Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tovuti Rasmi ya Rais

Habari

Waziri: Tumevuka lengo kusambaza umeme, tupangiwe jipya


 

            SERIKALI imekiomba Chama cha Mapinduzi (CCM) kuipangia upya malengo ya kusambaza umeme kwa wananchi kwa sababu malengo yaliyopangwa katika Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa 2010 yamefikiwa na kupitwa hata kabla ya kumalizika kipindi cha miaka mitano.

            Aidha, Serikali imesema kuwa upo uwezekano mkubwa kwamba usambazaji wa umeme unaweza kufikia asilimia 50 ya wananchi wote wa Tanzania ifikapo mwakani kwa sababu umeme sasa unasambazwa kwa kasi isiyokuwa ya kawaida.

            Ombi hilo la Serikali limetolewa jana, Ijumaa, Julai 18, 2014 na Waziri wa Nishati na Madini, Mheshimiwa Sospter Muhongo, wakati alipozungumza katika mkutano wa hadhara ambao umehutubiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, mjini Mbamba Bay, Wilaya ya Nyasa, Mkoa wa Ruvuma.

            Waziri Muhongo ameuambia umati huo wa wananchi kuwa Ilani ya uchaguzi ya CCM ilikuwa imeipa Serikali jukumu la kusambaza umeme hadi kwa asilimia 30 ya wananchi.

            "Hivi ninavyozungumza Mheshimiwa Rais tayari tumevuka lengo hilo na kufikia asilimia 36 na kwa kasi hii tunayokwenda nayo haitashangaza kama tufikia asilimia 40 ama hata 50 ya kuwasambazia wananchi umeme."

            Ameongeza Waziri Muhongo: "Hivyo, tunakiomba chama chetu kitupangie malengo mapya yanayokwenda na kasi mpya ambayo Wizara yangu inaionyesha. Tunataka chama kitupe malengo mapya kwa sababu yale tuliyopewa tumevuka, tena kwa mbali."

            Kuhusu usambazaji wa umeme katika Wilaya ya Nyasa, Waziri Muhongo amesema vijiji 58 kati ya vijiji 73 vya Wilaya hiyo vitasambaziwa umeme katika mradi ambao tayari umeanza ikiwa ni idadi ya juu ya usambazaji umeme vijijini. Mradi huo uliozinduliwa jana na Rais Kikwete mjini Mbamba Bay unatarajiwa kukamilika Juni mwakani.

            Kuhusu hali ya umme ilivyo katika mkoa mzima wa Ruvuma, Waziri Muhongo amesema kuwa kiasi cha shilingi bilioni 26.5 zimetengwa kwa mwaka wa sasa wa fedha kwa ajili ya kusambaza umeme katika mkoa huo.

            Hata hivyo, Waziri amesema kuwa mkoa huo una uwezo wa kutosha wa kuzalisha umeme wake wenyewe. Amesema kuwa mkoa unahitaji kiasi cha megawati 6.2 wakati mkoa wenyewe una uwezo wa kuzalisha megawati 10.3.

            Kuhusu gharama za kuunganisha umeme vijijini, Waziri Muhongo amesema kuwa gharama hizo zimeteremshwa kiasi kikubwa na kubakia 27,000 tu. "Gharama hizo kila mtu anaweza kulipa akiuza hata majogoo wawili tu."

            Waziri pia ametumia nafasi hiyo kuwaelezea wananchi kuhusu uamuzi wa Serikali wa kuligawa Shirika la Umeme la Taifa - TANESCO- ili kuongeza ufanisi ambao utaifikisha Tanzania mahali pa kuuza vocha za kununulia umeme madukani kama zinavyouza vocha za simu.          

Mwisho!

 

Imetolewa na;

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu – Dar es Salaam.

19 Julai,2014