujio wako na tunakushukuru kwa sana kuungana nasi kwenye Maadhimisho haya
Ndugu wananchi, Mabibi na Mabwana;
Benki ya Maendeleo ya Afrika ni taasisi muhimu sana yenye kutoamchango mkubwa wa maendeleo kwa Bara letu. Inatoa ufadhili wa fedha lakini pia ushauri wa kitaalam. Kwa bahati nzuri, Tanzania ni miongoni mwa nchi waanzilishi na piawanufaika wakubwawa Benki hii. Mathalan, tangu imeanza kufanya shughuli zakehapa nchinimwaka 1971, tumenufaika na ufadhili wa kifedha yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 3.457, ambapo kwa sasa wanatekeleza hapa nchini jumla ya miradi 25 yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.986.
Kesho natarajia kuambatana na Mhe. Dkt. Adesina kwenda Kondoa kuzindua barabara ya Dodoma – Babati yenye urefu wa kilometa 251 ambayo tumeshirikiana na Benki ya Maendeleo Afrika kuijenga. Benki hii pia ndio waliotufadhili kujenga barabara ya Dodoma – Iringa yenye urefu wa kilometa 260, barabara ya Bububu – Mkokotoni yenye urefu wa kilometa 31 pamoja na kuboresha barabara za vijijini zenye urefu za urefu kilometa 21 Zanzibar.
Kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Watanzania wote napenda kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu nyingi Benki ya Maendeleo Afrika kwa ufadhili wanaotoa kwa nchi yetu. Baada ya kutokahapa Uwanjani, nitaenda kufanya mazungumzo na Dkt. Adesina. Na kwa jinsi ninavyomfahamu, nina uhakika, ataahidi mambo mengine mazuri kwa nchi yetu, ikiwemo miundombinu katika Manispaa ya Dodoma.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Watanzania wenzangu;
Mabibi na Mabwana;
Sio siri kuwa katika kipindi cha Miaka 54 ya Muungano wetu, nchi yetu imepata mafanikio mengi makubwa. Fanikio la kwanza na kubwa kabisa ni kudumisha na kuimarisha Muungano wenyewe. Wapo wenzetu wengi walijaribu kuunda Muungano kama wetu, lakini hawakufanikiwa. Sisi tumeweza, na leo Muungano wetu umefikisha miaka 54. Sambamba na hilo, tumeweza kuuimarisha. Mathalan, tumeongeza idadi ya maeneo ya ushirikiano. Mwaka 1964 wakati nchi zetu zinaungana, maeneo ya ushirikiano yalikuwa 11 tu. Lakini mpaka sasa tuna maeneo ya ushirikiano 22, na yote yameongezwa kwa mujibu wa sheria na kufikia maridhiano.
Vilevile, Muungano wetu umeifanya nchi yetu kuwa yenye sauti, nguvu, kujiamini na kuheshimika kimataifa. Tumeweza kulinda uhuru na mipaka yetu; na tunajiamulia mambo yetu sisi wenyewe. Zaidi ya hapo, Muungano wetu umeiwezesha nchi yetu kutoa mchango mkubwa katika masuala mbalimbali ya kimataifa, ikiwemo kusaidia harakati za ukombozi, kutetea haki za wanyonge pamoja na kusuluhisha migogoro sehemu mbalimbali duniani.
Halikadhalika, Muungano wetu umetuwezesha kupata mafanikio makubwa katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Sio siri kuwa Tanzania ya leo sio ile ya mwaka 1964.Tumejenga miundombinu ya umeme pamoja na usafiri wa nchi kavu, anga na majini. Aidha, tumeimarisha na kuboresha upatikanaji wa huduma za jamii. Idadi ya taasisi za kutolea elimu na na huduma za afya nazo zimeongezeka maradufu. Haya ni baadhi tu ya mafanikio tuliyopata katika kipindi cha miaka 54 ya Muungano wetu. Yapo mengine mengi. Nikiyataja yote tutakesha.
Napenda kutumia fursa hii kwanza kabisa kuwashukuru na kuwapongeza waasisi wetu, Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere pamoja na Sheikh Karume kwa mchango wao mkubwa uliosaidia kupatikana kwa mafanikio haya. Nimefurahi kuona kuwa katika Sherehe hizi tunaye Mama Fatuma Karume. Tunawashukuru sana mama yetu pamoja na Mama Maria Nyerere kwa kuendelea kuunga mkono Muungano wetu.
Napenda pia kuwashukuru na kuwapongeza viongozi waliowafuatia kwa michango yao mbalimbali waliyoitoa. Natambua mchango wa Marais Wastaafu Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa na Mzee Kikwete; Marais wote wa Zanzibar Wastaafu, Makamu wa Rais na Mawaziri Wakuu Wastaafu, pamoja na viongozi na wazee wote wastaafu ambao wametumikia Taifa kwa uaminifu na uadilifu mkubwa katika kuimarisha Muungano wetu. Tunawashukuru sana wazee wetu. Lakini kwa namna ya pekee kabisa, napenda niwashukuru Watanzania wote kwa michango yenu mbalimbali iliyowezesha kupatikana kwa mafanikio haya. Niseme tu kwamba, bila ninyi, mafanikio haya niliyoyataja kamwe yasingepatikana.
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Hakuna jambo zuri lenye kukosa kasoro. Muungano wetu pia changamoto zake. Lakini. kwa bahati nzuri, pande zote mbili za Muungano zimeweka utaratibu mzuri wa kushughulikia changamoto zilizopo. Nitumie fursa hii kumpongeza Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, Mwenyekiti wa Kamati ya kushughulikia masuala ya Muungano, kwa kazi kubwa na nzuri, ambayo Kamati yake inafanya kushughulikia changamoto zilizopo. Nawapongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Serikali zote mbili, ambao ni wajumbe wa Kamati hiyo.
Nina matumaini makubwa kuwa, kupitia majadiliano yanayoendelea kwenye Kamati hii na kwa ushirikiano wa wananchi wote, hatimaye tutaweza kumaliza changamoto zilizopo. Na katika hili, niseme tu kwamba nimefurahishwa na kaulimbinu ya Sherehe za Muungano Mwaka huu, ambayo inasema “Miaka 54 ya Muungano: Muungano wetu ni Mfano wa Kuigwa Duniani; Tuuenzi, Tuulinde, Tuuimarishe na Kuudumisha kwa Maendeleo ya Taifa Letu”. Tukitekeleza kwa vitendo kaulimbiu hii tutaweza kutekeleza dhamira ya waasisi yetu.
Waheshimiwa Viongozi na Wageni Waalikwa;
Ndugu Watanzania wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Leo sio siku ya hotuba. Ni siku ya sherehe. Na kwa hakika, baada ya kushuhudia burudani nzuri kutoka kwa askari wetu, vijana chipukizi na vikundi mbalimbali vya burudani, haitakuwa busara niendelee kuwachosha kwa hotuba ndefu. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba mniruhusu niseme masuala machache ya mwisho.
Kwanza, napenda kurudia tena kuwakumbusha Watanzania wenzangu kwamba Muungano wetu ndiyo nguvu yetu na silaha yetu kama Taifa. Hivyo, kila mmoja wetu ana wajibu wa kuulinda. Wananchi mna wajibu wenu, na Serikali nayo ina wajibu wake. Kwa upande Serikali, napenda niwahakikishie kuwa Serikali zetu mbili, yaani ya Jamhuri ya Muungano na ile ya Zanzibar, inaoongozwa na Mhe. Dkt Shein, zipo imara katika kuulinda Muungano wetu. Tutashirikiana katika kuulinda na kamwe, narudia tena, kamwe hatutamwonea aibu au huruma mtu yeyote, awe wa hapa nchini au nje ya nchi, mwenye nia ya kuvuruga Muungano wetu.
Pili, napenda kuendelea kuwahimiza Watanzania wenzangu tuendelee kuilinda na kuitunza amani yetu. Amani ni suala muhimu. Amani ni msingi wa maendeleo. Hivyo, Watanzania tushirikiane katika kuilinda amani yetu. Msikubali kutumika na watu wachache wenye nia ya kuharibu amani yetu; lakini pia toeni ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama. Kwa upande wetu Serikalini, kama nilivyosema kuhusu Muungano, ipo imara katika kuilinda na kuitunza amani yetu. Hatutamwonea soni mtu yeyote mwenye nia ya kuvuruga amani tuliyonayo nchini kwetu.
Tatu, napenda kutumia fursa hii, leo tunaposheherekea Miaka 54 ya Muungano wetu, kuwahakikishia Watanzania na hasa wana-Dodoma kuwa, azma ya Serikali kuhamia hapa Dodoma ipo palepale. Hakuna kurudi nyuma. Na tayari watumishi zaidi ya 3,800 wameshahamia, nami kama nilivyoahidi, nitahamia mwaka huu. Dodoma ndio Makao Makuu ya Tanzania. Nimefurahi sana kumsikia Mwanamuziki Mkongwe, Mzee Chidumule, akiimba wimbo kuhusu Makao Makuu Dodoma. Huwa nafurahi pia kumsikiliza Mtangazaji wa TBC, Marini Hassan, akiipamba na kuisifu Dodoma. Na kwa kweli, hivi sasa, Dodoma inapendeza. Juzi wakati nikija Dodoma, nilikuja kwa ndege. Nimeshuhudia Dodoma inavyozidi kukua na kupendeza. Kwa sababu hiyo, na kwa mamlaka niliyonayo, leo napenda kutamka rasmi kuipandisha hadhi Manispaa ya Dodoma, kuwa Jiji. Naziagiza Mamlaka husika zikamilishe taratibu za sheria zinazotakiwa. Sambamba na hilo, napenda nimtamke rasmi aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma kuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma. Serikali tutaendelea kuchukua hatua za kuliboresha Jiji hili kulingana na hadhi yake. Dodoma Oyee!
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana, napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kutoa shukrani zangu nyingi kwa Kamati ya Maandalizi kwa kufanikisha Maadhimisho haya. Yamefana sana. Uwanja umefurika na nimeona wananchi wengi walikuwa nje. Hongereni sana wana-Kamati.
Tunavishukuru vyombo vya ulinzi na usalama, vikundi vya burudani, chipukizi na wakufunzi, pamoja na waandishi wa habari kwa kufanikisha sherehe hii. Napenda pia kutoa shukrani nyingi kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma, chini wa kiongozi wenu Mheshimiwa Dkt. Mahenge, kwa kutukaribisha vizuri kwenye Mkoa wenu. Mmedhihirisha kuwa kweli hapa ni Makao Makuu ya Nchi yetu. Hongereni sana.
Mungu Ubariki Muungano wetu!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni Sana kwa kunisikiliza”

- Apr 24, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE BUNGE LA AFRIKA MASHARIKI DODOMA, TAREHE 24 APRILI, 2018
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KWENYE BUNGE LA AFRIKA MASHARIKI
DODOMA, TAREHE 24 APRILI, 2018
Mheshimiwa Martin Ngoga, Spika wa Bunge
la Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Kivenjija, Naibu wa Pili
wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Uganda,
ambaye pia ni Waziri wa Afrika Mashariki
na Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri la
Jumuiya ya Afrika Mashariki;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Waheshimiwa Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki;
Waheshimiwa Wabunge wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Liberat Mfumukeko, Katibu Mkuu
wa Jumuiya ya Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Mheshimiwa Binilith Mahenge,
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Mabalozi pamoja na Wakuu
wa Taasisi za Kimataifa mliopo;
Wadau Mbalimbali wa Maendeleo mliopo;
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi
na Usalama;
Waheshimiwa Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Najisikia furaha na heshima kubwa kusimama mbele yenu leo kuhutubia kwa mara ya kwanza Bunge la Afrika Mashariki, ambalo nalo linafanyika hapa Dodoma kwa mara ya kwanza. Nakushukuru Mheshimiwa Ngoga, Spika wa Bunge la Afrika Mashariki, kwa kunialika; lakini pia nawashukuru Wabunge wote wa Bunge hili la Afrika Mashariki kwa uamuzi wenu wa kufanya kikao hiki hapa Dodoma.
Kwa hakika, mmefanya uamuzi mzuri sana. Baadhi yenu mnafahamu kuwa moja ya sababu zinazotajwa kusababisha kuvunjika kwa Jumuiya yetu ya mwanzo ya Afrika Mashariki mwaka 1977, ilikuwa ushiriki mdogo wa sekta binafsi na wananchi. Wananchi walio wengi hawakuifahamu vizuri Jumuiya yetu. Hivyo basi, utaratibu huu wa kufanya vikao vya Bunge hili sehemu tofauti tofauti ndani ya Jumuiya unatoa fursa kwa wana-Afrika Mashariki wote kuifahamu vyema Jumuiya yao, shughuli inazofanya pamoja na manufaa yake.
Kwa sababu hiyo, napenda kurudia tena kupongeza uamuzi huu wa kufanya kikao hapa Dodoma. Na niseme tu kwamba hamjakosea kuamua kufanya kikao chenu hapa Dodoma. Hapa ni katikati mwa nchi yetu. Ni Makao Makuu ya Serikali pamoja na Chama Tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM). Sambamba na hilo, wananchi wa Dodoma ni wakarimu. Lakini hapa Dodoma kuna sifa nyingine. Hapa ni maarufu sana kwa kuzalisha zabibu tamu zaidi duniani, ambayo hata ukinywa mvinyo wake huwezi kupata “hangover”. Kwa hiyo, unaweza kufanya mkutano mchana, jioni ukapata mvinyo na kesho yake ukaendelea na Mkutano kama kawaida. Haya yote yanafanya Dodoma iwe sehemu nzuri sana ya kufanyia Mikutano. Hivyo basi, ni imani yangu kuwa Waheshimiwa Wabunge wa Afrika Mashariki mmefurahia uwepo wenu hapa Dodoma.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimetangulia kusema kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kuhutubia Bunge hili tangu nichaguliwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi Oktoba 2015. Lakini, nafahamu pia kuwa Bunge hili la Nne la Afrika Mashariki, nalo ni jipya. Limeanza kazi mwezi Desemba 2017. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwapongeza Wabunge wote wa Bunge hili la kwa kuchaguliwa kwenu. Hakuna shaka, mmechaguliwa kwa vile wana-Afrika Mashariki wana imani kubwa juu yenu. Wana uhakika kuwa mtawawakilisha vyema katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo la Jumuiya yetu. Niwaombe sana msiwaangushe.
Naomba pia mniruhusu kutumia fursa hii, kwa namna ya pekee kabisa, kumpongeza Mheshimiwa Ngoga kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge hili. Kwa bahati nzuri, yeye ni Spika wa Tano wa Bunge la Afrika Mashariki. Na mimi ni Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo basi, namuahidi kumpa ushirikiano wa kutosha katika kipindi chote cha uongozi wake wa Bunge hili.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge;
Wakati ninapowapongeza kwa kuchaguliwa, napenda mtambue kuwa jukumu lililo mbele yenu ni kubwa sana. Ninyi ni Wawakilishi na pia ni sauti ya wana-Afrika Mashariki wote. Hili ni jukumu kubwa. Lakini, zaidi ya hapo, kama mnavyofahamu, mmechaguliwa katika kipindi cha kipekee sana. Kipindi ambacho Jumuiya yetu imepiga hatua kubwa za kimaendeleo lakini pia inakabiliwa na changamoto nyingi.
Kama mjuavyo, Ukanda wetu wa Afrika Mashariki hivi sasa unasifika kwa ukuaji uchumi wa kasi duniani. Aidha, tumefanikiwa kwa kiwango kikubwa kuondoa vikwazo vya biashara na uwekezaji. Hii imefanya biashara na uwekezaji miongoni mwa Nchi Wanachama kuongezeka maradufu. Mathalan, kabla ya kuanza kwa Umoja wa Forodha (Customs Union) mwaka 2005 biashara yetu (yaani intra-East African trade) ilikuwa na thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.8. Lakini, tangu tuanzishe Umoja wa Forodha na kuanza kutekeleza Itifaki ya Soko la Pamoja (Common Market), biashara yetu imeongezeka hadi kufikia zaidi ya Dola za Marekani bilioni 5 hivi sasa. Zaidi ya hapo, idadi ya wanachama nayo inaongezeka, na kuna nchi nyingi tu zinatamani kujiunga nasi.
Haya, bila shaka, ni mafanikio makubwa. Hivyo basi, ninyi Waheshimiwa Wabunge wa Bunge la Nne la Afrika Mashariki mnao wajibu mkubwa kwanza wa kuhakikisha mafanikio haya yanalindwa lakini pili yanaendelezwa kwa nguvu zaidi. Na katika hilo, nimefurahi kusikia kuwa kwenye kikao chenu hiki, pamoja na masuala mengine, mmejadili Miswada miwili muhimu; mmoja kuhusu Taasisi ya Fedha ya Jumuiya (East African Monetary Institute) na mwingine kuhusu Takwimu (Statistics Bill). Kama mnavyofahamu, Jumuiya yetu imeweka hatua nne za ushirikiano. Utekelezaji wa hatua mbili za mwanzo, yaani Umoja wa Forodha na Soko la Pamoja, kama nilivyoeleza awali unaendelea. Sasa tunaelekea hatua ya tatu, ambayo ni Ushirikiano wa Masuala ya Kifedha (Monetary Union). Ili kufikia hatua hiyo, miswada hii miwili mliyoijadili ni muhimu sana. Hivyo basi, nawapongeza sana kwa kuijadili miswada hiyo.
Sambamba na hilo, nimeambiwa kuwa kabla ya kuja hapa Dodoma, mmetembelea miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye Jumuiya yetu kwa lengo la kujielimisha na kujionea wenyewe utekelezaji wake. Hapa nchini, mmetembelea Bandari ya Dar es Salaam, Kituo cha Ukaguzi wa Magari pale Vigwaza, Zanzibar; lakini pia mmeshiriki kwenye zoezi la upandaji miti katika Chuo Kikuu cha Dodoma. Hili nalo ni jambo jema. Moja ya majukumu mliyonayo ni kusimamia utekelezaji wa maamuzi na miradi ya maendeleo. Hivyo basi, nawapongeza kwa kuamua kutembelea maeneo hayo ili kujionea utekelezaji wa miradi hiyo ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge
wa Bunge Afrika Mashariki;
Kama nilivyosema awali, mbali na mafanikio yaliyopatikana, Jumuiya yetu pia inakabiliwa na changamoto kadha wa kadha. Tuna matatizo ya migogoro, ambayo imekuwa ikigharimu maisha ya watu wengi. Vikwazo vya biashara na uwekezaji pia bado vipo. Kuna changamoto za kutoaminiana. Changamoto hizi na nyingine ambazo sikuzitaja, ninyi Wabunge, mkiwa sauti na wawakilishi wa wana-Afrika Mashariki wote, mnao wajibu wa kuzitafutia majibu ili kuzimaliza, na hatimaye kuweza kuimarisha utengamano wa Jumuiya yetu na halikadhalika kujenga umoja miongoni mwa viongozi, watendaji na wana-Afrika Mashariki wote kwa ujumla.
Kama mjuavyo, sisi wana-Afrika Mashariki ni kitu kimoja. Hivyo, tunapaswa kupendana. Sisi ni ndugu. Mheshimiwa Spika Ngoga ni raia wa Rwanda lakini nafahamu ameishi na kusoma hapa nchini hadi Chuo Kikuu. Lugha yetu pia ni moja, na nimefurahi Mheshimiwa Spika Ngoga umesisitiza umuhimu wa kutumia lugha ya Kiswahili kwenye shughuli zetu badala ya kuendelea kutumia za Mataifa mengine. Haya yote yonadhihirisha kuwa sisi ni ndugu. Nimefurahi hata hapa mmekaa kama ndugu na watu wanaopendana. Hivi ndivyo haswaa inapaswa iwe. Hatupaswi kutengana, bali kushirikiana katika kuleta maendeleo kwa nchi zetu pamoja na Jumuiya yetu kwa ujumla. Tusipofanya hivya hivyo, tutawaangusha wananchi wetu ambao wanatuamini.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa
Wabunge wa Afrika Mashariki
Ukiachilia mbali changamoto hizo nilizozitaja, zipo changamoto nyingine mbili zenye kuikabili Jumuiya yetu ambazo naomba mniruhusu nizielezee kidogo. Changamoto ya kwanza, ni ukosefu wa viwanda. Nchi zetu zina utajiri mkubwa wa rasilimali. Tuna madini, mifugo, bidhaa za kilimo, uvuvi, misitu, n.k. Kwa bahati mbaya, utajiri huo bado haujatunufaisha vya kutosha. Na moja ya mambo yenye kusababisha hali hii ni kukosekana kwa viwanda kwenye nchi zetu. Matokeo yake tumekuwa tukiuza rasilimali hizo nje ya nchi huku zikiwa ghafi na hivyo kutukosesha mapato ya kutosha. Kama mnavyofahamu, bei ya bidhaa ghafi kwenye soko la dunia mara nyingi huwa zipo chini. Mbali na upotevu huo wa mapato, tatizo jingine, ambalo mimi naliona kuwa kubwa, ni kwamba, kwa kuuza rasilimali ghafi nje ya nchi, maana yake tunapeleka fursa za ajira kwa watu wa mataifa mengine. Kama tungekuwa na viwanda vyetu vya kuchakata, kusindika au kuongeza thamani rasimali hizo, fursa hizo za ajira zingeenda kwa wananchi wetu.
Ni kwa kutambua hilo, Serikali ninayoiongoza imeweka mkazo mkubwa sana kwenye suala la ujenzi wa viwanda. Na nafurahi mwitikio umekuwa mkubwa. Wawekezaji wengi, wakiwemo kutoka Nchi Wanachama wa Afrika Mashariki, hivi sasa wanawekeza kwenye sekta ya viwanda hapa nchini. Nitumie fursa hii, kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wa Afrika Mashariki kulipa mkazo suala hili la ujenzi wa viwanda, hususan kwa kuhakikisha Sera na Sheria zinazotungwa kwenye Jumuiya yetu pamoja na Nchi Wanachama zinawavutia wawekezaji wengi, lakini pia zinalinda viwanda vyetu. Ndio! Ni lazima tulinde viwanda vyetu. Tusipofanya hivyo, vitakufa. Jumuiya yetu ina watu wapatao milioni 170. Hili ni soko kubwa kwa viwanda vyetu.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge;
Changamoto ya pili ambayo ningependa kuielezea inahusu uimarishaji wa miundombinu, hususan ya usafiri na nishati ya umeme. Miundombinu hii ni muhimu sana katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi miongoni mwa Mataifa. Hata suala la kukuza sekta ya viwanda haliwezi kufanikiwa endapo nchi zetu hazitaboresha au kuimarisha miundombinu hii. Lakini, kwa bahati mbaya, tafiti nyingi zilizofanyika miaka ya nyuma kidogo iliyopita zilionesha kuwa Ukanda wetu wa Afrika unakabiliwa na matatizo ya miundombinu ya usafiri na nishati ya umeme. Hii imefanya gharama za usafiri na umeme kuwa juu. Mathalan, tafiti zilionesha kuwa gharama za usafiri kwenye Ukanda wetu ni mara 4 hadi 5 ukilinganisha na nchi za Asia Mashariki, Marekani na Ulaya; na zinachangia kuongeza gharama za bidhaa kwa asilimia 40.
Sekta ya umeme pia ina matatizo. Mathalan, kwa mujibu wa Power Africa, mwaka 2015, nchi zote sita wanachama wa Afrika Mashariki, ukijumlisha Sudan Kusini, zilikuwa na takriban Megawati 6,500. Nadhani sio lazima mtu awe mtaalam wa hesabu au uchumi ili kufahamu kuwa kiwango hiki cha umeme ni kidogo kuweza kuhimili mahitaji ya uchumi wa kisasa. Na mbaya zaidi ni kwamba, hata bei ya umeme nayo ipo juu ukilinganisha na maeneo mengine duniani. Hali hii imechangiwa na mambo mengi; mojawapo nchi zetu kushindwa kutelekeleza miradi ya umeme kwa kutumia vyanzo vilivyopo. Tumekuwa tukiwategemea sana wawekezaji kutoka nje ambapo wengi wanataka kupata faida kubwa.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge;
Pamoja na changamoto za miundombinu nilizozitaja, ni wazi kuwa katika miaka ya hivi karibuni, Nchi Wanachama zimejitahidi sana kuimarisha miundombinu. Kwa mfano, kwenye barabara, hivi sasa mtu anaweza kutoka hapa Dodoma kwenda Kampala, ama Kigali au Nairobi kwa barabara ya lami. Na barabara nyingi bado zinaendelea kujengwa. Sisi Tanzania hivi sasa tunaendelea na ujenzi barabara za kuungaisha mikoa ya Tabora, Rukwa na Kigoma ambazo zitarahisisha usafiri kati yetu na wenzetu wa Burundi na Rwanda. Aidha, tunajenga barabara ya Nyakanazi hadi Kidahwe ambayo itaboresha usafiri kati yetu na wenzetu wa Uganda.
Ukiachilia mbali barabara, hivi sasa ndani ya Jumuiya yetu kuna miradi mingi mikubwa ya miundombinu ya usafiri inatekelezwa; na baadhi inatekelezwa kwa ushirikiano wa Nchi Wanachama. Mathalan, Kenya tayari wamekamilisha ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Bandari ya Mombasa kwenda Nairobi, ambayo inalenga kuboresha usafiri kwenye Ushoroba wa Kaskazini (Northern Corridor). Sisi Tanzania tumeanza kutekeleza mradi wa kupanua Bandari ya Dar es Salaam pamoja na ujenzi Reli ya Kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) ili kuboresha usafiri kwenye Ushoroba wa Kati (Central Corridor) ambao unahudumia nchi za Burundi, Rwanda, Uganda na pia nchi ya DRC. Tunakarabati meli zetu na tumeanza kutengeneza meli mpya kubwa kwa ajili ya kuboresha usafiri kwenye Ziwa Victoria. Kama mnavyofahamu, Ziwa hili ni kiungo muhimu cha usafiri kwenye Jumuiya yetu, hususan kwa nchi zinazozunguka Ziwa hilo (Tanzania, Kenya na Uganda). Inakadiriwa kuwa takriban watu milioni 40 wanaishi karibu na Ziwa hili.
Kwenye miundombinu ya usafiri pia tunashirikiana na wenzetu wa Uganda kutekeleza mradi mkubwa wa Bomba la Kusafirisha Mafuta (East African Oil Pipeline) kutoka Hoima hadi Bandari ya Tanga. Tumenunua ndege mpya 6 na tunapanua viwanja vyetu vya ndege 11 ili kuwezesha ndege kubwa kutua. Tunategemea hatua hizi zitaboresha usafiri wa anga sio tu hapa nchini bali kwenye Ukanda mzima wa Afrika Mashariki.
Kuhusu nishati ya umeme; kama mnavyofahamu, nchi yetu imegundua kiasi kikubwa cha gesi. Takriban futi za ujazo trilioni 57. Tumeanza kutumia gesi hiyo kutekeleza miradi ya kuzalisha umeme. Vilevile, tupo mbioni kuanza ujenzi wa mradi mkubwa wa kufufua umeme kwa kutumia maji wa Stiglier’s Gorge, ambao utazalisha takriban Megawati 2,100. Tunataka kwanza tuwe na umeme mwingi ambao ikibidi tutauza hadi kwa Nchi nyingine Wanachama; lakini pili tunalenga kupunguza uzalishaji wa umeme wa mafuta ili kuifanya bei ya umeme nayo iwe chini. Sambama na hayo, tunashirikiana na Nchi nyingine Wanachama kutekeleza baadhi ya miradi. Tunatekeleza na wenzetu wa Kenya mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 unaoanzia Zambia, kupita hapa Tanzania na kuelekea Kenya. Tunatekeleza na Uganda mradi wa kufufua umeme wa Kikagati – Murongo. Aidha, tupo kwenye majadiliano na Rwanda pamoja na Uganda kutekeleza mradi wa kuzalisha umeme pale Songezi.
Ni imani yangu kuwa miradi hii, pamoja na ile inayotekelezwa kwenye Nchi nyingine Wanachama itakapokamilika; tutakuwa tumefanikiwa kuimarisha huduma ya usafiri na upatikanaji umeme kwenye nchi zetu. Na hilo likitokea, sio tu tutakuza sekta ya viwanda, bali pia tutaimarisha Jumuiya yetu na kukuza uchumi kwenye nchi zetu. Ombi langu kwa wana-Afrika Mashariki tuendelee kujiamini. Mimi naamini, tukijiamini, tutaweza. Hivi punde, nimeeleza kuhusu ujenzi wa reli, ununuzi wa ndege na ujenzi wa meli mpya; haya yote tunayafanya kwa fedha zetu wenyewe. Naamini hata nchi nyingine zinaweza kufaya hivyo. Nitumie fursa hii pia kutoa wito kwa Sekretarieti ya Afrika Mashariki, kupitia kwa Katibu Mkuu wake ambaye nimefurahi yupo hapa, kuendelea kuratibu na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya miundombinu kwenye Jumuiya. Baadhi ya miradi inachukua muda mrefu kutekelezwa, ukiwemo wa Barabara ya Bagamoyo – Horohoro – Malindi.
Sambamba na hayo, nawasihi Waheshimiwa Wabunge wa Afrika Mashariki nanyi kulipa kipaumbele suala hili la ujenzi wa miundombinu. Kama mnavyofahamu, ujenzi wa miundombinu unahitaji fedha nyingi. Kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi kuhusu Miundombinu uliofanyika mapema mwaka huu Jijini Kampala ilielezwa kuwa nchi za Afrika Mashariki zinahitaji angalau Dola za Marekani bilioni 78 ili kuboresha na kuimarisha miundombinu. Hiki ni kiasi kikubwa. Hivyo basi, ninyi Waheshimiwa Wabunge mnao wajibu wa kuwashawishi na kuwahamasisha wawekezaji kutoka ndani na nje ya Jumuiya yetu kuwekeza kwenye eneo hili la miundombinu. Nimefurahi leo hapa tunao Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa. Ninaamini wataendelea kutuunga mkono katika eneo hili.
Mheshimiwa Spika wa Bunge la Afrika Mashariki;
Nimeongea mengi. Lakini, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba uniruhusu niseme mambo machache ya mwisho.
Jambo la kwanza, napenda kutumia fursa hii kueleza kuwa Tanzania ikiwa miongoni mwa waanzilishi wa Jumuiya hii itaendelea kuwa mwanachama mwaminifu. Tutaendelea kushirikiana na Nchi wengine Wanachama katika kutimiza dira na malengo ya Jumuiya hii. Tutaheshimu na kutekeleza maamuzi mbalimbali ambayo kama Nchi Wanachama tutayafikia kwa pamoja. Na katika hili, napenda kuarifu kuwa mwaka jana nchi yetu iliridhia Itifaki ya Jumuiya kuhusu Masuala ya Amani na Usalama (Protocol on Peace and Security). Mapema mwaka huu, nchi yetu imezindua Pasipoti Mpya ya Kielektroniki ya Afrika Mashariki ya Tanzania, kama ilivyoamualiwa na Jumuiya yetu. Hii yote inathibitisha kuwa Tanzania inaheshimu maamuzi ya Jumuiya hii.
Pili, Jumuiya yetu inazidi kukua. Hivi sasa ina Nchi Wanachama sita; na idadi ya watu wapatao milioni 170, kama ilivyoeleza. Hii imeziongezea nguvu nchi zetu. Na kama tukiendelea kushikamana, nina imani, Jumuiya yetu itazidi kuimarika, sauti yake itaongezeka na tutaheshimika kimataifa. Ninyi Wabunge wa Afrika Mashariki ni kiungo muhimu katika kuhakikisha hili linafanikiwa. Mkiwa wawakilishi wa wananchi mnayo nafasi kubwa ya kuwaunganisha wana-Afrika Mashariki wote; lakini pia kuwaelimisha na kuwatahadharisha dhidi ya watu wenye nia mbaya na Jumuiya yetu. Ni wajibu wenu kuwaelimisha wananchi ili umoja na mshikamano wetu uzidi kudumu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho. Baba wa Taifa letu na mmoja wa waasisi wa Jumuiya hii, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliwahi kusema, naomba nimnukuu “Unity will not make us rich, but it can make it difficult for Africa and the African peoples to be disregarded and humiliated”. Mwisho wa kunukuu.
Suala la tatu na mwisho, lakini sio mwisho kwa umuhimu; nadhani nitafanya makosa kama nitahitimisha hotuba yangu bila kueleza japo kwa ufupi hali ilivyo hapa nchini. Kwa ujumla, nchi yetu inaendelea vizuri. Kama mnavyofahamu, tu miongoni mwa nchi tano ambazo uchumi wake unakua kwa kasi Barani Afrika. Mwaka jana uchumi ulikua kwa asilimia Kisiasa, kama mnavyoona nchi yetu ni tulivu na ina amani. Muungano wetu pia unazidi kuimarika. Kesho kutwa unafikisha miaka 54. Kwa kuwa bado mtakuwa hapa Dodoma, nitumie fursa hii kuwaalika Sherehe za Muungano wetu, ambao ni wa pekee Barani Afrika, ambazo kwa bahati nzuri zitafanyika hapa Dodoma.
Mheshimiwa Spika wa Bunge la Afrika Mashariki;
Waheshimiwa Wabunge wa Afrika Mashariki
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa Wote, Mabibi na Mabwana;
Naomba nihitimishe kwa kuwashukuru Wabunge wa Afrika Mashariki kwa kunialika kuhutubia Bunge lenu. Narudia tena, Serikali ninayoingoza itatoa ushirikiano wa kutosha kwa Bunge hili. Namshukuru pia Mheshimiwa Spika Job Ndugai pamoja na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia shughuli hii ifanyike hapa kwenye eneo lenu. Na hii inadhihirisha uhusiano mzuri uliopo kati ya Bunge hili la Afrika Mashariki pamoja na Mabunge ya Nchi Wanachama.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru na pia kuwapongeza Vyombo vya Ulinzi na Usalama pamoja na Wananchi wa Mkoa wa Dodoma wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, kwa kuwapokea vizuri wageni wetu na kwa kuhakikisha amani na utulivu vinaendelea kudumishwa.
Waheshimiwa Viongozi, nilifundishwa na Mbunge wa hapa Dodoma kuwa wanasiasa huwa tuna mwisho na mwisho kabisa. Sasa naomba niseme la mwisho kabisa. Na hapa naomba ninukuu maneno mengine ya Mwalimu Nyerere aliyosema kwenye Sherehe za Miaka 50 Uhuru wa Ghana, nanukuu, “Kizazi changu kiliongoza jitihada za kuleta uhuru wa kisiasa wa Bara letu. Kizazi cha sasa cha Waafrika hakina budi kuchukua kijiti pale tulipoishia, na kwa nguvu mpya, kusukuma mbele maendeleo ya Bara letu”, mwisho wa kunukuu. Kwa kutumia maneno hayo ya Mwalimu Nyerere, napenda nitoe wito kwenu ninyi Waheshimiwa Wabunge na wana-Afrika Mashariki wote kushikamana na kushirikiana, na kwa pamoja tushike kijiti na kuendeleza pale walipoishia waasisi na viongozi wetu waliotangulia.
“Mungu Libariki Bunge la Nne la Afrika Mashariki”
“Mungu Ibariki Jumuiya Yetu ya Afrika Mashariki”
“Ahsanteni Sana kwa Kunisikiliza”

- Apr 23, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA JENGO LA PSPF NA OFISI ZA MAKAO MAKUU YA BENKI YA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWENYE UFUNGUZI WA JENGO LA PSPF NA OFISI
ZA MAKAO MAKUU YA BENKI YA NMB
DODOMA, TAREHE 23 APRILI, 2018
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda, Waziri Mkuu
Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi
Vijana, Ajira na Walemavu;
Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Naibu
Waziri wa Fedha na Mipango;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge,
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Waheshimiwa Wazee wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi
na Usalama mliopo;
Wenyeviti wa Bodi za PSPF na NMB;
Mheshimiwa Makongoro Nyerere,
Mwakilishi wa Mama Maria Nyerere;
Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
Mama Irene Isaka, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka
ya Usimamizi ya Mifuko ya Jamii
Bwana Adam Mayingu,
Mkurugenzi Mkuu wa PSPF;
Mama Ineke Bussemaker,
Mkurugenzi Mkuu wa NMB;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali,
Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Ndugu Wafanyakazi wa NMB na PSPF mliopo;
Wageni Waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa Mawaziri Wahusika kwa kunialika kwenye hafla hii ya uzinduzi wa Jengo la PSPF pamoja na Ofisi za Makao Makuu ya NMB na Tawi lake la Kambarage hapa Dodoma.
Napenda pia niwashukuru wana-Dodoma pamoja na wageni waalikwa wote kwa kujitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hili. Nimefurahi kumwona Spika wa Bunge, Waziri Mkuu Mstaafu Mzee Pinda pamoja na wazee wengine wa Dodoma. Lakini, nimefarijika zaidi kuona kuwa katika hafla hii tunaye Ndugu Makongoro Nyerere, Mwakilishi wa Mama Maria Nyerere. Ahsante sana kwa kujumuika nasi.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema, tupo hapa kwa ajili ya kufanya matukio makubwa mawili. Kwanza, kuzindua Jengo hili la PSPF, lijulikanalo kwa jina la Dodoma Plaza; na pili, kuzindua Makao Makuu ya NMB hapa Dodoma pamoja na Tawi la Kambarage.
Napenda nitoe pongezi nyingi kwa PSPF kwa kujenga jengo hili zuri na la kisasa kabisa hapa Dodoma. Limeboresha na kupendezesha mandhari ya hapa Dodoma, ambako ni Makao Makuu ya Nchi yetu. Nimefurahi kusikia kuwa Jengo hili limesanifiwa na ujenzi wake kusimamiwa na Watanzania; na kwamba takriban Watanzania 250 walipata ajira wakati wa ujenzi. Zaidi ya hapo, nimefurahi sana kusikia takriban asilimia 98 ya Jengo hili tayari limepangishwa. Nafahamu kuwa ipo baadhi ya Mifuko ya Jamii imejenga majengo kama haya lakini yamekosa wapangaji. Ninyi inaonekana mlifanya utafiti wa kutosha kabla ya kujenga jengo hili. Hivyo, hongereni sana PSPF.
Kwa upande wa NMB, nanyi nawapongeza sana. Kama mnavyofahamu, mimi ni mteja wenu; tena wa muda mrefu. Zaidi ya hapo, kama mjuavyo, Serikali inamiliki asilimia 32 ya hisa kwenye Benki hii. Nikiwa kama mteja wenu na Kiongozi wa Serikali ambayo ina hisa asilimia 32, huwa najisikia furaha sana kila nikiona Benki hii inazidi kufanikiwa. Napenda kutumia fursa kuipongeza NMB kwa kuwa Benki namba moja kwa kufikisha huduma zake sehemu kubwa ya nchi yetu, ikiwemo vijijini. Mkurugenzi Mtendaji, Mama Bussemaker ameeleza kuwa, kupitia matawi yake 216, ATMs 800 na Mawakala 6,000; Benki hii imeweza kufikisha huduma sehemu kubwa ya nchi yetu, takriban asilimia 98 ya Wilaya za nchi yetu. Na asilimia 60 ya huduma hizo zipo maeneo ya vijijini. Hongera sana NMB. Ninyi mmejitofautisha na benki nyingine ambazo huwa zinafanya kazi maeneo ya mijini pekee.
Sambamba na hilo, napenda kuwapongeza NMB kwa kufungua Ofisi za Makao Makao na kuanzisha Tawi ambalo mmeliita Kambarage, jina la Baba wa Taifa letu. Huu ni uamuzi wa busara, na niwaambie tu kuwa hamjakosea kulipa Tawi lenu Jina la Kambarage. Kwanza, kwa sababu historia benki yenu kimsingi ilianzia 1967 ambapo Serikali iliyoongozwa na Baba wa Taifa ilianzisha Benki ya Taifa ya Biashara (National Bank of Commerce – NBC) baada ya kutaifisha benki zilizokuwepo. Mwaka 1997, NBC iligawanywa na kuundwa taasisi tatu, yaani NBC Holding Corporation, NBC (1997) na Benki hii ya NMB, ambayo ilibinafishwa mwaka 2005 na kuendelea mpaka sasa. Pili, kama mnavyofahamu, mwaka 1973, wakati Baba wa Taifa akiwa Rais wa nchi yetu, Serikali ilifanya uamuzi wa kuhamia Dodoma. Hivyo, kuliita Tawi lenu la hapa Dodoma jina la Baba wa Taifa ni jambo sahihi kabisa. Na napenda nitumie fursa hii kumshukuru Mama yetu, Mama Maria Nyerere, kwa kuridhia Tawi hili kupewa jina la Baba wa Taifa. Ni matumaini yangu kuwa wafanyakazi wa Tawi hili watamuezi Baba wa Taifa kwa vitendo. Watachapa kazi kwa bidii na uadilifu mkubwa.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Benki pamoja na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inatoa mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi yetu. Kwanza, kupitia huduma za kifedha inazotoa kwa wananchi. Inakadiriwa kuwa Watanzania wapatao milioni 4.7 wana akaunti za benki ambazo huzitumia kuhifadhi fedha zao. Benki pia zinatoa mikopo kwa wananchi na hivyo kusaidia kupunguza umaskini. Kwa upande wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, takwimu zinaonesha kuwa hivi sasa ina wanachama milioni 2.2 nchini. Wanachama hao hunufaika na huduma mbalimbali za kifedha zinazotolewa na Mifuko hiyo, ikiwemo mafao ya uzeeni, pensheni, mikopo, n.k.
Pili, Mifuko ya Hifadhi na Benki inachangia kukuza uchumi wa nchi. Mathalan, hivi punde tumesikia kuwa PSPF imewekeza kwenye Kiwanda cha Sukari Kagera, Kiwanda cha Nguo cha 21st Century kilichopo Morogoro na wanaendelea kushirikiana na mifuko mingine kufufua kiwanda cha maturubai, ambacho nacho kipo Morogoro. Kupitia viwanda hivi, Serikali inapata mapato, ambayo yanatumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kuboresha huduma za jamii. Kwa upande wa Benki, tumesikia kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, NMB imelipa kodi kwa Serikali kiasi cha shilingi bilioni 402. Aidha, mwaka jana (2017), NMB imetoa kwa Serikali gawio la shilingi bilioni 16.525. Wamewawezesha wakulima wadogo wadogo wapatao 800,000 na kutoa misaada mbalimbali ya kijamii, ambapo mwaka jana pekee, walitoa shilingi bilioni 1.4 kwa ajili ya kununua madawati 6,000 na kompyuta 300. Na hivi punde tu hapa wamekabidhi shilingi milioni 50 za msaada. Mambo hayo yote kwa ujumla wake yanachangia kukuza uchumi.
Pamoja na ukweli huo, napenda niseme jambo moja kwa NMB. Kama mlivyosema ninyi wenyewe, mwaka jana mlitoa gawio la shilingi bilioni 16.525. Lakini mimi nimefuatilia na miaka ya nyuma, kuanzia mwaka 2010. Katika kufuatilia huko, nikagundua kuwa kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo, kuanzia 2014/2015 hadi 2016/2017, mmekuwa mkitoa gawio linalofanana, yaani shilingi bilioni 16.525. Hii kwa kweli imenishtua na kunikwaza. Nimejiuliza hivi ni kweli kwa miaka yote hiyo faida ilikuwa ikifanana? Sikupata majibu ya uhakika. Hivyo basi, niuombe Uongozi wa NMB kuliangalia suala hili; na ni matumaini yangu kuwa gawio la mwaka huu wa fedha (2017/2018) litakuwa tofauti. Nitumie fursa hii pia kutoa wito kwa Watendaji wa Serikali wanaotuwakilisha kwenye NMB nanyi kufuatilia kwa karibu.
Mabibi na Mabwana, faida ya tatu ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na Benki ni kutoa fursa za ajira kwa wananchi. Wapo Watanzania wengi ambao wameajiriwa kwenye Benki na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Mathalan, nimeambiwa kuwa, hivi sasa, Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii ina watumishi wapatao 2,000, bila kujumlisha wafanyakazi waliopo kwenye miradi iliyoazishwa na mifuko hii. Kwa upande wa NMB, tumesikia kuwa wenyewe wana watumishi wapatao 3,400 na kama nilivyosema awali, ina mawakala 6,000. Nchi yetu ina benki zaidi ya 50 kwa hiyo mnaweza kukadiria fursa za ajira zilizotolewa.
Hizi ni baadhi tu ya faida za taasisi za kifedha ambazo zinachangia maendeleo ya nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kuzipongeza taasisi zote za fedha nchini kwa michango yao kwenye maendeleo ya nchi yetu. Kwa namna ya pekee, naipongeza sana PSPF pamoja na mifuko mingine ya hifadhi nchini kwa kuitikia vizuri wito wa Serikali wa kujenga viwanda. Nimearifiwa kuwa kwa pamoja, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, ipo kwenye hatua mbalimbali za kutekeleza miradi ya viwanda 16. Aidha, nazipongeza benki ambazo zimekuwa zikitoa mikopo kwa wawekezaji mbalimbali kujenga viwanda nchini.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Licha ya faida hizo pamoja na pongezi hizo nilizozitoa, ni ukweli usiopingika kuwa sekta ya fedha nchini bado inakabiliwa na changamoto nyingi. Lakini nitataja kubwa mbili. Kwanza, ni uchanga wa sekta yenyewe. Ni kweli kuwa hivi sasa tuna benki zaidi ya 50 na tulikuwa na takriban Mifuko ya Hifadhi ya Jamii saba. Lakini hii haiondoi ukweli kuwa sekta ya fedha nchini bado ni changa. Mathalan, nimeeleza hapo awali kuwa hivi sasa ni takriban Watanzania milioni 4.7 tu ndio wana akaunti za benki na wanachama wa Mifuko ni milioni 2.2. Kwa nchi yenye idadi ya watu milioni 55, idadi hii ni ndogo sana. Lakini zaidi ya hapo, kwa taarifa nilizonazo, Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii ina ukwasi wenye thamani ya shilingi trilioni 12.23 na ukwasi wa Benki zetu zote hauzidi shilingi trilioni 30. Hiki ni kiasi kidogo sana cha ukwasi kwa kuzingatia ukubwa wa nchi yetu na mahitaji tuliyonayo. Hivyo basi, taasisi za fedha hazina budi kujiimarisha, hususan kwa kuongeza idadi ya wanachama ili hatimaye kuweza kukuza mitaji iliyonayo.
Changamoto ya pili, ambayo mimi naiona ni ubora wa huduma zinazotolewa na taasisi za fedha nchini. Nimeeleza hapo awali kuwa, ukiondoa Benki hii ya NMB, benki nyingi zimejikita zaidi mijini na kuacha maeneo ya vijijini ambako ndiko kuna Watanzania wengi. Takriban asilimia 70 ya Watanzania wanaishi vijinini. Lakini, zaidi ya hapo, riba kwenye benki zetu zipo juu sana. Kwa upande wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, nako kuna matatizo ya ucheleweshaji wa malipo lakini pia hata viwango vya mafao vinalalamikiwa kuwa vipo chini. Na hii ndio sababu iliyoifanya Serikali kuamua kuiunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iliyopo na kuunda Mifuko miwili, yaani National Social Security Fund (NSSF) na The Public Service Social Security Fund (PSSSF), ambao utahudumia watumishi wa umma.
Tumeamua kuunda mifuko hii miwili ili kuondoa utitiri wa mifuko uliokuwepo na ushindani usio na tija baina ya mifuko hiyo, ambao ulikuwa ukiongeza gharama za uendeshaji na kusababisha wanachama kulipwa mafao madogo. Hivyo basi, tuna imani kuwa, baada ya kuuganisha mifuko hiyo na kuunda miwili, sasa aina na viwango vya mafao vitaongezeka. Na binafsi nadhani, suala hili la kuunganisha mifuko, linafaa pia kuigwa na benki zetu. Nimefurahi kusikia kuwa baadhi ya benki, hususan zenye kusuasua katika utendaji kazi, zimeanza taratibu za kuungana. Hili ni jambo zuri.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimekuja hapa kuzindua Jengo la PSPF na kufungua Ofisi za Makao Makuu NMB hapa Dodoma pamoja na Tawi la Kambarage. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba mniruhusu niseme maneno machache ya mwisho. Kwanza, narudia tena kuwapongeza wafanyakazi wa NMB na PSPF kwa kazi nzuri mnayoifanya. Endeleeni kujituma. Serikali ipo pamoja nanyi. Nitumie fursa hii kuwahimiza Watanzania kujiunga na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii lakini pia kufungua akaunti za benki kwa ajili ya usalama wa fedha zenu.
Suala jingine, ni kwa watani zangu wa Dodoma. Kwanza, nimemsikia kilio chenu kupitia Mbunge wenu kuhusu adha ya kodi na tozo mbalimbali, ambazo zimekuwa zikiathiri biashara ya mchuzi wa zabibu. Kwa bahati nzuri Mawaziri, Watendaji wa Serikali pamoja na Waheshimiwa wako hapa. Bila shaka wamesikia; na nina imani wataenda kulifanyia kazi suala hilo. Nitumie fursa hii pia kuwaarifu wana-Dodoma kuwa sasa mambo mazuri mengi yanakuja kwenye Mkoa wenu. Mwezi Machi mwaka huu nilikutana na Bwana Ricardo Tadeu, Makamu wa Rais wa Kampuni ya AB INBEV, ambayo inamiliki asilimia 57 ya hisa za TBL. Aliniambia kuwa TBL imepaga kujenga kiwanda hapa Dodoma kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 100. Hivyo, nawasihi wana-Dodoma kuchangamkia fursa zinazokuja. Kwa upande wake, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu na kuboresha huduma za jamii. Nitumie fursa hii kuwapongeza viongozi wa Mkoa wa Dodoma kwa jitihada wanazozifanya za kuufanya Mji wa Dodoma kuwa wa kisasa.
Suala la mwisho ni kuhusu ombi la Mwenyekiti wa Bodi ya PSPF kuhusiana na viwanja vilivyopo karibu na eneo hili. Katika hili, napenda niwe tu mkweli. Suala hili siwezi kuliingilia. Namini wenye viwanja hivyo wamevipata kihalali. Hivyo basi, kama mnataka kuwaondoa, ni vyema ninyi wenyewe mzungumze nao. Wakikubali, wawauzie au muwape viwanja maeneo mengine. Lakini hilo ni lenu ninyi wenyewe. Mimi siwezi kuliingilia.
Baada ya kusema hayo sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta hapa la kuzindua Jengo la Dodoma Plaza, lenye thamani ya shilingi bilioni 37.02 mali ya PSPF, pamoja na Ofisi za Makao Makuu ya NMB na Tawi la NMB Kambarage hapa Dodoma.
Munngu Ibariki PSPF!
Mungu Ibariki NMB!
Mungu Ibariki Sekta ya Fedha Nchini!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Apr 11, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA TAASISI YA JAKAYA MRISHO KIKWETE DAR ES SALAAM, TA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KWENYE UZINDUZI WA TAASISI YA JAKAYA
MRISHO KIKWETE
DAR ES SALAAM, TAREHE 11 APRILI, 2018
Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu
wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na Mwenyekiti wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete;
Mheshimiwa Mzee Ali Hassan Mwinyi,
Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Jamhuri
ya Muunganowa Tanzania;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi mliopo;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Wakuu wa Taasisi
za Kimataifa mliopo;
Waheshimiwa Wadhamini wa Taasisi ya
Jakaya Mrisho Kikwete kutoka
Mataifa mbalimbali;
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Wawakilishi wa Asasi za Kiraia mliopo;
Wageni Wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa katika hafla hii. Aidha, kwa namna ya pekee kabisa, napenda nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Mstaafu, Mzee Jakaya Mrisho Kikwete kwa kunialika kushiriki naye katika hafla hii ya kuzindua taasisi yake inayojulikana kwa jina la Jakaya Mrisho Kikwete Foundation. Nakushukuru sana Mzee Kikwete.
Napenda pia kuwakaribisha wageni mbalimbali hapa Ikulu. Ningependa niwaarifu kuwa Ukumbi huu ambapo tupo leo, ulijengwa wakati wa Uongozi wa Rais Mstaafu Mzee Kikwete. Hivyo, alivyonialika kwenye Ukumbi mwingine kuzindua Taasisi yake; nilisema hapana, na kumwambia tutafanya kwenye Ukumbi huu, ambao aliujenga. Nashukuru alikubali, na nawashukuru pia wageni wote kwa kuhudhuria kwa wingi.
Kwa mliotoka nje ya Tanzania, ambao wengi wenu ni wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete, karibuni sana hapa Tanzania. Nchi yetu ni tulivu, ina amani na watu wake ni wakarimu sana. Aidha, nchi yetu ina vivutio vingi vya utalii. Mbuga za Serengeti na Ngorongoro, Visiwa vya Zanzibar, Mlima Kilimanjaro na vigine vingi. Ni imani yangu kuwa kabla hamjaondoka mtapata fursa ya kutembelea baadhi ya vivutio hivyo.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama mnavyojua, tupo hapa kwa ajili ya kuzindua Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete. Napenda kutumia fursa hii, hapa mwanzo kabisa, kumpongeza kwa dhati, Mheshimiwa Rais Mstaafu, Mzee Kikwete, kwa uamuzi wake wa kuanzisha Taasisi hii. Sote hapa tunafahamu, Mzee Kikwete ametoa mchango mkubwa sana kwa nchi yetu; tangu akiwa mtumishi wa Chama, Jeshini na kwenye Wizara mbalimbali alizoziongoza. Lakini alitoa mchango mkubwa zaidi, wakati akiwa Rais wa nchi yetu, kuanzia mwaka 2005 hadi aliponiachia mimi kijiti mwaka 2015. Aliitumikia kwa uadilifu na uaminifu mkubwa nchi yetu. Najua sisi wanadamu hatuna kawaida ya kuwasifu watu wakati wakiwa hai. Lakini leo mimi naomba nimsifu Mzee Kikwete akiwa hai.
Alisimamia vizuri mageuzi ya kiuchumi; ujenzi wa miundombinu; uboreshaji wa huduma mbalimbali za jamii, hususan afya, elimu na maji; ukuzaji wa demokrasia; na pia aliitangaza vyema nchi yetu kimataifa. Watanzania tutaendelea kumkumbuka kwa kusimamia ujenzi wa Shule za Kata, Chuo Kikuu cha Dodoma, Hospitali ya Mloganzila, ujenzi wa miundombinu, ikiwemo barabara na Bomba la Gesi, n.k. Kwa hakika, umetufanyia mambo mengi sana. Tunakushukuru sana; na nina uhakika, mchango wako, utaendelea kukumbukwa vizazi hadi vizazi.
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana;
Pamoja na mchango mkubwa ambao tayari ameutoa kwa nchi yetu, Mzee huyu, baada ya kustaafu; kutokana na mapenzi makubwa aliyonayo kwa nchi yetu na Bara letu la Afrika, na baada ya kuona bado ana nguvu za kutosha na kwa kutambua uzoefu mkubwa alionao. Kama mnavyofahamu, Mzee Kikwete, mbali na kuwa Rais wa nchi yetu, ameshika nyadhifa mbalimbali ndani na nje ya nchi. Amekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC); Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC); Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU); Mjumbe wa Jopo la Watu Mashuhuri la Kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu kukabiliana na Majanga ya Afya, ikiwemo Ebola; Mjumbe wa Jopo la Kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Lishe; Jopo la Kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Afya ya Wanawake, Watoto na Vijana; Balozi wa Heshima wa Chanjo Duniani; aliwahi kuwa Mjumbe wa Kamati ya Usuluhishi wa Mgogoro wa Cote d’Ivoire na hivi sasa ni Mwakilishi wa Umoja wa Afrika kwenye Mgogoro wa Libya.
Kwa kuzingatia hayo yote, Mzee Kikwete, ameona aendelee kuitumia nchi yetu na Bara letu zima la Afrika; kupitia Taasisi hii aliyoianzisha. Nakupongeza sana Mzee Kikwete. Kwa hakika, umefanya jambo jema. Umeiga mifano ya watangulizi wako, Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, Mzee Mwinyi na Mzee Mkapa; ambao nao baada ya kustaafu wameendelea kutoa michango yao kwa njia mbalimbali, ikiwemo kuanzisha taasisi kama hii. Na hii inapaswa kuwa changamoto kwa wastaafu na wazee wengine. Kustaafu sio mwisho wa kutoa mchango kwa Taifa lako. Kustaafu ni hatua tu. Kila mtu, ambaye Mwenyezi Mungu amemjalia umri mrefu, itafika wakati atastaafu. Mimi pia Mwenyezi Mungu akinipa umri, na ukomo wangu wa kuongoza nchi yetu kwa mujibu wa Katiba ukifika, nitastaafu. Na kwa kweli sifikirii na wala sina mpango wa kuongeza muda. Muda ukifika nitaachia kijiti kwa mwingine, na kuungana na watangulizi wangu akina Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa na Mzee Kikwete.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Tumesikia hivi punde kuwa Taasisi hii ya Jakaya Mrisho Kikwete itajishughulisha na masuala makubwa manne. Kwanza, masuala ya afya. Sisi sote hapa tunafahamu umuhimu wa sekta ya afya. Taifa haliwezi kupata maendeleo endapo wananchi wake hawatakuwa na afya njema. Eneo la pili, ambalo Taasisi hii itashughulikia, ni masuala ya maendeleo ya vijana. Kama tujuavyo, vijana ni kundi rika muhimu katika jamii na Taifa kwa ujumla. Uhai wa Taifa lolote lile upo mikononi mwa vijana. Hii ni kwa sababu vijana wapo wengi. Mathalan, hapa nchini ni takriban asilimia 60. Zaidi ya hapo, vijana wana nguvu na uthubutu. Lakini, licha ya ukweli huo, ni wazi kuwa, duniani kote, kundi hili la vijana ndilo lenye kukabiliwa na matatizo mengi, ikiwemo ukosefu wa ajira, elimu na ujuzi, pamoja na changamoto nyingine za kimalezi (mmong’onyoko wa maadili, dawa za kulevya, n.k.). Hivyo basi, mikatati ya makusudi inahitajika kushughulikia changamoto mbalimbali zenye kuwakabili vijana.
Eneo la tatu, ambalo tumeambiwa Taasisi hii itashughulikia ni kilimo. Sote hapa tunafahamu umuhimu wa sekta ya kilimo kwa maendeleo ya nchi. Uchumi wa nchi nyingi za Afrika unategemea sekta hii ya kilimo. Nikitoa mfano wa hapa nchini, sekta hii imeajiri takriban asilimia 70 ya Watanzania. Inatuhakikishia usalama wa chakula. Inachangia takriban asilimia 25 ya Pato la Taifa na asilimia 30 ya mauzo ya nje. Sekta ya kilimo pia inatoa takriban asilimia 60 ya malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu. Hii yote inadhihirisha kuwa sekta ya kilimo ni muhimu. Hivyo, nimefurahi kuona Taasisi hii itashughulika pia na vijana.
Eneo la nne, ni utawala bora na amani. Hili nalo ni eneo muhimu sana. Hivyo basi, nimefurahi kuona kuwa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete imeamua kushughulikia pia eneo hili la Utawala Bora na Amani.
Kwa ujumla, niseme tu kwamba, maeneo yote manne ambayo Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete imechagua kuyashughulikia ni muhimu sana. Na bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, maeneo hayo manne ni ya kipaumbele kwa Serikali nyingi za Afrika hivi sasa, ikiwemo Serikali ninayoingoza. Hivyo basi, nakupongeza sana Mzee Kikwete kwa kuchagua kwa umakini maeneo hayo. Na nimefurahi kuona kuwa kaulimbiu ya Taasisi hii inasema “Transforming Lives Through Collaboration”, yaani “Kuboresha Maisha ya Watu kwa Ushirikiano na Wadau Wote”. Hii ina maana kuwa Taasisi hii imeazimia kufanya kazi kwa kushirikiana na si kushindana na Serikali. Hili ni jambo jema. Na napenda nitumie fursa hii nikuhakikishie Mzee Kikwete kuwa Serikali ninayoingoza inaunga mkono Taasisi yako na tutashirikiana nayo kwa kwa karibu, kwa hali na mali, katika kutekeleza malengo iliyojiwekea.
Mheshimiwa Rais Mstaafu, Mzee Kikwete;
Umeeleza hivi punde kuwa, japokuwa Taasisi yako itashughulikia mambo manne, lakini mmepanga kuanza na suala la afya, na hasa mtaelekeza nguvu katika mapambano dhidi ya vifo vya akina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano. Hili ni jambo jema sana. Kama nilivyosema awali, sekta ya afya ni nyeti na muhimu kwa maendeleo ya Taifa lolote. Lakini, zaidi ya hapo, sote hapa tunafahamu kuwa vifo vya akina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano ni miongoni mwa changamoto kubwa zenye kulikabili Bara letu. Takwimu zinaonesha kuwa Nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara ndizo zinakabiliwa zaidi na changamoto ya vifo vya wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.
Nitumie fursa hii kukupongeza sana Mzee Kikwete. Wakati wa Uongozi wako nchi yetu ilipata mafanikio makubwa katika eneo hili. Tuliweza kupunguza idadi ya vifo vya watoto chini ya umri wa miaka mitano kutoka 112 mwaka 2004/2005 hadi kufikia 67 mwaka 2014/2015, kwa kila watoto 1,000. Aidha, vifo vya wajawazito vilipungua kutoka wastani wa vifo 800 mwaka 2004/2005 hadi kufikia 432 mwaka 2014/2015, kwa kila vizazi hai 100,000. Hongera sana Mzee Kikwete.
Serikali ya Awamu ya Tano ninayoingoza imejipanga kuendeleza mafanikio haya. Na nimefurahi Waziri wa Afya yupo hapa. Suala la kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wa chini ya miaka mitano tumeliweka kuwa miongoni mwa vipaumbele vya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/2017 – 2020/2021). Kupitia Mpango huo, tunalenga kupunguza vifo vya watoto wa chini ya miaka mitano kutoka 67 hadi 45 kwa kila watoto 1,000, na vifo vya wajawazito kutoka 432 hadi kufikia 250, kwa kila vizazi hai 100,000. Na tayari tumeanza kuchukua hatua. Mathalan, ili kukabiliana na tatizo la vifo vya akina mama wajawazito, hivi sasa tunavipanua na kuviboresha takriban vituo vya afya 208 nchi nzima ili kuviwezesha kutoa huduma dharura za upasuaji. Hatua hii bila shaka itasaidia kupunguza vifo vya wajawazito wakati wa kujifungua.
Kuhusu vifo vya watoto chini ya umri wa miaka 5, hivi sasa watoto wote wanapata huduma za chanjo bure; na dawa za chanjo zipo za kutosha. Ni matumaini yetu kuwa, kutokana na hatua hizi na nyingine nyingi tunazozichukua, na kwa kushirikiana na wadau wengine, ikiwemo Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete, tutaweza kukabiliana na changamoto ya vifo vya wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano. Dying while giving life is unacceptable. Vilevile, vifo vya watoto wetu wadogo havikubaliki. Ni lazima tushirikiane kuzuia vifo hivyo.
Mheshimiwa Rais Mstaafu, Mzee Kikwete;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Hapa sio mahali pa hotuba. Tupo hapa kwa ajili ya kushuhudia uzinduzi wa Taasisi ya Rais wetu mstaafu ya Jakaya Mrisho Kikwete. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu naomba niseme masuala machache ya mwisho.
Jambo la kwanza, napenda kurudia tena kukupongeza Mheshimiwa Rais Mstaafu Mzee Kikwete kwa kuanzisha Taasisi hii na napenda nikuahidi tena kuwa Serikali ninayoingoza itashirikiana na karibu sana na Taasisi yako. Nawaomba pia wadau mbalimbali waiunge mkono Taasisi hii. Nawashukuru na kuwapongeza wadhamini waliojitolea kumsaidia Rais wetu Mstaafu katika kuendesha Taasisi hii. Niwaombe pia Mabalozi, hususan wa nchi za Afrika, mlioshiriki katika uzinduzi huu, kuitangaza Taasisi kwenye nchi zenu. Kama mlivyosikia, Taasisi hii sio kwamba itaendesha shughuli hapa Tanzania pekee bali kwenye Bara zima la Afrika. Hivyo, nawasihi muitangaze na kuiunga mkono.
Jambo la pili, napenda kuahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itashirikiana na taasisi zote za kiraia zinazofanyakazi hapa nchini zenye lengo la kuwaletea maendeleo Watanzania. Hata hivyo, niwe mkweli, Serikali ninayoingoza, kamwe; haitashirikiana au kuifumbia macho taasisi yoyote ya kiraia yenye malengo ya kuvuruga amani ya nchi yetu au kuharibu maadili ya Watanzania. Taasisi kama ambayo Mheshimiwa Rais Mstaafu amezitolea mfano hivi punde, ambazo zinafadhiliwa ili kuvuruga amani na utulivu ndani ya nchi, kamwe hatutaziuga mkono.
Jambo la tatu na la mwisho, lakini sio mwisho kwa umuhimu, napenda kutoa shukrani zangu kwa Mheshimiwa Kikwete. Nafahamu nimemshukuru mara kadhaa. Lakini, nitaendelea kufanya hivyo kila wakati nikipata nafasi. Bila ya Mzee huyu, huenda leo mimi nisingekuwa Rais. Hivyo, namshukuru sana. Lakini pia, nawashukuru viongozi wengine wastaafu, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Karume, Makamu wa Rais Mzee Bilal, Mawaziri Wakuu Wastaafu, Makamu Wenyeviti wastaafu wa CCM kwa kunilea na kuniongoza. Sina cha kuwalipa zaidi ya kusema ahsanteni. Naahidi nitaendelea kuwaenzi. Niwaombe Watanzania wote tuendelee kuwaenzi wazee na wastaafu wetu. Na niseme tu kuwa, binafsi, kila ninapokutana na Marais wastaafu, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Mzee Karume pamoja na viongozi wengine wastaafu, huwa najisikia faraja sana. Wanaifundisha na kuniongoza. Na hii ndio sifa yetu kubwa sisi Watanzania. Sio kwenye nchi nyingi, utakuta viongozi wastaafu; au viongozi wastaafu na waliopo madarakani; wanakutana na kukaa pamoja. Sehemu nyingine jambo hili haliwezekani kabisa. Na mifano ipo mingi.
Baada ya kusema hayo, sasa ninayo furaha kutamka kuwa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete imezunduliwa Rasmi. Naitakia mafanikio mema na makubwa Taasisi hii.
Mungu Mbariki Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete!
Mungu Wabariki Marais na Viongozi wengine Wastaafu!
Mungu Ibariki Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete!
Mungu Zibariki Taasisi zote za Kiraia zenye nia njema na Nchi yetu!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Apr 07, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA NYUMBA ZA ASKARI POLISI ARUSHA, TAREHE 7 APRILI, 2018
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA NYUMBA ZA ASKARI POLISI ARUSHA, TAREHE 7 APRILI, 2018
Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba,
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi;
Mheshimiwa Mhandisi Hamad Masauni;
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi;
Mheshimiwa Mrisho Gambo,
Mkuu wa Mkoa wa Arusha;
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani;
Mheshimiwa Simon Sirro, Inspekta Jenerali
wa Polisi pamoja na Wakuu wa Vyombo
vya Ulinzi na Usalama mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali mliopo;
Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Maafisa na Askari wa Jeshi la Polisi;
Waheshimiwa Wageni Wote Waalikwa;
Ndugu wana- Habari;
Wananchi wa Arusha, Mabibi na Mabwana:
Nitumie fursa hii, kwanza kabisa, kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa uhai na kutuwezesha kukutana siku ya leo. Kama mnavyofahamu, tarehe kama ya leo, miaka 46 iliyopita, nchi yetu ilimpoteza mmoja wa viongozi mahiri na shupavu, Hayati Mzee Abeid Aman Karume, ambaye aliuawa kwa kupigwa risasi tarehe 7 Aprili, 1972 wakati akiwa anacheza bao na marafiki zake kwenye Makao Makuu ya Ofisi ya CCM Kisiwandui, zilizopo Unguja, Zanzibar.
Kwa heshima yake, naomba sote tusimame kwa dakika moja ili tuweze kumkumbuka Kiongozi wetu huyu, ambaye alikuwa mwanamapinduzi na mtetezi mkubwa wa wanyonge. Tuzidi kumwombea kwa Mwenyezi Mungu aipumzishe roho yake mahali pema peponi. Amina.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Wakati anauwawa, Hayati Mzee Karume alikuwa Rais wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla, tunamkumbuka Hayati Mzee Karume kwa mambo mengi. Yeye ndiye aliongoza Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964 ambayo ndiyo yalihitimisha utawala wa Sultan na vibaraka wake. Aidha, Mzee Karume pamoja na Hayati Baba wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ndio walioasisi Muungano wa nchi yetu; Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wao ndio waliosaini Hati za Muungano baada ya kufikia makubaliano ya kuziunganisha nchi zao mbili, yaani Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Hii maana yake ni kwamba, bila ya jitihada za Hayati Mzee Karume, huenda Zanzibar bado ingekuwa ipo chini ya utawala wa Sultan, kupitia vibaraka wake; na huenda pia Taifa jipya la Tanzania, ambalo baadaye mwezi huu linafikisha miaka 54, lisingezaliwa.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Ukiachilia mbali mchango huo mkubwa alioutoa, Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla tutaendelea kumkumbuka Hayati Mzee Karume kwa uamuzi wake wa kugawa ardhi bure kwa wananchi pamoja na kujenga nyumba kwa ajili ya watu wasiojiweza. Leo hii ukienda Zanzibar, utaziona nyumba zilizojengwa na Hayati Mzee Karume wakati wa uongozi wake.
Kwa kutambua mchango mkubwa alioutoa Mzee Karume kwa nchi yetu, Serikali iliamua tarehe 7 Aprili ya kila mwaka iwe siku ya mapumziko (Karume Day). Lengo ni kuwapa Watanzania fursa ya kumkumbuka lakini pia kutafakari namna ya kuenzi maisha yake. Hivyo basi, leo tunapoadhimisha miaka 46 ya Kifo cha Mzee Karume, nawasihi Watanzania tuenzi maisha yake, hususan kwa kulinda uhuru wetu, kudumisha amani na umoja wetu, pamoja na kuchapa kazi kwa bidii. Haya ndiyo mambo ambayo Mzee Karume aliyapigania sana enzi za uhai wake.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyoeleza hivi punde kuwa, moja ya mambo ambayo sisi Watanzania tutaendelea kumkumbuka Mzee Karume, ni uamuzi wake wa kuwajengea wananchi nyumba. Nami leo nimefurahi kuja hapa Arusha, ambapo pamoja na kuiadhimisha Siku hii ya Karume Day, muda mfupi uliopita, nimepata fursa ya kuzindua nyumba 31 za Jeshi la Polisi. Inspekta Jenerali wa Polisi Simon Sirro ameeleza hivi punde kuwa tarehe 27 Septemba, 2017 jumla ya nyumba 13 za askari polisi ziliteketea kwa moto; na kuziacha takriban familia 14 bila makazi ya kuishi.
Kufuatia tukio hilo la kusikitisha, Serikali pamoja na kuzitafutia makazi ya muda familia hizo, ilitoa shilingi milioni 250 kwa ajili ya kujenga nyumba mpya 13. Na kama mlivyosikia, Wafanyabiashara wa Mkoa wa Arusha nao walichangishana na kufanikiwa kupata fedha za kujenga nyumba 18. Hivyo, leo nimezindua jumla ya nyumba 31. Hii ina maana kuwa janga lile la moto, pamoja na kwamba lilituhuzunisha sana, limeleta neema. Kwa “Kisukuma” hii unaweza kusema “It was a blessing in disguise”. Ziliungua nyumba 13, lakini sasa zimejengwa nyumba 31.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Nitumie fursa hii kuwashukuru wananchi wa Arusha, kwanza kwa misaada mbalimbali mliyotoa wakati lilipotokea janga la moto. Nimeambiwa kuwa, wana-Arusha mlitoa chakula, maji, dawa, n.k., kwa waathirika. Nawashukuru na kuwapongeza sana.
Pili, na kwa namna ya pekee kabisa, napenda nitoe shukrani zangu nyingi kwa wananchi waliochangisha fedha zilizowezesha kujengwa kwa nyumba hizo 18. Ahsanteni sana wananchi wa Arusha. Na napenda kusema kuwa, kupitia kwenu wana-Arusha, mimi binafsi nimejifunza jambo, na hasa baada ya kufahamu kuwa nyumba hizi 31 zimejengwa kwa takriban shilingi milioni 700. Nimebaini kuwa kama nikitoa shilingi bilioni 10, na fedha hizo zikasimamiwa na kutumika vizuri, tunaweza kujenga nyumba nyingi kwenye mikoa mbalimbali nchini na hivyo kupunguza tatizo la makazi kwa askari wetu.
Na kwa kweli baada ya kufahamu hilo, na pia baada ya kusikia maelezo mazuri kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi na kushuhudia maonesho ya kijasiri kutoka kwa askari wetu wa Jeshi la Polisi, napenda kutumia fursa hii kuahidi kuwa Serikali itatoa shilingi bilioni 10 kwa Jeshi la Polisi ili ziweze kuzitumia kujenga nyumba za askari wa ngazi za chini katika mikoa mbalimbali nchini. Niwaombe Wakuu wa Mikoa mingine pamoja na wananchi kwa ujumla, wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, nanyi kuangalia uwezekano wa kusaidia jitihada za Serikali za kupunguza tatizo la makazi kwa askari wetu. Mimi wakati nikiwa Mbunge nakumbuka niliwahi kutoa shilingi milioni 25 kutoka Mfuko wa Jimbo kuchangia ujenzi wa nyumba za askari kwenye Jimbo langu.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Jeshi letu la Polisi linapaswa kuungwa mkono kutokana na kazi nzuri na kubwa linayoifanya. Nchi yetu ipo salama na ina amani kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama. Kama isingekuwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, huenda amani tunayojivunia hivi sasa isingekuwepo. Na hii ndio maana huwa nawashangaa sana baadhi ya watu, wakiwemo wanasiasa wenzangu, ambao kila siku hawachoki kubeza na kulikebehi Jeshi letu la Polisi. Huwa nawashangaa sana.
Ninyi wananchi ni mashahidi; miezi michache tu iliyopita, katika Mkoa wa Pwani, sehemu za Ikwiriri, Kibiti na Rufiji, watu walikuwa wakiuawa kila kukicha. Jumla ya watu 59, (raia 42 na askari 17) waliuawa. Na jambo la kushangaza na kusikitisha ni kwamba, wengi waliouawa walikuwa viongozi wa Serikali na Chama cha Mapinduzi. Lakini kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na askari wetu wa Jeshi letu la Polisi pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, hivi sasa vitendo hivyo vimekomeshwa. Hali ni shwari; na wananchi wanaendelea na shughuli zao kama kawaida.
Nitumie fursa hii kulipongeza sana Jeshi la Polisi kwa kufanikiwa kukomesha vitendo hivyo vya uhalifu. Napenda niwahakikishie kuwa Watanzania wengi wanathamani na kutambua kazi yenu. Kebehi zinazotolewa dhidi yenu na watu wachache zisiwayumbishe au kuwakatisha tamaa. Serikali ipo pamoja nanyi. Tutaendelea kuliboresha Jeshi lenu pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, hususan kwa kuwapatia vifaa na zana za kisasa. Zaidi ya hapo, tutaendelea kuboresha mazingira yenu ya kazi pamoja na maslahi yenu. Inspekta Jenerali wa Polisi ameeleza baadhi ya mambo ambayo Serikali inafanya katika kuliboresha Jeshi la Polisi.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Nitumie fursa hii kujibu pia baadhi ya maombi ambayo hivi Inspekta Jenerali wa Polisi amewasilisha kupitia Risala yake. Niseme tu kwamba maombi yenu yote nimeyapokea na Serikali itayafanyia kazi. Lakini kuhusu ombi lenu la kupewa kibali cha kuajiri askari wapya, niziagiza mamlaka husika kutoa kibali kwa Jeshi la Polisi kuajiri askari wapya 1,500. Hata hivyo, nitoe wito kwa Jeshi la Polisi, kuhakikisha watakaoajiri wawe ni wale tu waliohitimu vizuri mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT). Na kuhusu ombi la kupandishwa vyeo Maafisa wa Polisi, nawagiza mkakamilishe uchambuzi wenu wa ndani na kisha mniletee mapendekezo ya askari wanaostahili kupandishwa vyeo. Lakini hapa pia nitoe angalizo, msimpendelee au kumwonea mtu yeyote. Majina mtakayoleta yawe ni wale tu ya wanaostahili kupandishwa.
Sambamba na hayo, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza Viongozi wa Jeshi la Polisi kurekebisha kasoro ndogo ndogo chache zilizopo ndani ya Jeshi lenu, ambazo zimekuwa zikichafua sifa yenu nzuri. Wapo askari wachache; wachache sana, ambao wanalichafua Jeshi lenu. Wanapenda kuchukua rushwa, wanawanyanyasa wananchi, ikiwemo kuwabambikizia wananchi kesi. Rekebisheni mapungufu haya, kwanza, kwa kuongeza umakini katika kuajiri; pili, imarisheni mafunzo mnayotoa kwa askari; na tatu, kwa wale wachache watakaothibitika kufanya vitendo vyenye kulichafua Jeshi lenu, msisite kuwachukulia hatua kali za kinidhamu. Nimefurahi Inspekta Jenerali umeeleza baadhi ya hatua za kinadhamu mnazozichukua kwa baadhi ya askari wanaokiuka miiko na maadili ya Polisi. Endeleni kuchukua hatua hizo.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wananchi;
Mabibi na Mabwana;
Leo ni Siku ya Kumbukumbu ya Hayati Mzee Karume. Nimeitumia siku hii pia kufanya uzinduzi wa nyumba 31 za Jeshi la Polisi hapa Arusha. Hata hivyo, haitakuwa vyema kuhitimisha hotuba yangu bila kuwaeleza wana-Arusha mipango na mikakati mbalimbali ambayo Serikali yenu inaitekeleza kwa lengo la kuleta maendeleo kwa nchi yetu.
Tangu tuingie madarakani, takriban miaka miwili na nusu iliyopita, Serikali ya Awamu ya Tano, kwa nia ya kuendeleza jitihada zilizofanywa na Awamu zilizotangulia, imechukua hatua mbalimbali zenye lengo la kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Tumeimarisha nidhamu kwenye utumishi wa umma; tumeongeza mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi pamoja na biashara haramu ya dawa za kulevya. Aidha, tumeimarisha usimamizi na ulinzi wa rasilimali zetu, ikiwemo madini na maliasili mbalimbali. Bila shaka, jana mmeshuhudia nimezindua Ukuta pale Mererani ili kudhibiti wizi na utoroshaji wa madini yetu ya Tanzanite.
Sambamba na hayo, tumeongeza ukusanyaji mapato. Kwa mujibu wa Takwimu zilizotolewa mara ya mwisho na Mamlaka ya Mapato (TRA), mwezi Desemba 2017, tulikusanya shilingi trilioni 1.6. Haijawahi kutokea nchi yetu kukusanya mapato makubwa ya kodi kiasi hicho. Na napenda kutumia fursa hii kuwapongeza wana-Arusha na Watanzania kwa ujumla kwa kuitikia vizuri wito wa Serikali wa kulipa kodi. Nchi yetu ni lazima tuijenge sisi wenyewe. Hatuna mjomba wala shangazi wa kuja kutujengea.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kutokana na kuongeza ukusanyaji mapato, tumeweza kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kuboresha huduma za jamii. Tayari mmesikia kuhusu hatua tunazochukua kwenye afya na elimu. Lakini tunajenga pia barabara. Hapa Arusha, tayari tumekamilisha ujenzi wa barabara ya njia nne yenye urefu wa kilometa 14.1 kutoka Sakina hadi Tengeru, kwa gharama ya shilingi bilioni 72.09; na ujenzi wa Barabara ya Mchepuko wa Kusini “Southern Bypass” unaendelea. Vilevile, kwenye Barabara ya Mto wa Mbu – Ngarasero hadi Loliondo, tumeanza ujenzi wa kipande cha Waso – Sale chenye urefu wa kilometa 49 kwa gharama ya shilingi bilioni 87. Halikadhalika, TARURA imetengewa takriban shilingi bilioni 6.28 kufanya ukarabati wa barabara mbalimbali za mijini na vijijini katika Mkoa huu wa Arusha, ambazo hazipo chini ya TANROADS.
Tunakarabati njia ya reli kutoka Tanga kuja hapa Arusha ili kurahisisha usafiri na usafirishaji. Tunapanua bandari zetu kuu za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga kwa gharama ya takriban shilingi trilioni 1.2. Tunataka wananchi wa Arusha wapokee mizigo yao katika Bandari ya Tanga na waisafirishe kwa reli hadi hapa. Tunavipanua pia viwanja vyetu vikubwa vya ndege vya Dar es Salaam na KIA kwa gharama ya shilingi bilioni 650. Tunatumia fedha nyingine takriban shilingi bilioni 500 katika kujenga au kufanya marekebisho ya viwanja vya ndege 11 kwenye Mikoa mbalimbali ili kutekeleza Sera yetu ya Usafirishaji, ambayo inaelekeza kila Mkoa kuwa na Kiwanja cha Ndege. Tumenunua pia ndege mpya sita. Tunachukua hatua hizi ili kukuza sekta ya utalii nchini. Ninyi wana-Arusha mnafahamu vizuri, asilimia 70 ya Watalii duniani hutumia usafiri wa anga. Hivyo basi, bila kuimarisha usafiri wa anga ni vigumu kukuza sekta ya utalii.
Sambamba na hayo, tunatekeleza pia miradi ya maji karibu kwenye kila mkoa nchini. Mathalan, hapa Arusha, tunatekeleza mradi mkubwa wa kuchimba visima virefu 56 kwa gharama ya shilingi bilioni 476, ambazo tumekopeshwa kwa masharti nafuu na Benki ya Maendeleo ya Afrika. Mkuu wa Mkoa amenieleza suala la kodi ya ongezeko la thamani ambalo linachelewesha utekelezaji wa mradi huo. Tatizo hilo tutalishughulikia ili mradi huo uweze kukamilika.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu wana-Arusha, Mabibi na Mabwana;
Mbali na kutekeleza miradi ya maendeleo na kuboresha huduma za jamii, tunaendelea kushughulikia kero nyingine zenye kuwakabili wananchi wetu, hususan wananchi wa kipato cha chini. Tumepunguza utitiri wa kodi kwenye kilimo, mifugo na uvuvi. Tumeanza usajili wa wajasiliamali wadogo (mama lishe, machinga, n.k) kwa kuwapatia vitambulisho maalum vitakavyowawezesha kuendesha shughuli zao kwa uhuru bila kubughudhiwa.
Haya ni baadhi tu ya mambo ambayo tumetekeleza katika kipindi cha miaka miwili na nusu iliyopita. Yapo mengine mengi, ambayo kwa sababu ya muda siwezi kutaja. Hivyo basi, nitumie fursa kuwasihi wana-Arusha na Watanzania kuendelea kuiunga mkono Serikali, hususan kwa kudumisha amani na umoja wetu na bila kusahau kuchapa kazi kwa bidii. Amani ndio msingi wa maendeleo. Nawapogeza wana-Arusha hivi sasa mpo mstari wa mbele katika kudumisha amani. Hii imefanya hata shughuli za kiuchumi, ikiwemo utalii na ujenzi wa viwanda, ziendelee kustawi na kushamiri. Nimeambiwa mpaka sasa mmejenga viwanda vipya 46. Hongereni sana wana-Arusha.
Nawasihi muendelee kudumisha amani, lakini pia toeni ushirikiano kwa viongozi wenu wote. Maendeleo hayana chama. Hii ndio sababu ilinifanya kabla ya kuanza kuhutubia niwape fursa Waheshimiwa Wabunge wote wa Arusha kueleza shida na kero zilizopo kwenye majimbo yao. Na napenda nitumie fursa hii kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge wote kuwa kero zenu nimezichukua na tutazishughulikia. Lakini niwe mkweli, suala la kuwapa ng’ombe Wafugaji wa Kimasai ambalo Mbunge wa Longido amenieleza, hilo Serikali haitafanya kwa vile hilo sio jukumu la Serikali. Jukumu la Serikali ni kuwawekea wananchi mazingira mazuri ya kuendesha shughuli zao za maendeleo, ikiwemo kutekeleza miradi ya maji, kujenga barabara, n.k., lakini sio kutoa ng’ombe bure. Hilo, kwa kweli, hatutafanya.
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana;
Nimezungumza mengi. Naomba nihitimishe kwa kurudia tena kuwaomba Watanzania kuitumia Siku hii ya Kumbukumbu ya Hayati Mzee Karume kutafakari mchango wake na kuuenzi. Aidha, napenda kuwashukuru tena viongozi wa Jeshi la Polisi kwa kunialika kuzindua nyumba 31 za askari polisi hapa Arusha. Nawapongezeni pia kwa kazi nzuri na kubwa mnazozifanya. Nawapongeza pia wale wote walioshiriki kwenye maonesho na burudani mbalimbali. Kila mtu aliyeko hapa, amefurahi. Hongereni na tunawashukuru sana.
Wito wangu kwenu endeleeni kuchapa kazi kwa bidii. Msimuogope au kumwonea mtu yeyote. Vilevile, jitahidini kurekebisha kasoro ndogo ndogo zilizomo kwenye Jeshi letu. Na katika hili, napenda niseme kuwa lipo jambo jingine moja ambalo huwa naona kila mara likifanywa na viongozi wa Jeshi la Polisi japokuwa huwa halinifurahishi sana. Jambo lenyewe ni kuwaona askari polisi wakishiriki shughuli za uchomaji wa mashamba ya bangi. Mimi nadhani hiyo sio kazi ya Jeshi la Polisi. Kazi yenu ni kuwakamata wahalifu. Hivyo basi, badala ya ninyi kuchoma bangi, hakikisheni mnawakamata wahusika ili wao wenyewe ndio wafanye kazi ya kuchoma mashamba hayo. Mkifanya ninyi mnalidhalilisha Jeshi lenu.
Mwisho lakini sio mwisho kwa umuhimu, napenda nitumie fursa hii kuwashukuru wana-Arusha, mkiongozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, Mrisho Gambo, kwa mapokezi yenu makubwa. Tangu nimechaguliwa kuwa Rais nimekuja Arusha mara nyingi. Lakini, mara zote nimepata mapokezi mazuri. Ahsanteni sana wana-Arusha.
Baada ya kusema hayo: Mungu Libariki Jeshi la Polisi!
Mungu Wabariki Wana-Arusha!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Apr 03, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA MRADI WA KUFUFUA UMEME WA KINYEREZI II, DAR ES SALAAM...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UZINDUZI WA MRADI WA KUFUFUA UMEME WA KINYEREZI II, DAR ES SALAAM, TAREHE 3 APRILI, 2018
Mheshimiwa Medard Kalemani, Waziri wa Nishati;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati;
Bwana Hiroyuki Kubota, Mwakilishi wa Balozi
wa Japan nchini;
Waheshimiwa Wabunge mliopo mkiongozwa na
Mbunge wa hapa Mheshimiwa Bonna Kaluwa;
Dkt. Alexander Kyaruzi, Mwenyekiti wa Bodi
ya Wakurugenzi ya TANESCO;
Dkt. Tito Mwanuka, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO;
Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA);
Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Sumitomo Mitsui
Corporation ya Japan;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Waheshimiwa Wageni wengine Waalikwa;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri na Viongozi wa Wizara ya Nishati kwa kunialika kuja kuzindua Mradi huu wa Kufufua Umeme Megawati 240 kwa kutumia gesi asilia hapa Kinyerezi. Ahsanteni sana. Nawashukuru pia wananchi wa Kinyerezi kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kushuhudia tukio hili, licha ya mvua nyingi kuendelea kunyesha. Ahsanteni sana wana-Kinyerezi.
Naomba pia mniruhusu nitumie fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, niipongeze Wizara ya Nishati pamoja pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kazi nzuri mnayoifanya. Waswahili husema “mnyonge mnyogeni lakini haki yake mpeni”. Siku hizi, TANESCO, mnajitahidi sana kufanya kazi. Hongereni sana. Endeleeni hivyo hivyo. Serikali ipo pamoja nanyi. Nampongeza Mkandarasi, Kampuni ya Sumitomo Corporation ya Japan, kwa kuutekeleza mradi huu kwa haraka. Kama tulivyosikia, Mradi huu, ambao unatekelezwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya combined cycle (yaani gesi na mvuke unaozalishwa na mtambo wa kufufua umeme), awali ulipangwa kukamilika mwezi Septemba 2018, lakini leo mwezi Aprili 2018, tayari. Hongera sana kwa Kampuni ya Sumitomo. Mmetekeleza kwa vitendo dhana yetu ya “Hapa Kazi Tu”. Nawapongeza na kuwashukuru pia kwa kutoa ajira nyingi kwa Kitanzania. Nimeambiwa kuwa kati ya wafanyakazi takriban 2,000 wa Kampuni hii ambao wameshiriki kwenye utekelezaji wa Mradi huu, asilimia 95 ni Watanzania. Hii maana yake ni kwamba fedha nyingi za kutekeleza Mradi huu zimebaki hapa nchini. Tunawashukuru sana.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Umeme ni injini na mhimili muhimu katika ukuzaji uchumi na kuboresha maisha ya binadamu. Umeme unachochea shughuli za uzalishaji na hivyo kutoa fursa za ajira na kuboresha maisha ya watu. Azma na dhamira yetu ya kujenga uchumi wa viwanda haiwezi kutimia bila ya kuwa na umeme wa kutosha na wa uhakika. Ni kwa sababu hiyo, inatia moyo sana kuona kuwa, pamoja na matatizo tuliyonayo ambayo nitayaeleza muda mchache ujao, hali ya umeme nchini sio mbaya sana. Mmesikia hivi punde kuwa mahitaji ya umeme nchini hivi sasa ni Megawati 1,051, lakini tunaozalisha ni Megawati 1,513.3. Haya ni mafanikio makubwa ambayo hatuna budi kujipongeza.
Hata hivyo, pamoja na takwimu hizo za kutia matumaini, ni wazi kuwa jitihada za makusudi zinahitajika ili tuweze kuwa na umeme unaokidhi mahitaji ya uchumi wa kisasa. Mathalan, sisi leo tunajivunia kuwa na Megawati 1,513.3; lakini yapo Mataifa mengine, wakiwemo marafiki zetu wa karibu, ambao wana umeme mwingi zaidi. Kwa mfano, wenzetu wa Ethiopia wana takriban Megawati 4,300 na hivi sana wanakamilisha ujenzi wa Bwawa la kuzalisha Megawati nyingine 6,000. Hii peke yake inaonesha kuwa jitihada za makusudi zinahitajika ili kuongeza uzalishaji wa umeme nchini.
Lakini ukiachilia mbali mfano huo, utafiti uliofanywa na Ofisi yetu ya Takwimu mwaka 2015, ulionesha kuwa asilimia 36.6 tu ya Watanzania ndio walikuwa wameunganishwa na umeme, bila shaka, hivi sasa itakuwa imeongezeka. Zaidi ya hapo, Watanzania wengi, takriban asilimia 60 wanatumia mkaa, kuni au mafuta ya taa kupata nishati. Hali hii imechangawia na bei ya umeme nchini kuwa juu na hasa kwa kuwa umeme wetu mwingi vado unazalishwa kwa kutumia mafuta (dizeli); na kama mnavyofahamu baadhi ya mikataba ya kuzalisha umeme tuliyoingia ni mibovu. Athari za kutumia kuni na mkaa zinafahamika. Kwanza, inachangia kuharibu mazingira, ambapo katika nchi yetu inakadiriwa kuwa kila mwaka tunapoteza hekta 400,000 za misitu. Pili, matumizi ya kuni na mkaa yana athari nyingi za kiafya.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana:
Ni kutokana na sababu hizo, uzalishaji wa umeme imekuwa kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Tano. Na hii ndio sababu leo nimefurahi kuja hapa kuzindua mradi huu wa Kinyerezi II ambao utaongeza kwenye Gridi yetu ya Taifa Megawati 240. Nitumie fursa hii kuishukuru Serikali ya Japan kwa kushirikiana nasi katika kutekeleza mradi huu. Kama mlivyosikia, gharama za mradi huu ni Dola za Marekani milioni 344, sawa na shilingi bilioni 758. Serikali yetu imetoa Dola za Marekani milioni 51.6 sawa na takriban shilingi bilioni 120, na wenzetu wa Japan wametupatia Mkopo wa Masharti nafuu wa Dola za Marekani milioni 292.4. Tunawashukuru sana. Nimefurahi kuona kuwa katika shughuli hii tunaye Mwakilishi wa Balozi wa Japan, Bw. Kubota, pamoja na Wawakilishi wa Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) na Benki ya Maendeleo ya Japan. Tunaomba mtufikishie shukrani zetu nyingi kwa Mfalme, Waziri Mkuu pamoja na Wananchi wote wa Japan.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana:
Mbali na mradi huu wa Kinyerezi II, hivi sasa tunafanya upanuzi wa Kinyerezi I ili kuuongezea wa kuzalisha umeme kutoka Megawati 150 za sasa hadi kufikia Megawati 325. Mradi huu ambao unatekelezwa na Serikali kwa asilimia 100 kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 188, takriban shilingi bilioni 400, nao nimeambiwa unatarajia kukamilika mwakani (2019). Miradi mingine ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia ambayo ipo kwenye hatua mbalimbali ni Kinyerezi III utakaozalisha Megawati 600, Kinyerezi IV Megawati 330, Mradi wa Mtwara Megawati 300, Somanga Fungu Megawati 330, n.k. Lakini, zaidi ya hapo, hivi sasa tupo mbioni kuanza utekelezaji wa Mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa maji wa Stiglier’s Gorge, ambao utatoa Megawati 2,100. Ni matumani yangu kuwa Wizara ya Nishati itakamalisha mapema taratibu za kumpata Mkadarasi wa kutekeleza mradi huo.
Lengo letu ni kwamba, ikifika mwaka 2020, nchi yetu iwe na angalau Megawati 5,000. Na tukiweza kutimiza lengo hilo, tutaanza kuwabana TANESCO nao wapunguze bei ya umeme. Nchi yetu ina vyanzo vingi vya kuzalisha umeme, ikiwemo gesi asilia, maji, jua, upepo, makaa ya mawe, nyuklia, n.k. Hivyo, haiwezekani bei ya umeme iendelee kuwa juu. Nitumie fursa hii kukaribisha makampuni au watu binafsi kuwekeza kwenye sekta ya umeme nchini. Lakini nitoe angalizo kwamba hatutakuwa tayari kushirikiana na wawekezaji matapeli na wenye nia ya kujinufaisha wao zaidi.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana:
Kama mjuavyo, ili umeme uweze kumfikia mtumiaji una hatua tatu muhimu. Hatua ya kwanza, ni kufufua au kuzalisha umeme wenyewe. Pili, usafirishaji; na tatu ni usambazaji. Hivyo basi, mbali na mipango na mikakati ya kuzalisha au kufufua umeme ambayo nimetoka kuielezea hivi punde, Serikali pia inatekeleza miradi mikubwa ya kusafirisha umeme. Hivi karibuni tumekamilisha mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga umbali wa wa kilometa 632. Miradi ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Singida - Namanga umbali wa kilometa 414; Mbeya – Nyakanazi msongo wa kilovoti 400; na Makambako – Songea kilovoti 250 nayo inaendelea.
Kuhusu miradi ya usambazaji umeme, hivi sasa tupo kwenye utekelezaji wa Mradi mkubwa wa Kupeleka Umeme Vijijini Awamu ya Tatu ambapo tunalenga ikifika mwaka 2020/2021 vijiji vyote nchini viwe vimefikiwa na miundombinu ya umeme. Hadi kufikia mwezi Desemba 2016 takriban vijiji 4,395 kati ya 12,268 tayari vilikuwa vimefikiwa na miundombinu ya umeme. Hivyo, Awamu hii ya Tatu utafikisha kwenye vijiji vilivyosalia ambavyo idadi yake ni 7,873. Ni matumaini yangu kuwa kutokana na hatua tunazochukua, baada ya muda mfupi ujao, nchi yetu itakuwa sio tu na umeme wa kutosha, bali pia umeme wa uhakika na wenye kupatikana kwa gharama nafuu. Na hii ndio moja ya sababu iliyonisukuma kuigawa Wizara ya Nishati na Madini ili kuwa Wizara ya Nishati peke yake na Madini peke yake.
Waheshimiwa Viongozi, na Ndugu Wananchi;
Nimekuja hapa kwa ajili ya kuzindua Mradi wa Kufufua Umeme Megawati 240 wa Kinyerezi unaotumia teknolojia ya kisasa ya combined cycle. Tayari nimemshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunialika. Nimeipongeza Wizara, TANESCO pamoja na Mkandarasi kwa kumaliza mradi mapema. Nimewashukuru marafiki zetu wa Japan kwa kutupatia mkopo wa masharti nafuu; na nimeeleza mikakati tuliyonayo ya kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini. Hata hivyo, kabla sijahitimisha, napenda nieleze masuala machache ya mwisho.
Kwanza, napenda kuhimiza Wizara ya Nishati, kupitia TANESCO na REA, kuongeza kasi ya kuunganishia wananchi umeme. Niwaombe wananchi nanyi mchangamkie fursa za kuunganishiwa umeme. Serikali imepunguza gharama za kuunganisha umeme kwa kiwango kikubwa. Sambamba na hilo, naziomba taasisi za umma na binafsi, za hapa nchi na nje ya nchi, kuongeza kasi au kuchangamkia fursa ya kusambaza gesi asilia kwa wananchi ili kupunguza athari za matumizi ya mkaa na kuni nchini. Changamkieni pia fursa za kusambaza umeme wa jua.
Pili, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO ameeleza kuwa channgamoto kubwa iliyokumba mradi huu ni kodi na tozo mbalimbali ambazo zimeongeza gharama za mradi kutoka Dola za Marekani milioni 344 hadi kufikia Dola za Marekani milioni 356.2. Nitumie fursa hii kurudia wito wangu kwa taasisi za Serikali kufanya kazi kwa karibu na kwa ushirikiano, hususan katika kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo kama hii. Hivi majuzi nilikuwa Bohari ya Dawa kupokea msaada wa magari 181 kutoka Global Fund; nao waliilalamikia Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kuwa kikwazo cha kutoa dawa bandarini. Magari ya Polisi yalikwama muda mrefu Bandari kwa sababu ya kodi. Niziombe basi, taasisi za Serikali kufanya kazi kwa ushirikiano; lakini bila kuathiri utendaji wenu.
Tatu, ni kwenu watani zangu wa Dar es Salaam. Serikali inahamia Dodoma, lakini dhamira yetu ya kuifanya Dar es Salaam kuwa Jiji la Kisasa bado ipo pale pale. Kama tulivyoahidi wakati wa kampeni, hivi sasa tunaendelea na ujenzi wa madaraja ya juu pale TAZARA na Ubungo ili kupunguza tatizo la foleni. Mwaka huu pia tunatarajia kuanza ujenzi wa Awamu ya Pili ya miundombinu ya magari ya mwendokasi kutoka Kariakoo kwenda Mbagala. Ujenzi wa Kiwanja cha Ndege unaendelea vizuri, na kama mlivyosikia jana tumeipokea ndege yetu nyingine mpya. Ujenzi wa Reli ya Kisasa kwenda Morogoro na Dodoma unaendelea. Bandari ya Dar es Salaam nayo inapanuliwa. Vilevile, Serikali imepata Mkopo kutoka Benki ya Dunia wenye thamani ya shilingi bilioni 660 ambazo zitatumika kujenga barabara zenye urefu wa kilometa 210, masoko, Stendi ya Mabasi pamoja mifereji mikubwa ya kilometa 40, ikiwemo katika Bonde la Msimbazi. Miradi hii imepangwa ikamilike mwaka 2020.
Kuhusu elimu, Mkoa wa Dar es Salaam unatengewa wastani wa shilingi bilioni 1 kila mwezi kwa ajili ya elimu bila malipo. Mwaka huu wa fedha, tayari umepokea shilingi bilioni 7.27; na tangu mpango huu uanze, umeshapokea shilingi bilioni 25.84. Sambamba na fedha hizo za elimu bila malipo, katika Mwaka huu wa Fedha, Mkoa umepokea shilingi bilioni 3.5 ili kujenga na kukarabati miundombinu, ambapo jumla ya shule za msingi 4 na sekondari 12 zinakarabatiwa, zikiwemo shule kongwe za Azania, Jangwani na Tambaza.
Kuhusu afya, ninyi ni mashahidi upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya unazidi kuimarika. Ujenzi wa miundombinu unaendelea. Hospitali za Rufaa za Mkoa za Amana, Mwananyamala na Temeke zimeboreshewa miundombinu. Tunajenga hospitali za Wilaya ya Konondoni (Mabwepande) na Ilala (Kivule). Vituo vya afya vya Kimbiji (Kigamboni), Mtoni Kijichi, Charambe navyo vinakarabatiwa ili viwe na uwezo wa kutoa huduma za dharura, hususan upasuaji kwa wajawazito. Hospitali za Kitaifa zilizopo hapa Dar es Salaam, ikiwemo Muhimbili tunaendelea kuiboresha. Na kama mnavyofahamu, Hospitali ya Mloganzila nayo imeanza kazi na hivyo kupunguza mzigo kwa Muhimbili.
Haya niliyosema ni baadhi tu ya mambo ambayo tuliahidi na tumeanza kuyatekeleza. Niwaombe wana-Dar es Salaama na Watanzania kwa ujumla, endeleeni kuiunga mkono Serikali, lakini tushirikiane kuitunza amani yetu. Tusikubali watu wachache, kwa maslahi yao binafsi, watuondoe katika ajenda yetu ya maendeleo au watufarakanishe kwa misingi ya ukabila, udini, ukanda, n.k. Niliapa kuilinda amani ya nchi yetu, naahidi nitailinda kwa nguvu zangu zote.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta hapa la Kuzindua Mradi wa Kufufua Umeme wa Kinyerezi utakaozalisha Megawati 240.
Mungu Ibariki Miradi yetu ya Umeme!
Mungu wabariki Wana-Dar es Salaam!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza’

- Apr 02, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA MRADI WA KUSIMIKA MFUMO WA RADA NNE ZA KU...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA MRADI WA KUSIMIKA MFUMO WA RADA NNE ZA KUONGOZA NDEGE
KWENYE VIWANJA VYA JULIUS NYERERE,
KILIMANJARO, MWANZA NA SONGWE
DAR ES SALAAM, TAREHE 2 APRILI, 2018
Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Ujenzi,
Uchukuzi na Mawasiliano;
Mheshimiwa Dkt. Sira Ubwa, Waziri wa Ujenzi,
Mawasiliano na Usafirishaji wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Waziri mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam
pamoja na Wakuu wa Mikoa mingine mliopo;
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu;
Waheshimiwa Wabunge mliopo hapa;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo hapa;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Ndugu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania;
Viongozi na Wafanyakazi wa TCAA, ATCL, TAA;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali,
Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Waheshimiwa Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa kushuhudia tukio hili. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri Prof. Mbarawa kwa kunialika katika hafla hii ya Uzinduzi wa Mradi wa Mfumo wa Rada kwa ajili ya kuongoza ndege kwenye Viwanja vyetu vya Julius Nyerere (Dar es Salaam), Kilimanjaro (KIA), Mwanza pamoja na Songwe. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Rada ni chombo au nyenzo muhimu sana sio tu kwa ajili ya usafiri wa anga, bali pia usalama na maendeleo ya nchi kwa ujumla. Licha ya ukweli huo, nchi yetu hivi sasa ina rada moja tu ya kiraia, ambayo inatumika kuongozea ndege. Rada hiyo ipo hapa kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere hapa Dar es Salaam; na ina uwezo wa kuhudumia asilimia 25 tu ya anga letu. Na kwa bahati mbaya, uwezo wa Rada hiyo ambayo ilinunuliwa mwaka 2002 ili itumike kwa kipindi cha miaka 12, nao umepungua sana kutokana na uchakavu. Hii imefanya baadhi ya mashirika ya ndege yasite kufanya shughuli zao hapa nchini.
Ni kutokana na hali hiyo, leo nimefurahi sana kuja hapa kuweka Jiwe la Msingi la Mradi huu wa Usimikaji Mfumo wa Rada Nne kwenye Viwanja vyetu vya hapa Dar es Salaam, Kilimanjaro, Mwanza na Songwe. Kwa hakika, nimefurahi sana. Na nimefurahi kwa sababu, sasa nina hakika kuwa Mradi huu utakapokamilika, tutakuwa na uwezo wa kuliona anga letu lote pamoja na anga za nchi jirani, hususan Burundi na Rwanda, ambazo Shirika la Kimataifa la Anga (ICAO) limetukasimu. Hii pia itaimarisha usalama wa nchi yetu; itarahisisha shughuli za uongozaji ndege na pia itaiongezea nchi yetu mapato. Hivi sasa tunapoteza wastani wa shilingi bilioni 1.2 ya tozo ya kuongozea ndege kwa mwaka kutokana na ICAO kukasimu sehemu ya anga la nchi yetu kwa majirani zetu wa Kenya. Hivyo, nina uhakika kuwa Mradi huu ukikamilika, sehemu hiyo tutarejeshewa na tutaweza kukusanya fedha tunazozipoteza.
Napenda kutumia fursa hii kuipongeza Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini kwa kuanza kutekeleza mradi huu. Kama mlivyosikia, Mradi huu utagharimu takriban shilingi bilioni 67.3. Asilimia 45 ya fedha hizo zinatoka kwenye vyanzo vya ndani vya Mamlaka, ambavyo wamepata baada ya kuamua kujibana. Serikali Kuu imewaunga mkono kwa kuwaongezea asilimia 55 iliyobaki. Hii maana yake ni kwamba fedha zote za kutekeleza mradi huu zimetolewa na Serikali. Hongereni sana TCAA. Nahimiza taasisi nyingine nazo ziige mfano wenu.
Nitutumie fursa hii pia kuwapongeza viongozi na wafanyakazi wa TCAA kwa kazi nzuri mnayoifanya ambayo inailetea sifa nchi yetu. Hivi punde Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ameeleza kuwa mmevuka lengo la usalama ICAO la asilimia 60 kwa kupata asilimia 64.35. Nawapongezeni sana kwa kuvuka lengo hilo tena kwa kipindi kifupi sana. Mwaka 2013 mlipata asilimia 37.8. Hongereni sana. Nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri kuwa nitakuwa tayari kumpokea Rais wa ICAO wakati wowote ili niweze kupokea tuzo ambayo TCAA imepata.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kama alivyogusia Mheshimiwa Waziri kuwa Mradi huu wa Rada ni sehemu ya miradi mingi inayotekelezwa nchini kwa lengo la kuboresha na kuimarisha usafiri wa anga. Kama mnavyofahamu, katika dunia ya sasa usafiri wa anga ni muhimu sana, hususan katika masuala ya biashara (ikiwemo kusafirisha maua, mbogamboga, minofu ya samaki na nyama) na pia kukuza sekta ya utalii. Zaidi ya asilimia 70 ya watalii duniani wanatumia usafiri wa anga. Na kama mjuavyo, nchi yetu ni miongoni mwa nchi zinazoongoza kwa kuwa na vivutio vingi vya utalii, na katika kipindi kifupi kijacho, tumejipanga kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu kutoka milioni 1.3 ya sasa hadi milioni 5. Kwa sababu hiyo, uimarishaji wa usafiri wa anga ni jambo lisilokwepeka.
Hivyo basi, mbali na Mradi huu wa Rada, tumenunua ndege mpya sita. Tatu tayari zimewasili, ikiwemo moja ambayo itawasili baadaye leo. Ndege nyingine tatu zinatarajiwa kuwasili baadaye mwaka huu, ikiwemo ndege kubwa ya Boeing Dreamliner yenye uwezo wa kubeba watu 262. Mbali na ununuzi wa ndege, tunafanya upanuzi wa viwanja vikubwa vya Dar es Salaam na Kilimanjaro kwa gharama ya takriban shilingi bilioni 650. Aidha, tunafanya upanuzi wa viwanja vingine 11 vya mikoani kwa gharama ya shilingi bilioni 500. Ni matumaini yangu kuwa miradi hii ikikamilika, usafiri wa anga nchini utaimarika. Na kama mnavyofahamu, tunaendelea pia kuimarisha usafiri wa reli, maji na barabara.
Mheshimiwa Waziri, Mabibi na Mabwana;
Nimekuja hapa kwa ajili ya kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Rada. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba nieleze masuala mawili ya mwisho.
Mosi, nazihimiza Wizara, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege na Msimamizi wa Mradi huu kuhakikisha mnamsimamia kwa karibu Mkandarasi, Kampuni ya Thales Las France SAS, ili mradi huu ukamilike mapema, ikiwezekana kabla ya muda uliopangwa. Niombe pia Mamlaka ya Usafiri wa Anga kuhakikisha mnaandaa wataalam wa kutosha kwa ajili ya kuendesha na kutunza Rada tunazojenga. Nimefurahi kusikia kuwa wataalam takriban 33 tayari wapo Ufaransa kwa ajili ya mafunzo.
Pili, naziagiza mamlaka husika kuimarisha ulinzi na usalama kwenye viwanja vyetu. Hakikisheni viwanja vyote vinakuwa na vifaa vya kisasa vya ukaguzi wa abiria lakini pia mipaka ya viwanja vyote ilindwe. Tukio la aibu na la kusikitisha lililotokea Mwanza halipaswi kujirudia tena.
Tatu, katika maelezo yako Mheshimiwa Waziri umeeleza wasiwasi wako kuwa ujenzi wa Mradi huu unaweza kuchelewa kukamilika kwa sababu ya tatizo la fedha linalokabili ujenzi wa jengo jipya la kuongeza ndege katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Napenda kuiagiza Wizara ya Ujenzi kumsimamia kwa karibu Mkandarasi anayetekeleza ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Amekuwa akisuasua sana na kutoa visingizio vingi. Fedha za kutekeleza mradi huo zipo. Hivyo basi, narudia tena kuwaagiza kumsimamia Mkandarasi huyo kwa karibu. Mradi huo umechelewa sana kukamilika; hivyo tusiruhusu uendelee kuchelewa na kukwamisha ujenzi wa Rada.
Suala la nne na la mwisho, napenda nitumie fursa hii kuwaarifu wana-Dar es Salaam na Watanzania kwa ujumla kuwa nchi yetu inaenda vizuri. Tupo vizuri. Mwaka jana (2007) uchumi wetu ulikua kwa asilimia 7 na hivyo kuifanya nchi yetu kuwa miongoni mwa nchi tano ambazo uchumi wake unakuwa kwa kasi kubwa Barani Afrika. Na hii pia ndio imetuwezesha kununua ndege sita, tunajenga reli, tunajenga barabara, tunatekeleza miradi ya umeme, tunaboresha huduma za afya, elimu na maji. Tusingekuwa vizuri kiuchumi tusingeweza kufanya mambo hayo yote kwa mpigo. Nitumie fursa hii kuwapongeza Watanzania wote kwa kuendelea kulipa kodi. Miradi hii yote tumeweza kuitekeleza kutokana kodi zenu. Hivyo, endeleeni kulipa kodi, lakini pia chapeni kazi kwa bidii, na bila kusahau tuzidi kudumisha amani na mshikamano wetu. Serikali, kwa upande wake, ipo imara katika kuhakikisha amani ya nchi yetu inaendelea kudumu.
Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi;
Waheshimiwa Viongozi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nihitimishe hotuba yangu kwa kukushukuru tena Mheshimiwa Waziri kwa kunialika. Aidha, narudia tena kuipongeza Wizara, Mamlaka ya Usafiri wa Anga pamoja na taasisi nyingine zilizopo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kazi nzuri na kubwa mnazoendelea kuzifanya. Hongereni sana. Endeleeni kufanya kazi kwa kujituma. Serikali ipo pamoja nanyi.
Mabibi na Mabwana; Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta hapa la kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Mfumo wa Rada kwa ajili ya Viwanja vya Ndege vya Julius Nyerere, Kilimanjaro, Mwanza na Songwe utakaogharimu shilingi bilioni 67.3, ambazo zote zitatolewa na Serikali yetu.
Mungu Ubariki Mradi huu wa Ujenzi wa Rada!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
.jpg)
- Mar 26, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA MAGARI MAPYA 181 YA BOHARI YA DAWA YA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA MAGARI MAPYA 181 YA BOHARI YA DAWA YALIYOTOLEWA NA MFUKO WA DUNIA
WA KUPAMBANA NA UKIMWI, MALARIA NA KIFUA KIKUU
DAR ES SALAAM, TAREHE 26 MACHI, 2018
Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto;
Waheshimiwa Manaibu Mawaziri mliopo;
Bwana Linden Morrison, Mwakilishi wa Mtendaji Mkuu
wa Mfuko wa Dunia wa Kupambana na UKIMWI,
Kifua Kikuu na Malaria (Global Fund);
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Dkt. Mpoki Ulisubisya, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto;
Ndugu Makatibu Wakuu mliopo;
Bwana Laurean Rugambwa Bwanakunu,
Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa;
Viongozi wengine wa Serikali, Vyama vya Siasa
pamoja na Viongozi wa Dini mliopo;
Ndugu Wafanyakazi wa Bohari ya Dawa;
Wageni waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa uzima na kutuwezesha kukutana hapa. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Afya kwa kunialika kwenye tukio hili muhimu la Uzinduzi wa Magari 181 ya Bohari ya Dawa, ambayo nchi yetu imepatiwa msaada na Mfuko wa Dunia wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria (Global Fund. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri kwa kunialika.
Napenda pia nitumie fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kutoa shukrani zangu nyingi kwa Global Fund kwa kutoa msaada huu wa magari 181 kwa Bohari yetu ya Dawa. Nimeambiwa kuwa baada ya kupata magari haya, ambayo thamani yake ni shilingi bilioni 20.75, sasa Bohari ya Dawa itakuwa na jumla ya magari 213 kutoka 32 iliyokuwa nayo awali. Hii, bila shaka, itaongeza ufanisi na utendaji kazi wa Bohari yetu ya Dawa, hususan katika kusambaza dawa na vifaa tiba sehemu mbalimbali nchini. Hivyo basi, tunawashukuru sana Global Fund kwa kutupatia msaada huu.
Lakini niseme tu kwamba, hii sio mara ya kwanza kwa Global Fund kutupatia msaada. Tangu Mfuko huu uanzishwe mwaka 2003, nchi yetu imenufaika na misaada yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.9, sawa na zaidi ya shilingi trilioni 4, hadi kufikia mwezi Julai 2017. Kama mnavyofahamu, Mfuko huu ndio pia umetoa fedha kwa ajili ya kujenga nyumba 480 za watumishi wa afya sehemu mbalimbali nchini, kupitia Taasisi ya Benjamin William Mkapa.
Ukiachilia mbali misaada hiyo, mwezi Julai mwaka jana, Mfuko huu uliidhinisha kiasi kingine cha Dola za Marekani milioni 591, takriban shilingi trilioni 1.1, kitakachotumika hadi mwaka 2020, kwa ajili ya kupambana na magonjwa ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Malaria pamoja na kuboresha na kuimarisha huduma za afya nchini. Tunawashukuru sana marafiki zetu hawa wa Global Fund. Nimefurahi kuona kuwa katika hafla hii tunaye mwakilishi wa Global Fund, Bwana Morrison. Kwa niaba yangu binafsi, na kwa niaba ya Serikali na Watanzania wote, naomba utufikishie shukrani zetu nyingi kwa uongozi wa juu wa Global Fund. Tunawasihi mzidi kuunga mkono jitihada zetu za kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu, Malaria pamoja na kuboresha na kuimarisha sekta ya afya nchini. Tunaahidi kuitumia vizuri misaada yenu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sekta ya afya ni nyeti na muhimu kwa maendeleo ya Taifa lolote. Bila kuiimarisha sekta hii ni ndoto kupata maendeleo. Hata azma na dhamira yetu ya kuwa nchi ya uchumi wa kati wenye kuongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025, haiwezi kutimia kama hatutaweka mkazo kwenye sekta ya afya. Hii ni kwa sababu, ili kufikia azma hiyo, tunahitaji wananchi wenye afya njema; watakaoweza kushiriki kikamilifu shughuli za kiuchumi na uzalishaji, kama vile ujenzi wa viwanda, kilimo, uvuvi, ufugaji, utalii, biashara, n.k.
Kwa kuzingatia hilo, na kwa nia ya kuendeleza jitihada zilizofanywa na awamu zilizotangulia, Serikali ya Awamu ya Tano imetoa kipaumbele kikubwa kwenye sekta ya afya. Hivi sasa sekta ya afya ni miongoni mwa zinazoongoza kwa kutengewa fedha nyingi. Mathalan, katika Mwaka wa Fedha 2015/2016 ilitengewa shilingi trilioni 1.8, Mwaka wa Fedha 2016/2017 shilingi trilioni 1.9 na Mwaka huu wa Fedha imetengewa shilingi trilioni 2.2. Moja ya maeneo yaliyonufaika zaidi na ongezeko hili la bajeti ni eneo la dawa na vifaa tiba. Bajeti ya kununua dawa imeongezeka maradufu, kutoka shilingi bilioni 31 Mwaka wa Fedha 2015/2016 hadi kufikia shilingi bilioni 251 Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mwaka huu wa Fedha (2017/2018) imefikia shilingi bilioni 269.
Nitumie fursa hii kuwapongeza sana Wizara ya Afya pamoja na Bohari ya Dawa kwa kazi nzuri ya kuhakikisha dawa zinapatikana nchini. Niwapongeze pia uamuzi wa kuanza kununua dawa na vifaa tiba moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji. Uamuzi huo umesaidia sana kudhibiti bei za dawa nchini. Sina shaka, ufanisi na utendaji kazi wenu mzuri ndio umewesha Bohari yetu ya Dawa kukasimiwa jukumu la kununua dawa, vifaa tiba na vitendanishi kwa niaba ya nchi zote za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Hongereni sana Bohari ya Dawa. Ni matumaini yangu kuwa magari haya 181 mliyopewa na Global Fund, yataboresha zaidi utendaji wenu wa kazi, na hasa katika kuhakikisha upatikanaji na usambazaji dawa nchini. Na katika hili, niwahimize Bohari ya Dawa kuendelea kufungua Maduka ya Dawa sehemu mbalimbali nchini ili kuongeza uhakika dawa nchini.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ukiachilia mbali eneo la dawa, Serikali inaendelea na ujenzi pamoja na ukarabati wa miundombinu ya vituo vya kutolea huduma za afya. Tumejenga vituo vipya vya kutolea huduma za afya vipatavyo 268 na hivyo kuifanya nchi yetu kuwa na vituo vya kutolea huduma za afya vipatavyo 7,284. Vituo vingine vya kutoa huduma za afya vinaendelea kujengwa sehemu mbalimbali nchini, ikiwemo ujenzi wa Hospitali za Mikoa mipya ya Njombe, Geita, Katavi na Simiyu. Sambamba na ujenzi wa vituo hivyo vipya, hivi sasa tunaboresha vituo vya afya 204 nchi nzima. Moja ya malengo ya uboreshaji huo ni kuviwezesha vituo hivyo kufanya upasuaji wa dharura lengo likiwa kupunguza vifo vya akimama wajawazito na mtoto kutoka wastani wa vifo 556 katika kila vizazi hai 100,000 hivi sasa hadi kufikia angalau vifo 292 mwaka 2020. Naziipongeza Wizara ya Afya na TAMISEMI kwa kusimamia ujenzi wa vituo hivyo.
Tumeendelea pia kuimarisha huduma za kibingwa kwenye Hospitali zetu za Rufaa za Muhimbili, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Taasisi ya Mifupa (MOI), Taasisi ya Saratani ya Ocean Road pamoja na hospitali za rufaa za Bugando, Mbeya na KCMC. Aidha, tunaziimarisha Hospitali zetu za Benjamini Mkapa iliyopo Chuo Kikuu cha Dodoma pamoja na Hospitali yetu ya kisasa kabisa ya Mloganzila, ambayo niliizindua mwezi Novemba 2017. Ni wazi kuwa hatua hizi tunazozichukua sio tu zitaboresha na kuimarisha sekta ya afya nchini, bali pia zitaiwezesha nchi yetu kufikia azma yake ya kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Mheshimiwa Waziri wa Afya;
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kuzindua magari haya 181 yaliyotolewa na Global Fund kwa Bohari yetu ya Dawa. Hata hivyo, kabla sijatekeleza jukumu hilo, naomba mniruhusu niseme masuala machache ya mwisho.
Suala la kwanza ni kuhusu utunzaji wa magari haya. Kama mlivyosikia, magari haya yamegharimu fedha nyingi. Hivyo basi, Bohari ya Dawa mnao wajibu wa kuhakikisha magari haya yanatunzwa. Hakikisheni mnatafuta madereva makini ili magari haya yatumike kwa muda mrefu. Nitashangaa sana na kwa kweli nitasikitika sana, endapo baada ya mfupi kupita, nitasikia magari haya yameharibika.
Pili, naendelea kuhamasiha taasisi na wafanyabiashara kuwekeza kwenye viwanda vya dawa nchini. Kama ambavyo mmesikia, Serikali imeongeza bajeti ya dawa hadi kufikia shilingi bilioni 269. Ukijumlisha na michango kutoka kwa wafadhili mbalimbali, bajeti ya dawa hivi sasa inafikia takriban shilingi bilioni 460, kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema. Zaidi ya hapo, kama nilivyogusia awali, Bohari yetu ya Dawa imepewa dhamana na Global Fund kununua dawa kwa ajili ya nchi zote za SADC. Lakini, pamoja na mafanikio hayo, inasikitisha kuona kuwa asilimia 94 ya dawa ambazo Bohari ya Dawa inanunua zinatoka nje ya nchi. Kama tungekuwa na viwanda vya dawa, fedha nyingi zingebaki hapa nchini na Watanzania wangepata ajira. Ni kwa sababu hii nazidi kukihimiza ujenzi wa viwanda vya dawa nchini. Na nitumie fursa hii kutoa wito kwa Wizara ya Afya kubuni mkakati wa kuwahamasisha wafanyabiashara na wataalam wa hapa nchi kujenga viwanda vya dawa. Serikali itakuwa tayari kuwaunga mkono.
Tatu, pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali za kuimarisha upatikanaji dawa nchini, ninazo taarifa kuwa wakati mwingine Bohari ya Dawa imekuwa ikikumbana na vikwazo katika kuingiza dawa nchini kutoka taasisi mbalimbali za Serikali. Kwa kweli, mimi huwa nashangaa sana. Inakuwaje taasisi moja ya Serikali inaikwamisha taasisi nyingine. Taasisi za Serikali hazipaswi kukwamishana katika utendaji kazi. Zinao wajibu wa kufanya kazi kwa ukaribu na ushirikiano. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuzihimiza taasisi za Serikali kuacha kukwamishana. Na niseme tu kwamba, Serikali haitavumilia kuona taasisi yake moja ikikwamisha shughuli za taasisi nyingine. Hilo likitokea, hatutasita kuchukua hatua. Lakini kuhusu suala hili la Bohari ya Dawa, naagiza Wizara ya Wizara ya Afya kulishughulikia na hasa kwa sababu, kwa mujibu wa taarifa nilizonazo, kikwazo kikubwa cha uingizaji dawa kimekuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TDFA), ambayo nayo ipo chini ya Wizara ya Afya. Hili ni suala lenu la ndani; hivyo hamna budi kulishughulikia ninyi wenyewe.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kumshukuru tena Mheshimiwa Waziri kwa kunialika. Aidha, narudia tena kuwashukuru Global Fund kwa kutupatia msaada huu wa magari pamoja na misaada mingine wanayotoa kwa nchi yetu. Nawapongezeni tena Bohari ya Dawa kwa kazi nzuri na kubwa mnayoifanya, lakini pia nawahimiza kutunza magari haya.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kuzindua magari 181 yenye thamani ya shilingi bilioni 20.75 ambayo yametolewa na Mfuko wa Dunia wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria.
Mungu Ibariki Global Fund!
Mungu Ibariki Bohari ya Dawa!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Mar 14, 2018
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI KWENYE HAFLA YA KUWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA RELI MPYA YA KISASA (STAND...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI KWENYE HAFLA YA KUWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA RELI MPYA YA KISASA (STANDARD GAUGE RAILWAY – SGR) STESHENI YA IHUMWA, DODOMA, TAREHE 14 MACHI, 2018
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Mizengo Pinda, Waziri Mkuu Mstaafu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Philip Mangula, Makamu Mwenyekiti
wa Chama Cha Mapinduzi – Bara;
Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa,
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo hapa;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge,
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo hapa;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Mheshimiwa Balozi wa Uturuki nchini;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Profesa John Kandoro, Mwenyekiti wa Bodi
ya Shirika la Reli Tanzania;
Bwana Masanja Kadogosa, Mkurugenzi Mtendaji
wa Shirika la Reli Tanzania;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Viongozi na Wafanyakazi wa Makampuni
ya Yapi, Merkezi (Uturuki) na Mota Engil ya Ureno;
Wafanyakazi wa Shirika la Reli nchini;
Ndugu Wananchi, Wana-Habari, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa leo hii. Aidha, napenda kuushukuru Uongozi wa Wizara ya Ujenzi pamoja na Shirika la Reli nchini kwa kunialika kushiriki kwenye tukio hili muhimu na la kihistoria la kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge) kutoka Morogoro hadi Dodoma (Makutopora), umbali wa kilometa 422. Nakumbuka, tarehe 12 Aprili mwaka jana, mlinialika kuweka Jiwe la Msingi la Awamu ya Kwanza la Mradi huu pale Pugu, Dar es Salaam. Na leo mmenialika tena, nawashukuruni sana.
Napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru wananchi wa hapa Ihumwa, maeneo jirani pamoja na Mkoa mzima wa Dodoma kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika tukio hili. Nimepita hapa Ihumwa mara nyingi, lakini sikuwa nikifahamu kuwa Kitongoji hiki ni kikubwa. Leo nimejionea mwenyewe; na kwa namna mlivyojitokeza kwa wingi kwenye tukio hili, napenda kuwaahidi kuwa Serikali itajenga barabara kutoka pale Barabara Kuu (Dar –es Salaam – Dodoma) hadi hapa stesheni. Waziri wa Ujenzi yupo hapa, hivyo basi, ni matumaini yangu kuwa amenisikia.
Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi;
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Ni jambo lililo wazi kuwa miundombinu imara ya usafiri ni kichocheo muhimu cha ukuaji uchumi katika nchi. Bila kuwa na miundombinu hiyo, ni ndoto kupata maendeleo. Moja ya changamoto kubwa zenye kulikabili Bara la Afrika ni kukosekana kwa miundombinu imara na ya uhakika ya usafiri.
Hali hii inasababisha gharama za usafiri kuwa juu ukilinganisha na Mabara mengine. Tafiti zinaonesha kuwa gharama za usafiri katika Bara la Afrika ni kubwa kuliko maeneo mengine duniani. Mathalan, wastani wa bei ya kusafirisha kontena moja la futi 20 kwenye nchi za Afrika Mashariki, umbali usiozidi kilometa 1,500, ni Dola za Marekani 5,000. Bei hii ni sawa kabisa na gharama ya kusafirisha kontena lenye ukubwa kama huo kutoka China hadi Tanzania, umbali wa kilometa 9,000.
Kwa ujumla, tafiti zinaonesha kuwa kukosekana kwa miundombinu imara ya usafiri kunashusha Pato la nchi za Afrika kwa asilimia 2 na kuongeza gharama za usafirishaji kwa asilimia 40. Hii ndio moja ya sababu inayozifanya nchi zetu zishindwe kushindana na nchi za Mabara mengine katika masuala ya biashara, uwekezaji na halikadhalika maendeleo ya viwanda. Ni kwa sababu hiyo, leo nimefurahi sana kuja hapa Ihumwa kuweka Jiwe hili la Msingi la Awamu ya Pili ya Mradi wa Reli hii ya Kisasa kutoka Morogoro hadi Dodoma, ambayo nchi yetu imeamua kuijenga kwa fedha zake yenyewe. Nimefurahi sana.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kuna njia kuu nne za usafiri. Usafiri wa anga, maji, barabara na reli. Hata hivyo, tafiti zimethibitisha kuwa usafiri wa njia ya reli ni bora, salama, wa haraka na nafuu zaidi ukilinganisha na njia nyingine, hususan katika kusafirisha shehena kubwa ya mizigo na idadi kubwa ya abiria. Ripoti ya Benki ya Maendeleo ya Afrika ya Mwaka 2015 kuhusu Usafiri wa Reli (Rail Infrastructure in Africa: Financing Policy Option) inaeleza kuwa, napenda kunukuu kwa Kiswahili,“Rail Transport is critical to supporting economic development and, unless this mode of transport is developed, Africa may not realize its full potential in exploiting its abundant natural resources and wealth”, mwisho wa kunukuu. (Nikinukuu maneno hayo kwa lugha yetu adhimu ya Kiswahili, Ripoti hiyo ya AfDB inasema kuwa, Usafiri wa reli ni mhimili muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi na, endapo usafiri huu hautaboreshwa au kuimarishwa, Afrika kamwe haitaweza kutumia rasilimali na utajiri ilionao). Hii inadhihirisha kuwa usafiri wa njia ya reli ni muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi.
Kwa bahati nzuri, nchi yetu inazo njia kuu mbili za usafiri wa reli. Reli ya Kati iliyojengwa enzi za ukoloni, kati ya mwaka 1899 na 1929; na ile ya TAZARA inayounganisha nchi yetu na ndugu zetu wa Zambia, ambayo ilijengwa miaka ya 1970 kwa msaada wa marafiki zetu wa China. Hata hivyo, utendaji kazi wa reli hizi sio wa kuridhisha sana kutokana na uwekezaji mdogo, ubovu wa miundombinu, uchakavu wa vitendea kazi, ikiwemo vichwa vya treni na mabehewa, pamoja na matatizo ya uongozi yaliyokuwepo.
Naupongeza uongozi mpya ukiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Bwana Masanja Kadogosa pamoja na watumishi wote wa Shirika la Reli kwa kuanza kuchukua hatua za kuboresha na kuimarisha usafiri wa reli nchini, hususan Reli ya Kati. Mmeanza kufanya ukarabati wa reli kutoka Tanga hadi Arusha. Mapato pia yameanza kuongezeka. Hii inadhihirisha kuwa Watanzania tukiamua tunaweza. Siku za nyuma, tuliwahi kukodisha Shirika hili kwa Kampuni kutoka nje, lakini matokeo hayakuwa mazuri. Lilizidi kudidimia. Hivyo basi, naipongeza Wizara, uongozi mpya wa Shirika na watumishi wote kwa jitihada mnazozifanya za kuliimarisha Shirika hili.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ujenzi wa reli hii mpya na ya kisasa, ambayo itatumia umeme na dizeli, utaongeza tija na ufanisi katika usafiri wa reli nchini. Kwa haraka haraka, naomba nitaje baadhi ya faida zitakazoletwa na reli hii.
Faida ya kwanza, reli hii itarahisisha usafiri wa mizigo na abiria. Tumesikia hivi punde kuwa mwendokasi wa reli hii itakuwa kilometa 120 kwa treni za mizigo na kilometa 160 kwa saa kwa treni za abiria. Hii ina maana kuwa mtu ataweza kusafiri kutoka Dar es Salaam hadi hapa Dodoma kwa kutumia saa 3 tu, kutoka wastani wa saa 5 hadi 6 zinazotumika hivi sasa kwa usafiri wa gari na saa 12 zinazotumika sasa kwa kutumia reli. Aidha, mtu atasafiri kwa kutumia saa 9 tu hadi Mwanza kutoka saa 36 za reli ya sasa. Ni dhahiri kuwa hii itarahisisha huduma za usafiri sio tu hapa nchini bali pia kwenda nchi jirani.
Aidha, reli hii itaongeza biashara hapa nchini pamoja na nchi za jirani. Kama mnavyofahamu, nchi yetu inapakana na takriban nchi 8, ambapo 6 hazina Bahari; hivyo, kutegemea kupitishia mizigo yao kwenye Bandari zetu. Inakadiriwa kuwa reli hii itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani milioni 17 kwa mwaka, ukilinganisha na tani milioni 5 za sasa. Hii, bila shaka, itaongeza mapato kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam, lakini pia itaimarisha biashara, hususan kati ya nchi yetu na nchi zinazohudumiwa na Ushoroba wa Kati (Central Corridor), yaani Burundi, DRC, Rwanda na Uganda.
Vilevile, ujenzi wa reli hii utasaidia kutunza barabara zetu. Kama mnavyofahamu, tumepiga hatua kubwa katika ujenzi wa barabara za lami. Mikoa mingi tayari imeunganishwa kwa barabara za lami. Mathalan, Mkoa wa Dodoma hivi sasa umeunganishwa na Mikoa ya Manyara, Morogoro, Singida na Iringa kwa lami. Hata hivyo, barabara zetu, wakati mwingine, zimekuwa zikiharibika mapema kutokana na kutumika kusafirisha mzigo mkubwa. Hivi punde tumesikia kuwa reli hii ya kisasa itakuwa na uwezo wa kubeba mzigo wa takriban tani 10,000 kwa mara moja, sawa na malori (semi trailers) 500 yenye uwezo wa kubeba tani 20. Hii, bila shaka, itasaidia sio tu kutunza barabara zetu, bali pia kupunguza gharama za kukarabati barabara hizo mara kwa mara.
Halikalidhalika, ujenzi wa reli hii utasaidia kukuza sekta nyingine za kiuchumi. Kama mnavyofahamu, ustawi wa sekta zote za kiuchumi (kilimo, uvuvi, ufugaji, viwanda, madini, utalii, n.k.) unategemea miundombinu ya usafiri. Ni vigumu sana kukuza sekta hizo za kiuchumi bila kuwa na miundombinu imara ya usafiri.
Sambamba na hayo, ujenzi wa reli hii ya kisasa utatoa ajira. Inakadiriwa kuwa jumla ya ajira 30,000 za moja kwa moja na nyingine 600,000 zisizo za moja kwa moja zitatolewa wakati wa ujenzi wa reli hii. Hii itasaidia kupunguza tatizo la ajira nchini. Zaidi ya hapo, reli hii itasaidia kupunguza uharibifu wa mazingira. Kama mnavyofahamu, reli hii itakuwa pia inatumia umeme, ambao hautoi hewa ya ukaa kwa wingi, na hivyo kusaidia kutunza mazingira yetu.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Hizi ni baadhi tu ya faida za ujenzi wa reli hii. Zipo nyingine nyingi. Hivyo basi, sisi Watanzania hatuna budi kujivuna na kujipongeza kwa kutekeleza mradi huu. Ndio; sisi Watanzania ni lazima tujivune. Tuna kila sababu ya kujivuna. Nchi yetu imebarikiwa sana. Ni kubwa, na kama mlivyosikia hivi majuzi imetangazwa kuwa, hivi sasa tumefikia takriban milioni 54. Hii inatuongezea nguvu na sauti kimataifa, lakini pia ni mtaji mkubwa katika harakati zetu za kujiletea maendeleo. Wenzetu wa China wametumia fursa kama hii (ukubwa wa nchi na idadi ya watu, bilioni 1.3) kujiletea maendeleo. Hivyo basi, na sisi tunaweza kutumia fursa hii kuharakisha maendeleo kwenye nchi yetu.
Hata hivyo, ni wazi kuwa, ukubwa wa nchi na idadi ya watu peke yake, sio hoja. Ni kwa namna gani tunatumia ukubwa wa nchi na idadi ya watu tuliyonayo ndio jambo la msingi zaidi. Nchi ya Denmark ni ndogo na ina idadi ya watu wapatao milioni 5. Lakini, nchi hii ni tajiri na wanatoa misaada hadi kwa nchi yetu. Hii imewezekana kwa vile wamejipanga vizuri na wanajituma katika kufanya kazi. Ndio sababu na mimi kila wakati nimekuwa nikiwasisitiza Watanzania kufanya kazi. Maendeleo si lelemama. Hakuna njia ya mkato katika kutafuta maendeleo. Usipofanya kazi, kila siku utakuwa unalalamika kuwa “vyuma vimebana”.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza Watanzania wenzangu tuzidi kuchapa kazi. Mbali na ujenzi wa reli hii, hivi sasa tunatekeleza au tupo mbioni kuanza kutekeleza miradi mikubwa ya miundombinu, ikiwemo Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga; Mradi wa Kufufua Umeme wa Stiglier’s Gorge na Usambazaji wa Umeme Vijijini (REA); Upanuzi wa Bandari za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga; upanuzi wa viwanja vya ndege, ujenzi wa barabara; utengenezaji wa meli katika Ziwa Victoria na Maziwa mengine; n.k. Miradi hii itatoa ajira nyingi, zaidi ya milioni moja. Hivyo basi, nawasihi sana Watanzania tuzichangamkie.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimekuja hapa kwa ajili ya kuweka Jiwe la Msingi la Mradi huu wa Reli ya Kisasa kutoka Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Mwanza na Kigoma; na hatimaye kuelekea nchi za Burundi na Rwanda. Nimetumia muda mwingi kueleza umuhimu na faida za mradi huu. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, napenda kueleza mambo manne ya mwisho.
Jambo la kwanza, ni kuhusu utekelezaji wa mradi huu. Natoa wito kwa Wizara ya Ujenzi, Mshauri Msimamizi pamoja na Mkandarasi kuhakikisha Mradi huu unakamilika kwa wakati. Nimefurahi kuwa ujenzi wa Awamu ya Kwanza kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro unaendelea vizuri. Hakikisheni miradi hii yote inakamilika mapema iwezekanavyo, ikiwezekana kabla ya muda uliopangwa. Watanzania wana hamu kubwa ya kuona mradi huu unakamilika.
Pili, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza Watanzania wote kuendelea kulipa kodi ili kutekeleza miradi ya maendeleo kama hii, pamoja na kuboresha huduma mbalimbali za jamii. Kama mnavyofahamu, ujenzi wa reli hii kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza, yenye urefu wa kilometa 1,219 na ambao utajengwa kwa awamu tano, utagharimu takriban shilingi trilioni 15. Katika awamu hizi mbili za mwanzo, yaani kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro na Morogoro hadi Dodoma umbali wa kilometa 722, Serikali itatumia takriban shilingi trilioni 7.062. Ukiachilia mbali mradi huu, Serikali inatekeleza miradi mingine mingi ya maendeleo, kama nilivyoitaja hapo awali, ikiwemo ujenzi wa barabara. Hapa Dodoma tumepanga kujenga barabara ya mzunguko yenye urefu wa kilometa 100.
Tunafanya upanuzi wa bandari zetu kubwa za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga. Tumepanga kununua meli mpya kubwa kwenye Ziwa Victoria. Tunafanya ukarabati wa viwanja vya ndege takriban 11 nchini. Tumenunua ndege mpya sita. Tunajiandaa kuanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa umeme wa Stiglier’s Gorge pamoja na kutekeleza Awamu ya Tatu ya Kupeleka Umeme Vijijini, ambapo tunataka ifikapo mwishoni mwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 tuwe tumefikisha huduma hiyo kwenye vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na huduma ya umeme, takriban 7800 nchi nzima, vikiwemo vilivyopo katika Mkoa huu wa Dodoma. Tunatekeleza miradi mikubwa ya maji katika mikoa yote nchini, ikiwemo hapa Dodoma.
Sambamba na hayo, kama mnavyofahamu, hivi sasa tunatoa elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi Sekondari, ambapo kila mwezi tunatenga takriban shilingi bilioni 23.8. Tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo ya vyuo vikuu hadi kufikia takriban 123,000, ambapo katika Mwaka huu wa Fedha tumetenga shilingi bilioni 427.544. Aidha, tunaendelea kuboresha huduma za afya, hususan kwa kujenga miundombinu. Kwenye kila Mkoa tunapeleka fedha kwa kujenga au kukarabati miundombinu. Ninyi wana-Dodoma ni mashahidi. Tunafanya upanuzi wa Hospitali yenu ya Mkoa na kukarabati vituo vitano vya afya, vikiwemo vya Makole na Bahi. Tumeongeza pia bajeti ya kununulia dawa na vifaa tiba, ikiwemo katika Hospitali ya Rufaa ya Benjamin Mkapa iliyopo Chuo Kikuu cha Dodoma, ambayo Serikali imeipatia vifaa vya kisasa kama MRI, CT-Scan pamoja na vifaa vya kupandikiza figo na kufanya upasuaji bila kuchana.
Miradi na shughuli hizi zote zinahitaji fedha. Tena nyingi. Na Serikali inapata fedha kupitia kodi. Hivyo, napenda kutumia fursa hii kuwasihi Watanzania wote kuendelea kulipa kodi. Baadhi ya wafanya biashara wanatoa risiti za thamani ndogo ukilinganisha na gharama halisi za bidhaa. Hivyo, nawasihi wafanya biashara kutoa risiti halali, lakini pia nawahimiza wananchi kudai risiti kila wakati mnaponunua bidhaa au huduma yoyote ile. Lakini, nitumie fursa hii pia kuziomba mamlaka husika, hususan Wizara ya Fedha na Mamlaka ya Kodi nchini (TRA) kutafakari viwango vya kodi zetu nchini. Kwenye baadhi ya maeneo nadhani vipo juu sana na kusababisha kudorora kwa shughuli za biashara na halikadhalika maendeleo ya viwanda. Viwango vya juu vya kodi, ndivyo pia vinawafanya baadhi ya wananchi watafute mbinu za kukwepa kulipa kodi na hivyo kuikosesha Serikali mapato. Hivyo basi, naziomba mamlaka husika kulitafakari kwa kina suala hili la kodi. Mimi naamini, kama tutapunguza utitiri na kuweka viwango vyenye kustahili au kulingana na shughuli na vipato vya Watanzania, sio tu wananchi wengi watahamasika na kuona fahari kulipa kodi, bali pia tutastawisha shughuli za biashara na maendeleo ya viwanda nchini.
Jambo la tatu, napenda kuwahimiza Watanzania wenzangu kuendelea kuilinda na kudumisha amani yetu. Mheshimiwa Waziri Mkuu amelielezea suala hili vizuri. Hivyo basi, itoshe tu kusema kuwa amani ndio msingi wa maendeleo katika Taifa lolote. Bila ya amani, hakuna maendeleo. Tuendelee kuitunza amani yetu tuliyoachiwa na waasisi wetu, wakiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Tusikubali kuchonganishwa na watu wasioitakia mema nchi yetu kwa kisingizio chochote kile. Na napenda kutumia fursa hii kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kulinda amani yetu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jambo la nne na la mwisho, lakini sio kwa umuhimu, ni kwenu watani zangu Wagogo. Fursa sasa zinakuja katika Mkoa wenu. Reli hii inajengwa na itapita kwenye Mkoa wenu. Serikali inahamia Dodoma; ambapo mimi pia natarajia kuhamia mwaka huu. Viwanda vingi navyo vimeanza kujengwa. Mathalan, nafahamu kuwa Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii imepanga kutekeleza miradi kadhaa ya viwanda hapa Dodoma, ikiwa ni pamoja na kufufua Kiwanda cha kusindika nafaka na kukamua mafuta cha National Milling Corporation (NMC), Kiwanda cha kutengeneza matofali na vigae, na Kiwanda cha Kusindika Juisi na Mvinyo wa Zabibu ambacho kitajengwa Chinangali, Chamwino.
Sambamba na hayo, tunatarajia kuanza ujenzi wa Kiwanja kikubwa cha michezo hapa Dodoma mjini kwa ufadhili wa marafiki zetu wa Morocco. Wataalam wetu wanatarajia hivi karibuni kwenda Morocco kupeleka mchoro wa Kiwanja. Tunatarajia pia kuanza ujenzi wa Kiwanja Kikubwa cha Ndege eneo la Msalato ili ndege kubwa ziweze kutua hapa Dodoma. Hizi ni fursa kwenu, hivyo basi, nawasihi mjipange vizuri kuzitumia, hususan katika kupambana na umaskini pamoja na tatizo la ajira.
Mheshimiwa Waziri;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kukushukuru tena Mheshimiwa Waziri kwa kunikaribisha kwenye hafla hii. Aidha, napenda kurudia tena kuwahimiza kuhakikisha Mradi huu unakamilika kwa wakati.
Nawashukuru pia wananchi na viongozi mbalimbali kwa kujitokeza kwa wingi kwenye tukio hili. Nakushukuru pia Mheshimiwa Spika pamoja na Wabunge kwa kupitisha bajeti ya ujenzi wa reli hii. Nawashukuru wana-habari pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kuweka Jiwe la Msingi la Awamu ya Pili ya Mradi wa Reli ya Kisasa kutoka Morogoro hadi Dodoma (Makutopora), ambao utagharimu shilingi trilioni 4.3 ambazo zote zitatolewa na Serikali.
Mungu Ibariki Reli yetu ya Kisasa!
Mungu Wabariki wana-Dodoma!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Feb 09, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA ALIYOINDAA KWA AJILI YA MABALOZI NA VIONGOZI WA TAASI...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA ALIYOINDAA KWA AJILI YA MABALOZI NA VIONGOZI WA TAASISI
ZA KIMATAIFA KUKARIBISHA MWAKA MPYA 2018
IKULU, DAR ES SALAAM, 9 FEBRUARI, 2018
Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje
na Ushirikiano wa Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Brahin Salem Buseif, Balozi wa Saharawi
na Kaimu Kiongozi wa Mabalozi nchini;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi
na Mashirika ya Kimataifa;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Habarini za Jioni. Karibuni sana hapa Ikulu. Nawashukuru, Waheshimiwa Mabalozi, kwa kukubali mwaliko wangu wa kuhudhuria hafla hii, ambayo kwenye utamaduni wa kidiplomasia, imezoeleka duniani kote. Tanzania na sisi tumekuwa tukifanya hafla hii kila mwaka; na bila shaka, tutaendelea kuifanya. Hata hivyo, napenda kuwaarifu kwamba, mwaka huu, huenda utakuwa wa mwisho kwa hafla hii kufanyika hapa Dar es Salaam. Tunatarajia, kuanzia mwakani, kufanyia Dodoma, Makao Makuu ya nchi yetu.
Hivyo basi, niwaombe, Waheshimiwa Mabalozi, mwakani, mjiandae kuja Dodoma, ambako viongozi wengi wa Serikali tayari wamehamia, ikiwa ni pamoja na Mawaziri, Waziri Mkuu na Makamu wa Rais. Mimi pia natarajia kuhamia mwaka huu. Hivyo, nawasihi na nyie muanze kufikiria kuhamia Dodoma. Dodoma ni pazuri na ni katikati mwa nchi yetu. Naupongeza Umoja wa Mataifa na mashirika yake kwa kuanza mchakato wa kuhamia Dodoma, ambapo mwezi Desemba 2017, walifungua Ofisi za Muda. Hongereni sana Umoja wa Mataifa; na napenda kutumia fursa hii kuwaarifu kuwa Serikali imeamua kugawa bure viwanja vyenye ukubwa wa Ekari 5.5 kwa kila Ofisi ya Kibalozi iliyopo nchini. Hivyo, nawahimiza kuchangamkia fursa hiyo.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Hivi sasa ni takriban mwezi mmoja na siku kadhaa umepita tangu kuanza kwa Mwaka Mpya 2018. Kwa utamaduni wetu sisi Watanzania, mwaka ukianza, hadi mwezi Machi, huwa tunaendelea kupeana heri ya mwaka mpya. Hivyo basi, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, napenda kutumia fursa hii, kuwawatakia heri ya Mwaka Mpya wa 2018, ninyi Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa, familia pamoja na watumishi wenu. Aidha, naomba mnifikishie salamu zangu za Heri ya Mwaka Mpya 2018 kwa Wakuu wa Nchi pamoja na Taasisi na Mashirika, ambayo mnayawakilisha vizuri hapa nchini.
Nafahamu kuwa, kwa baadhi yenu, hii ni mara ya kwanza kushiriki katika hafla hii hapa Tanzania. Napenda nirudie tena kuwakaribisha sana nchini kwetu. Tanzania ni nchi nzuri; watu wake ni wakarimu na ina vivutio vingi vya utalii. Nina uhakika, mmeshasikia kuhusu Visiwa vya Zanzibar, Mlima Kilimanjaro, pamoja na Mbuga za Serengeti na Ngorongoro. Lakini, mbali na vivutio hivyo vinavyotambulika ulimwenguni kote, tunavyo vivutio vingine vingi vizuri. Mti mrefu zaidi Barani Afrika upo hapa nchini, tena karibu kabisa na Mlima Kilimanjaro. Aidha, tuna Hifadhi ya Taifa ya Ruaha ambayo ni kubwa zaidi nchini na inasifika kwa kuwa na tembo wengi. Vilevile, tunayo Hifadhi ya Taifa ya Kitulo ambayo inasifika kwa kuwa na aina nyingi za maua ya ndwele ya asili ambayo hayapatikani sehemu nyingine yoyote duniani; na halikadhalika Maporomoko ya Mto Kalambo, kule Rukwa, ambayo ni ya pili kwa kuwa na kina kirefu Barani Afrika, baada ya yale ya Tugale yaliyopo nchini Afrika Kusini. Hivyo basi, nawahimiza, mkipata muda, tembeleeni vivutio hivyo ili mjionee uzuri wa Tanzania. Tunawaomba pia muwahamasishe wananchi wenu kuja kutembelea vivutio vyetu.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, duniani kote, katika kipindi cha mwanzo wa mwaka kama hiki; ni jambo la kawaida kufanya tafakari ya masuala ya mwaka uliopita na kupanga mikakati ya mwaka mpya. Kwetu sisi Tanzania, Mwaka 2017, ulikuwa wenye mafanikio makubwa katika ngazi ya kitaifa na kimataifa; japo changamoto nazo zilikuwepo.
Mathalan, katika ngazi ya kitaifa, mwaka jana, tuliendelea kutekeleza Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka mitano wa 2016/17 – 2020/2021, unaolenga kuifanya nchi yetu kuwa ya uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025, kama ambavyo Dira ya Taifa ya Maendeleo inavyoelekeza. Na katika kutekeleza Mpango wetu, tuliweka pia mkazo katika kushughulikia matatizo yaliyokuwa yakitukwamisha katika kupiga hatua za kimaendeleo. Kama mjuavyo “Ukitaka kupata maendeleo, badala ya kuongeza tu bidii, jambo la kwanza unatakiwa kushughulikia au kurekebisha mambo yanayokukwamisha kupata maendeleo”. Mathalan, ukitaka kujitosheleza kifedha, njia nzuri sio kuongeza bidii ya kutafuta fedha, bali unatakiwa kwanza kudhibiti matumizi ya kile kidogo unachokipata. Na vilevile, ukitaka kupungua unene, njia nzuri sio kuanza kufanya mazoezi, bali ni kuacha kufanya mambo yanayosababisha uwe mnene.
Kwa kuzingatia hilo, mwaka 2017, tuliendelea kushughulikia matatizo yenye kuikwamisha nchi yetu kupata maendeleo. Tulizidisha mapambano dhidi ya rushwa, wizi na uporaji wa rasilimali zetu. Kama mnavyofahamu, miongoni mwa mambo yanayozikwamisha nchi za Afrika kupata maendeleo ya haraka kiuchumi, Tanzania ikiwemo, ni vitendo vya rushwa, ukwepaji kodi na uporaji wa rasilimali. Ripoti ya Jopo la Umoja wa Afrika lililoongozwa na Rais wa Zamani wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki, iliyotolewa mwaka 2015, ilibainisha kuwa katika kipindi cha miongo mitatu iliyopita nchi za Afrika, Tanzania ikiwemo, zimepoteza takriban Dola za Marekani trilioni 1.8, wastani wa Dola za Marekani bilioni 50 – 80 kwa mwaka. Aidha, Ripoti hiyo iliendelea kueleza kuwa, hivi sasa, nchi za Afrika, kila mwaka, zinapoteza wastani wa Dola za Marekani bilioni 150 kutokana na rushwa, wizi, ukwepaji kodi na uporaji wa rasilimali.
Hivyo basi, katika mwaka 2017, tumeendelea kuchukua hatua za kudhibiti vitendo hivyo. Tumepitisha sheria ya kulinda na kusimamia rasilimali zetu ili ziweze kuinufaisha nchi yetu. Ni wazi kuwa hatua hii huenda haikuwafurahisha baadhi ya watu, lakini ilitulazimu tuichukue ili kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa nchi yetu. Sambamba na hilo, tumeendelea kuziba mianya ya ukwepaji kodi, na hivyo kuweza kuongeza ukusanyaji mapato. Mathalan, katika kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba 2017, tulifanikiwa kukusanya kodi kiasi cha shilingi trilioni 7.87, sawa ongezeko la asilimia 8.45 ukilinganisha na mapato ya kipindi kama hicho mwaka 2016. Lakini, kubwa zaidi ni kwamba, mwezi Desemba 2017, mapato ya kodi yaliyokusanywa ni shilingi trilioni 1.66. Kiwango hiki ni kikubwa zaidi kuwahi kukusanywa hapa nchini.
Kutokana na hatua tunazozichukua, uchumi wetu umeendelea kuimarika. Katika nusu ya kwanza ya mwaka 2017, uchumi ulikua kwa asilimia 6.8, na hivyo kuifanya nchi yetu kuongoza katika Ukanda wetu wa Afrika Mashariki, lakini pia kuwa miongoni mwa nchi tano ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kubwa Barani Afrika. Tulifanikiwa pia kudhibiti mfumko wa bei, ambapo mwezi Desemba 2017 ulifikia asilimia 4. Kwa ujumla, wastani wa mfumko wa bei nchini mwaka jana ulikuwa chini ya asilimia 5.5, kiwango ambacho ni cha chini ukilinganisha na nchi nyingi za Afrika. Akiba ya fedha za kigeni nayo imeongezeka; na tumeweza kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na kuboresha huduma za jamii, hususan zile zenye kuwagusa wananchi wengi kama vile afya, elimu na maji. Na hii, bila shaka, ndio moja ya sababu iliyoifanya nchi yetu itajwe kuongoza kwa uchumi shirikishi kwa nchi za Kusini mwa Bara la Afrika.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Mbali na kushughulikia matatizo ya rushwa, wizi, ukwepaji kodi, n.k.; tumeendelea kushughulikia changamoto nyingine zilizokuwa zikikwamisha maendeleo ya nchi yetu. Kama mnavyofahamu, ukiachilia mbali vitendo vya rushwa pamoja na wizi na ubadhirifu wa rasilimali, changamoto nyingine kubwa inayokabili Bara la Afrika, ni tatizo la kukosekana kwa miundombinu imara ya usafiri na nishati ya umeme. Mathalan, kwa mujibu wa Ripoti ya Maendeleo ya Afrika (Africa Progress Report) ya mwaka 2015, watu zaidi ya milioni 600, ambao ni takriban nusu ya watu wote wa Bara la Afrika, hawatumii umeme. Takwimu pia zinaonesha kuwa nchi za Kusini mwa Bara la Afrika, zote kwa pamoja, ukiondoa Afrika Kusini, zinatumia umeme kidogo ukilinganisha na nchi ya Hispania. Aidha, matatizo haya ya umeme yanachangia kushusha kwa asilimia 2.4 Pato la Afrika. Lakini, ukiachilia mbali umeme, gharama za usafirishaji Barani Afrika ni kubwa ukilinganisha na Mabara mengine kutokana na ama kukosekana au udhaifu wa miundombinu ya usafiri. Mambo haya yote kwa pamoja, ndio yanasababisha mchango wa Bara la Afrika kibiashara na uwekezaji duniani kuwa mdogo sana.
Kwa kutambua hilo, tumeendelea kuchukua hatua za kuimarisha miundombinu ya usafiri pamoja na upatikanaji wa umeme. Sehemu kubwa ya nchi hivi sasa imeunganishwa kwa barabara; na nyingine zinaendelea kujengwa. Aidha, mwaka 2017 tumeanza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge) kutoka hapa Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Mwanza na Kigoma. Reli hii baadaye itaungana na reli za kwenda nchi za Burundi na Rwanda. Ujenzi wa kipande cha Dar es Salaam hadi Dodoma chenye urefu wa kilometa 712 tayari umeanza na utagharimu kiasi cha shilingi trilioni 7.062, zote zitatolewa na Serikali yetu. Aidha, hivi karibuni, wakati wa ziara ya Rais Kagame wa Rwanda, tumekubaliana kuanza ujenzi wa kipande cha kutoka Isaka kwenda Kigali nchini Rwanda. Sambamba na hayo, tunaendelea na upanuzi wa viwanja vya ndege vikubwa vya Dar es Salaam, Zanzibar, Kilimanjaro pamoja na vingine takriban 11 katika mikoa mbalimbali lengo likiwa kukuza sekta yetu ya utalii. Vilevile, tunafanya upanuzi mkubwa na kuboresha utendaji wa bandari zetu kuu za Dar es Salaam na Mtwara kwa gharama ya takriban shilingi trilioni 1.1. Tunatekeleza miradi hii kwa vile takriban asilimia 90 ya shehena ya mizigo inayokuja hapa nchini upitia kwenye bandari hizi. Aidha, Bandari ya Dar es Salaam inategemewa na nchi nyingine majirani. Tunaiboresha pia Bandari ya Tanga, hususan baada ya nchi yetu pamoja na Uganda kuingia makubaliano ya kutekeleza mradi mkubwa wa Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga. Ujenzi wa Bomba hilo lenye urefu wa kilometa 1,415 utaanza mwaka huu, ambapo, kama mtakavyokumbuka, mwaka jana, mimi na Rais Museveni wa Uganda tuliuwekea jiwe la msingi.
Kuhusu umeme, tunaendelea na utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuzalisha, kusafirisha na kusambaza umeme. Mwaka 2017, tumeanza Awamu ya Tatu ya kupeleka Umeme Vijiji, ambapo tunatarajia kufikisha umeme kwenye vijiji 7,873. Lengo letu ni kwamba, ifikapo Mwaka wa Fedha 2020/2021, vijiji vyote nchini viwe vimefikiwa na miudombinu ya umeme. Tunatekeleza pia miradi mikubwa ya kuzalisha umeme, hususan kwa kutumia gesi yetu asilia. Aidha, mwaka huu, tunatarajia kuanza utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa kutumia maji wa Stiglier’s Gorge, ambao utazalisha Megawati 2,100. Tunataka ikifika mwaka 2020, nchi yetu angalau iwe Megawati 5,000 kutoka Megawati 1,460 za sasa. Nafahamu kumekuwa na maneno maneno kuhusu mradi wetu wa Stiglier’s Gorge; ukihusishwa na uharibifu wa mazingira katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Ukweli ni kwamba, hakutakuwa na uharibifu wowote. Tumefanya tathmini ya kina ya mazingira, na tumeweka mikakati ya kudhibiti uharibifu. Zaidi ya hapo, mradi huu, utatekelezwa katika eneo dogo sana. Ni chini ya asilimia 4 ya eneo zima la Hifadhi ya Ruaha. Hivyo, hakuna uwezekano wowote wa kuathiri mazingira ya eneo hilo.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Kuhusu azma yetu ya kujenga viwanda, ninyi Waheshimiwa Mabalozi mnafahamu vizuri kuwa hakuna nchi duniani kote imewahi kupata maendeleo ya kiuchumi bila kutegemea viwanda. Mnafahamu pia kuwa, sekta ya viwanda ni muhimu katika kupiga vita umaskini na tatizo la ajira. Hivyo basi, mwaka 2017 tumeendelea na jitihada za kujenga uchumi wa viwanda nchini. Na napenda kuwaarifu kwamba, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, takriban viwanda 3,500 vimejengwa. Na vingine vingi vinaendelea kujengwa. Naishukuru sekta binafsi ya hapa nchini na kutoka nje kwa namna ilivyoitikia vizuri wito wa Serikali yetu wa kujenga viwanda. Nafahamu kuwa wapo baadhi ya watu ambao wanaeneza uzushi kuwa sisi hatupendi sekta binafsi. Hiyo sio kweli hata kidogo. Tunaipenda sekta binafsi na tunathamini na kutambua mchango wao. Na tunafahamu vizuri kuwa katika dunia ya sasa sekta binafsi ni mhimili muhimu katika kujenga uchumi.
Kwa sababu hiyo, tutaendelea kushirikiana na sekta binafsi ya hapa nchini na ile ya nje. Tutaendelea pia kushughulikia vikwazo mbalimbali vinavyoikabili sekta hii, ikiwa ni pamoja na kurekebisha sera na sheria zetu pale inapobidi; kuongeza vivutio vya uwekezaji na biashara; kushughulikia matatizo ya urasimu, rushwa, utitiri wa kodi, n.k. Hivyo basi, nahimiza sekta binafsi kuendelea kuwekeza hapa nchini. Na niwaombe Waheshimiwa Mabalozi, nanyi wahimizeni wafanyabishara kutoka nchi zenu kuja kuwekeza hapa nchini. Nchi yetu ina fursa nyingi za uwekezaji. Ukiachilia mbali sekta ya viwanda, tuna fursa kwenye sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, utalii, ujenzi wa miundombinu, huduma, n.k. Aidha, nchi yetu ina soko kubwa. Tunapakana na nchi takriban 8, lakini pia sisi ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na halikadhalika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, ambazo kwa pamoja zina idadi ya watu wapatao milioni 500. Hili ni soko kubwa kwa mwekezaji yeyote.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Kimataifa, mwaka 2017, nchi yetu imeendelea kushiriki kikamilifu kwenye masuala mbalimbali katika ngazi ya Kikanda, Bara na duniani kwa ujumla. Kama mjuavyo, msingi mkuu wa Sera yetu ya Mambo ya Nje ni kuimarisha ujirani mwema, ushirikiano wa kikanda na kimataifa. Hivyo, tumeendelea kutekeleza Sera hiyo. Mimi pamoja na viongozi wenzangu, tumefanya ziara na kushiriki kwenye mikutano mbalimbali ya kimataifa. Binafsi, mwaka jana, nilihudhuria Mkutano wa Umoja wa Afrika na kutembelea nchi ya Uganda. Aidha, tulipata bahati ya kutembelewa na viongozi kadhaa wa nchi na taasisi za kimataifa, ikiwa ni pamoja na Waziri Mkuu wa Ethiopia, Hailemariam Dessalegn; Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma; Rais wa Uganda, Yoweri Museveni; Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, Kanda ya Afrika, Dkt. Makhtar Diop; Rais wa Benki ya Dunia, Dkt. Jim Yong Kim; na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Mhe. Tao Zang; pamoja na viongozi wengine wengi. Wakati wa ziara hizo, tuliweza kufikia makubaliano mbalimbali yenye lengo la kuimarisha ushirikiano, hususan kwenye nyanja za kiuchumi.
Mwaka jana pia, tumeendelea kushirikiana na nchi pamoja na taasisi nyingine za kimataifa katika kushughulikia changamoto mbalimbali zinazokabili Kanda, Bara na dunia yetu kwa ujumla. Na moja ya changamoto hizo ni suala la migogoro. Kama mnavyofahamu, tangu imepata uhuru, mwaka 1961, nchi yetu imekuwa mstari wa mbele katika kutafuta amani Barani Afrika na duniani. Tumeshiriki na tunaendelea kushiriki katika harakati za usuluhishi wa migogoro ya Burundi, DRC, n.k. Tunafarijika kuona kuwa amani nchini Burundi inaendelea kuimarika; na tunaendelea kuwahimiza wahusika kwenye migogoro nchini DRC, Sudan Kusini, n.k., kumaliza tofauti walizonazo ili kuweza kurejesha amani kwenye nchi zao.
Mbali na ushiriki wetu katika usuluhishi wa migogoro, nchi yetu, hivi sasa, ina vikosi kwenye misheni za kulinda amani nchini DRC, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Lebanon, Sudan na Sudan Kusini. Nitumie fursa hii, kuzishukuru nchi na taasisi za kimataifa zilizotutumia salamu za rambirambi na pole kufuatia tukio lililotokea tarehe 8 Desemba 2017 la kuuawa kwa askari wetu 15 na wengine 43 kujeruhiwa, wakati wakiwa katika jukumu la kulinda amani nchini DRC. Tukio hili, kwa hakika, liliacha majonzi na simanzi kubwa kwa Watanzania. Hata hivyo, napenda niseme kuwa, kama Taifa, halijatukatisha tamaa wala kutuyumbisha. Tutaendelea kushiriki katika harakati za kutafuta amani mahali popote duniani, na tutaendelea kushiriki kwenye misheni za kulinda amani. Tunaushukuru Umoja wa Mataifa kwa kuunda Timu kuchunguza chanzo cha tukio la tarehe 8 Desemba, 2017. Tunaihimiza Timu iliyoundwa kukamilisha mapema uchunguzi wake, ili chanzo kijulikane, wahusika wafahamike na hatimaye sheria ifuate mkondo wake.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Katika mwaka huu wa 2018, Tanzania itaendelea kutekeleza Mpango wake wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Tutazidisha mapambano dhidi ya rushwa na ubadhirifu. Tutaendelea kuimarisha miundombinu ya kiuchumi, hususan ya usafiri na nishati ya umeme. Tutaboresha huduma mbalimbali za kijamii, hususan elimu, afya a maji.
Sambamba na hayo, tutaendelea kushiriki kwenye masuala mbalimbali ya kimataifa. Tutakuwa wanachama waaminifu wa taasisi za Kikanda, katika Bara na kimataifa, ambazo sisi ni wanachama. Tutaendelea kushiriki kwenye usuluhishi wa migogoro; na vikosi vyetu vitandelea kushiriki kwenye misheni za kulinda amani. Vilevile, tutaendelea kutekeleza mipango na malengo mbalimbali ya kikanda, kibara na kidunia, ikiwemo Ajenda ya Umoja wa Afrika ya 2063 na Ajenda ya Umoja wa Mataifa ya Malengo Endelevu ya 2030. Na moja ya malengo ya dunia tuliyopanga kutekeleza, ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2030 tuwe tumezuia maambukizi mapya ya Virusi Vya Ukimwi (VVU). Na katika kufikia azma hii, tumeanzisha Mfuko wa Udhamini wa Ukimwi, ambapo tumelenga kukusanya kiasi cha shilingi trilioni 6 katika kipindi cha miaka mitano ijayo. Hivyo basi, tunawaomba mtuunge mkono.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Nafahamu, katika hafla kama hii, hotuba huwa haziwi ndefu. Lakini leo, nimeeleza mengi. Nimefanya hivyo, kwa kuwa, kama nilivyosema awali, hii huenda itakuwa mara ya mwisho kwa sherehe hizi kufanyika hapa Dar es Salaam. Mwakani ni Dodoma. Na kwa sababu hiyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba mniruhusu nieleze masuala matatu ya mwisho.
Suala la kwanza; muda mfupi uliopita, nimeeleza kuwa Tanzania itaendelea kushiriki kwenye misheni za kulinda amani. Na napenda kusisitiza tena kuwa tutaendelea kushiriki kwenye misheni hizo. Hata hivyo, wakati nikisisitiza hilo, napenda kueleza masikitiko yetu kuhusu uamuzi wa Umoja wa Mataifa kuanza kutekeleza sera ya kupunguza gharama kwenye misheni za kulinda amani. Ni kweli, uendeshaji wa misheni za kulinda amani ni gharama kubwa. Lakini, ni ukweli pia usiopingika kuwa, hakuna gharama inayozidi uhai wa watu na umuhimu wa amani. Tanzania tunauona uamuzi huu wa kupunguza gharama utadhoofisha jitihada za kutafuta amani kwenye maeneo yenye migogoro; na kuhatarisha maisha ya walinda amani pamoja na raia wasio na hatia wanaoishi kwenye maeneo yenye migogoro. Hivyo basi, tunauomba Umoja wa Mataifa pamoja na Nchi Tano Wanachama wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa kutafakari upya uamuzi huo.
Suala la pili, ni kuhusu uamuzi wetu wa hivi karibuni wa kujitoa kwenye Mpango wa Majaribio wa Kutafuta Suluhu ya Kudumu ya Tatizo la Wakimbizi (Comprehensive Refugee Response Framework – CRRF). Kwanza kabisa, napenda kueleza kuwa, nchi yetu, tangu imepata Uhuru mwaka 1961, imekuwa ni miongoni mwa nchi zenye kupokea wakimbizi wengi. Mpaka sasa tunaendelea kuwapokea; na bila shaka, tutaendelea kuwapokea; lakini wale tu wenye kustahili na kwa kuzingatia sheria za kimataifa. Nchi yetu pia imeweka historia duniani kwa kuwa ya kwanza kutoa uraia kwa wakimbizi wapatao 150,000 kwa wakati mmoja. Hakuna nchi imewahi kufanya hivyo. Hata hivyo, kutokana na sababu za usalama, tumelazimika kujitoa kwenye Mpango wa CRRF, ambao pamoja na masuala mengine, unaelekeza kutolewa kwa ardhi kwa ajili ya wakimbizi, kuwaruhusu kutembea mahali popote na kutoa vibali vya ajira. Tumeamua kujitoa kwa sababu tunadhani kuwa, katika kipindi hiki cha sasa ambacho dunia inakabiliwa na changamoto za usalama, ikiwemo ugaidi, kushamiri kwa biashara ya binadamu na makosa mengine ya kimataifa, utekelezaji wa Mpango huu unaweza kuleta madhara makubwa ya kiusalama kwa nchi yetu. Lakini, mbali na hilo, tumesita kuendelea na Mpango huu kutokana na uzoefu tulioupata wakati tulipotoa uraia kwa wakimbizi 150,000. Wakati tunatoa uraia, jumuiya ya kimataifa iliahidi ingetoa fedha za kuwapatia makazi na masuala mengine muhimu. Lakini, mpaka sasa, hakuna fedha iliyotolewa; na badala yake tumeanza kushawishiwa kukopa fedha za kuwahudumia wakimbizi. Hali hii imetukatisha tamaa; na tunaona itakuwa ni kuibebesha mzigo mkubwa Serikali yetu. Hivyo basi, tunaiomba jumuiya ya kimataifa ituelewe.
Suala la tatu na la mwisho ni kuhusu taarifa za kukamatwa kwa meli zenye kupeperusha bendera ya Tanzania, ambazo zimejihusisha kwenye matukio ya uhalifu. Taarifa hizi kwa hakika zimetusikitisha sana sisi kama Taifa, kwa sababu zinachafua jina na sifa nzuri ya nchi yetu. Hata hivyo, ningependa kufafanua kuwa, kimsingi, meli hizo si za kwetu; zimesajiliwa tu hapa Tanzania. Kama mnavyofahamu, usajili wa meli za nje ni jambo la kawaida na linafanywa na nchi mbalimbali duniani. Hata hivyo, kutokana na matatizo yaliyojitokeza, Serikali imeamua kuchukua hatua. Tumesitisha usajili wa meli zote 470 zilizosajiliwa hapa nchini zenye kupeperusha bendera yetu, na tumeanza kufanya uchunguzi wa kina kuthibitisha uhalali wa shughuli zao. Zile zitakazobainika kukiuka sheria na taratibu, tutazifutia usajili. Sambamba na hilo, tumesitisha usajili wa meli mpya kutoka nje mpaka pale itakapotangazwa tena. Tumechukua hatua hizo, ili nchi yetu isitumike kuwa kichaka cha kujificha wahalifu.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Mashirika na Taasisi za Kamataifa;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu, kwa kurudia tena kuwashukuru kwa kuhudhuria hafla hii. Aidha, nawashukuru kwa namna ambavyo nchi zenu na mashirika mnayowakilisha yanavyoshirikiana vizuri na nchi yetu katika nyanja mbalimbali: kiuchumi, kisiasa, kijamii, kiulinzi na usalama, n.k. Mchango wenu ni mkubwa sana. Bila ninyi, huenda mambo mengi tuliyotekeleza mwaka jana, yasingewezekana. Hivyo basi, tunawashukuru sana; na kupitia kwenu, tunaendelea kuziomba nchi na taasisi mnazoziwakilisha ziendelee kutuunga mkono. Kwa upande wetu, tutazidi kuimarisha uhusiano wetu na nchi, mashirika na taasisi zenu.
Baada ya kusema hayo, napenda kurudia tena kuwatakia Heri ya Mwaka Mpya 2018. Uwe mwaka wa Amani na Mafanikio.
“Ahsanteni kwa kunisikiliza”

- Feb 01, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MGENI RASMI, MAADHIMISHO YA SIKU YA SHERIA, DAR ES SALAAM, TAREHE 1 FE...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
MGENI RASMI, MAADHIMISHO YA SIKU
YA SHERIA, DAR ES SALAAM,
TAREHE 1 FEBRUARI, 2018
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu
wa Tanzania;
Mhe. Tulia Akson Mwansasu (Mb), Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi (Mb),
Waziri wa Sheria na Katiba;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Waziri mliopo;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi,
Katibu Mkuu Kiongozi;
Mhe. Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa
wa Dar es Salaam;
Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu mliopo;
Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
Waheshimiwa Majaji Wakuu Wastaafu;
Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufaa,
Mheshimiwa Jaji Kiongozi;
Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu;
Mheshimiwa Msajili Mkuu na Mtendaji Mkuu wa Mahakama;
Naibu Rais wa Chama cha Wanasheria Tanzania Bara;
Mkurugenzi wa Mashtaka;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Waheshimiwa Wageni wetu kutoka Guatemala;
Waheshimiwa Wasajili, Mahakimu na Mawakili;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Awali ya yote, napenda na mimi niungane na walionitangulia katika kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa leo. Tulikutana mara ya mwisho kwenye sherehe kama hizi, mwaka jana 2017; nakumbuka ilikuwa tarehe 2 Februari. Naamini kuna wenzetu tulikuwa nao mwaka jana, lakini leo hatunao. Hatuna budi kuwakumbuka wote waliotutoka. Hivi karibuni, tumeondokewa na mwanafamilia mwenzetu, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa, Mheshimiwa Robert Kisanga. Wakati wa uhai wake, Jaji Kisanga alitoa mchango mkubwa kwa Mahakama na Taifa kwa ujumla. Hivyo basi, tunawaombea wote waliotutoka wapumzike mahali pema peponi. Amina.
Napenda pia kutumia fursa hii kuushukuru uongozi wa Mahakama chini ya Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania, kwa kunialika kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini. Hii ni mara yangu ya tatu kushiriki kwenye Siku ya Sheria tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa nchi yetu. Nimefurahi kuona kuwa miongoni mwetu leo, tunaye pia Naibu Spika wa Bunge, Mheshimiwa Tulia Akson. Huu ni uthibitisho tosha kuwa mihimili yetu mitatu ya Dola ina mahusiano mazuri na inafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa. Sisi sote ni kitu kimoja. Lengo letu ni moja: kuleta maendeleo kwa nchi yetu. Lakini zaidi ya hapo, kama Mheshimiwa Jaji Mkuu alivyosema, sisi sote ni wadau muhimu wa Siku hii ya Sheria. Bunge ndilo lenye kutunga sheria; Mahakama inazitafsiri; na sisi Serikali (Utawala) ndio wenye jukumu la kusimamia utekelezaji wake. Hivyo basi, nakushukuru tena Mheshimiwa Jaji Mkuu kwa kutualika kushiriki katika siku hii muhimu.
Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana:
Ni wazi kuwa Maadhimisho ya Siku ya Sheria ni muhimu sana. Ni muhimu, kwanza kabisa, kwa sababu ya umuhimu wenyewe wa sheria. Hivi punde tu Mheshimiwa Jaji Mkuu ameeleza kuwa sheria ni muhimu katika kudumisha amani na pia kuleta maendeleo kwa wananchi na nchi kwa ujumla. Lakini zaidi ya hapo, sheria ni muhimu katika kutoa haki. Na kama mjuavyo, haki ni hitaji kubwa katika jamii. Nikinukuu usemi mmoja wa Kiingereza unasema, “Justice is the great interest of man on earth”. Hivyo basi, kwa kuadhimisha Siku hii ya Sheria, maana yake ni kwamba nchi yetu inatambua umuhimu wa sheria katika kusimamia haki, kudumisha amani na kuleta maendeleo katika nchi.
Lakini ukiachilia hilo la umuhimu wa sheria, Maadhimisho haya ya Siku ya Sheria ni muhimu kwa vile yanatoa fursa kwa vyombo vinavyohusika na masuala ya sheria na utoaji haki (yaani Mahakama, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jeshi la Polisi, Magereza, TAKUKURU, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Mawakili, n.k.) kukutana na kufanya tafakuri ya masuala mbalimbali, wanajadili mapungufu na mafanikio waliyopata katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita; na kupanga mikakati ya mwaka mpya, ikiwemo kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza pamoja na kuboresha au kuimarisha mafanikio yaliyokwishapatikana.
Napenda kutumia fursa hii kuvipongeza vyombo vyote vinavyohusika na masuala ya sheria na haki nchini kwa kazi kubwa na nzuri ya kusimamia sheria na kutoa haki kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita. Na kwa namna ya pekee kabisa, naipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri iliyofanya ya kutoa haki. Kama sote tujuavyo, Mahakama ndio chombo pekee cha kutoa haki nchini. Mheshimiwa Jaji Mkuu ameeleza kuwa katika mwaka uliopita Mahakama iliweza kupunguza kwa kiwango kikubwa mlundikano wa kesi au mashauri, hususan katika Mahakama za Mwanzo, Wilaya na Hakimu Mkazi. Mathalan, Mahakama za Mwanzo hadi kufikia mwezi Desemba mwaka jana zilibakiwa na mashauri 14 yaliyozidi umri wa miezi 6 (kipindi ambacho kinatafsiriwa na mahakama kuwa mlundikano). Na kwa kuzingatia kuwa zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yote ya mahakama, yanafunguliwa kwenye ngazi ya Mahakama za Mwanzo, ni wazi kuwa haya ni mafanikio makubwa. Lakini nafahamu, bila ya kupata ushirikiano kutoka vyombo vingine, Mahakama peke yake isingeweza kupata mafanikio haya. Hivyo basi, navipongeza vyombo vilivyofanikisha kupatikana kwa mafanikio haya. Hongereni sana.
Mheshimiwa Jaji Mkuu pamoja na Viongozi
wa Vyombo vingine vya kusimamia sheria na haki:
Licha ya mafanikio mliyopata mwaka jana pamoja na pongezi nilizozitoa kwenu hivi punde, jambo moja lipo dhahiri: Usimamizi wa sheria na mfumo wa utoaji wa haki nchini bado unakabiliwa na matatizo mengi. Na moja ya matatizo hayo ni kupungua kwa uadilifu kwa watumishi wachache wa vyombo vyetu vyenye dhamana ya kusimamia sheria na kutoa haki. Nasema ni wachache kwa vile nafahamu kuwa watumishi wengi wa vyombo hivi ni wazuri na waadilifu. Lakini, hawa wachache, hatupaswi kuwaacha kwa kuwa matendo yao yanavichafua sana vyombo vyetu. Hawa ndio wanaowadai rushwa na kuwabambikiza kesi wananchi; wanachelewesha upelelezi na kuharibu ushahidi; na pia ndio wenye tabia ya kutoa hukumu za upendeleo au kuchelewa kuandika hukumu. Naipongeza Tume ya Utumishi wa Mahakama, ambayo ipo chini ya Jaji Mkuu, kwa kuwachukulia hatua za kinidhamu, ikiwemo kuwafukuza au kuwastaafisha, watumishi wa mahakama wapatao 112 ambao walibainika kuhusika na vitendo vya rushwa na kukiuka maadili.
Nafahamu, miongoni mwa waliostaafishwa wapo Mahakimu 27, wakiwemo 14 ambao wamefukuzwa kazi. Awali, Mahakimu hawa wote walishinda kesi mahakamani, lakini baadaye Tume iliamua kuwastaafisha. Mbali na Mahakimu, watumishi wengine 67 wa Mahakama nao walifukuzwa kazi. Hongera sana Jaji Mkuu. Tume imetekeleza kwa vitendo kauli aliyowahi kutoa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, nanukuu “kazi ya ujaji au uhakimu inahitaji uadilifu wa hali ya juu. Kama Jaji au Hakimu sio mwaminifu au mwadilifu kazi hiyo haimfai, akatafute kazi nyingine”, mwisho wa kunukuu. Narudia tena kukupongeza Mheshimiwa Jaji Mkuu na nakusihi kuendelea kuwachukulia hatua kali watumishi wa Mahakama wasio waadilifu, ikiwemo kulifuatilia kwa karibu suala la baadhi ya watumishi wa Mahakama kuomba vibali vya kwenda likizo nje ya nchi kila mwaka. Suala hili halitoi picha nzuri kwa Mahakama. Utafiti uliofanywa na Taasisi isiyo ya Serikali ya TWAWEZA hivi karibuni umebaini kuwa rushwa nchini imepungua kwa asilimia 85 ukilinganisha na miaka 5 iliyopita. Hata hivyo, Jeshi la Polisi na Mahakama bado mnaongoza kwa vitendo vya rushwa. Utafiti huu haupaswi kupuuzwa. Hivyo basi, nakuomba Mheshimiwa Jaji Mkuu kuendelea kuzidisha mapambano dhidi ya rushwa. Aidha, navihimiza vyombo vingine, (Polisi, TAKUKURU, Magereza, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mwendesha Mashtaka, n.k) navyo kuiga mfano ulioanza kuoneshwa na Mahakama katika kupiga vita rushwa pamoja na vitendo vingine vya ukiukwaji wa maadili.
Mbali na suala la uadilifu, tatizo la ucheleweshaji wa kesi bado lipo ama katika kufanya upelelezi, kusikiliza au katika kutoa maamuzi. Jaji Mkuu ameeleza jitihada zinazofanywa na Mahakama kutatua tatizo la mlundikano wa kesi; na nimempongeza. Lakini tatizo bado lipo. Yeye mwenyewe ameeleza kuwa kufikia mwezi Desemba 2017, Mahakama za Wilaya na Hakimu Mkazi, zilikuwa na jumla ya mashauri 2,334 ambayo zina umri zaidi ya mwaka mmoja. Na amekiri pia kuwa kwenye Mahakama Kuu na Mahakama kuna mlundikano mkubwa zaidi. Ni kweli kuwa baadhi ya kesi zinachelewa kwa sababu zinazoelezeka, lakini nyingine hazina sababu za msingi. Unaweza kukuta ushahidi wote upo; lakini utasikia upelelezi bado unaendelea; au kunakuwa na kusuasua kwenye kusikiliza au kutoa maamuzi ya kesi husika. Pale Ikulu huwa napokea malalamiko mengi ya wananchi kuhusu ucheleweshaji wa kesi, kwa vile wanadhani naweza kuingilia kati. Lakini huwa nawajibu sina mamlaka hayo. Sana sana tu huwa nawashauri waendelee kufuatilia mahakamani. Lakini hata ninyi wenyewe mmeona hivi karibuni, baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuanza kuwasikiliza wananchi wenye madai mbalimbali, idadi kubwa ya watu imejitokeza. Hii inadhihirisha kuwa bado tuna matatizo makubwa kwenye mfumo wetu wa utoaji haki. Hivyo basi, niviombe vyombo husika kuliwekea mkakati maalum suala hili la ucheleweshaji wa kesi, ikiwa ni pamoja na kupanga mikakati ya kuwabaini na kuwashughulikia wanaozichelewesha kwa uzembe au kutaka kujipatia rushwa.
Nasema hivyo, kwa sababu ucheleweshaji wa kesi una athari nyingi kuanzia kwa mtu mmoja mmoja, kwenye jamii na nchi kwa ujumla. Ninyi Wanasheria mna msemo wenu “Haki iliyocheleweshwa ni sawa na Haki iliyonyimwa”. Lakini mbali na kunyima haki, ucheleweshaji wa kesi umechangia kuvuruga amani na utulivu kwenye baadhi ya maeneo na kusababisha watu kupoteza maisha au kupata majeraha ya kudumu. Vilevile, kuna athari nyingi za kiuchumi. Mathalan, kwa taarifa nilizonazo ni kwamba, kuna kesi 139 zenye kuhusiana na masuala ya kodi zilizofunguliwa kwenye Baraza la Kodi (Tax Appeals Board) na Baraza la Usuluhishi wa Kodi (Tax Appeals Tribunal). Kesi hizi, ambazo zimefunguliwa kati ya mwaka 2009 hadi 2015, zina thamani ya shilingi bilioni 169.1 na Dola za Marekani milioni 38.2. Endapo kesi hizi zingetolewa uamuzi, huenda baadhi yake Serikali ingeshinda na kupata fedha kwa ajili ya kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo. Lakini, mbali na kuiokosesha Serikali mapato, ucheleweshaji wa kesi umefanya baadhi ya makampuni, zikiwemo benki, kufilisika. Na hii ni moja ya sababu zinazofanya riba za mikopo ya benki zetu kuwa juu. Wenye Benki wana hofu kuwa wakikopesha inawezekana mkopo usirudishwe, na hata aliyeshindwa kurejesha mkopo, akishitakiwa huenda ikachukua muda mrefu hukumu kutolewa. Badala yake, wanaamua kupandisha riba, ili mtu mmoja akishindwa kurejesha mkopo, aweze kufidiwa na mwenzie.
Mheshimiwa Jaji Mkuu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nafahamu kuwa matatizo niliyoeleza sio mageni. Sote tunayafahamu na mara kwa mara tumekuwa tukiyajadili. Mimi mwenyewe niliyazungumza mwaka juzi kwenye Sherehe kama hizi, mwaka jana nikayazungumza tena; na leo nimeyarudia. Nimefanya hivyo kwa makusudi kabisa. Lengo langu nilitaka tukumbushane ili kwa pamoja tuyatafutie majibu yake. Kuna hadithi inayomhusu Mwanasayansi mmoja Maarufu Duniani, Dkt. Albert Einstein. Siku moja alikuwa akisimamia Mtihani wa Fizikia kwenye darasa lake. Mmoja wa wanafunzi akamuuliza: “Dkt. Einstein, mtihani huu mbona kama wa mwaka jana?” Dkt. Einstein akamjibu “Ndio ni kama wa mwaka jana, lakini mwaka huu natarajia kuwa majibu yatakuwa tofauti.” Hivyo basi, na mimi nimeamua kuzungumzia tena mapungufu haya ili tuendelee kuyatafutia ufumbuzi wake, ikiwezekana majibu mapya kulingana na dunia ya sasa.
Na kwa sababu hiyo, nimefurahi sana kusikia kuwa kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria Mwaka huu inasema “Matumizi ya TEHAMA katika Utoaji Haki kwa Wakati na kwa Kuzingatia Maadili”. Kaulimbiu hii ni nzuri sana. Jaji Mkuu, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Makamu Rais wa Chama Cha Wanasheria wameeleza vizuri na kwa kirefu suala la TEHAMA. Lakini, na mimi niseme tu kwa ufupi kwamba, TEHAMA ina nafasi kubwa katika kushughulikia matatizo mengi yanayokabili mfumo wa usimamizi wa sheria na utoaji haki nchini. TEHAMA itaongeza kasi ya utoaji haki (mathalan kupitia video conference); itadhibiti uzembe na vitendo vya ukiukwaji wa maadili kwa watumishi, ikiwemo majalada kupotea na vitendo vya rushwa. Aidha, TEHAMA itapunguza gharama za uendeshaji Mahakama na kuimarisha ukusanyaji wa mapato. Hivyo basi, nawapongeza Mahakama kwa kaulimbiu hii na kwa kuanza kufanya kazi kwa njia ya TEHAMA. Endeleeni hivyo hivyo. Na sisi Serikali tutaendelea kuwaunga mkono.
Mbali na matumizi ya TEHAMA, Mahakama na vyombo vingine havina budi kutekeleza mikakati mingine ya kushughulikia mapungufu yaliyopo kwenye mfumo wetu wa sheria na utoaji haki. Mathalan, mwaka jana (2017), Serikali ilipitisha Sheria kuhusu Msaada wa Kisheria (Legal Aid Act) ili kuwasaidia wananchi kupata msaada wa kisheria na hatimaye kurahisisha shughuli za utoaji haki. Lakini, jambo la kusikitisha ni kwamba, mpaka sasa kanuni za Sheria hiyo bado hazijakamilika. Na ni miezi takriban tisa sasa imepita. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kuagiza vyombo husika, hususan Wizara ya Sheria na Katiba pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kuhakikisha kuwa ndani ya mwezi mmoja ujao, kanuni hizo ziwe tayari zimekamilika.
Sambamba na hayo, ni vizuri kama Mahakama itaendelea kuhimiza utaratibu wa kuwa na mahakama za kuhama hama (mobile courts). Wakati nikiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi nilishuhudia ufanisi wa mahakama za kuhama hama. Endeleeni pia kuhimiza usuluhishi. Usuluhishi utapunguza sio tu mlundikano wa kesi bali pia idadi ya wafungwa kwenye Magereza yetu. Wakati wa Sherehe za Uhuru mwaka jana nilieleza kuwa nchi yetu ilikuwa na takriban wafungwa takriban 38,000. Wafungwa wanaigharimu Serikali fedha nyingi. Mathalan, katika kipindi cha miaka minne iliyopita, Serikali ilitenga kiasi cha takriban shilingi bilioni 100 kwa ajili ya kuwatunza na kuhudumia wafungwa. Mwaka wa Fedha 2014/2015 zilitengwa shilingi bilioni 22.3; Mwaka 2015/2016 shilingi bilioni 21.6; Mwaka 2016/2017 shilingi bilioni 27.3 na Mwaka huu wa Fedha shilingi bilioni 19.8. Hiki ni kiasi kikubwa ambacho kingeweza kutumika katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.
Hivyo basi, nadhani sasa wakati umefika wa kuanza kuweka msisitizo katika adhabu mbadala, hususan kwa makosa madogo madogo. Najua sheria zipo, kinachohitajika ni kuweka utaratibu na mikakati ya kuzisimamia. Sambamba na hilo, Jeshi la Magereza hamna budi kuweka mikakati itakayowezesha kujitegemea kwa kuwatumia vizuri wafungwa. Hii pia itawasaidia wafungwa kuweza kujitegemea pindi wakimaliza vifungo vyao. Hivi majuzi nilitoa msamaha kwa wafungwa; lakini nimesikitika kusikia kuwa baadhi yao tayari wamekamatwa kwa uhalifu. Hii inaonesha kuwa wakiwa jela wafungwa hawapati mafunzo ya kutosha. Hivyo, ipo haja kwa Magereza kuangalia upya mafunzo inayotoa kwa wafungwa. Tunataka mtu akifungwa, wakati akitoka awe amebadilika na kuwa mtu mwema.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Katika hotuba yake, Mheshimiwa Jaji Mkuu ameeleza baadhi ya changamoto zinazoikabili Mahakama. Ametaja uhaba wa vifaa na vitendea kazi, uhaba wa miundombinu, upungufu wa watumishi (Majaji), maslahi, n.k. Serikali inafahamu changamoto hizi. Na bila shaka, mnatambua jitihada tunazozichukua katika kuzishughulikia. Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, Serikali imetoa takriban shilingi bilioni 40 ili kuiwezesha Mahakama kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa miundombinu, ambayo hivi punde Mheshimiwa Jaji Mkuu ameitaja. Ujenzi wa Mahakama Kuu mbili (Kigoma na Mara); za Hakimu Mkazi 5 na za Wilaya 16.
Naipongeza Mahakama kwa kusimamia vizuri miradi hiyo. Aidha, nawapongeza kwa kuanza kutekeleza mpango wa kuhamia Dodoma. Nawaahidi kuwa mtakapokuwa tayari kuanza ujenzi Dodoma, Serikali itawaunga mkono.
Nitumie fursa hii pia kuwashukuru washirika wetu mbalimbali wa maendeleo, ambao tunashirikiana nao katika kuboresha Mahakama zetu. Benki ya Dunia imekuwa ikifadhili miradi mingi ya Mahakama. Nimefurahi kuona Mwakilishi wa Dunia yupo hapa. Tunawashukuru sana. Endeleeni kutuunga mkono, hususan katika masuala haya ya sheria na utoaji haki; na halikadhalika katika mapambano dhidi ya rushwa.
Kuhusu changamoto ya uhaba wa watumishi (Majaji) pamoja na maslahi yenu, Serikali imezichukua na itazifanyia kazi. Tutasubiri kupokea mapendekezo yenu ya majaji wapya pamoja na maboresho ya maslahi yenu. Lakini, ningependa niseme kwamba, katika kushughulikia changamoto hizi, tutazingatia uwezo wa Serikali.
Mheshimiwa Mkuu;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nihitimishe hotuba yangu kwa kuushukuru tena uongozi wa Mahakama kwa kunialika kwenye shughuli hii muhimu. Aidha, nawapongeza kwa kazi kubwa mnayoifanya. Ombi langu kwenu, shirikianeni na vyombo vingine, katika kushughulikia mapungufu yaliyopo katika mfumo wetu wa kutoa haki na kusimamia sheria. Kila mmoja wetu, akatimize wajibu wake katika kuwatumikia Watanzania.
Mungu Ibariki Siku ya Sheria!
Mungu Ibariki Mahakama ya Tanzania!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Jan 31, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA PASIPOTI YA KIELEKTRONIKI DAR ES SALAAM,...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA PASIPOTI YA KIELEKTRONIKI
DAR ES SALAAM, TAREHE 31 JANUARI, 2018
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein, Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza
la Wawakilishi Zanzibar;
Mheshimiwa Tulia Akson Mwansasu, Naibu Spika
wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Marais Wastaafu wa Serikali zetu mbili,
Mzee Mwinyi na Mzee Karume;
Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi pamoja na Mawaziri na Manaibu
Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Mheshimiwa Abdulhamid Yahya Mzee, Katibu Mkuu
Kiongozi wa Serikali ya Zanzibar;
Mheshimiwa Paul Sherlock, Balozi wa Ireland, pamoja
na Mabalozi wengine mliopo;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Mheshimiwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam;
Waheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Dkt. Anna Peter Makakala, Kamishna Mkuu wa Uhamiaji;
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama mliopo;
Mwakilishi wa Kampuni ya HDI Global;
Waheshimiwa Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Ndugu Watumishi wa Idara ya Uhamiaji mliopo;
Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, naungana na walionitangulia kuzungumza katika kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa leo. Aidha, natoa shukrani zangu nyingi kwa Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya Ndani pamoja na Kamishna Mkuu wa Uhamiaji, Dkt. Makakala, kwa kunialika katika tukio hili muhimu na la kihistoria kwa nchi yetu. Ahsanteni sana.
Napenda pia, hapa mwanzoni kabisa, kuwapongeza Watumishi wa Idara ya Uhamiaji kwa kazi mnazofanya. Kwa hakika, mnafanya kazi kubwa na nzuri. Hivi punde, Kamishna Mkuu wa Uhamiaji ameeleza baadhi ya mafanikio mliyopata katika kipindi kifupi kilichopita. Mmeanza kutumia mfumo wa ukusanyaji mapato kwa njia ya kielektroniki katika Ofisi zenu za Makao Makuu zilizopo hapa Dar es Salaam na Zanzibar. Aidha, mmeanza kutumia Mfumo wa Kuhakiki Hati za Vibali vya Ukaazi (e -Verification System) na pia mmeitikia wito wa Serikali wa kuhamia Dodoma. Hongereni sana Idara ya Uhamiaji kwa mafanikio hayo.
Ndugu Wananchi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sio siri kuwa Idara hii ya Uhamiaji ni nyeti na muhimu katika nchi yoyote. Ni muhimu kwanza katika suala la ulinzi na usalama; lakini pia ni muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi ya nchi. Kamishna Mkuu wa Uhamiaji ameeleza baadhi ya majukumu ya Idara yetu ya Uhamiaji kwa mujibu wa Sheria. Na baadhi ya majukumu hayo ni: (i) kutoa pasipoti na hati nyingine za kusafiria kwa raia wa Tanzania; (ii) kutoa hati za ukaazi kwa raia wa kigeni waliokidhi matakwa ya sheria; na (iii) kuratibu maombi ya wageni wanaoomba uraia wa Tanzania. Haya ni majukumu makubwa ambayo yanadhihirisha unyeti na umuhimu wa Idara hii.
Lakini pamoja na unyeti na umuhimu nilioueleza, ni wazi kuwa katika miaka ya hivi karibuni, Idara hii ililegalega kiasi. Ninyi nyote hapa ni mashahidi wa namna nchi yetu ilivyogeuka kuwa uchochoro wa wahamiaji haramu. Kila siku vyombo vya habari vilikuwa vikiripoti. Pasipoti zetu nazo zilikuwa zikigawiwa kiholela na wakati mwingine kuangukia kwa wahalifu, wakiwemo wafanyabiashara wa dawa za kulevya. Hii imeharibu sana taswira ya nchi yetu, na hivyo kufanya baadhi ya Watanzania kupata taabu kuingia kwenye baadhi ya nchi. Wengine wamepewa Pasipoti za Tanzania huku wakimiliki Pasipoti za nchi nyingine, kinyume kabisa cha sheria ya nchi yetu. Sambamba na hayo, vibali vya ukaazi pamoja na uraia wa nchi yetu navyo vilitolewa bila kuzingatia taratibu. Kuna raia wengi wa kigeni wamepata uraia bila kuwa na sifa stahiki na baadhi wameweza hadi kushika nyadhifa muhimu Serikalini. Wapo pia waliopewa vibali vya ukaazi kiujanjaujanja; wengine hawana sifa yoyote. Lakini zaidi ya hapo, ukusanyaji wa mapato ya viza na vibali vya ukaazi nao ulikuwa hauridhishi. Fedha nyingi zilikuwa zikipotea. Haya ni baadhi ya mapungufu yaliyokuwepo katika Idara hii, ambayo yalifanya watu wengi waione kuwa imeshindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo.
Na hii ndio moja ya sababu zilizonisukuma mimi kufanya mabadiliko ya uongozi wa Idara hii. Nikamteua mwanamama, Dkt. Makakala, kuwa Kamishna Mkuu. Nimemteua mwanamama kwa makusudi. Kama mnavyofahamu, akinamama ni waaminifu. Na nashukuru hajaniangusha. Ameanza vizuri. Ameeleza hivi punde kuwa mwaka jana pekee, Idara ya Uhamiaji imekamata takriban wahamiaji haramu 15,068. Siku za nyuma idadi ya waliokatwa ilikuwa ndogo. Hivyo basi, nakupongeza sana Kamishna Mkuu. Nafahamu kuwa bado kuna mapungufu; lakini natambua jitihada ulizoanza kuzichukua. Nakuhimiza uendelee kushughulikia mapungufu yaliyosalia bila ya uoga wowote. Na nawasihi watumishi wa Idara ya Uhamiaji kuendelea kumpa ushirikiano wa kutosha.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Tumekutana hapa kwa shughuli maalum. Kufanya Uzinduzi wa Pasipoti ya Kielektroniki (e-Passport) ya Tanzania. Bila shaka, sote tunaifahamu posipoti pamoja na umuhimu na kazi zake. Baadhi yetu tunazo. Lakini, kwa ujumla, niseme tu kwamba, Pasipoti ni nyaraka inayomwezesha mtu kusafiri kutoka nchi moja kwenda nyingine. Kwa kawaida, nyaraka hii hutolewa na nchi kwa raia wake, na kwa maana hiyo hutumika pia kumtambulisha mtu uraia wake. Lakini, wakati mwingine, nchi inaweza kutoa pasipoti hata kwa mtu asiye raia wake (mathalan, mwekezaji au mtaalam wa jambo fulani). Aidha, katika zama za sasa, zipo baadhi ya taasisi zenye kutambulika kimataifa, ambazo nazo hutoa pasipoti kwa watumishi wake. Baadhi ya taasisi hizo ni Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki, Umoja wa Afrika, Umoja wa Mataifa, n.k.
Kwa kuzingatia hayo yote, ni dhahiri kuwa tukio hili la leo ni muhimu sana. Ni muhimu kwanza kutokana na umuhimu wa Pasipoti nilioueleza hivi punde; lakini pili kwa sababu Pasipoti hii tunayoizindua leo ni ya pekee sana. Kama mnavyofahamu, nchi yetu nayo ina Pasipoti yake. Pasipoti hii imekuwepo na tumekuwa tukiitumia kwa muda mrefu sasa. Mfumo uliotumika kuitengeneza ni wa kizamani na haikuwekewa usalama wa kutosha. Hii ndio sababu imekuwa rahisi kwa baadhi ya kuighushi. Zaidi ya hapo, taarifa zilizomo kwenye Pasipoti ya zamani ilikuwa ni lazima zisomwe kwenye mashine. Hii ndio sababu, Watanzania wakitaka kutembelea baadhi ya nchi, walilazimika kwanza kuzituma Pasipoti zao kwenda nchi hizo au kwenye Balozi za jirani, ili kupata viza.
Pasipoti tunayoizindua leo, kama nilivyosema, ni ya kielektroniki. Ina alama nyingi za usalama (security features). Hii itasaidia kupunguza kama sio kuondoa kabisa uwezekano wa kughushiwa. Zaidi ya hapo, kwa kuwa Pasipoti hii ni ya kielektroniki, baadhi ya taarifa zake zitaweza kusomeka kwenye mifumo ya kielektroniki bila kulazimika kuipeleka Pasipoti yenyewe. Hii itaokoa muda, itapunguza gharama na uwezekano wa kupotea pindi Pasipoti zinaposafirishwa kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kuomba viza.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Hivi punde Kamishna Mkuu ameeleza kuwa uzinduzi wa Pasipoti hii ya Kielektroniki ya Tanzania inaashiria kuanza kwa utekelezaji wa mradi mkubwa wa Uhamiaji Mtandao (e-Immigration), ambao umepangwa kutekelezwa kwa awamu nne. Baada ya kuzindua Pasipoti hii, Awamu inayofuata, ambayo ni ya pili, itahusu kufunga mfumo wa Viza ya Kieletroniki (e-Visa) pamoja na Hati ya Ukaazi ya Kielektroniki. Awamu ya tatu itahusu Usimamizi wa Mipaka kwa njia ya Kielektroniki (e-Border Management System); na Awamu ya Nne itahusu kupanua huduma za uhamiaji mtandao kwenye Ofisi za Balozi zetu pamoja na Wilaya zenye shughuli nyingi za kiuhamiaji.
Napenda kutumia fursa hii, kuipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Idara ya Uhamiaji pamoja na taasisi nyingine zilizohusika kwa kuanza kutekeleza mradi huu wa Uhamiaji Mtandao. Mimi naufahamu vizuri Mradi huu na nimekuwa nikiufuatilia kwa karibu. Haikuwa jambo rahisi kufikia hatua hii. Kamishna Mkuu wa Uhamiaji ameeleza hivi punde kuwa gharama za mradi huu ni Dola za Marekani milioni 57.82, sawa na takriban shilingi bilioni 127.2. Lakini, awali ulipangwa kutekelezwa kwa Dola za Marekani milioni 226, zaidi ya shilingi bilioni 400. Ikabidi tuingilie kati ndipo tukaipata Kampuni ya HDI Global ya Marekani, ambayo ilikubali kuutekeleza kwa kiasi hicho cha Dola za Marekani milioni 57.82. Kama alivyosema Kamishna Mkuu, Kampuni ya HDI Global ni ya kimataifa na imekidhi viwango vyote.
Hivyo basi, naishukuru Kampuni hii kwa kubali kutekeleza mradi huu kwa gharama nafuu. Aidha, naishukuru sana Serikali ya Ireland kwa ushirikiano waliotupa kumpata Mkandarasi huyu. Nimefarajika kuona kuwa Balozi wa Ireland, Mheshimiwa Sherlock, pamoja na Mwakilishi wa Kampuni ya HDI Global tunao hapa. Tunawashukuru sana. Vilevile, nawashukuru na kuwapongeza Watanzania wote kwa kuwezesha kuanza utekelezaji wa mradi huu. Fedha zote za kutekeleza mradi huu zinatolewa na Serikali. Na kama mnavyofahamu, Serikali inapata fedha kupitia kodi zenu mnazolipa. Hivyo basi, hongereni sana Watanzania. Na nawasihi muendelee kulipa kodi ili kuiwezesha Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo kama hii pamoja na kuboresha huduma mbalimbali za jamii.
Nawasihi pia kuendelea kuunga mkono mradi huu. Hivi punde imeelezwa kuwa pasipoti hii mpya ya kielektroniki itapatikana kwa gharama za shilingi 150,000. Bei hii ipo juu kuliko bei ya sasa. Lakini Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri kuwa bei hii imezingatia gharama za utengenezaji pamoja na ukubwa na ubora pasipoti hii mpya. Pasipoti hii itakuwa na kurasa nyingi kuliko ya zamani; na pia, kama ilivyoelezwa, bei hii ipo chini ukilinganisha na bei ya Pasipoti kama hii kwenye nchi nyingine. Hivyo basi, hatuna budi tuikubali na hasa kwa kuzingatia kuwa ongezeko hili la bei limetokana na maboresho tuliyofanya katika kuimarisha usalama wa Pasipoti zetu. Na niwaombe pia Watanzania wenzangu, tukipata Pasipoti hizi tuzilinde na kuzitunza; kwani kuna taarifa kuwa baadhi ya watu walipewa Pasipoti, wakaziuza na kisha kusingizia kuwa zimepotea. Naamini ujanja kama huo hauwezi kufanyika kwenye Pasipoti zetu mpya kwa vile zimeongezewa alama za usalama.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kuzindua Pasipoti ya Kielektroniki ya Tanzania. Hivyo, sitapenda kuwachosha kwa hotuba ndefu. Lakini, kabla sijahitimisha hotuba yangu, ninayo masuala mengine machache ambayo ningependa niyaeleze.
Suala la kwanza linahusu umuhimu wa kutekeleza kwa wakati na kusimamia kwa umakini mkubwa mradi huu. Kama ilivyoelezwa, mradi huu una awamu nne, ambazo zote zimepangwa kukamilika ndani ya mwaka huu wa 2018. Hivyo basi, hakikisheni mnakamilisha kama ilivyopangwa. Tunataka kuona wananchi wetu pamoja na wageni wanaotutembelea wanapata huduma nzuri za kiuhamiaji na tena za haraka. Nimefurahi kusikia kuwa katika kutekeleza Mradi huu, wadau karibu wote wanaohusika na masuala ya uhamiaji (NIDA, RITA, Jeshi la Polisi, Idara ya Wakimbizi, Bodi ya Utalii, BRELA, TRA, n.k.) wameshirikishwa, na kutakuwa na mfumo wa mawasiliano. Hii, bila shaka, itaongeza ufanisi na kasi ya utendaji kazi.
Kwa sababu hiyo, nitashangaa kama, pamoja na kuanza kwa mradi huu, wananchi watachukua muda mrefu kupata Pasipoti zao au kupata majibu ya kutopewa kwa kukosa vigezo. Nitashangaa, kama malalamiko ya upatikanaji viza yataendelea kusikika, kama ilivyotokea wakati wa Sherehe za Waumini wa Madhehebu ya Bohora mwaka juzi na wakati wa ujio wa Timu ya Everton ya Uingereza mwaka jana. Nitashangaa, kama vibali vya ukaazi vitatolewa kiholela na kwa watu wasio na sifa. Nitashangaa pia kama ukusanyaji wa mapato hautaongezeka. Nitashangaa sana. Lakini, ningependa pia kusema kuwa, katika kutekeleza mradi huu, kuweni sana makini, hususan katika masuala yanayohusu usalama na uraia wa nchi yetu. Na katika hili, nawapongeza Idara ya Uhamiaji kwa kuanzisha zoezi la utambuzi wa watu wasio raia nchini. Zoezi hili liwe endelevu, na lifanyeni kwa kushirikiana na mamlaka nyingine ili kuwatambua wote wanaoishi nchini bila vibali, wenye kufanya kazi bila vibali vya kazi na ukaazi au wanaofanya kazi zinazoweza kufanywa na Watanzania. Hivi majuzi wameingia wakimbizi zaidi ya 1,000 kutoka DRC; lakini nimeambiwa walioripoti Kambini wahafiki 1,000. Wengine watakuwa wameingia mitaani. Watafuteni na kuwakamata.
Suala la pili, ambalo linahusiana na hilo la kwanza, ni kuhusu uadilifu na uaminifu. Ni kweli kabisa kuwa Mfumo huu wa Uhamiaji Mtandao ni mzuri sana. Lakini, kama mjuavyo, mfumo kama mfumo peke yake hauwezi kuleta matokeo tunayoyataka. Ufanisi wa Mfumo huu utategemea sana uadilifu na utendaji kazi wa watumishi wa Idara hii. Natambua kuwa bado wapo watumishi wa Idara hii ambao hawataki kubadilika. Wanaendelea na utaratibu wa zamani wa kuendekeza vitendo vya rushwa. Kwa bahati nzuri, watu hao sio wengi. Ni wachache. Lakini, vitendo vyao vinaichafua sana Idara hii nyeti na muhimu katika nchi. Hivyo basi, Kamishna Mkuu hakikisha watu hawa unawashughulikia bila woga. Wakati mwingine, huwa nashangaa sana kuona wakimbizi haramu wanakamatwa baada ya kuwa wamepita kwenye maeneo mengi ya nchi. Ifike wakati sasa, ikibainika mhamiaji haramu alivuka eneo fulani bila kukamatwa, mathalani Mkoa fulani; basi kiongozi wa Mkoa husika achukuliwe hatua. Ashushwe cheo au hata kufukuzwa kazi. Ndio, wafukuzwe tu. Wapo Watanzania wengi tu wazalendo wanatafuta kazi.
Suala la tatu, ni kuhusu changamoto zinazoikabili Idara ya Uhamiaji alizosema Kamshna Mkuu. Upungufu wa vitendea kazi, vifaa, n.k. Serikali inatambua changamoto zenu zote na baadhi tumeanza kuzishughulikia. Mtakumbuka kuwa ni hivi majuzi tu Serikali imenunua nyumba 103 za watumishi wa Uhamiaji kule Dodoma kwa gharama ya takriban shilingi bilioni 3. Kuhusiana na suala la kuhamia Dodoma, nawaahidi kuwapatia shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Makao Makuu Dodoma. Nawaahidi pia kuwa Serikali itaendelea kutatua changamoto zenu nyingine, ikiwemo kuboresha maslahi yenu, kadri uwezo wetu kifedha utakavyozidi kuimarika. Kama nilivyosema awali, Idara ya Uhamiaji ni nyeti na muhimu kwa usalama, ustawi na maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Suala la nne na la mwisho, lakini sio kwa umuhimu, ni kwa wana-Dar es Salaam. Nawashukuru sana kwa kujitokeza kwa wingi kwenye shughuli hii. Nawahakikishia Serikali yenu imejipanga kuwaletea na kutatua shida zenu mbalimbali. Mathalan, nafahamu moja ya kero kubwa katika Jiji hili, ni suala la msongamano wa magari barabarani. Tumeanza kuchukua hatua. Tunajenga madaraja ya juu pale TAZARA na Ubungo, yote kwa pamoja, kwa gharama ya takriban shilingi bilioni 290.45. Aidha, mwaka huu (2018) tunatarajia kuanza ujenzi Awamu ya Pili ya mradi wa Barabara za Mabasi ya Mwendokasi kutoka mjini hadi Mbagala (Kilwa Road) yenye urefu wa kilometa 20.3. Halikadhalika, mwezi Februari, 2018 tunatarajia kuanza upanuzi wa Barabara ya Morogoro kuwa ya njia sita kutoka Kimara hadi Kiluvya, urefu wa takriban kilometa 16. Na kama mnavyofahamu, tumeanza ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa kuanzia hapa Dar es Salaam kuelekea Dodoma, umbali wa takriban kilometa 712 ambapo kiasi cha shilingi trilioni 7.062 kinatarajiwa kutumika; chote kitatolewa na Serikali. Reli hii, ambayo itaelekea Mikoa ya Mwanza na Kigoma na kisha kuungana na reli za kwenda Burundi na Rwanda, ikikamilika itarahisisha sana usafiri kati ya hapa Dar es Salaam, jiji kubwa la biashara, na Dodoma, Makao Makuu ya nchi yetu.
Sambamba na hayo, tunaboresha huduma nyingine za kijamii, ikiwemo maji, afya na elimu. Mwezi Juni, 2017 nilizindua mradi wa Maji wa Ruvu Juu pale Mlandizi kwa ajili ya Jiji la Dar es Salaam na maeneo ya jirani. Hivi sasa tunatekeleza mradi wa kuchimba visima virefu vya Mpera na Kimbiji kwa ajili ya kusambaza kwenye maeneo ambayo kwa sasa hayana mtandao wa mabomba. Miradi hii yote itaboresha upatikanaji wa huduma za maji. Kwenye afya, tunaendelea kuboresha hospitali zetu za Taifa zilizopo hapa Dar es Salaam: Muhimbili na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road. Aidha, hivi majuzi tu nilizindua Hospitali kubwa na ya kisasa ya Mloganzila, ambayo inaipunguzia mzigo Hospitali yetu ya Taifa ya Muhimbili. Mpaka sasa zaidi ya wagonjwa 140 tayari wamehamishiwa Mloganzila. Tutaendelea kuijengea uwezo Hospitali hii ya Mloganzila. Vilevile, tunaziboresha hospitali zetu za Wilaya: Amana, Mwananyamala na Temeke pamoja na vituo vya afya vipatavyo vitano katika Jiji hili, vikiwemo viwili katika Wilaya hii ya Temeke (Yombo Vituka na Maji Matitu) ili kuviwezesha kutoa huduma ya dharura za upasuaji, hususan kwa akinamama wajawazito. Kwenye elimu, ninyi nyote mnafahamu mambo tunayofanya ya kupanua wigo na kuboresha elimu nchini, kuanzia elimu ya msingi hadi chuo kikuu.
Nina imani, kwa hatua hizi tunazochukua, Jiji la Dar es Salaam litazidi kuwa bora. Wito wangu kwenu wananchi endeeleni kuiunga mkono Serikali, hususan kwa kudumisha amani na umoja, kuchapa kazi kwa bidii na bila kusahau kulipa kodi.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wananchi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimezungumza mengi. Napenda niishie hapa. Nawashukuru tena wenyeji wa shughuli hii kwa kunialika. Aidha, nawashukuru wenzangu tuliohudhuria hafla hii pamoja na wana-Dar es Salaam. Ahsanteni sana kwa kujitokeza kwa wingi kwenye tukio hili muhimu na la kihistoria kwa nchi yetu.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kuzindua Pasipoti ya Kielektroniki ya Tanzania.
Mungu Ibariki Pasipoti ya Kielektroni ya Tanzania!
Mungu Ibariki Idara ya Uhamiaji!
Mungu Wabariki Wana-Dar es Salaam!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Dec 20, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UWEKAJI JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA OFISI YA TAIFA YA TAKW...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango;
Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa John Malecela, Waziri Mkuu Mstaafu;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mwenyekiti wa Kamati
ya Bunge ya Bajeti;
Mheshimiwa Ian Myles, Balozi wa Canada nchini;
Mheshimiwa Mama Bella Bird, Mwakilishi
wa Benki ya Dunia nchini;
Waheshimiwa Wabunge na Mstahiki Meya
wa Manispaa ya Dodoma;
Ndugu Mkurugenzi Mkuu pamoja na Watumishi
wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo hapa;
Wageni Waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu, kwa kutupa uhai na kutuwezesha kukutana hapa leo. Aidha, naushukuru uongozi wa Wizara ya Fedha pamoja na Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kunialika kwenye hafla hii ya kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu hapa Dodoma, ambako ndiko Makao Makuu ya Nchi yetu. Ahsanteni sana.
Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wageni wote waalikwa pamoja na wananchi wa Dodoma kwa kujitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hili. Nina uhakika kuwa mmejitokeza kwa wingi sio tu kwa sababu mnafahamu manufaa ya Jengo hili kujengwa hapa Dodoma, Makao Makuu ya Nchi yetu; bali pia kwa kuwa mnatambua umuhimu wa takwimu kwa maendeleo ya nchi.
Waheshimiwa Viongozi;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Nafahamu kuwa wengi wetu hapa tunajua umuhimu wa takwimu. Hata hivyo, napenda kutumia fursa hii kusisitiza kuwa takwimu ni muhimu. Na ni muhimu katika nyanja zote. Iwe kiuchumi, kisiasa, kijamii na halikadhalika kiulinzi na usalama; na hata kiutamaduni.
Takwimu, na hasa zikiwa sahihi, zinaiwezesha Serikali kutambua mahitaji ya nchi au wananchi; kuweka malengo na kuandaa mipango ya maendeleo; pamoja na kufuatilia utekelezaji wake. Mathalan, kupitia takwimu za idadi ya watu, Serikali inatambua kiasi gani cha fedha kinachotakiwa kutengwa kwa ajili ya kununua dawa; au kufahamu mahali gani shule au kituo cha afya kijengwe.
Sambamba na hayo, takwimu zinaliwezesha Taifa kujipima limefikia hatua gani kimaendeleo, hususan kwa kutumia vigezo mbalimbali, ikiwemo pato la taifa, wastani wa umri wa kuishi, kiwango cha vifo kwa makundi mbalimbali (watoto wachanga, akinamama wajawazito) n.k. Zaidi ya hapo, takwimu ni muhimu kwa nchi kama yetu kwa ajili ya kufahamu utajiri na rasilimali tulizonazo, kama vile madini, gesi, mafuta, wanyama pori, mifugo, rasilimali za kwenye maji, n.k.
Hivyo basi, kwa ujumla, naweza kusema kuwa, takwimu ni muhimu sio tu katika nyanja zote, bali pia katika ngazi zote. Iwe ngazi ya mtu mmoja mmoja, familia, taasisi ya Serikali au isiyo ya Serikali; na Taifa kwa ujumla. Hii ndio sababu kuna usemi wa Kiingereza usemao “Without good statistics, the development process is blind”. Tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi ya usemi huu ni kwamba “bila ya takwimu sahihi, ni vigumu kupata maendeleo”.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Ni kutokana na ukweli huo, napenda kutumia fursa hii kuipongeza Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya katika kuandaa takwimu mbalimbali nchini. Hongereni sana. Napenda pia kutumia fursa hii, kuwapongeza kwa uamuzi wenu wa kujenga Ofisi hii hapa Dodoma. Kama mnavyofahamu, Serikali imedhamiria kwa dhati kabisa kuhamia Dodoma. Hivyo basi, ujenzi wa Jengo hili, ambalo, bila shaka litaboresha mandhari ya Mji wa Dodoma, unaenda sambamba na azma ya Serikali ya kuhamia Dodoma. Nimefurahi kusikia kuwa kazi ya ujenzi wa Jengo hili umekuwa ukitoa wastani wa ajira za moja kwa moja zipatazo 120 kwa siku; na kwamba kazi ya usanifu, ushauri na usimamizi inafanywa na Wataalam wa Tanzania. Hili ni jambo zuri kwa vile linawajengea uwezo wataalam wetu wa ndani.
Lakini, kwa namna ya pekee, napenda kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu nyingi kwa washirika wetu mbalimbali, ambao wameufadhili mradi huu utakaogharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 11.6 hadi kukamilika. Tunaishukuru Benki ya Dunia, Shirika la Maendeleo la Uingereza (DfID) na Shirika la Maendeleo la Canada. Tunawashukuru sana; na nimefurahi kuona wawakilishi wa Taasisi hizi tuko nao hapa. Pokeeni shukrani zetu nyingi, na tunawaomba muendelee kutuunga mkono. Nawahakikishia kuwa kila senti mtakayotupatia tutaitumia vizuri. Hakuna hata senti moja itakayopotelea kwenye mifuko ya watu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Mwanzoni mwa hotuba yangu nimeeleza kuwa takwimu ni muhimu kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo kutambua ukuaji uchumi wa Taifa. Hivyo basi, kwa kuwa leo nimekuja hapa kuweka Jiwe la Msingi la Ofisi ya Takwimu; na kwa kuwa nipo hapa Dodoma, Makao Makuu ya Nchi; napenda kutumia fursa hii, kueleza kwa kifupi tu hali ya ukuaji uchumi wa nchi yetu kwa kutumia takwimu mbalimbali.
Kwa ujumla, napenda kusema tu kuwa, ukuaji wa uchumi wetu unaendelea vizuri. Mathalan, katika nusu ya kwanza ya mwaka huu, uchumi ulikua kwa kasi ya asilimia 6.8. Kasi hii imeiwezesha nchi yetu kuongoza katika eneo la Afrika Mashariki, lakini pia kuifanya kuwa miongoni mwa nchi ambazo uchumi wake unakua kwa kasi barani Afrika. Aidha, mfumko wa bei umeendelea kuwa chini, ambapo mwezi Novemba 2017 umefikia asilimia 4.4. Na hii inamaanisha kuwa ugumu wa maisha umepungua kinyume na baadhi ya watu wanavyosema kuwa “vyuma vimekaza”. Wengi ambao kwao vyuma vimekaza ni wale ambao walizoea fedha za bure, ikiwemo kupitia watumishi hewa, safari za nje, semina, n.k. Kwa wenye kujituma, vyuma haviwezi kukaza. Mathalan, kwa mkulima wa korosho ambaye bei imeongezeka kutoka wastani wa shilingi 2,000 kwa kilo hadi shilingi 4,000, unadhani kwake vyuma vitakaza? Lakini pia tujiulize, hivi kweli inawezekana kwa mtu wa kule kwetu Chato, ambako bei saruji imeshuka kutoka wastani wa shilingi 27,000 hadi shilingi 15,000 kwa mfuko iwe vyuma kwake vimekaza?
Mbali na kupungua kwa mfumko wa bei, akiba ya fedha za kigeni za nchi yetu imeongezeka. Hivi sasa imefika Dola za Marekani bilioni 5.82. Kiasi hiki cha fedha kinatuwezesha kununua nje bidhaa na huduma kwa miezi mitano. Kiwango kilichowekwa na Jumuia ya Afrika Mashariki ni angalau miezi minne. Hizi ni baadhi tu ya takwimu zinazoonesha kuwa uchumi wetu unaendelea vizuri. Nafahamu kuwa wapo watu wanaojaribu kupotosha ukweli huo; lakini nawaomba Watanzania muwapuuze watu hao na badala yake mziamini takwimu zinazotolewa na Ofisi yetu ya Takwimu, ambayo hivi punde Mwakilishi wa Benki ya Dunia, Mama Bella Bird, ameisifu kuwa ni mojawapo ya taasisi bora Barani Afrika.
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Ni dhahiri kuwa takwimu za ukuaji uchumi pekee kama haziendi sambamba na maendeleo na ustawi wa maisha ya watu hazina umuhimu wowote. Upo usemi wa Kiingereza usemao “You cannot feed the hungry on statistics (Huwezi kumlisha au kumshibisha mtu mwenye njaa kwa takwimu)”. Aidha, Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, aliwahi kusema kuwa “Maendeleo ya Uchumi ni lazima yafungamanishwe na Maendeleo ya Watu”. Kwa kutambua hilo, Serikali inafanya kila jitihada ili kuhakikisha kuwa maendeleo ya kiuchumi yaliyopatikana yanawiana na maendeleo na ustawi wa maisha ya watu. Hii ndio sababu, tumeweka mkazo mkubwa katika kuboresha huduma za jamii, ambazo zinawagusa wananchi wengi.
Mathalan, kama mnavyofahamu, hivi sasa tunatoa elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi sekondari. Mpaka kufikia mwezi Novemba 2017, Serikali imetumia kiasi cha shilingi bilioni 535 tangu utaratibu huu uanze mwezi Desemba 2015. Mkoa wa Dodoma pekee umepokea kiasi cha shilingi bilioni 16.6. Bila shaka, mtakubaliana nami kuwa, utaratibu huu umewezesha watoto wengi kutoka familia maskini kupata fursa ya elimu. Na hii inathibitishwa na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza. Na kama mnavyofahamu, njia rahisi ya kumsaidia mtu maskini, ni kumpa elimu.
Sambamba na elimu, tumeboresha huduma za afya nchini, ambapo tumeongeza bajeti ya dawa pamoja na kununua vifaa vya uchunguzi, vitanda, magodoro na mashuka; na halikadhalika tumeajiri watumishi wapya wa afya. Mathalan, nimeambiwa kuwa upatikanaji wa dawa muhimu kwenye Mkoa huu, umefikia asilimia 90 hivi sasa. Aidha, hapa Dodoma tumekamilisha jengo la wodi ya akina mama katika Hospitali ya Mkoa kwa gharama ya shilingi milioni 600, na tunatarajia kuanza ukarabati na ujenzi wa miundombinu mingine ya hospitali hiyo kwa gharama ya takriban shilingi bilioni 2.5. Vilevile, jumla ya vituo 5 vya afya, kikiwemo cha Makole na Bahi, tumevikarabati kuviwezesha kutoa huduma za dharura, ikiwemo upasuaji kwa akina mama wajawazito. Uboreshaji wa vituo hivyo umegharimu shilingi bilioni 2.5.
Sambamba na hayo, Hospitali ya Benjamin Mkapa nayo imeanza kutoa huduma; ambapo Serikali imeipatia vifaa vya kisasa kama MRI, CT-Scan pamoja na vifaa vya kupandikiza figo na kufanya upasuaji bila kuchana mwili. Vilevile, hivi sasa tupo kwenye mazungumzo na marafiki zetu wa Israel ili kuanzisha kitengo cha Huduma za Wagonjwa Mahututi cha Kisasa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa. Hatua hizi, bila shaka, zimeimarisha upatikanaji wa huduma ya afya hapa Dodoma.
Tunachukua pia hatua za kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji. Kwenye kila Mkoa hivi sasa kuna miradi ya maji inayotekelezwa. Hapa Dodoma, tumetekeleza miradi kadhaa ya maji, ukiwemo Mradi wa kupeleka maji Chuo Kikuu cha Dodoma. Lakini sambamba na miradi hiyo, tupo mbioni kuanza ujenzi wa mradi wa mkubwa wa maji wa Bwawa la Farkwa kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 420, zaidi ya shilingi bilioni 920, ambapo mpaka sasa usanifu na mchoro wake umekamilika. Bwawa hili litakapokamilika, linatarajiwa kuondoa kabisa tatizo la maji katika Wilaya za Bahi, Chemba, Chamwino na hapa Manispaa.
Hizi ni baadhi tu ya hatua tunazochukua kuhakikisha maendeleo ya kiuchumi tuliyoyapata tunayatafsiri kwenye maisha ya watu. Lakini mbali na hatua hizi za kuboresha huduma za jamii, tumeelekeza nguvu katika kuimarisha miundombinu ya usafiri na umeme, ambayo nayo ni muhimu sana sio tu katika kukuza uchumi bali pia kuleta ustawi katika maisha ya wananchi. Tunajenga reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza; tunatekeleza miradi mikubwa ya umeme.
Waheshimiwa Viongozi;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kuweka Jiwe la Msingi la Jengo hili. Hivyo, nisingependa kuwachosha kwa hotuba ndefu. Hata hivyo, kabla sijahitimisha, ninayo masuala kama manne ambayo ningependa niyaseme.
Suala la kwanza, kama mtakavyokumbuka, mwanzoni mwa hotuba yangu nimeeleza kuhusu umuhimu wa takwimu. Lakini ili takwimu ziwe muhimu ni lazima ziwe sahihi. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuhimiza Ofisi ya Takwimu kuendelea kuandaa taarifa zenu kwa weledi mkubwa. Aidha, natoa wito kwa wananchi na Taasisi zote za Serikali kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Ofisi ya Taifa ya Takwimu pindi wakihitaji taarifa mbalimbali. Sambamba na hayo, natoa onyo kwa wale watu wote wenye kutoa takwimu za uongo au upotoshaji. Naziagiza mamlaka husika kuchukua hatua dhidi ya watu wa namna hiyo. Sheria ya Takwimu kifungu Namba 37 kifungu kidogo cha 3 hadi cha 5 kinatamka wazi kwamba mtu au Taasisi akitoa takwimu za uongo au kusababisha wananchi kushindwa kutoa ushirikiano kwa ofisi ya Taifa ya Takwimu, adhabu yake ni kifungo cha miezi sita hadi miaka mitatu, ama kulipa faini kati ya shilingi milioni moja hadi shilingi milioni kumi; au adhabu zote kwa pamoja. Nimefurahi kusikia kuwa mchakato wa kuifanyia marekebisho sheria hiyo ili kuiongezea makali umeanza. Haiwezekani taasisi za kitaifa na kimataifa zenye wajibu wa kutoa takwimu zitoa takwimu fulani, halafu ajitokeze mtu mwingine aseme kuwa ana takwimu nyingine zinazotofautiana na hizo. Jambo hili halikubaliki.
Suala la pili, napenda pia kutumia fursa hii kurudia wito wangu nilioutoa hivi majuzi wakati nafungua tawi la CRDB kwa Wizara ya Fedha pamoja na Benki Kuu kuhusu kuimarisha usimamizi wa Benki, matumizi ya Dola, pamoja na usajili wa makampuni ya Simu na Benki kwenye mfumo wa ukusanyaji mapato kwa njia ya Kielectroniki. Mheshimiwa Waziri wa Fedha, hakikisha suala hili linatekelezwa kabla ya mwisho wa mwaka huu. Na pia Mheshimiwa Waziri fuatilia suala la umiliki wa Kampuni ya Simu ya Airtel, ambalo kwa taarifa zilizopo, ni mali ya Serikali.
Suala la tatu, mwezi Juni mwaka huu, wakati nikiwa pale Kijitonyama kuzindua Kituo cha Data na Mfumo wa Ukusanyaji Mapato kwa njia ya Kielektroniki niliagiza kuwa Taasisi zote za Serikali kutumia Kituo cha Data cha Taifa na kuachana na utaratibu wa kila taasisi kutengeneza Kituo chake. Mheshimiwa Waziri katika taarifa yake ameeleza kuwa Ujenzi wa Jengo hili utahusisha pia ujenzi wa kanzidata. Hivyo basi, natoa wito kwenu kutafakari suala hili vizuri. Kama hakuna sababu za msingi za kujenga kanzidata yenu wenyewe, ni vyema mtumie Kituo cha Data cha Taifa, ambacho kina viwango vya kimataifa na Serikali ilitumia fedha nyingi kuwekeza.
Suala la nne, ni kwa wana-Dodoma wote. Dodoma sasa inafunguka. Fursa nyingi za kiuchumi zinakuja, hususan kutokana na uamuzi wa Serikali kuhamishia Makao Makuu hapa Dodoma. Aidha, kuna miradi mingi na mikubwa imepangwa kutekelezwa hapa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa, kutoka Dar es Salaam kupita hapa Dodoma kuelekea mikoa ya Mwanza na Kigoma. Ujenzi wa kipanda cha Reli hii kutoka Dar Es Salaam mpaka hapa Dodoma (Makutupora) chenye urefu wa takriban kilometa 712 kimeanza kujengwa kwa gharama ya shilingi trilioni 7.062 ambazo zote zitatolewa na Serikali. Sambamba na hayo nafahamu kuwa Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii imepanga kutekeleza miradi kadhaa ya viwanda hapa Dodoma, ikiwa ni pamoja na kufufua Kiwanda cha kusindika nafaka na kukamua mafuta cha National Milling Corporation (NMC), Kiwanda cha kutengeneza matofali na vigae, na Kiwanda cha Kusindika Juisi na Mvinyo wa Zabibu ambacho kitajengwa Chinangali, Chamwino. Hivyo basi, nawasihi sana wana-Dodoma kujipanga vizuri kutumia fursa hizo.
Mwisho kabisa, nawashukuru tena kwa kunikaribisha. Aidha, nawapongeza tena Ofisi ya Takwimu kwa kazi nzuri mnayoifanya. Nawashukuru pia tena washirika kwa misaada yenu mbalimbali mnayotupatia. Naomba muendelee na moyo huo.
Mabibi na Mabwana; baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kuweka Jiwe la Msingi la Jengo la Ofisi ya Taifa ya Takwimu hapa Dodoma.
Mungu Ibariki Ofisi ya Taifa ya Takwimu!
Mungu Ibariki Dodoma!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 18, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI WA CCM KWENYE UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA TISA WA TAIFA W...
Soma zaidiHotuba
Ndugu Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar
na Makamu Mwenyekiti wa CCM - Zanzibar;
Ndugu Philip Mangula, Makamu Mwenyekiti
wa CCM- Tanzania Bara;
Ndugu Wenyeviti na Makamu Wenyeviti
Wa CCM wa Taifa Wastaafu mliopo;
Ndugu Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM;
Ndugu Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Ndugu Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu mliopo;
Ndugu Wake za Viongozi Wastaafu mkiongozwa
na Mama Maria Nyerere na Fatuma Karume;
Ndugu Wajumbe wa Kamati Kuu;
Ndugu Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa;
Ndugu Viongozi Wastaafu mliopo;
Ndugu Wawakilishi wa Vyama Rafiki
na Shindani vya CCM mliopo;
Ndugu Viongozi na Wazee Wastaafu wa CCM mliopo;
Ndugu Wageni Wetu Wote Waalikwa: Viongozi wa
Serikali na Dini mliopo;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Ndugu Wana-CCM Wenzangu; Mabibi na Mabwana:
CCM OYEE! MAPINDUZI, DAIMA!
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, kwa kutujulia uhai na kutuwezesha kukutana hapa Dodoma leo. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwakaribisha ndugu wajumbe pamoja na wageni wote waalikwa katika Mkutano huu Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) unaofanyika hapa Dodoma; Makao Makuu ya Chama chetu pamoja na Serikali. Karibuni sana.
Natambua kuwa baadhi yenu mmelazimika kusafiri umbali mrefu kuja kuhudhuria Mkutano huu. Hivyo basi, napenda nitumie fursa hii kuwapa pole ya safari. Bila shaka, mmesafiri umbali mrefu kuja kuhudhuria Mkutano kwa kuwa mnafahamu umuhimu wake, lakini pia hii ni ishara ya mapenzi ya kweli mliyonayo kwa Chama hiki. Na ningependa kutumia fursa hii kuwapongeza wajumbe wote wa Mkutano huu kwa kuchaguliwa kwenu. Hongereni sana.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu na Wana-CCM Wenzangu;
Mkutano huu unafanyika zikiwa zimepita takriban wiki 3 tangu nchi yetu ifanye Uchaguzi Mdogo wa Madiwani katika kata 43. Na kama mtakavyokumbuka, katika uchaguzi huo, Chama chetu kilishinda viti vya udiwani 42. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kutoa pongezi nyingi kwa wanachama, wapenzi na mashabiki wa CCM kwa ushindi mkubwa tuliopata.
Kwa tathmini yangu binafsi, ushindi huu tuliopata umetokana na mambo makubwa manne. Kwanza kabisa, ni matokeo ya uungwaji mkono mkubwa na kukubalika kwa Chama chetu miongoni mwa Watanzania. Pili, unatokana na uimara na ukomavu wa Chama chenyewe. Sio siri kuwa Chama hiki ni kikongwe. Mwaka huu kimetimiza miaka 40 tangu kianzishwe. Hakuna Chama kikongwe kama hiki hapa nchini. Kimeongoza Dola tangu kimeanzishwa mwaka 1977 na tangu kurejeshwa kwa Mfumo wa Vyama vingi nchini 1992. Kina mashina, matawi, pamoja na wanachama, wapenzi na washabiki nchi nzima. Na katika kudhihirisha kuwa Chama hiki ni kikubwa na kikongwe, ni katika kudhihirisha hili, ninyi wenyewe mnajionea hapa viongozi wakuu wastaafu wa Chama na Serikali wapo hapa. Tunaye hapa Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Mzee Karume, Mzee Malecela, Mzee Msekwa, Mzee Msuya, Mzee Dkt. Salim na Mzee Pinda. Hii inadhihirisha kuwa Chama hiki ni kikongwe na kina hazina kubwa.
Sababu ya tatu, iliyotufanya tushinde Uchaguzi huu ni kwamba tunatekeleza kwa vitendo mambo tuliyoahidi wakati wa Kampeni kupitia Ilani yetu ya Uchaguzi ya Mwaka 2015 – 2020. Na nne, tumeshinda kwa vile hivi sasa wana-CCM tuna umoja. Na tunashirikiana. Hivyo basi, napenda kurudia tena kuwapongeza wana-CCM kote nchini kwa ushindi tuliopata.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema kuwa huu ni Mkutano Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama chetu. Mkutano Mkuu wa CCM wa Taifa ndiyo kikao kikubwa zaidi kuliko vyote vya Chama; na kina madaraka ya mwisho kwa mujibu wa Katiba. Kwa kuzingatia hilo, na kwa kuwa Chama chetu ni Chama Tawala, ni dhahiri kuwa Mkutano huu ni muhimu sana. Maamuzi yatakayofanywa na Mkutano huu yatakuwa na athari (impact) sio tu kwenye Chama chetu bali Taifa letu kwa ujumla.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu na Wana-CCM Wenzangu;
Kama mnavyofahamu, Mkutano huu una ajenda kubwa tatu. Kwanza, utapokea na kujadili Taarifa ya Kazi za Chama itakayotolewa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na kutoa maelekezo ya mipango ya utekelezaji wa Siasa ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano ijayo. Aidha, Mkutano huu utapokea na kujadili Taarifa za Serikali zote mbili (yaani Muungano na Zanzibar) kuhusu utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi pamoja na uongozi wa Serikali na Nchi kwa ujumla. Vilevile, Mkutano huu utafanya uchaguzi wa Mwenyekiti wa CCM Taifa; Makamu wake wawili, mmoja wa Zanzibar na mwingine Tanzania Bara; pamoja na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa.
Na kwa mujibu wa ratiba iliyopo, Taarifa ya Kazi za Chama itawasilishwa na Katibu Mkuu wa Chama, Ndugu Abdulrahaman Kinana. Aidha, Taarifa za Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi na Uendeshaji wa Serikali zitawasilishwa na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idd kwa upande wa Serikali ya Zanzibar. Kwa sababu hiyo, hotuba yangu haitagusia sana masuala hayo. Nitajikita zaidi katika suala la uchaguzi wa Chama chetu na nitaeleza baadhi ya mambo ambayo natamani sana kuona Chama hiki kikifanya katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama mnavyofahamu, tangu mwezi Aprili mwaka huu Chama chetu pamoja na Jumuiya zake zote tatu (Umoja wa Wazazi, Umoja wa Wanawake na Umoja wa Vijana) kimekuwa kwenye zoezi muhimu la uchaguzi. Tulianza uchaguzi kwenye ngazi ya mashina, kisha tukaelekea kwenye ngazi ya tawi, kata, wilaya na mkoa; na kwenye Jumuiya, uchaguzi tayari umekamilika hadi katika ngazi ya Taifa. Nimefarijika sana kuona kuwa katika zoezi hili la uchaguzi wagombea wengi walijitokeza, tena wengi sana. Hii inathibitisha ukukomavu wa demokrasia ndani ya Chama chetu.
Baada ya kukamilisha uchaguzi wa Chama kuanzia ngazi ya shina hadi mkoa; na kwa upande wa Jumuiya hadi ngazi ya Taifa; sasa tunakwenda kuhitimisha zoezi la uchaguzi wa Chama katika ngazi ya Taifa. Kama nilivyotangulia kusema, Mkutano huu utamchagua Mwenyekiti wa CCM Taifa; Makamu Wenyeviti wawili, pamoja na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa. Na nawaomba ndugu wajumbe mchague kwa umakini. Usimchague mtu kwa sababu ya urafiki, udini, ukabila, ukanda, au kwa kutegemea kupata maslahi fulani fulani binafsi. Zaidi ya hapo, kamwe! Narudia tena, kamwe, msimchague mtoa rushwa. Ahadi Namba 3 ya mwana- CCM inasema, nanukuu, “rushwa ni adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa”, mwisho wa kunukuu.
Ndugu zangu wana-CCM, Chama chetu kimedhamiria kwa dhati kabisa kupambana na rushwa. Hivi majuzi mmesikia wenyewe tulitengua matokeo ya kura za maoni ya kupata mgombea wa Ubunge kule Singida baada ya kupatikana kwa tuhuma za rushwa. Na niwahakikishie kuwa, hata kwenye uchaguzi huu, endapo itathibitika kuna wagombea wameshinda kwa kutoa rushwa, hatutasita kutengua. Rushwa ni kansa. Rushwa ni adui wa haki. Ninyi wenyewe ni mashahidi kuwa kuna wakati ilikuwa vigumu kwa mtu kwenye Chama chetu kupata uongozi bila kutumia rushwa. Lakini, nimeshukuru sana Mwenyekiti Mstaafu Mzee Kikwete, kama isingekuwa uimara wake mimi nisingepata nafasi hivyo. Ahsante sana Mzee Kikwete. Hivyo basi, nawasihi sana wana-CCM wenzangu, msimchague mtoa rushwa. Badala yake, chagueni watu waadilifu, wachapakazi, wasio endekeza makundi na wenye mapenzi ya dhati kwa Chama chetu.
Ndugu Wana-CCM wenzangu;
Nafahamu kuwa jukumu langu leo ni kufungua Mkutano wetu. Lakini kabla sijafanya hivyo, ninayo masuala mawili ambayo ningependa kueleza. Suala la kwanza, linahusu zoezi la uchaguzi tulilolifanya ndani ya Chama chetu mwaka huu. Kwenye uchaguzi wowote ule kuna kushinda au kushindwa. Hivyo basi, wakati tunaelekea kuhitimisha zoezi la uchaguzi kwenye Chama chetu, ninalo ombi moja kwenu. Uchaguzi huu tulioufanya kwenye Chama chetu kuanzia mwezi Aprili 2017 hadi mwezi huu wa Desemba 2017 usiwe chanzo cha mifarakano au kuvurugika kwa umoja na mshikamano ulioanza kujengeka ndani ya Chama chetu. Bali utuimarishe na kutufanya kuwa wamoja zaidi.
Tuwapongeze wale walioshinda; na napenda kutumia fursa hii kuwapongeza wale wote waliochaguliwa kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi kwenye Chama pamoja na Jumuiya zake. Hongereni sana. Ushindi mlio upata ni uthibitisho wa imani kubwa waliyonayo wana-CCM juu yenu.
Kwa wale ambao kura hazikutosha, msikate tamaa au kuwa wanyonge. Kama nilivyosema, kwenye uchaguzi wowote kuna kushinda na kushindwa. Safari hii kura hazikutosha; lakini huenda kwenye uchaguzi ujao, nanyi mkaibuka washindi. Hivyo, jambo la msingi kwenu hivi sasa ni kuchapakazi kwa bidii na kuwaunga mkono viongozi waliochaguliwa. Na niwaombe sana ndugu wajumbe na wana-CCM kwa ujumla, sasa tuyavunje makundi yote tuliyoanzisha wakati wa Uchaguzi. Uchaguzi umekwisha. Wakati wa kampeni umekwisha. Sasa, tunatakiwa tuchape kazi ili kukiimarisha zaidi Chama chetu. Napenda kutumia fursa hii kueleza kuwa, kamwe; narudia tena, kamwe, Chama hakitamvumilia mtu yeyote mwenye kuendeleza makundi. Awe ni kiongozi aliyechaguliwa, awe mgombea aliyeshindwa ama mwanachama wa kawaida.
Ndugu Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Suala la pili ambalo ningependa kueleza linahusu maono niliyonayo ya namna ambayo natamani Chama chetu kifanye kazi katika kipindi cha miaka mitano ijayo. Na hili, nitalieleza kwa kirefu kidogo. Hivyo, nawaomba ndugu wajumbe mnivumilie kiasi.
Ndugu wajumbe na wana-CCM wenzangu, Mkutano wetu huu Mkuu wa Tisa wa Taifa unafanyika katika mazingira ya kipekee sana. Ni ya kipekee kwa sababu, kwanza, unafanyika katika kipindi ambacho Chama chetu kimetimiza miaka 40. Pili, unafanyika wakati nchi yetu imetimiza miaka 25 tangu kurejeshwa kwa Mfumo wa Vyama vingi. Na tatu, ambalo nadhani ni kubwa na muhimu zaidi ni kwamba, Mkutano huu unafanyika katika mwaka ambao Chama kimeanza kutekeleza Awamu ya Nne ya Mradi wa kuimarisha na kujenga uhai wa Chama.
Kama mnavyofahamu, ukiachilia mbali suala la ukongwe na kukomaa kidemokrasia, kama ambavyo nimeeleza awali; sifa nyingine muhimu na kubwa zaidi ya CCM, ni utaratibu wake wa kujitathmini na kujikosoa mara kwa mara, na kisha kufanya mageuzi yanayokwenda sambamba na wakati na hali halisi. Ni kutokana na ukweli huo, tangu imeanzishwa mwaka 1977, CCM imetekeleza awamu tatu za miradi ya kujenga na kuimarisha Chama. Mradi wa kwanza ulitekelezwa kati ya mwaka 1985 hadi 1987, ambapo Mwenyekiti wa wakati huo, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alizunguka nchi nzima kwa lengo la kukiimarisha Chama, hususan katika ngazi za chini.
Na wakati akihitimisha Awamu hiyo ya Kwanza, Baba wa Taifa alitangaza kuzindua Awamu ya Pili ya Mradi wa kuimarisha Chama, ambao pamoja na masuala mengine, ulihimiza Chama katika ngazi zote na kujenga itikadi; kuwa na mpango kazi unaotekelezwa; na kuimarisha mfumo wa nidhamu na demokrasia ndani ya Chama. Awamu ya Tatu ya Mradi wa kujenga na kuimarisha Chama ilianza kufuatia hotuba aliyotoa mtangulizi wangu, Mwenyekiti Mstaafu, Mzee Kikwete, wakati wa kupokea Uenyekiti wa Chama hapa hapa Dodoma tarehe 25 Juni, 2006. Msisitizo katika Awamu hii ilikuwa kujenga uongozi imara kwa kuhakikisha kuwa nafasi zote za uongozi ndani ya Chama zinakamilika; na viongozi wanakuwa mfano wa kuigwa kwa kuonesha njia.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Wakati Chama kikiendelea kutekeleza Awamu ya Tatu ya uimarishaji Chama, kutokana na mabadiliko na changamoto mbalimbali, haja ya kukifanyia Chama chetu mageuzi makubwa ya kimfumo, muundo na utendaji ilijitokeza. Hivyo basi, kufuatia majadiliano ya kina na ya muda mrefu yaliyofanyika; na hususan baada ya Chama kutazama itikadi yake, mwenendo wake, matendo yake, dhamira yake, malengo yake pamoja na kuangalia nidhamu ya viongozi wake. Na baada ya Chama kusikiliza sauti ya wanachama na wananchi kwa ujumla. Kama mnavyofahamu, Chama hiki ni cha wananchi wote. Hatimaye, mwezi Machi mwaka huu (2017), Chama chetu kilikubali kufanya mageuzi kupitia Mkutano Mkuu.
Mageuzi yaliyofanyika yamejikita katika mawanda makubwa matatu: mfumo, muundo na utendaji. Msingi mkuu wa mageuzi haya ni kukirejesha Chama kwa wanachama ili kukifanya kuwa kimbilio la wananchi. Na malengo mahususi ya mageuzi tuliyofanya ni kuongeza tija na ufanisi katika utendaji wa Chama, uwajibikaji miongoni mwa viongozi; pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji wa Chama.
Mambo muhimu yaliyozingatiwa katika mageuzi haya ni kupunguza idadi ya vikao na wajumbe wa vikao ili kuondoa urasimu, kuongeza tija ya vikao husika na halikadhalika kupunguza gharama. Kwa kuwakumbusha tu, tumepunguza idadi ya wajumbe wa Mkutano huu Mkuu kutoka 2,422 hadi 1,706. Tumepunguza wajumbe wa Halmashauri Kuu kutoka 388 hadi 163; na Kamati Kuu kutoka 34 hadi 26. Tumefanya hivyo, ili viongozi watumie muda mwingi kushughulikia matatizo ya wanachama na wananchi kwa ujumla, badala ya kutumia muda mwingi kukaa ofisini na kushiriki kwenye vikao.
Tunaamini kuwa, endapo Chama kitaweza kushughulikia vizuri matatizo ya wananchi, kitaweza kuwavuta watu wengi zaidi kujiunga nacho. Katika mageuzi tuliyofanya pia, tumefuta utaratibu wa mtu mmoja kuwa na vyeo zaidi ya kimoja. Tumefuta vyeo ambavyo havikuwepo Kikatiba (kamanda, mlezi, n.k). Mageuzi tuliyoyafanya pia yamehimiza uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa viongozi na wanachama, pamoja na kusisitiza Chama chetu kujitegemea kiuchumi. Ili kuhakikisha kuwa mageuzi tuliyofanya yanapata msingi wa kisheria, tumelazimika kuifanyia marekebisho Katiba ya Chama pamoja na Jumuiya zake.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Sio siri kuwa mageuzi tuliyoyafanya mwaka huu ni makubwa sana. Na ni lazima tuyasimamie. Na watu wa kwanza ambao watawajibika kuyasimamia ni viongozi ambao wamechaguliwa kushika nafasi mbalimbali hivi karibuni. Napenda kutumia fursa hii kuwasisitiza viongozi wote wa Chama waliochaguliwa kwenda kusimamia mageuzi tuliyoyafanya. Na niseme tu kuwa binafsi nitafurahi sana endapo viongozi waliochaguliwa wataweza kusimamia masuala makubwa manne, ambayo Mkutano huu ukiridhia unaweza kuyafanya kuwa ndiyo malengo makuu ya Mradi wa Awamu ya Nne ya kujenga na kuimarisha Chama.
Suala la kwanza kabisa, ni kukiimarisha Chama chetu kwa kuongeza idadi ya wanachama. Kama mnavyofahamu, lengo kuu la Chama chochote cha siasa ni kushinda uchaguzi na kushika Dola. Na katika nchi ya kidemokrasia kama yetu, mtaji pekee wa kufanikisha hili ni kwa Chama kuhakikisha kinakuwa na idadi kubwa ya wanachama, wapenzi na washabiki. Hivyo basi, viongozi mliochaguliwa, jukumu lenu la kwanza, ni kuhakikisha kuwa mnaongeza idadi ya wanachama, wapenzi na washabiki wa Chama chetu katika maeneo yenu. Tunataka ikifika wakati wa uchaguzi, washindani wetu, wasiambulie chochote.
Jambo la pili, ambalo naomba viongozi waliochaguliwa kulisimamia ipasavyo, ni katika kuhakikisha kuwa Chama chetu kinajitegemea kiuchumi. Chama chetu ni kikubwa na kikongwe. Hivyo, ni aibu kwa Chama hiki kuwa tegemezi. Kwa sababu hiyo, natoa wito kwa viongozi wote waliochaguliwa kuhakikisha Chama chetu kinajitegemea kiuchumi. Hivyo, tuwahimize wanachama waliopo kwenye maeneo yenu kulipa ada zao za mwaka. Na njia nzuri ya kuwashawishi wanachama kulipa ada ni kuhakikisha kunakuwa na uwazi katika ukusanyaji na matumizi wa mapato. Watu wanataka waone fedha zao wanazotoa zimeenda na kufanya nini. Sambamba na kuweka uwazi kwenye mapato na matumizi, jengeni utamaduni wa kuwatembelea wanachama. Msikae ofisini kuwasubiri wanachama walete michango. Na niwaombe wana-CCM wenzangu tujitahidi kulipa ada zetu za mwaka. Zama za kusubiria matajiri watulipie ada zetu wakati wa kampeni, zimepitwa na wakati. Ni lazima sisi wenyewe tujitoe. Chama kitajengwa na wenye chama, siyo matajiri wachache.
Njia nyingine ya kuhakikisha Chama kinajitegemea kiuchumi ni kusimamia vizuri rasilimali za Chama. Kama ambavyo nimesema mara kadhaa, Chama hiki kina rasilimali nyingi: viwanja vya michezo, majengo, mashamba, n.k.; lakini kwa bahati mbaya, kwa muda mrefu, rasilimali hizi hazijakinufaisha Chama chetu. Hii imetufanya, tutegemee zaidi ruzuku na michango ya wahisani. Mathalan, mapato ya Chama kwa mwaka wa fedha 2014/2015 ilikuwa takriban shilingi bilioni 29.35. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 21.95 ni ruzuku na michango ya hiari. Mwaka 2015/2016, mwaka wa uchaguzi, mapato yalikuwa shilingi bilioni 73.19, ambapo ruzuku na michango ya hiari ni shilingi bilioni 56.82; na katika mwaka 2016/2017, mapato yalikuwa shilingi bilioni 40.01, ambapo ruzuku na michango ya hiari ni shilingi bilioni 27.56. Hii inadhihirisha kuwa uwezo wetu wa kujitegemea ni mdogo. Ni lazima turekebisha hali hii, na kwa bahati nzuri tumeanza kuchukua hatua, ikiwemo kufanya uhakiki wa mali zetu zote, halikadhalika tupo mbioni kuanzisha mfumo wa kielektroniki utakaokiwezesha Chama kutambua na kusimamia rasilimali na mali zake zote, mapato na kusimamia uendeshaji kwa ujumla. Hivyo basi, niwaombe viongozi wapya mkaendeleze jitihada zilizoanzishwa.
Sambamba na hilo, viongozi wapya hamna budi kubuni miradi mipya. Na katika hili, niseme tu kwamba, itakuwa aibu kwa Chama chetu, ambacho Serikali yake inahubiri ujenzi wa uchumi wa viwanda, tutashindwa hadi ikifika mwaka 2020 kuanzisha angalau kiwanda kimoja.
Tatu, nawasihi sana viongozi wapya, kila mtu mahali pake alipo, ahakikishe kuwa Chama chetu kinakuwa kiungo kati ya Serikali na wananchi. Chama, hususan Chama tawala kama chetu, kinao wajibu wa msingi wa kuwaeleza na kuwafafanulia wananchi umuhimu wa utekelezaji mipango na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali. Zaidi ya hapo, kinao wajibu wa kuchukua maoni, mapendekezo na kero mbalimbali za wananchi na kuziwasilisha Serikalini. Niwe mkweli, hivi sasa, Chama chetu hakitekelezi vizuri jukumu hili. Tumekuwa hodari sana wa kufanya kampeni na kuhakikisha Chama kinashinda uchaguzi. Lakini, baada ya hapo, huwa tunajiweka pembeni, ama kwa kuvaa sura ya Userikali au kwa kuwaogopa watendaji wa Serikali. Nilisema kwenye Mkutano Mkuu uliopita, viongozi wa Chama hawapaswi kuwaogopa watendaji wa Serikali, hususan katika kutetea maslahi ya wananchi wanyonge.
Katika kusisitiza umuhimu wa Chama chetu kuwa kiungo kati ya Serikali na wananchi, napenda ninukuu maneno yafuatayo, ambayo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyatamka tarehe 7 Juni, 1968 alipohutubia Mkutano Mkuu wa Chama cha Uganda People’s Congress, na nitanukuu kwa lugha yetu adhimu ya Kiswahili:“Kazi ya Chama kilicho imara ni kuwa daraja linalowaunganisha wananchi na Serikali yao. Ni wajibu wa Chama kuwasaidia wananchi kuelewa Serikali yao inafanya nini na kwanini; na kuwashawishi wananchi kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali yao, ikiwemo kuondoa umaskini wao....Zaidi ya hapo, Chama kina jukumu au wajibu wa kuwasemea wananchi (The Party must speak for the people)”, mwisho wa kunukuu.
Hivyo basi, nawasihi sana viongozi wapya, nendeni makatekeleze jukumu hili ipasavyo. Pongezeni pale inapobidi kupongeza, na kosoeni inapobidi. Na ili muweze kutekeleza jukumu hili vizuri, hakikisheni kuwa mnakuwa karibu na wananchi, lakini pia mnaifahamu vizuri mipango ya Serikali na mikakati ya kutekeleza mipango hiyo, ikiwemo bajeti zinazotengwa. Nitashangaa na kwa kweli nitasikitika, kama nitaona wananchi wanadai kufahamishwa mapato na matumizi ya Serikali ya Kijiji, huku Mwenyekiti wa CCM wa Shina au Tawi yupo; nitashangaa wananchi walalamike kuhusu ubadhirifu katika ujenzi wa kituo cha afya au shule wakati Mwenyekiti wa CCM na Kamati ya Siasa ya Kata wapo; na vilevile nitashangaa wananchi kushindwa kuelewa umuhimu wa kununua ndege, kujenga reli ya standard gauge na mradi wa umeme wa Stiglier’s Gorge wakati kuna Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Mkoa na Wajumbe wa Halmashauri Kuu na Mbunge wa CCM. Nitashangaa sana. Na niwaombe viongozi wa Serikali kutoa ushirikiano na ufafanuzi kwa viongozi wa Chama. Lakini ningependa pia kusema kuwa wana-CCM mkitaka kukosoa jambo linalofanywa na Serikali, mkumbuke kuwa ninyi ni Chama Tawala. Mnazo njia nyingi za kufikisha mapungufu mnayoyaona kwenye Serikali. Kuna usemi ambao Umoja wa Wazazi hupenda kuutumia, usemao “Uchungu wa Mwana, Aujuaye Mzazi”. CCM Oyeee! Mapinduzi, Daima mbele!
Jambo la nne, na la mwisho lakini sio kwa umuhimu, ambalo ningependa viongozi wapya mlipe mkazo unaostahili, ni uadilifu. Na uadilifu unapaswa kuanza na ninyi. Kiongozi anapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwa wanachama na wananchi kwa ujumla. Haifai, na kwa kweli, kamwe Chama hakitamvumilia kiongozi au mwanachama wa CCM mwenye kutuhumiwa au kujihusisha na vitendo vya rushwa, utapeli, wizi, ubadhirifu, ujambazi, ulevi uliopindukia, kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya, n.k. Upo usemi wa enzi usemao “Mke wa Mfalme hapaswi hata kuhisiwa kuwa anachepuka”. Hivyo basi, kama kuna viongozi wa namna hiyo wamechaguliwa, ni vyema wakajirekebisha.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema, taarifa ya Utekelezaji wa Ilani na uendeshaji wa Serikali zitawasilishwa na Waziri Mkuu na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Hata hivyo, napenda nitumie fursa hii kueleza mambo machache kuhusiana na masuala hayo. Kwanza kabisa, kama mnavyofahamu, jukumu kubwa la Serikali zetu mbili ni kuhakikisha amani, umoja na Muungano wa nchi yetu unadumishwa. Hii pia ni moja ya ahadi zilizopo kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi. Bila shaka, mtakubaliana nami kuwa Serikali zetu mbili zimeweza kutekeleza jukumu na ahadi hii kikamilifu. Nchi yetu ipo salama na ina utulivu. Muungano wetu upo imara. Na watanzania tumeendelea kuwa wamoja. Watu wachache waliojaribu kutishia amani, Muungano na umoja wetu tumewadhibiti kikamilifu.
Suala la pili ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu utekelezaji wa ahadi kubwa ya uchaguzi ya kujenga nchi ya uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025. Ahadi hii nayo tunaitekeleza vizuri. Uchumi wetu unaendelea kuimarika, ambapo nchi yetu ni miongoni mwa nchi chache barani Afrika ambao uchumi wake unakua kwa kasi. Aidha, mfumuko wa bei unaendelea kushuka, ambapo mwaka huu mwezi Novemba ulishuka kumefikia asilimia 4.4. Vilevile, akiba ya fedha za kigeni imefikia Dola za Marekani milioni 5,820.4 mwezi Septemba 2017. Kiasi hiki kinaiwezesha nchi yetu kulipia gharama ya kununua bidhaa kwa miezi mitano. Hii ina maana kwamba leo hii Watanzania tunaweza kukaa bila kufanya kazi yoyote kwa miezi mitano na tukaendelea kupata huduma kama kawaida. Lakini hii haimanisha kwamba watu waache kufanya kazi. Ni lazima tuendelee kufanya kazi. Kama maandiko matakatifu yanavyosema, asiye fanyakazi na asile. Nanyi mnafahamu kuwa mtu asiye kula maana yake atakufa.
Kuhusu ujenzi wa Viwanda, kwa kipindi cha miaka 2 iliyopita takriban Viwanda vipya 3,306 vimejengwa, na hizi ni takwimu za mwezi Juni 2017. Lakini jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba viwanda vingine vinajengwa na hata vile vya zamani vimeanza kufufuliwa. Mathalan, Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii (NSSF, ZSSF, PSPF, GEPF, Bima ya Taifa ya Afya, LAPF na WCF) hivi sasa inatekeleza miradi takriban 15 ya viwanda, ambavyo nimeambiwa kuwa vitazalisha takriban ajira 350,000. Baadhi ya miradi ni ulimaji wa mashamba ya Miwa na ujenzi wa Viwanda vya Sukari vya Mkulazi na Mbigiri mkoani Morogoro, ambako pia kutakuwa na uzalishaji wa umeme utakaoingizwa kwenye Gridi ya Taifa; Ufufuaji wa Vinu vya Kusindika Nafaka na Ukamuaji Mafuta vya Shirika la Usagishaji la Taifa (National Milling Corporation – NMC) vilivyopo hapa Dodoma, Iringa na Mwanza; Ufufuaji wa Kiwanda cha Bidhaa za Ngozi pale Karanga, Moshi Mjini; Kiwanda cha Katani na Agave Syrup itokanayo na mabaki ya mkonge Mkoani Tanga; Kiwanda cha Madawa TPI Arusha; Kiwanda cha Kutengeneza Matofali ya Kuchoma na Vigae hapa Dodoma; Kiwanda cha Kusindika Tangawizi Kilimanjaro; Kiwanda cha Nyama cha Nguru Ranch Morogoro; Kiwanda cha Mvinyo wa Zabibu hapa Dodoma; Kiwanda cha bidhaa za hospitali (pamba na maji tiba) Simiyu, n.k. Naipongeza Mifuko hii kwa kuitikia wito wa Serikali wa kujenga viwanda. Na hii ndio sababu nahimiza Chama chetu nacho kushiriki katika utekelezaji wa ahadi hii.
Ndugu Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu;
Wageni wetu Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Nimezungumza mengi. Hivyo basi, napenda nihitimishe hotuba yangu kwa kuwashukuru wajumbe wa Mkutano huu kwa kuhudhuria kwa wingi. Aidha, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru, Makamu wangu wawili, Mheshimiwa Dkt. Shein na Mzee Mangula kwa ushirikiano mkubwa walionipa tangu nilipochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chama chetu mwezi Julai mwaka jana. Nimejifunza na naendelea kujifunza mambo mengi kupitia kwao. Lakini, kwa namna ya pekee, namshukuru Mzee Kinana pamoja na Sekretarieti ya Chama kwa ujumla kwa kunisadia katika kutenda kazi za Chama na kufanya mageuzi mbalimbali. Nakushukuru sana Mzee Kinana. Na ni matarajio yangu kuwa Mzee huyu ataendelea kunisaidia katika kazi.
Napenda pia kutumia fursa hii, kuwashukuru wageni wetu waalikwa, Wawakilishi pamoja na Mabalozi mnaowakilisha Vyama Rafiki vya CCM kutoka nchi mbalimbali. Tunawashukuru sana kwa kushiriki nasi katika Mkutano huu. Napenda pia kuwashukuru wawakilishi wa vyama shindani mliohudhuria Mkutano huu. Mmeonesha ukomavu mkubwa wa kisiasa. Licha ya tofauti zetu za kiitikadi, lengo letu sisi sote ni kuijenga nchi yetu. Hii ndio sababu nimefarijika sana kwa kuja kuhudhuria Mkutano huu. Ahsanteni sana. Maendeleo hayana Chama japo naamini kuwa maendeleo ya kweli yataletwa na CCM.
Nitumie fursa hii pia kuwashukuru viongozi wetu wastaafu, wakiwemo Wenyeviti na Makamu Wenyeviti Wastaafu, Makatibu Wakuu Wastaafu, pamoja na na wazee wetu wengine, wakiwemo mama zetu wapendwa, Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume kwa kuja kushiriki nasi kwenye Mkutano huu. Tunawashukuruni sana.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwashukuru viongozi na wanachama wapya ambao wamejiunga na Chama chetu hivi karibuni. Na napenda kuwaarifu kuwa wapo wengi wanaotamani sana kujiunga na Chama chetu.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa Mkutano Mkuu wa Tisa wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi umefunguliwa rasmi hapa Dodoma. Nawatakia wajumbe wenzangu Mkutano mwema na maamuzi ya busara.
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!
Mapinduzi, Daima!
Mungu Wabariki Wajumbe wa Mkutano huu!
Mungu Ibariki CCM!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Dec 14, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA CHAMA CHA WALIMU TANZANIA (...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Mwalimu Leah Ulaya, Kaimu Rais
wa Chama Cha Walimu Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Seleman Jafo, Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais – TAMISEMI;
Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu
na Mafunzo ya Ufundi;
Mheshimiwa George Mkuchika, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais – UTUMISHI;
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu;
Waheshimiwa Mwalimu Janet Magufuli,
Mke wa Rais, na Mwalimu Mary Majaliwa, Mke wa Waziri Mkuu;
Mheshimiwa Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Mheshimiwa Makatibu Wakuu mliopo;
Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama
vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);
Ndugu Katibu Mtendaji wa Tume ya Utumishi wa Walimu;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi
mliohudhuria kutoka Ndani na Nje ya Tanzania;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa
wa Chama Cha Walimu Tanzania;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote napenda niwashukuru sana walimu kwa kunikaribisha. Kwangu mimi, leo ni siku ya pekee sana. Na nakiri kwamba nimefurahi sana. Nimefurahi, kwanza, kwa kupata fursa hii adhimu ya kuzungumza nanyi walimu wenzangu. Kama mnavyofahamu, mimi ni mwalimu. Mke wangu naye ni mwalimu. Nazijua shida na raha za ualimu. Hivyo basi, kuwepo mahali hapa, ni faraja kubwa kwangu. Lakini, jambo la pili lililonifurahisha ni kwamba, sasa nimetambua kuwa Chama Cha Walimu kimedhamiria kufanya kazi na Serikali. Ahsanteni sana walimu wenzangu. Na napenda kutumia fursa hii kuwahikikishia kuwa Serikali itashirikiana na ninyi kwa karibu.
Kabla sijaendelea zaidi, napenda nami niungane nanyi katika kutoa salamu zangu za pole kwa familia, ndugu na jamaa wa Marehemu Alhaji Yahya Msulwa, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CWT, ambaye aliaga dunia tarehe 17 Novemba, 2017, wakati akiwa kwenye maandalizi ya Mkutano huu. Sambamba na hilo, kama mnavyofahamu, leo nchi yetu imeiaga rasmi miili ya askari wetu mashujaa 14 waliouawa hivi karibuni nchini DRC wakiwa katika ulinzi wa amani. Hivyo basi, naomba tuzidi kuwaombea mashujaa wetu roho zao zipumzike mahali pema pepoi. Aidha, tuwaombee mashujaa wengie waliojeruhiwa kwenye tukio hilo ili wapone kwa haraka. Amina.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Walimu Wenzangu;
Leo ni mara yangu ya kwanza kukutana rasmi na walimu tangu nimechaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano ya Nchi yetu. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru walimu kote nchini kwa kura nyingi mlizonipa zilizoniwezesha kuibuka mshindi kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita. Ahsanteni sana walimu wenzangu. Nawaahidi kufanya kazi kwa bidii kwa manufaa ya Watanzania wote.
Napenda pia kutumia fursa hii, kutoa shukrani zangu nyingi kwa uongozi wa CWT kwa uamuzi wenu wa kuhamishia Mkutano huu hapa Dodoma. Kama mnavyofahamu, Mkutano huu awali ulipangwa kufanyika Arusha. Lakini baadaye, mliamua kuuhamishia hapa Dodoma. Nawashukuru sana. Hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya nchi yetu. Hapa pia ni Makao Makuu ya Ofisi za Bunge. Aidha, hapa ni mahali ambako, chuo kikubwa zaidi katika eneo zima la Afrika Mashariki na Kati, Chuo Kikuu cha Dodoma, kipo. Hivyo basi, nina imani kuwa Wajumbe wa Mkutano wamefurahi kuja kufanya mkutano wao hapa Dodoma.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sekta ya elimu ni nyeti na muhimu katika jamii na pia kwa maendeleo ya Taifa lolote. Sisi Waswahili tuna msemo usemao “Elimu ni Ufunguo wa Maisha”. Marafiki zetu Wachina nao wana msemo usemao, naomba niunukuu kwa Lugha yetu adhimu ya Kiswahili, “Ukitaka kuwekeza kwa mwaka mmoja, panda mpunga; Ukitaka kuwekeza kwa miaka kumi, panda miti; lakini ukitaka kuwekeza katika maisha, wekeza kwenye elimu”. Hii yote ni katika kudhihirisha kuwa elimu ni muhimu kwa mtu mmoja mmoja, katika jamii na kwa maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Na bila shaka, kwa kutambua umuhimu huo, Serikali za Awamu zote za nchi yetu, ya kwanza hadi ya sasa, imeweka mkazo mkubwa katika kukuza na kuboresha sekta hii. Juzi kwenye Maadhimisho ya Sherehe za Uhuru nimeeleza kuwa wakati tunapata Uhuru, mwaka 1961, baada ya utawala wa Kikoloni uliodumu kwa takriban miaka 76, nchi yetu ilikuwa na shule za msingi 3,100. Lakini katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru wetu, tumeweza kujenga shule za msingi mpya 14,279 na hivyo kutufanya tuwe na jumla ya shule za msingi 17,379. Katika kipindi hicho Shule za sekondari zilikuwa 41, lakini hivi sasa zipo 4,817. Tulikuwa na Chuo Kikuu kimoja, lakini leo hii tuna vyuo vikuu 48.
Mtakubaliana nami kuwa haya ni mafanikio makubwa sana. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi zangu nyingi kwa viongozi wa awamu zote za nchi yetu kwa kufanikisha kupatikana kwa mafanikio haya. Pamoja na pongezi hizo nilizozielekeza kwa viongozi watangulizi wangu, upo usemi usemao “unaweza kuwa na shule, chuo au chuo kikuu bila ya kuwepo kwa majengo, vitabu, madawati, maabara, chaki na kalamu; lakini kamwe huwezi kuwa na shule au chuo bila ya walimu”. Kwa maana hiyo, pongezi nyingi zaidi inafaa ziwaendee ninyi walimu. Hivyo basi, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania napenda kutumia fursa hii kutoa pongezi nyingi sana kwenu walimu kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya ya kuwaelimisha Watanzania. Kwa hakika, walimu mnafanya kazi kubwa sana. Hongereni na ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CWT;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyotangulia kusema hapo awali, Serikali za Awamu zilizotangulia zimefanya juhudi kubwa za kukuza na kuendeleza sekta ya elimu nchini. Kwa lengo la kuendeleza mafanikio hayo, na sisi Serikali ya Awamu ya Tano tunachukua hatua mbalimbali za kupanua wigo na kuboresha sekta ya elimu. Kama mnavyofahamu, hivi sasa tunatekeleza elimu bila malipo kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo awali tulikuwa tukitenga shilingi bilioni 18.77 kwa mwezi kugharamia, lakini kuanzia mwezi Julai 2016 tuliongeza fedha hizo hadi kufikia shilingi bilioni 23.868. Hii maana yake ni kwamba, tangu utaratibu huu uanze mwezi Desemba 2015 hadi Novemba 2017, Serikali imetumia kiasi cha takribani shilingi bilioni 535.
Ninyi walimu ni mashahidi wazuri. Uamuzi wa Serikali wa kuanzisha elimu bila malipo, umeleta mafanikio makubwa sana, hususan katika kuongeza idadi ya wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza na kidato cha kwanza. Lakini, kutokana na ongezeko hilo la wanafunzi, zilijitokeza changamoto, ikiwemo upungufu wa madawati, vyumba vya madarasa, pamoja na vifaa na vitendea kazi vingine. Kutokana na matatizo hayo, Serikali ilianza kuchukua hatua ili kushughulikia.
Tulishirikiana na wadau mbalimbali, wakiwemo wananchi, na kuweza kupunguza kwa takriban asilimia 95 tatizo la madawati kwenye shule zetu za msingi na sekondari nchini kote. Aidha, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, Serikali imejenga na kukarabati miundombinu katika shule za msingi na sekondari 365, zikiwemo shule za sekondari kongwe 88; kwenye halmashauri 129. Miundombinu hiyo ni nyumba za walimu 12, vyumba vya madarasa 1,435, mabweni 261, majengo ya utawala 11, mabwalo 6, matundu ya vyoo 2,832, maktaba 4, na visima vya maji safi 4. Aidha, katika bajeti ya Mwaka huu wa Fedha 2017/2018, Serikali, kupitia bajeti ya Halmashauri, imetenga shilingi bilioni 126.65 kwa ajili ya kujenga na kukarabati miundombinu ya shule za msingi na sekondari, itakayojumuisha nyumba za walimu 2,364; madarasa 6,636; vyoo 9,355; madawati 118,921; mabweni 157; hosteli 176 na maabara zipatazo 1,817. Waheshimiwa Mawaziri wahusika hakikisheni haya yanatekelezwa.
Sambamba na hayo, tumeanza kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha elimu yenyewe. Ninyi walimu ni mashahidi, mwaka huu wa 2017 tumegawa vifaa vya maabara kwenye shule za sekondari 1,696 pamoja na vifaa vya wanafunzi wenye mahitaji maalum katika shule za msingi 213 na shule za sekondari 22.
Ukiachilia mbali Elimu ya Msingi na Sekondari, Serikali pia inaboresha Elimu ya Juu, hususan kwa kutoa mikopo kwa wanafunzi. Idadi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu wanaopewa mikopo imeongezeka kutoka 98,300 mwaka 2015 hadi kufikia takriban 124,000 hivi sasa. Hii imewezekana baada ya Serikali kuongeza bajeti ya mikopo kutoka shilingi bilion 373 hadi kufikia shilingi bilion 483. Wanafunzi walimu wanaonufaika na mikopo ya elimu ya juu ni 22,867, ambapo mwaka huu Serikali itatumia shilingi billion 79.63 kuwagharamia. Na ninyi wenyewe ni mashahidi kuwa hivi sasa mikopo inatolewa kwa wakati; na hata rufaa za mikopo hivi sasa zinashughulikiwa mapema. Wito wangu kwa walimu wanaopata mikopo; wakimaliza, wakubali kufanya kazi kwenye vituo wanavyopangiwa.
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Mbali na kupanua wigo na kuboresha sekta ya elimu, tunafanya jitihada za kuboresha maslahi na kushughulikia kero mbalimbali za walimu. Hivi punde mmemsikia Kaimu Katibu Mkuu wa CWT akiipongeza Serikali kwa jitihada inazofanya kuboresha maslahi ya walimu na kushughulikia kero mbalimbali zinazowakabili. Mathalan, ameipongeza Serikali kwa kutoa Waraka wa Muundo Mpya wa Watumishi wa Walimu; Upandishwaji madaraja ya Walimu; uanzishaji wa Tume ya Utumishi wa Walimu, n.k.
Lakini, licha ya hatua hizo, Serikali pia imefanya mambo mengine mengi ya kuboresha maslahi na kushughulikia kero za walimu. Mathalan, awali nilieleza kuwa Serikali iliongeza kiwango cha ruzuku inayopelekwa kwenye shule kutoka shilingi bilioni 18.77 hadi shilingi bilioni 23.868 kwa mwezi. Kiasi kilichoongezeka ni mahususi kwa ajili ya kutoa posho za madaraka kwa Wakuu wa Shule na Waratibu wa Elimu Kata. Tangu utaratibu huu uanze tayari tumetoa shilingi bilioni 86.56. Niwaombe watu wanaopewa, posho hizo ziwaongezee motisha ya kufanya kazi kwa maslahi ya Taifa. Aidha, naziagiza mamlaka za uteuzi kutoa vyeo kwa watu wenye sifa na wenye kustahili.
Sambamba na hilo la kutoa posho, tangu tumeingia madarakani, tumetoa kiasi cha shilingi bilioni 56.92 kulipia madeni ya walimu, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 14.23 tumelipa madeni ya mshahara na shilingi bilioni 42.69 ni madeni yasiyo ya mshahara. Kadri tutakavyokamilisha uhakiki wa madeni, tutalipa madeni yote halali.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
NduguWajumbe wa Mkutano;
Licha ya jitihada mbalimbali zilizofanywa na Serikali katika kuimarisha sekta ya elimu na kuboresha maslahi ya walimu nchini, ni dhahiri kuwa sekta ya elimu na ninyi walimu wenyewe bado mnakabiliwa na matatizo kadhaa. Mathalan, tuna upungufu wa madarasa, vyoo, nyumba za walimu, madawati na maabara.
Sambamba na matatizo hayo, hivi punde, Kaimu Katibu Mkuu wa CWT, katika Risala yake, ameeleza matatizo na kero mbalimbali zenye kuwakabili walimu. Ametaja suala la upandishaji vyeo kwa wakati; suala la walimu waliopandishwa madaraja mwaka jana na kisha kusitishwa; malipo ya walimu wastaafu; suala la posho ya kufundishia (teaching allowance); upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi; n.k. Amezungumzia pia hofu mliyonayo walimu kuhusu uwezekano wa kupungua kwa mafao ya kustaafu kufuatia uamuzi wa kuiunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii ili ibaki miwili.
Kama nilivyotangulia kusema hapo awali, mimi ni mwalimu. Hivyo basi, hata kabla sijawa Rais, nilikuwa nikizifahamu shida na matatizo mbalimbali yanayowakabili walimu wa Tanzania. Na kama nilivyosema, Mke wangu, naye ni mwalimu; na amekuwa kila mara akinikumbusha kuhusu masuala ya walimu. Lakini, mbali na yeye, kwa bahati nzuri viongozi wengi niliowateua kushika nyadhifa mbalimbali ni walimu. Waziri Mkuu ni mwalimu. Mke wake ni mwalimu Hapa pia tunao Mawaziri Mhagama na Prof. Ndalichako, ambao wote ni walimu. Na wote hawa wamekuwa wakiwatetea sana. Lakini zaidi ya hapo, Makamu wa Rais, Mama Samia, naye ni mtetezi mkubwa sana wa walimu. Kwa hiyo, viongozi wote wamekuwa wakiwatetea sana ninyi walimu.
Na niseme tu kuwa, kutokana na kazi kubwa ambayo ninyi walimu mnayoifanya, ni haki yenu kutetewa na kwa kweli Serikali inao wajibu wa kuhakikisha inashughulikia shida na kero zenu. Mimi binafsi natamani sana; tena sana, kuona shida mbalimbali za walimu zinaisha kabisa. Hata haya, matatizo mliyonieleza leo ningetamani sana nitoe majibu yake yote hapa hapa ili yaweze kushughulikiwa mara moja. Lakini, hilo ni jambo lisilowezekana. Kama mnavyofahamu, uwezo wa Serikali bado mdogo na majukumu iliyonayo ni mengi. Mbali na kushughulikia sekta ya elimu, tunawajibika kushughulikia masuala ya afya, maji, umeme, barabara, ulinzi, n.k., ambayo yote haya ni muhimu kwa nchi, lakini pia ni muhimu hata kwenu ninyi walimu. Walimu mnahitaji huduma bora za afya, mnahitaji maji, umeme, barabara, ulinzi na usalama, n.k.
Kwa sababu hiyo, Serikali inawajibika kuhakikisha kuwa kidogo kinachopatikana, tunakigawa kwenye sekta zote muhimu. Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alipata kusema, nanukuu, “Ndama hunyonya kiwango cha maziwa ambacho mama yake anacho”. Hivyo, nawasihi sana walimu wenzangu, kwa kile kidogo tunachokileta kwenu mkipokee na kuiona dhamira nzuri ya Serikali ya kushughulikia shida na kero zenu mbalimbali. Napenda tu niwahakikishie kuwa Serikali inatambua kero zenu zote na kadri uwezo wa Serikali kifedha utakavyokuwa ukiongezeka, tutaendelea sio tu kuboresha maslahi yenu bali sekta ya elimu kwa ujumla.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano huu;
Pamoja na maelezo hayo, napenda kutolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizotolewa na Kaimu Katibu Mkuu katika Risala yake. Moja ya hoja aliyoizungumza ni uhaba wa walimu wa sayansi nchini. Ni kweli kuwa tatizo hili lipo na limeongezeka baada ya Serikali kuanza kutoa elimu bila malipo, ambapo idadi ya wanafunzi kwenye shule zetu imeongezeka. Serikali inachukua hatua mbalimbali kushughulikia tatizo hili. Mwaka huu pekee tumeajiri walimu wa masomo ya sayansi na hisabati wapatao 3,462. Aidha, walimu wengine wapatao 15,135, wakiwemo wa sayansi, wanatarajiwa kuajiriwa wakati wowote baada ya vyeti vyao kuhakikiwa na kuthibitishwa uhalali wake.
Vilevile, tunaendelea kupanua wigo wa kuzalisha walimu. Mathalan, kati ya wanafunzi 22,867 wanaosomea ualimu niliowataja awali na ambao Serikali inawapa mikopo ya vyuo vikuu, wanafunzi 13,510 ni wa masomo ya sayansi na hesabu. Zaidi ya hapo, Serikali ipo katika ukarabati wa vyuo vyake takriban 20 na ujenzi wa vyuo 3. Ujenzi na ukarabati huu utakapokamilika, utaongeza idadi ya udahili wa wanafunzi wa ualimu kutoka 20,535 hadi kufikia wanafunzi takriban 30,000. Hatua hizi, bila shaka, zitapunguza tatizo la uhaba wa walimu.
Hata hivyo, nafahamu kuwa wakati mwingine, tatizo la uhaba wa walimu linatokana na mgawanyo usio linganifu. Shule nyingi za mijini zina walimu wengi kuliko mahitaji yake. Hivyo niziombe Mamlaka husika kuliangalia suala hili kwa umakini. Lakini huu usiwe mwanya wa kuwahamisha walimu bila kufuata utaratibu. Agizo langu kuhusu kutomhamisha mwalimu mpaka atakapolipwa stahiki zake liko pale pale. Lakini pia nitoe wito kwenu walimu; mkipangiwa kazi mahali, mkubali kwenda.
Suala jingine ambalo Kaimu Katibu Mkuu amelizungumzia ni hofu mliyonayo kuhusu uwezekano wa kupungua kwa malipo ya mkupuo baada ya kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii. Hakuna kitakachopungua. Lengo la Serikali kuiunganisha mifuko ya jamii na kubakisha miwili ni kuongeza ufanisi na tija katika mifuko hiyo. Kama mnavyofahamu, kutokana na mifuko kuwa mingi, ililazimu kila mfuko kutumia fedha nyingi kutafuta wanachama. Jambo hili liliongeza gharama za uendeshaji kwenye mifuko hiyo na hivyo kusababisha mifuko hiyo kutoa mafao madogo ya kustaafu kwa wanachama wake. Sasa tumeamua kuwa na mifuko miwili tu; mmoja kwa ajili ya watumishi wa umma na mwingine sekta binafsi. Hii itasaidia sio tu kuondoa ushindani usio na tija, bali pia unatarajia kuiwezesha mifuko hii kutoa mafao mazuri zaidi kwa wanachama wake wanaostaafu. Hivyo basi, napenda kuwatoa hofu walimu wenzangu kwamba mafao hayatapungua. Lakini sambamba na hilo, sheria ya kuunganisha mifuko bado haijatungwa. Mswada umesomwa mara moja Bungeni. Na sasa maoni ya wadau mbalimbali yanaendelea kupokelewa. Hivyo, na ninyi CWT mnayo nafasi ya kuendelea kutoa maoni yenu ili kuboresha mswada huo.
Kuhusu suala la posho ya kufundishia (teaching allowance), mtakumbuka kuwa kwa mujibu wa Waraka wa Watumishi wa Serikali Na.1 wa mwaka 1996 kuhusu Mfumo, Miundo na Ngazi Mpya za Mishahara kwa Watumishi wa Serikali kuanzia tarehe 1 Julai, 1996 posho zote zilijumuishwa katika mishahara. Lengo lilikuwa kuboresha mishahara na mafao ya uzeeni ya Watumishi. Kufuatia utekelezaji wa Waraka huo, nyongeza halisi ya mshahara wa kima cha chini baada ya kujumuishwa posho katika mishahara ilikuwa ni asilimia 55.2; na nyongeza halisi ya kima cha juu baada ya kujumuishwa posho katika mshahara ilifikia asilimia 36.9. Hii ndio sababu posho ya kufundishia waliyokuwa wakipewa walimu, iliondolewa. Pamoja na maelezo hayo, natambua umuhimu wa posho hii. Hivyo, napenda kurudia tena kadri mama ndama atakapoongeza maziwa, tutaangalia uwezekano wa kurejesha posho hii ili kuwapa motisha walimu wetu. Hivyo, nawaomba Watanzania tuchape kazi kwa bidii ili kuongeza uwezo wetu kiuchumi.
Kuhusiana na suala la mafunzo kwa walimu, Serikali inafahamu umuhimu wa kuwapatia mafunzo endelevu ya mara kwa mara walimu wetu. Na kwa kweli tumekuwa tukifanya hivyo. Jumla ya walimu 5,920 wa masomo ya sayansi, hisabati na kiingereza wamepata mafunzo hivi karibuni. Na tutaendelea kutoa mafunzo hayo.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano huu;
Suala jingine ambalo ningependa nilizungumzie ni kuhusu madeni mbalimbali ya walimu. Serikali inatambua uwepo wa madeni hayo. Na tumekuwa tukiyalipa. Kama nilivyosema awali, tangu tumeingia madarakani tayari tumelipa madeni ya walimu yenye thamani ya shilingi bilioni 56.92. Lakini, madeni bado yapo. Hivi punde Kaimu Katibu Mkuu wenu ameeleza kuwa hivi sasa walimu wanaidai Serikali kiasi cha shilingi bilioni 25.6. Napenda, kwanza kabisa, kuwapongeza viongozi wa CWT kwa kuwa wakweli. Nakumbuka kuwa kuna wakati aliwahi kujitokeza mmoja wa viongozi wa CWT na kusema kuwa walimu wanaidai Serikali takriban shilingi trilioni 1.5. Hivyo, nawapongeza sana viongozi wa sasa wa CWT kwa kuwa wakweli. Na kwa kuwa mmeonesha uungwana na mmekuwa wakweli, napenda kuwahakikishia kuwa mara tu tutakapomaliza kuhakiki deni hili, tutawalipa mara moja.
Lakini pia ningependa kutumia fursa hii kueleza kuwa, Serikali imekuwa ikichelewa kulipa madeni yenu pamoja na ya watumishi wengine wa umma, kutokana na kuwepo kwa matatizo kadhaa, ikiwemo tatizo la watumishi hewa na wenye vyeti feki. Hii ndio sababu mwaka jana tuliamua kusitisha zoezi la upandishaji vyeo na madaraja kwa watumishi; na tukaanzisha zoezi la uhakiki kwa watumishi wote wa Serikali. Zoezi la uhakiki mpaka sasa limetuwezesha kubaini watumishi hewa wapatao 19,706, ambao walikuwa wakiigharimu Serikali kiasi cha shilingi bilioni 19.848 kwa mwezi, sawa na shilingi bilioni 238.17 kwa mwaka. Aidha, tumeweza kubaini watumishi wenye vyeti feki wapatao 12,000, wakiwemo walimu 3,655. Baada ya kukamilisha zoezi hili, Serikali mwezi Novemba 2017, imewapandishaji vyeo watumishi 59,967, wakiwemo walimu na ambao marekebisho ya mishahara yao itaanza kutolewa kuanzia mwezi huu. Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 159.33 kwenye bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya marekebisho hayo ya mishahara.
Na kuhusu zoezi la uhakiki wa madeni, lenyewe bado linaendelea. Na kimsingi, zoezi hili ni endelevu. Hata hivyo, nawahakikishia kuwa kadri tutakavyokuwa tunakamilisha uhakiki wa madeni tunayodaiwa, tutayalipa. Wito wangu kwenu walimu wenzangu, endapo unafahamu kuwa katika madeni uliyowasilisha Serikalini kuna udanganyifu, ni vyema ujaze upya. Na niwaombe viongozi wa CWT kupitia tena madeni yote ya walimu ili kujiridhisha; na mkijiridhisha pelekeni madeni hayo kwa viongozi wa Wilaya na Mikoa, nao wakijiridhisha na kuweka saini zao; baada ya hapo madeni hayo yawasilishwe kwa Waziri Mkuu. Nawaahidi kuwa, Serikali ikijiridhisha kuwa madeni hayo ni sahihi, tutayalipa mara moja. Lakini nitoe onyo kwamba, endapo itatokea mtu ameidhinisha madeni yenye udanganyifu, naye tutawachukulia hatua.
Kuhusiana na hoja zenu nyingine mlizoziwasilisha, ikiwemo upandishaji wa vyeo kwa wakati; Serikali kutoa mikopo ya ujenzi wa nyumba isiyo na riba; uhaba wa vifaa vya kufundishia; kushirikishwa katika mabadiliko yoyote ya mitaala; masomo ya TEHAMA; Serikali imepokea hoja zenu zote na tutashirikiana nanyi katika kuzitafutia ufumbuzi. Nafahamu baadhi ni masuala ya kiutendaji tu na hayahitaji gharama yoyote; hivyo, naziagiza mamlaka husika kushughulikia kwa haraka. Na kwa yale yenye kuhitaji fedha, tutaendelea kuyashughulikia taratibu, kadri uwezo wa Serikali kifedha utakavyokuwa ukiimarika.
Waheshimiwa Viongozi;
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Jukumu langu leo ni kufungua tu Mkutano wenu. Lakini kabla sijatekeleza suala hili, ninalo suala moja la mwisho ambalo ningependa kulizungumza. Nafahamu kuwa, kwenye Mkutano huu, pamoja na mambo mengine, mtafanya uchaguzi wa Rais wa CWT kuziba nafasi iliyoachwa wazi na Rais wenu Mstaafu, Mwalimu Gratian Mukoba. Napenda kutumia fursa hii kuwasihi sana walimu wenzangu, kuchagua kwa umakini mkubwa. Chagueni mtu atakayeshughulikia masuala yenu. Na kamwe msichague mtu mwenye nia ya kuitumia CWT kutekeleza maslahi yake binafsi.
Sio siri kuwa kuna wakati mliwachagua watu ili wawaongoze na kuwatumikia, lakini hawakufaya hivyo. Badala yake, walitumia Chama hiki kutekeleza maslahi yao binafsi. Na walitumia Chama chenu kujinufaisha. Niwaulize walimu wenzangu, hivi mnafahamu fedha za michango mnazokatwa kila mwezi zinatumikaje? Au mmeshawahi kujiuliza kuhusu utendaji kazi wa Benki yenu na ni namna gani inawanufaisha? Sina hakika kama mnafahamu. Lakini niwaambie, kwa taarifa nilizonazo, Benki yenu haifanyi vizuri, na ni miongoni mwa Benki ambazo wakati wowote inaweza kufungwa. Nakumbuka wakati fulani nilialikwa kwenda kuizindua lakini sikwenda, baada ya kujiridhisha kuwa Benki hiyo haifanyi vizuri na haipo kwa maslahi ya walimu. Ni watu wachache tu ndio wananufaika nayo. Hivyo basi, nawasihi tena walimu wenzangu, katika uchaguzi huu, msichague watu wenye nia ya kujinufaisha kupitia CWT.
Lakini zaidi ya hapo, msiwachague watoa rushwa. Rushwa ni ugonjwa. Ni kansa. Ukimchagua mtoa rushwa hutoweza kamwe kumuuliza michango yenu ya kila mwezi inatumikaje; na utashindwa kumuuliza manufaa yaliyopatikana kwenye Benki yenu. Hivyo basi, narudia tena kuwasihi walimu wenzangu katika uchaguzi huu chagueni vizuri. Chagueni watu watakaowatetea na kuwasemea matatizo yenu. Na kamwe msimchague mtu ambaye lengo lake ni kuigombanisha CWT na Serikali. Mapambano mara nyingi hayajengi. Na niwashauri walimu wenzangu, wakati mwingine, mkitaka kufanikisha jambo, tumieni ule usemi usemao, “If you want to win an enemy, join him and work with him…” Siwapigii kampeni; lakini kwa dhati kabisa nawapongeza viongozi wa sasa wa CWT kwa kuonesha nia ya kweli ya kuwatetea na kushughulia shida za walimu. Wameonesha kuwa wapo tofauti na wapo tayari kufanya kazi na Serikali. Huo ndio unapaswa kuwa muelekeo wa CWT hivi sasa. Mimi naamini kuwa kama Serikali na CWT tukiwa kitu kimoja tutaweza kushughulikia matatizo mengi yanayowakabili walimu tena kwa haraka.
Mheshimiwa Kaimu Rais wa CWT,
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Ndugu Wajumbe wa Mkutano;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuushukuru tena uongozi wa CWT kwa kunikaribisha kufungua Mkutano huu. Aidha, kwa namna ya pekee, naushukuru uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kukubali kuwa wenyeji wa Mkutano huu. Tunawashukuru sana na tunawashukuru pia walimu wanafunzi wa Chuo hiki kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kwenye ufunguzi wa Mkutano wa CWT.
Halikadhalika, nawashukuru viongozi wa vyama vya wafanyakazi kwa kuhudhuria kwenye Mkutano huu. Na vilevile, nawashukuru wageni wote waalikwa kutoka ndani na nje kwa kuamua kutenga muda wenu kuja kushiriki kwenye Mkutano huu. Mwisho lakini sio kwa umuhimu, wajumbe wa Mkutano huu, na nawaomba mfikishe salamu kwa walimu wote nchini kuwa Serikali ipo pamoja nao.
Baada ya kusema hayo, sasa natamka rasmi kuwa nimeufungua Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa CWT. Nawatakia Mkutano mwema.
Mungu Ibariki CWT!
Mungu Wabariki Walimu Wote!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”
- Dec 13, 2017
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UFUNGUZI WA TAWI JIPYA LA BENKI YA CRDB DODOMA, TAREHE 13 DESEMB...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa John Malecela, Waziri Mkuu
Mstaafu wa Tanzania;
Ndugu Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
Ndugu Ally Hussein Laay, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi
wa Benki ya CRDB;
Dkt. Charles Kimei, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB;
Waheshimiwa Viongozi mbalimbali mliopo hapa;
Waheshimiwa Wazee wa Mkoa wa Dodoma;
Wageni Waalikwa wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu kwa kutupa afya njema na kutuwezesha kukutana hapa leo. Napenda pia, kwa namna ya pekee kabisa, kuushukuru uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na Benki ya CRDB kwa kuniliaka kushiriki kwenye tukio hili la kuzindua Tawi la Benki yenu hapa Dodoma.
Napenda kukiri kuwa nimefurahi sana kushiriki kwenye hafla hii. Nimefurahi kwa sababu kwanza mimi ni mteja wa Benki ya CRDB kwa muda mrefu; tangu nikiwa Mwanafunzi wa Chuo Kikuu. Zaidi ya hapo, hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya nchi yetu. Ni hivi karibuni tu tumefanya maamuzi makubwa ya kuhakikisha Serikali yote inahamia Dodoma ifikapo mwaka 2020. Kama mnavyofahamu, Waziri Mkuu pamoja na Viongozi na Watendaji wa Wizara tayari wamehamia. Aidha, Makamu wa Rais naye anatarajiwa kuhamia mwezi huu; na mimi nitahamia mwakani.
Ni dhahiri kuwa, kutokana na uamuzi huu wa kuhamia Dodoma, idadi ya watu katika Mji huu hapa itaongezeka sana. Na huduma za taasisi kama za benki zitahitajika zaidi. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuushukuru na kuupongeza uongozi wa Benki hii kwa uamuzi wenu wa kufungua Tawi hili hapa Dodoma. Kwa kufungua Tawi hili, mmeunga mkono uamuzi wa Serikali wa kuhamia Dodoma. Ahsanteni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Sekta ya benki ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi. Ni muhimu kwanza kabisa katika ukuzaji uchumi. Sekta ya benki inatoa mchango mkubwa katika pato la taifa. Mathalan, mwaka 2014, sekta hii ilichangia asilimia 3.4 ya pato la taifa; mwaka 2015 na mwaka jana 2016 ilichangia asilimia 3.6. Aidha, benki zinachangia ukuaji uchumi kupitia ulipaji wa kodi kwa Serikali. Hivi punde mmetoka kumsikia Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dkt. Kimei, akisema kuwa katika kipindi cha miaka 10 iliyopita Benki yake imelipa kodi zaidi ya shilingi bilioni 800 na hivyo kuiwezesha kushinda tuzo ya kuwa mlipaji kodi bora mara kadhaa. Hongereni sana CRDB.
Lakini mbali na kukuza uchumi, sekta ya benki ni muhimu katika kupiga vita umaskini. Benki zinashiriki katika kupiga vita umaskini, kupitia kwanza mikopo inayoitoa kwa wananchi, hususan wafanyabiashara na wajasiliamali wadogo kama vile machinga na mama lishe. Pili, zinachangia kupiga vita umaskini kwa namna inavyoshiriki katika kukuza sekta nyingine. Kama mnavyofahamu, sekta ya benki ni muhimu sekta nyingine zote. Iwe viwanda, kilimo, uvuvi, ufugaji, ujenzi, biashara, usafirishaji; na hata sekta za huduma kama afya, elimu, maji, n.k. Kwa mfano, benki ikitoa mkopo wa mtaji wa kujenga kiwanda; kupitia mkopo huo, wananchi watapata ajira wakati wa ujenzi na baada ya kiwanda kukamilika. Fikiria pia benki ikitoa mkopo kwa ajili ya ujenzi wa barabara; wakati wa ujenzi wa barabara hiyo wananchi wanapata ajira, lakini pia ikikamilika itapunguza gharama na usafiri kwa wananchi, na hivyo kusaidia kupunguza umaskini.
Sambamba na hayo, sekta ya benki ni umuhimu kwa vile inatoa ajira za moja kwa moja. Mathalan, nimeambiwa kuwa Benki hii imetoa ajira kwa Watanzania wapatao 3,200. Lakini pia sekta ya benki ni muhimu kwa vile inawasaidia wananchi kutunza amana (fedha) kwa usalama, na wakati wowote wakihitaji, wanapewa. Tena kwa siku hizi, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, hata ukihitaji fedha zako usiku wa manane unazipata kwa njia ya ATMs au Simu kiganjani.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kwa kuzingatia hayo yote, ni dhahiri kuwa sekta ya benki ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa lolote. Na kwa sababu hiyo, inatia moyo kuona kuwa kwa takriban miongo mitatu iliyopita, sekta ya benki imezidi kuimarika hapa nchini. Mathalan, mwaka 1990, nchi yetu ilikuwa na benki 3 tu, lakini kwa sasa nchi yetu ina zaidi ya benki 58. Na jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba miongoni mwa benki zinazofanya vizuri ni Benki hii ya CRDB, ambayo kwa takriban asilimia 86 zinamilikiwa na Watanzania (asilimia 40 watu binafsi, asilimia 21 Serikali na mifuko ya pensheni ina asilimia 15).
Hivi punde, Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Kimei, ameeleza mafanikio ambayo Benki hii imepata tangu kuanzishwa kwake mwaka 1996. Baadhi ya mafanikio aliyoyataja ni kuongezeka kwa rasilimali zake kutoka thamani ya shilingi bilioni 54 hadi kufikia shilingi trilioni 5.5; kupanua wigo wa benki kutoka matawi 19 hadi 260, ukiachilia mbali ATMs 600 ilizonazo, Mawakala 3,000, SACCOS shirikishi 455 na matawi ya kutembea 21. Benki pia imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi trilioni 3.5; ambapo shilingi trilioni 1 zimekwenda kwenye sekta mbili za kilimo na viwanda. Aidha, kama nilivyosema awali, benki imelipa kodi ya shilingi bilioni 800 na kutoa ajira 3,200 kwa Watanzania. Vilevile, mwaka huu, baada ya kuwabana sana hatimaye wametoa gawio la shilingi bilioni 19 kwa Serikali. Na natumaini wataendelea kutupa gawio letu kila mwaka. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kwa dhati kabisa, kutoa pongezi nyingi sana kwa Benki hii chini ya Dkt. Kimei kwa kazi kubwa inazofanya kwa ajili ya kukuza uchumi lakini pia kupiga vita umaskini katika nchi yetu.
Mtakumbuka kuwa Benki hii kihistoria ilikuwa ikimilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali, wakati huo ikijulikana kama Tanzania Rural Development Bank (TRDB). Mwaka 1996 ilibinafsishwa ili kuongeza ufanisi wake. Kwa mfano mzuri uliooneshwa na Benki hii, ni dhahiri kuwa kama mashirika na taasisi zote zilizobinafsishwa zingefanya kazi kama Benki hii, nchi yetu ingekuwa imepiga hatua kubwa za kimaendeleo. Lakini mashirika na viwanda vingi vilivyobinafsishwa, hivi sasa havifanyi kazi.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jukumu langu leo ni kufungua benki hii. Hata hivyo, kabla sijatekeleza jukumu hilo, ninayo masuala machache ya kueleza. Suala la kwanza kabisa, ni malalamiko kuhusu kupungua kwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi. Serikali inalitambua suala hili, na kupitia Benki Kuu, imechukua hatua mbalimbali kulishughulikia. Mathalan, Mwezi Aprili, mwaka huu tuliamua kupunguza kiwango cha kisheria cha sehemu ya amana inayotakiwa kuwekwa benki kuu na benki za Biashara kutoka asilimia 10 hadi asilimia 8. Sambamba na hilo, tumeshusha riba ya Benki Kuu (discount rate) mara mbili kutoka asilimia 16 hadi 12 mwezi Machi 2017, na mwezi Agosti tukaishusha tena hadi asilimia 9. Pamoja na hayo, tumetoa mikopo maalum kwa benki za biashara na halikadhalika Benki Kuu inanunua fedha za kigeni kwenye soko la jumla la benki ili kuongeza ukwasi wa shilingi kwenye uchumi. Hatua nyingine tulizochukua ni kuendelea mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuongeza chachu katika shughuli za uchumi.
Kutokana na hatua hizi, hali ya ukwasi imeanza kuimarika na kusaidia kupunguza riba katika soko la fedha baina ya benki (IBCM rate) kutoka asilimia 13.69 mwezi Desemba 2016 hadi asilimia 3.29 mwezi Novemba 2017. Aidha, riba katika soko la dhamana za Serikali zimepungua kutoka wastani wa asilimia 15.12 mwezi Desemba 2016 hadi asilimia 8.76 mwezi Novemba 2017. Kwa matokeo haya, tuna matumaini makubwa kuwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi utazidi kuimarika katika siku za hivi karibuni.
Suala jingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu benki kushiriki kwenye shughuli za maendeleo. Kama nilivyosema hapo awali, sekta ya benki ni muhimu kwenye sekta zote, ikiwemo viwanda na kilimo. Hivyo basi, napenda kutoa wito kwa benki zote nchini kuangalia wa kutenga fedha nyingi za mikopo kwenye sekta hizi mbili. Kama mnavyofahamu, nchi yetu kwa sasa imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda; na miongoni mwa viwanda tunavyolenga kuvijenga ni vile vinavyotumia zaidi malighafi za hapa nchini, hususan mazao ya kilimo. Hivyo basi, naziomba benki kuunga mkono dhamira hiyo ya Serikali. Nimefurahi kusikia kuwa ninyi CRDB mmekuwa mkitenga asilimia 15 kwa ajili ya sekta ya viwanda, na mwakani mmepanga kuongeza hadi kufikia asilimia 20, sawa na shilingi bilioni 700. Hongereni sana. Na naziomba benki nyingine ziige mfano wenu.
Napenda pia kuzungumzia kidogo suala la benki kupanua wigo wa mtandao wenu. Ni kweli kuwa idadi ya benki imeongezeka hapa nchini. Lakini kwa bahati mbaya, benki nyingi zipo Dar es Salaam na kwenye baadhi ya miji mikuu ya mikoa na wilaya. Mathalan kwa taarifa za mwaka 2015 asilimia 36.3 ya matawi yote ya Benki yalikuwa Dar es Salaam asalimia 7.1 Arusha, asilimia 6.5 Mwanza, asilimia 5.4 Mbeya na asilimia 4.6 Moshi. Ni benki chache tu ndizo zina matawi kwenye vijijini. Hivyo, natoa wito kwenu kusambaza huduma zenu hadi vijijini, ambako Watanzania wengi wanaishi. Na ninaposema kusambaza huduma hadi vijijini simaanishi kwamba lazima mjenge majengo, ninachomaanisha ni kwenu ninyi kubuni njia mbalimbali za kufikisha huduma za kibenki kwa wananchi waliopo vijijini, ikiwemo kuanzisha matawi mengi zaidi ya kutembea, kuingia ubia na mawakala (Bank Agents), kuanzisha huduma za kifedha za kwa njia za mtandao (Sim Banking, Internet Baking n.k.) kama ambavyo ninyi CRDB na baadhi ya Benki nyingi mmeanza kufanya.
Nina imani mkiweza kufikisha huduma zenu hadi vijijini, sio tu mtawasaidia wananchi kupata huduma za kibenki bali pia itawaongezea benki nchini ukwasi wa kutosha. Kwa mujibu wa taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania ya mwaka 2015, ukwasi wa benki zote nchini mwaka 2014 ulikuwa una thamani ya shilingi trilioni 22.5. Kiasi hiki bado ni kidogo sana ukilinganisha na mahitaji makubwa ya fedha (mikopo) yaliyopo hapa nchini. Mathalan, Mpango wetu wa Taifa wa Maendeleo wa miaka mitano, ambao tumeanza kuutekeleza katika mwaka wa fedha 2016/2017 unahitaji kiasi cha shilingi trilioni 107. Hivyo, nawahimiza benki kusambaza huduma zenu kwenye maeneo ya vijijini ili muweze kuongeza ukwasi katika benki zenu. Aidha, nawakaribisha wawekezaji wengine kuja kuwekeza kwenye sekta hii ya benki hapa nchini.
Jambo jingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu tatizo la riba za mikopo kuendelea kuwa juu. Riba za mikopo hapa nchini bado zipo juu. Natambua kuwa tatizo hili linasababishwa na mambo mengi, ikiwemo kutokuwepo kwa taarifa za kutosha za wakopaji, wasiwasi wa benki kutolipwa na wakopaji na hivyo kuongeza gharama za ufuatiliaji, n.k. Pamoja na matatizo hayo, Serikali imechukua hatua mbalimbali, ambazo binafsi nilidhani zingeweza kushusha kiwango cha riba nchini ili kuwawezesha wananchi, hususan wa kipato cha chini kuchukua mikopo. Mojawapo ya hatua hizo ni kuanzisha Mfumo wa Kuhifadhi Taarifa za Wakopaji ( yaani Credit Reference Bureau) ambao unaziwezesha benki zote kuwatambua wakopaji na kuweza kuchukua tahadhari stahiki. Aidha, tunaendelea kutoa vitambulisho vya taifa ambavyo kwa sasa vina taarifa nyingi. Hivyo, basi naziomba benki kuanza kupunguza viwango vya riba. Aidha, naihimiza Benki Kuu kukamilisha zoezi la kutangaza Sera ya Riba (Policy Rate), ambayo itazifanya taasisi za kifedha kuwa na riba zinazowiana na sera hiyo. Vilevile, napenda kutumia fursa hii kuwahimiza wananchi kuwa na utamaduni wa kurejesha mikopo. Dawa ya deni ni kulipa. Na niiombe Mahakama ya Biashara kuharakisha kesi zinazohusiana na madeni ya mikopo.
Mbali na hayo, napenda kutoa wito kwa Wizara ya Fedha na Benki ya Kuu kudhibiti matumizi ya ya fedha za kigeni (Dola) nchini. Na jambo hili, liende sawia na kuongeza usimamizi kwa Maduka ya Kubadilisha Fedha (Bureau De Change). Ni lazima tuondokane na utaratibu wa matumizi holela ya fedha za kigeni nchini; lakini pia Maduka ya Kubadilisha Fedha yasitumike kuwa sehemu za kutakatisha fedha zisizo halali kutoka nje. Aidha, natoa wito kwa Benki Kuu kuongeza usimamizi katika uanzishaji na uendeshaji wa shughuli za Kibenki hapa nchini. Kabla Benki haijaanzishwa wamiliki wake wafuatiliwe kwa makini; na halikadhalika, benki inayoshindwa kujiendesha ifutwe hata kama ni ya Serikali.
Sambamba na hayo, mtakumbuka kuwa mwezi Juni mwaka huu, nikiwa pale Kijitonyama kuzindua Kituo cha Data na Mfumo wa Ukusanyaji Mapato kwa njia ya Kielektroniki, niliagiza kuwa benki zijiunge na Mfumo huo wa kukusanya mapato kwa njia ya kielektroniki. Na nakumbuka Kamishna wa TRA aliahidi kuwa hadi mwezi Desemba makampuni yote ya benki na simu yatakuwa yamejiunga. Hivi sasa tupo katikati ya mwezi Desemba, lakini kwa taarifa nilizonazo ni benki chache tu ndizo tayari zimejiunga na mfumo huo. Benki nyingi pamoja na baadhi ya Makampuni ya Simu bado hazijajiunga na mfumo huo. Napenda kurudia tena agizo langu kwa benki na kampuni zote za simu kuhakikisha zinajiunga na mfumo huo kabla ya mwaka huu kwisha. Kwa kampuni ya simu au benki itakayoshindwa kutekeleza agizo hili, taratibu husika zifanyike, ikiwezekana makampuni au benki hizo zifungiwe kufanya kazi nchini.
Jambo la mwisho ambalo ningependa kulisema ni kutoa wito kwa Watanzania wote kutumia huduma za kibenki hususan kwa kufungua akaunti za benki. Mbali na usalama, benki inasaidia mtu kupanga matumizi yake vizuri. Unakuwa huwezi kutumia fedha ovyo. Lakini, nawasihi na nanyi wamiliki wa Benki kuimarisha mifumo yenu ya usalama ili kukabiliana na vitendo vya wizi kwa njia za mtandao. Aidha, wachukulieni hatua watumishi wenu ambao sio waaminifu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kuushukuru tena uongozi wa CRDB kwa kunikaribisha na kwa zawadi ya hundi ya kiasi cha shilingi milioni 100 mliyonikabidhi. Hundi hii mmenikabidhi hadharani. Hivyo basi, na mimi naikabidhi kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ili fedha hizo zikatumike kwa ya kujenga Wodi katika Hospitali ya Mkoa. Siku moja nitakuja kuikagua hiyo wodi.
Mwisho kabisa lakini sio kwa umuhimu napenda kuwapongeza LAPF kwa kujenga jengo hili hapa Dodoma. Jengo ni zuri sana.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kufungua Tawi la Sita la Benki ya CRDB hapa Dodoma.
Mungu Ibariki CRDB!
Mungu zibariki Benki zote nchini!
Mungu wabariki wana-Dodoma!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 09, 2017
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE SHEREHE ZA MIAKA 56 YA UHURU WA TANZANIA BARA, DODOMA, TA...
Soma zaidiHotuba
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Omar Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Waheshimiwa Marais Wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa na Mzee Kikwete;
Waheshimiwa Viongozi Wakuu Wastaafu wa Serikali zetu mbili mliopo, Mzee Bilal, Mzee Malecela, Mzee Kificho;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi Wakuu mliopo, mkiongozwa na Mama Maria Nyerere na Mama Fatuma Karume;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa Dkt. Binilith Mahenge, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Wabunge;
Waheshimiwa Mabalozi na Viongozi wa Taasisi za Kimataifa;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni waalikwa wote;
Wananchi Wenzangu, Mabibi na Mabwana:
Kabla ya kuanza hotuba yangu, naomba sote tusimame kwa dakika moja kuwaombea mashujaa wetu, askari 14, waliouawa wakiwa katika jukumu la kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) juzi. Tunamwomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mashujaa wetu mahali pema peponi na kuwaponya askari waliojeruhiwa. Amina.
Baada ya utangulizi huo, napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wetu, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha kuiona siku hii adhimu kwenye historia ya nchi yetu. Siku kama ya leo ya Jumamosi, tarehe 9 Desemba mwaka 1961, Jamhuri ya Tanganyika, hivi sasa Tanzania Bara, ilipata Uhuru wake. Uhuru huu ulihitimisha utawala wa kikoloni uliodumu nchini kwa takriban miaka 76; ikijumuisha miaka 33 ya Utawala wa Ujerumani na miaka mingine 43 ya Utawala wa Uingereza.
Kama mnavyofahamu, harakati za kutafuta Uhuru wa nchi yetu ziliongozwa na Chama cha Tanganyika African National Union (TANU), ambacho mwaka 1977 kiliungana na Chama cha Afro Shiraz (ASP), ambacho kiliongoza mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964, na kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama Tawala. Hii ndiyo historia yenyewe. Haiwezi kubadilika. Uhuru wa nchi yetu uliletwa na Vyama Mama vya CCM, yaani TANU na ASP. Hivyo basi, leo tunaposheherekea Miaka 56 ya Uhuru wa Tanganyika (Tanzania Bara), hatuna budi kuwashukuru na kuwapongeza Wazee wetu 17, ambao mwezi Julai 1954, wakiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, walianzisha Chama cha TANU. Tunawakumbuka pia wananchi wote, ambao kabla na wakati wa Chama cha TANU, walishiriki katika harakati za kutafuta uhuru wa nchi yetu. Nafahamu wengi wao tayari wametangulia mbele za haki; hivyo, kwa niaba ya Watanzania wote, namwomba Mwenyezi Mungu azipumzishe roho zao mahali pema peponi. Amina!
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Ni ukweli usiopingika kuwa, katika kipindi cha Miaka 56 ya Uhuru wa nchi yetu, tumepata mafanikio makubwa. Ndio! tumepata mafanikio makubwa, tena sana tu. Nafahamu wapo watu ambao wakisikia kauli hiyo huwa wanaumia; lakini huo ndio ukweli. Nchi yetu imepiga hatua kubwa za maendeleo tangu kupata Uhuru. Naomba nitoe mifano michache. Wakati tunapata Uhuru, baada ya utawala wa takriban miaka 76 ya Kikoloni, nchi yetu ilikuwa na mtandao wa barabara wenye urefu kilometa 33,600. Kati ya barabara hizo ni kilometa 1,360 tu ndio zilikuwa na lami. Kwa sasa tuna mtandao barabara wenye kilomita 122,500, ambapo kilometa 80,000 zipo chini ya TAMISEMI na zinahudumiwa na TARURA; kilometa 36,000 zipo chini ya TANROADS, na kilometa 6,500 zipo chini ya Hifadhi za Wanyama za Taifa (TANAPA). Aidha kati ya Mtandao huo wa barabara, kilometa 12,679.55, ni za lami. Sambamba na hayo, kuna jumla ya kilometa 2,480 zinazoendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na barabara nyingine zenye urefu wa kilometa 7,087 zipo kwenye hatua mbalimbali za maandalizi kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Vilevile, tumejenga madaraja makubwa 17, na mengine 14 yapo kwenye hatua mbalimbali.
Ukiachilia mbali ujenzi wa barabara, wakati tunapata Uhuru, nchi yetu ilikuwa na vituo vya kutolea huduma za afya 1,095 (hospitali 98, vituo vya afya 22 na zahanati 975), leo hii tuna vituo 7,293 (hospitali 178, vituo vya afya 795 na zahanati 6,285). Wakati tunapata Uhuru tulikuwa na Shule za Msingi 3,100 hivi sasa zipo 17,379; shule za sekondari zilikuwa 41 hivi sasa zipo 4,817; na tulikuwa na Chuo Kikuu kimoja tu, lakini leo vipo 48. Madaktari waliosajiliwa walikuwa 403, ambapo kati yao Watanganyika walikuwa 12 tu, leo tuna madaktari 9,343. Mwaka 1961, Wahandisi wazalendo walikuwa wawili (2) tu; lakini hadi kufikia mwezi Juni 2017 nchi yetu imefikisha wahandisi 19,164. Makandarasi nao walikuwa wawili tu (2), lakini hivi sasa wakandarasi waliosajaliwa wamefikia 9,350. Halikadhalika, wakati tunapata Uhuru, wastani wa umri wa mtu kuishi ulikuwa miaka 37, leo hii wastani ni miaka 61. Mifano ipo mingi. Siwezi kuitaja yote leo.
Itoshe tu kusema kuwa katika kipindi cha miaka 56 ya uhuru wetu, tumepiga hatua kubwa za kimaendeleo kwenye nyanja mbalimbali, ikiwemo huduma za jamii, ulinzi, umeme, kilimo, utalii, biashara, mifugo, uvuvi, demokrasia, diplomasia, utamaduni, n.k. Zaidi ya hapo, na pegine kubwa zaidi ni kwamba, katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru, tumeweza kulinda na kudumisha amani, umoja na Muungano wetu.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kuwashukuru na kuwapongeza kwa dhati kabisa Viongozi wa Awamu zote za Serikali zetu mbili, ya Muungano na ya Zanzibar, kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 56 ya Uhuru wa nchi yetu. Na nimefarijika sana kuona kuwa viongozi wastaafu wa nchi yetu, Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Mzee Bilal, Mzee Malecela tunao hapa. Na niwaambie ndugu zangu Watanzania kuwa mambo kama haya ya kuwaona viongozi wastaafu wakishiriki kwenye tukio kama hili kwa pamoja ni nadra sana Duniani. Sio kwenye nchi zote jambo kama hili linawezekana. Kwenye nchi nyingine haiwezekani. Hivyo basi, nawasihi Watanzania wenzangu tuzidi kudumisha amani na umoja wetu. Na mimi namuomba Mwenyezi Mungu siku moja niweze kuhudhuria tukio kama hili nikiwa nimeungana na viongozi wengine wastaafu.
Lakini mbali na kuwapongeza viongozi wastaafu kwa mafanikio yaliyopatikana, napenda kuwapongeza Watanzania wote: wakulima, wafanyakazi, wavuvi, wafugaji, wafanyabiashara, wasanii, n.k.; kwa michango yenu ya hali na mali iliyowezesha kupatikana mafanikio niliyoyataja na mengine ambayo sikuyataja. Bila ya ninyi kujitoa, mafanikio haya kamwe yasingepatikana. Navipongeza pia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama (JWTZ, Polisi, Usalama wa Taifa, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto, n.k.), kwa kushiriki kikamilifu na kufanikisha kupatikana kwa mafanikio haya. Napenda kuwahakikishia vyombo vyote vya ulinzi kuwa Serikali yenu ipo pamoja nanyi na tutaendelea kushughulikia changamoto mbalimbali zinawakabili.
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Sherehe za Uhuru wa Tanzania Bara mwaka huu zinafanyika hapa Dodoma. Hapa Dodoma ndio Makao Makuu ya Nchi yetu. Na zitaendelea kufanyika hapa. Napenda niwahakikishie ndugu Watanzania kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza mambo yote mazuri yaliyopatikana, na kutekeleza mambo mengine mapya kwa lengo la kuhakikisha kuwa Watanzania wote wanafaidi matunda ya uhuru.
Ombi langu kwa Watanzania endeleeni kuziamini Serikali zetu mbili, za Muungano na ya Zanzibar. Mimi na mwenzangu Dkt. Shein, tunaahidi kuwa tutasimamia na kutekeleza mambo yote tuliyowaahidi, ikiwemo ahadi zilizomo kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi. Na kutekeleza hayo, hatutambagua mtu kwa misingi ya dini, kabila, itikadi ya kisiasa, jinsia au rangi. Daima tutakuwa watumishi wenu.
Ndugu wananchi,
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Leo wakati tunaadhimisha Sherehe za Miaka 56 ya Uhuru wa Tanzania Bara, napenda kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa Ibara ya 45 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa mamlaka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa msamaha kwa wafungwa wa makosa mbalimbali. Kwa faida ya hadhira hii, napenda kuinukuu Ibara hiyo, kama ifutavyo:
45 (1) bila kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Ibara hii, Rais anaweza kutenda lolote kati ya mambo yafuatayo:-
(a) kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia mbele ya mahakama kwa kosa lolote, na aweza kutoa msamaha huo ama bila ya masharti au kwa masharti, kwa mujibu wa sheria;
(b) kumwachilia kabisa au kwa muda maalum mtu yeyote aliyehukumiwa kuadhibiwa kwa ajili ya kosa lolote ili mtu huyo asitimize kabisa adhabu hiyo au asitimize adhabu hiyo wakati wa muda huo maalum;
(c) kuibadilisha adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa kosa lolote iwe adhabu tahafifu;
(d) kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa ajili ya kosa lolote au kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu ya kutoza, au kuhozi (au kuchukua) kitu cha mtu mwenye hatia ambacho vinginevyo kingechukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka utaratibu utakaofuatwa na Rais katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa Ibara hii.
(3) Masharti ya Ibara hii yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Zanzibar na kwa adahabu zilizotolewa Tanzania Zanzibar kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge inayotumika Zanzibar, halikadhalika, masharti hayo yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Bara kwa mujibu wa sheria.
Sambamba na Ibara hii inayompa Rais mamlaka ya kutoa msamaha, nimesoma pia Presidential Affair Act ya mwaka 1962 cap 9 of Tanzania.
Ndugu Watanzania wenzangu;
Hivi sasa nchi yetu ina wafungwa wapatao 39,000, ambapo wanaume ni takriban 37,000 na wanawake ni 2,000. Kati ya wafungwa waliopo magerezani, wafungwa 522 wamehukumiwa adhabu ya kifo, ambapo wanaume ni 503 na wanawake ni 19. Idadi ya wafungwa waliofungwa kifungo cha maisha ni 666, ambapo wanaume ni 655 na wanawake 11.
Hivyo basi, kwa mujibu wa mamlaka niliyopewa na Katiba kupitia Ibara ya 45, nimeamua kutoa msamaha kwa wafungwa 8,157. Kati ya wafungwa hao niliowapa msamaha, wafungwa 1,828 watatoka leo na waliosalia 6,329 watapunguziwa vifungo vyao vya kukaa gerezani na kutoka kulingana na vifungo vyao. Vilevile, kwa kutumia Ibara hiyo ya 45, nimetoa msamaha kwa wafungwa 61 waliokuwa wamehukumiwa kunyongwa. Halikadhalika, nimeamua kutoa msamaha kwa wafungwa kutoka Familia ya Nguza (Nguza Vicking na Johnson Nguza). Wengi niliowapa msamaha, hususan waliohukumiwa kunyongwa na kufungwa vifungo virefu, wametumikia vifungo vyao kwa muda mrefu na wameonesha tabia njema na kujutia makosa yao.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Nimeeleza mambo mengi; mengi sana. Hivyo, napenda niishie hapa. Lakini kabla sijahitimisha, napenda nitoe shukrani zangu nyingi kwa Kamati ya Maandalizi kwa kufanikisha Sherehe hii. Sherehe zimefana sana. Hongereni sana wana-Kamati. Tunavishukuru pia vyombo vya ulinzi na usalama, vikundi vya burudani, chipukizi na waandishi wa habari kwa kufanikisha sherehe hii.
Kwa namna ya pekee, napenda kuwashukuru wageni wetu waalikwa waliokuja hapa kushiriki nasi katika shughuli hii muhimu na ya kihistoria kwa taifa letu.Tunawashukuru Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi mbalimbali za Kimataifa. Napenda niwahakikishie kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Mataifa yenu pamoja na Taasisi mnazoziwakilisha.
Napenda pia kuwashukuru wana-Dodoma wote, mkiingozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, Mheshimiwa Mahenge, kwa ukarimu mkubwa mliotuonesha na kwa kujitokeza kwa wingi kwenye Sherehe hizi. Nimejionea mwenyewe kuwa watu wengi wapo nje. Hii ina maana kuwa mnahitaji uwanja mpya. Na kwa bahati nzuri, rafiki zetu wa Morocco wamekubali kutujengea Uwanja Mpya hapa Dodoma, ambapo Jiwe la Msingi tunatarajia kuliweka mwezi Machi au Aprili 2018. Sambamba na hilo, napenda kuwahakikishia wana-Dodoma kuwa dhamira ya Serikali kuhamia Dodoma ipo pale pale. Hakuna kurudi nyuma. Makamu wa Rais atahamia kabla ya mwisho wa Mwaka huu, na mimi nitahamia mwakani. Tutaendelea kuboresha miundombinu pamoja na upatikanaji wa huduma za jamii hapa Dodoma, hususan kwa kuwa hivi sasa mji huu ndio kioo cha nchi yetu. Ahadi yetu ya kujenga barabara ya mzunguko, uwanja wa michezo, njia ya reli kutoka kitongoji cha Chalinze hadi hapa mjini pamoja na kuboresha huduma za maji na afya zipo pale pale. Nawaomba muendelee kutuamini. Na kamwe hatutawaangusha.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kurudia tena kuwashukuru viongozi wastaafu kwa kuja kujumuika nasi kwenye sherehe hizi. Aidha, navishukuru vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na nzuri wanazofanya kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa kisiwa cha amani. Wito wangu kwa Watanzania tuendelee kuenzi na kudumisha tunu za Amani, Muungano pamoja na Umoja na Mshikamano, ambazo tumeachiwa na waasisi wetu, Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere na Mzee Abeid Karume.
Mungu Ibariki Tanzania!
Mungu Wabariki Watanzania!
“Ahsanteni Sana kwa kunisikiliza”