Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tovuti Rasmi ya Rais

Habari

Rais Magufuli awasimamisha kazi kamishna Mkuu wa Uhamiaji na Kamishana wa Uhamiaji anayeshughulikia utawala na fedha


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewasimamisha kazi Kamishna Mkuu wa Uhamiaji Bwana Sylvester Ambokile na Kamishna wa Uhamiaji anayeshughulikia Utawala na fedha Bwana Piniel Mgonja   ili kupisha uchunguzi, kufuatia dosari alizozibaini Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mheshimiwa Charles Kitwanga alipotembelea Idara ya Uhamiaji hivi karibuni.

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amezitaja dosari hizo kuwa ni pamoja na tuhuma za rushwa, ukusanyaji mbaya wa maduhuli ya serikali, ukiukwaji wa taratibu za manunuzi na utendaji mbovu.

Balozi Sefue amesema watendaji hao wakuu wa Uhamiaji wamesimamishwa kazi mara moja hadi hapo uchunguzi utakapokamilika na kwamba endapo watabainika kutokuwa na makosa Rais ataamua hatma yao.

Katika Hatua nyingine Rais John Pombe Magufuli amemrejesha Bwana Eliakim Chacha Maswi kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, baada ya kukamilisha kazi maalum aliyomtuma kuifanya katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Kabla ya kurejeshwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Bwana Maswi aliteuliwa kuwa Kaimu Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema, Rais Magufuli amefanya mabadiliko hayo kwa lengo la kumtafuta mtu mwenye utaalamu wa kuendeleza kazi iliyofanywa na Bwana Maswi.

Gerson Msigwa

Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU

Dar es salaam

20 Januari, 2016