Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Tovuti Rasmi ya Rais

Habari

MHE. RAIS SAMIA SULUHU HASSAN AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA MKURUGENZI WA KITUO CHA KUDHIBITI NA KUZUIA MAGONJWA BARANI AFRIKA (AFRICA CDC) DKT. JOHN NKENGASONG LEO TAREHE 27 JULAI, 2021IKULU JIJINI DAR ES SALAAM.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, leo tarehe 27 Julai, 2021 amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Barani Afrika (Africa CDC) Dkt. John Nkengasong Ikulu Jijini Dar es Salaam.

 

Dkt. Nkengasong amempongeza Mhe. Rais Samia kwa hatua mbalimbali anazochukua katika kukabiliana na ugonjwa wa UVIKO 19 na kusema kuwa kituo cha Africa CDC kinaunga mkono jitihada hizo za Serikali ya Tanzania katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.

 

Amesema Africa CDC, imedhamiria kushirikiana na nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) ikiwemo Tanzania kuweka mipango ya pamoja na kutumia fursa zinazopatikana kupitia kituo hicho katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa UVIKO 19 ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa chanjo na usambazaji wake. Africa CDC wameanzisha mpango wa Safari za Kuaminika (Trusted Travel) utakaowawezesha wanachama wa AU kusafiri ndani na nje ya Bara la Afrika bila vikwazo vitokanavyo na ugonjwa wa UVIKO 19.

Aidha, Mhe. Rais Samia amemshukuru Dkt. Nkengasong kwa uamuzi wake wa kuja Tanzania kwa lengo la kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Serikali na kumjulisha kuwa tayari Tanzania ina Kamati Maalum ya kitaifa inayoratibu masuala yote yanayohusu ugonjwa wa UVIKO 19 na ipo tayari kufanya kazi na wataalamu kutoka Africa CDC katika kukabiliana na ugonjwa huo na kueleza kuwa Tanzania imejiunga na Mpango wa Covax (Covax facility)  kwa lengo la kunufaika na fursa zitokanazo na mpango huo ikiwemo upatikanaji wa chanjo.

Halikadhalika, Mhe. Rais Samia amemhakikishia Dkt. Nkengasong kuwa Tanzania iko tayari kufanya kazi na Africa CDC haraka iwezekanavyo ili kukabiliana na ongezeko la kusambaa kwa ugonjwa wa UVIKO 19 katika nchi wanachama wa Umoja wa Afrika.