Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tovuti Rasmi ya Rais

Habari

SERIKALI YATENGA FEDHA UJENZI WA NYUMBA ZA WALIMU


Serikali imetenga Shilingi Milioni Mia Tano (Tshs 500m) kwa  Halmashauri 41 nchini kwa ajili ya ujenzi wa nyumba bora za Walimu.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete amewaambia Wananchi wa Tanga, jana tarehe 27 Machi,2014 wakati akihutubia Mkutano wa hadhara katika barabara ya Karume kuwa;

"Tayari Halmashauri za Mkinga, Pangani na Kilindi zimeshapata pesa hizo , na tumetenga kiasi kama hicho kwa kila Halmashauri zingine nchini  ili kuboresha makazi na Nyumba za Walimu " Rais amesema.

Fedha hizo ni sehemu ya fedha iliyotengwa maalum na Serikali kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu katika Halmashauri arobaini na  moja (41) nchini kote katika kipindi cha Mwaka wa fedha wa 2013/14.

Halmashauri zingine zitakazofaidika na mpango huo ni Mlele, Nsimbo , Meatu, Makete, Ngorongoro na Longido. Pia Halmashauri za Bagamoyo, Mafia, Kisarawe, Rufiji,, Kigoma, Kasulu, Kibondo, Nachingwea, Kilwa, Liwale,Ruangwa  Rorya, Chunya, Ileje, Rungwe, Kilombero, Ulanga, Newala, Tandahimba na Nanyumbu  zitafaidika na mpango huo wa Serikali.

Aidha, Halmashauri za Ukerewe, Sengerema, Kwimba, Tunduru, Namtumbo na Sikonge pia zimo katika mpango huo wa Mwaka huu wa fedha.

Halmashauri za Muleba, Ngara, Nkasi, Kiteto na Simanjiro nazo zimo katika mpango huu ambao Serikali imedhamiria kuutekeleza ili hatimaye  kuwatengenezea mazingira mazuri walimu hapa nchini.

Rais amemaliza awamu ya kwanza ya ziara yake ya kikazi Mkoani Tanga ambapo ametembelea, kukagua shughuli za maendeleo na kufungua miradi ya Barabara, Maji, Soko na Maabara Mkoani Tanga.

Katika ziara yake hiyo Rais ametembelea Wilaya za Handeni, Korogwe, Muheza na Tanga ambapo katika awamu ya pili Rais amepanga kutembelea Mkinga, Lushoto, Kilindi na Pangani.

Rais amerejea jijini Dar es Salaam jana jioni.

Mwisho!

Imetolewa na;

Premi Kibanga
Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi,
Tanga.

28 Machi,2014