Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tovuti Rasmi ya Rais

Habari

Mjadala Bunge Maalum la Katiba halininyimi usingizi Rais Kikwete


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho

Kikwete amesema kuwa hana wasiwasi na hali ya mjadala mkali uliotawala

Bunge Maalum la Katiba kwa sababu ni muhimu kwa mjadala kuhusu Katiba

Mpya ukawa wa kina ili kuweza kupata Katiba bora kwa Watanzania.

Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa Katiba ya Tanzania haitapatikana

kwa mikutano ya kisiasa nje ya Bunge Maalum la Katiba bali ndani ya Bunge hilo

ambako ni dhahiri kuwa mjadala utatawaliwa na nguvu ya hoja na busara.

Rais Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na

Usalama ametoa ufafanuzi huo mchana wa leo, Ijumaa, Juni 20, 2014, wakati

alipotoa Mhadhara (Lecture) kuhusu Usalama wa Taifa (The Security of the

Nation) kwenye Chuo cha Taifa cha Ulinzi – National Defence College – kilichoko

Kunduchi, Dar Es salaam.

Wakati wa kipindi cha maswali na majibu, ofisa mmoja wa Jeshi la

Kenya alimwuuliza Rais Kikwete kama alikuwa na wasiwasi kuhusu mjadala

unaoendelea nchini kuhusu Katiba Mpya unaweza kuvuruga usalama wa

Tanzania.

Rais Kikwete amemjibu: “Sina wasiwasi hata kidogo kwa sababu

hatukutarajia kuwa mjadala wa Bunge Maalum la Katiba kuhusu jambo hili kubwa

ungekuwa rahisi. Yalipojitokeza maoni ya Tanzania kupata Katiba Mpya, tuliunda

Tume na tume hiyo ikatoa ripoti yake ambayo ndiyo inajadiliwa katika Bunge

Maalum. Hatukutarajia kuwa mjadala kuhusu ripoti ungekuwa rahisi kwa wajumbe

kutoa majibu ya ndiyo ama hapana.”

Ameongeza Rais Kikwete: “Kinachoendelea ni jambo muhimu na la

lazima...najua wakati mwingine majadiliano yalikuwa makali mno lakini hili ni jambo

zuri. Aina ya mfumo na muundo wa Serikali lilizusha mjadala mkali lakini hayo ni

matokeo ya hali halisi ya masuala yanayojadiliwa.”

“Ni imani yangu kuwa tutafikia mwisho. Mwisho upi, hilo ni suala la Wajumbe

wa Bunge Maalum la Katiba kuamua. Muhimu ni kwamba Katiba Mpya inaweza

kupatikana kutoka Bungeni tu siyo kupitia mikutano ya hadhara nje ya Bunge. Huko

hakuna Katiba huko kuna mikutano ya hadhara na siasa tu. Katiba itapatikana kwa

mijadala na kwa nguvu ya hoja ndani ya Bunge letu.”

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

IKULU

DAR ES SALAAM

20 Juni, 2014