Hotuba

- May 08, 2021
HOTUBA YA MHE. SAMIA SULUHU HASSAN, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA KITABU CHA HISTORIA YA MAISHA (TAWASIFU) YA MHESHIMIWA...
Soma zaidiHotuba

- May 01, 2021
HOTUBA YA MHESHIMIWA SAMIA SULUHU HASSAN, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI MKOANI MWANZA, TA...
Soma zaidiHotuba

- Apr 22, 2021
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA SAMIA SULUHU HASSAN, WAKATI WA KULIHUTUBIA BUNGE LA 12 LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA DODOMA...
Soma zaidiHotuba

Hotuba

- Jan 01, 2021
HOTUBA YA MHESHIMIWA SAMIA SULUHU HASSAN, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA WAFANYAKAZI DUNIANI MKOANI MWANZA, TA...
Soma zaidiHotuba

- Nov 13, 2020
Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Wakati wa kufungua rasmi Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, WAKATI WA KUFUNGUA RASMI BUNGE LA 12 LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA DODOMA, 13 NOVEMBA 2020
Mheshimiwa Spika;
Mara ya mwisho nilipoingia kwenye Ukumbi huu Kulifunga Bunge la 11, tulibahatika kuwa na Marais wetu Wastaafu watatu. Lakini leo, wapo wawili. Mmoja, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, ametangulia mbele za haki. Hivyo basi, kabla ya kuanza hotuba yangu, nawasihi sote tusimame tumkumbuke pamoja na wabunge wote waliofariki dunia tangu kufungwa kwa Bunge la 11. Mwenyezi Mungu aiweke roho ya Marehemu Mzee Mkapa pamoja na marehemu wetu wote mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Spika;
Baada ya utangulizi huo, napende niseme kwamba, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 91 Ibara ndogo ya kwanza imempa dhamana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kulifungua rasmi Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni kwa sababu hiyo, nimekuja hapa leo kulihutubia Bunge hili kwa lengo la kutimiza masharti hayo ya Kikatiba.
Napenda nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyetujalia neema ya uhai na kutuwezesha kuiona siku ya leo. Aidha, nakupongeza wewe, Mheshimiwa Job Ndugai, Mbunge wa Jimbo la Kongwa kwa kuchaguliwa, kwa mara nyingine, kuliongoza Bunge hili ukiwa Spika. Hongera sana. Nampongeza pia Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson kwa kuchaguliwa kwa mara nyingine kuwa Naibu Spika; tena mara hii akiwa Mbunge wa kuchaguliwa kutoka Jimbo la Mbeya Mjini. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. Tulia. Huu ni uthibitisho kwamba, nchi yetu, kupitia Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi, inawaamini sana wanawake.
Kama mnavyofahamu, Makamu wetu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, naye ni mwanamama. Aidha, Bunge hili la 12 nalo lina Wabunge wengi wanawake. Kwa msingi huo, napenda nitumie fursa hii kuahidi kuwa, Serikali ninayoingoza, itaendelea kuwaamini wanawake katika kushika nafasi mbalimbali za uongozi. Wanawake na akinamama Oyee!!!
Napenda pia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchaguliwa kwenu kuwa Wabunge wa Bunge hili la 12. Mmechaguliwa kwa vile wananchi wana imani kuwa mna uwezo wa kuwawakilisha vizuri. Hivyo basi, nawasihi msiwaangushe wananchi waliowachagua. Watanzania wana imani kubwa sana na Bunge hili.
Nitumie fursa hii pia kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kuridhia na kumpitisha Mheshimiwa Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ahsanteni sana.
Mheshimiwa Spika;
Nimekuja kulizindua Bunge hili baada ya nchi yetu kufanikiwa kumaliza Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba, 2020 kwa uwazi amani na utulivu mkubwa. Kwa msingi huo, napenda nirudie kuipongeza Tume yetu ya Taifa ya Uchaguzi kwa kusimamia vizuri zoezi la Uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu; kuanzia kwenye uandikishaji wapiga kura; uchukuaji na urejeshaji fomu za wagombea; usimamizi wa kampeni na pia zoezi la kupiga kura na utoaji matokeo mapema. Kwa hakika, Tume imedhihirisha uwezo mkubwa katika kusimamia Uchaguzi bila kutegemea misaada kutoka nje. Mheshimiwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Mstaafu Semistocles Kaijage; Makamu Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mstaafu Hamid Mahmoud Hamid; Makamishna wa Tume; Mkurugenzi wa Uchaguzi, Dkt. Wilson Mahera pamoja na Watendaji wote wa Tume; hongereni sana kwa kazi nzuri.
Lakini, kwa namna ya pekee, nawapongeza kwa namna mlivyotumia vizuri fedha mlizotengewa. Kama inavyofahamika, Uchaguzi wa Mwaka huu uligharamiwa na Serikali kwa asilimia 100, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 331 kilitengwa. Hata hivyo, mpaka Uchaguzi umekamilika, Tume imetumia shilingi bilioni 262 tu. Hii ni ishara ya uadilifu mkubwa walionao Viongozi na Watendaji wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Hongereni sana. Natoa rai kwa Taasisi nyingine kuiga mfano mzuri wa Tume hii.
Kwa moyo wa dhati kabisa, narudia kuwashukuru Viongozi wetu wa Dini kwa kutuongoza vyema kwa sala na dua katika kipindi chote cha Uchaguzi; na hatimaye tumeweza kumaliza Uchaguzi wetu salama. Nawasihi endeleeni kuliombea Taifa letu ili libaki katika mikono ya Mwenyezi Mungu.
Narudia pia kuvishukuru vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kusimamia vizuri amani na utulivu wa nchi yetu na mipaka yake wakati wote wa Uchaguzi. Hii ni ishara kuwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ni imara na vinafanya kazi kwa ueledi mkubwa. Hongera sana kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama.
Kwa namna ya pekee kabisa, natoa shukrani nyingi kwa Watanzania wenzangu wote kwa kushiriki vizuri na kuonesha utulivu mkubwa kwenye Uchaguzi uliopita; kuanzia kwenye zoezi la uandikishaji wapiga kura, wakati wa kampeni, upigaji kura na kupokea matokeo. Hakuna shaka, Uchaguzi wa Mwaka huu, kwa mara nyingine, umeuthibitishia ulimwengu kuwa sisi Watanzania ni wapenda amani, tunajitambua, hatudanganyiki na tumekomaa kidemokrasia. Ahsanteni sana Watanzania wenzangu.
Mheshimiwa Spika;
Masuala yote muhimu tuliyopanga kutekeleza kwenye miaka mitano ijayo, tumeyaweka kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2020 – 2025 ambayo ina kurasa 303. Kwa bahati nzuri, Waheshimiwa Wabunge wengi wa Bunge hili wanaifahamu vizuri Ilani hiyo kwa vile wameitumia katika kuomba kura kwa wananchi kwenye Uchaguzi Mkuu uliomalizika.
Lakini, sambamba na masuala hayo yaliyomo kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi wa mwaka 2020 – 2025, tutaendelea pia kutekeleza na kusimamia mambo yote niliyoeleza wakati nikizindua Bunge la 11, tarehe 20 Novemba, 2015.
Kama mtakavyokumbuka, kwenye Hotuba hiyo ya kuzindua Bunge la 11 nilieleza mambo mengi sana, ambayo, kimsingi, yalitoa falsafa, dira na vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano. Baadhi tumeyatekeleza vizuri; yapo ambayo hatujayatekeleza kwa ukamilifu na mengine yapo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji. Kwa hiyo, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendelea kusimamia na kutekeleza mambo yote niliyoyaeleza kwenye Hotuba ya Kuzindua Bunge la 11. Hii ndiyo sababu nimeamua kuigawa tena Hotuba yangu ya Uzinduzi wa Bunge la 11 kwenu Waheshimiwa Wabunge ili mkaisome na hatimaye ikawaongoze katika kutekeleza majukumu yenu vizuri.
Hata hivyo, pamoja na hayo yote, naomba Mheshimiwa Spika uniruhusu nitaje baadhi ya mambo muhimu tutakayoyapa kipaumbele kikubwa katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Mheshimiwa Spika;
Jambo la kwanza na muhimu tutakalolipa kipaumbele kikubwa kwenye miaka mitano ijayo ni kuendelea kulinda na kudumisha tunu za Taifa letu, yaani Amani, Umoja na Mshikamano, Uhuru wa Nchi yetu, Muungano na Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Na katika hilo, naahidi kushirikiana kwa karibu sana na Rais mpya wa Zanzibar, Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi. Kamwe, hatutakuwa na mzaha na yeyote mwenye kutaka kuhatarisha amani ya nchi yetu; mwenye nia ya kuvuruga umoja na mshikamano wetu; na pia mwenye kutaka kutishia Uhuru wetu, Muungano pamoja na Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Napenda pia kutumia fursa hii kumwahidi Mheshimiwa Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwamba, kwenye miaka mitano ijayo, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itatoa ushirikiano mkubwa na kufanya kazi kwa karibu na Serikali ya Zanzibar. Kwa kifupi, naweza kusema, tutafanya kazi kwa pamoja kwa lengo la kuleta maendeleo kwa pande zetu zote mbili za Muungano. Na katika hilo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa hotuba nzuri aliyoitoa wakati wa kuzindua Baraza la Wawakilishi. Kwenye hotuba yake alitoa dira, mwelekeo na kutaja vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Nane ya Zanzibar. Hongera sana kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Mwinyi kwa hotuba nzuri. Kupitia Bunge hili, napenda nimwahidi Mheshimiwa Rais Dkt. Hussein Mwinyi kuwa, nitampa ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza yote aliyoahidi wakati wa Uzinduzi Rasmi wa Baraza la Wawakilishi.
Mheshimiwa Spika;
Sambamba na kulinda na kudumisha tunu za nchi yetu, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendelea kuimarisha utawala bora, hususan kwa kusimamia nidhamu kwenye utumishi wa umma pamoja na kuzidisha mapambana dhidi ya rushwa, wizi, ufisadi na ubadhirifu wa mali za umma. Kwenye miaka mitano iliyopita, tuliwachukulia hatua za kinidhamu watumishi 32,555 na kuiwezesha nchi yetu kushika nafasi ya kwanza kati ya nchi 35 za Afrika kwa kupambana na rushwa, kwa mujibu wa Transparency International; na pia kushika nafasi ya 28 kati ya nchi 136 duniani kwa matumizi mazuri ya fedha za umma kwa mujibu wa Utafiti Jukwaa la Dunia (World Economic Forum) wa mwaka 2019.
Hata hivyo, watumishi wazembe bado wapo; wala rushwa bado wapo; na pia wezi na wabadhirifu wa mali ya umma bado wapo. Kwa hiyo, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendelea kushughulikia matatizo hayo. Na kwa kifupi, niseme, utumbuaji majipu utaendelea. Hata hivyo, kwa upande mwingine, tutaendelea kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi ya watumishi wetu wote ili yaendane na hali halisi ya maisha ya Watanzania. Kwa hiyo, watumishi wasiwe na wasiwasi.
Mheshimiwa Spika;
Kwenye miaka mitano ijayo pia, tumejipanga kuendeleza jitihada za kukuza uchumi. Kama unavyofahamu, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tulijitahidi kusimamia vizuri uchumi wetu, ambapo ulikua kwa wastani wa asilimia 7 kwa mwaka. Aidha, Pato ghafi la Taifa limeongezeka kutoka shilingi trilioni 94.349 mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 139.9 mwaka 2019; tulidhibiti mfumuko wa bei, kutoka asilimia 6.1 mwaka 2015 hadi kufikia wastani wa asilimia 4.4 na kuongeza akiba ya fedha ya kigeni kutoka Dola za Marekani bilioni 4.4 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 5.2 mwezi Julai, 2020 ambazo zinatuwezesha kununua bidhaa na huduma kwa miezi 6.
Zaidi ya hapo, kwenye miaka mitano iliyopita, tuliongeza mauzo yetu ya nje kutoka Dola za Marekani bilioni 8.9 mwaka 2015 hadi Dola za Marekani bilioni 9.7 mwaka 2019; na pia kuvutia uwekezaji wenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 14.6, sawa na zaidi ya shilingi trilioni 30. Aidha, tulifanikiwa kupunguza umasikini wa kipato hadi kufikia asilimia 26.4 kwa takwimu za mwaka 2017/2018. Mafanikio haya, bila shaka, ndiyo yamewezesha, mwezi Julai 2020, nchi yetu kutangazwa kuingia kundi la nchi za uchumi wa kati kutoka kundi la nchi masikini. Na mafanikio hayo yamepatikana miaka mitano kabla ya muda uliopangwa, yaani mwaka 2025.
Kwa hiyo, kwenye miaka mitano ijayo tunakusudia kuendeleza mafanikio ya kiuchumi yaliyopatikana na tutahakikisha ukuaji uchumi unawanufaisha wananchi, hususan kwa kuinua vipato vyao, kupunguza umasikini na tatizo la ajira. Na katika hilo, tunalenga kukuza uchumi wetu kwa wastani wa angalau asilimia 8 kwa mwaka na pia kutengeneza ajira mpya zipatazo milioni 8. Tutaendelea pia kuboresha sera zetu za uchumi jumla na sera za fedha (yaani macroeconomic and monetary policies), na pia kuhakikisha viashiria vyote vya uchumi; ikiwemo thamani ya sarafu yetu, mfumko wa bei pamoja na viwango vya riba; vinabaki kwenye hali ya utulivu.
Tutaongeza pia jitihada za kuwawezesha wananchi wetu kiuchumi kwa kuwapatia mikopo isiyo na riba ama yenye riba nafuu, ikiwemo mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri zetu; na pia kupitia Mifuko na Programu mbalimbali zilizoanzishwa na Serikali, ambayo kwa idadi zipo 18. Baadhi ya Mifuko hiyo ni Mfuko wa Maendeleo ya Vijana (YDF); Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake (WDF); Mfuko wa Taifa wa Kuendeleza Wajasiriamali (NEDF); Mfuko wa Kutoa Mikopo kwa Wajasiriamali Wadogo (SELF Microfinance Fund), Mfuko wa Kudhamini Mikopo ya Mauzo ya Nje; Mfuko wa Kilimo Kwanza. n.k. Tutaimarisha usimamizi wa Mifuko hii na kuhakikisha Watanzania wanaifahamu.
Najua Mifuko hii mingi ipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu; hivyo basi, nakuagiza Mheshimiwa Waziri Mkuu, hii ikawe kazi yako ya kwanza kuishughulikia; ikiwezekana, mwangalie uwezekano wa kuiunganisha baadhi ya mifuko ili ifanye kazi kwa tija zaidi na kupunguza gharama za uendeshaji. Nataka Mifuko hii ikiwasaidie wananchi wa kawaida, wakiwemo machinga, akina baba na mama lishe pamoja na wajasiriamali wengine wadogo.
Sambamba na kutoa mikopo, tutaendelea kutekeleza Program mbalimbali za kukuza ujuzi na maarifa, ikiwemo maarifa ya ujasiriamali, ili kuwapa ujuzi na uzoefu wananchi wetu utakaowawezesha kujiajiri ama kuajirika ndani na nje ya nchi. Tutaendelea pia kutekeleza Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili tuliouzindua mwezi Februari 2020, ambao utagharimu takriban shilingi trilioni 2.032. Tutahakikisha fedha hizo zinawafikia walengwa, ambao ni wananchi masikini.
Muhimu zaidi ni kwamba, katika kipindi cha miaka mitano ijayo, sekta binafsi itapewa umuhimu wa pekee sana. Tunataka mtu yeyote atakayetaka kuwekeza asisumbuliwe kwa kuwekewa vikwazo vya aina yoyote. Watanzania ni matajiri lakini baadhi yao wanasita kuwekeza hapa nchini kwa kuogopa kusumbuliwa na maswali yasiyo na msingi. Tunahitaji kuwa na Mabilionea wengi wa Kitanzania. Nataka Watanzania wote washiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa nchi yao.
Sambamba na kuwekeza, Watanzania wahamasishwe kuweka fedha kwenye Benki za hapa nchini ili kusaidia benki zetu kufanya biashara na kuimarisha mzunguko wa fedha na kupunguza riba kwa wakopaji. Waheshimiwa Wabunge na Watanzania mnaonisikiliza, wakati wa kufanya mambo bila woga ni sasa. Kwenye miaka mitano ijayo pia tutafungua milango kwa sekta binafsi kufanya majadiliano na Serikali ili kutafuta mwafaka ya migogoro ya biashara (business disputes) iliyopo kwa faida ya pande zote mbili. Lengo letu ni kuona Tanzania inakuwa mahali pazuri pa kufanya biashara duniani. Kwenye miaka mitano iliyopita, tumefuta tozo 168, ambapo 114 zitahusu kilimo, mifugo na uvuvi na tozo nyingine 54 za biashara.
Mheshimiwa Spika;
Mbali na hatua hizo; kwa lengo la kukuza uchumi, kupambana na umasikini, na pia kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira, tunakusudia, kwenye miaka mitano ijayo, kuweka mkazo mkubwa katika kukuza sekta zetu kuu za uchumi na uzalishaji, hususan kilimo, ufugaji, uvuvi, viwanda, madini, biashara na utalii. Sekta hizi ndizo zenye kuajiri Watanzania wengi. Kwa hiyo, ni wazi, tukifanikiwa kuzikuza, uchumi wetu utakua kwa kasi na hivyo kupunguza matatizo ya umasikini na ukosefu wa ajira nchini.
Kwa msingi huo, kwenye KILIMO, tunakusudia kuongeza tija na kukifanya kilimo chetu kuwa cha kibiashara. Lengo ni kujihakikishia usalama wa chakula, upatikanaji wa malighafi za viwandani na pia kupata ziada ya kuuza nje. Ili kufanikisha hayo, tutahakikisha pembejeo na zana bora za kilimo, ikiwemo mbegu, mbolea, viatilifu/dawa na matrekta, vinapatikana kwa uhakika na kwa gharama nafuu. Tutaongeza pia eneo la umwagiliaji kutoka hekta 561,383 hadi hekta milioni 1.2 mwaka 2025 ili kupunguza utegemezi kwenye mvua.
Tutaimarisha mifumo ya upatikanaji wa mitaji kwa wakulima wadogo na wawekezaji kwa kushirikisha taasisi za fedha, ikiwemo Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo pamoja na benki nyingine. Tutashughulikia pia tatizo la upotevu wa mazao (yaani post harvest loss), ikiwemo kwa kukamilisha ujenzi wa vihenge na maghala maeneo mbalimabli nchini ambayo yataongeza uwezo wetu wa kuhifadhi mazao kutoka tani 190,000 za sasa hadi tani 501,000. Takwimu zinaonesha kuwa, kila mwaka, nchi yetu inapoteza wastani wa kati ya asilimia 30 – 40 ya mavuno yake kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kukosekana kwa miundombinu ya kuhifadhi. Zaidi ya hapo, tunakusudia kuanzisha bidhaa mbalimbali za huduma ya Bima ya Kilimo na pia kuingia makubaliano ya kibiashara na nchi walaji na wanunuzi wa mazao ili kupata soko la uhakika.
Mazao ya kimkakati tunayolenga kuyapa kipaumbele kikubwa ni pamba, korosho, chai, kahawa, tumbaku, mkonge, michikichi, cocoa, alizeti na miwa; lakini pia mazao ya chakula. Nchi yetu kila mwaka inaagiza tani 800,000 za ngano na kwa ujumla, tunatumia wastani wa shilingi trilioni 1.3 kuagiza chakula kutoka nje. Hii ni aibu kwa nchi kama Tanzania. Hivyo basi, ni lazima tutafute majawabu ya suala hili. Na hii ndiyo ikawe kazi ya kwanza ya Waziri wa Kilimo nitakayemteua.
Lakini, zaidi ya hapo, tutaweka mkazo mkubwa kwenye kilimo cha mazao ya bustani (matunda, mbogamboga, maua na viungo), ambacho kinakua kwa kasi kubwa nchini. Hivi sasa nchi yetu inashika nafasi ya 20 kwa kuzalisha kwa wingi mazao hayo duniani na mauzo yetu ya nje yameongezeka kutoka Dola za Marekani milioni 412 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Marekani milioni 779 mwaka 2018/2019. Hii ndiyo sababu, hatuna budi kukiendeleza kilimo cha mazao hayo. Na katika hilo, napenda kuriafu Bunge hili Tukufu kuwa, kwenye miaka mitano ijayo, tunakusudia kununua ndege moja ya mizigo ili kurahisisha uzafirishaji wa mazao ya bustani, lakini pia minofu ya samaki pamoja na nyama. Wakulima wetu ni lazima watajirike na shughuli wanazozifanya; hivyo basi, Mawaziri wa Kilimo, Biashara, Mambo ya Nje na Mabalozi wajipange vizuri kwa hili.
Kwa upande wa MIFUGO, kama mnavyofahamu, nchi yetu inashika nafasi ya pili kwa mifugo Barani Afrika. Tuna ng’ombe milioni 33.4; mbuzi milioni 21.3; kondoo milioni 5.65; punda 657,389; lakini pia tuna idadi kubwa ya kuku, bata, kanga, n.k. Hata hivyo, ukweli ni kwamba, sekta hii bado haijatunufaisha vya kutosha.
Kwa kuzingatia hilo, kwenye miaka mitano ijayo, tunakusudia kuikuza sekta ya mifugo ili ichangie ukuaji uchumi na kupunguza matatizo ya umasikini na ukosefu wa ajira nchini. Tutaongeza maeneo ya ufugaji kutoka hekta 2,788,901 za sasa hadi hekta 6,000,000. Tunataka wafugaji wasiteswe na mifugo yao. Mifugo ni utajiri. Sambamba na hayo, tutahamasisha ufugaji wa kisasa; tutaongeza vituo vya kuzalisha mbegu bora na pia kuongeza uzalishaji wa chakula cha mifugo viwandani kutoka tani 900,000 hadi milioni 8.
Zaidi ya hapo, tutakamilisha ujenzi wa machinjio saba unaoendelea maeneo mbalimbali nchini, ambapo, kwa pamoja, zitakuwa na uwezo wa kuchinja ng’ombe 6700 na mbuzi 11,000 kwa siku. Ujenzi wa machinjio hizo sio tu utasaidia kupatikana kwa nyama bora itakayouzwa hadi kwenye masoko ya kimataifa bali pia utawezesha upatikanaji wa ngozi bora kwa ajili ya kutengeneza bidhaa za ngozi. Takwimu zinaonesha kuwa, takriban asilimia 90 ya ngozi inayozalishwa nchini kwa sasa haina ubora unaohitajika; na sababu mojawapo ni uchinjaji wanyama kienyeji. Kwa hiyo, machinjio yanayojengwa yatapunguza tatizo hilo.
Nitumie fursa hii, kuikaribisha sekta binafsi kuwekeza kwenye viwanda vya kutengeneza bidhaa za mifugo (nyama, ngozi, maziwa, kwato, n.k.). Na katika hilo, tunaahidi kutoa vivutio maalum kwa watakaowekeza kwenye viwanda hivyo ambavyo vitasaidia kuinua vipato vya wafugaji wetu na pia kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania. Na hapa, nataka niweke bayana kuwa, watendaji watakaokwamisha ujenzi wa viwanda hivyo tutawashughulikia.
Mheshimiwa Spika;
Nchi yetu pia imebarikiwa kuwa na maeneo mengi yanayofaa kwa shughuli za uvuvi, ikiwemo Ukanda wa Pwani, Maziwa, mito na mabwawa. Hali hii inafanya sekta hii kuwa na nafasi ya kutoa mchango mkubwa kwenye kukuza Pato la Taifa na pia kupambana na umasikini na tatizo la ajira. Hata hivyo, kwa sasa, mchango wake bado ni mdogo. Hivyo basi, kwenye miaka mitano ijayo tunakusudia kuikuza sekta hii, ikiwemo kuimarisha shughuli za uvuvi kwenye Bahari Kuu, ambako tumekuwa tukipoteza mapato mengi. Kwa mujibu wa Ripoti ya Kamati ya Bunge kuhusu Shughuli za Uvuvi wa Bahari Kuu ya Mwaka 2018; shughuli za uvuvi kwenye Bahari Kuu zinaweza kuingizia Serikali mapato ya moja kwa moja ya takriban shilingi bilioni 352.1 kwa mwaka endapo mifumo ya usimamizi na udhibiti ingekuwa imara na samaki wangechakatwa hapa nchini. Hata hivyo, mapato yaliyokuwa yamekusanywa kwa kipindi cha miaka tisa (2009 hadi 2017) yalikuwa shilingi bilioni 29.79, sawa na shilingi bilioni 3.3 kwa mwaka. Kiwango hiki cha mapato hakikubaliki.
Hii ndiyo sababu, tunataka, kwenye miaka mitano ijayo, kuisimamia vizuri shughuli za uvuvi wa Bahari Kuu ili Taifa letu linufaike na rasilimali zake, kwa kuhusisha sekta binafsi. Kwa bahati nzuri, tayari, mwaka huu (2020) tumetunga Sheria Mpya ya Kusimamia na Kuendeleza ya Uvuvi wa Bahari Kuu. Aidha, tumepanga kununua Meli 8 za Uvuvi kwa kushirikiana na Shirika IFAD (4 upande wa Zanzibar na 4 upande wa Tanzania Bara) ili zishiriki katika uvuvi wa Bahari Kuu. Kama mnavyofahamu, suala la uvuvi wa bahari kuu ni la Muungano. Tunakusudia pia kujenga Bandari kubwa ya Uvuvi itakayotoa ajira zipatazo 30,000; na tutaendelea kuihamasisha sekta binafsi kujenga viwanda vya kuchakata samaki.
Sambamba na kusimamia Bahari Kuu, tutakuza shughuli za uvuvi kwenye Maziwa yetu Makuu (Victoria, Tanganyika na Nyasa) pamoja na Mito yetu mikubwa. Tutahamasisha wavuvi wetu wadogo kujiunga kwenye vikundi ili tuweze kuwapatia mitaji, ujuzi, vifaa na zana za uvuvi; na halikadhalika tutapitia upya tozo na maeneo mbalimbali ili kuwapunguzia wavuvi kero na kuvutia uwekezaji. Tutahamasisha pia watu binafsi kujenga mabwawa na kufuga kisasa kwa kutumia vizimba. Sekta ya uvuvi ni lazima itoe mchango mkubwa kwenye uchumi wa nchi yetu. Wateule wote wa sekta hii ni lazima walisimamie hili.
Mheshimiwa Spika;
Ni ndoto kufikiria kwamba utaweza kukuza uchumi au kupambana na umasikini pamoja na tatizo la ukosefu wa ajira bila kuelekeza nguvu katika kukuza sekta ya viwanda. Duniani kote, sekta ya viwanda ndiyo mhimili mkuu wa kukuza uchumi, kupambana na umasikini pamoja na matatizo ya ajira. Kwenye miaka mitano iliyopita, tulifanikiwa kujenga viwanda vipya takriban 8,477 ambavyo vilitengeneza ajira zipatazo 480,000, ambapo Mkoa wa Pwani uliongoza kwa kujenga viwanda vingi.
Hivyo basi, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendeleza jitihada za kukuza sekta hiyo. Mkazo mkubwa tutauweka kwenye viwanda vyenye kutumia malighafi zinazopatikana kwa wingi hapa nchini (mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi); vyenye kuajiri watu wengi; na ambavyo bidhaa zake zinatumika kwa wingi hapa nchini (nguo, bidhaa za ngozi, mafuta ya kula, sukari, saruji, n.k.).
Ili kuvutia uwekezaji kwenye sekta ya viwanda, tutaendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji, ikiwemo kuangalia masuala ya kodi na kuondoa vikwazo na urasimu. Pamekuwepo na urasimu mwingi na kusumbuliwa kwa wawekezaji kwa kuzungushwa zungushwa na hivyo kuwafanya wakate tamaa. Mimi nataka mwekezaji mwenye fedha akija apate kibali ndani ya siku 14. Kwa sababu hiyo, nimeamua suala la uwekezaji ikiwa ni pamoja na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kulihamisha kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda Ofisi ya Rais ili hao wanaokwamisha nikapambane nao mwenyewe. Lakini, zaidi ya hapo, tumepanga kujenga Ukanda na Kongani (clusters) za viwanda kila mkoa kulingana na mazao na maliasili zinazopatikana.
Mheshimiwa Spika;
Kwenye miaka mitano iliyopita tumepata mafanikio makubwa kwenye sekta ya madini. Mapato yameongezeka kutoka shilingi bilioni 168 mwaka 2014/2015 hadi shilingi bilioni 527 mwaka 2019/2020. Mchango wa sekta ya madini kwenye Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 3.4 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 5.2 mwaka 2019. Zaidi ya hapo, kwa mara ya kwanza, katika historia ya nchi yetu, mwaka 2019, sekta ya madini iliongoza kwa kutuingizia fedha nyingi za kigeni, Dola za Marekani bilioni 2.7. Nitumie fursa hii kulipongeza Bunge la 11 kwa kutoa mchango mkubwa katika kupatikana kwa mafanikio haya.
Nina imani kuwa Bunge hili la 12 litafuata nyayo za Bunge la 11. Na katika hili, napenda niliarifu Bunge hili Tukufu kuwa, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendelea kuimarisha ulinzi na usimamizi wa madini yetu, (kama tulivyofanya kwa kujenga Ukuta Mirerani) kwa kuimarisha Sheria zetu ili madini yetu yasitoroshwe na Serikali kukoseshwa mapato. Aidha, tunakusudia kuendelea kufanya majadiliano na wawekezaji wakubwa kwa kuzingatia mfano wa Makubaliano yaliyofikiwa kati ya Serikali na Kampuni ya Barrick yaliyowezesha kuundwa kwa Kampuni ya Twiga Minerals Corporation. Nchi yetu imebarikiwa kuwa na madini mbalimbali, ikiwemo dhahabu, almasi, Tanzanite, chuma, bati, nickel, copper, n.k. Aidha, tuna gesi aina mbalimbali, kama vile ethane, helium, ambayo hivi karibuni zimepatikana futi za ujazo bilioni 138 kwenye Ziwa Rukwa, ambazo zinaweza kuhudumia dunia kwa miaka 20. Hii ndiyo sababu, kila siku nimekuwa nikisema, sisi sio masikini; sisi ni matajiri. Nchi yetu ni tajiri sana.
Lakini, kuhusu madini pia, kwenye miaka mitano ijayo pia tutaendelea kuliimarisha Shirika letu la Taifa la Madini (STAMICO) ili lishiriki kikamilifu kwenye shughuli za madini; kuwawezesha wachimbaji wetu wadogo, ikiwa ni pamoja na kuwatengea maeneo ya uchimbaji, kuwapatia mafunzo, mikopo pamoja na vifaa. Na katika natambua kuwa, wapo baadhi ya watu wamepewa leseni za utafiti na uchimbaji lakini hawajazifanyia kazi; tutazifuta leseni zao, na maeneo hayo kuyagawa kwa wachimbaji wengine, hususan wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo ni muhimu sana katika kukuza sekta ya madini.
Tutaendelea pia kuimarisha masoko ya madini pamoja na kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji, uyeyushaji, usafishaji na utengenezaji wa bidhaa za madini. Tunataka madini yachimbwe hapa Tanzania, yachenjuliwe, yayeyushwe na kisha bidhaa za bidhaa za madini zitengenezwe hapa hapa Tanzania; na ndipo ziuzwe nje ama watu kutoka nje waje kununua bidhaa za madini hapa nchini. Ni imani yetu kuwa, kutokana na hatua tulizopanga kuzichukua sekta ya madini itaweza kuchangia angalau asilimia 10 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2025.
Mheshimiwa Spika;
Utalii ni sekta nyingine ambayo tutaipa mkazo mkubwa kwenye miaka mitano ijayo. Sekta hii imeajiri takriban watu milioni 4. Kwenye miaka mitano iliyopita, ilikua kwa kiwango cha kuridhisha, ambapo idadi ya watalii waliotembelea nchini iliongezeka kutoka watalii 1,137,182 mwaka 2015 hadi watalii 1,510,151 mwaka 2019. Mapato nayo yaliongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.9 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 2.6 mwaka 2019. Nitumie fursa hii kuipongeza Hifadhi yetu ya Taifa ya Serengeti kwa kuchaguliwa kuwa Hifadhi Bora Barani Afrika kwa mwaka 2020.
Kwenye miaka mitano ijayo, tumejipanga kuongeza idadi ya watalii hadi kufikia milioni 5 mwaka 2025 na mapato kutoka Dola za Marekani bilioni 2.6 za sasa hadi Dola za Marekani bilioni 6. Hatua tutakazochukua ni pamoja na kupanua wigo wa vivutio vya utalii, ikiwemo kukuza utalii wa mikutano na uwindaji wanyamapori; kuimarisha utalii wa fukwe; kujenga miundombinu ya kuwezesha meli za utalii kuzuru nchini na kuongeza kasi ya utangazaji wa vivutio vyetu. Vilevile, tutazihamaisha taasisi na watu binafsi kuanzisha ranchi, mashamba na bustani za wanyama, kama inavyofanyika nchi nyingine, ili kuzuia ujangili na kukuza utalii; lakini pia kuongeza vipato na fursa za ajira kwa Watanzania. Na katika hilo, napenda kuwaarifu Watanzania, kupitia Bunge hili Tukufu kuwa, tumepunguza bei kwa ajili ya kupata wanyama wa mbegu. Mathalan, bei ya nyati wa mbegu imepungua kutoka Dola za Marekani 1,900 hadi kufikia shilingi laki mbili; Pofu kutoka Dola za Marekani 1,700 hadi shilingi 310,000 na Swala kutoka Dola za Marekani 150 hadi shilingi 90,000. Hivyo basi, nawasihi Watanzania wenzangu, popote walipo, kuchangamkia fursa hiyo; ambayo itachochea pia uanzishaji wa butcher za wanyama pori.
Zaidi ya hapo, tutaendelea kupitia upya kodi na tozo mbalimbali ili kuzifuta ama kupunguza kodi zenye kero. Kwenye miaka mitano iliyopita, tulipunguza ada ya leseni ya biashara ya utalii kwa wakala wa kusafirisha watalii yenye idadi ya magari chini ya manne kutoka Dola za Kimarekani 2,000 hadi Dola za Marekani 500 na matokeo yake idadi ya kampuni za Kitanzania zimeongezeka kutoka 643 mwaka 2015 hadi 1,687 mwaka 2020.
Mheshimiwa Spika;
Tuna imani, hatua hizi nilizoeleza zitatuwezesha kufikia malengo tuliyojiwekea ya kukuza uchumi kwa angalau asilimia 8 kwa mwaka, kuinua vipato vya Watanzania, kupunguza umasikini na kutengeneza ajira mpya milioni 8. Hata hivyo, najua, ili kufikia malengo haya, tunategemea sana kupata ushirikiano kutoka sekta binafsi. Kama mnavyofahamu, sekta binafsi ndiyo injini ya kujenga uchumi wa kisasa.
Hivyo basi, narudia kuikaribisha sekta binafsi ya hapa nchini na kutoka nje kuwekeza katika sekta nilizozitaja; na ambazo sikuzitaja. Na napenda niwahakikishie watu wa sekta binafsi kuwa, Tanzania ni mahali pazuri na sahihi pa kuwekeza. Nchi yetu ina amani na utulivu; tumebarikiwa kuwa na fursa nyingi za uwekezaji; nchi yetu ipo kwenye eneo la kimkatati; sisi pia ni Wanachama wa jumuiya mbili, EAC na SADC, ambazo zina soko la watu takriban milioni 500. Kwa hiyo narudia, kuikaribisha sekta binafsi kuwekeza hapa nchini. Na kwa bahati nzuri, tangu mwaka jana, tumeanza kutetekeleza Mpango wetu wa Kuboresha Mazingira ya Biashara nchini (yaani Blueprint for Regulatory Reforms to Improve the Business Environment in Tanzania). Hivyo basi, mazingira ya biashara na uwekezaji, kwenye miaka mitano ijayo, yanatarajiwa kuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Spika;
Ili kukuza uchumi pamoja na sekta za uzalishaji ni lazima tuimarishe miundombinu, hususan ya usafiri na nishati ya umeme. Kamwe, huwezi kukuza sekta za kilimo, ufugaji, uvuvi, viwanda, uchimbaji madini na utalii bila kuimarisha miundombinu na huduma za usafiri pamoja na upatikanaji wa huduma za umeme. Kwa hiyo, kama ilivyokuwa kwenye miaka mitano iliyopita, tutaendelea kuweka mkazo mkubwa kwenye ujenzi wa miundombinu ya usafiri na kuboresha huduma za usafirishaji. Tutakamilisha miradi tuliyoianzisha na kuanza kutekeleza miradi mipya. Na katika hilo, tumepanga, kwenye miaka mitano ijayo, kukamilisha ujenzi wa kilometa 2,500 za barabara za lami na kuanza ujenzi wa barabara za lami zenye urefu wa kilometa 6,006; ili hatimaye tuweze kufikia lengo letu la kuunganisha mikoa na wilaya zote kwa barabara za lami. Barabara hizo zimetajwa kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi na nyingine zinatokana na ahadi nilizotoa kipindi cha Kampeni. Tumepanga pia kukamilisha ujenzi wa madaraja 7 na kuanza mengine 14, likiwemo Daraja la Kigongo – Busisi, Wami na Pangani.
Zaidi ya hapo, tutaendelea kushughulia tatizo la msongamano wa magari kwenye miji na majiji yetu, hususan Arusha, Dar es Salaam, Mbeya, Mwanza na hapa Dodoma, ambako tumepanga kujenga barabara ya mzunguko ya njia nne yenye urefu kilometa 110; ambapo Wakandarasi wawili tayari wamepatikana na ujenzi utaanza hivi karibuni.
Kwa upande wa usafiri wa reli, tumepanga kuendelea kuimarisha usafiri wa Reli ya Kati na TAZARA. Aidha, tutakamilisha ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam – Dodoma na kuanza ujenzi wa vipande vya reli ya Mwanza – Isaka; Makutopora – Tabora; Tabora – Isaka – Tabora – Kigoma na Kaliua – Mapanda – Kalema. Zaidi ya hapo, tutanunua vichwa vya treni ya njia kuu 39 na kukarabati 31; tutanunua mabehewa ya mizigo 800 na kukarabati 690; na pia tutanunua mabehewa 37 ya abiria na kukarabati 60.
Kuhusu usafiri wa majini, tumepanga kukamilisha upanuzi wa bandari zetu kuu za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara pamoja na zilizopo kwenye Maziwa yetu Makuu (Victoria, Tanganyika na Nyasa). Tumepanga pia kununua meli mpya ya mizigo kwa ajili ya kutoa huduma Bahari ya Hindi. Tutakamilisha ujenzi wa meli mpya, kukarabati meli ya Mv. Butiama na kuanza ujenzi wa meli ya kubeba mabehewa (ferry wagon) Ziwa Victoria. Tutaikarabati MV. Liemba na MT. Sangara pamoja na kuanza ujenzi wa meli mpya ya kubeba abiria 600 na mizigo tani 400; na nyingine kubwa ya kubeba mizigo tani 4,000 kwenye Ziwa Tanganyika.
Kuhusu usafiri wa anga, tutajenga kiwanja kipya cha Msalato, tutafanya upanuzi na ukarabati wa viwanja vya ndege 11, vikiwemo vya Kigoma, Shinyanga, Sumbawanga, Tabora, Mtwara na Songea na pia kujenga kwa kiwango cha lami njia za kutua na kuruka ndege kwenye viwanja vya Iringa, Lake Manyara, Tanga, Musoma, Lindi, Kilwa Masoko, Njombe, Singida na Simiyu. Zaidi ya hapo, tutanunua ndege mpya tano, ambapo kama nilivyosema, moja itakuwa ya mizigo.
Ujenzi wa miundombinu hii ya usafiri pamoja na uboreshaji wa huduma za usafirishaji sio tu utachochea shughuli za uchumi na uzalishaji lakini pia itakuwa ni hatua nzuri ya kuelekea kufikia malengo yetu ya kuifanya nchi yetu kuwa lango kuu la biashara kwenye Ukanda huu; na hivyo kuweza kunufaika na nafasi ya kijiografia.
Mheshimiwa Spika;
Kuhusu sekta ya nishati, tutaendelea kuimarisha miundombinu ya nishati na pia kuboresha upatikanaji wa huduma za umeme. Na katika hilo, tunakusudia kukamilisha ujenzi wa Bwawa la kufua Umeme la Nyerere litakalozalisha Megawati 2,115 na kuanza ujenzi wa miradi mingine ya umeme wa maji Ruhudji Megawati 358; Rumakali Megawati 222; Kikonge Megawati 300 na pia umeme wa gesi asilia Mtwara Megawati 300; Somanga Fungu Megawati 330, Kinyerezi III Megawati 600 na Kinyerezi IV Megawati 300; pamoja na miradi mingine midogo midogo. Aidha, tunakusudia kuzalisha umeme Megawati 1,100 kwa kutumia nishati jadidifu (jua, upepo, jotoardhi).
Tumepanga pia kukamilisha Miradi wa kusafirisha umeme wa Msongo wa kilovoti 400 wa Singida – Arusha – Namanga na Iringa – Mbeya – Tunduma ambayo itaunganisha nchi yetu na majirani zetu wa Kenya na Zambia. Tutatekeleza mingine ya kuunganisha maeneo ya humu nchini kwenye Gridi ya Taifa, ikiwemo Kigoma. Kwenye miaka mitano iliyopita, tulitekeleza miradi mingi ya kusafirisha umeme na hivyo kupunguza matumizi ya umeme wa mafuta; na tukaweza kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 719 kwa mwaka.
Kuhusu umeme pia, kwenye miaka mitano ijayo, tumepanga kufikisha umeme kwenye vijiji vyote ambavyo bado havijafikishiwa umeme, ambapo idadi yake haizidi 2,384. Kwenye miaka mitano iliyopita, kwa takwimu za hadi jana, tumefikisha umeme kwenye vijiji 9,884; kutoka vijiji 2,018 mwaka 2016. Nchi yetu ina vijiji 12,280. Miradi hii yote ya umeme itakapokamilika, sio tu itatuwezesha tuwe na umeme wa kutosha na kufikisha umeme kwenye maeneo yote nchini, bali pia itatufanya tuwe na ziada ya kuweza kuuza nje.
Sambamba na hayo, kuhusu nishati, kwenye miaka mitano ijayo, tutaanza utekelezaji wa Miradi ya kielelezo (flagship projects) ya Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga lenye urefu wa kilometa 1,445 pamoja na Mradi wa Kusindika Gesi Asilia (LNG) Mkoani Lindi. Zaidi ya hapo, tutaendelea kuhamasisha matumizi ya gesi asilia na gesi ya mitungi majumbani, kwenye taasisi, viwanda na magari ili kupunguza uharibifu wa mazingira na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Spika;
Dunia hivi sasa ipo kwenye Mapinduzi ya Nne ya Viwanda (yaani The Fourth Industrial Revoulution) ambayo yanaongozwa na sekta ya mawasiliano (ICT). Shughuli nyingi duniani, kwa sasa, zinafanyika kwa kutumia TEHAMA. Hivyo basi, sisi nasi hatuna budi kwendana na kasi hiyo ya kukua kwa sekta ya mawasiliano. Kwa msingi huo, tumepanga, kwenye miaka mitano ijayo, pamoja na masuala mengine, kufikisha miundombinu ya Mkongo wa Taifa kwenye maeneo mengi ya nchi yetu, hususan Wilayani, tutaongeza wigo wa matumizi ya mawasiliano ya kasi (yaani broadband) kutoka asilimia 45 ya sasa hadi asilimia 80 mwaka 2025. Aidha, tumepanga kuongeza watumiaji wa internet kutoka asilimia 43 ya sasa hadi asimilia 80 mwaka 2025 na pia kuboresha matumizi ya simu za mkononi ili kupatikana nchi nzima. Zaidi ya hapo, tutatoa kipaumbele kwenye masuala ya utafiti na ubunifu kwenye TEHAMA; tutawatambua na kuwasajili wataalam wote wa TEHAMA; na tunakusudia kuweka anuani za makazi (postikodi) maeneo mbalimbali nchini. Tutaimarisha pia usalama kwenye masuala ya Mawasiliano.
Sambamba na kukuza huduma ya mawasiliano, tunakusudia kuendelea kuboresha huduma za jamii, hususan afya, elimu na maji. Kuhusu AFYA, kama unavyofahamu, kwenye miaka mitano iliyopita tumepata mafanikio makubwa, ikiwemo kujenga vituo vya kutolea huduma za afya 1,887 (zahanati 1,198, vituo vya afya 487, hospitali za wilaya 99, Hospitali za Rufaa za Mikoa 10 na Hospitali za Rufaa za Kanda 3). Vilevile, tumepunguza vifo vya akinamama wajawazito kutoka wastani wa vifo 11,000 kwa mwaka mwaka 2015 hadi kufikia wastani wa 3,000 hivi sasa na halikadhalika rufaa za kupeleka wagonjwa nje zimepungua kwa asilimia 90 baada ya kuimarisha huduma za kibingwa.
Kwa msingi huo, kwenye miaka mitano ijayo, tunakusudia kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, hususan zahanati, vituo vya afya na Hospitali za Wilaya kwenye maeneo ambako hazipo. Tutaimarisha pia upatikanaji wa dawa, vifaa na vitendanishi na kuongeza watumishi wa afya pamoja na kuimarisha Mifuko yetu ya Bima ya Afya ili kufikia lengo la kuwawezesha wananchi wote kupata Bima ya Afya. Wakati wa ugonjwa wa corona, mbali na kumtunguliza mbele Mwenyezi Mungu, tiba za asili au tiba mbadala zimesaidia sana. Hivyo basi, kwenye miaka mitano, tunakusudia kuimarisha kitengo cha utafiti wa tiba mbadala. Hatupaswi kudharau dawa zetu za asili ama tiba mbadala; na kwa sababu hiyo, matibabu na maduka rasmi ya dawa za asili yataruhusiwa. Zaidi ya hapo, tutaimarisha huduma za matibabu ya kibingwa na ubingwa bobezi ili kufikia viwango vya kimataifa. Tunataka huduma zote za afya zipatikane hapa nchini; na ikiwezekana watu kutoka nje waje kutibiwa hapa nchini. Na kimsingi, tayari wameanza kuja kutibiwa.
Kwenye ELIMU, tutaendelea kutoa elimu ya msingi na sekondari bila malipo; tutaongeza bajeti ya mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuongeza idadi ya wanufaika. Aidha, tutaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya elimu, ikiwemo shule, madarasa, mabweni, maabara, maktaba, ofisi na nyumba za walimu, hosteli pamoja na kumbi za mihadhara. Tutahakikisha tunaendelea kuboresha elimu inayotolewa ili iweze kutoa maarifa na ujuzi wa kutosha kwa wahitimu. Tutahimiza ufundishaji wa masomo ya sayansi na hisabati, hususan kwa wanafunzi wa kike; ambapo tunakusudia kujenga Shule moja ya Sekondari kwenye kila Mkoa kwa ajili ya kufundisha masomo ya sayansi kwa wasichana. Tutaweka pia mkazo mkubwa kwenye elimu ya ufundi. Na katika hilo, tunalenga kuanzisha vituo mahiri vya mafunzo kwa taasisi za elimu ili kuzalisha vijana wenye uwezo unaohitajika Kitaifa, Kikanda na Kimataifa, ambapo kiasi cha Dola za Marekani milioni 75 kimepangwa kutumika: Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam itabobea katika TEHAMA, Taasisi ya Teknolojia Mwanza itabobea kwenye masuala ya Ngozi, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji kitakachobobea katika taaluma za usafiri wa anga na Chuo cha Ufundi Arusha kitabobea katika nishati jadidifu.
Kuhusu MAJI, mafanikio makubwa sana yamepatikana kwenye miaka mitano iliyopita. Tumetekeleza miradi ipatayo 1422 yenye thamani ya takriban shilingi trilioni 2.2. Hii imefanya upatikanaji wa maji safi na salama uongezeke kutoka asilimia 47 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 70.1 mwaka 2020 kwa vijijini; na kwa mijini kutoka asilimia 74 mwaka 2015 hadi asilimia 84 mwaka 2020.
Hata hivyo, napenda nikiri, nilipokuwa kwenye Kampeni moja ya changamoto kubwa niliyoelezwa na wananchi ilikuwa shida ya maji, hususan maeneo ya vijijini. Kwa msingi huo, kwenye miaka mitano ijayo, tutajitahidi kuelekeza nguvu zaidi katika kushughulikia, ikiwemo kwa kuhakikisha fedha zinazopelekwa vijijini kutekeleza miradi ya maji zinatumika vizuri. Nataka kuona miradi ya maji inayojengwa inakamilika kwa wakati. Watendaji wawe wabunifu na kuacha kufanya kazi kwa mazoea. Mito na Maziwa yetu yatumike kikamilifu katika kuwafikisha maji kwa wananchi.
Kwenye miaka mitano ijayo pia, tutaimarisha Mfuko wa Taifa wa Maji ili kuuongezea uwezo wa kifedha wa kutekeleza miradi ya maji. Tutakamilisha pia miradi mikubwa, ukiwemo wa Miji 28 utakaogharimu shilingi trilioni 1.2; Mradi wa Maji wa kutoa maji Ziwa Victoria unaogharimu takriban shilingi bilioni 600 na Mradi Mkubwa wa Arusha wenye thamani ya shilingi bilioni 520. Lakini, nitumie fursa hii pia kuwasihi Watanzania kulinda vyanzo vya maji na miundombinu inayojengwa. Na nitoe wito kwa viongozi wote, mkiwemo Waheshimiwa Wabunge, kulifanya suala la kutunza vyanzo vya maji na miundombinu yake kuwa ajenda muhimu katika shughuli zenu.
Mheshimiwa Spika;
Kwenye miaka mitano ijayo, tumejipanga kuendelea kuimarisha na kukuza uhusiano wetu na nchi mbalimbali kwa kuzingatia Sera yetu ya Mambo ya Nje inayoweka msisitizo diplomasia ya kiuchumi. Tutakuza urafiki na ujirani mwema na pia tutashiriki kikamilifu kwenye shughuli za Kikanda, Kibara na Kimataifa, hususan kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC); Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC); Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa. Tutaendelea pia kushiriki kwenye shughuli za kulinda amani.
Halikadhalika, kwenye miaka mitano ijayo, tutaendeleza jitihada za kukuza na kuimarisha demokrasia, kulinda uhuru na haki za wananchi na vyombo vya habari. Hata hivyo, ningependa kukumbusha kuwa, lengo la demokrasia ni kuleta maendeleo na sio fujo; na hakuna demokrasia isiyo na mipaka. Aidha, Uhuru na Haki vinakwenda samabamba na wajibu. Hakuna uhuru au haki isiyo na wajibu. Vyote vinakwenda sambamba.
Mheshimiwa Spika;
Kama nilivyoahidi wakati wa kipindi cha Kampeni, kwenye miaka mitano ijayo tutaendelea kuboresha mazingira ya kufanya biashara kwa wajasiriamali wadogo (machinga, mama lishe, baba lishe, waendesha boda, bajaji, n.k.). Kama mnavyofahamu, kwenye miaka mitano iliyopita, tulianzisha utaratibu wa kutoa Vitambulisho Maalum kwa wajasiriamali wetu wadogo. Kwenye miaka mitano ijayo, tunakusudia kuviboresha vitambulisho, ikiwemo kuweka picha na taarifa nyingine muhimu, kama ilivyo kwenye Vitambulisho vya Taifa au Pasipoti. Hii itawawezesha wafanyabiashara watakaotumia vitambulisho hivyo kutambulika, ikiwemo kwenye benki na hivyo kupata mikopo kwa ajili ya kukuza biashara. Hii itawawezesha wafanyabiashara wetu wadogo kukua na kutajirika. Na hilo ndilo lengo letu. Tunataka wafanyabiashara wetu wadogo wawe wanakua na kutajirika; na sio siku zote wabaki kuwa wafanyabiashara wadogo.
Kwenye miaka mitano ijayo pia, tutakuza sekta ya sanaa, michezo na utamaduni ambayo inakua kwa kasi kubwa hivi sasa. Kama nilivyoahidi wakati wa Kampeni, tutaikuza zaidi sekta hii, hususan kwa kuimarisha usimamizi wa masuala ya Hati Miliki ili wasaniii waweze kunufaika na kazi zao; tutahuisha Mfuko wa Utamaduni na Sanaa ili kuwasaidia wasanii wetu, ikiwemo kupata mafunzo na mikopo. Tutaanza pia kutenga fedha kidogo kidogo kwa ajili ya kuziandaa Timu zetu za Taifa. Na katika hilo, napenda kutumia fursa hii kuitakia heri Timu yetu ya Taifa, Taifa Stars, kwenye mechi yao dhidi ya Tunisia baadaye leo pamoja na Mwanamasumbwi wetu, Hassan Mwakinyo, ambaye naye ana pambano letu. Watanzania tunataka ushindi.
Mheshimiwa Spika;
Kwenye miaka mitano iliyopita, tumefanikiwa kuhamishia Makao Makuu ya Serikali hapa Dodoma. Viongozi na Watumishi wote wa Serikali wenye kustahili kuhamia Dodoma tayari wamehamia. Kwenye miaka mitano ijayo, tutakamilisha ujenzi wa ofisi na pia kuendelea na ujenzi wa makazi ya watumishi. Zaidi ya hapo, tutaendelea kutekeleza miradi ya miundombinu, ambayo tayari nimeitaja (barabara ya njia nne, Uwanja wa ndege wa Msalato) na kushughulikia suala la upatikanaji maji katika Jiji la Dodoma.
Masuala mengine ambayo tutayapa kipaumbele ni kama ifuatavyo:
Uendelezaji na uboreshaji wa makazi wa wananchi, ambapo tutahakikisha vifaa vya ujenzi vinapatikana kwa gharama nafuu na mikopo ya ujenzi inapatikana kwa riba nafuu;
Tutashughulikia pia masuala ya mabadiliko ya tabianchi;
Tutashughulikia masuala ya watu wa makundi maalum, ikiwemo wazee na watu wenye ulemavu;
Tutaendeleza vita dhidi ya biashara haramu ya dawa za kulevya;
Tutaimarisha sekta ya misitu na nyuki, ikiwemo kwa kuanzisha viwanda vya mazao ya nyuki ili sekta hiyo itoe mchango mkubwa kwenye uchumi wa nchi yetu. Tutahamasisha pia ufugaji wa nyuki.
Tutahakikisha wamiliki wa magari wanatoa mikataba kwa madereva ili kuipa hadhi inayostahili kazi hiyo na kuchochea shughuli za huduma za usafirishaji. Na katika hiyo, ikiwezekana, itatungwa Sheria mahususi.
Tutashughulikia pia kero mbalimbali za wananchi, ikiwemo migogoro ya ardhi, mirathi, n.k. Na katika hili napenda kuwaagiza viongozi wa Serikali kuanzia ngazi za vijiji, kata, tarafa, wilaya na mikoa kuhakikisha wanatenga siku maalum za kukutana na wananchi kwenye maeneo yao ili kusikiliza kero zao na kuzipatia ufumbuzi.
Mheshimiwa Spika;
Kwa ujumla, mambo tuliyopanga kutekeleza ni mengi; ni mengi sana. Baadhi nimeyaeleza na yapo mengine mengi ambayo yameelezwa vizuri kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM yenye kurasa 303, lakini kwa sababu ya muda sitoweza kuyaeleza yote. Hivyo basi, nawaagiza Mawaziri nitakaowateua pamoja na Watendaji kuisoma vizuri, kuielewa na kuitafsri vizuri Ilani hiyo katika Sera na Mipango Kazi ya Utekelezaji kwenye Wizara au Taasisi wanazoziongoza ili ikifika mwaka 2025, tuwe tumeitekeleza yote.
Lakini, najua, ili kuweza kutekeleza Ilani yetu vizuri, tutahitaji sana kupata ushirikiano kutoka kwenye Bunge hili. Kama mnavyofahamu, Bunge ni kiungo muhimu kati ya Serikali na Wananchi. Kwa hiyo, nina uhakika, endapo tutashirikiana vizuri, miaka mitano ijayo itakuwa ya maajabu na mafanikio makubwa kwa nchi yetu. Na binafsi, sina shaka kwamba, Bunge hili litatoa ushirikiano wa kutosha kwa Serikali.
Hata hivyo, napenda niweke bayana kuwa, ninaposema tunaomba ushirikiano haimaanishi kwamba tunataka muunge mkono kila kitu. La hasha! Penye kukosoa kusoeni; lakini kwa hoja na kutoa mapendekezo ya namna ya kushughulikia. Tunahitaji constructive criticism na sio kukosoa kwa lengo la kukosoa tu. Na katika hilo, kwa upande wetu Serikali, tunaahidi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Bunge hili ili kuliwezesha kutimiza majukumu yake ipasavyo. Tutatoa pia ushirikiano kwa Mhimili wa Mahakama, ili nao uweze kutimiza majukumu yake ya kusimamia haki nchini. Kama mnavyofahamu, Mahakama ni muhimu sana katika kuongoza Serikali. Ni muhimu katika kujenga maelewano katika jamii, kudumisha amani na usalama na pia kuchochea shughuli za kiuchumi.
Mheshimiwa Spika;
Kwa mujibu wa Katiba yetu, mimi ni sehemu ya Bunge hili. Hivyo basi, kabla sijahitimisha, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wageni wetu wote walioungana nasi kwenye tukio hili. Baada ya kusema hayo, sasa natamka kwamba nimelifungua rasmi Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Asanteni kwa kunisikiliza!
Mungu libariki Bunge letu na Wabunge wake!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa Kunisikiliza”

- Jun 16, 2020
Hotuba ya Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Wakati wa kulihutubia kwa mara ya mwisho Bunge la kumi na Moja la Jamhuri ya M...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KULIHUTUBIA KWA MARA YA MWISHO BUNGE LA KUMI NA MOJA LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, UKUMBI WA BUNGE, DODOMA, TAREHE 16 JUNI, 2020
Mheshimiwa Spika;
Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aliyetujalia uhai na kutuwezesha kuiona siku ya leo. Kama, Mheshimiwa Spika unavyofahamu, wapo wenzetu ambao tulikuwa nao wakati wa kuzindua Bunge hili, lakini leo hatuko nao. Wametangulia mbele za haki. Hivyo basi, kwa heshima yao naomba tusimame kwa dakika moja kuwakumbuka. Mwenyezi Mungu azipumzishe roho zao mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa Spika, kabla sijaendelea zaidi, naomba kutambua uwepo wa viongozi mbalimbali kwenye Ukumbi huu. Nimefurahi kuwaona Waheshimiwa Marais wetu Wastaafu wote wapo hapa, pamoja na Makamu wa Rais Wastaafu na pia Mawaziri Wakuu wastaafu, akiwemo Mheshimiwa Lowasa na Mheshimiwa Sumaye. Hii ndiyo Tanzania.
Kwa namna ya pekee, napenda nikushukuru wewe, Mheshimiwa Spika, Job Ndugai, Mbunge wa Kongwa, kwa kunipa kibali cha kuja kulihutubia Bunge hili. Aidha, nawashukuru Naibu Spika, Mheshimiwa Tulia Ackson, pamoja na Wenyeviti wa Bunge, Mheshimiwa Andrew Chenge na Mheshimiwa Najma Giga, kwa ushirikiano wenu. Ahsanteni sana. Hiki ni kielelezo cha uhusiano mzuri uliokuwepo kati ya mihimili yetu mitatu katika kipindi chote cha miaka mitano iliyopita.
Nitumie fursa hii pia kueleza kuwa, tangu nimeingia ndani ya Bunge hili leo nimeshuhudia mabadiliko mengi makubwa, tofauti na ilivyokuwa wakati mimi nikiwa Mbunge. Hivi sasa nimeona hata Waheshimiwa Wabunge wanatumia vifaa vya kisasa kama vile tablets. Enzi zetu, vifaa hivyo, havikuwepo. Hivyo basi, nakupongeza sana Mheshimiwa Spika kwa ubunifu huu; na nawapongeza pia Waheshimiwa Wabunge kwa kuweza kuvitumia vifaa hivi; na hivyo kulifanya Bunge lenu kuwa la kisasa namna hii.
Mheshimiwa Spika;
Tarehe 20 Novemba 2015, nilikuja hapa kulizindua Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Leo tena, kwa madhumuni ya kutimiza matakwa ya Katiba yetu, nimekuja kulihutubia kwa mara ya mwisho, ili hatimaye kuweza kuruhusu kuanza kwa mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba 2020.
Utakumbuka, Mheshimiwa Spika, kuwa wakati nikizindua Bunge lako Tukufu, nilitumia fursa hiyo pia kutoa mwelekeo, kueleza malengo na pia kutaja vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Tano. Siku ile, nakumbuka, nilieleza mambo mengi sana, ambayo nafarijika kuona kuwa mengi tumefanikiwa kuyatekeleza, kama ambavyo Waheshimiwa Mawaziri mbalimbali walieleza wakati wakiwasilisha Bajeti zao. Namshukuru pia Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambaye naye wakati wa kuwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Serikali alitoa ufafanuzi wa mafanikio tuliyoyapata. Aidha, jana, Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelezo ya kina kuhusu mafanikio yaliyopatikana.
Kwa ujumla, naweza kusema, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumeweza kutimiza wajibu wetu wa kuwatumikia Watanzania kwa kiasi kikubwa. Na tumeweza kufanya hivyo kutokana na ushirikiano mkubwa tulioupata kutoka kwa Watanzania wote. Nitumie fursa hii kuwashukuru ninyi Waheshimiwa Wabunge kwa kuishauri vyema na pia kuisimamia vizuri Serikali katika kutekeleza majukumu yake. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa Madiwani kwa kusimamia vizuri utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo kwenye maeneo yao. Kama mnavyofahamu, Madiwani ni kiungo muhimu kati ya wananchi na Serikali; lakini pia kati yenu Waheshimiwa Wabunge pamoja na wananchi. Hivyo, hatuna budi kuwashukuru Waheshimiwa Madiwani wetu.
Napenda pia nitumie fursa hii kuwashukuru watangulizi wangu - kuanzia Awamu ya Kwanza iliyoongozwa na Baba ya Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere; Awamu ya Pili, iliyoongozwa na Mzee Ali Hassan Mwinyi; Awamu ya Tatu ya Mzee Benjamin William Mkapa pamoja na Awamu ya Nne ya Mzee Jakaya Mrisho Kikwete– kwa kuweka misingi imara na kutengeneza mazingira yaliyowezesha kupatikana mafanikio hayo mbalimbali katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Na katika hilo, nawashukuru pia viongozi wetu wakuu wastaafu; Mzee wetu Mwinyi (Mzee Ruksa), Mzee wetu Mkapa (Mzee wa Ukweli na Uwazi) na Mzee Kikwete (Mzee wa Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya) kwa ushauri wao mbalimbali waliotupatia katika kipindi chote cha miaka mitano iliyopita. Nikiri tu kwamba ushauri wao umenisaidia sana mimi binafsi pamoja na Serikali ninayoingoza. Nawashukuru pia Makamu wa Rais Wastaafu, Marais wa Zanzibar Wastaafu na Mawaziri Wakuu Wastaafu kwa ushirikiano wao.
Mheshimiwa Spika;
Kama utakavyokumbuka, mojawapo ya ahadi kubwa niliyoitoa wakati wa kuzindua Bunge ilikuwa kudumisha amani, umoja, mshikamano, Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar pamoja na Muungano wetu; na halikadhalika kuimarisha amani, ulinzi, usalama na utulivu wa nchi yetu. Ninayo furaha kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba tumeitimiza ahadi hiyo kwa vitendo.
Watanzania tumebaki kuwa wamoja na tumeendelea kushirikiana licha ya tofauti zetu za dini, kabila, rangi, ufuasi vyama vya siasa au mahali tunakotoka. Muungano wetu pia umeendelea kuimarika. Tumeweza kushughulikia baadhi ya changamoto za Muungano na kufikia makubaliano, ikiwemo kuhusu suala la gharama za kushusha mizigo {landing fees) na pia kufuta kodi ya ongezeko la thamani pamoja na malimbikizo ya kodi hiyo ya shilingi bilioni 22.9 ambayo Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) lilikuwa likidaiwa na TANESCO. Tumefanikiwa pia kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Kuhusu amani, ulinzi na usalama, nchi yetu imeendelea kuwa Kisiwa cha Amani na mipaka yake imebaki kuwa salama. Utakumbuka kuwa, wakati tukiingia madarakani, kulikuwepo na wimbi kubwa la uhalifu wa kutumia silaha pamoja na vitendo vingine vya kihalifu, ikiwemo matukio ya mauaji kule Kibiti na Rufiji. Hata hivyo, kutokana na kazi kubwa iliyofanywa na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, vitendo vyote hivyo vilikomeshwa, na nchi yetu sasa ipo salama. Na katika kuthibitisha hilo, Ripoti ya Global Peace Index ya Mwaka 2020 imeitaja Tanzania kushika nafasi ya kwanza kwa amani na utulivu kwenye eneo la Afrika Mashariki na ya saba kwa nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kwa niaba yenu na kwa niaba ya Watanzania wote, navipongeza sana vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kusimamia amani nchini. Nawashukuru pia Watanzania kwa kutoa ushirikiano kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumejitahidi pia kuimarisha maadili, nidhamu na utendaji kazi Serikalini. Kama tulivyoahdi, hatukuwa na mzaha kwa viongozi na watumishi wazembe, walioshindwa kufanya kazi kwa weledi, nidhamu, maarifa na uadilifu. Viongozi na watumishi wa namna hiyo walichukuliwa hatua za kinidhamu, ikiwemo “kuwatumbua”, kuwashusha vyeo na mishahara, au kuwapa onyo kali.
Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, jumla ya watumishi 32,555 wamechukuliwa hatua mbalimbali, wakiwemo watumishi 15,508 ambao waliachishwa kazi kwa kukutwa na vyeti vya kughushi. Aidha, tulifuta ajira hewa 19,708 zilizoigharimu Serikali kila mwezi kiasi cha shilingi bilioni 19.8. Hatua hii ilitoa fursa ya kuajiri watumishi wapya wenye sifa wapatao 74,173. Vilevile, kufuatia hatua tulizochukua, tuliwapandisha vyeo watumishi 306,917 na kulipa madeni ya watumishi ya mishahara na yasiyo ya mishahara yenye thamani ya shilingi bilioni 472.6 (ya kimshahara shilingi bilioni 114.5 na yasiyo ya kimshahara shilingi bilioni 358.1). Waheshimiwa Wabunge, tulifanya haya kwa lengo kulinda heshima ya wafanyakazi na kuleta nidhamu kwenye utumishi wa umma.
Sambamba na kuimarisha nidhamu Serikalini, tulizidisha mapambano dhidi ya rushwa, uhujumu uchumi na ufisadi. Utakumbuka kuwa, wakati nikizindua Bunge hili niliahidi kuanzisha Mahakama ya Uhujumu Uchumi. Mahakama hiyo ilianzishwa mwaka 2016 na mpaka sasa imepokea mashauri 407, ambapo mashauri 385 tayari yamesikilizwa. Zaidi ya hapo, katika kupambana na adui rushwa, Taasisi yetu ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeweza kufungua mashauri 2,256; ambapo mashauri 1,926 tayari yametolewa uamuzi, na Serikali imepata ushindi kwenye mashauri 1,013.
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita pia TAKUKURU imefanikiwa kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 273.38, zikiwemo fedha walizokuwa wamedhulumiwa wakulima. Aidha, TAKUKURU imetaifisha fedha taslim shilingi milioni 899, Dola za Marekani 1,191,651, EURO 4,301,399, nyumba 8 zenye thamani ya shilingi bilioni 11.6, magari matano yenye thamani ya shilingi milioni 126 pamoja na viwanja vitano (5). Aidha, tumeweza kurejesha mali za Serikali zilizochukuliwa na watu binafsi ama taasisi kinyume cha sheria, zikiwemo nyumba na majengo 98 (ikiwemo Mbeya Hotel), mashamba 23, viwanja 298, kampuni 3, maghala 69. Vile vile, kiasi cha fedha na mali zilizowekewa zuio kusubiria kukamilika kwa taratibu za kisheria za utaifishaji ni shilingi bilioni 52.7; Dola za Marekani milioni 55.8; Euro milioni 4.3, magari 75, nyumba 41; viwanja 47 na mashamba 13.
Hii, bila shaka, inaonesha dhamira yetu isiyo na mashaka ya kupambana na rushwa na ufisadi. Naupongeza Muhimili wa Mahakama, TAKUKURU, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Jeshi la Polisi pamoja na wananchi kwa ujumla kwa kufanikisha mapambano haya. Lakini, nitumie fursa hii pia kuipongeza Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa kufanikiwa kudhibiti na kuvunja mitandao ya biashara hiyo haramu hapa nchini. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, jumla ya tani 97.99 za bangi, tani 85.84 za mirungi, kilo 567.96 za heroin na kilo 23.383 za cocaine zimekamatwa pamoja na watuhumiwa 37,104. Hatua hizi ndizo zilifanya Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), mwaka jana, kuipongeza nchi yetu kwa kupunguza uingizaji wa dawa za kulevya kwa asilimia 90. Lakini niseme, mafanikio haya yasingepatikana kama pasingekuwa na Sheria nzuri zilizopitishwa na Bunge hili. Hivyo basi, nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge kwa kazi nzuri mliyoifanya. Nawashukuru pia Watanzania kwa ushirikiano waliotoa katika kukabiliana na biashara hii haramu.
Mheshimiwa Spika;
Wakati nikizindua Bunge hili, nilieleza kwa kirefu sana kuhusu kutoridhishwa kwangu na hali ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Hivyo basi, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumejitahidi kushughulikia suala hilo, kwa kusimamia uadilifu kwa watumishi waliopewa dhamana ya kukusanya mapato, kuimarisha sheria za kodi, mifumo ya TEHAMA, kupanua wigo wa walipa kodi, kupunguza misamaha na kuziba mianya ya ukwepaji kodi, n.k.
Kutokana na hatua hizo, ukusanyaji wa mapato umeimarika. Mathalan, ukusanyaji wa mapato ya kodi kwa mwezi umeongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 mwaka 2015 hadi shilingi trilioni 1.3 hivi sasa; na mwezi Disemba 2019, TRA ilikusanya shilingi trilioni 1.987, kiwango ambacho ni cha juu kabisa kuwahi kukusanywa kwenye historia ya nchi yetu. Kwa upande wa mapato yasiyo ya kodi, nayo yameongezeka kutoka chini ya shilingi bilioni 688.7 mwaka 2014/2015 hadi kufikia shilingi trilioni 2.4 mwaka 2018/2019. Halikadhalika, mapato ya ndani ya Halmashauri yameongezeka kutoka shilingi bilioni 402.66 Mwaka 2015/2016 hadi shilingi bilioni 661 Mwaka wa Fedha 2018/2019. Hii imefanya mapato ya ndani kwa ujumla, kuongezeka kutoka shilingi trilioni 11.0 mwaka 2014/2015 hadi shilingi trilioni 18.5 Mwaka wa Fedha 2018/2019.
Sambamba na kuongeza ukusanyaji wa mapato, tumedhibiti matumizi ya fedha za Serikali kwa kuzuia au kupunguza safari za nje zisizo za lazima, semina, warsha, makongamano, matamasha na udanganyifu kwenye manunuzi. Aidha, tulipitia upya muundo wa Serikali ili kuongeza ufanisi na kubana matumizi yasiyo ya lazima. Katika zoezi hilo, tuliweza kupunguza idadi ya wizara kutoka 29 hadi 22; na pia kuunganisha taasisi, idara na vitengo mbalimbali. Vilevile, tumepitia miundo ya wizara, taasisi na idara zinazojitegemea 116 na kufanikiwa kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 17.4. Tumeunganisha pia Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoka mitano kuwa miwili kwa lengo hilo hilo la kuongeza ufanisi na kupunguza gharama za uendeshaji. Mabadiliko yote haya yalifanyika baada ya kupata baraka za Bunge hili Tukufu. Hivyo basi, nina haki kabisa ya kusema “ahsanteni sana Waheshimiwa Wabunge”. Bila ya ninyi, haya yote yasingefanyika.
Mheshimiwa Spika;
Kwa sababu ya kuongezeka kwa mapato na kudhibiti matumizi, Serikali iliweza kuongeza bajeti ya maendeleo kutoka wastani wa asilimia 26 hadi asilimia 40. Hii ndiyo imetuwezesha kuboresha huduma mbalimbali za jamii na kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo. Kwa upande wa huduma za jamii, tumepanua wigo na kuboresha upatikanaji wa huduma za elimu, afya pamoja na maji. Kwenye elimu, kama unavyofahamu, tulianza kutoa elimu bila malipo kwa shule za msingi na sekondari ambapo mpaka mwezi Februari 2020 tulikuwa tumetumia shilingi trilioni 1.01 kugharamia.
Lakini, mbali na kutoa elimu bure, tumeongeza idadi ya shule za msingi kutoka 16,899 mwaka 2015 hadi 17,804 mwaka huu; na shule za sekondari kutoka 4,708 mwaka 2015 hadi shule 5,330 mwaka 2020. Vilevile, tumekarabati shule kongwe za sekondari 73 kati ya 89, tumejenga mabweni 253 na vyumba vya maabara ya 227. Aidha, tumetoa vifaa kwenye maabara zipatazo 2,956 na tumepunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la uhaba wa madawati, ambapo idadi yake imeongezeka kutoka madawati 3,024,311 mwaka 2015 hadi kufikia 8,095,207; sawa na ongezeko la zaidi ya asilimia 200.
Kwa upande wa Vyuo vya Ualimu, tumekarabati vyuo 18, tumejenga upya vyuo viwili (Murutunguru na Kabanga) na halikadhalika tumepeleka kompyuta 1,550 kwenye vyuo vyote 35 vya ualimu kwa lengo la kuimarisha ufundishaji wa masomo ya TEHAMA. Kuhusu ngazi nyingine za elimu, tumeongeza Vyuo vya Ufundi (VETA) kutoka 672 mwaka 2015 hadi 712 mwaka 2020; na pia tumekarabati na kuboresha vifaa na miundombinu ya kufundishia katika vyuo 54 vya Maendeleo ya Wananchi (FDC). Vilevile, tumejenga hosteli, kumbi za mihadhari, mabwalo ya chakula na maktaba kwenye vyuo vikuu. Tumeongeza pia bajeti ya mikopo ya elimu ya juu kutoka shilingi bilioni 348.7 mwaka 2014/2015 hadi shilingi bilioni 450 mwaka huu wa Fedha 2019/2020.
Kutokana na hatua hizo, uandikishaji wa wanafunzi wa darasa la kwanza umeongozeka maradufu kutoka wastani wa wanafunzi milioni 1 mwaka 2015 hadi kufikia milioni 1.6 hivi sasa. Aidha, idadi ya wanafunzi wa kidato cha I – IV imeongezeka kutoka 1,648,359 mwaka 2015 hadi 2,185,037. Idadi ya wanafunzi wa VETA imeongezeka kutoka 117,067 mwaka 2015 hadi 226,767 mwaka 2020; na idadi ya wanafunzi wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC) imeongezeka kutoka 6,693 mwaka 2016/17 hadi 9,736 mwaka 2018/19. Kwa upande wa vyuo vikuu, idadi ya wanafunzi wanaojiunga mwaka wa kwanza imeongezeka kutoka 65,064 mwaka 2015 hadi 87,813 mwaka 2020; na wenye kupata mikopo wameongezeka kutoka 98,300 mwaka 2014/2015 hadi 130,883 mwaka 2019/2020. Kwa taarifa hii Waheshimiwa Wabunge, naamini nitakuwa sijakosea nikisema, kazi kubwa imefanyika kwenye sekta ya elimu.
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa sekta ya afya, tumeongeza idadi ya vituo vya kutolea huduma za afya 1,769, zikiwemo zahanati 1,198, vituo vya afya 487, hospitali za wilaya 71, hospitali za mikoa 10, ikiwemo Hospitali ya Mkoa wa Mara, (Mwalimu Nyerere Memorial Hospital) ambayo ujenzi wake ulikwama tangu miaka ya 1970. Vilevile, tumejenga hospitali za rufaa za kanda 3. Hii imefanya vituo vya kutolea huduma za afya kuongezeka kutoka 7,014 mwaka 2015 hadi kufikia 8,783 hivi sasa.
Zaidi ya hapo, tumeajiri watumishi wapya wa afya wapatao 14,479, wakiwemo madaktari wapya 1,000 tuliowaajiri hivi karibuni. Hii imeongeza idadi ya watumishi wa afya nchini kutoka 86,152 mwaka 2015 hadi 100,631 mwaka 2020. Tumeimarisha pia upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, ambapo tuliongeza bajeti yake kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015 hadi shilingi bilioni 270 hivi sasa; na pia tumenunua na kusambaza magari ya kubeba wagonjwa (Ambulances) 117. Vilevile, tumefanikiwa kusomesha madaktari bingwa 301 ambao wamewezesha kuimarisha matibabu ya kibingwa nchini, hususan kwa magonjwa ya moyo, masikio, figo, mifupa, ubongo, kansa, n.k.
Kutokana na hatua hizo, idadi ya akinamama wanaojifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma za afya imeongezeka kutoka asilimia 64 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 83 hivi sasa; vifo vya watoto wachanga (wenye chini ya siku 28) vimepungua kutoka wastani wa vifo 25 hadi vifo 7 kwa kila vizazi hai 1,000; na idadi ya rufaa za kwenda nje ya nchi zimepungua kwa asilimia 95. Aidha, kutokana na kuimarishwa kwa matibabu ya kibingwa, baadhi ya wagonjwa kutoka mataifa jirani wameanza kuja kutibiwa nchini, hususan magonjwa ya moyo. Hii inadhihirisha kuwa, tumefanya kazi kubwa sana katika kuboresha na kuimarisha sekta ya afya nchini. Ninyi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi.
Kuhusu maji, tumetekeleza miradi ya maji 1,423, ambapo miradi 1,268 ni ya vijijini na 155 ni ya mijini. Miongoni mwa miradi mikubwa inayoendelea kutekelezwa ni wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenda Nzega, Tabora na Igunga; Mradi wa Maji wa Arusha pamoja na mradi wa kupeleka maji kwenye miji 28 unaotekelezwa kwa gharama ya shilingi trilioni 1.2. Miradi mingine ya maji ilielezwa vizuri kwenye Hotuba ya Waziri wa Maji wakati wa kuwasilisha Bajeti. Na kutokana na jitihada zilizofanyika, upatikanaji wa majisafi na salama vijijini umeongezeka kutoka asilimia 47 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 70.1 mwaka 2020; na kwa mijini kutoka asilimia 74 mwaka 2015 hadi asilimia 84 mwaka 2020.
Tumeimarisha pia huduma za mawasiliano, hususan kwa kuboresha usikivu wa simu kutoka asilimia 79 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 94 mwezi Disemba 2019. Aidha, idadi ya watumiaji wa simu za mkononi pamoja na watumiaji data imeongezeka maradufu. Na hali hiyo imechangiwa zaidi na kupungua kwa gharama za kupiga simu kwa dakika moja kutoka shilingi 267 mwaka 2015 hadi shilingi 40 tu hivi sasa.
Sambamba na hayo, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumefanikiwa kufufua Shirika letu la Simu (TTCL) ambalo lilikuwa limekufa pamoja na kuongeza hisa zetu kwenye Kampuni ya Airtel kutoka asilimia 40 hadi asilimia 49. Huu ni ushahidi mwingine kwamba kazi tuliyotumwa na Watanzania tumeifanya kikamilifu.
Mheshimiwa Spika;
Mbali na kuboresha huduma za jamii, tumetekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo hususan katika ujenzi, uchukuzi na nishati ya umeme. Tumekamilisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa takriban kilometa 3,500 na hivyo kuifanya nchi yetu iwe na kilometa 12,964 za barabara za lami. Barabara nyingine zenye urefu wa zaidi ya kilometa 2,000 zinaendelea kujengwa. Aidha, kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu, tumejenga barabara za juu (flyover na interchange) Dar es Salaam ili kupunguza tatizo la msongamano wa magari na pia tumekamilisha ujenzi wa madaraja makubwa 13, likiwepo Daraja la Nyerere – Kigamboni, Daraja la Magufuli katika Mto Kilombero pamoja na Daraja la Sibiti; na wakati huo huo ujenzi wa madaraja mengine makubwa unaendelea, likiwemo Daraja la Kigongo - Busisi lenye urefu wa kilometa 3.2, Daraja la Salender lenye urefu wa kilometa 1.03 pamoja na Daraja la Wami lenye urefu wa meta 513.5.
Kwa ujumla, katika Awamu hii, hakuna Mkoa au Wilaya ambayo haikupatiwa fedha za kujenga barabara za lami. Makao Makuu ya Mikoa na Wilaya karibu zote sasa yanameremeta kwa lami na taa za barabarani. Na ahadi yetu ya kuunganisha Mikoa kwa barabara za lami nayo imetekelezwa kwa asilimia kubwa; na kwa Mikoa ya Rukwa-Katavi, Katavi-Tabora, Singida-Tabora, Tabora-Kigoma na Kigoma-Kagera nayo inaendelea kuunganishwa. Mathalan, barabara ya Mpanda – Tabora kilometa 359 wakandarasi wanne wanaendelea kujenga kwa kiwango cha lami; na barabara ya Manyoni – Tabora inakamilishwa kujengwa kwa lami. Vilevile, barabara ya kutoka Mpanda kwenda Kigoma na Kigoma hadi Nyakanazi zinaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hakika, kazi kubwa imefanyika.
Sambamba na kujenga barabara, tunakamilisha Awamu ya Kwanza ya ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro yenye urefu wa kilometa 300 na ujenzi wa Awamu ya Pili kutoka Morogoro hadi Makutupora umbali wa kilometa 422 umefikia asilimia 30. Miradi hii miwili inagharimu shilingi trilioni 7.062. Ujenzi wa sehemu ya Mwanza – Isaka – Dodoma ipo kwenye maandalizi. Tumekarabati pia reli ya zamani kutoka Dar es Salaam hadi Isaka kilometa 970 na halikadhalika tumefufua usafiri wa reli ya Dar es Salaam –Tanga – Moshi - Arusha, ambao ulisimama kwa takriban miaka 20. Lakini, katika kipindi cha miaka mitano, tumefanikiwa kurudisha tena usafiri wa treni kutoka Dar es Salaam kwenda Tanga, Moshi hadi Arusha. Huu ni uthibitisho kuwa kazi kubwa imefanyika.
Kwa upande wa usafiri wa maji, hivi sasa tunafanya upanuzi wa Bandari zetu kuu za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga. Vilevile, tumeboresha usafiri wa maji kwenye Maziwa yetu Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa kwa kuboresha bandari zake pamoja na kujenga na kukarabati meli. Kwenye Ziwa Victoria tumekarabati meli tano za Mv. Victoria, Mv. Butiama, Mv. Clarias, Mv. Umoja na Mv. Wimbi; na tunaendelea na ujenzi wa meli mpya kubwa ya “Mv. Mwanza, Hapa Kazi tu” itakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo. Kwenye Ziwa Victoria pia tumejenga Chelezo kubwa kuliko zote kwenye Ziwa Victoria ili kujenga na kukarabati meli.
Kwa upande wa Ziwa Tanganyika, tumekarabati meli ya mafuta ya MT. Sangara na tupo mbioni kuanza ukarabati wa MV Liemba. Kwenye Ziwa Nyasa tumejenga meli mpya ya kubeba abiria 200 na mizigo tani 200. Jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba wenzetu kule Zanzibar wamenunua meli kubwa mbili kwa ajili ya kutoa huduma katika Bahari ya Hindi. Aidha, mipango ya kujenga meli mpya kwa ajili ya kutoa huduma kati ya Bandari ya Mtwara na Comoro na kati ya Bandari ya Kalema na karemi nchini DRC, nayo inaendelea. Sambamba na hayo, tumejenga vivuko vipya na kukarabati vivuko vya zamani vipatavyo 17.
Kuhusu usafiri wa anga, tumekamilisha ujenzi wa Jengo jipya la Abiria (Terminal III) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere na tunaendelea na upanuzi wa Viwanja vya Kimataifa vya Kilimanjaro (KIA) na Abeid Aman Karume kule Zanzibar. Vilevile, ujenzi wa viwanja vingine 11 upo katika hatua mbalimbali, na tupo mbioni kumpata Mkandarasi wa kujenga Uwanja wa Kimataifa wa Msalato hapa Dodoma.
Tumekamilisha pia ujenzi rada Dar es Salaam, Kilimanjaro na Mwanza; na kule Songwe/Mbeya ujenzi wake unakaribia kukamilika. Sambamba na hilo, tumefufua Shirika letu la Ndege (ATCL) kwa kununua ndege mpya 11, ambapo 8 tayari zimewasili. Hii imeongeza idadi ya wasafiri wa anga nchini kutoka milioni 4.8 mwaka 2015 hadi milioni 5.8 mwaka 2018. Na faida nyingine ya kuwa na ndege tumeiona katika kipindi hiki cha mlipuko wa ugonjwa wa corona, ambapo kwa kutumia ndege zetu tumeweza kuwarejesha Watanzania wenzetu waliokwama nchi mbalimbali, ikiwemo India. Kama tusingekuwa na ndege zetu, ingekuwa vigumu kuwarejesha Watanzania hao.
Ukiachilia mbali uimarishaji wa miundombinu ya usafiri, tumeboresha upatikanaji wa nishati ya umeme. Tumekamilisha Mradi wa Kinyerezi II, ambao umetuongezea Megawati 240; na tunakaribia kukamilisha upanuzi wa mtambo wa Kinyerezi I utakaozalisha Megawati 325 kutoka Megawati 150 za sasa. Muhimu zaidi, tumeanza kutekeleza Mradi mkubwa wa Bwawa la Nyerere kwenye Bonde la Mto Rufiji. Mradi huu unagharimu shilingi trilioni 6.5 na utakapokamilika utazalisha umeme Megawati 2115, ambazo sio tu zitatuhakikishia umeme wa kutosha na wa gharama nafuu lakini pia utatusaidia kukabiliana na tatizo la uharibifu wa mazingira unaosababishwa na matumizi makubwa ya kuni na mkaa. Tunaendelea pia kutekeleza miradi mingine kwa kutumia vyanzo mbalimbali, ikiwemo maji, gesi asilia, jua, upepo, n.k. Aidha, tumekamilisha miradi mikubwa ya kusafirisha umeme, ikiwemo Mradi wa Iringa – Shinyanga; Makambako – Songea; Lindi – Mtwara; n.k.; pamoja na kuendelea kutekeleza Mradi wa Kupeleka Umeme Vijijini, ambapo tumeongeza idadi ya vijiji vilivyofikishiwa umeme kutoka 2,018 mwaka 2015 hadi vijiji 9,112 mwezi Aprili 2020. Nchi yetu ina vijiji 12,268; hivyo tumebakisha vijiji 3,156 tu kufikisha umeme kwenye vijiji vyote nchini.
Kutokana na hatua tulizochukua, idadi ya watumiaji wa umeme (energy access) imeongezeka kutoka asilimia 35 hadi asilimia 85. Na hii imechagizwa na ushushaji wa gharama za kuunganisha umeme kutoka shilingi 177,000 hadi shilingi 27,000. Mafanikio mengine tuliyoyapata kwenye sekta ya nishati ni kupunguza tatizo la kukatikakatika kwa umeme. Katika kipindi chote cha miaka mitano nchi yetu haikuwahi kuingia gizani. Zaidi ya hapo, tumeokoa kiasi kikubwa cha fedha kwa kuzima mitambo ya kuzalisha umeme wa mafuta. Kwa mfano, kwa kuzima mitambo ya IPTL, Aggreko na Symbion tumeokoa shilingi bilioni 719 kwa mwaka. Hii ndiyo imesaidia TANESCO sasa ianze kujiendesha yenyewe.
Mheshimiwa Spika;
Wakati nikizindua Bunge hili, nakumbuka niliahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ingeendeleza jitihada za Awamu zilizotangulia za kukuza uchumi pamoja na kukabiliana na matatizo ya umasikini na ukosefu wa ajira. Hivyo basi, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumejitahidi kutekeleza ahadi hiyo; hususan kwa kukuza sekta zetu kuu za uchumi na uzalishaji, ikiwemo viwanda, kilimo, biashara, madini pamoja na utalii. Kuhusu viwanda, tumejenga viwanda vipya 8,477, ambapo vikubwa ni 201, vya kati 460, vidogo 3,406, na vidogo sana 4,410. Hii imeongeza idadi ya viwanda nchini kutoka 52,633 mwaka 2015 hadi viwanda 61,110 mwaka 2020. Viwanda vipya vilivyojengwa vimeisaidia kuifanya nchi yetu kujitosheleza kwa baadhi ya bidhaa, ikiwemo saruji, nondo na bati. Aidha, viwanda vipya vimezalisha ajira 482,601.
Sambamba na kujenga viwanda, tumeendelea kuweka mkazo kwenye sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji. Kama unavyofahamu, sekta hii bado ni uti wa mgongo wa uchumi wa nchi yetu. Inachangia takriban asilimia 25 ya fedha za kigeni, asilimia 30 ya Pato la Taifa, asilimia 65 ya malighafi za viwandani, asilimia 70 ya ajira zote nchini na asilimia 100 ya mahitaji yetu ya chakula.
Hivyo basi, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita tumeendelea kuipa kipaumbele sekta hiyo. Tumeongeza upatikanaji wa pembejeo na zana za kilimo (mbegu bora, mbolea, viatilifu, matrekta), tumeongeza uzalishaji wa miche ya mazao ya kimkakati, tumejenga na kukarabati skimu za umwagiliaji, vihenge vya kuhifadhi mazao, tumetafuta masoko na kuviimarisha vyama vya ushirika. Vilevile, tumeongeza maeneo ya ufugaji kutoka hekta milioni 1.4 mwaka 2015 hadi hekta milioni 5 mwaka 2020 na hivyo kusaidia kupunguza migogoro kati ya wakulima na wafugaji. Tumejenga pia majosho mapya 104; tumeongeza idadi ya ng’ombe waliohamilishwa kutoka 105,000 mwaka 2015 hadi 514,700 mwaka 2020, tumetoa chanjo ya mifugo na kusambaza dawa za kuogeshea mifugo.
Tumeimarisha pia ulinzi na usimamizi wa rasilimali za uvuvi kwa kuanzisha Kanda Kuu tatu: Ziwa Victoria, Tanganyika na Pwani; pamoja na kudhibiti matumizi ya zana haramu. (Nakumbuka kuna wakati Waziri wa Uvuvi na Mifugo, Mhe. Mpina alikuwa akitembea na rula hadi kwenye migahawa). Zaidi ya hapo, tumehamasisha na kufanikiwa kuongeza idadi wafugaji samaki kutoka 18,843 mwaka 2015 hadi 26,474 mwaka 2020; tumeongeza idadi ya mabwawa kutoka 22,545 hadi 26,445; vizimba vya kufugia samaki (fish cages) kutoka 109 hadi 431; na uzalishaji wa vifaranga kutoka 8,090,000 hadi 14,531,487.
Sambamba na hayo, mwaka 2017, tulizindua Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Kilimo (ASDP – II) wenye malengo wa kukifanya kilimo chetu kuwa cha kisasa, cha kibiashara na chenye tija. Vilevile, tumeiongezea mtaji Benki yetu ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) wa shilingi bilioni 208 kupitia mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Serikali pia imeipatia TADB Dola za Marekani milioni 25.0 (sawa na shilingi bilioni 57.8) ili kuendesha Mfuko wa Dhamana kwa Wakulima Wadogo (SCGS) wenye lengo la kuchagiza mabenki na taasisi za fedha kuongeza utoaji wa mikopo kwa wakulima wadogo na makampuni madogo na ya kati ya kilimo (SMEs). Hii ina maana kuwa, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Serikali imeipa TADB shilingi bilioni 324.8 na hivyo kuiwezesha Benki hiyo kutoa mikopo ya moja kwa moja kwa wakulima, wafugaji na wavuvi yenye thamani ya shilingi bilioni 166.9 kwa riba nafuu.
Kutokana na hatua hizi, mafanikio makubwa yamepatikana. Mathalan, uzalishaji wa mazao ya chakula umeongezeka kutoka tani 15,528,820 mwaka 2015/2016 hadi tani 16,891,974 mwaka 2018/2019. Mahitaji yetu ya chakula kwa mwaka ni chini ya tani milioni 14. Kwa upande wa mazao ya biashara, uzalishaji umeongezeka kutoka tani 796,502 hadi tani 1,144,1631. Kwenye uvuvi, sangara kwenye Ziwa Victoria wameongezeka kutoka tani 417,936 mwaka 2016 hadi tani 816,964 mwaka 2020, na urefu wa sangara umeongezeka kutoka wastani wa sentimeta 16 hadi sentimeta 25.2. Vilevile, mauzo ya samaki wetu nje ya nchi yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 379 mwaka 2015 hadi shilingi bilioni 692 mwaka 2019. Haya sio mambo madogo.
Mheshimiwa Spika;
Kwa lengo la kukuza uchumi pia tumeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini, ikiwemo kuanza kutekeleza Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara nchini (Blueprint) na kuanzisha Wizara Maalum ya Uwekezaji iliyopo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Tumefanya marekebisho ya sheria mbalimbali na kupunguza urasimu katika kutoa vibali na pia kufuta tozo kero 173 ambapo tozo 114 zinahusu sekta ya kilimo, uvuvi na mifugo; tozo 54 za sekta nyingine mbalimbali; na tozo 5 zilikuwa zinatozwa na Wakala wa Usalama na Afya mahali pa Kazi.
Kutokana na hatua hizo, mafanikio makubwa yamepatikana kwenye nyanja za biashara na uwekezaji. Biashara yetu ya nje imeongezeka kutoka shilingi trilioni 11.5 mwaka 2014/2015 hadi kufikia shilingi trilioni 16.6 mwaka 2018/2019. Jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba, Tanzania imekuwa na urari chanya wa mauzo ya bidhaa kwenye masoko ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) pamoja na nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC). Mfano, kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kutoka mwaka 2015 hadi mwaka 2018, Tanzania imekuwa na urari chanya wa mauzo ya bidhaa kwa wastani wa Dola za Marekani milioni 288.04. Kuhusu uwekezaji, Kituo chetu cha Uwekezaji kimesajili miradi mipya 1,307 yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 14.607, zaidi ya shilingi trilioni 30, na itakapokamilika itatoa ajira 183,503.
Mheshimiwa Spika;
Kwenye sekta ya madini, mageuzi makubwa sana yamefanyika, ikiwa ni pamoja na kuanzisha Wizara mahsusi ya Madini, kudhibiti utoroshaji na usafirishaji wa madini ghafi nje ya nchi, kuanzisha masoko ya madini kwenye kila Mkoa, kuongeza ushiriki wa wafanyabiashara wetu wadogo kwenye mnyororo wa uchumi wa madini na kuwafutia ama kuwapunguzia viwango vya kodi. Zaidi ya hapo na muhimu zaidi, mwezi Julai 2017, tulipitisha Sheria ya Kulinda Rasilimali za Taifa (The Natural Wealth and Resources – Permanent Sovereignty - Act 2017), ikiwemo madini. Nakushukuru sana wewe Mheshimiwa Spika pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kupitisha Sheria hii muhimu sana kwa Taifa letu. Kwa hakika, mmeingia kwenye vitabu vya historia vya nchi yetu na naamini vizazi hadi vizazi vitawakumbuka.
Kupitishwa kwa Sheria hiyo ndiko kumewezesha kwa mara ya kwanza Watanzania kumiliki rasilimali zao kwa nguvu za kisheria. Na Sheria hiyo pia ndiyo imefanikisha kuanzishwa kwa Kampuni ya Twiga Minerals Company, ambayo Serikali yetu inamiliki hisa asilimia 16 na Kampuni ya Barrick asilimia 84 ya Hisa, na halikadhalika kutolewa kwa malipo ya fidia ya Dola za Marekani milioni 100 kati ya Dola za Marekani 300 ambazo Kampuni ya Barrick ilikubali kutulipa kufuatia majadiliano tuliyofanya. Napenda pia nikushukuru wewe, Mheshimiwa Spika, kwa Kuunda Kamati Maalum ya Bunge ya Kuchunguza Utoroshaji wa Madini ya Tanzanite, ambayo ilitoa ushauri wa kujenga Ukuta wa kilometa 25 katika Mgodi wa Mirerani, ambao Serikali iliutekeleza.
Kutokana na hatua mbalimbali tulizochukua, sekta ya madini sasa imeanza kukua kwa kasi kubwa, ambapo mwaka jana (2019) iliongoza kwa ukuaji (kwa asilimia 17.7), ikifuatiwa na ujenzi asilimia 14.1. Aidha, mapato yatokanayo na madini nayo yameongezeka. Mathalan, kwenye mwaka wa Fedha 2018/2019 zilikusanywa shilingi bilioni 346 kutoka shilingi bilioni 194 mwaka 2016/2017. Kwenye Mwaka huu wa fedha (2019/2020) tunatarajia tukusanye shilingi bilioni 470, ambapo mwezi Aprili 2020 pekee, licha ya kuwepo kwa tatizo la ugonjwa wa corona, tumekusanya shilingi bilioni 58. Haijawahi kutokea. Kiwango cha juu kabisa tulichowahi kukikusanya kwa mwezi ilikuwa shilingi bilioni 43.
Mafanikio mengine tuliyoyapa kwenye sekta ya madini ni kutolewa kwa leseni 221 za uchenjuaji madini, leseni 4 za uyeyushaji madini (smelting) na leseni 4 za usafishaji madini (refining). Vilevile, tumetenga hekta 38,567 kwa ajili ya uchimbaji mdogo na kuwapatia mafunzo wachimbaji wadogo 10,338. Kwa ujumla, hivi sasa wachimbaji wadogo hawabughudhiwi. Mtakumbuka, zamani wachimbaji wadogo waliendesha shughuli zao kama wakimbizi. Sisi tukasema, hatutaki kuona wananchi wetu wakiwa wakimbizi ndani ya Taifa lao. Na kweli, kwa hatua tulizochukua, tumeweza kujenga heshima kwa wananchi kwa kuwawezesha kutengeneza maisha yao bila bugudha.
Kuhusu utalii, tumechukua hatua mbalimbali za kukuza sekta hiyo ikiwemo kuanza kutekeleza Mpango wa Uendelezaji Utalii Nyanda za Kusini, kuanzisha hifadhi mpya 5 (Hifadhi ya Nyerere, Chato – Burigi, Ibanda-Kyerwa, na Rumanyika-Karagwe) na kuongeza jitihada za kutangaza vivutio tulivyonavyo kimataifa, ikiwemo kuanzisha Chaneli Maalum ya Utalii ya Televisheni ya Taifa. Aidha, kama tulivyoahidi, tumezidisha mapambano dhidi ya ujangili kwa kuanzisha Jeshi Usu na hivyo kusaidia kuongezeka kwa idadi ya wanyama waliokuwa kwenye hatari ya kutoweka kama vile faru na tembo. Mathalan, idadi ya faru imeongezeka kutoka 162 mwaka 2015 hadi 190 mwaka 2019; na tembo wameongezeka kutoka 43,330 mwaka 2014 hadi 51,299 mwaka 2019.
Kufuatia hatua hizo, idadi ya watalii na mapato yameongezeka. Kwa mfano, mwaka 2019 tulipokea watalii 1,510,151 kutoka watalii 1,137,182 mwaka 2015. Aidha, mapato yaliongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.9 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 2.6 mwaka 2019. Kama isingekuwa tatizo la kuibuka kwa janga la korona, naamini mwaka huu pia idadi ya watalii na mapato yake yangeongezeka.
Sekta nyingine, ambayo haijasemwa sana lakini kwa sasa ina mchango mkubwa kwenye uchumi wetu ni sanaa na utamaduni. Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Uchumi ya mwaka 2018, shughuli za Sanaa na Burudani ziliongoza kwa ukuaji mwaka 2018 ambapo ilikua kwa asilimia 13.7 na mwaka 2019 ilishika nafasi ya tatu kwa ukuaji wa asilimia 11.2. Hongereni sana wasanii wetu mbalimbali, hususan wa Bongo Fleva na Filamu. Kazi zenu sio tu zinaburudisha na kuchangia ukuaji uchumi, lakini pia zinaitangaza nchi yetu kimataifa. Na katika hilo, naipongeza Timu yetu Taifa ya Soka, ambayo baada ya takriban miaka 39 kupita, hatimaye mwaka jana (2019) ilifanikiwa kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Afrika. Nawapongeza pia wanamichezo wengine waliopeperusha vyema bendera yetu katika miaka mitano iliyopita, hususan katika ndondi na riadha. Mheshimiwa Spika, kutokana na mchango mkubwa unatolewa na wasanii na wanamichezo nchini, Serikali imejipanga, katika miaka mitano ijayo, kuweka mkazo mkubwa zaidi kwenye sekta hii ambayo imewaajiri vijana wetu wengi.
Sekta nyingine tulizoshughulikia na kutoa mchango kwenye ukuaji uchumi ni ulinzi, sayansi na teknolojia, habari, misitu, ufugaji nyuki, mazingira; n.k. Kwenye ulinzi, mathalan, tumeviimarisha vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, ikiwemo Jeshi, Polisi, Idara ya Usalama, Magereza, Uhamiaji, Zimamoto, TAKUKURU na Mamlaka ya Kudhibiti Madawa Kulevya, kwa kuvipatia vifaa na zana za kisasa). Kwa upande wa sayansi na teknolojia, tumeanzisha vituo mahiri vya mafunzo kwa taasisi za elimu ili kuzalisha vijana wenye uwezo unaohitajika Kitaifa, Kikanda na Kimataifa kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 75. Taasisi hizo ni: Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam itakayobobea katika TEHAMA na Taasisi ya Teknolojia Mwanza itakayobobea kwenye masuala ya Ngozi), Chuo cha Taifa cha Usafirishaji kitakachobobea katika taaluma za anga na Chuo cha Ufundi Arusha kitabobea katika nishati. Kwa sababu ya ufinyu wa muda sitoweza kuzielezea sekta zote. Itoshe tu kusema, Serikali imejitahidi kuimarisha sekta zote ili kukuza uchumi nchini.
Mheshimiwa Spika;
Kutokana na hatua tulizochukua za kuimarisha sekta mbalimbali, uchumi wa nchi yetu umeendelea kukua vizuri, ambapo kwa wastani, katika miaka mitano iliyopita, umekua kwa asilimia 6.9 kutoka ukuaji wa asilimia 6.2 mwaka 2015. Pato ghafi la Taifa limeongezeka kutoka shilingi trilioni 94.349 mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 139.9 mwaka 2019; kwa bei ya miaka husika (yaani current prices). Hii sio tu imetufanya tuwe miongoni mwa nchi zinazokua kwa kasi kiuchumi lakini imeifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi 10 zenye uchumi mkubwa zaidi Barani Afrika.
Tumefanikiwa pia kudhibiti mfumuko wa bei, kutoka asilimia 6.1 mwaka 2015 hadi kufikia wastani wa asilimia 4.4. Sambamba na hilo, akiba ya fedha ya kigeni imeongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 4.4 zilizokuwa zikitosheleza kununua bidhaa na huduma kwa miezi 4.3 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 5.3 mwezi Aprili, 2020 ambazo zinatowezesha kununua bidhaa na huduma kwa miezi 6.2. Kiwango hiki ni zaidi ya lengo lililowekwa kwenye EAC (miezi 4.5) na SADC (miezi 6).
Kwa upande wa mapambano dhidi ya umasikini, umasikini wa kipato umepungua hadi kufikia asilimia 26.4 mwaka 2017/2018. Na kwa lengo la kuendelea kupambana na umaskini, mwezi Februari 2020, tumezindua Kipindi cha Pili cha Awamu ya Tatu ya Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini (TASAF III), ambao utagharimu shilingi trilioni 2.032. Kuhusu kukabiliana na tatizo la ajira, kupitia jitihada zilizofanyika, ikiwemo utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo, tumefanikiwa kutengeneza ajira zipatazo 6,032,299. Kati ya ajira hizo, 1,975,723 zimezalishwa na sekta rasmi na ajira 4,056,576 zimezalishwa na sekta isiyo rasmi.
Mheshimiwa Spika;
Mafanikio mengine tumeyapata kwenye nyanja za sheria na utoaji haki. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumejitahidi kupunguza vitendo vya rushwa, ucheleweshaji na ubambikaji kesi, pamoja na tatizo la mlundikano wa wafungwa. Mathalan, ili kukabiliana na tatizo la ucheleweshaji wa kesi, Serikali iliteua Majaji wapya 17 wa Mahakama ya Rufani, Majaji 52 wa Mahakama Kuu na kuajiri watumishi wa mahakama 859, wakiwemo mahakimu 396. Aidha, tumejenga Mahakama Kuu mpya 2 (Mara na Kigoma); na kukarabati nyingine nne Dar es Salaam, Mbeya, Shinyanga na Sumbawanga. Tumejenga pia Mahakama za Hakimu Mkazi 5, za Wilaya 15 pamoja na Mahakama za Mwanzo 18, na halikadhalika tumeanzisha Mahakama ya Kutembea (mobile court), ambayo imeanza kufanya kazi kwenye Mikoa ya Dar es Salaam na Mwanza na mpaka mwezi Machi 2020 ilishasajili mashauri 337 na kusikiliza mashauri 274. Naipongeza Mahakama kwa kuchukua hatua za kupunguza mrundikano wa kesi, ikiwemo kuimarisha matumizi ya TEHAMA ambayo sio tu imeharakisha uendeshaji wa mashauri lakini pia imepunguza tatizo la rushwa kwa watumishi wa Mahakama.
Vilevile, katika jitihada za kukabiliana na tatizo la ucheleweshaji kesi, nilisaini Hati ya kuiimarisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na pia kuanzisha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali. Uwekaji saini Hati hiyo umeongeza tija na kuleta ufanisi mkubwa katika usimamizi na uendeshaji wa mashauri Mahakamani na pia kwenye Mabaraza ya Usuluhishi ndani na nje ya nchi. Zaidi ya hapo, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumewasamehe wafungwa 42,774 waliokuwa wakitumikia vifungo mbalimbali na hivyo kupunguza mlundikano magerezani. Aidha, katika zoezi la ukaguzi na kusikiliza changamoto za wafungwa na mahabusu, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka imewafutia kesi mahabusu 2,812.
Nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Jaji Mkuu, Jaji Kiongozi, Waheshimiwa Majaji wengine, Mahakimu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkurugenzi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka pamoja na Wakili Mkuu wa Serikali kwa kuimarisha mfumo wa utoaji haki nchini.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumeshughulikia pia kero mbalimbali za wananchi, hususan wakulima, wavuvi, wafugaji, wafanyabiashara, wafanyakazi, wajasiliamali; na bila kusahau migogoro ya ardhi. Kwa upande wa wakulima, wavuvi, wafugaji na wafanyabiashara; kama nilivyosema awali, tumefuta takriban tozo 114 zilizokuwa zikikwamisha shughuli zao. Kwa wafanyakazi, tayari nimeshaeleza kuhusu upandishaji vyeo na malipo ya madeni mbalimbali. Zaidi ya hapo, tumepunguza kodi ya mapato kutoka asilimia 11 hadi asilimia 9 na kulipa deni la shilingi trilioni 1.2 ambalo Serikali ilikuwa ikidaiwa na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii; na hivyo kuwezesha wastaafu kuendelea kulipwa mafao yao.
Kwa upande wa wajasiliamali wadogo, wakiwemo machinga, mama lishe, waendesha bodaboda na bajaji, tumejitahidi kuwawekea utaratibu mzuri wa kuendesha shughuli bila ya kubughudhiwa kwa kuwapatia vitambulisho maalum vilivyotolewa kwa gharama nafuu. Mwaka jana (2019) jumla ya wajasiliamali wadogo 1,591,085 walipatiwa vitambulisho na hivyo kuwafanya waondokane na usumbufu uliokuwepo. Mtakumbuka, zamani, kabla ya utaratibu huo kuanza, wajasiliamali wadogo walikuwa wakibugudhiwa sana na mgambo, ikiwemo kunyang’anywa mali zao. Hivyo, kwa kuanzisha utaratibu wa kutoa vitambulisho hivyo, tumedhihirisha kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ipo kwa ajili ya wanyonge.
Sambamba na kutoa vitambulisho kwa wajasiliamali wadogo, tumetunga Sheria yenye kuzitaka halmashauri zote kutenga asilimia 10 ya mapato yao kwa ajili ya kutoa mikopo isiyo na riba kwa wanawake (asilimia 4), vijana (asilimia 4) na wenye ulemavu (asilimia 2), ambapo hadi mwezi Machi kiasi cha shilingi bilioni 93.2 kilikuwa kimetolewa.
Kero nyingine tuliyoshughulikia ni ya migogoro ya ardhi. Baadhi ya hatua tulizochukua ni kuanzisha Ofisi za Ardhi kwenye Mikoa yote, ambapo sasa huduma zote za upangaji, upimaji, umilikishaji, utathmini pamoja na usajili wa hati, nyaraka, ramani na michoro zinapatikana. Hii imeongeza kasi ya urasimishaji makazi ya wananchi na pia utoaji hati. Jumla ya maeneo ya viwanja yaliyorasimishwa ni 764,158 na tumetoa hatimiliki za kimila 515,474. Kubwa zaidi, ni uamuzi uliofanywa na Serikali wa kuvirasimisha vijiji 920 kati ya 975 vilivyokuwa kwenye maeneo ya hifadhi.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumeimarisha pia uhusiano na ushirikiano na mataifa ya nje pamoja na taasisi za kimataifa. Hii ndiyo sababu tuliweza kuwapokea viongozi wa nchi na taasisi mbalimbali za kimataifa, ikiwemo Vietnam, India, uturuki, Afrika Kusini, DRC, Ethiopia, Misri, Rwanda, Zambia, Zimbabwe, Uganda, IMF, Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika, IFAD, n.k.
Katika kipindi hicho pia tumefungua Balozi mpya 8 (Algeria, Cuba, Israel, Korea, Qatar, Namibia, Sudan na Uturuki). Aidha, nchi mbili, Ethiopia na Poland, nazo zimefungua Balozi zao hapa nchini. Sambamba na hayo, tumeendelea kushiriki katika shughuli na mipango mbalimbali ya kimataifa, ikiwemo ulinzi wa amani, ambapo kwa sasa tuna askari wapatao 2,303 katika nchi za DRC, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Lebanon, Sudan na Sudan Kusini. Zaidi ya hapo, nchi yetu imeaminiwa kuongoza jumuiya mbili za kikanda, Jumuiya ya Afrika Mashariki kuanzia 2016 hadi 2017 na pia kuongoza SADC kuanzia Agosti 2019 hadi mwezi Agosti 2020 tutakapokabidhi. Na moja ya mafanikio tuliyoyapata katika kuongoza taasisi hizo, ni kuzishawishi Nchi Wanachama kuridhia lugha ya Kiswahili kutumika kwenye Taasisi hizo.
Mheshimiwa Spika;
Katika Ibara 151 (c) ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 – 2020, Chama Cha Mapinduzi kiliahidi, nanukuu “kusimamia azma ya Serikali ya kuhakikisha majengo yote ya Wizara za Serikali yanajengwa Dodoma badala ya Dar es Salaam”, mwisho wa kunukuu. Ninayo furaha kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa ahadi hiyo tumeitekeleza. Sio tu kwamba majengo ya Wizara zote yamejengwa Dodoma, bali Serikali yote tayari imehamia, ambapo tarehe 13 Aprili, 2019 nilizindua Mji wa Serikali pale Mtumba. Hii ina maana kuwa tumetekeleza ahadi yetu zaidi ya tulivyoahidi. Nina imani, kwa kutekeleza ndoto hiyo iliyodumu kwa miaka 47, sio tu tumemuenzi Baba wa Taifa lakini pia Wajumbe wa Mkutano wa Halmashauri Kuu TANU waliofikia uamuzi ya kuhamishia Makao Makuu ya nchi Dodoma mwaka 1973. Hivyo, naamini, Mheshimiwa Spika utanisemehe nikisema “CCM Oyee”. Hapo nilikuwa nachomekea tu.
Mheshimiwa Spika,
Kwa kifupi sana, haya ni baadhi tu ya mafanikio tuliyoyapata. Lakini, kama nilivyosema awali, tumefanya mengi, ambayo kama ningeamua kuyaeleze yote hapa, tunaweza kukesha. Kwa bahati nzuri, Watanzania wengi wameona na wanayajua. Hivyo basi, nina imani wataendelea kutuamini na kutupa dhamana ya kuongoza nchi yetu katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Na binafsi naamini, kutokana na misingi imara tuliyoiweka ya ukuaji uchumi pamoja na uzoefu mkubwa tulioupata, endapo wananchi wataendelea kutuamini na kutuchagua kuongoza nchi yetu katika miaka mitano ijayo, tutafanya mambo mengine makubwa zaidi na hatimaye kufanikiwa kutimiza ndoto na dhamira yetu ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati wenye kuongozwa na viwanda pamoja na huduma za kiuchumi (economic services) ifikapo mwaka 2025.
Mheshimiwa Spika;
Pamoja na mafanikio yaliyopatikana, zilijitokeza baadhi ya changamoto. Kama ujuavyo, hapa dunia sio rahisi kufanya jambo lisikumbane na changamoto ama vikwazo. Hivyo basi, sisi pia, katika miaka hii mitano, tumekumbana na changamoto/vikwazo mbalimbali; lakini kikubwa zaidi ni kuibuka kwa ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya corona.
Napenda nitumie fursa hii kulishukuru Bunge hili Tukufu kwa kupitisha Azimio la kunipongeza; japo ukweli ni kwamba pongezi hizi zinatustahili Watanzania wote, ikiwa ni pamoja na Bunge hili. Pamoja na hofu kubwa iliyokuwa imetawala, Bunge hili liliendelea na vikao vyake kama kawaida kwa lengo la kuwatumikia Watanzania; ingawa nafahamu wapo wachache walikimbia. Lakini niseme tu kwamba, kukimbia haikuwa jambo sahihi kwa sababu matatizo au changamoto hazikimbiwi. Kukimbia matatizo au changamoto ni ishara ya udhaifu, ni ishara ya woga lakini pia ni ishara ya kutojiamini. Siku zote njia sahihi ya kukabiliana na matatizo ni kukabiliana nayo.
Na hii ndiyo sababu sisi, tuliamua kukabiliana na ugonjwa wa corona, huku tukiwa tumemtanguliza Mwenyezi Mungu. Na tunashukuru, kwa kufanya hivyo, tumeweza mpaka sasa, kwa kiasi kikubwa, sio tu kufanikiwa kuushinda ugonjwa huo lakini pia kupunguza athari zake, zikiwemo athari za kiuchumi. Kama mnavyofahamu, Benki ya Dunia pamoja na Shirika la Fedha Dunia, yamebashiri kwamba asilimia 60 ya nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Janga la Sahara zitashuhudia ukuaji hasi wa uchumi mwaka huu (2020). Hata hivyo, sisi Tanzania, kutokana na hatua tulizochukua, uchumi wetu unatarajiwa kuendelea kukua vizuri kwa asilimia 5.5. Zaidi ya hapo, tumeweza kulinda ajira za wananchi wetu, tuna uhakika wa usalama wa chakula na pia tumeweza kuendelea na utekelezaji wa miradi yetu mikubwa ya kimkakati. Na hii inadhihirisha kuwa maamuzi yetu yalikuwa sahihi na maamuzi ya Bunge hili kuendelea na vikao nayo yalikuwa sahihi sana. Hongera sana Mheshimiwa Spika na hongereni sana Waheshimiwa Wabunge.
Nitumie fursa hii, kwa mara nyingine tena, kurudia kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuliepusha Taifa letu dhidi ya ugonjwa wa corona. Nawashukuru pia viongozi wa dini pamoja na madhehebu mbalimbali kwa kuitikia wito wa Serikali wa kufanya maombi maalum ya kumwomba Mwenyezi Mungu kutuepusha na Janga la Corona. Dua na maombi yao yamedhihirisha kuwa penye hakuna linaloshindikana. Namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja wajumbe wote wa Kamati ya Kitaifa ya kukabiliana na ugonjwa wa corona. Kwa namna ya pekee, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu kwa kufanya kazi kwa ujasiri mkubwa sana. Vilevile, navishukuru vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na madaktari na wauguzi wetu kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya na wanaoendelea kuifanya ya kuwahudumia wagonjwa wa corona.
Na kutokana na hali ya ugonjwa wa corona nchini kuendelea vizuri, napenda kutumia fursa hii kutangaza kuwa, kuanzia tarehe 29 Juni, 2020 shule zote kuanzia za awali, zifunguliwe na pia shughuli nyingine zote ambazo tulizizuia nazo zifunguliwe. Maisha ni lazima yarudi kama ilivyokuwa zamani. Hata hivyo, naendelea kuwasihi Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari na pia kuzingatia ushauri unaotolewa na wataalam wetu wa afya.
Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge;
Kabla ya kuhitimisha hotuba yangu napenda nirudie kuwashukuru Watanzania wote, wa makundi yote, wakiwemo wakulima, wafanyakazi, wafugaji, wavuvi, wafanyabiashara; kwa kuiunga mkono Serikali yetu, hususan kwa kudumisha amani na mshikamano, kuchapa kazi kwa bidii, kulipa kodi; lakini pia kwa kuwa tayari kufunga mkanda ili kuijenga Tanzania mpya. Nawashukuru pia viongozi wenzangu wote wa Serikali tulioshirikiana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Namshukuru Makamu wa Rais, Mwanamama shupavu na jasiri, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kunisaidia majukumu; Namshukuru Rais wa Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa ushauri na ushirikiano alionipa; namshukuru na kumpongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa heshima na unyenyekevu wake, uchapaji kazi wake mzuri na kutanguliza mbele maslahi ya taifa. Kwa hakika, amenisaidia sana. Aidha, namshukuru Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, pamoja na Katibu Mkuu Kiongozi, Mheshimiwa Balozi John Kijazi, kwa kufanya kazi kwa bidii bila kuchoka. Vilevile, nawashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kufanya kazi bila kuchoka. Nawashukuru pia Makatibu Wakuu; Wakuu wa Mikoa; Makatibu Tawala wa Mikoa; Wakuu wa Wilaya; Makatibu Tawala wa Wilaya; Wakurugenzi wa Wilaya, Manispaa na Majiji; Maafisa Tarafa; Watendaji wa Kata na Vijiji, Mabalozi wa nyumba kumi pamoja na watumishi wote wa Serikali kwa kufanikisha kupatikana kwa mafanikio yote niliyoyataja. Kwa ujumla wao, wote wamenisaidia sana kwenye kufanya kazi. Nawashukuru sana.
Natambua kuwa Mhe. Rais Dkt. Shein anamaliza muhula wake kwa mujibu wa Katiba. Hivyo, napenda kutumia fursa hii kumpongeza kwa utumishi uliotukuka akiwa Makamu wa Rais kwa miaka nane na Rais wa Zanzibar kwa miaka kumi. Mhe. Rais Dkt. Shein ameweka historia ya namna yake katika utumishi wa umma na ametoa mchango mkubwa kwenye Taifa letu. Hivyo basi, sasa anapokwenda kupumzika, namtakia kila la heri na tumwahidi kuendelea kumuenzi kama tunavyowaenzi viongozi wengine wastaafu.
Nakishukuru pia Chama changu, CCM, kwa kuisimamia vizuri Serikali na kuhakikisha Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2015 – 2020 inatekelezwa. Usimamizi mzuri uliofanywa na CCM kwa Serikali katika miaka hii mitano umedhihirisha maneno yaliyowahi kutamkwa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kwamba “Chama legelege huzaa Serikali legelege na Chama kikiwa imara, Serikali nayo huwa imara”.
Navishukuru pia vyama vingine vya siasa ambavyo vilitoa ushirikiano kwa Serikali katika kipindi cha miaka mitano iliyopita. Kama mnavyofahamu, wapo baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa ambao, licha ya tofauti zetu za kiitikadi, walikuwa pamoja na Serikali wakati wote. Na hivyo kusema kweli ndivyo inapaswa kuwa. Sisi sote ni wamoja na tunajenga Taifa moja. Aidha, ninawashukuru wana-habari kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kuhabarisha na kuelimisha umma wa Tanzania pamoja na dunia nzima kwa ujumla kuhusu masuala mbalimbali ya nchi yetu, hususan mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii tuliyoyapata katika kipindi hiki.
Kwa mara nyingine, narudia kulishukuru Bunge hili kwa ushirikiano mkubwa iliotoa kwa Serikali katika kipindi cha miaka mitano. Mbali na kuishauri na kuisimamia Serikali, Bunge hili ndilo lilikuwa likipitisha bajeti na miswada mbalimbali ya sheria iliyoiwezesha Serikali kutimiza majukumu yake kwa ufanisi. Kwa namna ya pekee kabisa, nawashukuru Wabunge wa Chama changu, Cha Mapinduzi, kwa kuiunga mkono Serikali yetu. Kusema kweli mmedhihirisha ule usemi usemao “uchungu wa mwana aujuaye mzazi”.
Nawashukuru pia wabunge wa vyama vingine kwa ushirikiano wao; japo walikuwepo baadhi ambao wenyewe kila jambo walikuwa wakipinga. Lakini nao tunawashukuru. Naamini, wakati ujao watakuwa wamejifunza kwamba kupinga pinga kila kitu sio vizuri.
Napenda pia nitumie fursa hii kuwashukuru washirika na wadau wetu mbalimbali wa maendeleo kwa ushirikiano mkubwa walitupatia. Ushirikiano wao ulitupa nguvu na ari ya kutekeleza miradi ya maendeleo. Hivyo basi, tunawashukuru sana washirika wetu wa maendeleo, ambao kwa bahati nzuri, wiki iliyopita, Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakati akiwasilisha hotuba ya Bajeti ya Serikali aliwataja. Na nimefurahi baadhi ya Waheshimiwa Mabalozi na washirika wetu wa maendeleo tupo nao hapa leo. Ahsanteni sana.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, namshukuru sana Mke wangu, Janet, na pia niwasihi muendelee kumwombea Mama yangu ambaye anaendelea kupambana na ugonjwa wa kiharusi kwa zaidi ya miaka miwili sasa.
Mheshimiwa Spika;
Mwanzoni mwa hotuba yangu, nilieleza kuwa, nimekuja kulihutubia Bunge hili la 11 kwa mara ya mwisho ili kuruhusu kuanza kwa mchakato wa Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika mwezi Oktoba 2020. Nyote mnfahamu, uchaguzi ni zoezi muhimu katika kukuza demokrasia katika nchi. Mbali na kuwapa wananchi fursa ya kuwachagua viongozi wawatakao, inatoa nafasi kwa viongozi kujua endapo bado wanaaminiwa na wananchi.
Na katika hilo, natambua kuwa baadhi yenu hapa mmeonesha nia ya kuwania tena na wapo waliotangaza kutowania tena. Nawatakia maisha mema wale waliotangaza kustaafu na nawatakia kila la kheri wale wanaowania tena. Naamini wengi wenu, hususan wale wenye kuvaa nguo za kijani, watarejea; lakini kwa wale ambao hawatabahatika kurejea, tunawashukuru kwa mchango wao kwenye Bunge hili.
Kwa upande wa Serikali, tumejipanga kuhakikisha uchaguzi wa mwaka huu, kama ilivyokuwa chaguzi zilizopita, unakuwa huru na haki. Kwa sababu hiyo, navisihi vyama vya siasa na wanasiasa kujiandaa vizuri kushiriki katika Uchaguzi huo. Navihimiza pia vyama kutoa fursa za kutosha kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu; aidha, na nawasihi wagombea kuepuka matusi na vurugu. Kama nilivyosema, sisi sote ni wamoja. Hivyo, tubishane kwa hoja kwa kushindanisha Ilani zetu. Lakini niseme, kwa yeyote atakayetaka kuleta vurugu, namtahadharisha kwamba Serikali ipo macho. Uchaguzi haumaanishi kuwa Serikali inaenda kulala. Serikali itaendelea kuwepo kusimamia sheria na taratibu za nchi.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita tumepata mafanikio mengi makubwa. Na mafanikio hayo ni matokeo ya ushirikiano ulikuweko miongoni mwa Watanzania wote. Hivyo, hatuna budi kuendelea kushirikiano kwa lengo la kuiletea maendeleo nchi yetu. Kama ambavyo nimekuwa nikisema mara nyingi, “Sisi Watanzania Tukiamua, Tunaweza”. F
Baada ya kusema hayo, sasa natamka kuwa Bunge hili litavunjwa rasmi kwa tarehe itakayotangazwa kwenye gazeti la Serikali.
Mungu Libariki Bunge la Tanzania!
Mungu Wabariki Wabunge Wote!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza’

- Jan 21, 2020
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA YA KUKARIBISHA MWAKA MPYA ALIYOIANDAA KWA AJILI YA M...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE
HAFLA YA KUKARIBISHA MWAKA MPYA ALIYOIANDAA KWA AJILI YA MABALOZI NA WAKUU WA MASHIRIKA YA KIMATAIFA
IKULU, DAR ES SALAAM, TAREHE 21 JANUARI, 2020
Mheshimiwa Prof. Palamagamba Kabudi, Waziri wa Mambo
ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro, Naibu Waziri wa Mambo
ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki;
Mheshimiwa Ahamada Fakih, Balozi wa Muungano wa Visiwa
vya Comoro na Kiongozi wa Mabalozi nchini;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi
za Kimataifa;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Dunia, kwa sababu ya utandawazi, mageuzi mbalimbali pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia; imekuwa imekuwa kila karne, kila muongo, mwaka, siku na kila dakika ikishuhudia mabadiliko mengi makubwa yakitokea. Na mabadiliko hayo yanazigusa nyanja zote: siasa, uchumi, ulinzi na usalama, jamii, utamaduni, diplomasia, na kadhalika.
Lakini, pamoja na mabadiliko hayo makubwa ambayo yamekuwa yakitokea duniani, yapo baadhi ya mambo ambayo yameendelea kudumu. Hayajabadilika. Na mojawapo ya mambo hayo ni suala la kutakiana heri ya mwaka mpya. Kila mwaka mpya unapoanza, imekuwa ni utamaduni uliojengeka duniani kote kwa watu kutakiana heri. Hivyo basi, nami napenda nitumie fursa hii, kwa niaba ya Serikali pamoja na Watanzania wote, kuwatakia Heri ya Mwaka Mpya wa 2020, ninyi Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa, familia pamoja na watumishi wenu. Aidha, kupitia kwenu, naomba salamu zangu za Heri ya Mwaka Mpya ziwafikie Wakuu wa Nchi, Serikali na Mashirika yote ambayo mnayawakilisha vizuri hapa nchini.
Natambua kuwa kwa baadhi yeu hapa hii ni mara yao ya kwanza kwenu kushiriki hafla ya namna hii hapa nchini. Hivyo basi, napenda niwakaribishe hapa Ikulu lakini pia nchini kwetu kwa ujumla. Kama ambavyo naamini mpaka sasa mmeshuhudia wenyewe, nchi yetu ni tulivu, ina amani, na watu wake ni wakarimu sana. Zaidi ya hapo, najua mnajua kwamba, nchi yetu ina vivutio vingi vya utalii, ikiwemo mbuga za wanyama, uoto mzuri wa asili (misitu, milima, mabonde, maporomoko), maeneo ya kihistoria na halikadhali fukwe nzuri za Bahari na Maziwa. Nawahimiza kutembelea vivutio hivyo ili kujionea uzuri wa Tanzania.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Mwaka 2020 una umuhimu wa pekee sana kwa Tanzania. Mwaka huu Serikali ya Awamu ya Tano ya nchi yetu ambayo Watanzania waliniamini na kunipa ridhaa ya kuongoza, itatimiza miaka mitano na hivyo kuhitimisha muhula wake wa kwanza. Aidha, mwezi Oktoba, nchi yetu itafanya Uchaguzi wake Mkuu. Kwa sababu hiyo, Salamu zangu za Mwaka Mpya kwenu kwa Mwaka huu, mbali na kufanya tahmini ya mwaka uliopita na kueleza mikakati ya mwaka tuliouanza kama ilivyo kawaida, zitagusia pia tathmini yangu ya miaka takriban minne na ushee, ambayo Serikali hii imekuwepo madarakani.
Mtakumbuka kuwa Serikali hii iliingia madarakani mwezi Novemba 2015. Na kama ilivyo kwa Serikali nyingi duniani, wakati wa kampeni za kuingia madarakani, kupitia Ilani yake ya Uchaguzi, tuliahidi mambo mengi kwa wananchi. Aidha, mtakumbuka kuwa, mwaka huo wa 2015 mwanzoni, Umoja wa Afrika ulipitisha Agenda yake ya Mandeleo ya Miaka 50 ijayo hadi mwaka 2063 (yaani the African Union Agenda 2063). Na mtakumbuka pia kuwa, miezi miwili tu kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano kuingia madarakani, yaani mwezi Septemba 2015, Umoja wa Mataifa nao ulipitisha Agenda yake ya Maendeleo Endelevu ya Mwaka 2030 (Agenda 2030 for Sustainable Development Goals – SDGs).
Hivyo basi, mara tu baada ya kuingia madarakani, Serikali, kwa kutumia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2025, Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa Mwaka 2015 – 2020; mipango ya kimataifa niliyoitaja pamoja na mingine ya kikanda, ikiwemo ya SADC na EAC; iliandaa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka mitano 2016/2017 – 2020/2021. Dhima kuu ya Mpango huu ni kujenga uchumi wa viwanda ili kuchochea mageuzi ya kiuchumi na maendeleo ya watu. Aidha, malengo ya Mpango huu ni kuhakikisha rasilimali na fursa za nchi zinatumika vizuri ili kujenga uchumi wa viwanda na kupunguza umasikini. Malengo mengine mahsusi ni kuimarisha kasi ya ukuaji mpana wa uchumi kwa manufaa walio wengi, kuongeza kasi ya kupunguza umaskini, kuongeza fursa ya ajira kwa wote, kuongeza upatikanaji na ubora wa huduma za jamii na kuongeza mauzo nje kwa bidhaa za viwandani.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Mabibi na Mabwana;
Ninayo furaha kueleza kuwa utekelezaji wa Mpango wetu wa Taifa wa Maendeleo unaendelea vizuri. Na kusema kweli, kupitia Mpango huo, nchi yetu imepata mafanikio makubwa sana. Kwa haraka haraka, naomba mniruhusu nitaje baadhi ya mafanikio yaliyopatikana.
Kwanza kabisa, tumeweza kulinda na kudumisha amani na usalama wa nchi yetu. Kama mjuavyo, moja ya sifa ambayo nchi yetu imejijengea duniani tangu kupata uhuru wake mwaka 1961, ni kudumisha amani na utulivu. Hivyo basi, Serikali ya Awamu ya Tano nayo imelipa umuhimu mkubwa suala la amani na usalama. Zaidi ya hapo, tumeweza kuimarisha Muungano wetu, ambapo mwezi Aprili mwaka huu utatimiza miaka 56. Napenda kutumia fursa hii kuvipongeza vyombo vyetu vyote vya ulinzi na usalama, viongozi wetu wa dini pamoja na Watanzania kwa ujumla kwa kuendelea kutunza na kudumisha amani nchini. Aidha, nawashukuru ninyi Waheshimiwa Mabalozi pamoja na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa kwa kuendelea kushirikiana nasi vizuri katika kulinda na kudumisha amani ya nchi yetu. Ahsanteni sana.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Kutokana na kuweza kudumisha amani, nchi yetu imeweza, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, kupata mafanikio mengi makubwa ya kiuchumi. Kwa wastani, tangu Serikali ya Awamu ya Tano imeingia madarakani, uchumi wetu unakua kwa asilimia 7. Tumeweza pia kudhibiti mfumko wa bei, ambapo katika kipindi cha miaka minne iliyopita mfumko wa bei kwa wastani kwa mwaka umekuwa chini ya asilimia 5. Mwaka jana, 2019, mfumko wa bei ulikuwa asilimia 3.5. Akiba ya fedha za kigeni nayo imeimarika, kutoka Dola za Marekani bilioni 4.123 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 5.579, kiasi ambacho kinatosheleza kuagiza bidhaa na huduma kwa kipindi kisichopungua miezi 6.3.
Mafanikio mengine ya kiuchumi yamepatikana katika ukusanyaji mapato, hususan mapato ya kodi ambayo yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 kwa mwezi mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 1.5 hivi sasa, ambapo mwezi Disemba 2019 zilikusanywa shilingi trilioni 1.9. Aidha, katika kipindi cha miaka minne iliyopita, nchi yetu imeweza kuvutia uwekezaji wa zaidi ya Dola za Marekani bilioni 13, sawa na shilingi trilioni 30, na kutengeneza ajira zaidi ya laki moja.
Biashara yetu ya nje nayo imeongezeka kutoka shilingi trilioni 11.5 mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 16.6 mwaka 2018. Ukuaji huu umechagizwa zaidi na kuimarika kwa shughuli kuu za kiuchumi na uzalisha nchini, ikiwemo kilimo, ujenzi, viwanda, madini na utalii. Mathalan, kwenye kilimo, uzalishaji wa mazao ya biashara umeongezeka kutoka tani 796,512 mwaka 2015/16 hadi tani milioni 1,141,774 mwaka 2019 sawa na ongezeko la asilimia 43.3. Sekta ya viwanda pia imeendelea kukua, ambapo kati ya mwaka 2015 hadi sasa viwanda vipya 4,877 vimejengwa.
Vilevile, baada ya mwaka 2017 kufanya marekebisho ya sheria ili kuongeza uwazi katika biashara ya madini pamoja na kuimarisha usimamizi, makusanya ya Serikali na mchango wa sekta hiyo umeanza kuongezeka. Mathalan, mauzo ya dhahabu nje ya nchi yameongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.469 mwaka 2017/2018 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 1.743 mwaka 2018/2019. Aidha, mapato ya Serikali kutokana na madini yameongezeka kutoka shilingi bilioni 168 mwaka 2014/2015 hadi shilingi bilioni 346 mwaka 2018/2019. Kwa upande wa utalii, idadi ya watalii imeongezeka kutoka milioni 1.1 mwaka 2015 hadi kufikia watalii milioni 1.5 mwaka 2018. Aidha, mapato ya utalii yameongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.9 mwaka 2015 hadi Dola za Marekani bilioni 2.488 mwaka 2018.
Waheshimiwa Mabalozi;
Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa;
Kwa sababu ya kukua kwa uchumi, nchi yetu imeweza kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo, hususan katika sekta ya miundombinu. Najua mnafahamu kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa unaoendelea kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma pamoja na ujenzi wa Bwawa kubwa la kuzalisha umeme, Megawati 2,100, katika Bonde la Mto Rufiji. Tumejenga pia barabara takriban kilometa 2,500; barabara nyingine zaidi ya kilometa 2,400 zinaendelea kujengwa; na wakati huo huo kuna kilometa 7,087 ambazo zipo kwenye hatua mbalimbali za maandalizi. Tumekamilisha ujenzi wa madaraja makubwa yapatayo 8, likiwepo Daraja la Magufuli katika Mto Kilombero lenye urefu wa meta 384; na ujenzi wa madaraja mengine unaendelea, likiwemo Daraja la Kigongo - Busisi lenye urefu wa kilometa 3.2, Daraja la Salender lenye urefu wa kilometa 1.1 pamoja na Daraja la Wami lenye urefu wa meta 513.5.
Tumefufua pia reli yetu ya kati kutokea Dar es Salaam – Tanga hadi Moshi ambayo ilikuwa haitoi huduma kwa zaidi ya miaka 20. Kwa upande wa usafiri wa maji, tunafanya upanuzi wa Bandari zetu kuu za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga; na wenzetu kule Zanzibar wapo kwenye hatua mbalimbali za ujenzi wa Bandari Mangapwani na Mpigaduri na wamenunua meli kubwa mbili, ambazo zinatoa huduma katika Bandari ya Hindi. Tupo pia kwenye hatua mbalimbali za ujenzi na ukarabati wa meli takriban 7 kwa ajili ya kutoa huduma katika Maziwa yetu Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa na pia kuboresha Bandari zake. Kuhusu usafiri wa anga, tayari tumekamilisha ujenzi wa Jengo jipya la Abiria (Terminal III) katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere na tunaendelea na upanuzi wa Uwanja wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume kule Zazibar pamoja na viwanja vingine 11. Aidha, ujenzi rada 4 (Dar es Salaam, Kilimanjaro, Songwe na Mwanza) unaendelea na pia tumefufua Shirika letu la Ndege (ATCL) kwa kununua ndege mpya 11, ambapo 8 tayari zimewasili. Hatua hizi zimewezesha kuongezeka kwa idadi ya wasafiri wa anga nchini kutoka wasafiri milioni 4.8 mwaka 2015 hadi wasafiri milioni 5.8 mwaka 2018. Bila shaka, mwaka jana (2019) watakuwa wameongezeka zaidi.
Tunaendelea pia kuimarisha upatikanaji wa nishati ya umeme nchini. Mbali na kutekeleza mradi mkubwa wa kufua umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, tunaendelea na miradi mingine kwa kutumia vyanzo mbalimbali ikiwemo maji, gesi asilia, jua, upepo, n.k. Aidha, tumekamilisha miradi mikubwa ya kusafirisha umeme, ikiwemo Mradi wa Iringa – Shinyanga; Makambako – Songea; Lindi – Mtwara; n.k.; pamoja na kuendelea na Mradi wa Kupeleka Umeme Vijiji, ambapo tumeweza kuongeza idadi ya vijiji vilivyofikishiwa umeme kutoka 2,018 mwaka 2015 hadi kufikia vijiji 8,587 hivi sasa.
Sambamba na kujenga miundombinu, kutokana na kuimarika kwa uchumi wetu, tumeweza kupanua wigo na kuboresha upatikanaji wa huduma muhimu za jamii, hususan afya, elimu na maji. Kwenye afya, tumejenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za afya, ikiwemo vituo vya afya 352 na hospitali za wilaya 69. Aidha, tumeajiri watumishi wa afya wapatao 8,000; tumeongeza bajeti ya dawa na vifaa tiba na kuimarisha huduma za kibingwa, hususan za magonjwa ya moyo, mifupa/mishipa, figo na kansa. Hii imetusaidia kupunguza kupeleka wagonjwa nje ya nchi.
Kuhusu elimu, kama mnavyofahamu, Serikali inaendelea kutoa elimu ya msingi hadi sekondari bila malipo, ambapo mpaka sasa tumetumia zaidi ya shilingi trilioni 1 kugharamia. Tumeongeza pia bajeti ya mikopo ya elimu ya juu kutoka shilingi bilioni 341 mwaka 2014/2015 hadi shilingi bilioni 450 mwaka huu wa Fedha 2019/2020. Hatua hizi zimeongeza udahili kwenye shule za msingi, sekondari pamoja na vyuo vikuu. Zaidi ya hapo, tumejenga miundombinu mbalimbali, ikiwemo madarasa, kumbi za mihadhara, maabara, maktaba, mabweni, hosteli, mabwalo ya chakula, nyumba za watumishi na ofisi. Kwa upande wa sekta ya maji, katika kipindi cha miaka minne iliyopita, tumetekeleza miradi ya maji yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 3. Hii imewezesha hali ya upatikanaji nchini kuimarika kutoka asilimia 56 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 71 hivi sasa (ambapo mijini ni asilimia 84 na vijijini asilimia 64).
Mafanikio mengine tuliyoyapata katika kipindi cha miaka minne iliyopita ni kuongeza mapambano dhidi ya rushwa; kuhamishia Makao Makuu ya Nchi yetu Jijini Dodoma na pia kufanya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ulio huru na haki mwaka jana.
Waheshimiwa Mabalozi;
Waheshimiwa Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Katika nyanja za kimataifa, kama mnavyofahamu, nchi yetu tangu ipate uhuru wake mwaka 1961, imekuwa mstari wa mbele katika masuala ya kimataifa. Hivyo basi, katika kipindi cha miaka cha miaka minne iliyopita, tukiongozwa na Sera yetu ya Mambo ya Nje inayoweka mkazo Diplomasia ya Uchumi, tumeweza kuimarisha uhusiano wetu na nchi mbalimbali pamoja na taasisi mbalimbali za kimataifa. Mimi pamoja na viongozi wenzangu tumeweza kufanya ziara kwenye nchi mbalimbali na kushiriki katika mikutano ya kimataifa. Mathalan, mwaka jana, binafsi nilitembelea nchi za Afrika Kusini, Namibia na Zimbabwe. Aidha, katika kipindi hicho viongozi mbalimbali wa nchi na taasisi za kimataifa walitembelea nchi yetu. Katika kipindi cha miaka minne iliyopita tumeweza kufungua Balozi mpya 7 (Algeria, Cuba, Israel, Korea, Qatar, Namibia na Uturuki).
Mtakumbuka pia kuwa wakati Serikali ninayoingoza ikiingia madarakani, nchi yetu ilikuwa Mwenyekiti wa EAC; jukumu ambalo tulipaswa kulikabidhi mwezi Februari 2016. Hata hivyo, Wakuu wa Nchi wa EAC waliamua kutuongezea mwaka mwingine mmoja hadi mwezi Machi 2017. Mwezi Agosti 2019, nchi yetu pia iliaminiwa na kukabidhiwa jukumu la kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya SADC, ambalo tunaendelea nalo hadi mwezi Agosti 2020. Sambamba na hayo, nchi yetu imeendelea kushiriki katika shughuli na mipango mbalimbali ya kimataifa, ikiwemo ulinzi wa amani, ambapo kwa sasa tuna askari wapatao 2,297 katika nchi za DRC, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Lebanon, Sudan na Sudan Kusini. Aidha, mwezi Julai 2019, Tanzania iliwasilisha Ripoti yake kwenye Umoja wa Mataifa kuhusu utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), na hivyo kuifanya iwe miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa duniani kufanya hivyo.
Haya ni baadhi tu ya mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka minne iliyopita. Na kama nyote mjuavyo, sehemu yoyote, mafanikio hupatikana kutokana na ushirikiano wa wadau mbalimbali. Hivyo basi, kwa moyo wa dhati kabisa, napenda kutumia fursa hii kuyashukuru mataifa na taasisi mbalimbali za kimataifa kwa ushirikiano mkubwa mliotupatia hadi kuweza kupatikana kwa mafanikio hayo. Tunawasihi muendelee kutuunga mkono.
Waheshimiwa Mabalozi;
Waheshimiwa Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Katika kipindi cha Mwaka 2020, Serikali imejipanga kuendelea kutekeleza Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, ambapo kipaumbele chetu kitakuwa kuendelea kudumisha amani na kuimarisha Muungano wetu. Vipaumbele vingine ni kukuza uchumi, ambapo tunalenga uchumi ukue kwa asilimia 7.1; kudhibiti mfumko wa bei ili usizidi asilimia 5; kuimarisha akiba ya fedha za kigeni; kuongeza ukusanyaji wa mapato; na kukuza sekta zetu kuu za uchumi na uzalishaji, yaani kilimo, viwanda, ujenzi, madini pamoja na utalii. Halikadhalika, tutaendelea kuboresha mazingira ya kufanya biashara na uwekezaji nchini. Kama mnavyofahamu, mwezi Julai 2019, nchi yetu imeanza kutekeleza rasmi Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara (yaani Blueprint for Regulatory Reforms to Improve the Business Environment). Napenda kutumia fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Mabalozi kuwashawishi wafanyabiashara kutoka kwenye nchi zenu kuja kuwekeza hapa nchini.
Sambamba na hayo, kama nilivyoeleza awali, mwaka huu mwezi Oktoba, nchi yetu itafanya Uchaguzi Mkuu. Zoezi la Uchaguzi ni muhimu kwa nchi yoyote inayofuata misingi ya kidemokrasia kama yetu. Hivyo basi, Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 unafanyika katika mazingira ya amani, uhuru na haki. Na kama ilivyo kawaida yetu, wakati ukifika, tutazikaribisha nchi na taasisi mbalimbali kuja kuangalia uchaguzi wetu ili kujionea jinsi nchi yetu ilivyokomaa katika nyanja za demokrasia.
Katika nyanja za kimataifa, tumejipanga mwaka 2020 kuendelea kukuza diplomasia yetu, kwa kuimarisha ujirani mwema na uhusiano na mataifa mengine. Tutaendelea pia kutekeleza majukumu yetu kimataifa kwa mujibu wa mikataba mbalimbali tuliyosaini na kuridhia, ikiwemo jukumu letu la kuwahudumia wakimbizi. Na katika hilo, napenda kutumia fursa hii kuishukuru Jumuiya ya Kimataifa kwa kuunga mkono utekelezaji wa zoezi la kuwarejesha kwa hiyari nchini mwao wakimbizi wa Burundi. Zoezi hili linafuata sheria, kanuni na taratibu zote za kitaifa, kikanda na kimataifa na linafanyika kwa ushirikiano wa karibu wa wadau wote wanaohusika ikiwemo Serikali ya Burundi na mashirika ya kimataifa ya UNHCR na IOM. Hata hivyo, tunasikitishwa na hujuma na propaganda zinazofanywa kwa lengo la kukwamisha zoezi hilo.
Mwaka huu, kama mjuavyo, Umoja wa Mataifa utatimiza miaka 75. Tangu kuanzishwa kwake mwaka 1945, Umoja huo umepata mafanikio mengi, lakini pia umeendelea kukabiliwa na chagamoto mbalimbali. Hivyo basi, tunaahidi kuendelea kushirikiana na mataifa yote duniani katika kushughulikia changomoto hizo ili kuufanya Umoja huo kuwa imara zaidi, ikiwemo kwa kuhimiza kuendelea kwa majadiliano ya kuufanyia mageuzi ili kujenga usawa na kuimarisha demokrasia ndani ya Umoja huo. Na katika hilo, tunaahidi kuendelea kutetea msimamo wa Umoja wa Afrika kama ilivyobainishwa kwenye Makubaliano ya Ezulwini (yaani Ezulwini Consensus) pamoja na Azimio la Sirte (yaani Sirte Declaration).
Tanzania pia itaendelea kushirikiana na mataifa mbalimbali katika kushughulikia changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia, ikiwemo masuala ya amani na usalama, hususan katika Bara letu la Afrika. Na katika hilo, tukiwa Wenyekiti wa SADC tutaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama nchini DRC na Lesotho. Naisihi jumuiya ya kimataifa kuendelea kuunga mkono jitahada za kutafuta amani katika nchi hizo na maeneo mengine duniani. Aidha, tutaendelea kushirikiana na mataifa mengine kushughulikia changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi. Kama mjuavyo, hii ni moja ya changamoto kubwa yenye kuikabili dunia kwa sasa. Nchi mbalimbali zimeendelea kukumbwa na majanga mbalimbali yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi. Mathalan, katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, nchi kadhaa za SADC, ikiwemo Afrika Kusini, Angola, Madagasacar, Malawi, Msumbiji na Zimbabwe zilikumbwa na majanga ya vimbunga, mvua kubwa na mafuriko yaliyosababisha vifo na uharibifu mkubwa wa miundombinu.
Nitumie fursa hii kurudia tena kutoa pole nyingi kwa nchi zote zilizokumbwa na majanga hayo. Majanga hayo yanatukumbusha umuhimu wa jumuiya ya kimataifa kushirikiana katika kuzuia athari zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi. Hivyo basi, natoa wito kwa mataifa yote duniani kushirikiana katika kuzuia na kukabiliana na athari zitokanazo na mabadiliko ya tabiachi ikiwa ni pamoja na kutekeleza Mikataba mbalimbali ya kimataifa, ukiwemo Mkataba wa Paris wa Mwaka 2015. Kwa upande wetu, Tanzania, tunaendelea kuchukua hatua zenye lengo la kukabiliana na athari za mabadiliko ya Tabianchi, hususan kwa kuhakikisha tunayatuza mazingira yetu. Mathalan, mwaka jana tulisisitisha matumizi ya mifuko ya plastiki.
Utekelezaji wa mradi mkubwa wa kuzalisha umeme katika Bonde la Mto Rufiji nao ni sehemu za jitihada zetu za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Kama mnavyofahamu, kwa sababu ya kukosekana kwa umeme wa uhakika, wananchi wetu wengi wamekuwa wakitumia kuni na mkaa; na hivyo, kwa wastani kwa mwaka nchi yetu inapoteza takriban ekari 400,000. Hivyo basi, tuna imani kuwa utekelezaji wa Mradi wa Umeme wa Bonde la Mto Rufiji utapunguza matumizi ya kuni na mkaa na hivyo kusaidia kulinda misitu yetu. Zaidi ya hapo, kutokana na kuongeza kwa majanga yatokanayo na athari za tabianchi katika Ukanda wetu, mwezi Februari 2020, Tanzania, ikiwa Mwenyekiti wa SADC, itakuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kwanza wa Mawaziri wenye dhamana ya kushughulikia masuala ya Majanga mbalimbali.
Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje;
Waheshimiwa Mabalozi;
Waheshimiwa Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Nimesema mambo mengi. Lakini kabla sijahitimisha naomba nizungumzie suala moja la mwisho, nalo ni kuhusu changamoto ya tax refund; ambayo ninyi Waheshimiwa Mabalozi mmekuwa mkiilalamikia sana. Napenda niseme kuwa Serikali inaifahamu changamoto hii. Lakini niseme tu kuwa, kimsigi, changamoto hii inatokana na baadhi ya wadau kukosa uaminifu na uadilifu. Hii imefanya Serikali kuongeza umakini zaidi ili kukabiliana na udanganyifu uliokuwa ukijitokeza katika eneo hilo. Hivyo basi, ili kuondoa changamoto hii, niwahimize wadau wote kushirikiana na kufanya kazi kwa uaminifu na uadilifu. Lakini nitumie fursa hii pia kutoa wito kwa Mamlaka ya Mapato kuhakikisha kuwa taratibu za uhakiki zinapokamilika kujitahidi kurejesha kwa wakati fedha zilizokusanywa kwa utaratibu wa tax refund kwa wahusika.
Mabibi na Mabwana; napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuwashukuru Waheshimiwa Mabalozi kwa kuhudhuria Hafla hii. Aidha, nawashukuru kwa ushirikiano mkubwa ambao nchi na taasisi mnazoziwakilisha zinatoa kwa nchi yetu. Napenda niwaahidi kuwa Serikali ninayoingoza itaendelea kushirikiana na na nchi pamoja tasisisi zote mnazoziwakilisha sio tu katika kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo na bali pia kwa lengo la kuifanya dunia kuwa mahali pazuri pa kuishi.
Mungu Ubariki Uhusiano uliopo kati ya Tanzania na nchi pamoja na Taasisi mbalimbali!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 12, 2019
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA WENYEKITI WA CHAMA CHA MAPINDUZI KWENYE HAFLA YA UFUNGUZI WA MAJADIL...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA WENYEKITI WA CHAMA CHA MAPINDUZI KWENYE HAFLA YA UFUNGUZI WA MAJADILIANO YA WAJUMBE WA HALMASHAURI KUU YA CCM TAIFA, MWANZA TAREHE 12 DESEMBA, 2019
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Makamu Mwenyekiti wa CCM- Zanzibar;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Philip Mangula, Makamu Mwenyekiti wa CCM – Tanzania Bara;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, Katibu Mkuu wa CCM;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi;
Ndugu Wajumbe wa Sekretarieti ya CCM;
Ndugu Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa;
Mabibi na Mabwana:
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye kwa neema zake ametujalia uzima na afya njema, na kutuwezesha kukutana mahali hapa. Namshukuru pia Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Bashiru Ally, kwa kunialika na kunipa heshima ya kuwa Mgeni Rasmi kwenye Hafla hii ya Ufunguzi wa Majadiliano ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Nimefurahi pia kuona mara hii, Vikao vya Chama pamoja na Majadiliano haya vyote vinanyika hapa Mwanza. Hili ni jambo zuri kwa kuwa Chama chetu ni cha Watanzania wote; na hivyo, tuna haki ya kufanyia vikao vyetu mahali popote nchini. Sisi ndio tumeshika hatamu za uongozi wa Dola.
Kabla sijaendelea, napenda kutumia fursa hii kukipongeza Chama Cha Mapinduzi, Wajumbe wa NEC, viongozi wa ngazi mbalimbali pamoja na wanachama wote kwa ushindi mkubwa na wa kishindo kwenye Uchaguzi Serikali za Mitaa. Katika maeneo mengi, baadhi ya Vyama viliamua kukimbia mapema. Na hii ni dalili njema kwa Uchaguzi Mkuu wa 2020.
Ndugu Wajumbe wa NEC:
Siku mbili zilizopita, tumesheherekea Maadhimisho ya Miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania Bara. Katika miaka hii yote, Chama Cha Mapinduzi ndicho ki, ukiacha miaka michache ya Uongozi wa Vyama – Mama vya TANU na ASP. Hivyo, kimsingi, tangu tumepata uhuru, CCM imeshika hatamu za uongozi kwa kipindi chote hiki; jambo ambalo ni nadra katika nchi nyingi za Afrika. Kwa hakika, hili ni jambo la kujivunia na kujipongeza sisi wote. Lakini pia imetimia miaka minne (04), tangu Chama chetu kishike hatamu za uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano; na sasa, umesalia mwaka mmoja kukamilisha kipindi cha miaka mitano ya Awamu ya Tano. Lakini, nina uhakika, kila Mjumbe aliyepo hapa angependa Chama chetu kiendelee kushika hatamu za uongozi miaka mingine ijayo. Na hilo litawezekana tu, endapo tutaweza kukidhi mahitaji na matarajio ya Watanzania.
Ni dhahiri kwamba, kama Chama, ili tuweze kufahamu endapo tunakidhi matarajio ya wananchi, hatuna budi kujenga utamaduni na uwezo wa kujitathimini, kujisahihisha na kubadilika. CCM must develop and enhance the capacity to re-invend itself. Tuepuke uongozi wa mazoea. Na kusema kweli, Vyama vingi vinavyojisahau na kuongoza Serikali kwa mazoea, hufikia hatua ya kupoteza imani ya wananchi na uhalali wa kisiasa. Ndicho kilichotokea kwa baadhi ya Vyama vingi vilivyopigania Uhuru Barani Afrika. Ndugu zangu tusifikie huko.
Kwa sababu hiyo basi, ninampongeza sana Katibu Mkuu na Sekretarieti yake kwa uamuzi wa kuandaa Semina hii ya Wajumbe wa NEC. NEC ni Chombo kikubwa cha maamuzi ndani ya Chama Cha Mapinduzi; hivyo Semina hii itumike kama fursa ya kutathimini utendaji wa Chama na Serikali, kwa lengo la kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mahali tulikotoka, mahali tulipo pamoja na mwelekeo wetu kama Chama. Lakini muhimu zaidi ni masuala mapana yanayotakiwa kuzingatiwa kwenye Mwelekeo wa Sera za Chama Cha Mapinduzi kwa Miaka kumi (10) ijayo, yaani 2020 – 2030, pamoja na mipango mahsusi tunayotaka kuitekeleza kupitia Ilani ya CCM ya mwaka 2020 – 2025. Majadiliano haya ya leo yatoe mwelekeo huo.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Washiriki;
Katika Hafla hii fupi ya Ufunguzi, sikusudii kuzungumzia kwa kina kuhusu mafanikio katika utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja shughuli zingine za Seriakali. Na kwa kweli, hiyo siyo kazi yangu; ni kazi ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Na hawa wote wapo hapa na watapewa fursa ya kufanya mawasilisho yao. Kwa upande wangu, nitataja baadhi tu ya hatua muhimu tulizochukua ili kukiimarisha Chama; changamoto tunazokabiliana nazo katika jitihada zetu za kuleta mageuzi nchini; na mwisho nitabainisha masuala machache ambayo, kwa maoni yangu, ningependekeza yazingatiwe kwenye Mwelekeo wa Sera za CCM katika Kipindi cha 2020 – 2030 na Ilani ya mwaka 2020 – 2025.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Washiriki:
Kama mtakavyokumbuka, nilipopewa ridhaa ya kuongoza Chama katika nafasi ya Mwenyekiti wa CCM Taifa, nilitambua haja ya kufanya mageuzi makubwa ndani ya Chama. Mageuzi hayo yalikuwa ni ya kimuundo, kiutendaji lakini pia kiuchumi. Lengo la kufanya mageuzi haya ilikuwa ni kuongeza ufanisi na kuondoa urasimu; kupunguza gharama za uendeshaji na pia kukijenga Chama kiuchumi. Kwa maoni yangu, mageuzi hayo yalikuwa hayaepukiki ili kulinda uhai wa Chama, kurejesha imani ya wananchi na heshima ya Chama chetu. Mageuzi hayo yalijengwa kwenye dhana ya Chama imara, Serikali Imara. Na kusema kweli, ilikuwa ni vigumu kuzungumzia mageuzi makubwa ndani ya Serikali, ilihali Chama kilichokabidhiwa Dola kipo hoi bin taaban. Hii ingesababisha mtanziko mkubwa wa kiuongozi.
Mageuzi makubwa tuliyofanya kimuundo na kiutendaji ni pamoja na kupunguza idadi ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa kutoka 342 hadi 168, hongereni sana wajumbe kwa maamuzi haya, na pia kuwaondoa Makatibu wa Mikoa katika orodha ya Wajumbe wa NEC. Aidha, tuliondoa kada za Katibu Msaidizi na Mhasibu wa Wilaya na Mkoa ili majukumu yao yatekelezwe na Katibu mmoja wa Wilaya au Mkoa. Vilevile, tuliamua kuunganisha Utumishi wa Chama na Jumuiya ili uwe chini ya usimamizi wa Sekretarieti ya NEC. Halikadhalika, tulifuta nafasi ya Katibu wa Uchumi na Fedha kwa ngazi za Mkoa hadi Tawi. Nawapongeza sana wajumbe wa NEC kwa maamuzi haya.
Kiuchumi, tulibaini kwamba, pamoja na uwingi wa rasilimali, mapato ya Chama yalikuwa ni kidogo sana na Chama kilikuwa hakiwezi kujiendesha. Kwa sehemu kubwa mali na rasilimali nyingi za Chama zilikuwa zikiwanufaisha watu binafsi, hususan viongozi wachache waliokuwa wamejimilikisha mali na rasilimali hizo. Chama kikabaki kuwa ombaomba na kutegemea fedha za matajiri wachache waliojiita wafadhili wa Chama. Matajiri hao wachache ndio walikuwa na maamuzi makubwa ndani ya Chama; hakuna mtu aliyefurukuta. Nikasema sitakubali uozo huu uendelee chini ya uenyekiti wangu na chini ua uongozi wenu. Hatuwezi kujenga Serikali na Taifa linalojitegemea wakati Chama kinachoongoza Dola ni tegemezi na ombaomba.
Hatua kubwa niliyochukua kama Mwenyekiti ni kuunda Tume ya Uhakiki wa Mali za Chama, maarufu kama Tume ya Makinikia ya Chama, chini ya Uenyekiti wa Dkt. Bashiri Ally Kakurwa, ambaye sasa ni Katibu Mkuu wa CCM. Tume hiyo ilifanya kazi kwa weledi mkubwa na kubaini kuwa, kwa miaka mingi, CCM ilikuwa shamba la bibi; kila mtu alikuwa akitafuna mali za Chama mahali alipo. Tukaanza kazi ya kurejesha mali za Chama, ikiwemo vyombo vya habari (kama vile Channel Ten), majengo, viwanja, vitalu vya madini, vituo vya mafuta, nk.
Vilevile, tukaanza kupitia upya mikataba mbalimbali ya biashara na uwekezaji ndani ya Chama, ikiwemo ile ya Vodacom, Jengo la Umoja wa Vijana Dar es Salaam, nk. Lakini muhimu zaidi, tukaanzisha Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi na Uendeshaji wa Mali na Rasilimali za Chama. Aidha, tumeunganisha umiliki wa mali na rasilimali za Chama na Jumuiya zake chini ya usimamizi wa Baraza moja la Wadhamini wa Mali za Chama na Jumuiya zake. Hatua nyingine muhimu tuliyochukua ni kuhakikisha mapato na matumizi ya fedha mikoani yanadhibitiwa na Mkao Makuu.
Jitihada hizi zote kwa pamoja, zimeongeza mapato ya Chama kutoka shilingi bilioni 46.1 mwaka 2015/16 hadi shilingi bilioni 59.8 mwaka 2018/19, sawa na ongezeko la asilimia 30. Muhimu zaidi, baada ya kuanza kuthaminisha upya (re-valuation) mali za Chama, thamani yake imeongezeka kutoka shilingi bilioni 41.033 mwaka 2016/17 hadi bilioni 974.66 hivi sasa, sawa na ongezeko la asilimia 2275.3. Nimearifiwa kuwa zoezi hili la re-valuation limefanyika katika mikoa 13 tu likijumuisha baaadhi ya mali za Jumuiya. Zoezi hilo litaendelea kwenye mikoa iliyosalia. Nina uhakika thamani ya mali za chama itakuwa ni ya Mabilioni na Mabilioni ya fedha.
Tafsiri yake ni kwamba mapato ya Chama yataendelea kuongezeka kwa kasi zaidi. Na katika hili, nampongeza sana Dkt. Haule na Idara nzima ya Uchumi na Fedha kwa jitihada zao kubwa walizofanya. Ni matumaini yangu, mkiendelea na jitihada hizi, Chama chetu kitaweza kujitegemea kwa asilimia mia moja badala ya kuwategemea watu wanaojiita wafadhili, lakini pia mtaweza kuongeza maslahi ya watumishi wa Chama, ambayo kwa sasa ni madogo sana. Jambo lingine la kujivunia na kufurahisha zaidi ni kwamba, katika miaka minne iliyopita, Chama chetu kimeendelea kupokea wanachama mbalimbali kutoka Vyama vya Upinzani, wakiwemo Wabunge na Madiwani. Hii imepelekea ruzuku ya Chama kuongezeka kutoka shilingi bilioni 12.4 kwa mwaka (mwaka 2015/16) hadi bilioni 13.5 kwa mwaka, hivi sasa.
Hayo ni baadhi ya mageuzi ya kimuundo, kiutendaji na kiuchumi tuliyotekeleza ndani ya Chama. Lakini ninafahamu changamoto zilizopo katika kuyafanya mageuzi haya yashuke chini kabisa hadi kwenye ngazi ya Tawi na Shina. Na hili ndilo jukumu la Sekretarieti ya Chama. Tambueni kuwa Chama ni Mashina na Matawi; elekezeni jitihada zenu huko. Ninaamini, mkifanya hivyo, Chama chetu kitakuwa imara zaidi.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe:
Mwelekeo wa Sera za Chama Cha Mapinduzi, kwa kipindi cha miaka kumi 2010 – 2020, ulijikita katika kujenga uchumi wa kisasa na kuwawezesha wananchi; vivyo hivyo na Ilani ya Uchaguzi ya 2015 – 2020 iliandaliwa kwa kuzingatia Mwelekeo huo. Lakini nikiri kwamba sisi, katika Serikali, hatukuitumia Ilani ya Chama kama Msahafu au Biblia. Ni kweli, tumetumia Ilani katika kutekeleza mambo mengi lakini hatukupenda kujizuia kufanya jitihada nyingine zenye maslahi mapana kwa Watanzania na Taifa kwa ujumla. Hivyo, pamoja na kutumia Ilani kama mwongozo, tuliona kuna umuhimu wa kuangalia mahitaji halisi ya maendeleo kwa sasa na kuchukua hatua muafaka. Hivyo, tulijadiliana na kukubaliana kwamba baadhi ya hatua za msingi hazina budi kuchukuliwa hata kama siyo sehemu ya Ilani, ili mradi zinalenga kuharakisha maendeleo na kuharakisha utekelezaji wa Ilani yenyewe.
Hivyo basi, mtaona kwamba mafanikio yatakayotajwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mkamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, kwa miaka minne iliyopita, baadhi yake yamebainishwa ndani ya Ilani na mengine hayatajwa kwenye Ilani. Hata hivyo, yote yamejielekeza kwenye kuleta mageuzi ya kijamii na kiuchumi nchini. Mathalan, mtaelezwa kuhusu mafanikio tuliyopata katika kuleta mabadiliko kwenye Utumishi wa Umma, hususan kurejesha heshima, nidhamu, uadilifu, uchapakazi, uzalendo na ari ya kujitolea kwa Taifa. Vilevile, mtaelezwa mfanikio makubwa katika sekta za kijamii kama vile afya, elimu, maji na umeme. Mtaelezwa pia kuhusu jitihada tulizofanya katika kuimarisha miundombinu ya usafiri na usafirishaji kama vile barabara, reli, maji na anga. Kwa ujumla, hakuna sekta iliyoachwa nyuma, iwe ni kilimo, ufugaji, uvuvi, utalii, ulinzi na usalama, nk. Haya yote yatawasilishwa kwenu Waziri Mkuu pamoja na Makamu wa Pili wa Rais na mnaweza kupata muda wa kuyatathimini zaidi. Lakini mafanikio yote hayo yanatokana na jitihada za pamoja na ushirikiano kati ya Chama na Serikali. Nami ninawashukuru sana viongozi wote wa Chama na Serikali pamoja na Watanzania wote kwa ujumla katika kufanisha haya yote.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe:
Katika utangulizi, nilisema ningezungumzia baadhi ya changamoto ambazo tumekuwa tukikabiliana nazo kama Serikali katika jitihada zetu za kuleta mageuzi ya kijamii na kiuchumi. Kusema kweli, mimi huwa sipendi sana kuzungumzia changamoto; huwa napenda kuzikabili moja moja, head on. Lakini kwa minajili ya hadhara hii, nitazitaja mbili tu. Moja kubwa ni kukosekana kwa utayari, miongoni mwa baadhi wananchi na viongozi pia, wa kukubali na kuendana na mabadiliko, yaani resistance to change. Bado watu wanashindwa au wanachelewa kuelewa kuwa tupo kwenye zama mpya ambapo nia yetu kubwa ni kujenga Taifa linalojitegemea kiuchumi. Hawajaelewa kwamba ni lazima tujenge nidhamu na uadilifu katika kazi na kuelekeza rasilimali zetu kwenye mikakati ya maendeleo inayolenga kuleta ukombozi kiuchumi. Na kwamba ni lazima tupige vita rushwa, uzembe na mambo mengine ambayo yatatuchelewesha kufika huko. Ninachokiona mimi bado kuna uzembe, kushindwa kuchukua maamuzi na kupenda fedha za dezo ambazo hazipo. Haya yote yanatokana na mazoea ya utegemezi na kushindwa kutambua kuwa tunapojenga misingi ya kujitegemea, hatuna budi kufunga mikanda na, wakati mwingine, kupata shida kwa muda ili tujitegemee.
Hiyo ni changamoto ya kwanza kubwa. Lakini ya pili ambayo ni kubwa pia ni hujuma dhidi ya jitihada za Serikali zinazofanywa na baadhi ya watu wasioitakia mema nchi yetu. Hujuma hizi zinalenga kufifisha jitihada zetu za kujikomboa kiuchumi kwa maslahi yao binafsi. Watu hawa kamwe hawataki kuona tunadhibiti rasilimali zetu ambazo walikuwa wakizivuna na kusafirisha wanavyotaka, bila kuulizwa na mtu. Zaidi ya hapo, watu hawa hawatakubali tutekeleze miradi mikubwa ya kimapinduzi itakayoharakisha maendeleo nchini, ikiwemo Bwawa la Nyerere, SGR au Kufufua Shirika la ATCL, wasingependa tutoe elimu bure, wasingependa tupeleke umeme katika vijiji vyote na mengine mengi. Wangependa tuendelee kuwategemea wao, ilihali wao wanaishi kwa kutegemea rasilimali zetu.
Hivyo, wanatumia kila njia kufifisha jitihada zetu na kupenyeza ajenda zao. Wakati mwingine, wanatumia Asasi za Kiraia (Civil Societies) na Mashirika yasiyo ya Kiserikali (NGOs) na kujifanya wanatufundisha demokrasia na haki za binadamu, ilihali wao wenyewe wanavunja misingi hiyo kwa kujenga mifumo ya kinyonyaji, kuchochea machafuko na kuingilia uhuru wa mataifa mengine. Wakati mwingine, watajenga mazingira ya taharuki na kusema ebola imeingia Tanzania. Ili mradi tu ionekane nchi haiko salama. Inatupasa tutambue kuwa hii ndiyo changamoto kubwa katika mapito yetu kuelekea ukombozi wa kiuchumi; na tusiposimama imara na kujenga uzalendo na moyo wa kujitolea kwa Taifa, hatuwezi kushinda. Ni lazima tujitambue, tujue tulipotoka, mahali tulipo na mwelekeo wetu kwa manufaa ya Watanzania.
Na mimi niwajulishe nyinyi wajumbe wa NEC, nyinyi ndio chombo muhimu cha kuleta mabadiliko katika Taifa hili, hayupo mwingine wa kuwasemea na hatapatikana kwa sababu Serikali hii inaongozwa na Chama Cha Mapinduzi, na kiongozi wa Serikali kupitia chombo kilichopo juu cha mafanikio ama kutokufanikiwa ni nyinyi wajumbe wa NEC mliopo hapa. Na ndio maana najitahidi kuzungumza kwa uwazi sana ili kusudi muelewe, mzijue changamoto lakini pia tujitafakari ni kwa namna gani Taifa tunaweza kulipeleka mbele ama kulirudisha nyuma katika maendeleo ya kiuchumi.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Washiriki:
Nilianza Hotuba yangu kwa kuwapongeza wana-CCM wenzangu kwa kushinda Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Nimewakumbusha pia kuhusu mageuzi tuliyofanya kwenye Chama chetu na mafanikio yaliyopatikana kutokana na mageuzi hayo. Nimewaeleza pia kuwa mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka minne iliyopita yatawasilishwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Lakini nimegusia pia kuhusu changamoto tunazokabiliana nazo.
Ninapoelekea kuhitimisha, naomba sasa nipendekeze kwenu baadhi ya masuala ninayodhani ni muhimu yakazingatiwa kwenye Mwelekeo wa Sera za Chama chetu kwa miaka 10 ijayo na Ilani ya Uchaguzi 2020 – 2025. Ingawa nitayataja masuala husika kisekta, msingi wa Mwelekeo wa Sera za CCM na Ilani uwe ni kujenga Taifa linalojitegemea ambalo nguzo kuu ya uchumi wake ni sekta ya viwanda. Tunataka tufike mahali ambapo Taifa letu litakuwa na uwezo wa kujitegemea kiuchumi na kutekeleza mipango yake ya maendeleo bila kutegemea misaada. Nilikwisha eleza ndugu zangu Tanzania Tajiri, sisi ni Matajiri kwelikweli, na hii narudi ndugu zangu kwa wajumbe wa NEC Tanzania ni Tajiri, ni Tajiri, walamsiwe na wasiwasi na utajiri wa Tanzania, sisi ni Matajiri kwelikweli.
Ndio maana tulipofanya mabadiliko katika sekta ya madini, mwanzoni tu makusanyo yalikuwa shilingi Bilioni 191, kwa taarifa nilizopata jana, makusanyo mwaka huu yatafika karibu shilingi Bilioni 600. Na baada kubadilisha ile sheria, sasa watu wanaotaka kushiriki na sisi katika madini wamejitokeza na wanakuja, ndio maana mmesikia hivi karibuni imetangazwa kampuni ya Twiga ambayo tutashirikiana na kampuni ya Barrick, na wiki hii wanakuja kwa ajili ya majadiliano na kumaliza kila kitu na pale faida tutakuwa tunagawa 50 kwa 50, hisa sisi tutakuwa na asilimia 16 na wao zilizobaki, siku za nyuma sisi ilikuwa sifuri, huu ndio mwelekeo tunaoutaka.
Tanzania tuna almasi nao tunafanya nao mazungumzo, hata jana walikjuwa na mazungumzo Dar es Salaam namna ya kubadilisha zile hisa. Lakini Tanzania tuna kila kitu, ukienda kule Zanzibar kuna mafuta, yale mafuta yakishakuwa Zanziba maana yake hata Bara yapo, tuna gesi ya etheny ipo, tuna helium, ukienda kule kwa Waziri Mkuu kuna graphite, anakanyaga udongo lakini ndani kuna graphite, ndugu zangu Wamwela hawajui ni kama Wasukuma ambavyo walikuwa hawajui almasi wakawa wanacheza nazo kwenye bao mpaka alipokuja Williamson, Tanzania ni Tajiri ndugu zangu. Kwa hiyo wala tusiogope kuyasemea haya na kusimama imara kulinda rasilimali zetu. Dhababu ipo kila mahali, inawezekana hata hapa ukichimba utakuta dhahabu kwenye jengo hili, dhahabu ipo kila mahali.
Ndugu zangu sisi ni matajiri, tuna chuma, yale mashapo ya chuma yaliyopo kule Liganga ni ya Mabilioni na Mabilioni na ndanbi ya kile chuma kuna titanium, kuna makaa ya mawe, yaani unapokwenda, kule kwenu Bukoba kuna madini ya kioo yapo yamejaa pale, kwenye maendeo alipozikwa Profesa Mulokozi ni madini ya kioo tu yamejaa pale, Kisarawe kule kuna madini ya kutengeneza malumalu bora kabisa duniani, Tanzania ndugu zangu ni matajiri, sisi ni matajiri ila hatujiamini kama sisi ni matajiri.
Mbuga za Wanyama, mpaka sasa tunaongoza tuna Hifadhi za Taifa 22 zina Wanyama wote, hata mti mrefu kuliko yote Afrika upo Tanzania, Mlima mrefu kuliko yote Afrika upo Tanzania Mlima Kilimanjaro, Mungu ametupendelea, Tanzania Hoyee
Kwa hiyo ndugu zangu wanjumbe nataka niwaeleze hili kwamba nchi hii ni Tajiri. Ni lazima Ilani tutakayoitengeneza au mwelekeo wa Chama Cha Mapinduzi ujielekeze ni namna gani tutaweza kuitumia hii rasilimali tuliyopewa na Mungu katika kujiletea mabadiliko ya kiuchumi sisi kama Taifa. Maamuzi hayo wa kuyafanya ni nyinyi wajumbe. Mtakayoyaamua ndio yatailazimu Serikali itakayoingia madarakani baada yam waka 2020 kutekeleza haya maamuzi yenu, nyinyi ndio walimunyinyi ndio viongozi, Serikali ni lazima itekeleze. Ndio maana nasema katika kikao hiki mjadili kwa uwazi kabisa, msimung’unye maneno, kama ni jipu pasua, kama ni mkia ukate. CCM Hoyeee
Hii misaada tunayopata ni ya kutupumbaza, ni ya kutupumbaza, lakini hata idadi yetu ya Watanzania tuliopo, sisi tuna idadi kubwa kuliko nchi yoyote ya Afrika Mashariki, tupo Milioni 55, idadi ya watu ni mtaji, ukitengeneza viatu vyako vitavaliwa na watu Milioni 55 kuliko nchi yenye watu wachache, kwa hiyo unapokuwa nan chi yenye idadi ya watu wengi ni soko, ni uchumi. Ndio maana China ipo juu katika uchumi duniani ni kwa sababu ina watu wengi kwa hiyo soko lipo, ukiuza kahawa hata kama Wachina wangekunywa kijiko kimoja kimoja kahawa yetu yote ingeliwa ni kwa sababu wana soko.
Sisi tuna ng’ombe Milioni 32.5 na ni wa pili katika Afrika, tumeweza kwa sababu tuna soko, lakini mifugo yetu tungeipeleka China kwenda kuliwa na watu Bilioni 1.3 au India watu Bilioni 1.3 ni soko. Kwa hiyo sisi Tanzania tuna soko kwa sababu tuna idadi kubwa ya watu. Na ukishakuiwa na soko wewe ni Tajiri, ukitengeneza nguo zako ukaziuza kwenye soko lako utaweza kuliko yule mwenye idadi ndogo ya watu. Kwa hiyo tutumia fursa ya kuwa na idadi kubwa katika Afrika Mashariki na pia katika Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) tuna watu wengi. Lakini pia tuitumie Ilani ya Uchaguzi tunayoiandaa ili iakisi fursa za nchi yetu ambayo imezungukwa na nchi 8. Kuzungukwa na majirani wa namna hiyo, wengine hawana njia ya kwenda bandarini ni uchumi, kwa sababu wakitaka kusafirisha mizigo yao ni lazima wapiti humu. Kwa hiyo unapaswa kutengeneza miundombinu itakayowalazimisha kupita hapa ili nyinyi mtengeneze fedha, ukishakuwa na bandari 3 kubwa, Bandari ya Tanga, Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Mtwara ni uchumi, bado bandari ya Zanzibar na Pemba, tuna bandari 5 katika nchi moja. Tukivitumia hivi vyote Tanzania ni Tajiri, tukitumia bandari yetu kutoka Moa hadi Msimbati zaidi ya kilometa 1,424, Zanzibar yote na Pemba imezungukwa na maji, Mafia Maji, Mwanza hii imezungukwa na maji, ziwa Victoria asilimia 51 lipo Tanzania, bado ziwa Tanganyika, ziwa Nyasa, bado na mito, sisi ni matajiri. Kwa hiyo ndugu zangu wajumbe tujielekeza katika mwelekeo huo wa kujitambua kuwa sisi ni matajiri, kwa hiyo mipango yetu tunapoipanga ambayo ni lazima itekelezwe na Serikali katika kipindi cha miaka 10 inayokuja iakisi utajiri wetu na ijielekeze kujenga uchumi wa Tanzania, Tanzania hoyeee.
===
Na katika hilo, nianze na sekta za kijamii, yaani afya, elimu na maji ambazo ndio msingi hasa wa kujenga nguvu kazi ya Taifa kwa ajili ya kuendeleza sekta zingine. Katika sekta ya afya, itafaa mwelekeo wetu uwe ni kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi kwa kuhakikisha kila Kata, Kijiji na Mtaa unakuwa na kituo cha kutolea huduma (health facility) na pia kujenga Hospitali za Wilaya kwenye Wilaya zote zilizosalia. Lakini la muhimu zaidi ni kupanua zaidi huduma za kibingwa (specialist services) hadi kwenye Hospitali za Mikoa. Kwenye elimu, tujielekeze kwenye kuinua viwango vya ubora wa elimu ya msingi na sekondari kwa kuongeza maabara na vifaa vya maabara, kuongeza walimu na kuboresha mitaala ili elimu iandane na mazingira halisi ya kitanzania na kuzalisha wahitimu wanaojitegemea.
Aidha, msukumo mkubwa uwe ni kuimarisha elimu ya ufundi na kuongeza zaidi idadi ya vyuo vya ufundi kama kitovu cha uhawilishaji wa teknolojia (technology transfer) na ukuzaji wa sekta ya viwanda. Kwenye Elimu ya Juu, hatuna budi kuhakikisha programu za mafunzo zinatolewa kulingana na mahitaji ya kisekta ya Taifa letu ili kuharakisha mageuzi ya kiuchumi. Vilevile, tuongeze uwezo wa Serikali kugharamia Elimu ya Juu kwa kuhakikisha kila mwanafunzi anapata mkopo. Muhimu zaidi, ni kuhakikisha mfumo mzima wa elimu unajengwa kwa kuzingatia mila na utamaduni wa kitanzania. Kwenye huduma ya maji, tuongeze vyanzo vya maji na kasi ya usambazaji ili kutosheleza mahitaji kwa asilimia mia moja (100), mijini na vijijini. Inawezekana haya ninayoyazungumza wengine wakasema haiwezekani, lakini nataka kuwaeleza ndugu zangu wajumbe wa NEC yanawezekana kwa sababu tupo kwenye Taifa Tajiri na sisi ni Matajiri.
Sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi zipewe msukumo mpya na wa kipekee, kwani ndizo kichocheo cha ukuaji wa sekta ya viwanda. Kuwepo na mikakati madhubuti ya kusimamia mnyororo mzima wa thamani kwa mazao yote ya kimkakati; kuanzia pembejeo, uzalishaji, mavuno, uhifadhi, usindikaji hadi masoko. Na utaratibu huu ufanyike kwenye mazao yote ya kilimo, ufugaji na uvuvi. Kwa sababu kuna wakati inafika hata mbegu za kupanda ni shida, inafika mahali hata mbegu za kupanda mahindi hapa tunaagiza nje. Suala jingine muhimu ni kuondoa kabisa utegemezi katika mbegu za mazao ya kilimo (seed dependency), ambapo kwa sasa, takriban asilimia 70 ya mbegu zinatoka nje. Hii ni aibu. Vilevile, tujenge Mfumo wa Ushirika ambao, pamoja na kuwa wa hiari, udhibitiwe na Serikali ili kumlinda mkulima. Tupunguze utegemezi wa mvua kwenye kilimo na kuongeza maeneo ya umwagiliaji. Kuwe na mikakati ya kuhamasisha na kukuza ufugaji wa samaki. Halikadhalika, tujizatiti kulifufua na kulikuza Shirika letu la Uvuvi la TAFICO na kutumia fursa za uvuvi wa bahari. Suala jingine muhimu liwe ni kukuza na kushamirisha zidi teknolojia ya kilimo (agro-mechanisation) na kuachana kabisa na matumizi ya jembe la mkono.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe wa NEC:
Katika miaka kumi ijayo, sekta ya viwanda iwe ndiyo nguzo kuu ya uchumi na mzalishaji mkuu wa ajira na bidhaa za viwandani (manufactured goods) ili kuchangia zaidi kwenye Pato la Taifa. Mnapokuwa na viwanda tatizo la ajira litapungua, kwa sababu vijana wetu ndio watakaoajiriwa kwenye viwanda hivyo. Jitihada zitaelekezwa kwenye kukuza teknolojia rahisi ya viwanda, hususan viwanda vidogo na vya kati na kuhakikisha kuwa hakuna bidhaa yoyote inayouzwa nje ya nchi bila kuongezewa thamani. Lakini lengo kuu liwe ni kuacha kabisa kuagiza nje bidhaa ambazo malighafi zake zinapakana hapa nchini kama vile nguo, viatu, mafuta ya kula, samani, nk. Ni aibu kwa nchi kama Tanzania imezungukwa na maji kila mahali lakini tunaagiza samaki kutoka nchi, ni aibu kwa nchi kama Tanzania ambayo ni ya pili Afrika kwa kuwa na mifugo mingi lakini bado tunaagiza viatu kutoka kwenye nchi ambazo hazina mifugo mingi, na wakati mwingine tunaagiza maziwa kutoka nje lakini ng’ombe wa Wagogo maziwa yao hatunywi. Sasa tujielekeze katika mwelekeo huo. Vilevile, kuwepo na mkakati mahsusi wa uhawilishaji wa teknolojia (technology transfer) kwa kuzingatia mahitaji mahsusi ya kisekta. Aidha, msukumo mkubwa uelekezwe kwenye ujenzi na uimarishaji wa vyuo vya ufundi na kuvitumia kama njia kuu ya uhawilishaji wa teknolojia, hususan teknolojia ya viwanda.
Katika sekta ya madini, lengo liwe ni kuhakikisha madini yote yanasindikwa na kuongezewa thamani kabla ya kuuzwa nje ya nchi na kuendelea kutoa kipaumbele na vivutio kwa wachimbaji wazawa, ili waweze kumiliki uchumi wa madini. Tusioneane wivu kwamba mzawa hawezi kuwekeza kwenye madini au kwenye nini, Vilevile, tuendelee kudhibiti soko la madini na kuongeza vituo vya mauzo, yaani mineral centres.
Kwenye sekta ya nishati, tujizatiti kuzalisha umeme wa kutosha na wa bei nafuu kwa kutumia vyanzo vyote tulivyonavyo kama vile maji, gesi asilia, upepo, jua, joto-ardhi na makaa ya mawe. Aidha, umeme usambazwe kwenye mitaa na vijiji vyote. Lengo kuu liwe siyo tu kutosheleza kwa ukamilifu mahitaji ya ndani lakini pia kuuza nishati ya ziada nje ya nchi.
Kuhusu sekta ya miundombinu ya usafiri na usafirishaji, tutaendelea kuboresha, kuimarisha, kuboresha na kupanua miundombinu ya barabara, reli, maji na anga. Mtandao wa barabara za lami utaendelea kupanuliwa hadi kwenye wilaya, mitaa na vijiji hili ndio liwe lengo letu katika miaka 10 inayokuja. Tukamilishe ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) pamoja na Matawi yake yote kwenye ushoroba wa kati yaani kwenda Mwanza, Tabora, Kigoma, Isaka na tuunganishe mpaka Kigali (Rwanda); Lakini pia tufufue maeneo mengine, ile ambayo imefika Moshi tutaiendeleza ifike mpaka Arusha na ile ya Mpanda nayo tuiimarishe ili biashara iweze kufanyika kimkakati kwa manufaa ya Watanzania wote. Tuimarishe Reli ya Kati ya zamani na kuongeza ufanisi wa Reli ya TAZARA. Lengo kuu liwe ni kupunguza kwa zaidi ya asilimia hamsini matumizi ya barabara katika usafirishaji wa mizigo kwenye Shoroba zote kuu za Kati, Kusini na Kaskazini. Tutaendelea kuboresha na kuimarisha ufanisi wa Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mtwara, Zanzibar na Pemba ili kuongeza ushindani na Bandari zingine. Tuimarishe bandari kwenye Maziwa yote Makuu pamoja na kuongeza zaidi idadi ya meli ili kuimarisha biashara na nchi jirani. Napenda kuipongeza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kununua meli mpya ambayo inafanya kazi, huu ni mfano mzuri wa kujitegemea wa kweli. Huu ni mfano wa kujitegemea wa kweli, kwa hiyo wakati ujao wanunue meli nyingine ziwe zinazunguka humu baharini zinakwenda Mtwara, zinakwenda Comoro, huu ndio utajiri na huu ndio Utanzania tunaoutaka. Zanzibar hoyee, Shein hoyeeee.
Kwenye usafiri wa anga, msukumo mkubwa uelekezwe kwenye ujenzi na upanuzi wa viwanja vya ndege, kuongeza idadi ya ndege na mtandao wa safari za ndani na nje ya nchi, hususan safari za kimkakati zinazolenga kukuza utalii na biashara.
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana:
Katika sekta ya utalii, tujiwekee mikakati ya kuongeza zaidi mchango wake kwenye Pato la Taifa kwa kuboresha miundombinu kwenye vivutio vyetu na kuvitangaza ndani na nje ya nchi, hususan kupitia Balozi zetu za nje. Na kwa kweli, kipimo kimojawapo cha utendaji kazi wa Balozi zetu za nje iwe ni idadi ya watalii wanaowaleta nchini. Tujiwekee malengo ya watalii milioni kumi (10,000,000) kwa miaka kumi ijayo. Idadi ya Watalii Zanzibar imeongezeka na idadi ya Watalii Tanzania Bara imeongezeka.
Halikadhalika, tunataka sekta ya mawasiliano itoe mchango mkubwa zaidi kwenye Pato la Mataifa. Hivyo, hatuna budi kujizatiti na kuhakikisha Kampuni yetu ya Simu ya TTCL inamiliki angalau asilimia 50. Aidha, tuimarishe usalama wa mawasiliano na kusimamia Sheria ya Makosa ya Kimtandao.
Kwa upande wa masuala ya uhusiano ya kimataifa, tuendelee na sera yetu ya kutofungamna na upande wowote. Tuendelee pia kujenga na kuimarisha uhusiano na mataifa mengine lakini, muhimu zaidi, diplomasia ya uchumi iwe ndiyo msingi wa uhusiano wetu kimataifa. We must determine what we want in relating with other nations. Aidha, tutumie jiograifia yetu ya kimkakati na ushawishi wetu wa kihistoria, hususan kwenye Ukanda wa Kusini, katika kupeleka mbele ajenda yetu ya uchumi na maslahi mapana ya Taifa.
Katika sekta ya ulinzi na usalama, tuendelee kuimarisha ulinzi na usalama wa ndani na mipakani. Aidha, majeshi ya Ulinzi na Usalama yahusishwe kikamilifu katika kulinda Miradi mikubwa ya kimkakati. Aidha, majeshi ya JKT na Magereza yajihusishe zaidi na shughuli za uzalishaji pamoja utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kambi za JKT ziongezwe ili kila mhitimu wa Kidato cha Sita apate fursa ya kupata mafunzo ili kujenga uzalendo na moyo wa kujitolea. Vilevile, kila Gereza liwe na shughuli mahsusi ya uzalishaji, kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, ufundi au viwanda, kulingana na maeneo na fursa zilizopo. Wafungwa wote wafanye kazi ili wakidhi mahitaji yao na kuchangia kwenye uchumi wa Taifa.
Waheshimiwa Viongozi;
Ndugu Wajumbe:
Natambua kuwa majadiliano haya ya leo ni ya siku moja na mtakuwa na masuala mengi ya kujadiliana. Hivyo, nisingependa kutumia muda wenu mwingi kwa kutoa Hotuba ndefu. Lakini, kama nilivyosema hapo awali, NEC ni Chombo kikubwa sana cha maamuzi. Mnapojadiliana na kufikia maazimio kuhusu Mwelekeo wa Sera za CCM kwa miaka kumi ijayo au Ilani ya 2020 – 2025, mnaamua pia kuhusu mustakabali wa Taifa letu. Hivyo, mtangulizeni Mungu na kuliweka mbele Taifa letu, ili tufikie mustakabali mwema. Baada ya kusema haya, sasa nafungua rasmi kikao cha majadiliano ya Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi. Nawatakia majadiliano na maazimio mema. Mwenyezi Mungu awabariki!
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!

- Nov 08, 2019
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO WA MAWAZIRI WA MAMBO YA NJE KUTOKA NCHI Z...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UFUNGUZI WA MKUTANO WA MAWAZIRI WA MAMBO YA NJE KUTOKA NCHI ZA AFRICA NA NORDIC, UKUMBI WA JULIUS NYERERE, DAR ES SALAAM-
TAREHE 08 OKTOBA, 2019
Waheshimiwa Marais Wastaafu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Makamu wa Rais na Mawaziri
Wakuu Wastaafu wa Tanzania mliopo;
Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi,
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Afrika Mashariki na Mwenyeji wa Mkutano
huu;
Waheshimiwa Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka
Nchi za Nordic na Afrika mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa
Mashirika ya Kimataifa mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wote wa Chama na
Serikali;
Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Najisikia furaha kubwa kuweza kushiriki, kwa mara ya kwanza, katika Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi za Afrika na Nordic. Hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano huu tangu kuanzishwa kwa utaratibu wa mikutano kama hii mwaka 2001. Hivyo basi, nitumie fursa hii kuwashukuru Waandaji wa Mkutano huu kwa kunipa heshima ya kuwa Mgeni Rasmi kwenye Hafla ya Ufunguzi wa Mkutano huu.
Aidha, kwa namna ya pekee kabisa, niwashukuru kwa kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano huu muhimu katika kukuza ushirikiano kati ya mataifa ya Nordic na Afrika. Ahsanteni sana.
Natambua kuwa wengi mmesafiri umbali mrefu, na baadhi yenu, hii ni mara ya kwanza kufika Tanzania. Hivyo basi, karibuni sana nchini kwetu, hususan kwenye Jiji letu la Dar es Salaam. Dar es Salaam maana yake ni mahali pa amani na usalama. Kwa sababu hiyo, nina uhakika kuwa Mkutano huu utafanyika kwa amani na salama; na kuleta mafanikio kwa pande zote mbili.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Mkutano huu ni wa siku moja. Kwa hiyo, nitajitahidi kuzungumza kwa kifupi ili nisiwachukulie muda wenu wa majadiliano. Mabibi na Mabwana, kwa ufupi kabisa, uhusiano kati ya nchi za Afrika na Nordic ni wa muda mrefu; na ulianza kabla ya uhuru wa nchi nyingi za Afrika kupatikana. Na kusema kweli, nchi za Nordic zilisaidia sana harakati za ukombozi kwenye nchi mbalimbali, hususan Kusini mwa Afrika.
Kama mnavyofahamu, Tanzania ilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ukombozi ya Afrika. Hivyo, harakati nyingi ziliendeshwa nchini mwetu, ambapo kulikuwa na kambi nyingi za wapigania uhuru. Hivyo, tunafahamu mchango mkubwa uliotolewa na nchi za Nordic, ikiwemo ujenzi wa kilichokuwa Chuo cha Wapigania Uhuru wa Afrika Kusini kilichofahamika kwa jina la Solomon Mahlangu Freedom College (SOMAFCO). Chuo hiki kilijengwa mwaka 1975 Mkoani Morogoro, takriban kilomita miambili kutoka hapa Dar es Salaam. Ikumbukwe kwamba, nyakati hizo, ilikuwa siyo rahisi kwa mataifa ya Ulaya kuja kuunga mkono jitihada za ukombozi Afrika lakini marafiki zetu
wa nchi za Nordic walikuja. Na huu ndio upekee wa nchi za Nordic.
Baada ya kusaidia harakati za kupigania uhuru, nchi za Nordic zimeendelea kuwa washirika wakubwa wa maendeleo ya nchi za Afrika. Tumekuwa tukishirikiana katika nyanja nyingi, ikiwemo afya, elimu, kilimo, sayansi na teknolojia, nishati, mazingira na, bila kusahau, masuala ya amani na usalama. Nchi za Nordic zimesaidia sana kujenga uwezo wa Bara letu kukabiliana na changamoto za migogoro.
Tanzania ni miongoni mwa wanufaika wakubwa wa ushirikiano uliopo na nchi za Nordic. Kabla na baada ya Uhuru, nchi yetu imenufaika na miradi mingi ya maendeleo, ikiwemo Kituo cha Elimu Kibaha (Kibaha Education Centre) na Kituo cha Utafiti wa Kilimo Uyole (Uyole Agricultural Research Centre).
Vilevile, nchi za Nordic zilitusaidia kujenga vyuo vya ufundi na pia kwenye Kampeni ya Kufuta Ujinga, yaani Literacy Campaign Programme, iliyotekelezwa kwenye miaka ya 1970 na kuiwezesha Tanzania kufuta ujinga kwa asilimia 98, na hivyo kuwa miongoni mwa nchi za kwanza kabisa Afrika kufikia kiwango hicho.
Zaidi ya hayo, sisi Watanzania tunakumbuka misaada tuliyopewa na nchi za Nordic kwenye miaka ya 1980, wakati baadhi ya mataifa makubwa na taasisi za kifedha za kimataifa zilipositisha misaada kwa nchi yetu.
Kwa kuzingatia hayo yote, napenda nitumie fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa ndugu na marafiki zetu wa nchi za Nordic kwa kuendelea kushirikiana na nchi yetu na nchi nyingine za Afrika kwa ujumla. Na tunawaomba Waheshimiwa Mawaziri kutoka nchi za Nordic mfikishe salamu na shukrani zetu kwa Wakuu wenu wa Nchi na Serikali.
Waheshimiwa Mawaziri;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Pamoja na uhusiano mzuri na mafanikio makubwa yaliyopatikana kwenye ushirikiano kati ya nchi za Afrika na Nordic, bado tuna fursa ya kuukuza uhusiano wetu na kuupa msukumo mpya ili kuleta manufaa makubwa zaidi kwa pande zetu mbili. Na suala hili ni muhimu kwa sababu, kwa muda mrefu, ushirikiano wetu umejikita zaidi kwenye kutoa na kupokea misaada, yaani donor-recipent relationship. Ushirikiano wa aina hii siyo endelevu na wala hauhitajiki katika mazingira ya sasa. Viongozi wengi wa Afrika tumetambua kuwa mustakabali wa Bara letu uko mikononi mwetu na kwamba uhuru wa kisiasa hauwezi kuwa na maana sana, endapo mataifa yetu yataendelea kuwa tegemezi kiuchumi. Hatuwezi kuwa na uhuru wa kujiamlia mambo yetu wenyewe endapo mataifa yetu yataendelea kuwa ombaomba.
Kutafuta ukombozi wa kiuchumi ndilo jukumu tuliloachiwa sisi viongozi wa sasa wa Africa. Hata Hayati Mwalimu Julius Nyerere alisema, katika moja ya hotuba zake kwamba “The first generation of leaders led Africa to political freedom. But we, the current generation of leaders, must pick up the flickering torch and lead Africa towards economic liberation”.
Hivyo basi, ni lazima tubadilishe mwelekeo na kuingia kwenye uhusiano wa kisasa baina ya mataifa ambao unajikita kwenye ushirikiano wa kiuchumi (economic partnership) kupitia biashara na uwekezaji. Diplomasia ya uchumi ndiyo iwe msingi wa uhusiano na ushirikiano baina ya mataifa yetu.
Kwa bahati nzuri, uwezo, fursa na mazingira ya kuingia kwenye ushirikiano madhubuti wa kiuchumi yapo. Kwa mfano, nchi za Nordic, ambazo zipo tano: Denmark, Finland, Iceland, Norway na Sweeden; licha ya kuwa na eneo dogo (kilomita za mraba milioni 3.5) na idadi ya watu wapatao milioni 27 tu; zina uchumi mkubwa. Pato lao kwa mwaka jana (2018) lilikuwa na thamani ya Dola za Marekani trilioni 1.7.
Kwa upande wetu Afrika, kama inavyofahamika, Bara letu ni kubwa (lina kilomita za mraba milioni 30.37) na idadi ya watu wapatao bilioni 1.2. Hata hivyo, kwa mwaka jana 2018, Pato la nchi zote za Afrika lilikuwa na thamani ya Dola za Marekani trilioni 2.334 tu.
Kusema kweli, sisi Waafrika tuna jambo kubwa la kujifunza. Kwa sababu, wakati nchi za Nordic zenye jumla ya watu milioni 27 tu, Pato lao kwa mwaka ni Dola za Marekani trilioni 1.7; sisi Tanzania ambao tuko milioni 55, mara mbili zaidi ya nchi za Nordic, Pato letu la Taifa kwa mwaka jana lilikuwa na thamani ya Dola za Marekani bilioni 56.99 tu.
Lakini hata ukilinganisha Pato la mtu mmoja mmoja katika nchi za Nordic na Afrika, tofauti ipo kubwa sana. Kwa mfano, ukigawa Pato la nchi za Nordic la Dola za Marekani trilioni 1.7 kwa watu milioni 27, maana yake pato la mtu mmoja ni wastani wa Dola za Marekani 62,963. Lakini kwenye nchi za Afrika ni wastani wa Dola za Marekani 1,945 tu. Tofauti hii ni kubwa sana; hivyo basi, sisi Waafrika ni lazima tujitafakari ili tujue tunapokosea na tujifunze kutoka kwa marafiki zetu wa nchi za Nordic.
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana
Bara letu la Afrika limebarikiwa kuwa na utajiri mwingi wa rasilimali na maliasili. Mathalan, Bara letu lina eneo kubwa lenye kufaa kwa kilimo. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, asilimia 30 ya ardhi yenye kufaa kwa kilimo duniani ipo Barani Afrika. Aidha, Afrika ina utajiri wa rasilimali za bahari kwenye ukanda wa pwani wenye urefu wa kilomita 30,500. Rasilimali zingine ni pamoja na mifugo, wanyamapori, misitu, madini, mafuta, gesi, vivutio vya utalii, nk.
Muhimu zaidi, ni kwamba, katika miaka ya karibuni, Afrika imefanya mageuzi makubwa kwenye nyanja za ulinzi na usalama. Licha ya kuendelea kwa baadhi ya migogoro, hali ya amani na usalama imeimarika. Uchumi pia unakua vizuri, ambapo Afrika inashika nafasi ya pili kwa kasi ya ukuaji wa uchumi duniani. Mathalan, mwaka 2018, uchumi wa Afrika ulikua kwa wastani wa asilimia 4.1. Na kati ya nchi 10 zenye uchumi unaokuwa kwa kasi zaidi duniani, tano zinatoka Afrika. Haya yote yanatoa fursa kwa pande zetu mbili kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi.
Waheshimiwa Viongozi;
Mabibi na Mabwana:
Nimetaja baadhi ya fursa za ushirikiano wa kiuchumi katika Afrika. Lakini hata hapa nchini, tumejaliwa rasilimali na maliasili lukuki na fursa za uwekezaji zipo kwenye sekta zote. Mathalan, tunayo madini karibu yote yanayopatikana duniani: dhahabu, almasi, rubi, sapphire, chuma, soda ash, shaba, nikeli, cobalt, tin, urania, helium, nk. Siwezi kuyataja yote hapa na mengine, kama vile tanzanite, yanapatikana hapa Tanzania pekee. Kwenye uvuvi, Tanzania ina ukanda wa pwani wenye urefu wa kilomita 1,424. Vilevile, tunayo mito na maziwa makubwa ambayo yanafaa kwa uvuvi. Utalii ni sekta nyingine yenye fursa nyingi za uwekezaji, kwani nchi yetu inashika nafasi ya pili duniani kwa uwingi wa vivutio vya utalii. Tuna mbuga ya wanyama, Mlima Kilimanjaro, fukwe nzuri, nk. Halikadhalika, zipo fursa nyingi sana kwenye sekta ya kilimo, mifugo, viwanda, nk.
Ni wazi kwamba pamoja na utajiri mkubwa wa rasilimali na maliasili, changamoto kubwa inayolikabili Bara la Afrika ni ukosefu wa viwanda. Afrika haitaweza kupiga hatua endapo itaendelea kuwa muuzaji wa bidhaa ghafi na muagizaji wa bidhaa za viwandani. Kwa sasa, asilimia 60 ya mauzo ya nje kutoka nchi za Afrika ni mazao ghafi. Ni lazima Waafrika tufike hatua ambapo tutaweza kusindika na kuongeza thamani ya mazao yetu, ikiwemo mazao ya kilimo, madini, uvuvi, nk.
Hivyo basi, kwa kuwa marafiki zetu wa nchi za Nordic wamepiga hatua kiteknolojia, hususan teknolojia ya viwanda, tushirikiane kujenga viwanda vya kusindika na kuongeza thamani ya mazao yetu kwa manufaa ya pande zetu mbili. Tunataka tusindike pamba na kutengeneza nguo hapa Afrika; tunataka tuchimbe madini na kuyachenjua hapa hapa Afrika; tunataka tuvue samaki na kuwasindika hapa hapa Afrika. Africa must produce, process, consume and export finished products. Viwanda ni moja ya vipaumbele vyetu vikubwa, na washirika wetu wa maendeleo pamoja na wawekezaji wengine makini watuunge mkono kwenye mwelekeo huo.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa:
Ili kuvutia biashara na uwekezaji katika sekta mbalimbali, ni muhimu kwa nchi za Afrika kuweka mazingira muafaka, ikiwemo miundombinu wezeshi pamoja na kuondoa urasimu kwenye sheria na taratibu zetu za biashara na uwekezaji. Na hapa, naomba mnimruhusu nitaje baadhi ya jitihada ambazo tumefanya na tunaendelea kufanya hapa nchini ili kuvutia wawekezaji katika maeneo mbalimbali niliyoyataja hapo awali.
Moja ya jitihada tulizofanya ni kupitia na kurekebisha sheria na taratibu mbalimbali za uwekezaji nchini, ikiwa ni pamoja na kutengeneza sheria za kuwalinda wawekezaji. Vilevile, tumeanzisha Wizara mahsusi yenye dhamana ya Uwekezaji chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ili ijihusishe moja kwa moja na kurahisisha mazingira na uratibu wa uwekezaji nchini. Lakini muhimu zaidi, tunatekeleza Mkakati wa Kurekebisha na Kuboresha Mazingira ya Biashara nchini, yaani The Blueprint for Regulatory Reforms to Improve Business Environment. Jitihada zingine ni kutenga kanda maalum kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na kanda maalumu za uwekezaji, yaani Export Processing Zones and Special Economic Zones.
Sambamba na hayo, kwa kutambua umuhimu wa miundombinu wezeshi kama kichocheo cha biashara na uwekezaji, hivi sasa, tunajenga na kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji, ikiwemo barabara, reli, usafiri wa majini na anga. Mathalan, hivi sasa tunajenga Reli ya Kisasa, yaani Standard Gauge Railway kwenye Ushoroba wa Kati yenye urefu wa kilomita 1,800 kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza, ambayo baadaye itatuunganisha na nchi jirani za Rwanda na Burundi. Vile vile, tumelifufua Shirika letu la Ndege la ATCL na kuboresha viwanja vyetu vya ndege na kusimika rada za kuongozea ndege. Tunapanua na kuboresha bandari zetu za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga pamoja zilizopo kwenye Maziwa yetu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.
Na upanuzi huu unaenda sambamba na ujenzi wa meli na vivuko. Zaidi ya hapo, tutakeleza Mradi mkubwa wa uzalishaji wa umeme wa maji kwenye Bonde la Rufiji utakaozalisha Megawati 2,115, na kuchangia kwa kiasi kikubwa kupunguza gharama za uzalishaji wa bidhaa viwandani na kwenye sekta nyingine.
Kwa kuzingatia hayo yote, nitumie fursa hii adhimu kuwakaribisha ndugu na marafiki zetu wa nchi za Nordic, pamoja na mataifa mengine, yakiwemo ya Afrika, kuja kuwekeza nchini mwetu. Mazingira ya uwekezaji ni muafaka na yanatabirika, kutokana na amani na utulivu wetu kisiasa, lakini pia mwenendo wa ukuaji wa uchumi ni mzuri ambapo, kwa sasa, ni wastani wa asilimia 7. Zaidi ya hapo, sisi ni wanachama wa SADC na EAC, ambazo kwa pamoja zina idadi ya watu wapatao milioni 450.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Kwa kuhitimisha, nisisitize kwamba nchi za Afrika na Nordic zinahitajiana, kutokana na ukweli kwamba zipo fursa ambazo Afrika tunazo lakini wenzetu wa Nordic hawana na vivyo hivyo kwa Afrika. Hivyo basi, Mkutano wenu hauna budi kuja na mikakati mahsusi ya ushirikiano wenye manufaa kwa pande zote. Our cooperation must be founded on a win-win principle. Nawatakia maazimio mema.
Asanteni kwa kunisikiliza!

- Aug 18, 2019
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEFU MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUFUNGA MKUTANO WA 39 WA WAKUU WA NCHI WA SADC DAR ES S...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEFU MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO
WA TANZANIA WAKATI WA KUFUNGA MKUTANO
WA 39 WA WAKUU WA NCHI WA SADC
DAR ES SALAAM, TAREHE 18 AGOSTI, 2019
Mheshimiwa Emmerson Mnangagwa, Mwenyekiti
wa Taasisi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC;
Waheshimiwa Wakuu wa Nchi wa SADC mliopo;
Waheshimiwa Wake wa Viongozi mliopo;
Waheshimiwa Viongozi mnaowakilisha Nchi Wanachama;
Mheshimiwa Mzee Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu
wa Awamu wa Pili wa Tanzania;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar n
a Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu wa Tanzania
(Mzee John Malecela na Peter Pinda);
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Othmani Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri mliopo;
Waheshimiwa Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Dkt. Stergomena Tax, Katibu Mtendaji
wa Sekretarieti ya SADC;
Waheshimiwa Wakuu wa Taasisi za Kikanda
na Kimataifa mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama mliopo;
Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Maafisa Waadamizi na Wajumbe wengine wa Mkutano;
Wageni Waalikwa Wote, Mabibi na Mabwana;
Naomba nianze kwa kutoa taarifa. Jana, baada ya kusoma sehemu ya Hotuba yangu ya Ukaribisho kwa Lugha ya Kiswahili; Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC walifurahi na kuvutiwa sana. Hivyo basi, tulipoenda tu kwenye Mkutano wetu wa Ndani, wote kwa pamoja na kwa kauli moja, walifanya uamuzi wa kukifanya Kiswahili kuwa Lugha Rasmi ya Nne ya SADC. Hii ndiyo sababu nimeamua kuhutubia kwa Kiswahili.
Napenda kutumia fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wakuu wa Nchi Wenzangu kwa uamuzi huu mkubwa na wa kihistoria, ambao pia unaendana na kumuenzi Baba wa Taifa letu, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kama mnavyofahamu, wakati wa uongozi wa Mwalimu Nyerere, Tanzania ilifanya kazi kubwa ya kusaidia harakati za ukombozi, hususan wa nchi za Kusini mwa Afrika. Nchi yetu ilitenga maeneo mengi kwa ajili ya kuanzisha Kambi za Wapigania Uhuru kutoka ANC, FRELIMO, MPLA SWAPO, ZANU-PF, (Nachingwea, Mgagawa, Kongwa, Kaole, Dakawa na Mazimbu), nimefurahi hivi majuzi tu Mheshimiwa Rais Ramaphosa alienda kutembelea Mazimbu hivi karibuni. Lakini hata Mheshimiwa Rais Mnangagwa wa Zimbabwe alipokuja alikwenda Bagamoyo (Kaole) ambako alipata mafunzo ya kupigania uhuru.
Tanzania pia, wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, ilisaidia kuzuia jaribio la mapinduzi nchini Shelisheli lililopangwa kufanywa na Utawala wa Makaburu wa Afrika Kusini. Baada ya kuzimwa kwa jaribio hilo, Mtanzania, Marehemu Brigredia Jenerali Hassan Ngwilizi, aliongoza nchi hiyo kwa muda. Hii ni mifano michache tu ya mchango uliootolewa na Tanzania chini ya uongozi wa Baba wa Taifa. Na katika harakati zote hizo, lugha ambayo ilitumika sana ni Kiswahili. Hivyo basi, uamuzi wa kukifanya Kiswahili kuwa Lugha Rasmi ya SADC ni sahihi na muafaka katika kuenzi kazi zilizofanywa na Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere.
Narudia tena kuwashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wakuu wa Nchi na Serikali kwa uamuzi huu mkubwa na wa kihistoria. Kwa hakika, mmeingia kwenye vitabu vya historia. Vizazi na vizazi vitawakumbuka. Kama mnavyofahamu, lugha ni chombo muhimu katika kuimarisha mahusiano baina ya watu lakini pia katika kukuza na kuimarisha ushirikiano na utengamano kati na baina ya mataifa. Mwanasosholojia na Mtaalam wa Lugha Dkt. Joshua Fishman aliwahi kusema, napenda nimnukuu “…a common indigenous language in the modern nation states is a powerful factor of unity…it promotes a feeling of single community. Additionally, it makes possible the expansion of ideas, economic targets and cultural identity”, mwisho wa kunukuu.
Kiswahili ni lugha ya Kiafrika; na sisi ni Waafrika. Hivyo basi, nina imani kuwa uamuzi huu wa kukifanya Kiswahili kuwa Lugha Rasmi ya SADC utasaidia kuimarisha uhusiano miongoni mwa wananchi wetu na pia kukuza na kuimarisha ushirikiano na utengamano kati ya mataifa yetu. Na napenda nitumie fursa hii, kuzisihi Nchi Wanachama ambazo Kiswahili hakitumiki, kuiga mfano wa Afrika Kusini, ambayo kuanzia mwakani, wataanza kufundisha Kiswahili kwenye shule zao. Sisi Tanzania tutakuwa tayari kuwaunga mkono, ikiwemo kwa kutoa walimu na nyenzo mbalimbali za kufundishia.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kwa ajili ya kuhitimisha Mkutano wetu. Kwa takribani siku mbili, tumekutana kujadili masuala mbalimbali yenye lengo la kuiletea maendeleo Jumuiya yetu. Napenda nitumie fursa hii kutamka kuwa, Mkutano wetu umekuwa wa mafanikio makubwa sana. Nasema hivyo, kwa sababu, kwanza, umefanyika kwenye mazingira ya utulivu, upendo, na maeleweno makubwa. Ni kweli, mara chache chache, kulikuwa na kutofautiana kwenye baadhi ya hoja, lakini tulijadiliana kwa urafiki mkubwa na hatimaye kuweza kufikia makubaliano.
Pili, Mkutano wetu ulikuwa wa mafanikio kwa sababu ya ajenda zenyewe tulizozijadili na maazimio tuliyoyafikia. Tumejadili ajenda nyingi na kufikia maamuzi makubwa, ambayo binafsi naamini, endapo yatatekelezwa, yataleta manufaa mengi kwenye Nchi Wanachama pamoja na Jumuiya yetu kwa ujumla.
Naomba, kwa haraka haraka, mniruhusu nitoe muhtasari wa baadhi ya masuala tuliyoyajadili na kuyafanyia maamuzi.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kama mnavyofahamu, Mkutano wetu umefanyika chini ya kaulimbiu isemayo “Mazingira Wezeshi ya Biashara kwa ajili ya Kuwezesha Maendeleo Jumuishi na Endelevu ya Viwanda, Kukuza Biashara na Kuongeza Fursa za Ajira (A Conducive Environment for Inclusive and Sustainable Industrial Development, Increased Intra-Regional Trade and Job Creation)”. Kaulimbiu hii ni mwendelezo wa kaulimbiu za Mikutano ya Wakuu wa Nchi iliyofanyika Zimbabwe mwaka 2014; Botswana mwaka 2015, Eswatini mwaka 2016, Afrika Kusini mwaka 2017 na Namibia mwaka 2018; ambapo zote ziliweka mkazo kwenye utekelezaji wa Mkakati na Mpango Mwongozo wa Maendeleo ya Viwanda wa SADC wa Mwaka 2015 – 2063 (the SADC Industrialization Strategy and Roadmap 2015 – 2063).
Kaulimbiu ya mwaka huu imeweka msisitizo katika kuboresha mazingira ya biashara, ikiwemo kuondoa vikwazo vya mipakani, ukiritimba kwenye maamuzi, rushwa, n.k.; ili kukuza sekta ya viwanda na kustawisha biashara kwenye Ukanda wetu. Ninayo furaha kuarifu kuwa Wakuu wa Nchi wamepitisha kaulimbi hiyo na kuilekeza Sekretarieti kusimamia utekelezaji wake na kisha kuwasilisha Ripoti kwenye Mkutano ujao wa SADC. Sambamba na hilo, kwa lengo la kukuza sekta ya viwanda kwenye Jumuiya yetu, Mkutano umezihimiza Nchi Wanachama kuendelea kutekeleza Mkakati na Mwongozo wa Maendeleo ya Viwanda wa SADC 2015 – 2063. Na kama mlivyoshuhudia, hivi punde, nchi zetu zimesaini Itifaki kuhusu Viwanda.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Wakati wa Mkutano wetu pia tumepokea Ripoti za Mwaka za Mwenyekiti wa SADC anayemaliza muda wake na Ripoti ya Mwaka ya Mwenyekiti anayemaliza muda wake wa Taasisi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC (SADC Organ). Wakuu wa Nchi wamewapongeza Wenyeviti hao, Mheshimiwa Rais Geingob na Mheshimiwa Rais Lungu, kwa kazi nzuri walizofanya katika wenye mwaka uliopita.
Wakuu wa Nchi pia wamekubaliana kuendelea kufuatilia suala la usalama nchini DRC; lakini pia wameitaka Falme ya Lesotho kuharakisha utungwaji wa sheria itakayoanzisha Mamlaka ya Kitaifa ya kusimamia Mabadiliko (National Reform Authority). Zaidi ya hapo, Wakuu wa Nchi wameiagiza Sekretarieti kuharakisha Uanzishaji wa Chombo cha SADC cha Kukabiliana na Majanga (SADC Disaster Preparedness and Response Mechanism) kitakachozisaidia Nchi Wanachama kukabiliana na majanga, kama vile mafuriko, ukame, njaa, vimbunga, magonjwa ya mlipuko, n.k.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Sambamba na hayo, Wakuu wa Nchi walipitia hali ya uchumi kwenye Ukanda wetu. Na kama ambavyo nilieleza jana, kwa sababu ya majanga mbalimbali yaliyozikumba baadhi ya Nchi Wanachama pamoja na matatizo mbalimbali ya kiuchumi duniani, Uchumi wa Ukanda wetu ulishindwa kukua kama ilivyotarajia, kwa asilimia 7.0; badala yake ulikua kwa asilimia 3.1.
Hivyo basi, Nchi Wanachama zimetakiwa kuendelea kuwekeza kwenye miundombinu na kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji na biashara; kwa kuwa ni mojawapo ya vikwazo kikubwa vya ukuaji uchumi kwenye Barani Afrika, ikiwemo kwenye Ukanda wa SADC. Zaidi ya hapo, tumekubaliana kuendelea kuboresha sera zetu za uchumi na fedha ili kuboresha mazingira ya ukuaji uchumi kwenye Ukanda wetu.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Masuala mengine tuliyojadili ni pamoja na suala la upatikaaji mapato (resources mobilization), ombi la Burundi kujiunga na SADC pamoja na suala la vikwazo kwa Zimbabwe. Kuhusiana na suala la mapato, Mkutano umezipongeza nchi zilizokamilisha kutoa michango au ada zao za mwaka, na kuzihimiza zile ambazo bado, kufanya hivyo. Aidha, Mkutano umepitisha Mpango wa Kuongeza Mapato wa SADC (SADC Regional Resource Mobilization Framework), ambapo Nchi Wanachama zitakuwa na hiari ya kuchagua yenyewe njia bora ya kuchangia.
Nitumie fursa hii, kwa niaba ya Jumuiya, kuwashukuru washirika na wadau wetu wa maendeleo kwa kutuunga mkono kifedha na katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. Kwenye Bajeti ya Mwaka 2019/2020 ambayo inafikia takriban Dola za Marekani milioni 74, washirika wetu wameahidi kuchangia takriban Dola za Marekani milioni 31, na kiasi kingine cha Dola za Marekani milioni 43 kitachangiwa na Nchi Wanachama.
Najua kwenye hadhira kama hii sio vizuri sana kutaja majina katika kutoa shukrani; maana upo uwezekano wa kuwasahau wengine. Hata hivyo, naomba mniruhusu nitaje baadhi ya washirika wetu ambao wamekuwa wakituunga mkono: Umoja wa Ulaya; Benki ya Dunia, Ujerumani, China, Sweden. Lakini, kwa namna ya pekee, napenda kuishukuru Benki ya Maendeleo ya Afrika pamoja na Global Fund kwa kwa michango wanayotoa kwa nchi zetu na Jumuiya yetu; hususan katika kujenga miundombinu, kwa upande wa Benki ya Maendeleo ya Afrika; na kukabiliana na magonjwa ya UKIMWI, Malaria na Kifua Kikuu kwa upande wa Global Fund.
Nitoe wito kwa Sekretarieti kuendelea kujitahidi kutumia vizuri fedha zinazotolewa na Nchi Wanachama pamoja na Washirika wetu wa Maendeleo. Fedha hizo zitumike kwa malengo yalikusudiwa, na hasa katika kutekeleza miradi ya maendeleo; badala ya kutumika kwenye semina, warsha au mikutano. Kama mnavyofahamu, michango inayotolewa na Nchi Wanachama inatoka kwa wananchi masikini. Hivyo basi, ni lazima matumizi ya fedha yalete manufaa kwa wananchi hao masikini. Mathalan, binafsi, nitafurahi sana kama nitaona fedha nyingi tunazochangia zinaelekezwa katika kutekeleza miradi ya maendeleo kama vile ujenzi wa shule, vituo vya afya, au kufanya usanifu wa miradi ya miundombinu, ambayo italeta matokeo chanya hapo baadaye.
Nimeleza hivi punde kuwa kwenye Bajeti ya 2019/2020, Nchi Wanachama zitachangia Dola za Marekani milioni 43. Kama tutaamua angalau Dola za Marekani milioni 3 zitumike kwenye kutekeleza miradi ya maendeleo kama kujenga vituo vya afya, itakuwa na tija kubwa kwa wananchi. Hapa Tanzania, kwa mfano, gharama za kujenga kituo kimoja cha afya ni takriban Dola za Marekani laki mbili; hivyo katika Dola za Marekani milioni 3, unaweza kujenga vituo visivyopungua 15; na hivyo kuleta manufaa makubwa kwa wananchi wetu.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Kuhusiana na ombi la Burundi, Mkutano umepokea taarifa kuhusu hatua iliyofikiwa ya nchi hiyo kuweza kujiunga. Hata hivyo, ilibainika kuwa, bado kuna maeneo ambayo hajakamilika vizuri. Hivyo basi, Mkutano umeiilekeza Sekretarieti kuiarifu Burundi kuhusu maeneo ambayo bado hajakamilika ili yafanyiwe kazi na hatimaye kuwezesha kutumwa tena kwa Timu ya Uchunguzi (verification mission). Kuhusu Zimbabwe, tumekubaliana kuwa tuendelee kujadiliana na kufanya mawasiliano na jumuiya ya kimataifa ili kuwezesha kuondolewa kwa vikwazo kwenye nchi hiyo, ikiwemo kupitia Mabalozi wetu waliopo sehemu mbalimbali duniani. Kwa ujumla, niseme tu kwamba, Viongozi wote wa SADC tumekubaliana na kutamka kwa kauli moja kwamba, tupo pamoja na Zimbabwe na kamwe hatutaiacha nchi hiyo.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Mwanzoni mwa hotuba yangu nilieleza kuwa Mkutano wetu umekuwa wa mafanikio makubwa. Lakini nikiri kuwa, mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa kutoka kwa Nchi Wanachama wenyewe, Sekretarieti pamoja na wadau wengine mbalimbali. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kurudia tena kuwashukuru Waheshimiwa Wakuu wa Nchi kwanza kwa kuhudhuria Mkutano huu kwa wingi sana; lakini pili kwa michango yenu mizuri wakati wa majadiliano.
Napenda pia niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri pamoja na Maafisa wetu Waandamizi kwa kazi kubwa mliyoifanya ya kuandaa Mkutano wa Wakuu wa Nchi. Mmeturahisishia sana kazi yetu. Kwa namna ya pekee, nawashukuru Watendaji wa Sekretarieti, wakiongozwa na Katibu wake Mtendaji mahiri, Dkt. Tax, kwa kufanya kazi kwa bidii, na bila kuchoka, wakati wa maandalizi, wakati wa Mkutano na mpaka muda huu tunapohitimisha. Hongereni na ahasanteni sana.
Nawashukuru pia wote waliofanya kazi nyuma ya pazia na kuwezesha kufanikisha Mkutano wetu. Navishukuru vyombo vya ulinzi na usalama, hususan kwa kuhakikisha usalama wa nchi na wageni wetu; nawashukuru wakalimani, vyombo vya habari, madereva, wahudumu, vikundi vya burudani na kadhalika.
Nawashukuru pia wageni wetu kutoka nchi mbalimbali. Tunawasihi sana, kama mnayo nafasi, msiondoke bila ya kutembelea vivutio tulivyo navyo. Kama mjuavyo, Tanzania ina vivutio vingi, ikiwemo visiwa vizuri vya marashi ya karafuu vya Zanzibar, Mlima Kilimanjaro, Mbuga za Serengeti na Ngorongoro. Hapa Tanzania pia ndio mahali penye mti mrefu zaidi Barani Afrika na pia Ziwa kubwa zaidi Barani Afrika, Ziwa Victoria.
Lakini pia, kwa wawekezaji, msiondoke bila kupata fursa ya kuwekeza. Tanzania ni mahali penye fursa nyingi za uwekezaji. Kwenye sekta za viwanda, kilimo, uvuvi, ufugaji, madini, gesi, nishati, utalii, n.k. Hivyo basi, nawasihi mchangamkie fursa hizo.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kabla ya kuhitimisha hotuba yangu, napenda kurudia tena kuwashukuru Waheshimiwa Wakuu wa Nchi kwa kuniamini na kunikabidhi jukumu la kuwa Mwenyekiti wenu. Nimelipokea jukumu hilo kwa uenyenyekevu mkubwa. Narudia tena kumpongeza Mwenyekiti anayemaliza muda wake, Mheshimiwa Rais Dkt. Geingob wa Namibia kwa kazi nzuri aliyoifanya katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita. Naahidi kuendeleza mambo yote mazuri aliyoyaanzisha.
Napenda pia kumpongeza kaka yangu, Mheshimiwa Emmerson Mnangagwa, Rais wa Zimbabwe, kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Taasisi yetu muhimu ya kusimamia masuala ya Siasa, Ulinzi na Usalama (SADC Organ). Naahidi kushirikiana naye kwa karibu ili kuhakikisha amani, utulivu na usalama unatawala kwenye Jumuiya yetu.
Natambua kuwa katika kipindi chetu cha Uenyekiti, takriban nchi nne zinatarajiwa kufanya uchaguzi (Botswana, Msumbiji, Namibia na Mauritius). Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuzitakia nchi hizo uchaguzi mwema. Nina matumaini makubwa kuwa chaguzi hizo zitafanyika kwenye mazingira ya amani na utulivu mkubwa na kwa kuzingatia vigezo vya Jumuiya yetu.
Waheshimiwa Wakuu wa Nchi;
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Jana wakati wa kuwakaribisha nilieleza kuwa mwaka huu nchi yetu inaadhimisha miaka 20 tangu kufariki kwa Baba wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kwa kuzingatia hilo, nawajibika kuhitimisha hotuba yangu, kwa kunukuu baadhi ya maneno yake ambayo aliyatoa mwaka 1997 wakati akihutubia Bunge la Afrika Kusini, alisema “Kila nchi inapaswa kutegemea raia wake na rasilimali ilizonazo katika kujiletea maendeleo. Hata hivyo, hiyo peke yake haitoshi. Ni lazima pia kushirikiana na nchi nyingine. Nchi zinaposhirikiana zinaongeza uwezo wa kujiletea maendeleo”, mwisho wa kunukuu. Kwa kutumia maneno hayo ya Baba wa Taifa letu, napenda kurudia tena kuwaomba Waheshimiwa Viongozi tushirikiane ili kuleta maendeleo kwenye nchi zetu na Jumuiya yetu kwa ujumla. Umoja wetu ndiyo nguvu yetu. Na katika hilo, nawaahidi kuwa, Tanzania ikiwa Mwenyekiti wa Jumuiya itashirikiana na Nchi zote Wanachama ili kufanikisha utekelezaji wa malengo na kuiletea maendeleo Jumuiya yetu.
Baada ya kusema, natamka kuwa Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi za SADC umefungwa rasmi. Nawatakieni wageni wetu wote safari njema wakati wa kurejea nyumbani.
Mungu Ibariki SADC!
Mungu Ibariki Afrika!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”.

- Aug 17, 2019
ACCEPTANCE SPEECH BY H.E. DR. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, PRESIDENT OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA ON THE OCCASSION OF ASSUMING THE CHAIMANSHIP OF THE SADC...
Soma zaidiHotuba
ACCEPTANCE SPEECH BY H.E. DR. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, PRESIDENT OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA ON THE OCCASSION OF ASSUMING THE CHAIMANSHIP OF THE SADC
DAR ES SALAAM, 17 AUGUST, 2019
Your Excellency Dr. Hage Geingob, President of the Republic of Namibia and Outgoing Chairperson of the SADC;
Your Excellency Edgar Chagwa Lungu, President of the Republic of Zambia and Outgoing Chairperson of the SADC Organ on Politics, Defense and Security Cooperation;
Your Excellencies Heads of State and Government
Your Excellencies, First Ladies;
Your Excellencies former Presidents of the United Republic of Tanzania (Ali Hassan Mwinyi, Benjamin William Mkapa and Jakaya Mrisho Kikwete);
Your Excellency Samia Suluhu Hassan, Vice President of the United Republic of Tanzania;
Your Excellency Dr. Ali Mohamed Shein, President of Zanzibar and Chairman of the Revolutionary Council;
Your Excellency Kassim Majaliwa, Prime Minister of the United Republic of Tanzania;
Your Excellencies Former Prime Ministers of the United Republic of Tanzania (Mzee Cleopa Msuya, Mzee Joseph Warioba, Mzee John Malecela, and Mzee Peter Pinda)
Your Excellency Netumbo Nandi – Ndaitwah, Deputy Prime Minister of the Republic of Namibia;
Leaders of Political Parties here present;
Your Excellency Chairman of the SADC Council of Ministers;
Honourable Ministers here present;
Your Excellency Dr. Stergomena Lawrance Tax, Executive Secretary of the SADC;
Your Excellencies Heads of Other Regional and International Organizations;
Excellencies High Commissioners and Ambassadors here present;
Distinguished Delegates and Other Invited Guests;
Ladies and Gentlemen;
I feel greatly honoured and yet privileged to be given this rare opportunity to address this Assembly for the second time this morning. Unlike the first time, this time around, I stand before Your Excellencies when you have given me a huge responsibility to chair this Organization for the next one year. Allow me, therefore, on behalf of the Government and People of the United Republic of Tanzania, as well as that of my own, to thank Your Excellencies Heads of State and Government of the SADC for the trust you have bestowed on me. Indeed, being a Chair of this body is a great honour not only to me personally but also to the Government and people of Tanzania. I thank you very much.
I know, this is not an easy job; it comes with high expectations, however, with great sense of humility, I humbly accept this responsibility. And I have all the confidence that, with Your Excellencies’ support and cooperation, I will be able to live to your expectations and to the expectations of the people of this sub-region. And to be honest, I have no reason not to believe that you will offer me all the needed support during my tenure.
You have been doing so since my inauguration as President of the United Republic of Tanzania in November 2015. In this connection, this being the first SADC Summit to attend, I would like to take the advantage of this occasion to thank Your Excellencies Heads of State and Government of the SADC for all the support and cooperation you have been extending to me since I took over the leadership of my dear country, Tanzania. I greatly appreciate your support and cooperation; and it is my desire to strengthen further these cooperation and partnerships for the benefits of our Community and all our Member States.
May I also seize this opportunity to reassure Your Excellencies, and whoever had any cause of doubt, that, Tanzania is fully committed to the SADC; its vision, goals, principles and ideals. Indeed, we always consider SADC as an integral part of our future. This is why we have continued to be an active member of SADC and effectively participate in the implementation of its various initiatives and programmes.
In short, I want to assure Your Excellencies that, during my tenure as the President of this country, the Tanzania that you very well know will remain the same. Indeed, I promise to follow the footsteps of all my predecessors, the late Father of the Nation, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere and Their Excellencies Ali Hassan Mwinyi, Benjamin William Mkapa and Jakaya Mrisho Kikwete. I know it is not an easy task, but I will try to the best of my ability; and so God help me.
Your Excellencies, Ladies and Gentlemen;
Before I proceed with my address, I would like to seize this opportunity to acknowledge the exemplary leadership of our Community by the Outgoing Chair of SADC, His Excellency President Dr. Hage Geingob, during the past one year. Indeed, as his Deputy, I must admit that, I benefited from his huge experiences, which I believe will help me for the new role I have just assumed. I particularly wish to commend Outgoing Chairperson for his dedication and commitment on the issues of infrastructure development and youth empowerment; as well as for ensuring that SADC actively participated and played its role in the efforts towards reducing the effects of cyclone Idai and Kenneth that had affected some SADC Member States. In this connection, allow me, once again, to extend my condolences and sympathy to all Member States that were affected by these unfortunate and tragic events.
I wish also to pay a glowing tribute to my brother, His Excellency President Edgar Chagwa Lungu of Zambia and the Outgoing Chairperson of the SADC Organ on Politics, Defense and Security Cooperation for his tireless efforts to promote peace, stability and democracy in our region. During his tenure, six Member States held their elections peacefully: Comoro, DRC, Eswatini, Madagascar, Malawi and South Africa. In this regard, I am sure you will all join me in congratulating Their Excellencies Andry Rajoelina of the Republic of Madagascar, Azali Assoumani of the Union of Comoros, Cyril Ramaphosa of the Republic of South Africa and Peter Mutharika of the Republic of Malawi for the victories in their respective countries. I wish also to commend the Kingdom of Eswatini for holdig its Parliametary election. But, in a very special way, I salute my dear brother, His Excellency Felix Tshekesedi, for emerging victorious in democratic elections, which enabled a peaceful transfer of power for the first time in DRC since its independence in 1960. This is indeed another testimony that democracy has continued to grow and take roots in our sub-region.
At this juncture, I cannot fail to express my appreciation to our Secretariat under the able leadership of Madam Executive Secretary, Dr. Stergomena Tax. During the preparations of this Summit, I was able to experience the sterling job this Secretariat has been doing to our region. But, this is yet another clear testimony that when women are given the opportunity, they can perform a remarkable work. It is for this reason also, we in Tanzania, decided in 2015 to elect a woman, as our Vice-President, Her Excellency Samia Suluhu Hassan. And I am glad that she has never failed us. Your Excellency Madam the Vice-President may you please rise up so that delegates can recognize you.
Your Excellencies;
Distinguished Invited Guests;
Ladies and Gentlemen;
It is an open secret that since its inception, SADC has recorded some important milestones; the elimination of colonialism and apartheid rule being the greatest of them all. But, in addition, thanks to the efforts undertaken by this Organization, peace and security, which forms the cornerstone of our political and socio-economic development, reign in most parts of our region. Indeed, there is no more peaceful and stable region on our continent than the SADC region. I should also mention that since the launching of the SADC Free Trade Area in 2008, intra-regional trade within the SADC region has been growing steadily; from 16 percent of the regional GDP to 22 percent in 2018. It is also pleasing to note that a strong democratic culture is now entrenched in our region and peaceful changes have become the norm.
These are indeed very important milestones. Despite these achievemets, our region is still confroted by many challenges. Yes, there are still many challenges facing our region. Due to time constraints, I will only highlight three of them.
Excellencies, Ladies and Gentlemen;
Just recently, I mentioned that our region is peaceful and more stable than any other part of this continent. This is not to say, however, that our region is free from the conflicts. In some of our countries, conflict situations still exist. In addition, there are other security threats, including international terrorism, organized crimes, climate change, drought, flood, hunger, diseases; that continue to face our region.
It is, therefore, imperative that we continue to work together to address these challenges. This is important because, as we all very well know, peace and security are the most critical pre-conditions for socio-economic development and transformation. Hence, our countries must continue to work hard to make sure that our region is free from conflicts. In this regard, on this matter of peace and security in our region, I urge Your Excellencies that we should always be encouraged by the wise words of one of the greatest sons of this sub-continent, His Excellency Robert Mugabe, former President of Zimbabwe, who once said, and I quote: “Never, never, never must we give up when it comes to the search for peace in any party of our region”, end of quote. As the Chair of the SADC for the next one year, we pledge our commitment to work with all the Member States in order to ensure that peace and security prevail in our region.
Excellencies, Ladies and Gentlemen;
Putting peace and security issues aside, the biggest challenge that, I see, currently confronting our sub-region is that of economic emancipation. In my welcome remarks I mentioned that in transforming the SADCC with double “C” into the SADC with single “C” in 1992, the Leaders of this region had one key objective: to use the political achievements to advance socio-economic development and transformation in our region. Needless to say, I am sure I will be speaking on behalf of many citizens in this region, that, this objective has not been realized, and to be honest, if there are no concerted efforts, it will take ages for this objective to be realized. And I am not saying this without evidences.
Last year, 2018, our region set a target of GDP growth of 7.0 percent; but it grew by only 3.1 percent. This was below the continent’s average growth of 3.5 percent; the Eastern African region growth of 5.7 percent; the Northern African region growth of 4.9 percent and the 3.3 percent growth in the Western African region. In addition, our intra-regional and extra-regional trade performance is also not so good. In 2017, the SADC region, with 16 Member States, a population of 327 million people, a total area of 9,882,959 square kilometers, and which is blessed with abundant and diverse natural resources, only exported goods worth US$ 143 billion. On the other hand, Mexico and Vietnam, countries with areas of 1,943,955 square kilometer and 331,210 square kilometer and a population of 132.5 million people and 97.5 million people each exported goods worth US$ 403 billion and US$ 214 billion, respectively. This clearly shows that our economies are not performing well; and we are still very far from achieving our economic objectives. I am saying this openly because there is no need to hide it. That is the truth.
Excellencies, Ladies and Gentlemen;
Of course, there are many reasons why our economies are not performing as expected; one of them being lack of information on the opportunities available in our respective countries. In May this year, for instance, I had the opportunity to visit four SADC countries. Three of them, due to drought and other natural disasters, were experiencing shortage of food. In this respect, it surprised me to hear that those countries were planning to import food stuff from outside Africa, while we in Tanzania were struggling to find markets for 2.5 million tons of our food surplus. But that is just one example. Due to lack of information, our countries are also importing cars, sugar, and fuel very far away from our region, while some SADC Member States; South Africa, Mauritius and Angola; for instance, are producing the same, respectively.
Exportation and importation costs also contribute to the poor economic performance of our region. Studies have shown that the costs relating to customs in our region are three times higher than in Asia and five times higher than in OECD countries. These costs compounded by the transportation cost, make the situation even worse. I am reliably informed, for instance, that it costs less overall to import animal feed and refined sugar from South America to our countries than to import the same from within our region.
Difference in trade and investment policies, laws, regulations and standards has also its fair share in hindering businesses and economic cooperation between and among SADC Member States and, thus, affecting our economic performance. For example, it is possible today for a good that is produced and cleared in one Member State to be denied to enter the market of another Member State for not being able to meet the quality standards. Why can’t we harmonize our policies, laws, regulations and our quality standards and be able to increase the volume and value of our intra and extra regional trade? Unless we do that, it will remain a day dream for our region to fully realize its economic objectives.
Your Excellencies;
Distinguished Invited Guests;
Ladies and Gentlemen;
At this juncture, allow me also to mention that, apart from those three challenges that I have just highlighted, there is one more challenge that hinders our efforts towards economic emancipation, which to me, is the biggest of them all. That challenge concerns the low level of industrialization in our region. Your Excellencies, history has taught us that no country or region in the world has ever developed without undergoing the process of industrialization. And even today, all developed nations are the industrialized countries.
Just to give you an idea of why the industrial sector is important, the World Trade Organization Statistical Review Report of 2018 indicates that the value of the global trade in 2017 reached US$ 23.01 trillion, of which US$ 17.73 trillion were merchandise trade and US$ 5.28 trillion commercial services. Of importance to note, however, is that, of the US$ 17.73 trillion merchandise trade, 70 percent, almost US$ 12.41 trillion, were manufactured goods. In that same year, Africa, in total, exported goods worth US$ 417 billion, and as I mentioned earlier, SADC exported goods worth US$ 143 billion. More than 60 percent of Africa’s and SADC’s exports were raw materials, mainly agricultural products, mining and fuel. That means that Africa, including the SADC region, has not benefited much from that increase of global trade.
This explains why Africa’s share in the global trade is less than 3 percent. It also explains why the terms of trade are always in favour of other regions. For instance, in the year 2017, Africa exported goods worth US$ 417 billion, but its importation was US$ 534 billion. The reason is simple. We are selling goods of low value. It, therefore, requires us, for instance, to sell not less than 20 tons of cotton, coffee or tea to buy just one tractor. And this also explains why our people continue to remain poor. Raw material in the world markets are sold at very low prices. In addition, due to low level of industrialization in our region, the problem of unemployment is increasing. By exporting our raw materials it means we are also exporting jobs.
Your Excellencies;
Distinguished Invited Guests;
Ladies and Gentlemen;
It is against this background that I would like to seize this opportunity to commend SADC for adopting the Industrialisation Strategy and Roadmap 2015 – 2063. I also commend the decision to prioritize industrialization in each year’s SADC Summit themes and for introducing Industrialisation Week prior to each Ordinary Summit. I am confident that these efforts will go a long way in promoting industrialization in our respective countries and the region at large. In this respect, I wish to assure this august body that issues pertaining to industrialization will be the top priority of our chairmanship.
To this end, I once again, applaud the efforts undertaken by our outgoing Chair, Namibia, to improve infrastructure in our region. There is no gain saying that infrastructure development is an important enabler of industrialization and market integration. That said, however, for our industrial sector to flourish, we must also work together to improve business environment in our region by addressing all impediments and bottlenecks, including transit delays, bureaucratic red-tape, corruptions. This is why Tanzania has chosen “A Conducive Business Environment for Inclusive and Sustainable Industrial Development, Increased Intra-Regional Trade and Job Creation” to be the theme of the SADC during her chairmanship. It is our sincere hope that the implementation of this theme will serve as a catalyst for sustainable industrial development, increased intra-regional trade and job creation in our region.
Your Excellencies Heads of State ad Government;
Before I conclude my statement, allow me to say what I have always been telling my compatriots, and I am sure you also do, that our countries are not poor. Our countries are not poor. They are very rich. We have all the resources to make us rich. Apart from a large population of 327 million people, the SADC region is home to a large number of wildlife and plant species that are of extremely importance; not to mention livestock and marine ecosystems. The region has also a wide diversity of ecozones, including grassland, bushveld, karoo, savannah and riparian zones. In addition, our region is endowed with hydrocarbons materials and mineral resources. Indeed, as a matter of fact, our region contributes to the world about 18 percent of cobalt, 21 percent of zinc, 26 percent of gold, 55 percent of diamond and 72 percent of platinum group of metals. Therefore, we are not poor.
These are indeed resources that one can hope to have in order to be rich. We must, therefore, work together to ensure that we exploit and utilize these resources for the benefits of our countries and our peoples. This is important because, it is only through cooperation that we will be able to utilize these resources effectively and achieve our objectives. And this is what the founding fathers of this Organization and our respective countries, including the Late Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mzee Kenneth Kaunda, the Late Samora Machel, the late Augustinho Neto, the Late Seretse Khama, the Late Nelson Mandela, Mzee Robert Mugabe, Mzee Sam Nujoma, to mention but a few, have taught us, that “the power of unity, when it is channeled with purpose to achieve an objective, can provide remarkable results”. It can even move a mountain. Indeed, it was because of unity, our founding fathers, with limited resources, were able to fight colonialism and emerged victorious.
This is why I appeal to Your Excellencies that, let us work together to ensure the dream that our founding fathers had in establishing this Organization is achieved and our goal for socio-economic transformation and emancipation of our region is realized. Indeed, I personally believe that if we can work together, our economy will not grow by 3.1 percent, we shall be able to improve trade between us, our industrial sector will grow, our contribution to the global trade shall increase, our people will no longer remain poor and decent jobs will be available to our young people.
In addition, I believe, if we work together, peace and security will prevail in our region and we shall also have strong early warning mechanisms and systems that will help us to deal or reduce the impact of natural disasters that have been frequently affecting our countries, including famine, diseass, floods, cyclones and drought.
Your Excellencies,
I have urged you to work together in order to achieve our objectives. However, at this juncture, allow me also, to challenge our Secretariat to assess itself. I am saying this because, all the problems that I have highlighted, which currently confronting our region; happen while we have our own Institution, that is Secretariat, which is supposed to help us Member States overcome them. I personally believe that, if our Secretariat would perform efficiently and effectively its function, it would have found answers to the question why over the past ten years our GDP growth has been increasing on a downward and irregular trend.
The last time that our GDP grew by more than 5 percent was the year 2008, whereby it grew by 5.7. Of course, in the year 2005, 2006 and 2007, our GDP also grew by 6.6 percent, 7.3 percent and 8.0 percent, respectively. However, since then, our economic growth has never grown by more than 5 percent: 2009 (0.6%), 2010 (4%), 2011 (4.0%), 2012 (4.4%), 2013 (4.3%), 2014 (3.4), 2015 (2.2%), 2016 (1.4%), 2017 (3.0%) and last year 2018 (3.1%).
Had our Secretariat also lived up to its duty, our countries would have known the reasons why, after two consecutive years of positive trade balance in 2010 and 2011, SADC region external position deteriorated to a negative balance of USD 17 billion in 2015, USD 9 billion in 2016 and improved a little bit in 2017 to USD 1 billion. These are some of the critical questions that our Secretariat must address and advice Member States accordingly for a new direction.
Excellencies, Ladies and Gentlemen;
It would certainly be remiss of me to end my speech without saying anything on Zimbabwe. As we are all aware, this brotherly and sisterly country has been on sanctions for a long time. These sanctions have not only affected the people of Zimbabwe and their Government but our entire region. It is like a human body, when you chop one of its parts, it affects the whole body. Therefore, I would like to seize this opportunity to urge the international community to lift up sanctions it imposed on Zimbabwe. This brotherly country, after all, has now opened a new chapter and it is ready to engage with the rest of the world. It is, therefore, I believe, in the interest of all parties concerned to see these sanctions removed. In this respect, I wish also to urge all SADC Member States to continue to speak with one voice on the issue of Zimbabwe.
Long Live SADC!
Long Live Africa!
“Aluta Continua”
“I thank you for your kind attention”.

- May 01, 2019
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,KWENYE MAADHIMISHO YA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI, MBEYA, TARE...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,KWENYE MAADHIMISHO YA SIKUKUU
YA WAFANYAKAZI DUNIANI, MBEYA, TAREHE 1 MEI, 2019
Ndugu Tumaini Nyamhokya, Rais wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA);
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
Mwakilishi wa Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Jenista Mhagama, Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi,
Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu;
Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri
wengine mliopo;
Mheshimiwa Albert Chalamila, Mkuu wa Mkoa
wa Mbeya pamoja na Wakuu wa Mikoa mingine mliopo;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Ndugu Makatibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu
mliopo;
Jaji Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi ya Mahakama Kuu pamoja na Waheshimiwa Majaji wengine mliopo;
Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani nchini;
Mwenyekiti wa Chama cha Waajiri Tanzania;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Ndugu Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Ndugu Qambos Sulle, Makamu wa Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi;
Dkt. Yahya Msigwa, Katibu Mkuu wa Shirikisho
la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA);
Viongozi Wengine mliopo wa Vyama Vishiriki vya TUCTA;
Viongozi Wengine wa Serikali mliopo;
Viongozi wa Vyama vya Siasa na Viongozi wa
Dini mliopo;
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;
Ndugu Wana-Mbeya, Mabibi na Mabwana:
Najisikia furaha kubwa sana, kwa mara nyingine tena, kuweza kushiriki Siku hii muhimu ya Wafanyakazi, ambayo huadhimishwa duniani kote kila mwaka. Napenda kwanza kabisa, kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na kutuwezesha kuiona siku ya leo.
Aidha, kwa namna ya pekee, napenda kutoa shukrani zangu nyingi na za dhati kwa Uongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), wakiongozwa na Rais wa Shirikisho, Ndugu Tumaini Nyamhokya, kwa kunialika kuwa Mgeni Rasmi kwenye Maadhimisho haya. Leo ni mara yangu ya nne TUCTA wamenialika kuwa Mgeni Rasmi tangu nimekuwa Rais. Mialiko hiyo ni ishara kwamba, vyama vya wafanyakazi nchini, vinaiunga mkono Serikali ninayoiongoza. Ninawashukuru sana na napenda niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nanyi katika kushughulikia masuala yenu pia kwa lengo la kusukuma mbele gurudumu la maendeleo katika Taifa letu.
Napenda pia kutumia fursa hii kuungana na wote walionitangulia kuzungumza kuwashukuru na kuwapongeza Waratibu wa shughuli hii, Chama cha Wafanyakazi wa Sekta ya Huduma za Mtandao wa Mawasiliano Tanzania (TEWUTA) kwa maandalizi mazuri ya Sherehe hizi. Hongereni sana. Sherehe zimefana.
Vilevile, nawashukuru wenyeji wetu, wananchi wa Mbeya mkiongozwa na Mkuu wenu wa Mkoa, kwa makaribisho yenu mazuri na kwa kujitokeza kwenu kwa wingi kwenye Maadhimisho haya. Ahsanteni sana wana-Mbeya. Waswahili husema “shughuli ni watu”.
Nawashukuru pia Viongozi wengine wa Serikali ambao wamehudhuria Maadhimisho haya, wakiongozwa Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu; Mheshimiwa Spika na Naibu Spika, Waheshimiwa Mawaziri, Waheshimiwa Wabunge, Viongozi wa Ulinzi na Usalama, n.k. Uwepo wenu hapo unadhihirisha kuwa mnawapenda sana wafanyakazi.
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu,
Mabibi na Mabwana;
Siku ya Wafanyakazi au maarufu Mei Mosi, ni siku ambayo dunia huitumia kuenzi na kutambua mchango unaotolewa na wafanyakazi katika kuleta maendeleo. Na hii ni kwa sababu, kama mjuavyo, maendeleo; katika ngazi yoyote ile, iwe mtu mmoja mmoja, familia, taasisi, au nchi; huwa ni matokeo ya kufanya kazi. Waingereza wana usemi usemao “all wealth is the product of labour” na mwingine unasema “Without labour, nothing prospers”. Hii yote ni katika kudhihirisha kuwa kazi na wafanyakazi ni muhimu sana katika kuleta maendeleo.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kwa niaba yangu binafsi na kwa niaba ya Serikali na Watanzania wote; kuwapongeza wafanyakazi wote hapa nchini kwa kuungana na wafanyakazi wengine duniani katika kuadhimisha Siku hii muhimu. Aidha, nawapongeza kwa mchango wenu mkubwa mnaoutoa katika kuiletea maendeleo nchi yetu. Napenda niwahakikishie kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nanyi, ikiwa ni pamoja na kushughulikia changamoto zenu mbalimbali. Ni imani yangu kuwa mtaendelea kufanya kazi kwa bidii, kama Serikali ya Awamu wa Tano inavyosisitiza kuwa “Hapa Kazi tu”. Tukifanya kazi kwa bidii, tutafanikiwa katika lengo letu la kuiletea maendeleo nchi yetu.
Ndugu Wafanyakazi, Mabibi na Mabwana;
Hivi punde tumetoka kusikia Risala nzuri ya TUCTA iliyosomwa na Katibu wake Mkuu, Bwana Msigwa. Kupitia Risala hiyo, Katibu TUCTA ameipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali inazochukua katika kujenga miundombinu na kuboresha huduma za jamii. Aidha, Risala imetaja baadhi ya kero za wafanyakazi pamoja na kutoa mapendekezo yenye nia ya kuchochea ukuaji uchumi nchini.
Namshukuru Katibu Mkuu wa TUCTA kwa Risala hiyo nzuri; na leo napenda nimpongeze kwa kujitahidi kuisoma kwa muda mfupi. He was brief and very clear. Hongera sana. Napenda nikuhakikishie Ndugu Katibu Mkuu wa TUCTA pamoja na wafanyakazi wote nchini kuwa, Serikali imepokea Risala yenu na tunaahidi kuwa yote yaliyomo kwenye Risala, tutayafanyia kazi. Hata hivyo, naomba mniruhusu nizungumzie baadhi ya masuala machache yaliyomo kwenye Risala hiyo.
Ndugu Wafanyakazi, Mabibi na Mabwana;
Baadhi ya hoja zilizotolewa kwenye Risala ni pamoja na maombi ya kutaka Bodi za Mishahara kukutana; kupunguza viwango vya kodi kwa watumishi wote; suala la watumishi wa darasa la saba na uboreshaji wa mazingira na usalama sehemu za kazi.
Napenda niseme kuwa, binafsi, sina tatizo na Bodi za Mishahara kukutana; na kusema kweli, sielewi ni kwa nini hazikutani. Kwangu mimi hata wakitaka kukutana leo, sina shida. Hivyo basi, namwagiza Waziri mwenye Dhamana kuhakikisha Bodi hizo zinakutana. Hata hivyo, napenda kutoa angalizo kuwa vikao vyao visiwe kichochoro cha kutumia fedha za Serikali vibaya.
Kuhusu suala la kupunguza viwango vya kodi na lenyewe sina matatizo nalo. Kama tuliweza kushusha kodi kutoka asilimia 11 had asilimia 9 kwa watumishi wa kima cha chini; bado tunaweza kuendelea kujadiliana kwa ngazi nyingine. Jambo la msingi na muhimu kwa Viongozi wa TUCTA na wafanyakazi ni kutambua kuwa Serikali ina sababu za msingi za kutofautisha viwango vya kodi kulingana na madaraja ya mishahara.
Kuhusiana na suala la watumishi wa darasa la saba, napenda niwahakikishie kuwa, Serikali hii haina ubaguzi kwenye suala la ajira. Katika kuthibitisha hilo, kati ya Watumishi 525,506 ambao Serikali imeajiri nchi nzima, wenye elimu ya darasa la saba wapo 98,615.
Kuhusu suala la uboreshaji wa Mazingira na Usalama sehemu za Kazi, natoa wito kwa waajiri wote kuhakikisha wanazingatia Sheria za Kazi, ikiwemo Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi. Aidha, Waajiri hawana budi kutekeleza matakwa mengine ya kisheria, ikiwemo kutoa mikataba ya ajira na pia kuruhusu uwepo wa vyama vya wafanyakazi sehemu zao za kazi. Kama mtakavyokumbuka, suala hili nimelieleza mara nyingi. Hivyo, kwa mara nyingine tena, naziagiza mamlaka husika kuhakikisha masharti hayo ya sheria yanatekelezwa.
Ndugu Rais wa TUCTA;
Ndugu Katibu Mkuu wa TUCTA;
Ndugu Wafanyakazi Wenzangu;
Sambamba na hayo, kama nilivyoeleza awali, kwenye Risala yenu mmetoa mapendekezo yenye nia ya kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira. Mmeshauri tuongeze bidii kwenye ujenzi wa viwanda vinavyotumia malighafi zinazopatikana nchini; kuongeza bidii katika kutangaza vivutio vyetu vya utalii; kusimamia vizuri masuala ya uchumi wa bahari, ikiwemo kununua meli ya mizigo itakayotoa huduma baharini, n.k.
Mapendekezo yenu yote ni mazuri; na tunakubaliana nayo kwa asilimia 100, japokuwa mengine, utekelezaji wake utategemea upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, napenda niwaarifu kuwa, baadhi ya mapendekezo tumeanza kuyafanyia kazi. Mathalan, kuhusu uchumi wa bahari; tumeanza kuchukua hatua za kulifufua Shirika letu la Uvuvi (TAFIRI), ambapo marafiki zetu wa Japan na Korea, wameonesha nia ya kutuunga mkono. Na kuhusu ununuzi wa Meli ya Mizigo, hilo na lenyewe halina shida. Tumeshaanza kujenga meli mpya za mizigo Ziwa Nyasa; na tunaendelea na ujenzi wa meli nyingine Ziwa Victoria na Tanganyika. Tukishishamaliza huko, tutaelekeza nguvu zetu katika Bahari ya Hindi.
Kwa upande wa utalii, ninyi wenyewe ni mashahidi. Tunajitahidi sana kutangaza vivutio vyetu vya utalii, vikiwemo vilivyo kwenye Ukanda huu wa Nyanda za Juu Kusini; ambavyo kwa bahati mbaya, kwa muda mrefu vilikuwa havitangazwi. Na kutokana na jitihada tulizoanza kuzifanya, idadi ya watalii imeendelea kuongezeka. Mwaka juzi tulipokea watalii milioni 1.2; lakini mwaka jana tumepokea watalii milioni 1.5.
Hivi majuzi mmeshuhudia wenyewe tumepokea takriban watalii 1,000 kutoka Israel. Aidha, Bodi yetu ya Utalii imeingia makubaliano na Kampuni moja ya China kuleta watalii 10,000 kwa mwaka, ambapo kundi la kwanza la watalii 342 linatarajiwa kuwasili nchini tarehe 12 mwezi huu.
Lakini katika juhudi hizo hizo za kuvutia watalii wengi zaidi; na kwa kutambua kuwa watalii wengi husafiri kwa ndege; tunafanya upanuzi wa viwanja vya ndege 11 na tayari tumenunua ndege mpya 8 kwa mpigo. Juzi mmeona, kwa mara ya kwanza, ndege ya abiria imetua kwenye Uwanja wa Ndege wa Nduli, Iringa, baada ya Uwanja kufanyiwa matengenezo.
Ndugu Wafanyakazi, Mabibi na Mabwana;
Ni kweli pia kuwa, kutokana na jitihada mbalimbali tulizozifanya kwa kushirikiana na ninyi wafanyakazi, Serikali imeweza kuongeza ukusanyaji wa mapato. Kwa mfano, mapato ya kodi yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 kwa mwezi mwaka 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 1.3 hivi sasa. Mapato yasiyo ya kodi pia yameongezeka, na hasa baada ya kudhibiti wizi wa rasilimali zetu na pia kuyabana mashirika na kampuni kulipa gawio. Mathalan, mwaka jana, Wizara ya Madini ilipanga kukusanya maduhuli ya shilingi bilioni 190; lakini wakakusanya shilingi bilioni 301. Aidha, mashirika na kampuni zilitoa gawio la shilingi bilioni 717.56 kwa Serikali; kutoka shilingi bilioni 130.686 Mwaka 2014/2015.
Haya ni mafanikio makubwa, ingawa changamoto bado zipo. Na changamoto kubwa iliyopo ni kwamba, gharama za uendeshaji wa Serikali bado zipo juu. Kwa mfano, kila mwezi inatulazimu kutumia takriban shilingi bilioni 580 kulipa mishahara; na wakati huo huo tunatakiwa kulipa madeni ya mikopo ya nyuma, kutekeleza miradi ya maendeleo pamoja na kulipia OC. Hivyo, mnaweza kujionea wenyewe, ni kiasi gani kinabaki baada ya matumizi hayo.
Na hapo ndiyo tumekuwa tukijiuliza maswali mengi kuhusu namna ya kutumia kiasi hicho kinachobaki. Tumekuwa tukijiuliza sana, kama ambavyo mkulima mwenye mbegu hujiuliza wakati wa njaa. Je, azitumie mbegu zake kwa chakula na baada ya muda mfupi arudi tena kwenye njaa; ama azitunze kusubiri msimu wa mvua ili azipande na kumletea mavuno mengi. Tumekuwa pia tukijiuliza kama ambavyo mfanyabiashara hujiuliza wakati wa mtikisiko wa kiuchumi au biashara; je, autumie mtaji wake wote kutatua shida alizonazo kwa wakati huo, ama atafute biashara au shughuli nyingine itakayomwongezea mapato. Tumekuwa tumejiuliza sana maswali hayo.
Na kama nilivyoeleza kwenye Sherehe za Mei Mosi mwaka jana, baada ya kutafakari kwa kina, sisi mliotupa dhamana ya kuwaongoza, tuliona ni busara tutumie kiasi kidogo tunachobakiwa nacho kuwekeza kwenye miradi ya maendeleo itakayosisimua na kuchochea uchumi shughuli za kiuchumi. Shughuli ambazo zitasaidia kuongeza fursa za ajira na kukuza uchumi kwa kasi.
Ni kwa kuzingatia hayo yote, tuliamua kutumia fedha inayobaki kuanza kujenga reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma kwa gharama ya shilingi trilioni 7.026. Tunajenga pia barabara; na napenda nitumie fursa hii kuwaarifu kuwa, jana Benki ya Maendeleo ya Afrika imeidhinishia nchi yetu mkopo wa shilingi bilioni 415.3 kwa ajili ya kujenga barabara ya mzunguko ya njia nne katika Jiji la Dodoma yenye urefu wa kilometa 110.
Zaidi ya hapo, tumeamua kukarabati na kujenga meli mpya kwenye Maziwa yetu Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa kwa takriban shilingi bilioni 287.9 na pia tunapanua Bandari zetu kuu tatu za Dar es Salaam, Mtwara na Tanga kwa zaidi ya shilingi trilioni 1.2. Tunafanya upanuzi wa viwanja vya ndege 11 na tumenunua ndege mpya 8. Aidha, tunatekeleza mradi mkubwa wa umeme katika Bonde la Mto Rufiji ambao utagharimu zaidi ya shilingi trilioni 6.5.
Ni imani yetu kuwa, miradi hii yote itakapokamilika, itarahisisha na kupunguza gharama za usafiri na upatikanaji wa nishati ya umeme; na hivyo, kuchochea shughuli za kiuchumi, ikiwemo viwanda, kilimo, biashara, uvuvi, ufugaji, utalii, uchimbaji madini. Na hayo yakitokea, uchumi wetu utaimarika na mapato ya Serikali yataongezeka.
Ndugu zangu Wafanyakazi, sambamba na kutekeleza miradi hiyo ya miundombinu, tunaendelea kuimarisha na kuboresha upatikanaji wa huduma muhimu za jamii, hususan elimu, afya na maji. Kwa mfano, kwa upande wa afya, tunajenga Hospitali za Wilaya 67 kwa gharama ya shilingi bilioni 105, tumekarabati vituo vya afya 352 kwa shilingi bilioni 184.67 na kuzipatia vifaa vyenye thamani ya shilingi bilioni 41.6. Tumeongeza pia bajeti ya afya kutoka shilingi bilioni 31 hadi shilingi bilioni 270. Kwenye elimu nyote mnafahamu kwamba tunatoa elimu bila malipo, tunajenga miundombinu na tumeongeza mikopo ya vyuo vikuu.
Kwa upande wa maji, tunayo miradi mingi mikubwa tunaitekeleza, ikiwemo Mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kwenye miji ya Nzega, Igunga, Tabora na Sikonge pamoja na mradi mwingine katika Jiji la Arusha, ambayo kwa pamoja tunatumia zaidi ya shilingi trilioni 1. Zaidi ya hapo, tumepata mkopo kutoka India wenye thamani ya shilingi trilioni 1.2 kwa ajili ya miradi ya maji kwenye miji 28, ambapo Mkoa wa Mbeya umepata miradi miwili yenye thamani ya shilingi bilioni 22.5. Tunatekeleza pia miradi ya kusambaza umeme vijijini.
Ni wazi kuwa uboreshaji huu wa huduma hizi muhimu za jamii utasaidia kupunguza gharama za maisha kwa Wafanyakazi na Watanzania kwa ujumla. Hii ni kwa sababu huduma za maji, afya na elimu sasa zinapatikana kwa urahisi na kwa gharama nafuu.
Ndugu Viongozi wa TUCTA;
Wafanyakazi Wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kwa kutekeleza miradi hiyo ya maendeleo na kuboresha huduma za jamii, haina maana kuwa tumeacha kushughulikia masuala ya maslahi ya wafanyakazi. La hasha! Tumeendelea kuyashughulikia. Mathalan, baada ya kukamilisha zoezi la uhakiki wa wafanyakazi hewa na wenye vyeti feki, tangu Mwaka wa Fedha uliopita, tumeanza kutoa nyongeza ya mwaka ya mshahara (annual increment) kwa watumishi 505,985 kwa gharama ya shilingi bilioni 72.8 ambapo shilingi bilioni 37.2 zimelipwa kwa walimu 270,878 na kiasi kingine cha shilingi bilioni 35.7 kwa watumishi wengine wapatao 235,107.
Mbali na nyongeza ya mwaka ya mshahara, kuanzia mwezi Novemba 2015, tumelipa malimbikizo ya mishahara yenye thamani ya shilingi bilioni 75.5 kwa watumishi 50,386. Kati yao, walimu ni 28,115 na wamelipwa shilingi bilioni 27.9. Vilevile, tumelipa shilingi bilioni 9.5 kwa watumishi wastaafu 1,829, ambao nao walikuwa wakiidai Serikali.
Ndugu Wafanyakazi wenzangu, miongoni mwa mabango ya Mei Mosi mwaka huu, mojawapo limeandikwa “tupandishe madaraja ili na sisi tupande bombardier”. Napenda niwaarifu kuwa, tangu mwezi Novemba 2015, tumewapandisha madaraja/vyeo watumishi 118,989 kwa gharama ya shilingi bilioni 29.5, ambapo walimu ni 75,502 na wamelipwa shilingi bilioni 16.3 na watumishi wasio walimu ni 43,487 na wamelipwa shilingi bilioni 13.2. Kwenye Mwaka ujao wa Fedha, tumepanga kuwapandisha vyeo watumishi 193,116. Sambamba na hayo, tumelipa madai mbalimbali yasiyo ya mishahara yenye thamani ya shilingi bilioni 291.3. Na mengi ya madai hayo, yalikuwepo kwa zaidi ya miaka 10.
Kama mlivyoona, kwenye maeneo mengi nimeamua kutofautisha kati ya watumishi walimu na wasio walimu, kwa kuwa walimu ni zaidi ya asilimia 50 ya watumishi wote Serikali.
Ndugu zangu Wafanyakazi;
Ukiachilia mbali hayo niliyoyaeleza, Serikali imelipa kiasi cha shilingi trilioni 1.5 kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Kabla ya kulipa fedha hizo, Mifuko hiyo ilikuwa ikidai Serikali kiasi cha shilingi trilioni 1.6 kwa kushindwa kupeleka michango ya watumishi wake tangu mwaka 2013. Hii iliifanya Mifuko ishindwe kulipa mafao ya wastaafu. Lakini baada ya kulipa deni hilo sasa wanawalipa wastaafu.
Lakini, kama mtakavyokumbuka, kufuatia uamuzi wa Serikali kuunganisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, liliibuka sekeseke kubwa kuhusu kikokotoo kipya kilichopendekezwa. Wafanyakazi wengi hawakuunga mkono kikokotoo hicho. Hivyo, baada ya kutafakari kwa kina, ilibidi tuchukue uamuzi mgumu wa kuendelea na kikokotoo cha zamani. Nasema ulikuwa uamuzi mgumu kwa vile, kikokotoo hicho kinachotumika nchini hakitumiki mahali kokote duniani. Ni sisi tu ndiyo wenye kukitumia. Hata kwenye nchi zilizoendelea hawakitumii. Na hii ndiyo sababu, Mifuko yote mitano ya Hifadha ya Jamii ilikuwa kwenye hali ngumu kiuchumi. Na hali hiyo ilichangiwa zaidi na Mifuko hiyo kujiingiza kwenye miradi isiyo na tija. Hata hivyo, kutokana na kilio cha wafanyakazi, tuliamua kuubeba mzigo huo mzito ili kuwalinda wafanyakazi wetu.
Masuala mengine ambayo Serikali imefanya kwa wafanyakazi ni pamoja na kujenga nyumba za walimu 11,078 na za watumishi wa afya 301. Zaidi ya hapo, baada ya kukamilisha zoezi la uhakiki, tumeajiri watumishi wapya 42,735 ambao kwa mwezi wanalipwa shilingi bilioni 25.8. Aidha, kwenye Mwaka wa Fedha 2019/2020 tumepanga kuajiri watumishi wengine wapya wapatao 45,000. Zaidi hayo, miradi ya miundombinu tunayoitekeleza (reli, umeme, viwanja vya ndege, barabara, n.k.) imetengeneza ajira nyingine nyingi.
Haya yote yanadhihirisha kuwa Serikali inawapenda sana Wafanyakazi. Hivyo basi, nawasihi wafanyakazi kuendelea kuchapa kazi kwa bidii ili kuiletea maendeleo nchi yetu. Wazee wetu wa zamani walijitoa mhanga kuikomboa nchi yetu kisiasa, ni jukumu letu kizazi cha sasa, kujitoa mhanga kuikomboa nchi yetu kiuchumi.
Ndugu Viongozi wa TUCTA;
Wafanyakazi Wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Mei Mosi mwaka huu inasema: “Tanzania ya Uchumi wa Kati inawezekana, Wakati wa Mishahara na Maslahi Bora kwa Wafanyakazi ni Sasa”. Na kutokana na kaulimbiu hiyo, Katibu Mkuu wa TUCTA amenikumbusha kuhusu ahadi yangu niliyoitoa mwaka jana, wakati wa Sherehe kama hizi zilizofanyika Iringa; kwamba, kabla sijaondoka madarakani, nitaongeza mshahara.
Napenda, kwanza, nimkumbushe Katibu Mkuu wa TUCTA kuwa bado sijaondoka madarakani. Aidha, kama nilivyoeleza, kutokana na hatua tulizochukua na tunazoendelea kuzichukua, uchumi wa nchi yetu umeanza kuimarika. Halikadhalika, miradi mingi tunayoitekeleza imeanza kuwanufaisha Watanzania, wakiwemo Wafanyakazi. Hivyo basi, nitumie fursa kuwasihi Wafanyakazi nchini kuendelea kuwa na moyo wa subira, maana subira yavuta heri. Waingereza husema “Before the reward there must be labour. You plant before you harvest”.
Ndugu Viongozi wa TUCTA;
Wafanyakazi Wenzangu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuwashukuru Viongozi wa TUCTA kwa kunialika. Aidha, nawashukuru kwa ushirikiano mkubwa mnaoutoa kwa Serikali. Hatuna budi kuendeleza ushirikiano huu.
Nawashukuru pia wageni wetu walioungana nasi kwenye Maadhimisho haya, wakiwemo Waheshimiwa Mabalozi. Lakini, kwa namna ya pekee, namshukuru Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani kwa kushiriki kwenye Maadhimisho haya. Napenda nimhakikishie kuwa Tanzania itaendelea kuheshimu Mikataba yote ya Kimataifa inayohusu masuala ya kazi, ambayo tumeisaini na kuiridhia.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, narudia tena kuwashukuru wana-Mbeya kwa kujitokeza kwa wingi kwenye Maadhimisho haya. Nawasihi mwendelee kuchapa kazi kwa bidii tukikumbuka kuwa “Hapa Kazi tu” ndiyo kaulimbiu yetu kuu katika Awamu hii ya Tano.
Mungu Wabariki Wafanyakazi wa Tanzania!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 12, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE HAFLA YA KUWEKA SAINI MKATABA WA MRADI WA KUZALISHA UMEME KWE...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWENYE HAFLA YA KUWEKA SAINI MKATABA WA MRADI
WA KUZALISHA UMEME KWENYE BONDE LA MTO RUFIJI
IKULU, DAR ES SALAAM, TAREHE 12 DESEMBA, 2018
Mheshimiwa Dkt. Mostafa Madbouly, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri;
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge
la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Prof. Ibrahim Juma,
Jaji Mkuu wa Tanzania;
Mheshimiwa Bashiru Ally, Katibu Mkuu
wa Chama Cha Mapinduzi;
Waheshimiwa Mawaziri kutoka Tanzania na Misri mliopo;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi na Wakuu wa Taasisi za Kimataifa;
Ndugu Makatibu Wakuu mliopo;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Wageni Waalikwa Wote, Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, napenda kumkaribisha Mgeni wetu, Mheshimiwa Dkt. Mostafa Madbouly, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri pamoja na ujumbe wake hapa nchini. Mheshimiwa Waziri Mkuu; karibu sana hapa Ikulu; karibu sana Dar es Salaam, na karibu sana Tanzania. Tunakushukuru sana kwa uamuzi wako wa kuja kuungana nasi katika tukio hili muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Hii ni ishara tosha kuwa nchi zetu mbili zina uhusiano mzuri.
Na niseme tu kwamba, Tanzania na Misri ni marafiki wa muda mrefu sana. Zamani kabisa, hata kabla ya kuja kwa wakoloni, wafanyabiashara kutoka Misri pamoja na Mataifa mengine ya Kiarabu na Asia walifika kwenye Ukanda wetu wa Pwani kufanya biashara; ambapo pia waliweza kueneza tamaduni zao, ikiwemo lugha ya kiarabu pamoja na dini. Inaelezwa kuwa hata muziki wa taarabu ambao ni maarufu sana hapa nchini, asili yake ni nchi ya Misri.
Uhusiano wetu huo ulikuzwa zaidi na waasisi wa mataifa yetu mawili, yaani Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Gamal Abdel Nasser wa Misri. Viongozi hawa wawili, ambao walishibana sana, walikuwa na maono yenye kufanana kwenye masuala mbalimbali. Kupitia viongozi hawa, mataifa yetu mawili yalitoa mchango mkubwa katika kuanzisha Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), hivi sasa unajulikana kama Umoja wa Afrika (AU); na pia katika harakati za ukombozi wa Bara letu. Kwa sasa, Mataifa yetu mawili yanashirikiana vizuri kwenye nyanja nyingi, ikiwemo biashara na uwekezaji.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Napenda pia nitumie fursa hii kuwashukuru wageni wetu mbalimbali (Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Mabalozi, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Mikoa, Viongozi wa Dini, Vyama vya Siasa, Wana-habari, n.k.) ambao wamekuja kujumuika nasi kwenye tukio hili. Kuwepo kwenu hapa ni uthibitisho kwamba mnatambua umuhimu wa mradi huu. Tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Waziri Mkuu Dkt. Madbouly;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kushuhudia Uwekaji Saini wa Mkataba wa Mradi wa Kufua Umeme wa Bonde la Mto Rufiji. Binafsi najisikia furaha kubwa sana. Kama mnavyofahamu, Mradi wa Umeme wa Bonde la Mto Rufiji ni wa muda mrefu sana. Ulianza tangu enzi za Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwenye miaka ya 1970. Kati ya mwaka 1976 mpaka 1980, Serikali yetu kwa kushirikiana na Serikali ya Norway, kupitia Kampuni ya Norplan & Hafslud, zilifanya upembuzi yakinifu (feasibility study), na kubaini kuwa, Mradi huu wa Bonde la Mto Rufiji una uwezo wa kuzalisha umeme Megawati 2,100. Hata hivyo, kwa sababu mbalimbali, ikiwemo matatizo ya kifedha, nchi yetu haikuweza kuutekeleza. Ni kwa sababu hiyo, nimefurahi sana leo tupo hapa, baada ya kipindi cha zaidi ya miaka arobaini, kushuhudia uwekaji saini wa Mkataba huu.
Nimefurahi pia kwa sababu, Mradi huu tunautekeleza kwa fedha zetu wenyewe, Dola za Marekani bilioni 2.9, sawa na takriban shilingi trilioni 6.558. Na jambo la kufurahisha zaidi ni kwamba, Kampuni itakayotekeleza Mradi huu, M/S Arab Contractors inatoka kwa marafiki zetu wa Misri, ambao ni Waafrika wenzetu. Huu ni uthibitisho kuwa sisi Watanzania tukiamua, tunaweza. Na pia Waafrika tukiamua, tunaweza.
Napenda kutumia fursa hii kuwapongeza Watanzania wote kwa kuweza kufikia hatua hii muhimu ya kuanza kutekeleza Mradi huu, ambao tumeusubiri kwa zaidi ya miaka 40. Naipongeza pia Kampuni ya M/S Arab Contractors kutoka Misri kwa kushinda zabuni ya mradi huu. Kampuni nyingi za nchi mbalimbali zilijitokeza kuomba zabuni hii; lakini iliyofanikiwa ni Kampuni ya M/S Arab Contractors. Hongereni sana.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi sana vya kuzalisha umeme. Na kimsingi, tunavyo karibu vyanzo vyote vya kuzalisha umeme: maji, gesi asilia, makaa ya mawe, jua, upepo, joto ardhi, pamoja na madini ya urania. Hata hivyo, kabla ya kuamua kutekeleza Mradi huu, ilibidi tukae chini na kutafakari kwa kina; ni chanzo kipi hasa kitatufaa katika mazingira yetu ya sasa. Na baada ya tafakuri hiyo, ambapo tulitumia vigezo vikubwa vinne: yaani uhakika wa chanzo chenyewe; gharama za utekelezaji (investment cost); gharama za uzalishaji (cost of generation); pamoja na tija au manufaa yanayotarajiwa kupatikana; tulibaini kuwa Mradi huu ndio unaifaa zaidi nchi yetu kwa sasa.
Kwanza, kwa sababu chanzo chake ni cha uhakika. Kama mnavyofahamu, Mradi huu utatekelezwa kwa kutumia maji yanayotoka kwenye mtandao wa mito iliyopo kwenye maeneo yenye wastani mkubwa wa mvua. Kwa tathmini ya awali, Mradi huu utazalisha umeme kwa zaidi ya miaka 60. Pili, gharama za utekelezaji sio kubwa sana ukilinganisha na vyanzo vingine. Kama nilivyosema, Mradi huu utagharimu shilingi trilioni 6.5. Kama tungeamua kuzalisha Megawati 2,115 kwa kutumia vyanzo vingine, tungelazimika kutumia fedha nyingi zaidi.
Zaidi ya hapo, gharama za kuzalisha umeme wa maji ni ndogo kuliko vyanzo vingine. Uniti moja ya umeme wa maji inazalishwa kwa shilingi 36; wakati uniti moja ya umeme wa nyuklia inazalishwa kwa shilingi 65; jua shilingi 103.05; upepo shilingi 103.05, joto ardhi shilingi 114.5; makaa mawe shilingi 118; gesi asilia shilingi 147; na mafuta shilingi 546. Hii inafanya umeme wa maji uwe nafuu sana kuuzalisha.
Muhimu zaidi ni kwamba, Mradi huu unatarajiwa kutaleta manufaa mengi makubwa kwa nchi yetu. Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Kalemani, ametaja baadhi ya faida hizo. Lakini faida nyingine kubwa ni kwamba, Mradi huu utatuzalishia umeme mwingi zaidi (Megawati 2,115) ambazo ni nyingi kuliko umeme wote ambao unazalishwa kwa sasa hapa nchini, takriban Megawati 1,560. Na kwa vile umeme huo utazalishwa kwa gharama nafuu, bei yake ya kuuza pia itakuwa nafuu. Tunatarajia, Mradi huu utakapokamilika, bei ya umeme nchini itashuka na kuwa nafuu kuliko ilivyo sasa. Zaidi ya hapo, Mradi huu utachochea shughuli nyingine za kiuchumi, ikiwemo viwanda, kilimo, utalii, uvuvi, michezo, n.k. Kwa sababu hiyo, narudia tena kuwapongeza Watanzania wote kwa kuanza kutekeleza mradi huu.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Nafahamu kuwa yapo madai kwamba Mradi huu utaharibu mazingira. Niseme tu kwamba, hiyo siyo kweli. Mradi huu, katika hali halisi kabisa, utasaidia kutunza mazingira yetu. Kwanza, kwa sababu, umeme wa maji ni rafiki wa mazingira. Pili, eneo litakalotumika kuutekeleza ni dogo; litakuwa kati ya asilimia 1.8 hadi asilimia 2 ya eneo zima la Hifadhi ya Selous, ambalo ni kubwa kuliko baadhi ya nchi. Sababu ya tatu ni kwamba, Mradi huu utapunguza ukataji miti nchini. Kwa mujibu wa Taarifa ya Tathmini ya Hali ya Misitu Nchini (National Forest Resources Monitorig and Assessment - NAFORMA) ya Mwaka 2013, mgawanyo wa matumizi ya nishati kwa sasa hapa nchini ni asilimia 92 kwa kuni na mkaa; petroli ni asilimia 7, na umeme ni asilimia 1. Matumizi ya mkaa kwa mwaka yanakadiriwa kuwa zaidi ya tani milioni 2.3, ambapo takriban asilimia 90 ya mkaa wote unaozalishwa, unatumika Dar es Salaam. Matumizi ya mkaa nchini yanatarajiwa kuongezeka maradufu ifikapo mwaka 2030.
Utafiti unaonesha kuwa, ili kuzalisha tani moja ya mkaa kwa kutumia matanuri ya kienyeji, zinahitajika tani 10 hadi tani 12 za miti. Hii maana yake ni kwamba, kwa tani milioni 2.3 za mkaa tunazotumia kwa mwaka, zinahitajika tani milioni 23 hadi milioni 27.6 za miti yenye kipenyo cha zaidi ya sentimita 32 kwa mwaka. Utafiti pia unaonesha kuwa kwa kila miti 18 yenye kipenyo cha sentimita 32, inatoa magunia 26 ya mkaa yenye kilo 53 kila moja. Kwa hiyo, tani milioni 2.3 za mkaa zinazozalishwa kwa mwaka, zinatumia miti milioni 30 yenye kipenyo kisichopungua sentimita 32. Hii ni idadi kubwa sana ya miti.
Hivyo, ni wazi kuwa upatikanaji wa umeme wa uhakika utaokoa idadi hii kubwa ya miti inayokatwa kwa mwaka; na hivyo kusaidia kutunza mazingira yetu. Hivi sasa, kwa sababu ya mahitaji ya mkaa, kila siku, zinavunwa hekta 583 za miti. Hii ni sawa na hekta 212,795 za miti kwa mwaka. Eneo la Selous lina ukubwa wa hekta milioni 5. Hivyo, kwa kasi ya ukataji miti ya sasa, inahitajika miaka 23 tu ili miti yote ya Selous iwe imemalizika; na hiyo ni kwa kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2013. Kwa vile idadi ya Watanzania inaendelea kuongezeka, ambapo kwa sasa tunakadiriwa kufikia milioni 55, inahitajika miaka isiyozidi 15 kumaliza miti yote ya Hifadhi ya Selous.
Ni kwa sababu hiyo, narudia tena kusisitiza kuwa Mradi huu ni muhimu sana kwa utunzaji wa mazingira ya nchi yetu. Tuna matumaini makubwa kuwa, utakapokamilika, wananchi wengi wataachana na matumizi ya kuni na mkaa na kuhamia kwenye umeme, ambao utapatikana kwa bei nafuu. Nawaombe basi wapenda-mazingira wote kuunga mkono mradi huu ambao utaisaidia nchi yetu kutunza mazingira. Kama mnavyofahamu, sisi Watanzania ni watunzaji wazuri sana wa mazingira. Tumetenga zaidi ya asilimia 32 ya nchi yetu kwa ajili ya hifadhi. Sina hakika kama ipo nchi nyingine duniani iliyotenga eneo kubwa kiasi hicho.
Mheshimiwa Waziri Mkuu;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Mabibi na Mabwana;
Kama nilivyosema awali, tupo hapa kushuhudia uwekaji saini ya Mkataba wa Mradi wa Umeme wa Mto Rufiji. Kwa sababu hiyo, sitapenda kuwachosha kwa hotuba ndefu. Hata hivyo, kabla sijahitimisha, naomba mniruhusu nisisitize mambo machache yafuatayo. Kwanza, narudia tena kusema kuwa Mradi huu utakapokamilika, utaipatia nchi yetu umeme wa uhakika na wa bei nafuu; na hivyo kuongeza kasi ya ujenzi wa viwanda na upatikanaji wa fursa za ajira kwa Watanzania. Bei ya umeme kwa sasa nchini ni Dola za Marekani senti 10.7. Kiwango hiki ni kikubwa ukilinganisha na nchi nyingine; ambapo kwa mfano kwa marafiki zetu wa Misri, ambao weyewe wana Megawati 30,000; bei yake ni senti 4.6; Korea Kusini senti 8; China senti 8; Afrika Kusini senti 7.4; India senti 6.8; Algeria senti 3, Ethiopia senti 2.4; Uingereza senti 0.15; na Marekani senti 0.12. Huu ni uthibitisho kuwa gharama za umeme hapa nchini zipo juu sana. Na gharama za umeme zikiwa juu, maana yake ni kwamba gharama za uzalishaji nazo zinakuwa juu. Hii ndiyo sababu bidhaa zetu za viwandani zinashindwa kushindana kimataifa.
Jambo la Pili; hivi punde tumesikia kuwa, baada ya leo kusainiwa kwa Mkataba huu, Mkandarasi atapewa muda wa miezi sita ya kumwezesha kukusanya vifaa; na utekelezaji wa mradi wenyewe utachukua miezi 36. Hii maana yake ni kwamba, mradi huu unatarajiwa kukamilika baada ya kipindi cha miaka mitatu na nusu kuanzia sasa. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii, kutoa wito kwa Mkandarasi kuhakikisha anakamilisha mradi huu kwa wakati; na ikiwezekana umalizike kabla ya muda, ili kudhihirisha kuwa, Waafrika tukiamua, tunaweza. Na binafsi, naamini kuwa Mkandarasi huyu atakamilisha Mradi huu mapema; na hasa kwa kuzingatia kuwa Wamisri ni wachapakazi sana. Waliweza kujenga Ma-piramidi, ambayo mpaka sasa yamebaki kuwa maajabu ya dunia. Hivyo, hata Mradi huu wataumaliza mapema sana. Na bahati nzuri, hata Rais wa Misri, ndugu yangu, Mheshimiwa Al-Sisi, amenihakikishia kuwa mradi huu utakamilika kwa wakati. Yeye mwenyewe alitamani sana kuwepo hapa leo, lakini baadaye tulikubaliana kuwa atakuja wakati wa Kuweka Jiwe la Msingi au Uzinduzi. Hata hivyo, ameniahidi atakuwa akifuatilia kwa karibu utekelezaji wa Mradi huu.
Tatu, napenda nitumie fursa hii kutoa wito kwa wananchi wanaoishi maeneo ambayo Mto Rufiji unaanza, unakopita na sehemu ambako Bwawa litajengwa; kuunga mkono mradi huu, hususan kwa kutunza vyanzo vya maji. Msikate au kuchoma moto miti kiholela, au kuendesha shughuli za kilimo na ufugaji karibu na vyanzo vya maji. Na hapa ninazungumza na wananchi wa Mikoa ya Pwani, Morogoro, Dodoma, Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Lindi na Singida. Natoa wito kwa Wakuu wa Mikoa hiyo kusimamia suala hili; na kwa bahati nzuri, wote mpo hapa.
Mabibi na Mabwana; siwezi kuhitimisha hotuba yangu bila kutoa pongezi zangu nyingi kwa Timu ya Wataalam waliosimama kidete kwenye majadiliano na mipango yote ya maandalizi ya Mradi huu, hadi leo tumeweza kufikia hatua hii. Kwa kutambua mchango wao mkubwa, naomba niwataje majina. Kwanza kabisa, ni Mwenyekiti wa Timu hiyo, Dkt. Leonard Chamuriho, Katibu Mkuu – Uchukuzi, ambaye pia aliongoza Timu yetu ya Majadiliano kuhusu ujenzi wa reli na ununuzi wa ndege. Wajumbe wengine wa Kamati hiyo ni:
- Mhandisi Patrick Mfugale – TANROADS (Mjumbe);
- Dkt. Tito Mwinuka – TANESCO (Mjumbe);
- Ndg. Elias Kissamo – NCC (Mjumbe);
- Ndg. Saidi Kalunde –Nishati (Mjumbe)
- Ndg. Hassan Lugwa – Ofisi ya Rais (Mjumbe);
- Ndg. Glory Kombe – NEMC (Mjumbe);
- Ndg. Beatrice Steven – TRA (Mjumbe);
- Ndg. Edson Mweyuge – AG Chambers (Mjumbe);
- Ndg. Yosepha Tamamu – Hazina (Mjumbe);
- Ndg. Jackson William – Nishati (Mjumbe);
- Ndg. Harold Katainda – TANROADS (Mjumbe);
- Ndg. Leonard Masanja – Nishati (Mjumbe);
- Ndg. James Luchagula – TANESCO (Mjumbe);
- Ndg. Lutengano Mwandambo – TANROADS (Mjumbe);
- Ndg. Stanslaus Kizzy – TANESCO (Mjumbe);
- Ndg. John Mageni – TANESCO (Mjumbe);
- Ndg. Justus Mtolela – TANESCO (Mjumbe);
- Ndg. Mhina Kiondo – Nishati (Mjumbe); na
- Ndg. Pakaya Mtamakaya – TANESCO (Mjumbe).
Hongereni sana wataalam wetu kwa kazi kubwa ya kizalendo mliyoifanya. Nimearifiwa kuwa Ndugu Stanslaus Kizzy anatakiwa kustaafu leo; lakini nimeamua kumwongezea muda mpaka mradi huu utakapokamilika; na kama watakuwepo wajumbe wengine watakaofikia umri wa kustaafu kabla ya mradi huu kukamilika, nao nawaongezea muda; kwa kuwa Timu hii ya Wataalam ndiyo itakayosimamia utekelezaji wa mradi huu. Nitumie fursa hii pia kuipongeza Wizara ya Nishati kwa mchango wake mkubwa kwenye Mradi huu. Aidha, naipongeza Timu ya Wataalam ya Misri, ambao nao wapo hapa.
Mheshimiwa Waziri Mkuu Dkt. Madbouly;
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha hotuba yangu kwa kurudia tena kuwapongeza Watanzania wote kwa kuanza kutekeleza Mradi huu. Tuendelee kushikamana. Kama mjuavyo, Mradi huu umekuwa ukipigwa vita sana. Na hii ni kwa sababu, umeme ni bidhaa muhimu na nyeti kwa Taifa lolote lile duniani. Baadhi ya wanaoupiga, wanafahamu kuwa, endapo tutafanikiwa kuutekeleza, tutakuwa tumepiga hatua kubwa za kimaendeleo. Hivyo basi, narudia tena kuwasihi Watanzania wenzangu tushikamane katika kutekeleza mradi huu. Na niseme tu kwamba, sisi Serikalini tumedhamiria kuutekeleza. Nalishukuru Bunge letu kwa kupitisha Bajeti ya mradi huu; na napenda kumhakikishia Mkandarasi kuwa fedha ya kutekeleza mradi huu tayari tunazo. Lakini nitoe wito kwa Watanzania wenzangu kuendelea kulipa kodi.
Mwisho kabisa, naipongeza tena Kampuni ya M/S Arab Contractors kwa kushinda kandarasi ya kutekeleza mradi huu. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu Dkt. Madbouly kwa kuungana nasi katika tukio hili. Naahidi kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na Misri katika ngazi ya kitaifa na kimataifa. Nirudie tena kuwashukuru wageni wetu mbalimbali mliohudhuria, wakiwemo Waheshimiwa Mabalozi na Viongozi wa Vyama vya Siasa. Lakini, kwa namna ya pekee kabisa, nawashukuru viongozi wa dini kwa kujitokeza kwenu kwa wingi. Hii ni ishara kuwa Mradi huu una baraka za Mwenyezi Mungu na utafanikiwa.
Baada ya kusema hayo:
Mungu Ubariki Mradi Huu!
Mungu Ibariki Kampuni ya Arab Contractors!
Mungu Ubariki Uhusiano wa Tanzania na Misri!
Mungu Ibariki Tanzania.
Mungu Ibariki Afrika!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 10, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE KIKAO KAZI NA VIONGOZI WA MAMLAKA YA MAPATO TANZANIA PAMOJA NA T...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE KIKAO KAZI NA VIONGOZI WA MAMLAKA YA MAPATO TANZANIA PAMOJA NA TAASISI NYINGINE ZA USIMAMIZI
UKUMBI WA MWALIMU JULIUS NYERERE,
TAREHE 10 DESEMBA, 2018
Mheshimiwa Philip Mpango,
Waziri wa Fedha na Mipango;
Waheshimiwa Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Balozi Mhandisi John Kijazi,
Katibu Mkuu Kiongozi;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa mliopo;
Ndugu Makatibu Wakuu mliopo;
Prof. Frolens Luoga, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
Ndugu Charles Kichere, Kamishna Mkuu
wa Mamlaka ya Mapato Tanzania pamoja
na Watendaji wengine wa TRA;
Wakuu wa Taasisi nyingine za Serikali mliopo;
Ndugu Makatibu Tawala wa Mikoa;
Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha tukutane hapa. Aidha, napenda nitumie fursa hii kuwapongeza waandaji, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kwa maandalizi mazuri ya kikao hiki. Nafahamu kuwa muda wa kuandaa kikao hiki ulikuwa mdogo; lakini mmejitahidi hadi kukifanikisha. Hongereni sana.
Kikao hiki, kimsingi, kina madhumuni makubwa mawili. Kwanza, kujadili suala la ukusanyaji mapato nchini, hususan mapato ya kodi. Na pili, kubadilishana mawazo ya namna ya kuboresha mazingira ya biashara nchini; ili hatimaye tuweze kuongeza uzalishaji pamoja na kukuza shughuli za kiuchumi (viwanda, kilimo, biashara, uwekezaji, n.k.). Hii ndio sababu kwenye kikao hiki, tumewaalika pia Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa. Hawa ni wadau muhimu katika masuala ya ukusanyaji kodi na pia kwenye uboreshaji wa mazingira ya biashara nchini.
Waheshimiwa Mawaziri;
Ndugu Watendaji wa Taasisi mbalimbali mliopo;
Suala ukusanyaji mapato, hususan mapato ya kodi, ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi. Wamerekani wana usemi “Hapa duniani kuna mambo mawili tu ya uhakika: kifo na kulipa kodi”. Aidha, Baba wa Taifa letu, Mwalimu Julius Nyerere, aliwahi kusema “Serikali isiyokusanya kodi ni Serikali mufilisi/iliyofilisika. Ni Serikali ya wala rushwa”. Hii inadhihirisha kuwa suala la ukusanyaji kodi ni muhimu sana katika nchi.
Ni kwa sababu hiyo, napenda niwapongeze watendaji wote wa TRA kwa kazi kubwa mnayofanya ya kukusanya kodi. Kwa hakika, kazi yenu ni ngumu sana. Tangu enzi na enzi, watoza kodi ni watu wasiopendwa. Kwa Wakristu, watakuwa wakifahamu habari za Zakayo. Alichukiwa na watu kwa sababu ya kazi yake ya kutoza kodi.
Nitumie fursa hii pia kuwapongeza wafanyakazi wa TRA kwa jitihada mbalimbali mnazofanya za kuongeza mapato. Wakati Serikali ya Awamu ya Tano inaingia madarakani, wastani wa makusanyo ya kodi kwa mwezi yalikuwa shilingi bilioni 850, lakini sasa ni shilingi trilioni 1.3. Hongereni sana.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Licha ya mafanikio hayo yaliyopatikana katika ukusanyaji kodi, ni wazi kuwa mfumo na taratibu zetu za kodi bado zina mapungufu. Baadhi ya mapungufu tuliyonayo ni wigo mdogo wa walipa kodi. Nchi yetu ina wigo mdogo sana wa kodi (tax base) kwa uwiano wa Makusanyo ya Kodi na Pato la Taifa (GDP) ukilinganisha na nchi nyingi za Afrika. Naomba nitoe takwimu chache zifuatazo:
Nchi |
Idadi ya watu |
Idadi yaw a walipa kodi |
Uwiano wa kodi kwa GDP (%) |
Tanzania |
52,554,628 |
2,273,153 |
12.8 |
Kenya |
46,600,000 |
3,940,00 |
18.5 |
Rwanda |
11,671,371 |
172,422 |
15.8 |
Uganda |
37,746,217 |
1,320,691 |
14.2 |
Burundi |
10,400,938 |
22,591 |
13.0 |
Afrika Kusini |
56,522,000 |
19,980,110 |
26.0 |
Botswana |
2,254,021 |
734,470 |
14 |
Zambia |
16,405,229 |
872,748 |
15.8 |
Msumbiji |
27,128,530 |
5,321,669 |
18.0 |
Namibia |
2,368,747 |
666,763 |
12 |
Wigo huu mdogo, kimsingi, unatokana na nchi yetu kushindwa kutumia vizuri vyanzo vya mapato vilivyopo katika kukusanya kodi. Kwanza, tumeshindwa kurasamisha sekta isiyo rasmi (informal sector), ambayo inakadiriwa kufikia asilimia 60 – 70. Hivi sasa tunakusanya kwenye sekta rasmi tu, ambayo ni asilimia 30 hadi 40. Hii maana yake ni kwamba tunakosa fedha nyingi kutoka sekta isiyo rasmi (kwenye kilimo, ufugaji, nyumba, huduma (hoteli), n.k.).
Aidha, nchi yetu bado haijafanikiwa kutumia vizuri rasilimali zake katika kukusanya mapato, na hasa ya kodi. Kwa mfano, Ripoti ya Kamati Maalum ya Spika wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu Uvuvi wa Bahari Kuu ilibainisha, na napenda ninukuu “kiwango cha mapato ambayo Taifa linapoteza kwa kipindi cha miaka 9 iliyopita (2009 – 2017) inakadiriwa kufikia shilingi trilioni 5.985”, mwisho wa kunukuu. Hiki ni kiwango kikubwa sana; na hii ni kwenye sekta ya uvuvi peke yake. Upotevu mkubwa wa mapato kama huo pia upo kwenye sekta za madini na uchimbaji wa gesi asilia. Hivyo basi, Wizara ya Fedha na TRA hamna budi kulifanyia kazi.
Ukiachilia mbali tatizo la kuwa na wigo mdogo wa walipa kodi, ufanisi katika kusanya kodi pia ni mdogo. Ni kweli kuwa, kama nilivyotangulia kusema, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita ukusanyaji kodi umeongeza. Hata hivyo, kiwango tunachokusanya bado ni kidogo; na nitatoa mfano. Kwenye Mwaka wa Fedha 2013/2014, wenzetu wa Kenya walipanga kukusanya Dola za Marekani bilioni 9.74, na walifanikiwa kukusanya Dola za Marekani bilioni 9.64. Sisi tulipanga kukusanya Dola za Marekani bilioni 4.8, tukakusanya Dola za Marekani bilioni 4.4. Katika Mwaka wa Fedha uliopita (2017/2018), Kenya ilipanga kukusanya Dola za Marekani bilioni 15.4, wakakusanya Dola za Marekani bilioni 14.3. Sisi tulipanga kukusanya Dola za Marekani bilioni 7.67, tukakusanya Dola za Marekani bilioni 6.8. Huu uthibitisho kuwa ufanisi wa ukusanyaji kodi nchini bado ni mdogo.
Tatu, viwango vya kodi nchini vipo juu. Yapo malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu viwango vya kodi wanavyotozwa. Na mfano mzuri ni kwenye kodi ya majengo. Kodi za majengo ni kubwa sana. Hii ndio sababu mapato na idadi ya majengo yaliyosajiliwa mpaka sasa ni ndogo sana. Mathalani, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, tumekusanya shilingi bilioni 74.5 tu; na majengo yaliyosajiliwa mpaka sasa ni milioni 1.6. Hiki ni kichekesho. Kwa ukubwa wa nchi yetu na idadi ya watu iliyopo, takriban milioni 55, haiwezekani tuwe na idadi hiyo ya majengo. Kilichofanya msajili idadi ndogo ni viwango vyenu kuwa juu.
Hivyo basi, napenda nitumie fursa hii kurudia tena maelekezo yangu niliyowahi kutoa siku za nyuma kwa TRA, kwamba, kodi ya nyumba iwe shilingi elfu kumi kwa nyumba za kawaida na shilingi elfu ishirini kwa nyumba za ghorofa zilizopo maeneo ya Wilayani na Vijijini; na shilingi 50,000 kwa nyumba za kawaida na kwa kila sakafu (floor) moja ya nyumba ya ghorofa kwa maeneo ya mijini. Na kodi hizo zitozwe kwa kuzingatia hati ya viwanja na sio idadi ya nyumba zilizopo kwenye kiwanja husika.
Nne, ni kuendelea kuwepo kwa mianya ya ukwepaji kodi. Pamoja na jitihada zilizofanyika, bado kuna ukwepaji mkubwa wa kodi kwenye Bonded Warehouses; EPZA, ICDs, maduka ya kubadilisha fedha za kigeni, bandari bubu pamoja na njia za magendo mipakani; na halikadhalika kupitia wafanyabiashara wanaosafirisha na kuingiza bidhaa nchini. Vilevile, baadhi ya wafanyabiashara, kwa kutumia udhaifu uliopo kwenye sheria zetu, wameendelea kukwepa kodi kwa ujanja wa kuongeza gharama za uzalishaji au kuongeza gharama za uendeshaji wa kampuni/masharika yao (transfer pricing and management fee). Zipo kampuni ambazo kila mwaka zinatangaza kupata hasara ili kukwepa kulipa kodi.
Tano, ni matatizo ndani ya TRA yenyewe. Mgawanyo wa watumishi usioendana na potentiality na majukumu katika mikoa na wilaya. Baadhi ya maeneo kuna watumishi wengi, lakini tija haionekani. Aidha, matumizi ya TEHAMA na mifumo ya kieletroniki, yakiwemo matumizi ya EFD, bado hayajaimarika na hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa mapato. Vilevile, kuna suala la kukosekana kwa ushirikiano ndani ya TRA. Mathalan, Meneja wa Mikoa na Wilaya hawawajibiki kwenye masuala ya Forodha na Huduma Saidizi kwa sababu tu wao wanatoka Idara moja ya Mapato ya Ndani. Na kwa upande mwingine, wanaohusika na Forodha nao hawawajibiki kwa Mameneja wa Mikoa na Wilaya isipokuwa kwa Kamishna wa Idara Kuu ya Forodha. Hili ni tatizo ambalo TRA ni lazima mlirekebishe.
Matatizo mengine yaliyopo kwenye TRA ni kupanga malengo bila kufanya utafiti; kuruhusu kuwepo wa watu wanaowakilisha walipa kodi kinyume cha sheria. Vilevile, baadhi ya watumishi wa TRA sio waaminifu. Mathalan, zipo tuhuma kuwa ni wafanyabiashara wachache tu wenye uhusiano na watumishi wa TRA ndio wameruhusiwa kuingiza mashine za EFD na risiti zake. Aidha, zipo tuhuma kuwa, kwa kutumia Mfumo wa Ukadiriaji wa Kodi kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati (Presumptive tax assessment); baadhi ya watumishi wamekuwa wakiomba rushwa ama kuwababimbikiza kodi kubwa wafanyabiashara wadogo na hivyo kulazimika kufunga biashara zao; hali inayofanya waichukie Serikali yao.
Hizo nilizotaja ni baadhi tu ya changamoto zinahusu mifumo na taratibu za kodi nchini. Lakini, ukiachilia mbali mapungufu hayo ya ukusanyaji kodi, nchi yetu pia haifanyi vizuri sana katika kukusanya mapato yasiyo ya kodi. Ni kweli kuwa tumefanikiwa kuongeza ukusanyaji wa mapato yasiyo ya kodi kutoka shilingi bilioni 284 Mwaka wa Fedha 2010/2011 hadi kufikia shilingi trilioni 2.2 katika Mwaka wa Fedha 2017/18. Hata hivyo, kiwango hiki bado ni kidogo.
Hivyo basi, natoa wito kwa mamlaka zote zinazohusika na ukusanyaji wa mapato nchini, ya kodi na yale yasiyo ya kodi, zikiwemo Halmashauri, kuongeza bidii katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameeleza hivi punde kuwa, fedha za mikopo na misaada kutoka kwa wahisani na wafadhili zinakuja taratibu sana; na hata zikija, wakati mwingine zinaambatana na masharti magumu. Hivyo basi, ni lazima sisi wenyewe tutafute mbinu za kujitegemea kifedha. Faida za kujitegemea kifedha zipo nyingi baadhi zimeanza kuziona; tumenunua ndege mpya saba kwa fedha zetu wenyewe, tunajenga reli, meli; tunaboresha huduma za jamii, ikiwemo elimu, maji na afya. Kesho kutwa tunaweka saini Mkataba wa kutekeleza mradi wa umeme wa Bonde la Mto Rufiji. Hivyo, narudia kuzihimiza mamlaka husika kuongeza bidii ya ukusanyaji mapato ya Serikali. Na katika kutekeleza jukumu, msimwogope au kumwonea mtu yeyote.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Sambamba na matatizo hayo ya ukusanyaji mapato niliyotaja, mazingira ya kufanya biashara nchini pia sio mazuri sana. Tuna shida katika kutoa vibali vya uwekezaji, huduma za usafirishaji, umeme, utitiri wa taasisi za usimamizi unaombatana na kodi, ada, ushuru na tozo mbalimbali. Ni kweli kuwa, katika miaka ya hivi karibuni, tumejitahidi sana kuimarisha miundombinu ya usafiri pamoja na upatikanaji wa huduma za umeme; ambapo, kwa mfano kesho kutwa tunaweka saini ya ujenzi wa mradi mkubwa wa kufua umeme wa Bonde la Mto Rufiji.
Hata hivyo, bado tuna matatizo ya ucheleweshaji kwenye Bandari, vizuizi barabarani (rasmi na visivyo rasmi), n.k. Wafanyabiashara wanahangaika sana kutoa mizigo yao bandarini; na wawekezaji inawachukua muda mrefu kupata vibali vya uwekezaji. Hii ndio sababu kwenye kikao hiki, tumewaalika pia Mamlaka ya Bandari, Shirika la Reli, Benki Kuu ya Tanzania, TIC, BRELA, TBS, TFDA, Mkemia Mkuu wa Serikali; lengo ni kutaka kutafuta ufumbuzi wa matatizo hayo yote. Nina imani, watu wa Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, Idara ya Kazi, NEMC, OSHA, pia wapo. Kama hawapo, mambo yatakayoamuliwa hapa, yafikishwe kwao.
Waheshimiwa Mawaziri;
Ndugu Watendaji wa Taasisi mbalimbali;
Nimeeleza mengi. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba niseme suala moja la mwisho. Ndugu zangu, upo uhusiano wa karibu sana kati ya mifumo au taratibu za kodi kwa upande mmoja; na kuimarika kwa mazingira ya biashara, kuongezeka kwa uzalishaji na mapato kwa upande mwingine. Taratibu za kodi zikiwa rahisi na viwango vyake vikiwa chini; watu uhamasika kufanya biashara na kuwekeza; na kama watu wengi watafanya biashara na kuwekeza, maana mapato nayo yataongezeka. Lakini kinyume chake; viwango vikiwa juu na taratibu zikiwa ngumu, mazingira ya biashara yanakuwa magumu, watu wanashindwa kufanya biashara na kuwekeza; na hatimaye mapato yanapungua. Kwa kuzingatia hayo, napenda kutoa wito ufuatao:
Kwanza, ni kwa TRA na mamlaka nyingine zinazohusika na ukusanyaji wa mapato nchini. Hakikisheni mnatengeneza mazingira rahisi ya watu kulipa kodi. Imarisheni mifumo ya kielektroniki ili watu wasilazimike kutembea umbali mrefu ama kutumia muda mwingi kulipa kodi. Muda ni mali. Aidha, kama nilivyosema hivi majuzi pale Arusha, pitieni upya viwango vya kodi mnazotoza. Watu wengi wanawalalamikia kuhusu viwango vyenu. Viwango vya kodi vikiwa chini, sio tu itawapunguzia gharama za kuwafuatilia walipa kodi bali pia itapunguza vitendo vya rushwa. Sambamba na hilo, nawasihi mpanue wigo wa walipa kodi.
Pili, ni kwa taasisi zinazohusika na masuala ya biashara na uwekezaji nchini. Nia na makusudi ya Serikali kuanzisha taasisi hizi ilikuwa kuongeza ufanisi. Lakini, kwa bahati mbaya, nyingi zimegeuka kuwa kikwazo. Wamekuwa kikwazo Bandarini; lakini pia pale TIC. Hivyo, natoa wito kwa taasisi hizo kujirekebisha, ikiwa ni pamoja na Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, NEMC, Idara ya Kazi. Nahimiza pia TPA pamoja na Shirika la Reli kuzidi kuboresha huduma zenu.
Tatu, ni kwenu Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa. Kama nilivyosema awali, ninyi ni wadau muhimu sana katika masuala ya kodi na uboreshaji wa mazingira ya biashara nchini. Sheria ya Kodi ya Mapato ya Tanzania ya Mwaka 2004 pamoja na Kanuni zake, Kanuni ya 41 (1), imeanzisha Kamati ya Wilaya ya ushauri kuhusu masuala ya kodi katika Wilaya. Aidha, Kanuni ya 41 (2) inamtaja Mkuu wa Wilaya kuwa Mwenyekiti na Afisa Mapato wa Wilaya wa TRA kuwa Katibu. Miongoni mwa watu wanaoweza kuteuliwa kuwa Wajumbe wa Kamati hii wanachaguliwa na Mkuu wa Mkoa, ambaye naye ana wajibu wa kudai kumbukumbu za vikao vya Kamati ili kufahamu masuala mbalimbali ya kodi katika Mkoa wake. Sina hakika, kama Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa mnafahamu hili. Na hii ndio sababu hasa ya kuwajumuisha kwenye kikao chetu hiki, ili mkasimamie haya yote mkishirikiana na viongozi walio chini yenu. Wakuu wa Mikoa pia mna wajibu wa kutengeneza mazingira mazuri ya biashara katika maeneo yenu, ikiwemo kutenga maeneo maalum ya kufanya biashara, hususan kwa wafanyabiashara wadogo, na pia maeneo ya uwekezaji.
Nne, ni kwa Watanzania wenzangu kwa ujumla. Napenda niwahimize kuendelea kulipa kodi. Kodi ndiyo inawezesha Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo na pia kuboresha huduma za jamii. Najua bado wapo Watanzania wachache wenye kuona fahari kukwepa kodi. Nitoe wito kwa TRA kuendelea kuwaelimisha watu wa namna hiyo. Zaidi ya hapo, hakikisheni mnatoa adhabu kali kwa wakwepa kodi.
Waheshimiwa Mawaziri;
Ndugu Watendaji wa Taasisi mbalimbali;
Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuwapongeza TRA kwa kuandaa Mkutano huu. Aidha, nawapongeza wote mliohudhuria Kikao hii. Nawatakia majadiliano mema, na yote mtakayoyaamua hakikisheni kuwa mnayatekeleza. Binafsi, nina matumaini makubwa kuwa, baada ya kikao hiki, tutaanza kuona mageuzi makubwa ya kiutendaji katika TRA pamoja na taasisi nyingine zinazohusika na masuala ya ukusanyaji mapato na uboreshaji wa mazingira ya biashara nchini.
Mwisho kabisa, kutokana na kasi ndogo ya zoezi la usajili wa wafanyabiashara wadogo, Ofisi yangu (TAMISEMI) imeamua kuandaa Vitambulisho vya Wafanyabiashara Wadogo, ambavyo vitawawesha kufanya shughuli zao kwa uhuru. Baada ya kumaliza hotuba yangu, nitamkabidhi kila Mkuu wa Mkoa vitambulisho 25,000 kwa ajili ya kwenda kuvigawa kwa wafanyabiashara wadogo kwenye mikoa yao. Kitambulisho hiki, ambacho kimewekewa alama za usalama zisizogushika kwa urahisi, kimsingi kitatolewa bure. Hata hivyo, wafanyabiashara wadogo itabidi wachangie gharama ndogo utenganezaji, kiasi cha shilingi 20,000 tu. Mfanyabiashara anayestahili kupata kitambulisho hiki ni mwenye kufanya mauzo (turnover) yasiyozidi shilingi milioni 4 kwa mwaka. Lakini, napenda kutumia fursa hii kutoa wito kwa wafanyabiashara wadogo watakaopata vitambulisho hivyo, kutokubali kutumiwa na wafanyabiashara wakubwa kukwepa kodi. Aidha, hakikisheni kuwa shughuli zenu mnazifanya kwenye maeneo yaliyoruhusiwa.
Mungu zibariki Mamlaka za Ukusanyaji Mapato nchini!
Mungu Zibariki Mamlaka zote zenye Kuhusika na Uboreshaji wa Mazingira ya Biashara nchini!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Dec 02, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UWEKAJI JIWE LA MSINGI LA MRADI WA MAJI SAFI NA MAZINGIRA W...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE UWEKAJI JIWE LA MSINGI LA MRADI WA MAJI SAFI NA MAZINGIRA WA ARUSHA, KIMYAKI, ARUMERU, TAREHE 2 DESEMBA, 2018
Mheshimiwa Prof. Makame Mbarawa,
Waziri wa Maji;
Mheshimiwa Mhandisi Isack Kamwelwe, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Mheshimiwa Alex Mubiru, Mwakilishi wa Benki ya Maendeleo Afrika nchini Tanzania;
Mheshimiwa Mrisho Gambo,
Mkuu wa Mkoa wa Arusha;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa CCM – Mkoa wa Arusha;
Waheshimiwa Wabunge mliopo;
Ndugu Makatibu Wakuu wa Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa;
Mstahiki Meya pamoja na Madiwani wa Jiji la Arusha;
Viongozi wengine wa Serikali mliopo;
Ndugu Wana-Arusha, Mabibi na Mabwana;
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa siku ya leo. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri Prof. Mbarawa kwa kunialika ili nami nishiriki katika tukio hili muhimu kwa wakazi wa Jiji la Arusha. Ahsante sana.
Napenda pia nitumie fursa hii kuwashukuru wana-Arumeru na wana-Arusha kwa ujumla kwa kujitokeza kwenu kwa wingi katika hafla hii. Lakini, kwa vile hii ni mara yangu ya kwanza kufika kwenye eneo hili tangu nimekuwa Rais, napenda niwashukuru wana-Arumeru kwa kunichagua. Nawaahidi kuendelea kuwatumikia kwa moyo wangu wote.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Maji ni rasilimali muhimu sana. Ni muhimu, kwanza, katika maisha ya binadamu. Ninyi nyote hapa mnafahamu kuhusu usemi usemao “maji ni uhai”. Usemi huu unamaanisha kuwa maisha ya binadamu yanategemea maji. Bila ya maji hakuna uhai. Lakini, zaidi ya hapo, maji ni muhimu kwa shughuli za kiuchumi na uzalishaji, ikiwemo kilimo, uvuvi, ufugaji, viwanda, utalii, ujenzi, n.k. Kwa ujumla, shughuli zote za maendeleo duniani zinahitaji maji.
Pamoja na ukweli huo, ni ukweli pia usiopingika kuwa upatikanaji wa maji nchini bado sio wa kuridhisha sana. Hadi kufikia mwaka 2015, takwimu zilionesha kuwa upatikanaji wa maji nchini ulikuwa wa kiwango cha asilimia 50.2. Hapa Arusha penyewe, kwa mfano, mpaka sasa uzalishaji wa maji ni mita za ujazo 40,000, sawa na asilimia 42.9 tu ya mahitaji ambayo ni mita za ujazo 93,270.
Ni kwakuzingatia hilo, Serikali ya Awamu ya Tano, kupitia Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 - 2020; na nimefurahi kuona Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha yupo hapa; tuliahidi kuwa tutaboresha upatikanaji wa maji nchini, hususan kwa kuhakikisha tunakamilisha miradi ya zamani ambayo ilikuwa imekwama na pia kutekeleza miradi mipya. Waswahili husema “ahadi ni deni”. Hivyo basi, leo nafurahi nipo hapa Arusha kuweka Jiwe la Msingi la Mradi huu. Hii maana yake ni kwamba, CCM ikiahidi jambo, inatekeleza.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Mradi wenu wa maji ni mkubwa sana. Kama mlivyosikia, utakapokamilika, utakuwa na uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 208,000, zaidi ya mara nne ya kiwango kinachozalishwa sasa; na mara mbili zaidi ya mahitaji yenu ya sasa. Kwa maana hiyo, maji yatakuwa mengi zaidi kuliko mahitaji yenu. Hongereni sana wana-Arusha.
Utekelezaji wa mradi huu utagharimu Dola za Marekani milioni 233.9, zaidi ya shilingi bilioni 520. Fedha hizi ni za mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (The African Development Bank – AfDB). Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuishukuru AfDB kwa kutupatia mkopo huu. Benki hii imekuwa ni mdau mkubwa wa maendeleo wa nchi yetu. Wameshirikiana nasi katika kutekeleza miradi mingi ya maendeleo. Kwa mfano, kwa upande wa sekta ya maji, hawa ndio walitupa mkopo wa kutekeleza Miradi wa Maji ya Sengerema na Nansio, ambayo tayari nimeizindua. Wametufadhili pia kwenye miradi ya miundombinu, hususan usafiri na umeme. Tunawashukuru sana.
Nimefurahi kuona Mwakilishi wa Benki hiyo nchini, Bwana Alex Mubiru pamoja wapo hapa. Tunawaomba utufikishie shukrani zetu nyingi kwa uongozi wa juu wa Benki. Tunaomba muendelee kutuunga mkono.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Mbali na mradi huu, Serikali inatekeleza miradi mingine mikubwa ya maji. Mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka miji ya Nzega, Igunga na Tabora wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 268, takriban shilingi bilioni 600. Aidha, tumepata mkopo kutoka India wenye thamani ya shilingi trilioni 1.2 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa kupeleka maji kwenye miji 25.
Hivi majuzi tu, tumepata fedha nyingine kutoka Benki ya Dunia, Dola za Marekani milioni 350, takriban shilingi bilioni 800, kwa ajili ya kufanya ukarabati wa miradi iliyokuwa imesimama au haifanyi kazi. Katika Mkoa wenu wa Arusha, mbali na mradi huu nitakaoweka Jiwe la Msingi leo, tunatekeleza miradi mikubwa ya maji Simanjiro, Longido, Loliondo pamoja na Karatu.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Ukiachilia mbali miradi ya maji, katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, Serikali imechukua hatua nyingine muhimu za kuiletea maendeleo nchi yetu. Tumeongeza bajeti ya mikopo ya elimu ya juu shilingi bilioni 365 hadi kufikia shilingi bilioni 427. Tunatoa elimu bure, ambapo kila mwezi tunatenga shilingi bilioni 23.863. Tumeongeza bajeti ya dawa kutoka shilingi bilioni 31 hadi shilingi bilioni 270 hivi sasa. Tumekarabati vituo vya afya zaidi ya 300. Tunajenga hospitali mpya za wilaya 67.
Tunajenga miundombinu ya barabara na tunasambaza umeme. Hapa Arusha, tumekamilisha ujenzi wa barabara ya kisasa ya njia nne ya Sakina - Tengeru yenye urefu wa kilometa 14.1. Aidha, hivi sasa tunajenga barabara za mzunguko zenye urefu wa kilometa 42.3. Hizi zote ni jitihada za kueletea maendeleo nchi yetu.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Wabunge wenu wameeleza kuhusu kusuasua kwa utekelezaji wa mradi wa kupeleka umeme vijijini na pia wameombea barabara ya kutoka Mianzini hadi Ngaramtoni yenye urefu wa takriban kilometa 18 ijengwe kwa lami. Napenda, kwanza kabisa, kutumia fursa hii kumwagiza Waziri wa Nishati kuhakikisha anamfuatilia kwa karibu Mkandarasi huyo aliyepewa zabuni ya kusambaza umeme hapa Arusha. Na endapo itathibitika kuwa, Mkandarasi hana uwezo, basi asisite kumchukulia hatua. Na kuhusu ujenzi wa Barabara, naagiza, kwanza, ipandishwe hadhi kuwa ya Mkoa, na taratibu za ujenzi zianze mara moja. Kwa bahati nzuri, Waziri wa Ujenzi upo hapa. Mnaweza kuanza na kipande cha kilometa 8 kutoka Mianzini hadi hapa; na kisha mmalizie sehemu iliyobaki ya kilometa 10 hadi Ngaramtoni. Kama zipo fedha zilizotengwa na TARURA kwa ajili ya kujenga barabara hii sasa zihamishiwe TANROADS. Lakini niwaombe wananchi nanyi muwe wavumilivu. Ujenzi wa barabara una taratibu zake.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kuweka Jiwe la Msingi la Mradi wa Maji wa Arusha. Kabla ya kuhitimisha hotuba yangu, napenda nitumie fursa hii kutoa wito kwa Wakandarasi wote kumi wanaotekeleza Mradi huu kuhakikisha wanaukamilisha kwa wakati. Sitaki kabisa kusikia habari za ucheleweshaji. Nayasema hayo kwa sababu nafahamu, moja ya changamoto zenye kuikabili sekta ya maji nchini ni kuchelewa kutekelezwa kwa miradi. Narudia tena hilo sitaki litokee kwenye Mradi huu. Nakupongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa kuanza kuchukua hatua dhidi ya wakandarasi wazembe wanaochelewesha miradi. Endelea hivyo hivyo. Lakini, nakuagiza pia Mheshimiwa Waziri kuhakikisha maeneo/vijiji ambavyo mradi huu utapita, wananchi wapate maji; na pia angalia uwezekano wa Mradi huu kufikisha maji kwenye kijiji cha Oldonyosambu, ambacho jana wananchi waliniomba maji.
Pili, ni kwenu wananchi. Kama mlivyosikia, Mradi huu ni wa mkopo. Baadaye Serikali itaulipa. Na Serikali haina njia nyingine ya kupata fedha zaidi ya kodi zenu. Hivyo, nawasihi sana, tulipe kodi. Nimesikitika sana kusikia tabia ya kukwepa kodi inashamiri. Baadhi ya watu wanatumia mbinu mbalimbali kukwepa kodi, ikiwemo kuwatumia wafanyabiashara wadogo kuwauzia bidhaa zao, kuacha kutumia mashine za kielektroniki, kutengeneza risiti feki ama kuandika risiti chini ya thamani halisi ya bidhaa husika.
Tabia za namna hiyo zinaikosesha sana Serikali mapato mengi, ambayo yangetumika kutekeleza miradi ya maendeleo. Hivyo basi, nawasihi sana wananchi tutambue umuhimu wa kulipa kodi. Na niwaombe sana marafiki zangu wamachinga, msikubali kutumika kukwepa kodi. Serikali ilimewaruhusu kufanya shughuli zenu kwa uhuru ili muweze kuinua vipato vyenu na kuondokana na umaskini. Nawasihi sana, msiitumie vibaya nia hiyo njema ya Serikali. Najua wenye tabia hiyo ni wachache. Wafichueni.
Napenda pia kutumia fursa hii kutoa wito kwa TRA kuwachukulia hatua kali wakwepa kodi. Lakini zaidi ya hapo, na ninyi inapaswa mjitathimini kwanini watu wanatafuta mbinu mbalimbali za kukwepa kodi. Wakati mwingine, chanzo ni ninyi wenyewe. Mnaweka viwango vikubwa sana vya kodi, ambavyo havilipiki. Ni bora muweke viwango vidogo vyenye kulipika kuliko kuweka viwango vikubwa visivyolipika.
Jambo la tatu, nawasihi wananchi kutunza vyanzo vya maji. Kama nilivyosema awali, maji ni rasilimali muhimu sana. Lakini, kwa bahati mbaya, rasilimali hii inaendelea kupungua kila kukicha kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu pamoja na uharibifu wa vyanzo vyake. Hivyo, nawasihi Watanzania tutunze vyanzo vyetu vya maji.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda kuwapongeza wana-Arusha na Watanzania kwa ujumla, kwa kuendelea kuitunza amani yetu. Amani ndiyo msingi wa maendeleo. Kwa sababu hiyo, nawasihi sana tuendelee kudumisha amani. Tusikubali kufarakanishwa kwa sababu ya dini zetu, makabila yetu au vyama vyetu. Maendeleo hayana chama. Mradi huu wa maji utamnufaisha kila mwananchi. Hivyo basi, hatuna budi kushikamana na kuwa kitu kimoja. Aidha, nawasihi muendelee kuchapa kazi kwa bidii. Wakati nakuja hapa, nimeshuhudia kila mahali pamelimwa. Hongereni sana wana-Arumeru. Hiyo ndio dhana halisi ya “hapa kazi tu”.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kusema kuwa nchi yetu inaendelea vizuri. Tunajenga miundombinu mbalimbali na kuboresha huduma za jamii. Tunajenga reli mpya ya kisasa. Tunafufua reli yetu kutoka Tanga kuja Arusha. Tumenunua ndege. Tunajenga barabara. Na tupo mbioni kuanza kutekeleza mradi mkubwa wa kuzalisha umeme wa Bonde la Mto Rufiji.
Tunaendelea kusimamia vizuri rasilimali zetu. Tangu tumepitisha sheria ya kulinda rasilimali zetu, mapato yameongezeka. Mwaka uliopita, tulipanga kukusanya shilingi bilioni 194, lakini tumekusanya shilingi bilioni 301. Lakini ninyi wana-Arusha mnafahamu vizuri. Zamani tulikuwa tukiibiwa sana tanzanite yetu. Sasa tumefanikiwa kudhibiti wizi huo baada ya kujenga ukuta kuzunguka mgodi pale Mererani.
Sambamba na hayo, tunaendelea kushughulikia kero mbalimbali (rushwa; utitiri wa tozo kwenye kilimo, mifugo na uvuvi; migogoro ya ardhi; n.k.). Yote haya lengo lake ni kuiletea nchi yetu maendeleo. Na kuhusu suala la mifugo, nakuagiza Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kushirikiana na Wizara ya Mifugo kuanzisha Mnada ili wananchi wauze mifugo yao kwa uhuru na kupata faida. Hiyo ndiyo namna ya kujenga uchumi wa kisasa. Badala ya kuwazuia wananchi kupeleka mifugo nje; wekeni mazingira mazuri yatakayowawezesha wananchi kufanya biashara hapa nchini.
Mungu Ubariki Mradi huu!
Mungu Ibariki Arusha!
Mungu Ubariki Uhusiano kati ya Tanzania na AfDB!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Nov 27, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UZINDUZI WA MAKTABA YA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM KAMPASI YA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KWENYE UZINDUZI WA MAKTABA YA CHUO KIKUU
CHA DAR ES SALAAM KAMPASI YA MLIMANI
TAREHE 27 NOVEMBA, 2018
Mheshimiwa Jaji Mstaafu Damian Lubuva, Mwenyekiti
wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;
Mheshimiwa Prof. Ibrahimu Juma,
Jaji Mkuu wa Tanzania;
Waheshimiwa Mawaziri Wakuu Wastaafu,
Mzee Joseph Warioba na Mzee Edward Lowasa;
Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu,
Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi;
Waheshimiwa Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Wang Ke, Balozi wa China nchini;
Mheshimiwa Paul Makonda,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Peter Serukamba, Mwenyekiti
wa Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii
pamoja na Wabunge wengine mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Prof. William Anangisye, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam;
Viongozi wengine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;
Waheshimiwa Viongozi wengine wa Serikali mliopo;
Ndugu Wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
(Wahadhiri, Watumishi na Wanafunzi);
Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda, kwanza kabisa, kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetuwezesha tukutane hapa. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Prof. Ndalichako, pamoja na uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kunialika kuzindua Maktaba hii, ambayo ni kubwa na ya kisasa kwa nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara. Nawashukuru sana kwa mwaliko wenu.
Leo ni mara yangu ya tano kufika kwenye Chuo Kikuu hiki tangu nimechaguliwa kuwa Rais. Nilifika mara ya kwanza kuweka Jiwe la Msingi la Maktaba hii. Kisha nilikuja kukagua ujenzi wa Hosteli zenu. Baadaye nikaja kuzizindua. Mwezi huu mwanzoni mlinialika kuhudhuria Mdahalo. Hivyo, leo ni mara ya tano. Ahsanteni sana wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hiki ni Chuo Kikuu kikongwe nchini, hivyo, nimekuwa nikifurahi sana kufika hapa. Na nashukuru, mara zote mmekuwa mkinipokea vizuri. Hata hivyo, napenda kusema kuwa, mimi navipenda vyuo vyote nchini. Hii ni kwa sababu, vyuo vyote ni vyangu.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kuzindua Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyojengwa kwa ufadhili wa marafiki zetu wa China kwa gharama ya Dola za Marekani milioni 41.28, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 90. Kama mlivyosikia, Maktaba hii ni kubwa na ya kisasa kwa nchi za Afrika zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara. Ina Jengo la Maktaba lenye uwezo wa kuhudumia wasomaji 2,100; eneo la makasha yenye uwezo wa kuweka vitabu laki nane; eneo la kusomea lenye kompyuta 160, ukumbi wa mikutano wa kukaa watu 600. Aidha, mradi huu umejumuisha Jengo la Taasisi ya Confucius inayofundisha lugha na tamaduni za Kichina kwa ajili ya wanafunzi wa Chuo hiki pamoja na Watanzania wengine.
Napenda kutumia fursa kumpongeza Mkandarasi aliyejenga Maktaba hii, Kampuni ya Jiangsu Jiangdu kutoka China kwa kukamilisha mradi huu kwa wakati; na kwa viwango vya hali ya juu sana. Kwa hakika, jengo linapendeza sana. Hongereni sana. Aidha, kama nilivyosema wakati wa kuweka Jiwe la Msingi, mradi huu ulipatikana wakati wa uongozi wa Awamu ya Nne. Hivyo, sisi wengine tumekuja kusimamia utekelezaji wake tu. Hivyo basi, kwa dhati kabisa, napenda kurudia tena kumshukuru na kumpongeza Rais wa Awamu ya Nne, Mzee Kikwete, pamoja na watendaji wote waliofanikisha kupatikana kwa Mradi huu. Tunawashukuru sana.
Kwa namna ya pekee kabisa, napenda kutoa shukrani zangu nyingi kwa marafiki zetu wa China kwa kutujengea Maktaba hii kubwa, nzuri na ya kisasa. Ahsanteni sana marafiki zetu wa China. Na niseme tu kwamba, China wamekuwa marafiki wa kweli wa nchi yetu kwa muda mrefu. Uhusiano huu uliimarika zaidi kutokana na urafiki uliokuwepo kati ya waasisi wa Mataifa yetu mawili, yaani Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere na Mwenyekiti Mao Zedong. Kupitia viongozi hao wawili, nchi zetu mbili zimekuwa zikishirikiana kwenye mambo mengi katika nyanja za kitaifa na kimataifa; ambapo sisi Tanzania tumenufaika na misaada mingi kutoka China. Jambo la kufurahisha ni kwamba, misaada kutoka China haina masharti. Wenyewe wakiamua kukupa, wanakupa tu. Walitujengea TAZARA, Kiwanda cha URAFIKI; lakini pia tunashirikiana nao kwenye nyanja afya, elimu, maji, kilimo, miundombinu, n.k. Tunawashukuru sana.
Nimefurahi katika hafla hii, tunaye Balozi wa China nchini, Mheshimiwa Wang Ke. Tunakuomba Mheshimiwa Balozi utufikishie shukrani zetu kwa Mheshimiwa Rais Xi Jinping, Serikali pamoja na wananchi wa China. Maktaba hii itatumika kwa miaka mingi ijayo. Hivyo basi, tunawashukuru sana; na napenda niahidi kuwa tutaendelea kushirikiana nanyi kwa karibu; na msaada mtakayotupatia, tutaitumia vizuri.
Ndugu Wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu;
Mabibi na Mabwana;
Maktaba ni nyumba ya maarifa; na ni taasisi muhimu sana kwa maendeleo ya sekta ya elimu. Maktaba inatoa mazingira mazuri na tulivu kwa watu kujisomea. Lakini, zaidi ya hapo, Maktaba inamwezesha mtu wa kipato chochote kusoma ama kuazima vitabu, ambavyo aghalabu, isingekuwa rahisi kuvipata kwa sababu ya bei. Hivyo, narudia tena kukipongeza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kupata Maktaba hii kubwa na ya kisasa. Nina imani Maktaba hii itasaidia kuboresha kiwango cha elimu inayotolewa katika Chuo hiki. Na katika hili, napenda kutoa wito kwa uongozi wa Chuo, kuendelea kusimamia ubora wa elimu. Baadhi ya changamoto ambazo zimeanza kusikika, hakikisheni mzishughulikia. Kama nilivyosema, Chuo hiki ni kikongwe na kinategemewa na Watanzania.
Ndugu Wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Moja ya vipaumbele vikubwa vya Serikali ya Awamu ya Tano ni kuimarisha na kuboresha sekta ya elimu nchini, kuanzia elimumsingi hadi vyuo vikuu. Tangu tumeingia madarakani tumechukua hatua mbalimbali kufikia azma hiyo. Kwa mfano, mbali na msaada huu kutoka China, kwenye Chuo hiki tumejenga majengo 20 ya hosteli yenye uwezo wa kubeba wanachuo 3,840, na hivyo kupunguza tatizo la makazi kwa wanafunzi.
Aidha, katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine kilichopo Morogoro, tumetoa shilingi bilioni 2 kwa ajili ya kujenga maabara kubwa (Multi-purpose Laboratory). Tuliwapatia pia shilingi milioni 700 za kujenga Mgahawa (Cafeteria) itakayochukua wanafunzi 400 kwa mpigo, na shilingi bilioni 2 nyingine za ujenzi wa hosteli zitakazochukua wanachuo 700.
Kwenye Chuo Kikuu cha Mzumbe, tunajenga hosteli itakayochukua wanachuo 1,000 kwa gharama ya shilingi bilioni 6.5 na pia tumetoa kiasi cha shilingi bilioni 2.84 kwa ajili ya kujenga Maktaba na Hosteli kwenye Kampasi yake ya Mbeya. Ujenzi na ukarabati wa miundombinu mingine (nyumba, maabara, kumbi za mihadhara, n.k.) inaendelea kwenye vyuo vikuu vya umma kwa gharama ya shilingi bilioni 18. Kwa upande wa elimumsingi, tumejenga na kukarabati miundombinu ya shule za msingi na sekondari 551 kwa gharama ya shilingi bilioni 84.7.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Mbali na kujenga miundombinu, tumepanua wigo na kuchukua hatua za kuboresha na kuimarisha elimu yetu. Nyote mnafahamu, hivi sasa tunatoa elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo kila mwezi tunatenga kiasi cha shilingi 23.8 kugharamia. Tumeongeza idadi ya wanafunzi wanaopata mikopo ya elimu ya juu kutoka 98,000 hadi kufikia 124,000 hivi sasa. Hii imewezekana baada ya Serikali kuongeza bajeti ya mikopo kutoka shilingi bilioni 348 mwaka 2014/2015 hadi kufikia shilingi bilioni 427 mwaka huu.
Nitumie fursa hii pia kuipongeza Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwa kutoa mikopo kwa wakati; japo mwaka huu nimesikia kuna ucheleweshaji kidogo. Baadhi ya wanafunzi hawajapata mikopo yao mpaka sasa. Wizara ya Fedha na Bodi ya Mikopo hakikisheni mnashughulikia suala hilo haraka. Lakini napenda kuipongeza pia Bodi kwa kuanza kusimamia vizuri suala la urejeshaji wa mikopo iliyotolewa. Mwaka 2015/2016 walikusanya shilingi bilioni 21.74 lakini mwaka jana (2017/2018) walikusanya shilingi bilioni 181.49. Hongereni sana.
Sambamba na hayo, Serikali imesambaza vifaa vya maabara vyenye thamani ya shiligi bilioni 16.9 kwenye shule za sekondari 1,696 pamoja na vifaa vya kufundishia kwenye shule za mahitaji maalum. Vilevile, tumenunua pikipiki 2,894 na magari 45 kwa ajili ya kuwezesha ukaguzi wa mara kwa mara. Tunafanya haya yote kwa ajili ya kuhakikisha elimu yetu inaendelea kuwa bora.
Waheshimiwa Viongozi mliopo;
Ndugu Wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kuzidua Maktaba. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, napenda nitoe wito kwa wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu kuhakikisha kwanza mnaitunza Maktaba hii ili iweze kutumika kwa muda mrefu. Kitunze kidumu. Aidha, hakikisheni Maktaba hii inakuwa na vitabu vya kutosha. Maktaba ni vitabu; sio jengo peke yake. Na katika hili, nawakumbusha waandishi na wachipishaji vitabu kote nchini kuhakikisha wanatekeleza Sheria inayowataka kupeleka nakala mbili za kila Chapisho wanaloandaa kwenye Maktaba Kuu pamoja na Maktaba ya Chuo Kikuu.
Pili, natoa wito kwa Bodi ya Huduma za Maktaba, taasisi za umma na binafsi, pamoja na Watanzania kwa ujumla kuhakikisha tunakuwa na maktaba nyingi kwenye maeneo yetu, ikiwemo majumbani, ili kuwajengea watoto wetu utamaduni wa kujisomea. Tafiti nyingi zinaonesha kuwa Watanzania wengi hawapendi kusoma vitabu.
Tatu, kama mlivyosikia, katika Mradi huu, mbali na Jengo la Maktaba, lipo jengo la kufundisha lugha ya Kichina. Nawasihi Watanzania wenzangu kuchangamkia fursa ya kujifunza lugha ya Kichina. Yapo manufaa mengi sana ya kujifunza lugha ya kichina kwa sasa. China ni Taifa kubwa lenye idadi ya watu takriban bilioni 1.3. Ni la pili kiuchumi duniani na pia limepiga hatua kubwa kwenye masuala ya sayansi na teknolojia. Hivyo, kujifunza Kichina kuna manufaa mengi. Mathalan, kwa taarifa nilizonazo, kila mwaka, watalii milioni 130 kutoka China hutembelea sehemu mbalimbali duniani. Nchi yetu hivi sasa imejipanga kuongeza idadi ya watalii kutoka China, hususan kwa kuanzisha safari za ndege za moja kwa moja kutoka China kuja hapa nchini. Hivyo basi, ni wazi kuwa watu wanaofahamu lugha ya kichina watahitajika zaidi ili kuwahudumia watalii kutoka China; na hasa kwa kuwa, Wachina wengi wanajua kichina pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu;
Mheshimiwa Balozi wa China;
Waheshimiwa Viongozi wengine mliopo;
Ndugu Wana-Jumuiya wa Chuo Kikuu;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kuushukuru uongozi wa Wizara ya Elimu pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kunikaribisha. Naahidi kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na Chuo hiki pamoja na vyuo vingine nchini. Natambua kuwa Chuo hiki kinakabiliwa na baadhi ya changamoto. Tutaendelea kuzishughulikia. Kama mlivyosikia kutoka kwa wanafunzi wa zamani, Chuo hiki kimetoka mbali hadi kufikia hapa. Hivyo basi, hata changamoto zenu za sasa nazo zitashughulikiwa. Na katika hilo, naahidi kuanza kushughulikia barabara zenu za hapa. Naiagiza TARURA kuziingiza kwenye Mpango wa Kuboresha Barabara za Jiji la Dar es Salaam.
Napenda kurudia tena kuwashukuru marafiki zetu wa China kwa kuendelea kutuunga mkono kwenye masuala mbalimbali. Tunawashukuru pia kwa kukubali kutujengea Chuo cha VETA kule Kagera, kutoa mafunzo ya watumishi wa Maktaba hii, pamoja na misaada mingine mingi mnayotupatia. Tunashukuru pia Waheshimiwa Mabalozi mliopo. Tunaahidi kuendelea kushirikiana na Mataifa pamoja na taasisi zenu kwa manufaa yetu wote.
Mwisho lakini sio kwa umuhimu, napenda nimshukuru na kumpongeza Waziri Mkuu Mstaafu, Mheshimiwa Lowasa, ambaye alikuwa mpinzani wangu kwenye kinyang’anyiro cha Urais mwaka 2015, kwa kujumuika nasi katika tukio hili. Ameonesha ukomavu mkubwa, ambao wanasiasa wengine wa nchi hii hawana budi kujifunza. Siasa sio uadui au uhasama.
Mungu Ibariki Maktaba hii!
Mungu Kibariki Chuo Kikuu cha Dar es Salaam!
Mungu Ubariki Uhusiano wa Tanzania na China!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni kwa kunisikiliza”

- Sep 27, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA YA UZINDUZI WA DARAJA LA JUU (FLYOVER) KATIKA MAKUTANO YA...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE HAFLA
YA UZINDUZI WA DARAJA LA JUU (FLYOVER) KATIKA MAKUTANO YA BARABARA ZA MANDELA NA NYERERE
ENEO LA TAZARA, TAREHE 27 SEPTEMBA, 2018
Mheshimiwa Elias Kwandikwa, Naibu Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Mheshimiwa Paul Makonda,
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Masaharu Yoshida,
Balozi wa Japan nchini;
Mheshimiwa Bashiru Ally,
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi;
Mheshimiwa Mama Kate Kamba,
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Selemani Kakoso, Mwenyekiti
wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu;
Waheshimiwa Wabunge wengine mliopo;
Mwakilishi wa JICA nchini Tanzania;
Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama mliopo;
Ndugu Viongozi wengine na Wafanyakazi wa Wizara
ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano;
Viongozi wa Vyama vya Siasa na Dini mliopo;
Waheshimiwa Wageni Wote Waalikwa;
Ndugu Wana-Dar es Salaam;
Mabibi na Mabwana:
Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa. Lakini, kama mjuavyo, wiki iliyopita, Taifa letu lilipatwa na simanzi kubwa kufuatia ajali ya kuzama kwa Kivuko cha Mv. Nyerere iliyosababisha vifo vya Watanzania wenzetu takriban 230. Kwa heshima ya marehemu hao, naomba sote tusimame ili tuweze kuwakumbuka kwa dakika moja. Roho za marehemu wetu zipumzike mahali pema peponi. Amina. Napenda, kwa mara nyingine tena, kutoa pole nyingi kwa familia zilizopoteza wapendwa wao. Aidha, nawaombea majeruhi wote wapone haraka.
Nawashukuru pia marafiki zetu kutoka nchi mbalimbali ambao wametutumia salamu za rambirambi na pole kufuatia ajali iliyotokea. Salamu zao, kwa hakika, zimetufariji sana. Tunawashukuru. Lakini, kwa namna ya pekee kabisa, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Watanzania wote kwa mshikamano mkubwa mlioonesha tangu kutokea kwa ajali hiyo mpaka sasa. Hongereni sana. Natambua kuwa wengi wetu bado tupo kwenye huzuni na simanzi kubwa; hata hivyo, hatuna budi kuendelea na kazi ya kulijenga Taifa letu. Hivyo ndivyo, hata Vitabu vyetu Vitakatifu vinatufundisha.
Lakini napenda kutumia fursa hii kutoa wito kwa Watanzania wenzangu, tutumie ajali iliyotokea kujitafakari kwa kina kwa lengo la kujifunza. Kila mmoja wetu ajitafakari. Viongozi wenye dhamana ya kusimamia vyombo vya usafiri watafakari na kujifunza. Watendaji wanaosimamia usafiri pia watafakari. Na halikadhalika, wananchi ambao ndio watumiaji wakubwa wa vyombo vya usafiri nao wanapaswa kujitafakari. Nina imani kuwa, kama sote tutatafakari vizuri na kuweza kujifunza, ajali kama hizi zitaepukika; na endapo zitatokea, basi madhara yake hayatakuwa makubwa sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Tupo hapa kushuhudia Uzinduzi wa Daraja la Juu (flyover) hapa TAZARA. Napenda kumshukuru Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Kamwelwe, kwa kunialika kushuhudia tukio hili la maendeleo na historia kwa nchi yetu. Hii ni “flyover” ya kwanza kabisa kujengwa hapa nchini. Hivyo basi, nasema “ahsante sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi kwa kunialika”.
Mtakumbuka kuwa takriban miezi 29 iliyopita, tarehe 16 Aprili 2016 nilikuja hapa kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Daraja hili la Juu. Leo nimekuja tena hapa kwa ajili ya kulizindua. Kwa hakika, nimefurahi sana. Kama mjuavyo, Daraja hili ni moja ya ahadi za CCM kwenye Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015. Hivyo, kukamilika kwake, ni uthibitisho kuwa CCM ikiahidi jambo, inalitekeleza. Nimefurahi sana kuona kwenye Hafla hii wenye Ilani yao pia wapo. Hongereni sana Wana-CCM kwa kuweza kutimiza ahadi hii.
Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana;
Kama walivyosema walionitangulia kuzungumza, Daraja hili, mbali na kurahisisha usafiri na kupunguza kero ya foleni barabarani, litasaidia kuzuia upotevu mkubwa wa fedha. Utafiti uliofanyika mwaka 2013, ulibainisha kuwa nchi yetu ilikuwa ikipoteza takriban shilingi bilioni 400 kwa mwaka kwa sababu ya msongamano wa magari barabarai. Zaidi ya hapo, Daraja hili litapendezesha mandhari ya Jiji la Dar es Salaam, ambalo ni miongoni mwa Majiji yanayokua kwa kasi Barani Afrika.
Hivyo basi, nitumie fursa hii kumpongeza Mkandarasi, Kampuni ya Sumitomo Mitsui Construction ya Japan iliyoshirikiana na Kampuni ya Mak Contractor ya Tanzania kwa kukamilisha mradi huu mapema. Daraja hili lilipangwa kukamilika tarehe 30 Oktoba 2018. Lakini, limekamilika mapema mwezi huu (Septemba). Hongera sana Wakandarasi pamoja na Wahandisi Washauri, Kampuni ya The Consortium of Oriental Consultants Global Ltd na Eight – Japan Engineering Consultants Inc. ya Japan.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda pia kutumia fursa hii kuishukuru Serikali ya Japan kwa kutuunga mkono katika kutekeleza mradi huu. Daraja hili limegharimu takriban shilingi bilioni 106.965. Sehemu kubwa ya fedha hizo zimetolewa na marafiki zetu wa Japan; na kiasi kingine kimechangiwa na Serikali yetu. Tunawashukuru sana marafiki zetu hawa wa Japan. Na niseme tu kwamba, Japan ni marafiki zetu wa kweli na tena wa muda mrefu. Tumeshirikiana nao katika kutekeleza miradi mingi ya maendeleo: kwenye sekta za miundombinu ya usafiri na nishati ya umeme; elimu; afya; kilimo; maji; ujenzi; n.k. Tunawashukuru sana. Nimefurahi kumwona Balozi wa Japan nchini, Mheshimiwa Yoshida, yupo hapa. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Balozi kwa kuja kuungana nasi katika tukio hili. Tunakuomba utufikishie shukrani zetu nyingi kwa Waziri Mkuu, Serikali pamoja na wananchi wa Japan.
Natambua kuwa siku chache zijazo utarejea nyumbani baada ya kumaliza muda wako hapa nchini. Tunaomba ukaendelee kuwa Balozi wetu. Na katika hili, nikuombe sana Mheshimiwa Balozi utusaidie kuikumbusha Serikali yako kuhusu ahadi iliyotoa ya kutusaidia kujenga Barabara ya Morocco – Mwenge; Daraja la Juu pale eneo la Gerezani pamoja na Barabara za Mzunguko (Ring – Roads) kule Dodoma. Watanzania tunasubiri kwa hamu kuona utekelezaji wa miradi hiyo.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda pia kutumia fursa hii kuipongeza Wizara ya Ujenzi pamoja na TANROADS kwa kusimamia vizuri utekelezaji wa Mradi huu. Nampongeza Prof. Mbarawa, ambaye wakati ujenzi wa Daraja hili unaanza, alikuwa Waziri wa Ujenzi. Lakini, kwa namna ya pekee kabisa, nampongeze Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Patrick Mfugale ambaye ameshiriki kikamilifu katika kubuni, kuandaa mchoro na kusimamia kwa karibu utekelezaji wa Daraja hili. Hongera sana Mhandisi Mfugale na wote ulioshirikiana nao.
Mengi tayari yameelezwa kumhusu Mhandisi Mfugale. Binafsi namfahamu sana. Nimefanya naye kazi kwa karibu wakati nikiwa Waziri wa Ujenzi. Najua uchapa kazi wake, uzalendo alionao, pamoja na uaminifu na ubunifu. Mbali na Daraja hili la Juu, ameshiriki pia katika kubuni michoro ya madaraja mengine makubwa nchini, ikiwa ni pamoja na Daraja ya Mkapa, Umoja, Kikwete, Magufuli kule Kilombero, n.k. Lakini zaidi ya sifa hizo zilizotajwa, Mhandisi Mfugale pia ni mtu muadilifu sana. Na kutokana na uadilifu wake, kuna wakati alikaribia kufukuzwa kazi.
Ni kwa kutambua na kuthamini mchango wake, nilipendekeza na nafurahi Wizara ilinikubali, kuliita Daraja hili la Juu hapa Tazara jina la Mhandisi Mfugale. Hivyo, kuanzia sasa hapa pataitwa Mfugale Flyover. Ni matumaini yangu kuwa hatua hii itatoa hamasa kwa Watanzania wengine kufanya kazi kwa kujituma, uadilifu na kuweka maslahi ya Taifa mbele. Na napenda kutumia fursa kuwasihi sana Watanzania, hususan wataalam wetu, kuiga mfano wa Mhandisi Mfugale. Wapo baadhi ya wataalam wetu sio wazalendo. Wanakubali kutumika katika kukwamisha maendeleo ya nchi yetu. Hii ni aibu kubwa sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Ujenzi wa Daraja hili la Juu ni moja ya mikakati mingi inayotekelezwa na Serikali ya kutatua tatizo la msongamano wa magari na kuliboresha Jiji letu la Dar es Salaam. Kama mnavyokumbuka, mwaka Juzi (2016) tulizindua Daraja la Nyerere (Kigamboni) na Mradi wa Magari ya Mwendokasi (BRT). Mwaka jana tuliweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Daraja la Pete/Mpishano (interchange) pale Ubungo, ambalo ujenzi wake unaendelea. Mwaka huu pia tumeanza ujenzi wa barabara ya njia sita kutoka Kimara Mwisho hadi Kiluvya na pia Ujenzi wa Daraja la Salender. Aidha, ujenzi wa Miundombinu ya Mabasi ya Mwendokasi Awamu ya Pili kutoka maeneo ya Kariakoo kwenda Mbagala unatarajiwa kuanza Mwaka huu wa Fedha; pamoja na Madaraja mengine ya Juu katika maeneo ya Chag’ombe, Uhasibu na Magomeni. Na kama mnavyofahamu, upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam pamoja na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere nao unaendelea.
Zaidi ya hapo, kupitia Mradi wa Uendelezaji wa Jiji la Dar es Salaam (Dar es salaam Metropolitan Development Project - DMDP), Serikali imeanza ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 210 katika Wilaya zote za Jiji la Dar es Salaam. Ninyi wananchi ni mashahidi, hivi sasa kuna barabara nyingi zinajengwa kwenye mitaa yetu. Na Mradi huu wa DMDP utahusisha pia ujenzi wa mifereji ya kuzuia mafuriko yenye urefu wa kilometa 40 (ikiwemo katika Bonde la Mto Msimbazi); kujenga masoko na stendi, mifumo ya maji taka, n.k. Miradi hii inatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 660. Nina imani kuwa miradi hii yote itakapokamilika, Jiji la Dar es Salaam litazidi kupendeza na kuwa la kisasa zaidi. Lakini, katika kuongeza ufanisi kwenye utadaji kazi, napenda kuiagiza TAMISEMI kuuhamishia TARURA Mradi huu wa DMDP.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda nihitimishe hotuba yangu kwa kurudia tena kuwashukuru na kuwapongeza wote walioshiriki katika ujenzi wa Daraja hili. Naishukuru Serikali ya Japan. Nawapongeza Wakandarasi na Wahandisi Washauri wa Mradi. Naipongeza Wizara ya Ujenzi. Naipongeza TANROADS, hususan Mtendaji wake Mkuu, Mhandisi Mfugale. Na mwisho lakini sio kwa umuhimu, nawapongeza Watanzania wote kwa kufanikisha ujenzi wa mradi huu.
Wito wangu kwa viongozi, watendaji na wananchi, tulitunze Daraja hili. Na katika hili, naiagiza Wizara kuhakikisha inafunga kamera kwenye daraja hili na kwenye miundombinu mingine ya namna hii tuliyoijenga ili kudhibiti vitendo vya uharibifu wa miundombinu yetu.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la Kuzindua Daraja hili la Mfugale hapa TAZARA.
Mungu Libariki Daraja hili!
Mungu Wabariki Wana-Dar es Salaam!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”

- Jul 23, 2018
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUPOKEA GAWIO KUTOKA KAMPUNI, TAASISI NA MASHIRIKA MBALIMBALI...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHE. DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUPOKEA GAWIO KUTOKA KAMPUNI, TAASISI NA MASHIRIKA MBALIMBALI
DAR ES SALAAM, TAREHE 23 JULAI, 2018
Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango,
Waziri wa Fedha na Mipango;
Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wengine mliopo;
Mheshimiwa Mhandisi Evarist Ndikilo,
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam;
Mheshimiwa Kate Kamba, Mwenyekiti wa CCM,
Mkoa wa Dar es Salaam;
Waheshimiwa Wenyeviti wa Kamati za Bunge za Uwekezaji na Mitaji ya Umma; Hesabu za Serikali; pamoja na Bajeti;
Waheshimiwa Wabunge wengine mliopo;
Ndugu Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu mliopo;
Waheshimiwa Mabalozi mliopo
Waheshimiwa Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama;
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa
pamoja na Dini mliopo;
Ndugu Athumani Mbuttuka, Msajili wa Hazina;
Wenyeviti wa Bodi, Watendaji Wakuu pamoja na Watumishi wa Taasisi, Makampuni na Mashirika mbalimbali mliopo;
Wageni wote Waalikwa, Mabibi na Mabwana:
Napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa uzima na kutuwezesha tukutane hapa. Aidha, namshukuru Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Philip Mpango, kwa kunialika kwenye tukio hili la kupokea gawio la shilingi bilioni 717.56 kutoka kwenye taasisi, makampuni na mashirika yapatayo 40, ambayo Serikali ina hisa ama inayamiliki kwa asilimia mia moja. Kwa hakika, hili ni tukio muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu; hivyo basi, napenda kurudia tena kukushuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kunialika.
Napenda pia kutumia fursa hii, hapa mwanzoni kabisa, kutoa shukrani na pongezi zangu nyingi kwa Wenyeviti wa Bodi, Watendaji Wakuu pamoja Watumishi wote wa Taasisi pamoja na Makampuni yote, ambayo leo yanakabidhi gawio kwa Serikali. Gawio hili litaiwezesha Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo na pia kuboresha huduma mbalimbali za jamii. Hivyo basi, tunawashukuru na hongereni sana.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Duniani kote, Serikali zina njia kuu mbili za kupata mapato yake. Njia ya kwanza ni kupitia makusanyo ya kodi. Wamerekani wana usemi usemao, “Nothing is certain but death and taxes (maanake ni kwamba, kuna mambo mawili tu ambayo ni hakika au ya lazima duniani, kifo na kodi)”. Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, naye aliwahi kusema, nanukuu “Serikali isiyokusanya kodi ni Serikali ya wala rushwa”, mwisho wa kunukuu.
Hii inaonesha kuwa, kodi ni chanzo muhimu cha kukusanya mapato ya Serikali. Na ninafurahi kuona kuwa, katika miaka ya hivi karibuni, licha ya kwamba bado hatujaweza kufikia malengo yetu kwa asilimia 100, Serikali imejitahidi sana kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya kodi. Mathalan, wakati Serikali ya Awamu ya Tano ikiingia madarakani, mwaka 2015, wastani wa makusanyo ya kodi kwa mwezi ulikuwa shilingi bilioni 850. Hivi sasa wastani kwa mwezi ni shilingi trilioni 1.3, ongezeko la takriban asilimia 65. Mapato kwa mwaka pia yamekuwa yakiongezeka. Katika mwaka wa Fedha 2016/2017 tulikusanya shilingi trilioni 14.4, lakini kwenye Mwaka wa Fedha uliopita (2017/2018), tumekusanya shilingi trilioni 15.5.
Kwa tathmini yangu binafsi, ongezeko hili limetokana na mambo makubwa mawili. Kwanza, hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kuziba mianya ya ukwepaji kodi. Pili, wananchi wengi kuhamasika kulipa kodi na hasa baada ya kuona kodi zao zinatumika vizuri. Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuipongeza Mamalaka ya Mapato (TRA) kwa kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya kodi. Waswahili husema “mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni”. Licha ya changamato ambazo bado zipo, lakini wamejitahidi. Hongereni TRA.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nitumie fursa hii pia kuwapongeza Watanzania wote kwa kuhamasika kulipa kodi. Endeleeni na moyo huo huo. Kodi zenu ndizo zinaiwezesha Serikali kutekeleza miradi ya miundombinu (ujenzi wa reli, barabara, bandari, viwanja vya ndege, utekelezaji wa miradi ya umeme, n.k.). Mathalan, kabla ya kuja hapa, nimetoka kushuhudia uwekaji saini Mkataba wa Ujenzi wa Daraja la Salender. Daraja hili, ambalo litapita kwenye Bahari, litajengwa kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 250 ambazo ni mkopo wa masharti nafuu kutoka Korea Kusini, na ambazo baadaye tutazilipa kupitia kodi zenu.
Zaidi ya hapo, kodi tunazokusanya kutoka kwa wananchi ndizo zinaiwezesha Serikali kuboresha huduma mbalimbali za jamii kama vile afya, elimu na maji. Hivyo basi, narudia tena kuwasihi Watanzania wenzangu kuendelea kulipa kodi ili kuiwezesha Serikali kutekeleza shughuli za maendeleo.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Ukiachilia mbali mapato ya kodi, njia ya pili inayoiwezesha Serikali kupata mapato, ni kupitia vyanzo visivyo vya kodi. Kuna vyanzo vingi visivyo vya kodi, lakini kimojawapo ni kupokea gawio kutoka kwenye taasisi au mashirika ambayo Serikali imefanya uwekezaji. Mathalan, hivi punde tumesikia kuwa Serikali yetu imewekeza kiasi cha shilingi trilioni 49.05 kwenye taasisi na makampuni mbalimbali. Na kama mtakavyokumbuka, wakati nikipokea gawio la TTCL, nilisema kuwa tunayo mashirika zaidi ya 90 yenye kustahili kutoa gawio kwa Serikali.
Lakini, licha ya idadi hiyo kubwa ya taasisi pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanyika, niwe mkweli, nchi yetu bado haijanufaika na uwekezaji ilioufanya. Gawio tunalopata ni dogo sana na mashirika mengi bado hayatoi gawio kwa Serikali. Mathalan, mwaka 2014/2015 tulipata gawio la shilingi bilioni 130.686 kutoka mashirika 24 tu. Mwaka 2015/2016 mashirika 25 yalitoa gawio la shilingi bilioni 249.3.
Hali hii haikuturidhisha. Kama mjuavyo, huwezi kuendesha nchi kwa kutegemea mapato ya kodi peke yake. Na baada ya kufanya utafiti, tuligundua mambo kadhaa yanayofanya taasisi na mashirika yetu yasitoe ama yatoe gawio dogo. Baadhi ya mambo hayo ni: uongozi mbovu; kutokuwepo kwa ufuatiliaji madhubuti, hususan kwenye mashirika ambayo Serikali ina hisa; udanganyifu; ubadhirifu; rushwa; n.k. Baada ya kugundua hayo, tulianza kuchukua hatua. Na ninafurahi kuona kuwa, hatua zetu zimeanza kuzaa matunda. Kama mlivyosikia, leo tunapokea gawio la shilingi bilioni 717.56. Haya ni mafanikio makubwa sana.
Hivyo basi, napenda kurudia tena kuwapongeza Wenyeviti wa Bodi, Watendaji Wakuu, Watumishi, Wasimamaizi pamoja na watu wote waliofanikisha Makampuni haya yote kutoa gawio kwa Serikali kwa Mwaka wa Fedha wa 2017/2018. Kwa namna ya pekee kabisa, napenda kuzitambua taasisi tatu zilizotajwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ambazo zimevuka malengo ya kutoa gawio kwa Mwaka wa Fedha uliopita. Hongereni sana. Binafsi nimefurahishwa zaidi na Shirika kama la TAZAMA, ambalo halikuwahi kutoa gawio, lakini leo limetoa. Hongereni sana. Ni matumaini yangu kuwa, katika Mwaka huu wa Fedha tuliouanza, makampuni na mashirika mengi yatatoa gawio kwa Serikali.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Hatukuja hapa kusikiliza hotuba. Tumekuja hapa kupokea fedha. Na kama mjuavyo, kwenye masuala ya fedha, huwa hakuna maneno mengi. Hata hivyo, kabla sijahitimisha hotuba yangu, naomba mniruhusu niseme masuala machache ya mwisho.
Suala la kwanza, napenda kurudia tena agizo langu kwa Msajili wa Hazina kuhakikisha mashirika na taasisi zote zenye kustahili kutoa gawio kwa Serikali zinafanya hivyo. Ni kweli, katika miaka hii miwili, gawio kwa Serikali kutoka kwenye taasisi na mashirika limeongezeka. Hata hivyo, kiasi kinachopatikana bado ni kidogo sana ukilingaisha na uwekezaji uliofanyika. Kama nilivyosema, tumewekeza zaidi ya shilingi trilioni 49. Haiwezekani tupate gawio la shilingi bilioni 717 tu kwa mwaka. Hivyo basi, Msajili wa Hazina hakikisha mashirika yote yanatoa gawio. Yatakayoshindwa, uongozi wake ubadilishwe ama mashirika hayo yafutwe kabisa.
Suala la pili, ambalo nitalieleza kwa kirefu kidogo, ni kuhusu ushirikiano kati ya sekta binafsi na Serikali, na hasa kwenye masuala ya uwazi katika biashara. Napenda nisisitize kuwa Serikali inatambua mchango wa sekta binafsi katika kuchangia maendeleo ya taifa letu. Na naahidi kuwa Serikali itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa sekta binafsi ya hapa nchini. Lakini, pamoja na ahadi hiyo, napenda niwe mkweli. Baadhi ya washirika wetu kutoka sekta binafsi sio waaminifu na wana tabia ya kufanya udanganyifu. Napenda nitoe mifano michache.
Mabibi na Mabwana;
Kama mjuavyo, baadhi ya kampuni au mashirika yanayofanya kazi hapa nchini yana kampuni zake tanzu au mama nje ya nchi. Hili kimsingi halina ubaya. Ubaya unakuja pale ambapo kampuni hizo tanzu au kampuni mama; zinapotumika kufanya udanganyifu wa kukwepa kodi, tozo, malipo ya mrahaba pamoja na gawio. Na udanganyifu huo mara nyingi hufanyika kwa kuongeza gharama za uendeshaji ili kupunguza kiwango cha faida ambacho kampuni zilizopo hapa nchini zinapata; ama zinaonekane zinapata hasara. Ujanja huu kwa kitaalamu unaitwa transfer pricing.
Mbinu mojawapo inayotumika ni katika ununuzi wa mitambo na vipuri. Ili kupandisha gharama za uendeshaji, kampuni za hapa nchini huagiza vifaa hivyo kupitia kampuni tanzu au mama zilizopo nje ili Serikali isifahamu gharama halisi. Kampuni hizo tanzu zikishanunua vifaa hivyo huviuza kwa kampuni za hapa nchini kwa bei ya juu; wakati mwingine mara tano zaidi ya bei halisi. Na kwa vile sheria zetu za kodi na uwekezaji zinatoa misamaha ya kodi, gharama hizi za kununua vifaa zinaendelea kukatwa katika mapato ya kampuni hizo miaka nenda miaka rudi; na hivyo kuzifanya kampuni hizo zisilipe kabisa ama zilipe kiwango kidogo sana cha kodi na tozo mbalimbali.
Njia nyingine inayotumika ni kupitia mikopo. Kampuni za hapa nchini huchukua mikopo kwa riba kubwa kutoka kwenye kampuni zao tanzu au mama zilizopo nje ya nchi. Hii inaongeza gharama za uendeshaji na kuzifanya kampuni za hapa nchini kila wakati zionekane zinajiendesha kwa hasara na hivyo kuzifanya zisilipe kodi. Lakini, cha kushangaza ni kwamba, licha ya kupata hasara, makampuni hayo yanaendelea kufanya kazi.
Mbinu nyingine inayotumika na makampuni kukwepa kutoa gawio au kulipa kodi na tozo mbalimbali, ni kupitia gharama za usimamizi (yaani management fee). Kampuni hizi hulipa menejimenti zao gharama kubwa; na wakati mwingine huajiri kampuni nyingine kuzisimamia kampuni zao. Hii inapandisha gharama za uendeshaji na kuzifanya kampuni husika zionekane zinapata hasara kila kukicha na hivyo zishindwe kulipa kodi na tozo nyingine.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Mambo haya yote kwa ujumla wake sio tu yanapunguza mapato kwa Serikali, bali pia yanasababisha kuwepo kwa hali ya kutoaminiana kati ya Serikali na Sekta Binafsi. Hivyo basi, nitumie fursa hii kuisihi sana sekta binafsi ya hapa nchini kushirikiana kwa karibu na Serikali. Fanyeni biashara zenu kwa uwazi. Acheni usiri. Kama unaendesha shughuli zako kihalali, kwanini ufichefiche?
Mathalan, nimearifiwa kuwa ipo kampuni moja ya madini ilikataa ombi la Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali la kwenda kuangalia mahesabu ili kujiridhisha kama kodi iliyolipwa TRA ni sahihi. Nimeambiwa kuwa Kampuni hiyo imekataa kwa kisingizio kuwa yenyewe ni kampuni binafsi. Wasichofahamu ni kwamba, Sheria ya Ukaguzi wa Umma inaipa Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali mamlaka ya kupata taarifa kutoka mtu au taasisi yoyote katika kutimiza majukumu yake ya ukaguzi katika Serikali.
Hivyo basi, nirudie tena wito wangu kwa sekta binafsi kutoa ushirikiano kwa Serikali. Sambamba na hilo, natoa wito kwa taasisi zote za Serikali zenye dhamana ya kusimamia uwajibikaji na kufuatilia shughuli za uwekezaji katika maeneo mbalimbali (madini, gesi, uvuvi wa bahari kuu, uzalishaji, kampuni za simu pamoja na taasisi za fedha) kuhakikisha zinatekeleza majukumu yake ipasavyo. Wakati mwingine “tunaliwa” kwa sababu ya uzembe wa watendaji wa Serikali. Hivyo basi, niziagiza mamlaka zote (TR, TIC, EPZA, CAG, TRA, BOT, n.k.) kutekeleza majukumu yenu.
Mathalan, natarajia kuwa, kuanzia sasa, Benki Kuu itahakikisha mikopo yote inayochukuliwa na kampuni za hapa nchini kutoka nje inasajiliwa kwa mujibu wa sheria. Aidha, natarajia, TRA itakuwa ikifanya ukaguzi wa mara kwa mara kwa biashara na mialama inayofanyika baina ya kampuni zenye mahusiano, hususan kampuni zilizopo hapa nchini na kampuni mama au tazu zilizopo nje, ili kudhibiti uhamishaji wa mali au utoroshaji wa faida.
Suala la mwisho, ni kwa TRA tena. Awali, nimewapongeza kwa kuongeza ukusanyaji wa mapato. Lakini napenda niwapongeze pia kwa hatua zenu za hivi karibuni za kuanza kuwarasimisha watu kutoka sekta isiyo rasmi (machinga, mamalishe, n.k.) pamoja na kutoa msamaha wa riba na faini kwa wafanyabishara mliokuwa mkiwadai. Hizi ni hatua nzuri ambazo naamini zitapanua wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato kwa Serikali. Hongereni sana.
Hata hivyo, hampaswi kubweteka. Ni lazima muendelee kuboresha mifumo yenu ya ukusanyaji kodi, kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulipa kodi na pia kuhakikisha viwango vya kodi mnavyoweka vinalipika. Zaidi ya hapa, napenda niseme, na hapa napenda niwe muwazi, baadhi ya watumishi wa TRA sio waadilifu. Wanapokea rushwa na kunyanyasa walipa kodi. Na tabia hizi ndizo zimekuwa zikichafua taswira ya TRA pamoja na Serikali. Hivyo basi, natoa wito kwa Kamishna Mkuu wa TRA kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi wa namna hiyo. Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kusema, nanukuu, “uvundo wa yai moja bovu ni mkali zaidi kuliko harufu ya mayai mengi mazima”, mwisho wa kuukuu. Msiwaache watu wachache wawachafue.
Lakini, nimpongeze Kamishna Mkuu kwa hatua mbalimbali anazochukua. Mara nyingi namuona akitembelea Mikoa mbalimbali kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kulipa kodi. Ni matumaini yangu kuwa endapo maafisa wengine wataiga mfano wake, basi makusanyo ya kodi yatazidi kuimarika.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Napenda kuhitimisha kwa kurudia tena kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kunialika kwenye shughuli hii. Aidha, nayapongeza tena makampuni yote 43 yaliyotoa gawio kwa Serikali katika Mwaka wa Fedha ulioisha wa 2017/2018. Napenda pia kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kazi nzuri wanayofanya ya kuishauri Serikali katika kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo.
Nawashukuru pia Waheshimiwa Mabalozi kwa kushiriki nasi kwenye tukio hili. Tunawasihi muendelee kuwahimiza na kuwahamasisha wawekezaji waaminifu kwenye nchi zenu kuja kuwekeza hapa nchini. Mwisho kabisa lakini sio kwa umuhimu, navishukuru na kuvipongeza Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kusimamia amani na utulivu wa nchi yetu. Bila amani, hakuna kodi. Bila amani, hakuna gawio; na bila ya amani hakuna maendeleo. Hivyo basi, navipongeza vyombo vya ulinzi pamoja na Watanzania wote kwa ujumla kwa kuendelea kuitunza amani yetu.
Baada ya kusema hayo, sasa nipo tayari kutekeleza jukumu lililonileta la kupokea gawio kutoka taasisi mbalimbali.
Mungu Zibariki Taasisi Zilizotoa Gawio!
Mungu Ibariki Tanzaia!
“Ahsanteni sana kwa Kunisikiliza”

- Jul 17, 2018
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI WA CHAMA CHA MAPINDUZI KWENYE UFUNGUZI WA MKUTANO M...
Soma zaidiHotuba
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JOHN POMBE JOSEPH MAGUFULI, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI WA CHAMA CHA MAPINDUZI KWENYE
UFUNGUZI WA MKUTANO MAALUM WA MAJADILIANO
KATI YA CHAMA CHA KIKOMUNISTI CHA CHINA
NA VYAMA VYA SIASA VYA NCHI MBALIMBALI ZA AFRIKA
HOTELI YA SERENA, DAR ES SALAAM, TAREHE 17 JULAI, 2018
Waheshimiwa Viongozi wa Vyama vya Siasa kutoka
Nchi mbalimbali za Afrika mkiongozwa na Mwenyeji
wenu Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Bashiru Ally;
Mheshimiwa Song Tao, Waziri wa Masuala ya Uhusiano wa
Kimataifa wa Chama cha Kikomunisti cha China;
Waheshimiwa Viongozi wa Chama na Serikali mliopo;
Waheshimiwa Wazee Wetu Wastaafu mliopo;
Mheshimiwa Wang Ke, Balozi wa China nchini;
Waheshimiwa Mabalozi wengine mliopo;
Waheshimiwa Wageni Wote Waalikwa;
Mabibi na Mabwana:
Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa. Binafsi, najisikia heshima kubwa kuwepo mahali hapa na kupata fursa hii adimu ya Kufungua Mkutano huu Maalum wa Majadiliano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China na Vyama Siasa vya Afrika, unaofanyika kwa mara ya kwanza nje ya China hapa Dar es Salaam. Kwa niaba yangu binafsi, na kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Serikali pamoja na Watanzania wote, napenda niwakaribishe wageni wetu wote hapa nchini.
Nawakaribisha Viongozi wa Vyama vya Siasa kutoka nchi mbalimbali za Afrika, ambao nimearifiwa kuwa mnatoka kwenye nchi zaidi ya 40 za Afrika. Karibuni sana. Vilevile, na kwa namna ya pekee kabisa, napenda kuukaribisha nchini ujumbe kutoka Chama cha Kikomunisti cha China (the Communist Party of China – CPC), ukiongozwa na Mheshimiwa Song Tao, Waziri wa Masuala ya Mambo ya Nje wa CPC. Karibuni Tanzania. Karibuni sana Dar es Salaam.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Napenda pia, hapa mwanzoni kabisa, kutumia fursa hii kuishukuru CPC kwa kuichagua Afrika kuwa sehemu ya kwanza nje ya China kufanya Mkutano huu. Kama mjuavyo, Mkutano wa Kwanza wa namna hii ulifanyika Beijing, China, tarehe 30 Novemba hadi 3 Desemba, 2017 na uliikutanisha CPC na Vyama Vya Siasa kutoka sehemu mbalimbali duniani. Hivyo basi, tunaishukuru CPC kwa kuichagua Afrika kuwa sehemu ya kwanza nje ya China kufanya Mkutano huu.
Vilevile, naishukuru CPC pamoja na Vyama vyote shiriki kwa kuichagua na kuridhia Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano huu. Tunawashukuru sana. Tunaahidi kuwa tutajitahidi kutimiza majukumu yetu ili Mkutano huu uwe wenye mafanikio makubwa. Na napenda niseme kuwa, hamjakosea kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano huu. Tanzania ni mahali sahihi kabisa pa kufanyia Mkutano huu. Zipo sababu nyingi zenye kufanya Tanzania iwe sehemu sahihi; lakini kwa sababu ya muda nitataja mbili. Kwanza kabisa, kama mjuavyo, mwenyeji wa Mkutano huu ni Chama Cha Mapinduzi (CCM); na sote hapa tunafahamu kuwa CCM ni miongoni mwa vyama vikongwe Barani Afrika, ambacho kimedumu madarakani kwa muda mrefu. Na kama mnavyofahamu, moja ya mila na desturi za Waafrika ni kuheshimu wakubwa. Hivyo basi, ni wazi kuwa uamuzi wa kufanya Mkutano huu hapa Tanzania ulikuwa sahihi kabisa.
Pili, kama ambavyo sote tunakumbuka, wakati wa harakati za kupigania uhuru wa Bara la Afrika, Tanzania ilikuwa Makao Makuu ya Kamati ya Ukombozi ya Umoja wa Nchi Huru za Afrika (Organization of the African Unity – OAU). Kupitia Kamati hiyo, ambayo ilikuwa chini ya Uenyekiti wa Baba wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Tanzania ilikuwa kitovu cha harakati za Ukombozi wa Bara letu. Wapigania Uhuru kutoka nchi mbalimbali waliishi na kupata misaada mbalimbali, ikiwemo mafunzo na mbinu za mapambano, na hatimaye kufanikiwa kuzipatia nchi zao uhuru. Hivi sasa nchi za Afrika zipo kwenye harakati za kujikomboa kiuchumi na sisi Tanzania tumedhamiria kuongoza mapambano haya ya kiuchumi. Hivyo basi, ni sahihi kabisa Mkutano huu kufanyika hapa Tanzania. Napenda kurudia tena kuwashukuru kwa kuridhia Mkutano huu kufanyika hapa Tanzania. Na kama nilivyoahidi, tutajitahidi kuufanya Mkutano huu uwe wa mafanikio makubwa kwa ustawi na maendeleo ya pande zetu mbili.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Uhusiano na ushirikiano kati ya Afrika na China ni wa kihistoria na ni wa muda mrefu sana. Kwa mujibu wa Mwana Historia wa Uchina, Li Anshan, uhusiano kati ya Afrika na China ulianza takriban miaka 138 kabla ya Ujio wa Kristo, ambapo kulikuwa na uhusiano wa kibiashara kati ya tawala mbalimbali za China na Watawala wa Misri na maeneo mengine ya Afrika. Kadri miaka ilivyozidi kupita, uhusiano huo ulizidi kukua na kupanuka na hasa kuanzia karne ya 14. Upo ushahidi mwingi wa kihistoria na vitu vya kale unaoonesha kuwepo kwa uhusiano wa karibu kati ya China na Afrika. Ushahidi huu unapatikana kwenye maeneo mengi kule China; na pia kwenye maeneo mbalimbali ya Afrika, ikiwemo Cairo, Bandari ya Aizhabu kule Sudan, maeneo ya Kenya, Somalia na halikadhalika Zanzibar hapa nchini Tanzania.
Pamoja na uhusiano huo wa kihistoria, ni ukweli usiopingika kuwa ushirikiano wetu ulikua na kuimarika zaidi kufuatia Mapinduzi ya Mwaka 1949 nchini China; na baada ya nchi za Afrika kuanza kupata uhuru kwenye miaka ya 1950 na mwanzoni mwa miaka ya 1960. Nchi nyingi za Afrika zilizopata uhuru zilianzisha uhusiano na China. Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo, mara tu baada ya kupata uhuru, ilianzisha uhusiano na China.
Na napenda niseme kuwa, China ilitoa mchango mkubwa sana katika harakati za ukombozi Barani Afrika. Kama nilivyosema awali, Tanzania chini ya Mwalimu Julius Nyerere ilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ukombozi wa OAU. Hivyo, tunafahamu mchango wa China katika harakati za ukombozi wa Bara letu. Ndugu zetu hawa walitoa silaha na vifaa mbalimbali kwa wapigania uhuru. Halikadhalika, waliwapatia wapigania uhuru mafunzo ya kijeshi na pia kiitikadi. Na kwa wasiofahamu, ni hawa hawa marafiki zetu Wachina ndio waliojenga Reli kati ya Tanzania na Zambia yenye urefu wa zaidi ya kilometa 1,800, maarufu kama reli ya TAZARA, ambayo ilitoa mchango mkubwa sana katika harakati za ukombozi, hususan Kusini mwa Bara la Afrika. Na bila shaka, kwa kutambua mchango wa China kwenye harakati hizo za ukombozi, nchi nyingi za Afrika zilisimama pamoja na China katika kuhakikisha inapewa hadhi yake kwenye Umoja wa Mataifa.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Baada ya nchi nyingi za Afrika kupata uhuru, uhusiano na China ulizidi kupanuka; kwenye masuala ya ulinzi na usalama, biashara, uwekezaji, ujenzi wa miundombinu, kilimo, afya, elimu, sayansi na teknolojia, mazingira, utalii, habari, utamaduni, n.k. Na mwaka 2000, Afrika na China zilianzisha rasmi jukwaa la ushirikiano (China – Africa Forum). Jukwaa hili, ambalo mikutano yake hufanyika kila baada ya miaka mitatu kwa kubadilishana kati ya Afrika na China, limeweka misingi imara ya ushirikiano kati ya pande hizi mbili. Mkutano wa Saba wa Jukwaa unatarajiwa kufanyika Beijing, China, mwezi Septemba 2018.
Tangu Jukwaa hili limeanzishwa, mafanikio mengi makubwa yamepatikana katika nyanja mbalimbali. Mathalan, biashara kati ya Afrika na China imeongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 10 na hivi sasa inakadiriwa kufikia zaidi ya Dola za Marekani bilioni 250. Aidha, uwekezaji wa China Barani Afrika umeongezeka kutoka Dola za Marekani milioni 200 mwaka 2000 na kufikia zaidi ya Dola za Marekani bilioni 35 hivi sasa. Hii imeifanya China kuwa mshirika mkubwa wa kiuchumi wa Afrika. Vilevile, nchi za Afrika inashirikiana na China katika kutekeleza miradi ya miundombinu, hususan ya usafiri, umeme na maji. Halikadhalika, China wamekuwa wakitoa misaada mbalimbali kwa Afrika katika nyanja za afya, elimu, kilimo, sayansi na teknolojia, n.k. Maelfu ya Waafrika wamepata fursa za udhamini wa masomo nchini China. Na kama ambayo mmesikia hivi punde kutoka kwa Mheshimiwa Tao, China itatoa nafasi 4,000 za mafunzo kwa viongozi wa vyama vya siasa vya Afrika.
Zaidi ya hapo, China inashirikiana na Umoja wa Afrika katika kuimarisha amani na usalama Barani Afrika kwa kutoa fedha, mafunzo kwa walinda amani kutoka nchi za Kiafrika, wanatoa vifaa vya kijeshi na pia China inaongoza kwa kuwa na walinda amani wengi kwenye Bara letu. Kwa ujumla, naweza kusema kuwa ushirikiano kati ya China na Afrika kwa sasa umefikia kiwango cha juu sana. Na jambo la kufurahisha ni kwamba ushirikiano wetu umejengwa kwenye misingi ya kuelewana na kuheshimiana. Na hii ndio sababu misaada ya China kwetu imekuwa haiambatani na masharti yoyote. Na hili ndilo haswaa nchi za Afrika tunataka; ushirikiano ambao sote tunajiona tupo sawa na sote tunanufaika. Tunawashukuru sana marafiki zetu hawa wa China kwa kuheshimu msingi huu mkubwa wa ushirikiano.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Licha ya mafanikio haya makubwa yaliyopatikana kwenye ushirikiano wetu, ni wazi kuwa bado tunayo fursa ya kuukuza na kuuimarisha. Tuna maeneo mengi ambayo tunaweza kuanzisha au kuimarisha ushirikiano.Tuna fursa kubwa ya kukuza biashara kati yetu. Mathalan, nchi zetu za Afrika tunahitaji soko la China kupanuliwa zaidi ili kuuza bidhaa zetu. Hivi sasa China ina watu watu wapatao bilioni 1.4. Hili ni soko kubwa ambalo nchi za Afrika inaweza kulitumia kwa ajili ya kuuza bidhaa zake mbalimbali (kahawa, chai, n.k.). Zaidi ya hapo, tunaihitaji China kuongeza uwekezaji Barani Afrika, hususan kwenye sekta za kilimo, viwanda, madini, utalii, n.k. Aidha, nchi za Afrika zingependa kukuza ushirikiano na China katika ujenzi wa miundombinu, hususan ya usafiri na nishati ya umeme. Tunahitaji pia kuendeleza ushirikiano na China kwenye masuala ya sayansi na teknolojia, utamaduni, kupata fursa za masomo kwa ajili ya kujenga uwezo wa wananchi wetu. Na vilevile, nchi za Afrika zinahitaji kushirikiana na China katika masuala ya kimataifa, ikiwemo masuala ya ulinzi na usalama, kushughulikia mabadiliko ya tabianchi pamoja na mageuzi kwenye umoja wa mataifa.
Hayo ni baadhi tu ya maeneo ambayo Afrika na China zinaweza kuimarisha ushirikiano. Na kama ukiniuliza mimi, hivi sasa ndio wakati muafaka wa kukuza ushirikiano kati ya Afrika na China. Nasema hivyo, kwa sababu, kama mjuavyo, mwaka 2013, Mheshimiwa Rais Xi Jinping wa China alianzisha mpango au mkakati ujulikanao kwa jina la “Belt and Road Initiative” wenye lengo la kukuza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati China, nchi nyingine za Asia pamoja na Mabara mengine, ikiwa ni pamoja na Bara letu la Afrika. Aidha, mwaka huu China imetimiza miaka 40 tangu ilipoanza kufanya mageuzi ya kiuchumi ambayo yameiletea mafanikio makubwa nchi hiyo; na mwaka jana China ilipitisha Mwogozo wa Maendeleo wa China hadi mwaka 2050 (a blueprint for China’s development) wenye lengo la kuifanya China kuwa ya kisasa na imara zaidi.
Kwa upande wetu Afrika, sote hapa tunafahamu kuwa mwaka 2015, kupitia Umoja wa Afrika, tulipitisha Agenda ya Maendeleo ya Afrika hadi kufikia mwaka 2063 (The AU Agenda 2063), ambayo lengo lake ni kujenga Afrika moja yenye ustawi na amani (an integrated, prosperous and peaceful Africa). Aidha, kama mjuavyo, nchi nyingi za Afrika hivi sasa zinaongoza kwa ukuaji uchumi duniani; na nyingine nyingi zinatekeleza Dira pamoja na Mipango ya Maendeleo yenye lengo za kuzifanya ziwe za uchumi wa kati katika kipindi cha muongo mmoja ujao. Haya yote yanafanya huu uwe ni wakati muafaka zaidi kwa Afrika na China kuimarisha uhusiano na ushirikiano; na hasa kwa sababu mipango na malengo yetu yanafanana.
Waheshimiwa Viongozi, Mabibi na Mabwana;
Ni kwa kuzingatia hayo yote, napenda nitumie fursa hii kutoa pongezi na shukrani zangu nyingi kwa vyama vyetu viwili, yaani Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) cha Tanzania ambavyo vimeshirikiana kuandaa Mkutano huu wa Majadiliano kati ya CPC na Vyama vya Siasa vya Afrika. Kama sote tujuavyo, vyama vya siasa ni taasisi muhimu ambazo zinatoa mchango mkubwa wa maendeleo duniani. Vyama Vya Siasa ni sauti ya watu lakini pia ndivyo vyenye kuunda na kuzisimia serikali. Hivyo basi, nina matumaini makubwa kuwa yote yatakayojadiliwa hapa yatakuwa yanawakilisha sauti za wananchi wetu; na kwa kuwa Mkutano huu unahusisha Watendaji Wakuu wa Vyama, basi maamuzi au mapendekezo yatakayofikiwa, ni lazima yatatekelezwa na Serikali zetu. Na kwa bahati nzuri, kama nilivyosema, Mkutano huu unafanyika miezi michache tu kabla ya kufanyika kwa Mkutano wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika na China mwezi Septemba 2018. Hivyo, nina imani baadhi ya mapedekezo ya mkutano huu yatajumuishwa kwenye Maazimio ya Mkutano huo wa Septemba kwa ajili ya kutekelezwa na Serikali zetu katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.
Nimefurahishwa sana na kaulimbiu ya Mkutano huu, ambayo inasema “Nadharia na Mikakati Halisi ya Vyama vya Siasa vya Afrika na China katika kutafuta Njia za Maendeleo kwenye nchi zetu (Theories and Practices of Chinese and African Political Parties in Exploring Development Paths Suitable to National Situation)”. Binafsi naiona kaulimbiu hii kuwa nzuri sana. Inatoa nafasi kwa vyama vyetu kujadili namna ya kukuza ushirikiano kati ya Afrika na China. Aidha, inatoa fursa ya kubadilishana mawazo na kupeana uzoefu wa namna Vyama vyetu vitaweza kushiriki kwenye masuala ya maendeleo; fursa zilizopo na changamoto ambazo vyama vyetu vinakumbana navyo katika kusimamia shughuli za maendeleo katika nchi zetu, n.k. Masuala haya yote ni muhimu katika kukuza ushirikiano wetu lakini pia katika kuleta maendeleo kwenye nchi zetu. Hivyo basi, niwaombe sana wajumbe wa mkutano huu mjadili kwa uwazi na kina masuala haya. Msiogope kujadili suala lolote. Kama nilivyosema, Vyama ni sauti ya watu lakini pia ndio vyenye kuunda Serikali. Hivyo mjadili kwa uwazi bila kuogopa. Naamini yapo mambo mazuri mengi ambayo Vyama vya Siasa kutoka nchi za Afrika zitajifunza kutoka Chama cha Kikomunisti cha China na pia yapo mambo mazuri ambayo CPC itajifunza kutoka kwetu Afrika.
Waheshimiwa Viongozi;
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Nimesema mengi sana. Nimeeleza kuhusu historia ya uhusiano kati ya Afrika na China; mafanikio yaliyopatikana; maeneo ya kuimarisha uhusiano; na kadhalika namna ambavyo vyama vyetu vinaweza kutoa mchango katika kukuza ushirikiano kati ya pande zetu mbili na pia kuleta maendeleo kwenye nchi zetu, hususan maendeleo ya kiuchumi. Hata hivyo, kabla ya kuhitimisha, napenda kurudia tena kuishukuru na kuipongeza CPC kwa kubuni wazo la kuanzisha majadiliano ya namna hii. Aidha, nawashukuru wajumbe kutoka nchi mbalimbali kwa kuhudhuria kwa wingi katika Mkutano huu.
Kwa niaba ya wana-CCM na Watanzania wote, tunawashukuru kwa kuichagua nchi yetu kuwa mwenyeji wa Mkutano huu. Narudia tena kusema hamjakosea kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huu. Mbali na sababu mbili nilizozitaja awali, Tanzania ina vivutio vingi vya utalii ambavyo huwafurahisha wageni wetu wengi. Fukwe za Zanzibar, Mbuga za Wanyama za Serengeti na Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro, n.k. Ni imani yangu kuwa, hata ninyi wajumbe wa Mkutano huu, kama sio wakati huu basi mtatafuta wakati mwingine kuvitembelea vivutio hivyo ili kujionea uzuri wa Tanzania.
Napenda kuhitimisha kwa kuahidi kwamba CCM pamoja na Serikali yake itaendelea kushirikiana na CPC, Serikali ya China pamoja na Vyama vingine Barani Afrika. Na katika hili, napenda niseme kuwa CCM na Serikali ya Tanzania kwa pamoja vinaishukuru CPC na Serikali ya China kwa misaada mbalimbali inayotupatia kwenye Chama na pia kwenye Serikali, hususan katika nyanja za afya, elimu, maji, kilimo, miundombinu, n.k. Nia yetu ni kuona ushirikiano wetu ukizidi kukua.
Hivi sasa, nchi yetu inatekeleza Dira yake ya Maendeleo ya Mwaka 2025 ambayo inalenga kuifanya nchi yetu kuwa nchi ya uchumi wa kati wenye kuongozwa na viwanda. Ili kufikia azma hiyo, tumebuni mipango na miradi mbalimbali ya kimkatati. Baadhi tumeshaiwasilisha kwa marafiki zetu mbalimbali, wakiwemo wa China, ili watuunge mkono. Miradi hiyo ni pamoja ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa kutoka hapa Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Mwanza na Kigoma, na kisha kwenda nchi za Burundi na Rwanda; ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo; miradi ya kufua na kusafirisha umeme; mradi wa kuchimba chuma pamoja na kufua umeme wa makaa ya mawe wa Mchuchuma na Liganga, na mradi mkubwa wa Kiwanda cha Kuchakata Gesi Asilia, n.k.
Hivyo basi, napenda kutumia fursa hii kuwaomba marafiki zetu wa China kutuuga mkono katika kutekeleza miradi hiyo mikubwa ya maendeleo kwa nchi yetu. Tunawakaribisha pia rafiki zetu wa China pamoja na nchi nyingine, zikiwemo za Afrika, kuja kuwekeza hapa nchini, hususan kwenye viwanda vya kusindika na kuongezea thamani mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi; kilimo chenyewe, uchakataji madini, sekta ya utalii, n.k. Aidha, tunawaomba marafiki zetu wa China waendelee kutupatia fursa za masomo hususan kwenye fani za afya, kilimo, mafuta na gesi, sayansi na teknolojia, n.k. Kwa namna hii ushirikiano wetu utazidi kuimarika na wananchi wetu watanufaika.
Baada ya kusema hayo, natamka rasmi kuufungua Mkutano huu. Nawatakia Wajumbe majadiliano mema na nina matumaini makubwa kuwa Mkutano huu utakuwa wa mafanikio.
Mungu Ubariki Ushirikiano kati ya Afrika na China!
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
“Ahsanteni sana kwa kunisikiliza”